Sweden yaibana zaidi Tanzania

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,299
33,079
Friday, 04 June 2010

staffan.jpg


Mwandishi Wetu


BALOZI wa Sweden aliyememaliza muda wake, Staffan Herrstrom jana alitoa hotuba kali ya kuitaka serikali kutekeleza ahadi inazozitoa, ikiwemo kuwafikisha mahakamani watuhumiwa wote wa kesi kubwa za rushwa na kuondokana na utamaduni wa kulipana posho.

"(Serikali) isiache hata jiwe moja juu ya jiwe jingine," ameeleza balozi huyo katika hotuba yake iliyokuwa na ujumbe mzito kwa serikali wakati wa hafla ya maadhimisho ya siku ya Sweden ambayo ilitumiwa kumuaga.


Katika hotuba hiyo kali inayosisitiza msimamo wa Sweden katika vita dhidi ya rushwa, Balozi Herrstrom alitaja mambo mawili makubwa na muhimu katika kuondoa umaskini ambayo yanatakiwa kushughulikiwa kuwa ni utekelezaji wa maamuzi yaliyokwishafikiwa na sera pamoja na haki za watoto.


Hotuba yake imekuja zaidi ya wiki moja baada ya Sweden na nchi nyingine wahisani kutangaza kuzuia theluthi moja ya mchango wao kwenye bajeti kuu ya serikali ya Tanzania, kufuatia kutoridhishwa na kasi ya utekelezaji wa masuala kadhaa, ikiwa ni pamoja na kubadilisha mfumo wa usimamizi wa fedha za umma na utekelezaji wa mazimio yaliyofikiwa wakati wa kusaini makubaliano ya kutoa fedha hizo.


Nchi hizo zilitangaza kuwa zimezuia Sh297 bilioni kwenye bajeti kuu ya serikali ya mwaka 2010/11 na kwamba, zinaendelea na mazungumzo na serikali, huku zikisema kuwa iwapo serikali haitatekeleza ahadi zake fedha hizo ambazo ni za walipa kodi wa nchi hizo zitahamishiwa kwa taasisi zisizo za kiserikali ili ziendelee kusaidia katika kupunguza umaskini.


Jana Balozi Herrtsron, ambaye nchi yake inachangia dola 45 milioni za Marekani kwenye bajeti hiyo, alikuwa mkali zaidi.


"Tekelezeni nia iliyoelezwa ya kushughulikia kesi zote kubwa za rushwa mkihakikisha kuwa watuhumiwa wote wa rushwa wanafikishwa mahakamani na kesi zote zinatolewa maamuzi muafaka. Iwe ni moja au zote, bila ya kuacha jiwe moja juu ya jingine," alisema balozi huyo katika hafla hiyo.


Kauli hiyo imetolewa wakati vita dhidi ya rushwa ikionekana kupoa, huku watuhumiwa wa rushwa kubwa wakianza kujitokeza hadharani baada ya kupotea kwa kipindi kirefu kutokana na kuelekezewa tuhuma kali kwa takriban miaka miwili.


Baada ya wahisani kuzuia fedha kwa mara ya kwanza takriban miaka mitatu iliyopita, serikali iliamka na kuwafikisha mahakamani watu wanaotuhumiwa kuiba fedha kwenye Akaunti ya Malipo ya Madeni ya Nje (EPA), kushughulikia ubadhirifu wa fedha za walipa kodi kwenye Benki Kuu ya Tanzania (BoT), kwa kuwafikisha mahakamani watuhumiwa na kushughulikia tuhuma za rushwa kwenye wizara iliyosababisha mawaziri wawili wa zamani kufikishwa mahakamani.


Lakini hatua hizo za serikali zimeonekana kutowagusa watuhumiwa wakubwa hasa kwenye suala la EPA, ambalo baadhi ya watuhumiwa walipata msamaha wa Rais baada ya kutakiwa kurejesha fedha hizo kabla ya Novemba mwaka 2008, huku tuhuma nzito kama za Meremeta Gold zikiwa hazijashughulikiwa kisheria.


Hata hivyo, vita hiyo inaonekana kupungua nguvu na wahisani wameonyesha kuwa na wasiwasi na mwenendo huo, ikiwemo Sweden.


Balozi Herrstrom, ambaye mapema wiki hii alizungumzia ugoigoi huo wa serikali katika kutekeleza ahadi zake, alizungumzia pia uhuru wa habari katika hotuba hiyo.


"Tekelezeni ahadi zote mlizotoa za kupata njia ya kisasa itakayohakikisha haki ya kupata habari inakuwepo; kuwepo kwa uhuru wa vyombo vya habari na hivyo kuwa na uwazi na uwajibikaji, kutekeleza mabadiliko sita muhimu yanayotakiwa kwa haraka sana, kama mabadiliko katika serikali za mitaa na usimamizi wa fedha za umma" alisisitiza balozi huyo.


"Tekelezeni azma mliyoeleza ya kuachana na utamaduni wa kulipana posho ambao ni hatari sana katika suala la ufanisi na utawala."


Balozi huyo pia ameitaka serikali kuwasilisha muswada wa Sheria ya Watoto na kusema: "Tafadhali tekelezeni ahadi mliyoweka ya kuruhusu wanafunzi wanaopata mimba ambao wanakuwa wazazi mapema, kuendelea na shule badala ya kutimuliwa hivyo kunyimwa haki yao ya kupata elimu".


Alisema jambo la pili muhimu ni haki za watoto, akitaka walindwe, wasikilizwe na kupewa uwezo na kutaka adhabu kali dhidi ya watoto ziondolewe.


"Tuweke ahadi ya pamoja kwa niaba ya watoto wa nchi hii. Watoto wote wa Tanzania Bara na Zanzibar wasipigwe na tuhakikishe kuwa Zanzibar inakuwa na sheria nzuri ya haki za watoto kabla ya uchaguzi mkuu," alisema.


Hotuba yake ya jana haitofautiani sana na hotuba aliyoitoa mwezi mmoja uliopita katika mkutano wa kitaifa wa kupambana na rushwa ulioandaliwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa(Takukuru), jijini Dar es Salaam.


Katika mkutano huo, Balozi Herrstrom alisema hakuna nafasi ya kupunguza kasi katika vita dhidi ya rushwa na kuitaka serikali kumsikiliza Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu (CAG) na kwamba ifanyie kazi mambo yote yanayoibuliwa na ofisi hiyo katika mwaka uliopita na kutekeleza mapendekezo yake.

Sweden yaibana zaidi Tanzania
 
hapo viongozi wetu hawajasikia..utafikiri wamezibwa masikio.....hiyo ndo perception ya nchi yetu nchi za nje,...hata akipanda ndege kwenda kutalii na kukinga bakuli kama alivyofanya kwenye misafari yake ya ajabuajabu, wanamcheka na kumshangaa sababu kama hizi....
 
Back
Top Bottom