Pdidy
JF-Expert Member
- Nov 22, 2007
- 50,974
- 22,166
Tanesco yaibuka na tahadhari mpya yataka Sh312 bilioni kununua mitambo
Na Leon Bahati
BAADA ya kimya cha muda mrefu, Shirika la Umeme (Tanesco) limeibuka na kuiangukia Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini ikiomba iikingie kifua ili itengewe Sh312 bilioni kwa ajili ya kununulia mitambo ya kuzalisha umeme wa dharura nchini, huku ikitahadharisha kuwa nchi inaweza kuingia gizani.
Shirika hilo limeamua kuachana na Wizara ya Nishati na Madini, ikidai kuwa ilishawasilisha maombi hayo muda mrefu, lakini ikaona hayafanyiwi kazi ndio maana limeamua kuyapeleka maombi hayo ya dharura kwenye kamati hiyo ili iikingie kifua.
Tanesco, ambayo sakata lake la kutaka kununuliwa kwa mitambo ya kuzalisha umeme wa dharura ya Dowans Tanzania Limited, lilizimwa na kamati hiyo ya Bunge, limesema kama serikali haitaharakisha mpango huo mapema, kuna hatari ya nchi kuingia gizani kwani tayari baadhi ya vituo vya umeme nchini vimezidiwa nguvu ya matumizi kwa asilimia 10.
Akiwasilisha ombi hilo mbele ya kamati hiyo, jana, mkurugenzi mtendaji wa Tanesco, Dk Idris Rashidi alisema upungufu huo wa umeme tayari umesababisha kuanza kwa mgawo wa umeme kwenye mikoa ya Kanda ya Ziwa na sasa tatizo hilo linaunyemelea mkoa wa Arusha.
Alisema mahitaji ya fedha hizo ni kwa ajili ya nakisi ya Sh44.23 bilioni kwa ajili ya kukamilisha seti za jenereta 12 zitakazozalisha umeme wilaya za Kasulu, Loliondo, Kibondo na Sumbawanga, Sh161 bilioni kwa ajili ya mtambo wa kuzalisha megawati 100 utakaowekwa Ubungo na Sh107 bilioni kwa ajili ya mtambo unaotumia mafuta mazito utakaowekwa Mwanza, ukitegemewa kuzalisha megawati 60 za umeme.
"Tanesco inaomba angalau Sh312 bilioni katika kipindi cha mwaka 2009/10 kukamilisha miradi hiyo ya umeme wa dharura. Inashauriwa fedha hizi zipatikane kwa wakati ili kukamilisha jitihada hizi kubwa kabla ya mwishoni mwa Juni, 2010," inasema taarifa ya Dk Rashidi.
Mkurugenzi huyo wa Tanesco alikabidhi ombi hilo kimaandishi kwa mwenyekiti wa kamati hiyo ya Bunge, William Shelukindo, ambaye ni mbunge wa Bumbuli kwa tiketi ya CCM na kusihi Bunge liipigie debe ili serikali iridhie kuipa fedha hizo.
Akifafanua ombi ya shirika lake, Dk Rashidi alisema ombi siyo geni kwa serikali, akiwa na maana kwamba tayari alishaliwasilisha, lakini akasema utekelezaji wake umekuwa ni wa kusuasua.
Hivyo, akaitaka Kamati ya Nishati na Madini iongeze nguvu ili serikali iidhinishe fedha hizo katika mwaka ujao wa fedha 2009/2010.
Alisisitiza serikali kupitisha fedha hizo mapema kwa sababu mchakato wa kununua mitambo hiyo mipya huchukua zaidi ya mwaka hadi kuwasili nchini na kuanza kufanya kazi.
Shelukindo alipokea ombi hilo lililokuwa kwenye karatasi yenye kurasa tatu na kuahidi kuwa kamati yake, italijadili na kuweka mikakati ya kuishinikiza serikali, ilitekeleze.
Kamati hiyo ilipokea ombi hilo wakati ikiwa njiani kwenda kutembelea kituo cha kuzalisha umeme wa megawati 45 kilicho Tegeta wilayani Kinondoni.
Ombi hilo, Tanesco imeligawanya katika sehemu tatu ambazo zinahusisha ununuzi wa jenereta 17 kwa maeneo ambayo hayafikiwi na mtandao wa gridi ya taifa na mitambo miwili, mmoja kwa ajili ya kuzalisha umeme kituo cha Ubungo jijini Dar es Salaam na mwingine Mwanza kwa ajili ya Kanda ya Ziwa.
Kuhusu suala la jenereta 17, Dk Rashidi alisema kuwa bunge tayari liliidhinisha kwenye bajeti ya mwaka 2008/2009, lakini kiwango cha fedha kilichotolewa kilitosha kununua jenereta mbili tu ambazo zinatarajia kuanza kufanya kazi mkoani Kigoma kabla ya Juni, mwaka ujao.
Dk Rashidi alisema Tanesco inahitaji Sh44.23 bilioni kwa ajili ya kununua jenereta 12, ambazo zitagawanywa katika miji ya Loliondo, Kasulu, Kibondo na Sumbawanga.
Zabuni ya kununua jenereta hizo, alisema Dk Rashidi, ilitolewa kwa kampuni ya M/S Zwart Techniek Januari mwaka huu na ilikuwa ikamilishwe ndani ya miezi 15 kwa mkataba wa Sh59.5 bilioni.
Mradi wa pili kwenye ombi hilo ni wa kununua mtambo wa megawati 100 inaotumia gesi asilia, ambao utagharimu Sh161 bilioni.
Dk Rashidi alisema kuwa lengo la mtambo huo ni kukidhi mahitaji ya umeme katika kipindi cha mwaka 2009/2010.
Mradi wa tatu ni wa kununua mtambo wa megawati 60 unaotumia mafuta ambao utawekwa Mwanza na ambao utaigharimu serikali Sh107 bilioni.
Dk Rashidi alisisitiza kuwa mitambo ya umeme kwenye Kanda ya Ziwa tayari inaelemewa kutokana na mahitaji ya umeme kuzidi kwa asilimia 10 ya uwezo wake.
Kwa sababu hiyo, alisema tayari wameanza kutoa umeme kwa mgawo eneo hilo.
Lakini alisema mradi huo ni wa dharura tu kwa sababu Tanesco inatengeneza njia ya Umeme kutoka Iringa hadi Shinyanga na inatarajia utakamilika katika kipindi cha miaka mitano, kuanzia 2010 hadi 2014.
Ombi hilo la Tanesco limekuja miezi michache baada ya vuta nikuvute iliyosababisha malumbano juu ya kununua ama kutonunua jenereta mbili za kuzalisha umeme wa dharura zinazomilikiwa na Kampuni ya Dowans ambayo ilirithi zabuni ya kuzalisha umeme wa dharura kutoka Kampuni ya Richmond Development Limited LLC iliyoshinda zabuni hiyo kwa utata.
Hata hivyo, serikali ilifikia uamuzi wa kutonunua jenereta hizo zilizokuwa zinauzwa kwa Sh90 bilioni na zenye uwezo wa kuzalisha megawati 100, badala yake ikaahidi kununua mpya.
Waliokuwa wanashawishi ununuzi wa jenereta hizo, walisema kuwa bado zipo katika hali nzuri, ni za bei nafuu na tayari zinafanya kazi badala ya kutumia muda mrefu kuziagiza hadi kuzifunga.
Lakini Kamati ya Shelukindo ilisema Sheria ya Manunuzi ya Umeme inakataza serikali kununua vitu vilivyokwishatumika.
Na Leon Bahati
BAADA ya kimya cha muda mrefu, Shirika la Umeme (Tanesco) limeibuka na kuiangukia Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini ikiomba iikingie kifua ili itengewe Sh312 bilioni kwa ajili ya kununulia mitambo ya kuzalisha umeme wa dharura nchini, huku ikitahadharisha kuwa nchi inaweza kuingia gizani.
Shirika hilo limeamua kuachana na Wizara ya Nishati na Madini, ikidai kuwa ilishawasilisha maombi hayo muda mrefu, lakini ikaona hayafanyiwi kazi ndio maana limeamua kuyapeleka maombi hayo ya dharura kwenye kamati hiyo ili iikingie kifua.
Tanesco, ambayo sakata lake la kutaka kununuliwa kwa mitambo ya kuzalisha umeme wa dharura ya Dowans Tanzania Limited, lilizimwa na kamati hiyo ya Bunge, limesema kama serikali haitaharakisha mpango huo mapema, kuna hatari ya nchi kuingia gizani kwani tayari baadhi ya vituo vya umeme nchini vimezidiwa nguvu ya matumizi kwa asilimia 10.
Akiwasilisha ombi hilo mbele ya kamati hiyo, jana, mkurugenzi mtendaji wa Tanesco, Dk Idris Rashidi alisema upungufu huo wa umeme tayari umesababisha kuanza kwa mgawo wa umeme kwenye mikoa ya Kanda ya Ziwa na sasa tatizo hilo linaunyemelea mkoa wa Arusha.
Alisema mahitaji ya fedha hizo ni kwa ajili ya nakisi ya Sh44.23 bilioni kwa ajili ya kukamilisha seti za jenereta 12 zitakazozalisha umeme wilaya za Kasulu, Loliondo, Kibondo na Sumbawanga, Sh161 bilioni kwa ajili ya mtambo wa kuzalisha megawati 100 utakaowekwa Ubungo na Sh107 bilioni kwa ajili ya mtambo unaotumia mafuta mazito utakaowekwa Mwanza, ukitegemewa kuzalisha megawati 60 za umeme.
"Tanesco inaomba angalau Sh312 bilioni katika kipindi cha mwaka 2009/10 kukamilisha miradi hiyo ya umeme wa dharura. Inashauriwa fedha hizi zipatikane kwa wakati ili kukamilisha jitihada hizi kubwa kabla ya mwishoni mwa Juni, 2010," inasema taarifa ya Dk Rashidi.
Mkurugenzi huyo wa Tanesco alikabidhi ombi hilo kimaandishi kwa mwenyekiti wa kamati hiyo ya Bunge, William Shelukindo, ambaye ni mbunge wa Bumbuli kwa tiketi ya CCM na kusihi Bunge liipigie debe ili serikali iridhie kuipa fedha hizo.
Akifafanua ombi ya shirika lake, Dk Rashidi alisema ombi siyo geni kwa serikali, akiwa na maana kwamba tayari alishaliwasilisha, lakini akasema utekelezaji wake umekuwa ni wa kusuasua.
Hivyo, akaitaka Kamati ya Nishati na Madini iongeze nguvu ili serikali iidhinishe fedha hizo katika mwaka ujao wa fedha 2009/2010.
Alisisitiza serikali kupitisha fedha hizo mapema kwa sababu mchakato wa kununua mitambo hiyo mipya huchukua zaidi ya mwaka hadi kuwasili nchini na kuanza kufanya kazi.
Shelukindo alipokea ombi hilo lililokuwa kwenye karatasi yenye kurasa tatu na kuahidi kuwa kamati yake, italijadili na kuweka mikakati ya kuishinikiza serikali, ilitekeleze.
Kamati hiyo ilipokea ombi hilo wakati ikiwa njiani kwenda kutembelea kituo cha kuzalisha umeme wa megawati 45 kilicho Tegeta wilayani Kinondoni.
Ombi hilo, Tanesco imeligawanya katika sehemu tatu ambazo zinahusisha ununuzi wa jenereta 17 kwa maeneo ambayo hayafikiwi na mtandao wa gridi ya taifa na mitambo miwili, mmoja kwa ajili ya kuzalisha umeme kituo cha Ubungo jijini Dar es Salaam na mwingine Mwanza kwa ajili ya Kanda ya Ziwa.
Kuhusu suala la jenereta 17, Dk Rashidi alisema kuwa bunge tayari liliidhinisha kwenye bajeti ya mwaka 2008/2009, lakini kiwango cha fedha kilichotolewa kilitosha kununua jenereta mbili tu ambazo zinatarajia kuanza kufanya kazi mkoani Kigoma kabla ya Juni, mwaka ujao.
Dk Rashidi alisema Tanesco inahitaji Sh44.23 bilioni kwa ajili ya kununua jenereta 12, ambazo zitagawanywa katika miji ya Loliondo, Kasulu, Kibondo na Sumbawanga.
Zabuni ya kununua jenereta hizo, alisema Dk Rashidi, ilitolewa kwa kampuni ya M/S Zwart Techniek Januari mwaka huu na ilikuwa ikamilishwe ndani ya miezi 15 kwa mkataba wa Sh59.5 bilioni.
Mradi wa pili kwenye ombi hilo ni wa kununua mtambo wa megawati 100 inaotumia gesi asilia, ambao utagharimu Sh161 bilioni.
Dk Rashidi alisema kuwa lengo la mtambo huo ni kukidhi mahitaji ya umeme katika kipindi cha mwaka 2009/2010.
Mradi wa tatu ni wa kununua mtambo wa megawati 60 unaotumia mafuta ambao utawekwa Mwanza na ambao utaigharimu serikali Sh107 bilioni.
Dk Rashidi alisisitiza kuwa mitambo ya umeme kwenye Kanda ya Ziwa tayari inaelemewa kutokana na mahitaji ya umeme kuzidi kwa asilimia 10 ya uwezo wake.
Kwa sababu hiyo, alisema tayari wameanza kutoa umeme kwa mgawo eneo hilo.
Lakini alisema mradi huo ni wa dharura tu kwa sababu Tanesco inatengeneza njia ya Umeme kutoka Iringa hadi Shinyanga na inatarajia utakamilika katika kipindi cha miaka mitano, kuanzia 2010 hadi 2014.
Ombi hilo la Tanesco limekuja miezi michache baada ya vuta nikuvute iliyosababisha malumbano juu ya kununua ama kutonunua jenereta mbili za kuzalisha umeme wa dharura zinazomilikiwa na Kampuni ya Dowans ambayo ilirithi zabuni ya kuzalisha umeme wa dharura kutoka Kampuni ya Richmond Development Limited LLC iliyoshinda zabuni hiyo kwa utata.
Hata hivyo, serikali ilifikia uamuzi wa kutonunua jenereta hizo zilizokuwa zinauzwa kwa Sh90 bilioni na zenye uwezo wa kuzalisha megawati 100, badala yake ikaahidi kununua mpya.
Waliokuwa wanashawishi ununuzi wa jenereta hizo, walisema kuwa bado zipo katika hali nzuri, ni za bei nafuu na tayari zinafanya kazi badala ya kutumia muda mrefu kuziagiza hadi kuzifunga.
Lakini Kamati ya Shelukindo ilisema Sheria ya Manunuzi ya Umeme inakataza serikali kununua vitu vilivyokwishatumika.