Slaa: Sasa nateua baraza la mawaziri

Herbalist Dr MziziMkavu

JF-Expert Member
Feb 3, 2009
42,320
33,125
headline_bullet.jpg
Asema litakuwa na mawaziri 20 tu, atarekebisha katiba
headline_bullet.jpg
Miaka mitano nyumba za matope, makuti kutoweka nchini



Karatu.jpg

Mgombea urais wa Tanzania kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Willibroad Slaa, akihutubia mkutano wa wa kampeni katika uwanja wa Bwawani mjini Karatu jana.



Mgombea urais kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Willibrod Slaa, ameanza kufikiria uundaji wa Baraza la Mawaziri la serikali yake. Alisema baraza hilo litakalokuwa la kwanza kuundwa na chama cha upinzani ikiwa Chadema itashinda, litakuwa na mawaziri na naibu mawaziri wasiozidi 20.
Dk. Slaa aliyasema hayo jana mjini Karatu, katika mkutano wa kampeni uliohudhuriwa na maelfu ya wakazi wa mji huo.
Karatu ni jimbo lililowakilishwa na Dk. Slaa akiwa mbunge wake tangu mwaka 1995 hadi mwaka huu alipoteuliwa na Chadema kuwania urais.
Dk. Slaa alisema ana wagombea wa kutosha wanaozidi 180 nchi nzima, na kwamba hata hivyo anatarajia kuunda baraza dogo hilo litakalokuwa na mawaziri wachapakazi, ili kuokoa fedha za umma na kuboresha utendaji wa serikali.
Alisema katika siku za kwanza za utawala wake, ataongoza nchi kwa Katiba iliyopo, inayomruhusu kuteua mawaziri kutoka miongoni mwa wabunge.
Hata hivyo, lengo lake ni kuanzisha mchakato wa kuandika upya Katiba ya Tanzania ambayo itampa fursa ya kuteua mawaziri wasiokuwa wabunge.
Dk. Slaa alisema kwa nyakati mbalimbali kwamba mabadiliko makubwa ya Katiba ni moja ya vipaumbele vyake katika siku 100 za mwanzo za utawala wake.
Alitumia mikutano yake ya jana kuwakumbusha wananchi kuwa serikali ya awamu ya nne imewatupa mkono, hivyo wana kila sababu ya kuiweka pembeni.
Alisisitiza kuwa serikali yake ikichaguliwa, itaingia madarakani kuongoza na si kutawala, akawaomba wana Karatu wamuunge mkono kama walivyofanya miaka 15 mfululizo alipokuwa mbunge wao.
Dk. Slaa pia alisema atakapoingia madarakani, serikali yake itatunga sheria ya kuwazuia wananchi kujenga nyumba za nyasi na matope, kama njia ya kuinua na kuboresha makazi yao.
Alisema ni jukumu la serikali kuwezesha wananchi kuishi kwenye nyumba bora, na kwamba mkakati wake ni kupunguza kodi za serikali katika vifaa vya ujenzi, kama bati, sementi, misumari, mbao na nondo ili kuwawezesha kumudumu gharama za manunuzi.
Hata hivyo, alisema licha ya kushuka kwa gharama ya vifaa hivyo, lazima serikali ifanye jitihada za kisheria ili kuwazuia wananchi kujenga nyumba za hovyo.
Kwa mujibu wa Dk. Slaa, kama mkakati huo utafanya kazi, miaka mitano ijayo nyumba zinazoezekwa kwa nyasi na matope zitakuwa zimetoweka.
Akizungumzia ahadi zake, Dk. Slaa, alisema ataanzisha mchakato wa kuandika Katiba mpya mara tu atakapoingia Ikulu.
Alisema ahadi zote alizotoa zinatekelezeka na kumshangaa mgombea wa urais kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Jakaya Kikwete, kuahidi kujenga viwanja vya ndege vipya, wakati kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL) ikiwa taabani.
Dk. Slaa alisema pia kuwa ni Watanzania wachache wenye uwezo wa kutumia usafiri wa anga na kueleza kuwa treni ndiyo suluhu ya matatizo ya usafiri nchini.
Wakati huo huo, Mchumba wa mgombea urais kupitia Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Josephine Slaa, amesema anamwachia Mungu tuhuma anazozushiwa.
Akizungumza kwenye mkutano wa hadhara mjini hapa jana, Josephine alisema hatajibizana na watu aliowaita kuwa wazushi dhidi ya uhusiano wake na Dk. Slaa.
“Watu wa Karatu najua kuwa mnajua ninawapenda ... mmesikia mengi lakini sitajibu kitu maana najua mtetezi wangu yu hai,” alisema Josephine.
Alisema atahakikisha anamtunza vilivyo Dk. Slaa ili awe na afya njema wakati wote, hasa katika harakati hizi za kampeni.
Awali, Dk. Slaa alipokuwa akimkaribisha Josephine, alieleza kushangaa kufunguliwa kesi ya madai badala ya jinai.
Alisema taarifa za 'kupora' mke wa mtu zimezushwa na wapinzani wake wa kisiasa kwa nia ya kumchafua.
“Kwa kuwa jambo hili lipo mahakamani nisingependa kulizungumzia, lakini najua walionishitaki ndio watakaolipa hiyo Sh bilioni 1 ... zitanisaidia kuboresha elimu na afya ya watu wangu,” alisema Dk. Slaa na kushangiliwa na maelfu ya wakazi wa Karatu.



CHANZO: NIPASHE
 
litakuwa na mawaziri na naibu mawaziri wasiozidi 20
ili kurahisisha hili si lazima mawaziri watajwe lakini angalau kwa sasa tungejua ni wizara zipi zitaundwa ku handle majukumu ya serikali ili itusaidie kupata picha halisi.
maana kama mawaziri na manaibu hawafiki 20 basi kutakuwa na wizara 10 mpaka labda 13 hivi
 
ili kurahisisha hili si lazima mawaziri watajwe lakini angalau kwa sasa tungejua ni wizara zipi zitaundwa ku handle majukumu ya serikali ili itusaidie kupata picha halisi.
maana kama mawaziri na manaibu hawafiki 20 basi kutakuwa na wizara 10 mpaka labda 13 hivi
Mimi binafsi hata hao 20 naona wengi. Hii nchi haihitaji mawaziri wengi, kazi kubwa inafanywa na watendaji yaani wakurugenzi. NI muhimu ku-streamline shughuli za serikali. Anyway kwa sasa tusubiri naamini atatufaanulia zaidi rais mtarajiwa cabinet na mipango yake...
 
Huyu mchungaji kaanza kuchanganyikiwa ! unateuwa baraza la mawaziri hata dalili ya kushinda hakuna? Au hyuy Mchungaji ni Child victim ya kanisa katoliki ? Pole babu na wafuasi wako!!
 
Huyu mchungaji kaanza kuchanganyikiwa ! unateuwa baraza la mawaziri hata dalili ya kushinda hakuna? Au hyuy Mchungaji ni Child victim ya kanisa katoliki ? Pole babu na wafuasi wako!!
Sijakuelewa, unasemake?
Ukiacha jazba unaweza ukaandika kitu ukaeleweka..haya, futa punzi, then andika sasa ukiwa umetulia.
 
Back
Top Bottom