Herbalist Dr MziziMkavu
JF-Expert Member
- Feb 3, 2009
- 42,318
- 33,125
Usafiri wa daladala Zanzibar
Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ) imesema hakuna sababu kwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, kutumia usafiri wa daladala wakati Serikali ilishawapa fedha za kununua magari siku nyingi.
Hayo yameelezwa na Waziri wa nchi Ofisi ya Waziri Kiongozi, Hamza Hassan Juma, kufuatia Mwakilishi wa Jimbo la Tumbe (CUF), Ali Mhammed Bakari kufunguliwa mashtaka Polisi kwa tuhuma za kumpiga mchuuzi wa samaki baada ya nguo zake kuchafuliwa na vumba la samaki ndani ya daladala.
Waziri Hamza alisema Serikali imekuwa ikiwagharamia wajumbe usafiri kwa kuwapa posho ya mafuta kila siku ili kuwawezesha kutekeleza majukumu yao katika mazingira ya utulivu.
Hakuna sababu kwa Wajumbe wa Baraza kutumia usafiri wa daladala kwa vile wote wanalipwa posho za mafuta, alisema waziri Hamza.
Alisema Serikali iliamua kuwapa fedha tasilimu Wajumbe wa Baraza hilo ili wanunue magari lakini inashangaza kuwepo baadhi yao wakionekana kutumia usafiri wa daladala wakiwa katika majukumu yao.
Waziri Hamza alisema Serikali inafahamu kama Mwakilishi wa Jimbo la Tumbe amefunguliwa mashtaka katika kituo cha Polisi Wete Pemba na Serikali inaviachia vyombo vya sheria ili kuona haki inatendeka katika suala hilo.
Waziri Hamza ambaye ni Waziri dhamana wa masuala ya Baraza la Wawakilishi alisema kwa kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, inasimamia misingi ya utawala bora ndo maana imeshindwa kuingilia kati suala hilo ili kuvipa nafasi vyombo vya sheria kuamua kwa kuzingatia ukweli wake.
Hata hivyo alisema wajumbe wote wa Baraza hilo wanayo kinga ya kutokamatwa na Polisi wanapotekeleza majukumu yao lakini wanapokuwa nje ya Baraza kinga hiyo hutoweka na kuwa sawa na raia wengine.
Aidha, alisema Serikali haijafuta posho za mafuta kwa Wajumbe wake kwa vile kazi wanazofanya ni nyeti na wanahitaji usafiri wa uhakika wanapokuwa katika majukumu ya kuwatumikia wananchi katika majimbo yao.
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI