Takukuru yawinda rushwa Bandari

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,299
33,082
Hosea%20E%283%29.jpg

Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Dk. Edward Hoseah.



Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa nchini (Takukuru) imesema kuwa inatambua kuwepo kwa vitendo vya rushwa katika Bandari ya Dar es Salaam na kwamba imejipanga kupambana navyo ili bandari ichangie kuongeza mapato ya serikali.
Kauli hiyo ilitolewa na Mkurugenzi Mkuu wa Takukuru, Dk. Edward Hoseah, jijini Dar es Salaam jana wakati akifungua warsha ya Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) kwa kushirikiana na Takukuru ambayo ilikuwa ikijadili njia za uboreshaji wa ufanisi katika utendaji wa bandari.
Dk. Hoseah alithibitisha kuwepo kwa rushwa katika bandari ya Dar es Salaam na kwamba hali hiyo inachangia kukosekana kwa ufanisi wa huduma.
Alisema kuwa bandari hiyo ina uwezo mkubwa wa kuiongezea serikali mapato na kwamba warsha hiyo itasaidia kubaini matatizo yote yanayojitokeza yakiwemo ya rushwa.
Alisema serikali imekuwa ikitegemea bandari katika kujikwamua na umasikini, lakini kumekuwa na malalamiko ya mara kwa mara kuhusu rushwa, jambo ambalo hurudisha nyuma maendeleo.
Dk. Hoseah alisema kuwa jukumu la kudhibiti rushwa halipo kwa Takukuru pekee bali wadau mbalimbali wanatakiwa kusaidiana nayo ili kutokomeza vitendo hivyo vinavyoathiri maendeleo ya nchi.
Aidha, alisema kwa kuwa taasisi yake imeshatambua kuwepo kwa vitendo vya rushwa bandarini na wamejipanga katika kudhibiti tatizo hilo ili kuhakikisha nchi inapata maendeleo ya kiuchumi.
“Siwezi nikasema hakuna rushwa bandarini kwani kuna vifaa mbalimbali vinakuwa vinaibiwa kwa mfano, gari linatolewa unakuta kioo hakipo au redio imetolewa je, vinatolewaje, na kwa upande wa getini vifaa hivyo vinapitishwaje wakati walinzi wapo kama sio rushwa inafanyika?” alihoji Dk. Hoseah.
Alisema chanzo cha rushwa kinapatika kwenye mkusanyiko wa watu wengi pamoja na mzunguko wa fedha hivyo sehemu kama hiyo ya bandari haiwezekani pakosekane rushwa.
Alisema kuwa kuna baadhi ya watu wanamtuhumu kwamba Takukuru haifanyi kazi vizuri, jambo ambalo alikanusha na kusema kuwa tuhuma hizo sio za kweli.
Dk. Hoseah alisema mpaka sasa wamekamatwa watu 18 wanaojihusisha na kesi kubwa za rushwa na kwa upande wa kesi ndogo zipo 420 na tayari zimeshaanza kusikilizwa katika mahakama mbalimbali nchini.
Aliongezea kuwa tangu uhuru hakujawahi kuwa na kesi nyingi za rushwa kama hizo, hivyo taasisi yake imafanya kazi kwa ufasaha katika kuhakikisha rushwa inadhibitiwa ili kuleta maendeleo.
Wakati huo huo, Dk. Hoseah alisema kuwa mazungumzo baina ya serikali ya Uingezeza na Tanzania yanaendelea vizuri kuhusu urejeshwaji wa fedha za ununuzi wa rada Sh. bilioni 60.
Alisema kuwa kwa sasa wapo kwenye mchakato wa kuhakikisha fedha hizo zinarudishwa Tanzania.
Dk. Hoseah alisema mazungumzo yanaendelea vizuri baina ya serikali hizo mbili na kwa sasa kinachosubiriwa ni kufikia makubaliano kuhusu chombo ambacho kitakabidhiwa fedha hizo.
Alisema suala hilo linashughulikiwa na ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa.
Hata hivyo, alisema suala la kurudishwa kwa fedha hizo linaweza kuchukua muda kutokana na taratibu.
Serikali ya Tanzania inataka fedha hizo zipokelewe na serikali wakati Uingereza inataka zipitie mashirika ya kujitolea.
Kauli hiyo ilitolewa na Dk. Hoseah ikiwa imepita miezi kadhaa tangu kampuni ya kutengeneza zana za kijeshi ya Uingereza, BAE Systems, kukubali kulipa faini ya Dola za Marekani milioni 450 ili kumaliza kesi mbalimbali zilizokuwa inaikabili kutokana na udanganyifu wa kuuza zana za kijeshi kwa nchi kadhaa duniani, Tanzania ikiwamo.
BAE Systems iliamua kulipa kiasi hicho cha fedha ili kumaliza kesi zilizofunguliwa dhidi yake na Ofisi ya Makosa Makubwa ya Jinai ya Uingereza (SFO) pamoja na Wizara ya Sheria ya Marekani.
BAE System iliiuzia Tanzania rada ya kijeshi kwa bei ya pauni za Uingereza milioni 28 takribani dola za Marekani milioni 60, huku kiasi cha dola milioni 12 zikitolewa kama rushwa. Kumekuwa na tuhuma dhidi ya waliokuwa maofisa kadhaa wa Tanzania kuhusishwa na rushwa hiyo.
Katika fedha za fidia, Wizara ya Sheria ya Marekani, italipwa Dola milioni 400, wakati SFO watalipwa Dola milioni 47.
Fedha za SFO zitakwenda kwa nchi, ambazo zilikuwa zikiendesha uchunguzi kuhusu biashara zilizofanywa na BAE System, ikiwamo Tanzania, Jamhuri ya Czech, Romania na Afrika Kusini.



CHANZO: NIPASHE
 
Well; nawapongeza pamoja na kuwa wamechelewa saaaaaaaaaaaaaaaaana; kikukbwa ni matokeo chanya, ndicho watanzania wanachosubiri!
 
Back
Top Bottom