Tutaacha lini kuwekeza katika anasa badala ya maendeleo?

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,790
288,009
Tutaacha lini kuwekeza katika anasa badala ya maendeleo? Thursday, 01 July 2010 10:29

Florence Majani
Mwananchi

NILIALIKWA katika kikao cha harusi. Wajumbe wakawa wanatoa michango kwa mashindano. Kila mmoja akijitahidi kutaja kiwango cha juu cha fedha ili aonekane naye amechangia kiasi kikubwa.


Lakini katika hali ambayo iliwashangaza wajumbe wengi katika kikao hicho, nikiwemo, mama wa bibi harusi alisimama na kutangaza kwamba atatoa Sh60milioni kuchangia harusi hiyo. Nilipigwa butwaa. Nikajiuliza, hiyo ni sherehe tu au kuna la ziada?


Nikatafakari na kugundua kuwa si huyu pekee anayetapanya fedha kwa ajili ya anasa ya siku moja. Wapo wengi na wanafanya hivyo kwa makusudi. Kwa ajili ya ufahari na starehe za muda mfupi tu.


Ni dhahiri kuwa, umaskini wa Watanzania unachangiwa kwa asilimia kubwa na ujinga na uzembe na uendekezaji wa starehe zisizo na msingi. Kwa nchi kama Tanzania, ambayo ni wachache wenye uwezo wa kifedha idadi kubwa wakiwa na maisha duni, haiingii akilini watu kutumbua fedha kwa kiasi kikubwa wakati watoto wanakosa hata madawati ya kukalia katika shule na wengine kujifungulia sakafuni.


Moyo wa uzalendo na kujitoa unahitajika katika kulijenga taifa hili. Umefika wakati wananchi tunapaswa kuachana na fikra za kuitegemea serikali kwa asilimia 100, huku wenyewe tukiwa tunachangia kulididimiza taifa katika lindi la umaskini kila kukicha. Kila mmoja wetu anayo dhamana ya kuangalia ni wapi anaweza kujitolea na kusaidia kwa uwezo alioanao.


Ni vyema Watanzania kufikiria upya kuhusu matumizi yetu, tuepuke kutapana fedha katika mambo ya anasa. Tuangalie vipaumbele vya wengi kama afya na elimu. Hii itasaidia kuinua kwa kiasi fulani hali ya maisha ya Watanzania. Umoja ni nguvu na utengano ni udhaifu.


Wananchi wakishirikiana kufanya mambo ya maendeleo, tutapiga hatua na kadri siku zinvyokwenda tutajikuta tunafanya mambo makubwa katika nchi yetu. Huyu akichangia kujenga nyumba za walimu na huyu akatoa madawati katika shule fulani, mwingine akatoa vitanda hospitalini itasaidia kwa kiwango fulani kunyanyua maisha ya Watanzania.


Uwepo wa uzalendo katika vichwa vya Watanzania ni jambo lisilotiliwa mantiki kabisa, badala yake kila mmoja anajali nafsi yake. Wahenga wanasema hata ubuyu ulianza kama mchicha, hivyo Watanzania wakianza kuwa na moyo wa uzalendo wa kuchangia maendeleo, tutafikia walipo wenzetu wenye maendeleo.


Kwa mfano, badala ya kutumia zaidi ya Sh70milioni kwa ajili ya sherehe ya kumuaga binti, fedha hizo, zingejenga hospitali vijijini au kununua vifaa vya hospital au madawati kwa ajili ya wanafunzi wanaoketi chini au vitanda kwa ajili ya wajawazito wanaolala mzungu wa wanne hospitalini.


Hivi karibuni mkereketwa mmoja wa masuala ya mpira wa miguu alitoa tiketi za Sh30,000 kila moja kwa mashabiki zaidi ya 100 kwa ajili ya kutazama mechi kati ya timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) na Brazil kwa mahesabu ya harakaharaka zilitolewa kama Sh90milioni. Ni fedha nyingi, watu wamekwenda kutazama mpira tu na kurudi nyumbani.


Wakati watu hao wakitazama mpira na kukenua, kuna wagonjwa wanaokosa huduma kwa kukosa Sh 10,000 tu za kumuona daktari, wengine wakifariki dunia kwa kukosa fedha za operesheni, walemavu wakichubuka miguu kwa kukosa baiskeli.


Mpaka sasa bajeti ya nchi yetu inategemea zaidi misaada na mikopo kutoka kwa wafadhili. Mpaka lini tutaendelea kutegemea wafadhili? Msaada kwa taifa uanzie nyumbani siyo kwa wageni ambao baadaye hutupa masharti magumu na kutufanya watumwa katika nchi yetu.


Masuala ya burudani yawepo lakini wakati mwingine yafanywe katika namna ya kuchangia huduma za maendeleo ya jamii.
Kwa mfano, wakati tetemeko la ardhi lilipoikumba Haiti, wanamuziki wengi wa Marekani walifanya matamasha, waliimba na fedha zilizopatikana zilipelekwa Haiti, kusaidia walioathirika.


Je, nasi hatuwezi kufanya matamasha ya muziki na michezo ili kupata fedha ambazo zitawekezwa katika maendeleo au huduma za jamii? Ni mamilioni ya fedha kiasi gani, hupatikana wakati wa mechi za mpira wa miguu? Fedha kiasi gani hupatikana wakati mashindano ya ulimbwende au tuzo za muziki? Ni mara ngapi umewahi kusikia msanii amefanya onyesho kisha akaagiza mapato yake yaende kwa watoto yatima au vinunuliwe vitanda hospitalini?


Hakika hayo hufanyika mara chache hapa Tanzania kila mtu anajali maisha yake tu. Sina maana kwamba tusifanye starehe na lakini zifanywe kwa kuangalia mustakabali wa hali zetu na za wenzetu. Kila mmoja ajali maisha ya wenzake pia.


Watanzania wenye uwezo wa kifedha, wanamuziki, wasanii wa fani nyingine na wanamichezo wajipange kuandaa matamasha au burudani za aina yeyote mara kwa mara kwa ajili ya kuchangia huduma za jamii badala ya kusubiri wakati wa maafa pekee.


Kila mtanzania awe na moyo wa kufanya kila awezalo ili naye achangie katika huduma za jamii. Wale wenye uwezo kiasi wawafikirie wale waliokosa kabisa huduma na wanaohitaji msaada.


 
mkuu,
kuna kila haja ya kuweza kurudia asili yetu ili kuruhusu kuwepo kwa maendeleo, ama kuweza kuyafikia
huku tukijetegemea kiakili, kimawazo na kimtazamo, kwa kuvipa kipaumbele vile tulivyo na uwezo
navyo pasi na kupalamia mfumo wa maisha ya watu wa nchi zilizoendelea,

ni kweli sisi kama taifa changa, tukiweza kumenage vizuri lasiri mali zetu kwa kujikongoja taratibu
tunaweza kufikia malengo hasa kwa kuwa tutakuwa na kile tulicho nacho,

tatizo viongozi wa nchi wanataka nchi ionekane ni miongoni mwa nchi zilizopiga hatua duniani, hasa kwa kutumia nafasi walizonazo kugharamia mambo na vitu vya anasa huku raia wakiwa hawajui hata kesho yao zaidi
ya kuiweka mikononi mwa Mwenyezi Mungu. tunataka tuonekane tunazo katikati ya walio nazo huku tuna harufu ya mikopo dunia nzima
 
Ni Tanzania tu wanafanya upuuzi huu saa hiyo Tshs60mil si kufuru na kukosa akili. Umaarufu ili iweje?
 
Watanzania wamerizika na harusi, vipaimara, send off n.k. halafu wakati huo huo wanalia njaa
 
kama mama kaamua kumfanyia binti yake harusi kwa tsh 60mil. kosa lake nini??hajamuomba mtu atoe hizo 60m katoa mwenyewe.....
wangapi humu wanaendesha magari yanayogharimu hadi tsh 60mil??je na nyinyi kwanini msinunue bajaj then balance mnunue madawati etc.....
hatujasaidia kutafuta hela za mtu fulani so msipangie watu jinsi ya kutumia hela zao,na hamlazimishwi kuchangia hizo harusi/vipaimara kama mnaona hazina mantiki msichangie.....
 
Nimefurahishwa na jinsi mwandishi huyu (Florence Majani) alivyoguswa na jinsi Watz tusivyoweza kuweka vipaumbele vyetu sawa sawa. Lakini upande mwingine hii inatupa picha ya hali halisi ya Tz, natamani nimpe changamoto huyu mwandishi ajaribu kufuatilia kuona hawa waliotoa jee shughuli zao za kiuchumi zinafana na kiwango cha michango waliyoahidi. Kangu mimi tatizo letu kubwa waTz tunaishi maisha yasiyoyetu, maisha ya mtu yanatokana na juhudi zake za kujitafutia. Mta anayejitafutia mwenyewe ana uchungu wa kila senti anayaoipata na kumfanya awe mwangalifu wa matumizi yake pia, huwezi kuniambia mtu anayejua uchungu wa kutafuta atachangia mil 60 hasa hapa Tz. Bahati mbaya mtu wa namna hii si rahisi hata kujua anahitajika kuchangia maendeleo, maana kwake maendeleo ni kitu kisichofanyiwa jitihada yoyote. Ni kitu kinachotokea kama ndoto, na ndio waTz wengi tulivyo. Hatuamini kwamba tukiweka jitihada katika jambo tunaweza kujiondoa katika hali duni tuliyonayo, isipokuwa sote tunategemea siku moja zitadondoka kama zinavyowadondokea wachache wetu. Matokeo yake ndio haya, hatujui hata jinsi ya kuzitumia.
 
Ni Tanzania tu wanafanya upuuzi huu saa hiyo Tshs60mil si kufuru na kukosa akili. Umaarufu ili iweje?

sio Tanzania tu....ASHLEY COLE,BECKHAM wamefanya harusi za over $3million hio tsh 60m ni kama $40,000......kama mtu ana uwezo mwache afanye,hujui anauwezo gani........
 
sio Tanzania tu....ASHLEY COLE,BECKHAM wamefanya harusi za over $3million hio tsh 60m ni kama $100,000......kama mtu ana uwezo mwache afanye,hujui anauwezo gani........
Ndugu yangu usimfananishe Ashley au Beckham na hali ya huku nyumbani, haya ni matatizo ndugu yangu. Hawa wanaelezwa hapa ndio hawa hawa wa mil 2,3 kwa mwezi.
 
kama mama kaamua kumfanyia binti yake harusi kwa tsh 60mil. kosa lake nini??hajamuomba mtu atoe hizo 60m katoa mwenyewe.....
wangapi humu wanaendesha magari yanayogharimu hadi tsh 60mil??je na nyinyi kwanini msinunue bajaj then balance mnunue madawati etc.....
hatujasaidia kutafuta hela za mtu fulani so msipangie watu jinsi ya kutumia hela zao,na hamlazimishwi kuchangia hizo harusi/vipaimara kama mnaona hazina mantiki msichangie.....

Mama huyo huyo unayemsifia anakwenda kwa waganga wa kienyeji kutibiwa.
 
Ndugu yangu usimfananishe Ashley au Beckham na hali ya huku nyumbani, haya ni matatizo ndugu yangu. Hawa wanaelezwa hapa ndio hawa hawa wa mil 2,3 kwa mwezi.

hilo jibu kwa aliesema mambo haya yanatokea tanzania tu,na pili huyu aliyechanga tsh 60million ni mama wa bibi harusi.....kama kaweza kutoa 60milion huyu sio mtu wa tsh 2,3 million kwa mwezi......kibongobongo huyo ni tajiri.
 
sio Tanzania tu....ASHLEY COLE,BECKHAM wamefanya harusi za over $3million hio tsh 60m ni kama $40,000......kama mtu ana uwezo mwache afanye,hujui anauwezo gani........

wewe ni mpumbavu na usituletee mambo yenu ya mwanaume kuvaa heleni
 
...nahisi kama muandishi alikosea kuhusu hiyo tarakimu ya mama. Labda aseme kuwa mama aliahidi mchango wa milioni SITA ana sio SITINI maana kama mzazi ana uwezo wa kugharamia shilingi milioni SITINI kwa ajili ya harusi ya binti yake, kwa nini asumbuke kualikaa watu kama waandishi wa habari ambao kipato chao kinajulikana, kuchangia harusi ya binti yake ?? Mama huyu alitakiwa kugawa kadi za mualiko tu na sio kutaka shilingi mbili tatu za watu kama huyo muandishi wa habari wakati tayari alikuwa na milioni SITINI :A S-eek: kibindoni!
 
Ni Tanzania tu wanafanya upuuzi huu saa hiyo Tshs60mil si kufuru na kukosa akili. Umaarufu ili iweje?
Sidhani kuwa hizo pesa za kumwaga hivyo zimepatikana kihalali. Nina mashaka kuwa pesa hizo zimepatikana kwa njia ya ufisadi au biashara haramu, na wanaozimwaga wana uhakika kuwa zingine zitakuja. Come easy, go easy!!
 
Back
Top Bottom