Tamko la Kamati Kuu ya Chadema: Jan 31 Jan, 2011

Baba Tina

Senior Member
Dec 22, 2010
131
2
Chama cha demokrasia na maendeleo (chadema) kimesema hakiko tayari kukishirikisha chama kilichoko serikalini kwenye kambi ya upinzani. Katibu mkuu wa chama hicho amesema chama hicho cha chadema kiko tayari kuvishirikisha vyama vingine kwenye kambi hiyo endapo vitasitisha uhusiano na chama cha CUF ambacho kinaunda serikali ya zanzibar pamoja na chama cha mapinduzi.

Source: TBC news leo usiku

================================


TAMKO LA KIKAO CHA KAMATI KUU YA CHAMA CHA DEMOKRASIA NA MAENDELEO (CHADEMA) KUHUSU HALI YA TAIFA.

Kamati Kuu ya CHADEMA katika kikao chake cha kawaida kilichofanyika tarehe 29-30 Januari 2011 jijini Dar es Salaam chini ya Mwenyekiti wa Taifa Mheshimiwa Freeman Aikael Mbowe (Mb), pamoja na mambo mengine, imepokea, kujadili na kutolea maazimio Taarifa ya Hali ya Siasa na Taifa kwa ujumla. Maazimio haya yapo katika maeneo matano yafuatayo.

1. Mchakato wa Upatikanaji wa Katiba Mpya.

Kamati Kuu imezingatia na kupongeza juhudi za Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni pamoja na wadau mbalimbali wa demokrasia nchini za kudai Katiba Mpya. Aidha, Kamati Kuu imejadili na kutafakari kwa kina maoni ya wadau mbalimbali juu ya mchakato unaofaa katika kupata Katiba Mpya, na kuzingatia kuwa njia sahihi ni ile itakayowashirikisha wananchi kikamilifu na kwa dhati bila kujali tofaui zao za kisiasa, dini, umri, elimu, kabila wala jinsia zao. Kamati Kuu imezingatia pia kwamba Tume ya Rais sio njia sahihi itakayowezesha upatikanaji wa Katiba Mpya yenye kuzingatia utashi, matakwa na mahitaji ya wananchi wa Tanzania. Hivyo basi:

  1. Kamati Kuu imepinga utaratibu wa kuunda Tume ya Rais katika uundaji wa Katiba Mpya
  2. Kamati Kuu imeunga mkono utaratibu wa kutumia Bunge katika kutengeneza na kusimamia mchakato utakaoletekeza upatikanaji wa Katiba Mpya
  3. Kamati Kuu imeipongeza Sekretariati yake kwa kumwagiza Mheshimiwa John Mnyika kuandaa na kuwakilisha Hoja Binafsi inayolitaka Bunge kuandaa sheria itakayoweka utaratibu na mchakato wa upatikanaji wa Katiba Mpya
  4. Kamati Kuu imewahimiza na kuwaomba wabunge wote wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuunga mkono Hoja Binafsi ya Mheshimiwa Mnyika kwa maslahi ya Taifa.

2. Mauaji yaliyofanywa na Jeshi la Polisi Jijini Arusha

Kamati Kuu imepokea kwa masikitiko taarifa ya vifo vya wananchi watatu wasio na hatia kwa kupigwa Risasi na askari wa Jeshi la Polisi kufuatia vurugu zilizosababishwa na Jeshi hilo katika harakati zao za kuzuia maandamano halali na yenye Baraka zote za Kamanda wa Jeshi la Polisi Wilayani Arusha. Aidha, Kamati Kuu imesikitishwa na uvurugwaji wa uchaguzi wa Meya wa Jiji la Arusha kulikofanywa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Arusha kwa maelekezo ya Chama cha Mapinduzi na Serikali yake. Katika maazimio yake:

  1. Kamati Kuu imewapa pole ndugu wa wafiwa wa vurugu za Arusha pamoja na wananchi wa Arusha na watanzania kwa ujumla
  2. Kamati Kuu imewapongeza Mwenyekiti wa Taifa wa CHADEMA, Mhe Freeman Mbowe, Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk Willibrod Peter Slaa, Mbunge wa Arusha Mjini Mhe Godbless Lema na viongozi wengine wa CHADEMA kwa juhudi zao kubwa za kuepusha shari na kutoa uongozi wa kisiasa pale ambapo wananchi wa Arusha walitelekezwa na viongozi wa Serikali ya CCM katika kipindi chote cha matatizo ya Arusha
  3. Kamati Kuu imeiagiza sekretariati ya CHADEMA kuendelea na harakati za kudai haki za wananchi wa Jiji la Arusha kwa njia za kisiasa.
  4. Kamati Kuu imewaagiza madiwani wa CHADEMA katika Halmashauri ya Jiji la Arusha kuendelea kuingia katika vikao vya Baraza la Halmahauri hiyo na kuwawakilisha wananchi waliowachagua kikamilifu na wahakikishe kuwa wanatumia nafasi yao kufanikisha uchaguzi wa Meya.

3. Matatizo ya Nishati ya Umeme na Gesi na Malipo kwa Kampuni Hewa ya Dowans

Kamati Kuu imesikitishwa na kupanda holela kwa bei za nishati muhimu za umeme na gesi, pamoja na kushindwa kwa serikali ya CCM katika kuwekeza kikamilifu katika sekta ya nishati hapa nchini. Aidha, Kamati Kuu imesikitishwa na kufadhaishwa sana na uamuzi wa CCM na serikali yake kuridhia kuilipa Kampuni hewa ya Dowans fedha za walipa kodi wa Tanzania zipatazo Shilingi bilioni 94, pamoja na kwamba Kampuni hii ilikwishaharamishwa na Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa niaba ya wananchi.

Kamati Kuu imetambua kuwa sakata la Dowans ni mwendelezo wa vitendo vya kifisadi ndani ya CCM na serikali yake ambavyo vimeligharimu taifa hili kwa miongo mitano iliyopita. Hivyo basi:

  1. Kamati Kuu imewahimiza wana CHADEMA, wabunge na wananchi kwa ujumla kuendelea kupinga kwa nguvu zote malipo ya Dowans
  2. Kamati Kuu imewaelekeza viongozi pamoja na wabunge wa CHADEMA kuendelea kuwahamasisha wananchi kupinga kwa njia mbalimbali za kisiasa na kisheria malipo ya Dowans na ufisadi mwingine hapa nchini
  3. Kamati Kuu imewapongeza na kuwashukuru wanaharakati wa taasisi za kiraia kwa ujasiri na moyo wao wa kizalendo kwa uamuzi wao wa kufungua kesi mahakamani ya kupinga malipo ya Dowans
  4. Kamati Kuu imeiasa Serikali ya CCM kutokuona aibu kutekeleza sera za CHADEMA zilizofanyiwa utafiti kuhusu namna ya kujenga na kuimarisha sekta ya nishati ya umeme na gesi hapa nchini ili nchi yetu iondokane na tatizo la kudumu la umeme.
  5. Kamati Kuu imeiagiza Secretariat yake kuanza maandalizi ya maandamano ya nchi nzima ya kupinga ongezeko la bei ya umeme, gesi na kuilipa Dowans. Na tarehe 24/02/2011 itakuwa siku ya kuanza maandamano kwenye Jiji la Mwanza na miji mingine kadiri ratiba itakavyotolewa.

4. Matokeo ya Kidato cha Nne

Kamati Kuu imeyapokea kwa masikitiko makubwa matokeo ya Kidato cha Nne yanayoonyesha kuwa nusu ya watahaniwa wote wamefeli Mtihani huo. Aidha, Kamati Kuu imezingatia na kusikitishwa na taarifa kuwa ni
asilimia 11.5 tu ya watahiniwa ndio waliopata daraja la I hadi la III. Ndio kusema kuwa karibu asilimia 90 ya vijana wote waliomaliza kidato cha nne mwaka 2010 hawawezi kuendelea na elimu yeyote ya juu na itakuwa ni vigumu sana kwa vijana hawa kupata aina yeyote ya ajira ya uhakika.

Aidha, Kamati Kuu imezingatia kuwa matokeo mabaya ya Kidato cha Nne yamesababishwa na sera dhaifu za serikali ya CCM zenye kulenga kughilibu wananchi kwa ajili ya mafanikio ya kisiasa kwa kukazania wingi wa majengo ya shule badala ya ubora wa walimu na ubora wa shule. Kutokana na hali hii:

  1. Kamati Kuu imeyatangaza matokeo ya Kidato cha Nne ya mwaka 2010 kuwa ni Janga la Kitaifa
  2. Kamati Kuu imeitaka Serikali ya CCM isione aibu kutekeleza sera za elimu za CHADEMA zilizoanishwa katika ilani yake ya mwaka 2010, ikiwemo sera ya kutoa elimu bure na kuboresha maslahi na mazingira ya kazi ya walimu ambazo zilielezwa na wataalamu wa elimu kwamba ndio sera sahihi za kufufua ubora wa elimu ya nchi yetu
  3. Kamati Kuu imeunda timu maalumu ya wataalamu wa elimu kwa ajili ya kutafiti kwa kina sababu za matokeo mabaya ya Kidato cha Nne na kutoa mapendekezo yake kwa Kamati Kuu katika kikao chake kitakachofanyika kabla ya Mwezi Mei 2011.

5. Kuhusu propaganda za udini hapa nchini

Kamati Kuu imesikitishwa na propaganda zinaendelezwa na viongozi wa juu wa Chama cha Mapinduzi, hususani Rais Kikwete, kuhusu kuwepo kwa mfarakano wa kidini hapa nchini. Kamati Kuu imezingatia kuwa wananchi wa Tanzania wameendelea kuishi kwa amani, upendo na mshikamano mkubwa bila kujali tofauti zao za kidini. Kamati Kuu imezingatia kuwa Viongozi wa juu wa CCM, na hasa Rais Kikwete, ameamua kuficha udhaifu wake wa kiuongozi chini ya zulia la udini ili wananchi waache kujadili mambo ya msingi ya Taifa hili, ikiwemo kushindwa kwa CCM kutekeleza ahadi ambazo imekuwa ikizitoa katika miongo mitano iliyopita. Hivyo basi:

  1. Kamati Kuu imewahimiza wananchi wa dini zote hapa nchini kuendelea kuishi kwa amani na mshikamano na kushirikiana katika shughuli mbalimbali za kiuchumi na kijamii bila kujali tofauti zao za dini, ukabila wala itikadi ya siasa
  2. Kamati Kuu imewataka viongozi wa juu wa CCM na hasa Rais Kikwete kuacha kuchochea mgawanyiko wa dini hapa nchini kama njia ya kuficha udhaifu wake wa uongozi
  3. Kamati Kuu imewahimiza viongozi wa dini zote hapa nchini kuendelea kukemea maovu yeyote katika jamii bila woga wala upendeleo kwani hilo ni jukumu lao la msingi.

6. Kuhusu Ushirikiano wa Vyama vya Siasa vya Upinzani

Kamati Kuu imeendelea kuzingatia umuhimu wa vyama vya siasa kushirikiana katika kuimarisha nguvu ya upinzani hapa nchini. Hata hivyo, Kamati Kuu imezingatia kuwa
Chama cha Wananchi (CUF) wamejiunga na CCM kuunda Serikali ya Umoja Kitaifa Zanzibar, na kwa kuwa Sheria inayoruhusu uwepo wa vyama vya siasa inahusu pande zote za Muungano, na kwa kuwa vyama vingine vya upinzani vyenye wabunge wamo katika ushirikiano na CUF, Kamati Kuu imeona kuwa CHADEMA haiwezi kuwa na ushirikiano wenye tija na vyama hivyo. Hivyo basi Kamati Kuu imemwagiza Kiongozi wa Kambi ya Upinzani kuunda Baraza la Kivuli kwa kuhusisha wabunge wa CHADEMA pekee.




7. Kuhusu mpango mkakati wa chama 2011-2016.

Kamati Kuu ilijadili na kupitisha mapendekezo ya mpango kazi wa chama kwenye Baraza kuu la chama .Pia ilijadili na kupitisha mpango kazi wa mwaka 2011-2012.

Tamko hili limetolewa leo tarehe 31/01/2011.

Dk Willibrod Peter Slaa
Katibu Mkuu


================================
 
Safi sana. Afadhali sasa tunaweza kujikita kwenye mambo mengine. CUF nao kwa nini wanang'ang'ania kuwa na Chadema wakati chenyewe ni chama kikomavu kinachoweza kufanya siasa peke yake? Mambo kama haya wangefanya TLP na UDP wenye mbunge mmoja mmoja
 
Its hard to understand ila yote kheri tu, tunataka wabunge imara na sio wababaishaji. Kushirikiana sio ishu kubwa maana hata kwenye kura still ccm watapita tuu.
 
Chama cha demokrasia na maendeleo (chadema) kimesema hakiko tayari kukishirikisha chama kilichoko serikalini kwenye kambi ya upinzani. Katibu mkuu wa chama hicho amesema chama hicho cha chadema kiko tayari kuvishirikisha vyama vingine kwenye kambi hiyo endapo vitasitisha uhusiano na chama cha CUF ambacho kinaunda serikali ya zanzibar pamoja na chama cha mapinduzi. Source: TBC news leo usiku.
 
kwa mujibu wa taarifa ya habri radio one ya saa mbili hakika nimefurahishwa na tamko la chadema na nimeona sasa ukombozi wa nchi umekaribia jamani ni vyema tukatoa taarifa kwa wapenzi na wanamageuzi kwa ujumla
 
Tafadhali koleza zaidi taarifa; je hayo maandamano ni ya nini na yanafanyika maeneo gani ya nchi?
 
Maandamano yanalenga wapi? Manake hii nchi ina matatizo mengi wala sijui tuanze kupinga lipi!
 
Uh,at last!
Ninge washangaa sana kushirikiana na chama tawala kwenye kambi ya upinzani
 
Chama cha ukweli na maamuzi ya ukweli yaliyojaa busara. Asanteni kwa zawadi ya kuwatosa CCM_B viongozi wetu wenye mlengo wa kuona mbali daima
 
Ni kweli kwani hata maandamano ya CUF yanayotangazwa kufanyika sidhani kama Maalim Seif ambaye ni katibu mkuu wa chama hicho atashiriki. Ninaona kiukweli hii ni dosari kubwa kwani kambi inatakiwa iwe na usiri mkubwa wa mambo yake naunga mkono washirikiane na vyama vingine vya siasa vilvyobaki.
 
Habari haijakamilika hebu jaribu kutujuza vizuri maana umegusa kwenye hisia za wadau wengi wenye hasira na nchi hii. Tunataka kujua maandamano yatafanyika wapi na kwa madhumuni yapi hasa?
 
Back
Top Bottom