The Hidden Truth ( Ukweli Uliofichika)
MTUNZI: Akida Siri Rambao
Contact: 0658328596
Email:
akidasiri@gmail.com
SEHEMU 1 (C): JINAMIZI LA SIKITIKO.
Mandal Hil Hospital, Kinondoni -Dar es Saalam
Ilipoishia
... daktari aliivua miwani na
kuiweka katika meza huku akiwa bado kashikilia karatasi la Winifrida kisha akaendelea “Majibu kidogo yameenda tofauti na historia yako mama” Winifrida moyo ukamlipuka Puuh!daktari alimtazama Winifrida, Winfrida akajikuta akifumba macho kwa nguvu huku moyo ukimzidi mapigo akaanzakulegea huku mikono ikishika tumbo lake la mshtuko...
Tuendeleeee....
Mheshimiwa Richard akamtupia macho mkewe akionekana kutokuelewa sentensi ya daktari, daktari akauma midomo
yake na kuiachia kwa pamoja, “Mama kizazi kinaonekana kimeathirika sana, na sababu kuu ya uathirikaji huu ni
utolewaji wa mimba kadhaa katika maisha yako hii ni mbaya sana” Winifrida alichukua kitambaa chake kidogo katika
mkoba wake na kujiwekea usoni akilia taratibu. Richard macho yakamtoka asijue la kufanya mapigo ya moyo yakaanza kubadili kasi yake ya kawaida “…na kitu kingine ni kuwa kizazi chako kwa sasa kimelegea, hizo ndio kesi mbili ambazo zimepelekea kutokushika mimba kwa muda wote huo mlio ishi pamoja” aliongea daktari. Richard akashika kichwa
kana kwamba amefiwa na mtu muhimu katika maisha yake, hasira zikampanda maradufu macho yakawa mekundu huku
kajiinamia hakujua afanye nini, ‘Mke wangu kwanini hukuniambia siri hii ya kutoa mimba jamani fedheha gani hii’
Richard alijiwazia, ‘Mume wangu nisamehe sikujua kama itafikia hatua hii mimi najuta bora ningekwambia mapema…lakini ningekwambia usingenipenda nani angenithamini, nani angenisomesha mimi, nani Richard wangu?' walikuwa wakiongea kupitia nafsi zao bila kutambua.
Winifrida alihisi kizunguzungu kwa taarifa hiyo mwili ulishindwa kujizuia kichwa kikiendelea kumuuma na kuwa kizito moyo wote ulichakaa kwa huzuni ya moyo na wasiwasi, daktari akaendelea “Lakini nitamuandikia dawa ambazo atazitumia kwa kipindi huku mkihudhuria maonano na daktari husika mara kwa mara kujua maendeleo yake huendasiku za usoni akapata ujauzito nani anajua, maana Mungu ni mkubwa sana na tuzidi kumuomba maana ni mwingi wa huruma na mwingi wa msamaha” aliongea kwa masikitiko.
Winifrida alitamani ayeyuke atokezee ulimwengu mwingine kabisa kwa uchungu aliokuwa nao na aibu maana aliona
amemvua nguo mumewe mbele ya ulimwengu. ‘Fadhira zote ulizonifanyia mumewe wangu leo nakulipa madudu hivi
maumivu ya aina hii, kwanini nisife?’ Winifrida alijiongelea nafsini, daktari akaendelea “Lakini nawaomba jambo moja msije mkaleta mfarakano kutokana na tukio hili wengi sana wakishamaliza na kuondoka hapa mapenzi na wanandoa wao yanapotea wengi wanaachana, wanasalitiana na hata wengine kujiua kwa sababu tu hawezi kuzaa…” Winifrida alinyanyua kichwa na kumtazama dokta kwa huzuni, ‘Ulijiuaje dokta kuhusu hisia zangu’ alijiongelea tena Winifrida “…Mkaemkijua watoto ni baraka toka kwa Mola, yeye ndiye humpa anaemtaka na humnyima anaemtaka na kumpa wakati anaotaka yeye mwenyewe, vipimo na madawa vipo ilikurahisisha mambo na uchunguzi ili kuweza kujua jinsi ya kutatua matatizo na kuyajua matatizo kama ilivyotokea, hivyo nawasihi sana nyinyi bado ni vijana tena ni watu maarufu
muende na mkawe mfano” dokta Abdi alimaliza, Richard akanyanyuka na kumpa mkono dokta bila kusema kitu akapokea karatasi alimtazama mkewe sekunde kadhaa kama mtu anae tamani kusema jambo huku akiwa kasimama
“Nyanyuka tuondoke” aliongea Richard huku akiwa wa kwanza kutoka, usoni akiwa na hasira ya waziwazi.
Nelson Mandela Road – Dar es Salam.
Ndani ya gari ya aina ya Mitsubish Lancer Winifrida alikuwa ni mtu wa kulia tu alilia mfano wa mtoto mdogo aliye na njaa
na kiu kikali japo hakutoa sauti lakini kilio chake cha kimya kimya kilileta hisia kuwa amezidiwa uchungu. Kilio chake
kilimpelekea macho kumvimba na kuwa mekundu. Richardyeye alionekana kama mtu asiye jali hali ya mkewe wala
hakujigusa, hakujipa nafasi ya kumtazama wala kumuongelesha mkewe tangu walipo toka hospitali na kuitiagari yake funguo, hakutia neno hata moja katika safari hiyo
yeye alikuwa macho mbele kama tochi huku akijinyusa nyusa tu kila wakati. Sura ya Richard ilionekana kukunjamana kama
karatasi iliyo kosa kazi na kukunjwa au kumfananisha na mtu aliyelamba ndimu au kunusa kitu chenye harufu mbaya.
Winifrida mara moja moja alimtupia macho mumewe kiwiziwizi lakini alichokutana nacho aliuona upweke na kuzidisha uchungu unaochoma ndani kwa ndani usioisha wala kupata nafuu huku tumbo likimsokota haswa.
PURPLE in Hotel, Temeke, Kurasini - Dar es Salam.
Kipindi Winifrida akiwa kaegemeza kichwa kwenye kioo cha mlango wa gari akashtushwa na breki kali sana iliyomfanya mwili kusukumwa mbele “Paaap” ilikuwa ni msaada tu wa mkanda wa usalama laa sivyo chochote kingetokea. Baada ya mshituko akaanza kuangaza kupitia katika kioo cha gari na
kuanza kuzirudisha kumbukumbu vizuri mwisho akaishia kusoma kibao kikubwa kilicho kaa pembeni mwa bustaniupande wa mbele ya gari walilopanda, “PURPLE in Hotel …mmh” alijigunia kwa sauti huku akiwa na wasiwasi na mshangao. Richard mikono ikiwa imeshikilia usukani wa gari
kichwa kakiinamisha akihema hovyohovyo, taratibu akatoa mikono katika usukani akajishika kichwa chake nakujiegemeza katika kiti alichokalia, macho akayafumba, zikapita dakika tano nzima pakiwa kimya ndani ya gari. “Naomba unifate tafadhali” Richard aliuvunja ukimya akaufungua mkanda na kutoka katika gari, Wini yeye hakuwa na lakufanya zaidi ya kufata amri ya mumewe huku maswali yakiendelea kumtawala ‘Purple in Hotel kuna nini? kwaniniisiwe nyumbani, na kwanini’ alijiuliza nafsini, Usilo lijua ni
usiku wa giza.
Richard alisogea hadi katika sehemu ya mapokezi huku akipokea salamu za watu waliomfahamu na wasio mfahamu
mahala hapo, baada ya kufika na kuongea maneno mawili matatu na mhudumu akatoa kiasi cha pesa taslim toka
kwenye waleti na kumpatia Mhudumu aliyekuwa mahala hapo akaegema na kuanza kuandika kitu, Mhudumu na yeye
akaikabili simu na kuiweka sikioni akiongea kitu kisha akarejesha sehemu yake. Richard akiwa mwingi wa mawazo
mkewe akiwa hatua kadhaa nyuma akimuangalia kwa kujiiba akiwa “Habari Mheshimiwa…” ilisikika sauti mgongoni mwa Richard na kumshitua akageuka na kumtazama kijana mtanashati aliyevalia sare za Hoteli hiyo “Ooh salama” alijibu “Mnaweza nifata tafadhari” aliongea tena kijana huyo na kuongoza njia huku akifatwa nyuma na Richard pamoja na
mkewe.
Richard aliendelea kujifuta maji kichwani na taulo huku akiwa anaufunga mlango wa bafu kipindi hicho Winifrida kajikalisha
na kujiinamia kwenye kona ya kitanda akiwa kama alivyo kuwa hakuvua wala kuvaa chochote. Richard akamsogelea
mkewe na kukaa karibu yake kwa huzuni kubwa, akamtazamamkewe kwa kumkagua vizuri kana kwamba ni mtu mwenye kumfananisha akabaki kutingisha kichwa chake kuonesha anakataa hali anayoiona au kuihisi kuwa sikweli “Samahani naomba nikuongeleshe tafadhari” alijikuta akiyatoa maneno hayo toka katika kinywa chake huku akimuangalia mkewe.
Winifrida aliyasikia maneno hayo akaunyanyua uso wake na kumtazama mumewe kwa aibu huku akikwepesha macho yake yasikutane na mumewe. “Hivi ni wewe kweli, niWinifrida wangu kweli wewe? Unajua umenikosea sana mke wangu!” maneno hayo yalipenya na kuingia kwenye masikio moja kwa moja hadi katika sakafu ya moyo wa Winifrida na yakatibua fukuto la uchungu lililokuwa limepoa poa kwa vijidakika kadhaa tangu wafike Hotelini hapo yakaleta mchafuko wa moyo. Winifrida alianza upya kulia yani kiasi cha kumshangaza mumewe ambae ndiye aliyekosewa “Wewe una nini unanikejeli au vipi?” Richard alishindwa kuzuia hasira zake alipaza sauti yake nzito juu na kumtazama kwa mshangao akanyanyuka alipo kaa na kusimama huku kajishika kiuno, Winifrida aliteremka taratibu na kukaa katika sakafu huku akilia kimya kimya akayasimamisha magoti yake huku kichwa kakiinamisha, “Nisamehe mume, Rich naona aibu, naona haya mimi kukuita mume wangu kwa dhambi nilizofanya nyuma ya mgongo wako sikukwambia mimi…” winifrida alijifuta machozi na kujikaza kuongea, “Sikujua kama yatafikia hapa, nikweli nilikuongopea historia ya maisha yangu asilimia hamsini sio ya kweli” Richard alimtupia macho ya hasira mkewe “…ila tangu umenioa miaka minne iliyopita, sijawahi kukudanganya nimekuwa nikiishi ndani ya ukweli na uwazi wa kila jambo kwako hiyo ndio ahadi niliyoiweka katika maisha yangu na wewe ni shahidi ” Winifrida akaangua kilio cha chini chini bila kunyamazishwa na mumewe aliye jisimamia pembeni akiwa kampa mgongo “Nipo tayari kuyakubali maamuzi yako mume wangu na hiyo itakuwa ndio adhabu inayo nifaa…” Richard alishtuka na kugeuka kumtazamaa mkewe kwa mshangao, “Ila kabla hujaamua chochote nataka kukupa ukweli mmoja kuwa sijawahi kumpenda mwanaume yoyote zaidi ninavyokupenda… nashukuru nimeweza kufurahia na kuridhika kwa mara ya kwanza ndani ya ndoa yangu”aliongea Winifrida kwa sauti ya mtetemo machozi yakimwagika macho ya Richard yalionekana kupata wingu la machozi uso sasa ukafunguka toka katika mikunjo kunjo ya ndita kwenye paji la uso, “Nilipata ujauzito mara kadhaa na wote walionipatia walipotea wote na kila mmoja alikuja na uongo wake na mimi nilikuwa muhitaji wa pesa kama ulivyokuta hali ya uchumi kwetu haikuwa shwari mzee wangu alivyokuwa mgonjwa gonjwa ningefanyaje?” aliongea tena Winifrida akiwa kapiga magoti akajifuta kamasi na machozi sasa yamekata na sauti imekauka inatoka kama mtu anae
nong’ona akaendelea “Mimi nilikupenda mwenyewe na nilikuvutia mwenyewe na wala sikuwa na tamaa na pesa zako,
na nilitamani uwe wangu maisha yote, sikupenda ughalimike kwa ajili yangu ila uliamua ukanisaidia, nilikufurahia sana
asante kwa hilo” Richard picha ikamjia jinsi alivyomkuta siku za mahusiano yao machanga alipokuwa anahudhuria siku za mwisho wa wiki katika mji wa Tanga, kumbukumbu ilimchosha akatingisha kichwa kuivuruga maana ilimuumiza
taratibu akajikuta anarudi kujikalisha katika kitanda kama zigo lililotupwa kwa kususwa “Puuuh”. Wini akaendelea
“Nilitamani nikuambie ukweli lakini uchafu wangu ungeujua ingekuwaje isingekuwa rahisi kunioa ungenitelekeza tu kama
wale wengine, niliogopa sana kukukosa niliogopa kukwambia niliogopa mimi” Winifrida alijikuta anatingisha kichwa
kusikitika, “Wewe ni mwanaume wa kipekee sana mume wangu, najivunia kuwa nawe, sasa nasubiri hukumu yako na nitaikubali bila kinyongo” Winifrida aliongea nakunyamaza shingo imeinama kama mtu anayesubiri kuchinjwa, Richard
alibaki kuwaza na kuwazua aamue lipi, saa zima na nusu likapita akiwaza tuu. ‘Ni mwanamke uliyenifunza nini maana
ya kupenda na maana ya penzi la dhati sasa mbona umeniumiza kiasi hiki, sijawahi jua uchungu wa penzi kumbe
inauma kiasi hiki?’ alibaki akijiwazia. Ushauri wa dokta kuhusu hali halisi na kukabiliana ilianza kuranda randa katika
kichwa chake ikijirudia rudia ‘Mungu wangu nifanyaje mimi siwezi kumuacha mke wangu siwezi’ Richard alijisemea
moyoni na kunyanyuka haraka haraka na kumkumbatia mkewe kwa masikitiko makubwa sana kiasi cha kumshangaza
sana Winifrida, wote wakaanza kuangua kilio cha huzuni huku wakiwa wamekumbatiana, ama kweli penzi ni kitu kisicho na mfano katika ulimwengu wote. Mabembelezano yalienda na walikuja tahamaki saa tatu usiku, wakaamua kuondoka zao.
Msasani, Kinondoni -Dar es Saalam
Mke na mume wakiwa kitandani wamejilaza kila mmojaakiwa na lake aliwazalo mke akajipindua na kuanza kuongea“Mume wangu unajua nina hofu na uoga sana juu ya dada zako, mama yako, jamaa zako na hata marafiki zako
watanichukuliaje maana dunia hii haina siri” aliongea Winifrida akageuka na kumtazama vizuri mumewe, “Mke
wangu sisi ndio tulio oana sawa? halafu kama Mungu ameamua tusipate hatutapata na kama amepanga tupate
tutapata, tena sasa huwenda tukapata mtoto mzuri mwenye hekima na busara hapo baadae” Richard aliongea na kuachia tabasamu jembamba na kukaza macho kuashiria kumaanishamaneno yake. Winifrida akatabasamu na kujivuta zaidi kwa mumewe, kwa pamoja wakajiweka sawa kuukaribisha usingizi.
Kijiji cha Mtamba, Matombo - Morogoro.
Majira ya saa nne asubuhi hivi, nje ya nyumba ya kisasa kwenye baraza walionekana wanawake watatu, wawili
walikuwa bize wakitembea kwa kupishana huyu akienda na huyu akirudi mikono kiunoni kichwa sakafuni mara wamekaa
mara wamesimama, walionekana wazi vichwa vyao vimebeba mzigo wa hasira kutokana na jazba walizokuwa nazo nyusoni, Lakini watatu wao mama wa makamo ya miaka hamsini mpaka kwenye siti yeye alikuwa kajiegemeza ukutani katika kibaraza hicho, kiganja chake cha mkono wa kuume alikigandisha shavuni mwake mguu mmoja kaukunja na
mwingine kunyooshwa. Mama huyo mtu mzima alibaki kujisikitikia tu aliwatazama wanawake hao waliokuwa mbele
yake kwa wakati huo walikoma kutembea wakabaki wamesimama na kuanza kunesa nesa kama wasoma ngonjera
waliokuwa wakitambiana kwa zamu.“…Mama sisi kesho piga ua lazima twende Dar”, ukimya wa muda mfupi ulivunjwa na
mmoja wao, mama wa watu alitoa kiganja cha mkono shavuni na kunyanyua uso wake kuwatazama kwa zamu wanawake
hao walio mbele yake “Sawa ila nawaomba sana wanangu msiende bila kumtaarifu kaka yenu” mama huyo mtu mzima
alikunjua mguu wake na kuunyoosha kwa mbele, “Nani?..sisi?...aaah mama hilo sahau” mwingine alidakia, alikuwa pande la mwanamke wa maji ya kunde, alionekana kufanana sana na mama huyo, maana alimchukua kila kitu.
“Hakuna cha taarifa wala nini sisi tumeshaaga waume zetu na wewe tumekuletea taarifa tu na sio kutaka ushauri au ruhusa, mwanamke mbaya sana yule bila shaka amempa limbwata
kaka yetu” alimaliza na kugeuza shingo kutazama pembeni mikono kiunoni huku akichezesha mguu kwa hasira. “Sawa
wanangu ila tu nawaomba msiende kumfanyia fujo wifi yenu sawa Ester?” Mama wa watu akageuka kumtazama mwanawe mkubwa aliyekuwa kachukizwa mno amejitazamia pembeni “Mama sikiliza, mimi na dada Ester tumekuletea wajukuu wangapi mpaka sasa je vipi mwanao wa kiume? Je! unajiskia raha sio mtu mheshimiwa eeh anasifa kubwa nchini kazi kumwaga hela za misaada tu kwa watu nani atazirithi mali zake? Sisi tumeshaamua ukitaka ni hivyo usipotaka ni hivyokwaheri” aliongea Ester kama cherehani akashika njia huku akiifunga vizuri kanga yake kiunoni, Eva nae hakukaa akafata nyuma na kumuacha mama huyo akiwasindikiza kwa machoya mshangao wakiingia ndani. Mama wa watu mawazo yakamchukua na kumkumbuka mumewe mzee Edward Kobero, kumbukumbu hizo hazikumuacha macho makavu mama huyo akajikuta akijifuta michozi na utuuzima wake kweli “Ukimuona mtu mzima analia ujue kuna jambo” Mama huyo akiwa bado jamvini alinyanyua kichwa kutazama nyumba anayoishi, ilikuwa nyumba ya kipekee sana na nzuri kuliko nyumba zote kijijini hapo, “Eeh Mungu msaidie mkwewangu dhidi ya shambulio la wanangu” alijisemea.
Ni kweli kilikuwa ni kitu cha kuhuzunisha sana kwa mama huyo wa watoto watatu, masikini alibahatika kupata mtoto
mmoja tu wa kiume kama wa dawa vile ambaye alimsomesha kwa pesa za kuungaunga tena kipindi kile alipo kuwa analimamboga mboga na matunda na kwenda kuuza Morogoro mjini,
alimkumbuka sana marehemu mumewe. Mumewe mzee Edward Kobero alikuwa anajishughulisha na kazi ya ulinzi
alishikwa na umauti baada ya kukosa matibabu stahiki ya jeraha la mguu lililotokana na shambulio la majambazi katika harakati za kujaribi kulinda mali ya bwana Mohammed Seifalijikuta akipigwa risasi ya paja, kwa uhaba wa hospitali na
pesa za kutosha kwa kipindi kile na kesi iliyomkabili toka kwa muajiri wake kwa kuhusishwa na wizi huo ikampelekea
kupatwa na umauti akiwa chumbani kwake.
Msasani, Kinondoni -Dar es Saalam.
Sauti za magari na milio ya ndege wakiimba nyimbo za kushukuru kuingia kwa siku mpya zilisikika kwa mbali toka
katika nyumba ya kipekee mfano wa kasri iliyokuwa ikitajwamiongoni mwa nyumba nzuri kuwahi kutokea nchini, kila apitaye aliishia kuitupia macho ya matamanio na kuishia na ndoto za alinacha. Wapendanao hao wakiwa sebureni pahala pa meza ya chakula Winifrida alilichukua koti la suti lililoegemezwa kwenye kiti kimoja wapo na kumvalisha mumewe ambaye alikuwa kasimama huku mdomo ukicheza cheza kumalizia chakula “Mke wangu basi usisahau kunywa dawa tafadhali sawa” Richard aliongea huku akiendelea kupitisha mkono huu na mkono ule katika mikono ya koti la suti alilokuwa anavalishwa na mkewe “ Usihofu mume wangu nitakunywa” Winifrida aliongea kwa tabasamu pana huku akiendelea kumuweka kola sawa mumewe, “...alafu kama kawaida yako umeacha chai kwenye kikombe” winifrida aliukunja mdomo kwa juu huku macho yakiwa katika kikombe katika meza ya chakula iliyokuwa karibu nao na kusitisha zoezi. “Mmh haya nipatie” aliongea Richard huku
akitabasamu na kukichukua kikombe mkononi mwa mkewe fundo moja tu akamliza chai yote akaitupia macho saa ya mkononi mwake “Saa mbili na robo sasa” aliongea kishaakamsogelea mkewe na kumpiga busu shavuni. “Unajua
siamini kama leo tumeikosa ibada hivi hivi mume wangu”“Wala usihofu sina budi kuufanya huu mkutano ni muhimu
sana… tena leo niandalie ugari wa dona nimeumisi sana,”Richard aliongea huku akiwa tayari ameshaufikia mlango
mkubwa wa kutoka nje. “Haya sawa take care Honey” “You too”. Winifrida akasogea hadi katika mlango akatoa kichwa
kumuangalia mumewe akiondoka, alibaki akitabasamu tuhuku paji la uso likiegemea mlango.
Baada ya Masaa kazaa.
“Habari za Ulimwenguni toka katika izaya ya kiswahili ya DeutscheWellemjini Boni mimi ni Ukhty Zukheirah Abdallah, Katika tarifa ya habari mchana huu, marekani yasitisha mashirikiano yake na Urusi juu ya Syria, wakati Uturuki ikiongeza muda wa hali ya hatari hadi mwakani na ripoti
ya Amnesty International ikifichuwa kwamba ni mataifa kumi tu duniani
yenye uchumi usiozidi asilimia mbili nukta tano...” sauti hiyo ilitokea katika redio ndogo iliyopakatwa kwenye mapaja na
bwana aliyevalia sare macho yakiwa
yameikodoloea redio masikio yamemsimama yakitega kila neno toka redioni akiwa juu ya kiti cha plastiki. Mara
akashtushwa na sauti ya geti ikigongwa kwa nje bira mpangilio kiasi cha kumfanya kukunja sura na kulitupia jicho la hasira geti lakini uso ukiwa hauna uhakika maana si kwa kugongwa huko, akatulia na kutegesha masikio shingo kaipindisha mkono ukiwa katika redio akipunguza sauti kuhakikisha kelele hiyo ya geti anaisikia vizuri, alipotambua kuwa ni kweli kuna mtu anagonga geti sura ikazidi kukunjamana. Akatazama katika kifaa maalumu kwenye ukuta kikionesha wanawake wawili na mabegi yao, alitulia
akabonyeza kitufe pembeni yake “Nyinyi kina nani na mna shida gani? Kwani hamja ona kitufe cha kengere mnagonga
hodi kama kuna ugomvi” aliongea na kusikilizia “Dada zake mheshimiwa Richard tufungulie au sio hapa” ilisikika sauti ikitokea katika kifaa hicho ukutani. “Subirini kidogo…" aliongea bwana huyo na kugeuka tayari kuondoka “Jumaa
kuna nini hapoo” Wini akiwa anarejesha mlango na kusimama aliongea kwa sauti “Kuna wanawake wawili wanasema ni
dada zake kaka Rich…” Wini akiwa amesimama moyo ukamlipuka kiasi cha kupeleka mkono kifuani akijizuia “…Je!
Niwaruhusu?” aliongea Jumaa ‘Mungu wangu wamefata nini tena?’ Wini alijiongelea nafsini, kabla hajapata jibu la swali lake Jumaa akaongea “…niwaruhusu waingie?” Wini akameza fundo la mate la uchungu lililopita kwa tabu kooni, mkono
ukiwa bado katika kitasa “Waruhusu” aliongea na kurudi ndani kinyonge. Juma akabofya sehemu na geti likajifungua
kwa umeme mambo ya teknolojia, wadada wawili hao wakaingia, “Hivi wewee kisa cha kutuweka masaa muda wote
nini hasa” Eva aliongea kwa ukali huku macho yakiwa kwa Jumaa hii ni baada ya kupiga hatua kazaa ndani ya uzio wa
ukuta wa matofali ulio nakshiwa vizuri na kupendeza.“Samahani mnisamehe siwatambui mimi ni mpya hapa
nilikuwa nauliza kwanza” Jumaa alijitetea “Alafu unaonekana mshamba mshamba imekuwaje kaka akakuweka mtu kama
wewe hapa mtu simple simple tu khaa!” Eva aliongea akimtazama kwa dharau, Jumaa kwa makini alibaki kumtazama wazi akionekana kuchukizwa machoni “Wote wapo?” Eva aliuliza “Aliyekuwepo ni dada Winifrida kaka Richard yeye alitoka tangu asubuhi” Jumaa alijibu akificha
macho yake asibainishe hasira zilizomuandama wakati huo,
“Shoga twende zetu” Eva alimgusa bega ndugu yake na kuongoza njia kuufuata mlango. “Ooh mawifi hao karibuni
jamani” Winifrida aliiweka rimoti katika meza akanyanyuka kwa furaha kuwasogelea wageni wake. Ester akamuangalia Winifrida kwa jicho la dharau huku kasimama, akampandisha
akamshusha “Fsyuuuuu…naona unajitanua tu kwa raha zako” Ester aliongea kwa majivuno. Winifrida alihisi mwili kupatwa
na baridi alihisi shari ikimnyemelea lakini akajizuia “Eeh bibi si unajua tena…” Wini alichombeza akinyoosha mkono
kulichukua begi la Ester macho yakiwa kayainamisha chini.‘Eeeh Mungu nipe usalama’ Winifrida alijisemea katika nafsi
yake “Fatuma njoo uchukue begi lingine unifate tafadhari”aliongea Wini huku akianza kulivuta, wakati huo Fatuma
akimfata alipo. Kisha akarudi, “Karibuni wifi zangu jisikieni mpo nyumbani” Wini alisogea pembeni na kukaa “Hivi we
mwanamke kwa kaka yetu ulichokikosa ni nini” Wini alishtushwa “Wifi Ester una maana gani sijaelewa” “Huelewi?
huelewi nini we mwanamke mchawi sana wewe” Ester safari hii aliamua kusimama kwa ghadhabu jicho limemtoka kwa
hasira kidole kakinyoosha kwa Wini, Wini alibaki kabung’aa tu kama mtu asiejielewa. “Sikiliza wewe kinyago cha mpapule tumekuvumilia tumechoka sawa tunataka utuambie kwanini umemroga kaka yetu, unachotaka hasa nini?” Eva nae alijinasua kwenye sofa na kumsogelea Wini akampiga singi
takatifu lililomfanya Wini kuinamia mto wa Sofa uliokuwa pembeni yake. Wini bado alikuwa hajang’amua kitu aliwaza
na kuwazua kipindi akiwa bado kajiegemeza kwenye mtokwenye sofa machozi yakimlengalenga kinachomaanishwa na wifi zake hakukipatia jawabu.
Fatuma alionekana kujiminya katika ukuta akishuhudia kila kitu juu ya mawifi
wakimshambulia Wini, alionekana kujiskia vibaya sana alitamani kwenda kumsaidia kulipiza mashambulizi lakini moyo ulimzuia “Eva mbona unazunguka zunguka tu…” Ester alimsogelea Wini karibu na kumuweka kati kama mwanamke
anae sutwa “…Sikiliza wewe mwanamke sisi tumechoka tunahitaji kuitwa mashangazi haiwezekani miaka kibao hii
umejikalia kama jiwe tu hujiskii vibaya mwanamke wewe” Winifrida alijivuta vuta kichovu na kukaa kitako, alijiinamia,
alijishika kichwa akiwaza maana safari hii tayari alishaelewa maana ya ujio huo nyumbani kwake. Uchungu uliendelea
kumjaa aliona wazi mwisho wake tayari ushafika hana msaada dunia sasa imeshaanza kumtazama alihisi kuchekwa
na kuzomewa na watu wengi, “Mwanamke jeuri huyu halafu hana haya huoni aibu? Hivi hujui Kama thamani ya mwanamke ni mtoto unajua nina hasira sana na wewe na tumekuja kistaarabu tunataka utulete watoto uliowafichamchawi wewe sisi kwetu tuna uzazi ukae na ulijue hilo”. Eva aliongea kwa uchungu sana karibia kutoa machozi, “Hebu fikiria ingekuwa wewe ndio dada yake ungejiskiaje eeh…” Ester aliongea nakumtia singi wifi yake lililopindisha shingo ya Winifrida “Tunachokiamini ni kuwa wewe ni mchawi habari zako tunazo kwa hiyari yako chagua kuondoka au laa sivyo…” Winifrida alinyanyuka kabla Eva hajamalizia kuongea akatoka mkuku mkuku akaziparamia ngazi kupanda juu kwa kasi kiasi cha kuwashangaza wifi zake wakabaki kutazamana.
“Na safari hii utaondoka tu na bado alaaaa” Eva alimrushia maneno na kweli yalimfikia Wini kabla hajaingia chumbani
kwake yalishadakwa na masikio yalikuwa kama mkuki maana yalimuingia moyoni akahisi kuna kitu kimekaa katika koo lake
kinamzuia kuhema aliufungua mlango na kuingia.
Masikini dada wa watu nguvu zilionekana kumuishia alijiona ni mtu aliyepoteza kitu cha thamani katika maisha yake na kutokana na kupoteza kwake basi nae thamani yake imeshuka daraja,hana thamani alijitupa kitandani na kuanza kumwaga kilio, kitanda hakikufaa alijinyanyua na kusogelea kioo cha kabati
huku akiendelea kulia na kujitazama alivyo umbwa “Masikini mimi nimeshajiaribu mimi ooh Mungu wangu” alijisemea kwa
uchungu mara likamjia wazo, alionekana kuanza kuhema hovyo hovyo alikurupuka na kukimbilia katika droo za kabati alitoa kila kitu na kutupa chini hakuambulia kitu akarudi katika nguo alizitoa na kuzikung’uta ili apate kitu ambacho
kinaweza kusaidia kutoa uhai wake. Baada ya kuambulia mikono mitupu akagutuka akasogelea kwenye dressing table
akachukua kisturi na kusogelea kabati akapanda juu yake na kuanza kupapasa papasa kwa makini akatoa tabasamu la
uchungu baada ya kukishika kitu alichokitarajia akashuka huku mkononi akiwa ameshikilia bastola akaiweka kitandani na kusogelea droo ya dressing table akachukua peni na Notebook alishusha pumzi nzito na kuanza kufikiria kidogo kisha akajituliza kitandani na kuanza kuandika huku machozi yakimtirika. Baada ya kufika tamati na kuridhika akaamua kuusoma kwa sauti.
Mume wangu Mpendwa,
Sioni sababu ya Mimi kuishi kutokana na sababu ya kutokuzaa najiskia vibaya sana mume wangu lakini sina jinsi, mawifi zangu ninaowapenda nao hawanipendi tena wananisema vibaya, sitaweza kuwa na amani kuishi na hali hii, kwanini nikupe maisha magumu mimi sitaki uishi kwa masononeko wakati ukweli ni kuwa mimi ndiye niliyekudhurumu hivyo basi sifai kuishi. Buriani mume wangu maisha mema.”
Wini alimaliza kuyasoma kwa sauti, ‘Inaniuma mume lakini haina budi najua hata nikiishi nitakuwa ni kama mti usio nafaida hautoi kivuli wala matunda wala kuni wala mbao wala majani na mizizi isio ponya hata ndege wataukimbia’ Wini
alijongelea nafsini kisha akasimama akaichukua bastola kitandani akaiweka karibu na sikio, jasho jembamba likaanza
kumtoka nyuma ya shingo huku akiwa kafumba macho.
Kipindi chote hicho mawifi hawakuwa na walijualo juu ghorofani, sebuleni sauti ya redio ilipandishwa ikawa juu wakawa ni wenye kucheza taarabu na kurusha maneno ya vijembe kwa wifi yao huku wakipongezana, Fatuma akiwa jikoni chakula hakipikiki kwa raha roho ilimuuma alitamani apande ghorofani akamliwaze dada ake lakini hakuweza kufanya hivyo.
Ghorofani Winifrida wazo la kujiua bado lilikuwa limeutawala mwili, akili na nafsi “qataa” huo ndio mlio pekee uliosikika
masikioni akatulia sekunde kadhaa kusikilizia maumivu ya risasi itakayopenya katika kichwa na kuvuruga ubongo,
Je Nini kitajiri?????
Itaendeleaaaa....
Mijadara muhimu
View attachment 1741102