Mgombea: Fanias Magesa, CHADEMA
Kinachogombewa: Uchaguzi mdogo wa Ubunge
Jimbo: Busanda, wilaya ya Geita
Uchaguzi: May 24, 2009
Utaalam: Mhandisi
Elimu: Shahada ya kwanza ya Uhandisi, Chuo Kikuu D'Salaam
Shahada ya pili ya Nishati Jadidifu, Chuo Cha Oldenburg, Ujerumani
Sera:
MIUNDO MBINU
Baadhi ya maeneo ya jimbo hayafikiki kwa urahisi na wakati wa mvua yanatenganishwa na mengine. Wananchi hawapaswi kuendelea kuvua nguo au kuingia ndani ya maji yanayofika kiunoni ili kupeleka mazao yao katika masoko ya uhakika na kupata mahitaji yao ya lazima. Niunge mkono tuongoze harakati za kuunganisha jimbo na kuzuia lisitengane kwa sababu ya uduni wa miundombinu (barabara na madaraja).
ELIMU
Kwenye sekta ya elimu, naahidi kushirikiana nanyi kuwezesha ujenzi wa mabweni katika sekondari 13 za kata zilizojengwa kwa nguvu za wananchi, kutafuta walimu na vifaa vya kufundishia. Mimba miongoni mwa wanafunzi ni nyingi katika shule hizi, mazingira ya kuishi na kusomea na kufundishia ni duni. Kwa pamoja tunaweza kuibadili hali hii.
MADINI
Kuna urasimu na dhuluma katika ugawaji na umilikishaji wa vitalu vya uchimbaji madini. Aidha kuna uduni wa vifaa vinavyotumika na wachimbaji wadogo wadogo wa madini jimboni Busanda. Nitashirikiana na wachimbaji kuongoza harakati za kuondoa urasimu, dhuluma na uduni wa vifaa vya uchimbaji jimboni.
KILIMO
Kwenye sekta ya Kilimo kuna ukosefu na uduni wa pembejeo jimboni Busanda. Dhana za kilimo zinazotumika ni duni. Aidha mazao yasiyozoeleka au kufahamika jimboni yameendelea kutolimwa japo yana tija kubwa.
Nitashirikiana na wananchi kuingiza mageuzi ya kilimo kwa kusaidia na kuhamasisha matumizi ya dhana bora, upatikanaji wa pembejeo na uingizaji wa mazao mapya yenye tija katika orodha ya yale yanayolimwa sasa. Pia nitashawishi kuingizwa kwa teknolojia ya ukaushaji wa matunda, mboga mboga na samaki, ili kukabiliana na tatizo la kushuka kwa bei wakati wa mavuno.
AFYA
Kuna uduni na ukosefu wa dawa, wataalamu na huduma za afya katika zahanati nyingi jimboni Busanda. Nitashirikiana na viongozi wengine kuhakikisha kwamba rasilimali kwenye sekta hii, ikiwemo mgawo wa ruzuku kwenye halmashauri unatumiwa ipasavyo katika kukabiliana na changamoto hizo.
ARDHI:
Sera za umiliki wa ardhi hazikidhi matakwa ya umma; na katika maeneo ambayo wananchi wamenyanganywa ardhi kwa sababu moja au nyingine wamekuwa wakipata fidia kidogo na wengine wakikosa kabisa. Hata wanaoendesha kilimo katika ardhi waliyopo bado tija imekuwa si ya kutosha. Kwa upande mwingine, rasilimali ikiwemo madini zimekuwa hazitumiki ipasavyo katika kuleta maendeleo.
Katika hali hii, mimi niliyepata fursa ya kusoma kwa kodi za wananchi wenzangu Shahada ya Uhandisi pale Chuo Kikuu cha Dar es salaam na baadaye kwenda kusoma shahada ya pili ya Nishati Jadidifu Chuo Cha Oldenburg nchini Ujerumani, naamini nina deni kwa wananchi wa Busanda na taifa kwa ujumla.
Sehemu ya kulipa deni hilo, ni kutumia taaluma yangu na utaalamu wangu wa uhandisi na nishati jadidifu kuwawakilisha, kuwatetea, na kushirikiana na wananchi wenzangu kuleta maendeleo katika Jimbo la Busanda na taifa kwa ujumla kwa kutumia rasilimali tulizopewa na Mungu. CHADEMA imeonyesha dhahiri kuwa na wabunge wenye kutetea rasilimali za taifa. Nikindelea kuzingatia maneno ya Mwalimu Nyerere; tunakosa mahitaji muhimu mawili ya maendeleo, siasa safi na uongozi bora.
Hivyo, kujitokeza kwangu kugombea na uamuzi wa wananchi wenzangu mbalimbali kuniunga mkono ni ishara ya dhamira ya pamoja katika kuleta siasa safi na uongozi bora katika jimbo letu la Busanda na taifa kwa ujumla ili kuunganisha watu watumie ardhi iliyopo katika kuleta maendeleo.
Tunachokiona leo, ni siasa chafu hususani ndani ya CCM; zenye kuchochea mifarakano na mivutano. Hapa wilayani Geita zimekuwa zikitokeza katika sura ya makundi ambayo hatimaye yamekuwa yakikwaza maendeleo.
Siasa hizi chafu, zimekuwa zikichafua fursa ya baadhi ya watu wazuri katika jamii kushindwa kuchaguliwa kuwa viongozi. Wakati umefika, wa wote wasiopenda siasa chafu, kuunga mkono mabadiliko; bila kujali kabila, chama au hali. Siasa hizo chafu, zinajitokeza pia wakati wa uchaguzi, siasa za kuwahonga wapiga kura, siasa za vitisho kwa wananchi, siasa za uongo na pengine siasa za ushirikina.
MIFUGO
Katika sekta ya mifugo kuna matatizo ya upatikanaji wa soko la uhakika la mazao ya mifugo. Hakuna hata kiwanda kimoja cha kusindika mazao ya wafugaji jimboni Busanda. Lazima wadau tushirikiane kuondokana na hali hii. Aidha tuhakikishe wafugaji wanapata maeneo ya uhakika ya kuchungia mifugo yao ili kuepusha migogoro baina ya wafugaji na wakulima. Katika sekta ya utumishi huduma na mazingira ya watumishi wa umma jimboni Busanda ni duni hasa kwa sekta za afya na elimu. Tutashirikiana na wafanyakazi kuweka msingi wa kutatua matatizo yao likiwemo lile la umbali mrefu wa kufuatilia mishahara yao na nyumba za kuishi.
NISHATI
Katika sekta ya nishati kuna tatizo la upatikanaji wa nishati ya uhakika jimboni Busanda. Nitaongoza harakati za upatikanaji wa umeme jimboni kwa kutumia njia mbalimbali ikiwemo uwezekano wa kuunganishwa kwenye mtandao wa taifa au kuangalia uwezekano wa kunufaika na sheria ya umeme ya mwaka 2008 ambayo inaruhusu ushiriki wa sekta binafsi katika kuzalisha na kuuza umeme kwa matumizi mbalimbali.
Aidha nitaongoza uingizwaji wa matumizi ya majiko yanayotumia kuni chache na vyanzo mbadala vya nishati ikiwemo pumba, jua, bayogesi katika taasisi na kaya ili kuboresha mazingira.Kwa ujumla, dhamira yangu ni kuwa mwakilishi wa wananchi ili tushirikiane katika kuhakikisha rasilimali zinatumika ipasavyo ikiwemo kupambana na ufisadi.Mathalani, kuna michango mbalimbali ya wawekezaji katika Wilaya ya Geita. Nitafuatilia uwezekano wa kupata ongezeko la michango hiyo kwa shughuli za maendeleo ya jimbo. Aidha, nitasimamia matumizi ya michango hiyo ili yawanufaishe wananchi zaidi na siyo kutumika kwa kazi nyinginezo za halmashauri kama vile utawala, mikutano na safari.
PERSONAL VALUES ZA UWAJIBIKAJI:
Mathalani, nilikwishaanza kujenga mabweni kama hosteli jirani na sekondari ya Butundwe jimboni Busanda, ili koboresha maisha ya kielimu ya watoto wetu. Nilijitolea kuonyesha njia katika suala hili. Naamini wote wanaoniunga mkono wanafanya hivyo wakielewa vyema uadilifu wangu na dhamira yangu ya kupambana na aina zote za ufisadi na changamoto za maendeleo. Watanzania tuungane mkono katika kurejesha utamaduni wa uwajibikaji katika taifa letu.
Nilipokuwa mtoto, baba yangu Bryceson Magessa wa Kijiji cha Nyakagomba alikuwa akinilea na kunifundisha kuhusu uwajibikaji. Ni malezi haya ndiyo yaliyonifanya hata nilipokuwa nikitekeleza miradi sehemu mbalimbali za nchi, nikumbuke uwajibikaji kwa watu wangu wa Busanda kupitia uunganishaji wa juhudi na maarifa.
Naamini, ni kwa sababu hiyo niko tayari kuacha kazi yangu ya muda mrefu Dar es salaam ili kutoa fursa ya kuwajibika kwa upana zaidi katika kutumikia umma katika jimbo letu la Busanda.
Ninaposimama mbele ya wananchi mkiwa mmenidhamini na wengine kuamua kunisindikiza kuja kurejesha fomu; naiona safari ya uwajibikaji wa pamoja tunayoianza katika kuleta demokrasia na maendeleo jimboni Busanda. Safari hii inahitaji baraka na kuungwa mkono na watu wote; bila kujali itikadi, kabila, eneo ama hali.
Ni mwito wa wajibu wa pamoja wa kutetea haki za wananchi, kukemea maovu na kuhamasisha maendeleo. Ni wajibu wa wazee wanaotaka kuona matunda ya uhuru waliyoyatazamia yanapatikana kwa kizazi cha sasa na vijavyo. Ni wajibu wa wanawake ambao ni chimbuko la maendeleo na wazazi wa ukombozi. Ni wajibu wa vijana ambao wameona mabadiliko katika mataifa mbalimbali na wamekuwa nguvu ya mabadiliko hayo.
Source: Excerpted from
Makala, Tanzania Daima.