Tanzia: Mwalimu Bahiya bint Abdulrahman

Mohamed Said

JF-Expert Member
Nov 2, 2008
21,418
31,051
SHAJARA YA MWANA-MZIZIMA:

Buriani Mwalimu Wetu Bi ‘Maalima’ Bahiya


Na Alhaji Abdallah Tambaza

1572462694704.png

JUMAMOSI ya Oktoba 19, mwaka huu, itabakia kuwa siku ya huzuni kubwa sana kwa umma wa Kiislamu wa Jiji la Dar es Salaam na vitongoji vyake, baada ya kutangazwa kifo cha ghafla cha mwanamama, mwanazuoni mkubwa wa Dini ya Kiislamu; ‘Bi Mwalimu’ Bahiya bint Abdulrahman.

‘Bi Mwalimu’, kama ambavyo wanafunzi wake walivyozoea kumwita— kwa heshima, mapenzi na upole — alifikwa na umauti wakati akiwa na watoto wake wa Madrassa aliokuwa akiwatayarisha kwa ajili ya visomo mbalimbali vya Maulid yanayotarajiwa kufanyika madrassani kwake siku chache zijazo, katika kuadhimisha mazazi ya Mtume Muhammad (saw) mnamo mwezi wa Mfungo Sita.

“Maneno yake ya mwisho kuyasikia ni ya watoto wadogo wanafunzi ‘wakitwalii’ (kufunzwa/kutayarishwa) hadithi za Bwana Mtume (saw), katika matayarisho ya Maulid yake ya mwaka huu…,”aliandika binti yake Mamzee, katika wasifu wa marehemu mamake.

Nilizipata habari hizi za kusikitisha na kushitua baada ya Sala ya Alasiri, Jumamosi ya Oktoba 19, nikiwa nimejipumzisha sebulini nyumbani kwangu Tuangoma.

Ndugu yangu Mwinyi-Khamis Mussa, kutoka Kariakoo, aliniarifu kwa simu kwamba ‘Maalim Bahiya amefariki Dunia muda mchache uliopita… habari za maziko yake zitatangazwa baadaye’.

Sasa, siku ya Jumapili ya Oktoba 20, ndiyo siku yaliyofanyika mazishi makubwa kabisa ya Mama Mwalim Bahiya, kwenye makaburi ya jamii ya Wangazija, yaliyopo Barabara ya Bibi Titi Mohammed, jijini Dar es Salaam.

Maelfu ya waombolezaji, walilisindikiza jeneza la marehemu, akiwamo Mzee Ali Hassan Mwinyi (rais mstaafu wa Tanzania); Mufti na Sheikh Mkuu wa Tanzania Sheikh Abubakar Zubeir, Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Sheikh Alhad Mussa Salum na Sheikh Mohammed Nassor, ambaye ni Msaidizi Maalumu wa Mufti ambaye pia ni Kiongozi wa Taasisi ya Kusoma na Kuhifadhi Qurani Tanzania, iliyoasisiwa na hayati Sheikh Yahya Hussein.

Wengine waliokuwapo ni pamoja na maimamu wa misikiti mbalimbali, masheikh waandamizi kutoka BAKWATA, walimu wa Madrassa na taasisi mbalimbali za Dini ya Kiislamu nchini, pamoja na ndugu, majirani na wakazi wa jiji la Dar es Salaam.

Ukubwa wa mazishi yale, unafananishwa na maziko mengine makubwa yaliyopata kutokea jijini Dar es Salaam ya hayati Sheikh Idrissa bin Saad, Sheikh Kassim Juma wa Chewa, na yale ya hayati Tambaza Mohammed Tambaza ya mwaka 2011.

Ukiyaondoa mazishi ya Mwalimu Nyerere na Moringe Sokoine, mazishi mengine makubwa ambayo yanaweza kufananishwa na ya Mwalim Bahiya, ni yale ya Sheikh Zubeir Yahya, Sheikh Yahya Hussein, Sheikh Issa bin Ausi na Maalim Abubakar Mzinga.

Wakati mwili wa marehemu ukiwa unazikwa kaburini mwake, maelfu kwa maelfu ya watu walikuwa wamejazana nje ya viwanja hivyo vya makaburi; huku kukiwa hakuna hata nafasi ya kutia mguu.

Wakati huohuo, watu wengine mamia kwa mamia walionekana kwa mbali wakiwa bado wanamiminika sehemu hiyo iliyokwishafurika umati pamoja na magari na vipando vyengine.

Lakini basi, pamoja na wingi huo ulioshuhudiwa kwa upande wa wanaume, mashuhuda wanasema, idadi ya kinamama waliokuja kumsindikiza ‘sheikhat’ wao, iliizidi ile iliyokuwa ya wanaume.

Kule nyumbani, baada ya jeneza kuwa limeshatoka na kuelekea msikitini, mabinti wawili wa almarhum mwalim Bahiya, walitoka kwa nguvu na kuwa wanalikimbiza na kulipungia mkono jeneza lilobeba mwili wa mama yao.

Kwa mujibu wa mpasha habari hizi, mabinti wale walifanya hivyo mpaka jeneza lilipopotea kuelekea barabara ya pili ndipo walipokubali kurejea ndani wakiwa wanalia sana kwa uchungu mkubwa.

Maalima Bahiya (85), alizaliwa Unguja na alihamia Dar es Salaam, kwenye miaka ya mwanzo kabisa ya 1950s, baada ya kuolewa na hayati Maalim Mzee bin Ali Komorian, aliyekuwa mmoja wa masheikh maarufu mjini Dar es Salaam.

Sheikh Mzee bin Ali Komorian na mkewe Bi Mwalim Bahiya, ndio baba na mama mzazi wa hayati Sheikh Ali bin Mzee Komorian (akiijita ‘Sheikh wa Darisalaama’), mmoja wa masheikh wakubwa walioishi kwenye jiji hili, aliyefariki Dunia mnamo mwaka 2015.

Hayati Mwalim Bahiya, ni mwalimu wa walimu wengi wa madrassa wa Jiji la Dar es Salaam, ambao kwa nyakati tofauti walipitia kwenye mikono yake kwa ajili ya kusomeshwa elimu ya Dini ya Kiislamu.

Mara zote amekuwa akijichukulia kama ‘mama mlezi’ wa maustadhi na walimu wa madrassa wanaochipukia ambao daima walikuwa wakimwendea kumtaka msaada huu ama ule katika masuala ya Dini na Dunia.

Aidha, pamoja na madrassa hiyo iliyokuwapo nyumbani kwake, hayati Mwalimu Bahiya, anatajwa pia kwamba aliwahi kufundisha katika shule ya Waislamu ya Aljamiatul Islamiya (sasa Shule ya Msingi Lumumba), kwenye miaka hiyo ya nyuma kabla ya Uhuru wa nchi hii, akiwa mmoja wa walimu wa mwanzo wa kike kufanya hivyo.

Walimu wengine ambao alifundisha nao hapo Aljamiatul Islamiya, ni pamoja na Bi Mgeni (mamake Sheikh Abdallah Awadh); Mwalim Sakina Arab, Mwalim Fatna na Mwalim Bi Kessi.

Kwenye miaka ile ya 1950s mpaka 1960s, jukumu la kutoa elimu ya Dini ya Kiislamu kwa shule zote za msingi za Dar es Salaam, aliachiwa Mwalim Bahiya alikamilishe kwa kujitolea kuifanya kazi hiyo bila malipo—akienda kwa mujibu wa ratiba leo shule hii na kesho shule ile— Mnazi Mmoja, Mchikichini, na Kitchwele Middle Schools.

Bila shaka yeyote, Allah Subhanahu Wataala, atamlipa mama yetu huyu kwa kazi hiyo kubwa aliyokuwa akiifanya ya kuzitembelea shule zote na kukaa pamoja na watoto wadogo wa Kiislamu akiwasomesha misingi ya mwanzo ya Dini –nguzo za Kiislamu, nguzo za imman na hadithi za Mtume.

Nakumbuka kama vile ilikuwa jana, pale shuleni Mnazi Mmoja, nilikopata elimu yangu ya Msingi (1958-1961), nilikuwa nikimwona mama yule akihangaika na watoto wa Kiislamu wapatao 800 walioketi ‘holini’ (ukumbi wa shule) kwa mafunzo ya Dini.

Akiwa mwalimu peke yake kwa kundi lote hilo, ilimuwia vigumu sana; maana kwa kawaida watoto wadogo lazima wafanye fujo hii ama ile; wakati wa kipindi kinapokuwa kikiendelea.

“Eh… jamani tulieni… nyamazeni… wee wacha kumfinya mwenzio wakati huu wa Dini… haya tusikilizaneni wanangu!”Mama yule alikuwa akiwapoza watoto waliopitiliza idadi ya darasa, kuacha mchezo wakati wa kipindi.

Wakati kwenye vipindi vya kawaida darasani idadi ya watoto ilikuwa ni 45 kwa kila mwalimu mmoja; kwenye kipindi cha Dini ya Kiislamu, watoto wote wa Kiislamu wapatao 800 hivi; aliachiwa Mwalimu Bahia peke yake, achakarike nao kwenye ‘holi’ la mkutano la shule.

Mungu alikuwa pamoja naye; siku zikawa zinasonga mbele! Huku wanafunzi wakifurahia kila ujio wake shuleni, maana uliambatana na yeye kuja na ‘kashata’ tamu zilizojaa hiliki na nazi, zilizotengenezwa kwa ustadi mkubwa, alizokuwa akimpa mmoja wa wanafunzi kuzitembeza wakati darasa likiendelea.

Alhamdullilah! Bila ya kuchoka, Mwalimu Bahiya, kila mara aliweza kutumia uzoefu wake wa ualimu na umama; kuwanyamazisha watoto, na hatimaye kupenyeza maneno mawili matatu ya Dini.

Miongoni mwa wanafunzi wake wengi, ambao kwa nyakati tofauti walipitia chini ya mikono yake, ni pamoja na Maalim Abdul bin Mwinyikhamis, ambaye kwa sasa ni Mudir wa Madrassa ya Maalim Mgaya iliyopo Mtaa wa Jangwani.

Wengine ni Sheikh Abbas bin Ramadhani Abbas, Imam Mkuu wa Masjid Mtoro, Kariakoo jijini, ambaye, habari zinasema alikuwa ni mmoja wa watu wa mwanzo kufika pale nyumbani na kuthibitisha kwamba ‘Bi Mwalim’ tayari alikuwa ameshaiaga Dunia.

Wanafunzi wake wengine ni pamoja na Maalim Khamis Bakiri, Sheikh Uwesu Kibosha na hayati Sheikh Zubeir Yahya, mwanazuoni mkubwa aliyekuwa Imam wa Msikiti wa Mtoro katika uhai wake.

Katika uhai wake, Bi Mwalim Bahiya, amekuwa mstari wa mbele katika kuwaombea madua na ‘maghfira’ watu wengi waliokuwa hai, wenye shida na matatizo mbalimbali, pamoja na wale ambao wameshatangulia ‘mbele za haki’.

Daima tumemshuhudia akiongoza ibada za mazishi, khitma, maulid, hakika na zile za kuwatoa wanawake wafiwa ‘eda’ wanapokuwa wamekamilisha miezi 4 na siku 10 ya kusubiria kabla ya kuwa huru baada ya vifo vya waume zao.

“Namkumbuka sana Mwalim Bahiya kwani ndiye aliyekuja kusoma Maulid yangu ya kutoka eda mwaka 1987 baada ya kufiwa na mume wangu,” alisema Bi Zaituni bint Suleiman, mama mzazi wa mwandishi huyu, aliposikia habari za msiba ule mzito.

Sheikh Abdul Ibn Mwinyi-khamis, yeye— pamoja na sifa nyingine kadhaa— amempambanua hayati Maalim Bahiya, kama ni mtu aliyeshiriki katika kuwarehemu na kuwaombea dua— kabla ya kwenda kuzikwa— ‘karibu ya nusu ya maiti wote ambao wamezikwa katika makaburi ya Kisutu na Ngazija, wakati wa shughuli za mazishi yao’.

Uwepo wake lilikuwa ni jambo la kawaida kwenye hafla zote za kike ikiwamo na ile ya Maulid ya Mfungo Sita ya Wanawake wote jijini ambayo hufanyika kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee au Viwanja vya Sabasaba, Mtoni, wilayani Temeke.

Familia ya ‘Bi Mwalim’ Bahiya, akiwamo hayati mumewe Sheikh Mzee bin Ali na mtoto wao hayati Sheikh Ali bin Mzee Komorian, bila shaka yeyote wanayo nafasi ya kipekee katika jamii ya Kiislamu kwa mchango wao mkubwa wa utunzi wa Kaswida, mashairi, utenzi na nyiradi mbalimbali za ibada.

Katika fani hiyo, huwezi kutofautisha baina yao maana Baba Mzee Komorian alikuwa mtunzi wa vitabu mbalimbali vya Dini ya Kiislamu, mashairi pamoja na utenzi (fani ambayo imesahaulika kwa sasa).

Hapo utamkuta Bwana mkubwa yule akiwa katika kiwango sawa na wale magwiji wengine wa lugha ya Kiswahili kama hayati Shaaban Robert, Saadan Abdul Kandoro, Mathias Mnyampala na Salim Ali Kibao.

Mtoto wake mzee huyo, hayati Sheikh Ali Komorian yeye alikuwa na mchango mkubwa sana katika utunzi wa mashairi ya Kaswida mbalimbali za kumsifu Mtume Muhammad, ambazo pamoja na kwamba yeye hayupo tena, lakini Kaswida zake bado ni hazina kubwa aliyowaachia Waislamu wenziwe.

Mwalim Bahiya bint Abdulrahman, leo hatunaye tena. Nafasi yake katika jamii ya Kiislamu jijini Dar es Salaam, itakuwa ngumu kupata mtu mbadala.

Mchango wake katika kuwasaidia watoto yatima, wajane, vikongwe na wasiojiweza ni habari nyingine kubwa ya kupigiwa mfano, kama anavyosimulia mmoja wa vijana wanafunzi wake Ustaadh Bhallo wa Kariakoo:

“Bi Mwalim, amekuwa na kawaida ya kuwalea na kuwahudumia watoto yatima na wale walio kwenye mazingira magumu kwa kugharamia huduma zao zote mpaka kuwasomesha kwenye ngazi za vyuo kwa gharama zake…

“Kamwe hakuwa mtu wa kupokea sadaka bali yeye ndiye aliyekuwa mstari wa mbele kuwasaidia watu waliokwenda kwake kwa shida mbalimbali… hakuna aliyerudi bure au mikono mitupu,”amesema Ustadh Bhallo

Wakati tukimwomba Allah ampe kitabu chake ‘mametu’ huyu kwa mkono wa kulia, ni vyema basi tukamalizia kwa Dua mashuhuri ya lugha ya Kiswahili iliyotungwa na familia ya Komorian, ambaye imekuwa ikisomwa na Sheikh Ali Komorian, kwa mbwembwe na madaha makubwa, katika uhai wake.

Dua hii yenye maombi mazito, ambayo kwa sasa imebaki kama haiba (legacy); imekuwa ikisomwa na Maalim Abdul kutoka Madrassa ya Mgaya kwa namna ileile:

Mikono tumeinua, kukuomba Yakarim,
Utakalo Mola huwa, bila dakika kutimu,

Mabayani utuepue, tusitiri yakarimu.
Yailahi tuepulie, kula baa na fitina,

Maradhi tuepushie, yajayo kula namna,
Mahabani ututie, kwa wakongwe na vijana,

Tumche na Mungu sana, tufe hali Islamu.
Tufe hali Islamu, tumche na Mungu sana,

Yailahi yasatari, tusitiri yalatifu,
Utupe riziki za kheri, viumbe vyako dhaifu,

Tuishi vyema uzuri, kwa hali ya ukunjufu,
Kula baya na machafu, tuepushie Allahu.

Ilahi mwenye huruma, huruma ni sifa yako,
Maasi aliyochuma, si kitu kwa wema wako,

Umtie Allahuma, ndani mwa pepo yako.
Yakarim Yarahym, mlaze mametu peponi.

Ameen!
 
Sio lazima usome shwaini
Mr Chopa,

Umefanya sivyo kumtukana.

Siwezi kukuhukumu lakini nadhani umeghadhibishwa na kule kuona kama vila kamdharau marehemu.

Si kitu.

Lakini kwako ilikuwa ni kumfahamisha kuwa marehemu alikuwa mama na mwalimu wetu ambae mfanowe haujapata kutokea Dar es Salaam na iitachukua miaka mingi kutokea mwalimu kama Bi. Bahia kwani ana wanafunzi katika familia moja kuanzia mume na mkewe na watoto wao na familia nzima wakawa wamesomeshwa Qur'an na yeye tofauti ikiwa ni miaka tu.

Baba na mama wamesomeshwa miaka ya 1950 na watoto miaka ya 1980 na wajukuu miaka ya 2000.

Madrasa ni ile ile na mwalimu ni yule yule na akisomesha bure.

Mwalimu Bahia ana wanafunzi kila pande ya dunia kuanzia Arabuni, Ulaya na Marekani.
Rambirambi nyingi zimepokelewa kutoka kwa wanafunzi wake kila pembe ya dunia na sasa hawa wanafunzi ni watu wazima na wamestaafu kazi.

Hakuna mtu aliyezaliwa Dar es Salaam ile ya 1950s na akakulia katika mazingira yale ambae hakuwa anamjua Mwalimu Bahia.

Mwalimu Bahia alikuwa anaingia katika nyumba za wakazi wa Kariakoo na kwengineko ama kwenye maulid au hakika ya mtoto au kwenye kufiwa.

Bi. Chiku mjukuu wa Bi. Chiku bint Said Kisusa kanitumia ujumbe ananambia kuwa, ''Mwalimu Bahia alikwenda hija na bibi yangu na waliporudi Mwalimu Bahia alikuja nyumbani kuniletea maji ya Zam Zam.

Kabla ya kunipa kunywa alinisomea dua ndefu sana na siku zote nikimpigia simu kuwa naumwa haipiti dakika teksi ishasimama nje ya nyumba yangu anakuja kunitazama basi hapo atanifanyia dua kisha ndiyo aniage.''

(Bi. Chiku bint Said Kisusa nimeweka paicha yake hapa akiwa uwanja wa ndege yeye na Bi, Tatu bint Mzee na Bi. Titi Mohamed wakimsindikiza Mwalimu Nyerere safari ya kwanza UNO 1955).

Hivi kwa mukhtasari hivi ndivyo alivyokuwa Mwalimu Bahia hadi umauti ulivyomfika.

Ndugu yetu hakuwa anamjua mwalimu na mama yetu Bi. Bahia na ndiyo fedhuli na dharau ile.

Tusimlaumu kwani Dar es Salaam ile si hii ya leo na si kila mtu kapitia malezi tuliyofunzwa sisi ya kuwa na subra, staha kwa umjuaye na usiyemjua.
 
Heci,

Ndugu yangu, kulikua na sababu gani kuandika haya yote mkuu? Si bora ungenyamaza kuliko kuandika haya hasa wakati wenzetu wanaomboleza na wapo kwenye majonzi ya mpendwa wao?

JF iko huru mtu kuandika anachotaka bila kutweza na kudhalilisha wengine. Ungeweza kuchagua kuandika habari za hao ambao ungependa watu wafaham taarifa zao bila kumshambulia mleta habari.
 
Mimi ni KAFIR ama MGALATIA

Haya nijibuni enyi wauminin

Alipokuwa hedhi huyu Bibi alimkabidhi nani mikoba yake?


Ukafiri wako upoje, kwanza elezea ndipo tukujibu, mfano mtu anapoitwa mwizi ni lazima awe kaiba kitu fulani.
 
Back
Top Bottom