Uchunguzi ufisadi wa Meremeta wayeyuka

Rutashubanyuma

JF-Expert Member
Sep 24, 2010
219,470
911,174
Uchunguzi ufisadi wa Meremeta wayeyuka
Send to a friend
Friday, 11 November 2011 21:21


Neville Meena, Dodoma
KUNA kila dalili kwamba uchunguzi uliokuwa ukikusudiwa na Bunge kuchimbua ufisadi wa zaidi ya Sh205.9 bilioni unaodaiwa kufanywa kupitia Kampuni ya Meremeta iliyokuwa ikimilikiwa na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) hautafanyika, Mwananchi limebaini.

Matumaini ya kuchunguzwa kwa kashfa hiyo yalitokana na hatua ya Spika wa Bunge Anne Makinda kuamua kupeleka jambo hilo katika kamati za Bunge zilizopo, badala ya kuunda kamati teule kama ilivyokuwa imependekezwa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe.

Zitto wakati wa mkutano wa nne wa Bunge la bajeti mwaka huu, aliwasilisha kwa Spika Makinda hoja binafsi akitaka bunge liunde kamati teule kuchunguza suala hilo ambalo Serikali imekuwa ikitaka lisiguswe kwa maelezo kwamba ni linagusa mambo ya ulinzi na usalama wa nchi.

Mtizamo huo wa Serikali ndiyo unaoonekana kukwaza uchunguzi ambao ulikuwa umekaribia kuanza pale Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashillilah alipoliambia Mwananchi mjini Dodoma kuwa: “Ninavyokumbuka ni kwamba suala hili lilishafungwa tangu bunge la tisa, Serikali ilishaweka wazi suala hili wakati wa Bunge la tisa”.

Dk Kashillilah alisema katika mazingira hayo haoni ni kwa jinsi gani jambo hilo linaweza kurejeshwa tena bungeni na kwamba hata hoja hiyo ikilazimishwa, itafika wakati itakwama na kutotoa matokeo yanayokusudiwa.

“Labda walazimishe tu na wanaweza kufanya hivyo lakini kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu zetu limekwisha. Kama tunavyojua sisi tunafanya kazi kwa mujibu wa taratibu zilizopo, kwa hiyo tukisimama hapo sidhani kama jambo hili litakuwa na tija,” alisema Dk Kashillilah ambaye wakati hoja hiyo ilipoibuliwa tena alikuwa kwenye likizo ya ugonjwa.

Kwa kauli ya Katibu huyo wa Bunge, ni dhahiri hoja ya Zitto itakuwa imekwaa kisiki hivyo suala la kilichojiri ndani ya Meremeta kubaki siri kubwa.

Msimamo wa Serikali

Maelezo ya Dk Kashillilah yanarejea msimamo uliowahi kutolewa bungeni na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda Juni 27, 2008 kwamba yuko tayari kusulubishwa lakini si kueleza undani wa Meremeta.

Akihitimisha Makadirio ya Bajeti ya Ofisi yake kwa mwaka 2008/09, Pinda alisema: “Meremeta haukuwa mradi wa uraiani ambako tungeweza tukasema jambo lolote tunalotaka kulisema, 'this is a unique situation' (haya ni mazingira ya kipekee).”

“Nilitaka tu niseme, mimi kusimama hapa nianze kusema 'this is what it was and this is what' (hiki ni kitu gani na ilikuwaje)…, hapana. Napata taabu, sitaweza. Sitaweza for a simple reason (kwa sababu nyepesi), tu kwamba ni jambo ambalo lina uhusiano wa karibu sana na masuala ya ulinzi na usalama wa nchi yetu,” alisema Pinda na kuongeza:

“Mengine yote niko radhi, ila kwa hili na kwa sababu nalijua na mimi, kwa kweli inafika mahali nasema hapana, nadhani iwe protected na tui-protect Serikali na tu-protect jambo hili ambalo linahusiana na ulinzi na usalama. Sasa kama mtaona hiyo inatosha, vyema. Mkiona mnisulubishe kwa sababu sijasema yote, well and good (ni vyema) vilevile.”

Mchakato wa uchunguzi

Mara ya mwisho, Spika alikuwa ameamua kupeleka suala hilo kwa Kamati ya Ulinzi na Usalama inayoongozwa na Mbunge wa Monduli (CCM), Edward Lowassa, lakini uchunguzi umebaini kwamba suala hilo bado halijawasilishwa rasmi mbele ya kamati hiyo.

Mkurugenzi wa Huduma za Bunge, John Joel ambaye alikuwa akikaimu nafasi ya Dk Kashillilah wakati akiwa likizo alithibitisha kwamba ofisi yake haikuwahi kuiarifu Kamati ya Lowassa kuhusu suala hilo.

Awali, baada ya Spika kupokea taarifa ya kusudio la Zitto la kutaka kuundwa kwa kamati teule, aliamua suala hilo lifanyiwe kazi katika Kamati ya Nishati na Madini. Hata hivyo, baadaye Spika Makinda alibatilisha uamuzi wake wa awali, hivyo kuamua kupeleka suala hilo katika Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama.

Zitto akiwa chanzo cha hoja hiyo aliwahi kupongeza uamuzi wa Spika kupeleka suala la Meremeta chini ya Kamati ya Nishati na Madini lakini suala hilo lilipohamishiwa Kamati ya Mambo ya Nje, alieleza wasiwasi kwamba ulikuwa ni mwanzo wa kuua hoja yake.

Zitto alianzisha hoja ya kuchunguzwa kwa Meremeta alipowasilisha barua kwa Katibu wa Bunge akitoa taarifa ya hoja ya kuunda Kamati Teule kwa ajili ya kuchunguza tuhuma za ufisadi kupitia kampuni hiyo ya uchimbaji wa dhahabu.

Barua hiyo ilitanguliwa na taarifa yake ya mdomo aliyoitoa bungeni Julai 13, mwaka huu kwa mujibu wa Kanuni ya Bunge Namba 117 (2)-(a) inayomruhusu kutoa taarifa ya kusudio lake la kuwasilisha hoja ya kutaka Bunge liunde Kamati Teule.

Mbunge huyo alimwandikia Spika Makinda barua kutoa taarifa ya hoja husika Julai 15, mwaka huu akisema: “Kuna haja ya kujua uhalali wa ongezeko la Dola 122milioni zilizoongezeka katika malipo yaliyofanywa.”

Historia ya Meremeta

Meremeta Ltd ni kampuni ya Kitanzania iliyokuwa ikimilikiwa na JWTZ kwa ajili ya mradi wake wa Nyumbu, Mkoa wa Pwani huku taarifa za usajili zilizotolewa na Msajili wa Kampuni wa Uingereza na Wales zikisema kuwa kampuni hiyo iliandikishwa nchini humo mwaka 1997 na kabla ya kufilisiwa hukohuko mwaka 2006.

Taarifa ya Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (Brela) ya Mei 31, 2005 inabainisha kwamba Meremeta Ltd ni tawi la kampuni ya kigeni iliyosajiliwa Tanzania, Oktoba 3, 1997 na kwamba hisa 50 za kampuni hiyo zilikuwa zinamilikiwa na Kampuni ya Triennex (Pty) Ltd. ya Afrika Kusini, wakati hisa 50 zilizobaki zilikuwa zinamilikiwa na Serikali ya Tanzania.

Utata kuhusu umiliki wa Meremeta Ltd unatokana na taarifa ya Brela ambayo pia inazitambua kampuni mbili za Kiingereza, London Law Services Ltd na London Law Secretarial Ltd kuwa wamiliki wa hisa moja kila moja ndani ya Meremeta.

Licha ya Serikali kutokuwa mmiliki pekee wa kampuni hiyo, BoT inadaiwa kuwa ililipa madeni yote ya Meremeta badala ya kusaidiana na washirika wake ambao kisheria wanaonekana kuwa walikuwa wakimiliki hisa katika kampuni hiyo.

Serikali Tanzania ilikuwa ikimiliki asilimia 50 ya hisa na kwa mujibu wa taarifa za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), uhalali wa malipo hayo ulikuwa na walakini kwani kiutaratibu Nedbank Ltd ilitakiwa iachwe idai fedha zake kutoka kwa mfilisi wa kampuni hiyo sawa na wadeni wengine.

Hatua ya kurejeshwa kwa mkopo huo pamoja na faida ya zaidi ya asilimia 1,000 ndilo chimbuko la kutaka kufanywa kwa uchunguzi huo.

 
kimya kingi kina mshindo mkuu....................na huu wa meremeta siyo utani..............
 
Back
Top Bottom