PreGE2025 Taratibu zisizoeleweka wakati wa uchaguzi wa serikali za mitaa zitukumbushe uhitaji wa 'reforms' kuelekea uchaguzi mkuu Oktoba

Mijadala ya Uchaguzi Mkuu wa Tanzania 2025 (Kabla)

Just Pray

JF-Expert Member
Joined
Nov 7, 2023
Posts
2,142
Reaction score
4,779
Utafiti uliofanyika dhidi ya mchakato wa uchaguzi wa serikali za mitaa mwaka 2024 unabainisha mila na desturi za kijamii na kijinsia zilivyoathiri ushiriki wa vijana na wanawake katika uchaguzi.

Katika kipindi chote cha uchaguzi, vijana na wanawake waliokuwa sehemu ya utafiti walibaini na kutoa maoni juu ya changamoto walizokumbana nazo, ambazo kwa namna moja au nyingine, zilionesha mtazamo wao juu ya uchaguzi na hisia zao kuhusu ushiriki.

Kuhusu mchakato wa uandikishaji, vijana na wanawake waliokuwa wapiga kura na wagombea waliona kuwa uandikishaji ni msingi wa uchaguzi wowote. Ikiwa uandikishaji utaenda vizuri, uchaguzi mzima unakuwa na mafanikio.

Hata hivyo, wakati wa uandikishaji, baadhi ya washiriki walibaini kuwepo kwa taratibu zisizoeleweka, kama vile kuandikisha watu bila kuhitaji ushahidi wa taarifa walizotoa. Majina na umri tu ndivyo vilivyoulizwa, na mtu aliandikishwa bila uthibitisho wowote. Washiriki walihisi kuwa hali hii ilifungua mianya ya udanganyifu na uwezekano wa kuwaandikisha watu walio chini ya umri au kutoka mitaa au vijiji vingine bila kujua.

“Watu walikuwa wanakuja tu kujiandikisha bila kuulizwa maswali yoyote. Walisema tu jina na umri, na waliruhusiwa kuondoka.” – Mshiriki, Mgombea wa kisiasa, Dar es Salaam.

Katika baadhi ya maeneo, washiriki waliripoti kuona idadi kubwa ya wapiga kura walioandikishwa kuliko ile iliyoonekana na mawakala wa upinzani katika vituo vya uandikishaji. Mgombea mmoja wa upinzani alidai kujaribu uhalali wa mchakato kwa kumtuma mtoto wa miaka 14 kujiandikisha, na mtoto huyo aliandikishwa bila kuulizwa chochote. Pia, kulikuwepo na taarifa za watu waliokufa kuwa kwenye orodha za wapiga kura, na wanajamii waliwatambua marehemu hao.

Aidha, huko Kigoma, washiriki waliripoti kuwa baada ya muda wa uandikishaji kuisha katika kituo kimoja, daftari lilipelekwa shule ya sekondari ya karibu, na wanafunzi wa kidato cha tatu na nne wakaandikishwa. Matukio haya yaliathiri kwa kiasi kikubwa imani ya wapiga kura na mtazamo wao juu ya uchaguzi wa serikali za mitaa.


Baadhi ya wapiga kura waliokuwa na sifa, hasa katika mikoa ambayo usajili wa BVR ulianza kama Mwanza na Kigoma, walichanganyikiwa na kudhani hawatakiwi kujiandikisha tena, hivyo wengi wao hawakupata nafasi ya kupiga kura kwa sababu hawakujiandikisha.

Orodha duni za wapiga kura ziliweka kikwazo kwa vijana na wengine kupiga kura. Siku ya uchaguzi, washiriki waliripoti kuwa baadhi ya wapiga kura walikumbana na changamoto kubwa za kupata majina yao katika orodha zilizobandikwa.

Orodha hizo zilichapishwa kwa wino hafifu na hazikuwa katika mpangilio wa alfabeti, jambo lililowafanya wapiga kura wengi, wakiwemo vijana, kushindwa kuyapata majina yao. Baadhi yao walikata tamaa na kuondoka bila kupiga kura.

Katika mikoa kama Dodoma na Tanga, waandishi wa habari waliokuwa wakihifadhi kumbukumbu walishuhudia wapiga kura wasiojiandikisha wakiruhusiwa kupiga kura katika vituo vya kupigia kura. Pia, baadhi ya washiriki walishuhudia wasimamizi wa uchaguzi na mawakala wa vyama vya siasa wakiwaelekeza wapiga kura kupigia chama tawala.

Aidha, baadhi ya waandishi wa habari, vijana na wasikilizaji wa "Niambie" walieleza kuwa kutokuwepo kwa picha za wagombea kwenye karatasi za kupigia kura kulikuwa changamoto kwa wapiga kura wasiojua kusoma na wenye ulemavu wa kuona, ambao walipata ugumu wa kuwatambua wagombea wao. Hali hii ilisababisha zoezi la upigaji kura kuchukua muda mrefu kuliko ilivyotarajiwa.

Mazingira yasiyofaa yaliathiri ushiriki wa watu wenye ulemavu katika uchaguzi wa serikali za mitaa. Washiriki wengi walieleza kuwa waliona watu wachache sana au kutowaona kabisa watu wenye ulemavu katika mchakato mzima wa uchaguzi. Katika maeneo yote ya utafiti, ilibainika kuwa vituo vya uandikishaji, kampeni na upigaji kura havikuwa rafiki kwa watu wenye ulemavu.

Kwa mfano, vituo vingi vilikuwa katika shule za msingi na ofisi za vijiji au mitaa ambavyo havikuwa na miundombinu rafiki kwa watu wenye changamoto za utembeaji. Huko Tanga, iliripotiwa kuwa vyoo katika maeneo hayo pia havikuwa rafiki kwa watu wenye ulemavu, huku kampeni nyingine zikiendeshwa maeneo ya milimani ambayo mazingira yake yalikuwa magumu na kuonekana kuwa kikwazo kwa ushiriki wa watu wenye ulemavu.

 
Yamefanyika mabaya zaidi
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…