BENKI Kuu ya Tanzania (BoT) imetoa
sarafu maalumu ya kumbukumbu ya
miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar
yenye thamani ya sh 50,000.
Gavana wa BoT, Profesa Benno
Ndulu, alisema jana kuwa sarafu hiyo
iliyotengenezwa kwa madini ya fedha
kwa asilimia 92.50, imetolewa kwa
ajili ya kumbukumbu tu na
haitaingizwa katika mzunguko wala
kutumika kwa kulipia malipo ya aina
yoyote.
Taarifa kwa vyombo vya habari
iliyotolewa jana na Idara ya
Uhusiano wa Umma na Itifaki ya BoT
ilimnukuu Profesa Ndulu akisema
sarafu hiyo imetolewa kwa idadi ya
vipande 3,000 kwa ajili ya tukio hilo
na kuwahimiza wananchi kuinunua
kwa ajili ya kumbukumbu hiyo.
Kwa mujibu wa Gavana, kutolewa kwa
sarafu hiyo kunakwenda sambamba
na utaratibu wa Benki Kuu kutoa
sarafu maalumu za aina hiyo kama
sehemu ya maadhimisho ya
kumbukumbu ya matukio mbalimbali
muhimu ya kitaifa na kimataifa.
Kwa kawaida, baada ya muda,
thamani ya sarafu kama hizi
huongezeka na kuwa na faida zaidi
kwa wanaozimiliki, alisema Profesa
Ndulu.
Gavana Ndulu alieleza sarafu hizo
zitapatikana Januari 5 kwa bei ya sh
50,000 katika matawi ya benki za
biashara zitakazokuwa zimepata
sarafu hizo kutoka Makao Makuu ya
Benki Kuu, Dar es Salaam na matawi
ya Benki Kuu yaliyoko Zanzibar,
Arusha, Mbeya na Mwanza.
Benki za biashara zinaweza pia
zikasambaza sarafu hizi kupitia
matawi yake, alisema gavana na
kuongeza taarifa za usambazaji
zitatolewa na benki hizo.
Katika sarafu hiyo, upande wa mbele
unaonyesha sura ya hayati Sheikh
Abeid Aman Karume na maandishi
yanayosomeka: Rais wa Kwanza wa
Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi. Upande mwingine wa
sarafu unaonyesha nembo ya Serikali
ya Mapinduzi Zanzibar, maandishi
yanayosomeka: Miaka Hamsini ya
Mapinduzi, thamani ya sarafu na
miaka 1964-2014