Nani amlipe mchezaji wa mkopo baina ya timu yenye mkataba naye na iliyoazimwa, ni makubaliano ya timu mbili hizo. Nini timu inayoazimwa mchezaji iilipe timu yenye mchezaji ni makubaliano yao, lakini si fedha ya kumnunua. la sivyo huyo mchezaji asingeambiwa ameenda kwa mkopo. Hili lisitofautishwe na mchezaji kuuzwa (sio kupelekwa) kwa mkopo, ambapo timu inayopokea mchezaji inaweza kuilipa timu inayouza mchezaji kwa awamu. ndivyo inavyotaka Real Madrid kwa Tottenham kuhusu Bale. Nje ya makubaliano hayo, malipo mengine yoyote baina ya timu iliyoazimwa na mchezaji ni makubaliano ya kiungwana, gentlemen's agreement, ambayo hayana mashiko kwenye mustakbali wa timu hiyo na mchezaji mbele ya chama husika cha mpira. Kwa maneno mengine, kunaweza kukawa na kulipana pesa baina ya Ngassa na Simba kwa nia ya kuendelea kuichezea Simba baada ya mkataba wake wa Azam kumalizika. Lakini makubaliano hayo ni kifunga-uchumba tu, si mahari wala sio ndoa. Kisheria ni kama MoU, hati ambayo kisheria haina nguvu za kimkataba. Kwa hivyo TFF si mahala sahihi pa Simba kupeleka malalamiko yao. Wanapaswa kufungua kesi ya madai Mahkamani ambako wakishinda, Ngassa anaweza kutakiwa kurejesha hicho kifunga-uchumba, na hata ziada kutokana na usumbufu alioipa Simba kwa kuipotezea muda na kuinyima fursa ya kupata mchezaji mbadala anayelingana na fedha waliotanguliza au anayelingana na Ngassa mwenyewe. Nje ya hivyo ni ku-boogie step.