Siri kuu kuhusu Escrow zafichuka

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,792
287,983

print_icon.gif

SIRI kuu ya James Rugemalira, kumwaga mabilioni ya shilingi kwa baadhi ya majaji wa mahakama kuu, viongozi waandamizi serikalini na madhehebu ya kidini, wabunge na viogogo wa Ikulu, zimeanza kufumuka.

Nyaraka mikononi mwa gazeti hili zinaonesha zaidi ya asilimia 90 ya wale waliopewa fedha na Rugemalira, ni wale waliomsaidia “kufanikisha ukwapuaji wa zaidi ya Sh. 324 bilioni kutoka Benki Kuu (BoT) na kujinasua katika mikono ya sheria.”

“Rugemalira alishika kila mmoja. Kuanzia Ikulu ya Jakaya Kikwete, TAKUKURU, mahakama, BoT, hazina, ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali, viongozi wa madhehebu ya kidini na hata baadhi ya mawaziri wa zamani wenye ushawishi serikalini,” ameeleza kiongozi mmoja mwandamizi kutoka Ikulu.

Amesema, “…fedha katika akaunti ya Escrow zilihusisha mtandao mpana ulioratibiwa na Rugemalira na Harbinder Sigh Seth (Singasinga).”

Majaji wa mahakama kuu, Aloycious Mujulizi na Eudeus Ruhangisa, ni miongoni mwa waliokuwa na mawasiliano ya mara kwa mara na Rugemalira; na walikuwa washauri wake wakuu wa kisheria.

Mawasiliano kati ya Jaji Mujulizi na Jaji Ruhangisa yalifanyika kupitia kwa Rugemalira mwenywe na katika eneo jingine kupitia kwa mkewe, Benedicta.

Jaji Mujulizi na Jaji Ruhangisa walitajwa bungeni na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), kuwa miongoni mwa vigogo waliopewa mgawo wa fedha hizo na Rugemalira.

Bunge liliagiza majaji hao wachunguzwe na wachukuliwe hatua za kinidhamu na kisheria.

Hadi sasa, hakuna taarifa zozote kuwa majaji walichunguzwa na kuchukuliwa hatua.

Rugemalira alikuwa akimiliki asilimia 30 ya hisa katika kampuni ya kigeni ya IPTL kupitia kampuni yake ya VIP Engineering and Marketing Limited.

Jaji Mujulizi na Ruhangisa walilipwa na Rugemalira kila mmoja Sh. 404 milioni.

Mabilioni ya shilingi yaliyohifadhiwa katika akaunti ya Escrow yalikwapuliwa na Harbinder Sigh Seth, aliyejiita mmiliki wa IPTL kwa msaada mkubwa wa Rugemalira na kile kilichoitwa, “amri ya mahakama.”

Seth alidai kumiliki IPTL kupitia kampuni yake ya Pan African Power Tanzania Limited (PAP).

MwanaHALISI linaweza kuthibitisha kuwa kati ya tarehe 13 na 26 Novemba 2014, kilikuwa kipindi ambacho Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), ilimhoji Rugemalira juu ya ukwapuaji wa fedha katika akaunti ya Escrow.

Aidha, ni katika kipindi hichohicho, Rugemalira alikuwa na mawasiliano ya mara kwa mara na Jaji Mujulizi na Ruhangisa.

Wengine waliokuwa na mawasiliano na Rugemalira katika kipindi hicho, ni waziri wa nishati na madini, Prof. Sospeter Muhongo; aliyekuwa waziri wa mambo ya nje na uhusiano wa kimataifa, Bernard Membe na aliyekuwa katibu mkuu wa wizara hiyo, Eliakimu Maswi.

Aliyepata kuwa waziri wa utawala bora, Mathias Chakawe; aliyekuwa mkurugenzi mkuu wa TAKUKURU, Edward Hoseah; aliyekuwa mwanasheria mkuu wa serikali (AG), Frederick Werema na aliyekuwa waziri wa viwanda na biashara, Dk. Abdallah Kigoda, walikuwa pia na mawasiliano na Rugelalira.

Wengine ni naibu gavana wa BoT, Dk. Enos Bukuku; aliyekuwa Mnikulu Mkuu wa Ikulu, Shaban Gurumo; aliyekuwa Kamishna mkuu mamlaka ya mapato (TRA), Rished Bade na aliyekuwa mwanasheria mkuu wa serikali wakati wa ujio wa IPTL nchini (1994), Andrew Chenge.

Orodha ya waliokuwa katika mawasiliano na Rugemalira inahusisha pia mawaziri wa zamani, Paul Kimiti na Wilson Masilingi; aliyekuwa mhariri mtendaji wa magazeti ya serikali – Daily News na Habari Leo – Gabriel Nderumaki; aliyewahi kuwa waziri wa nishati na madini, Wiliam Ngeleja na mkurugenzi wa kampuni ya G and S Consultancy Limited, Dk. Gideon Shoo.

Wengine ni aliyekuwa mkuu wa mkoa wa Kagera, Kanali mstaafu Constantine Massawe; Askofu Msaidizi wa Jimbo Katoliki la Bukoba, Methodius Kilain; Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Eusebius Nzigilwa na aliyekuwa waziri wa ardhi, nyumba na maendeleo ya makazi, Prof. Anna Tibaijuka.

Prof. Tibaijuka alikiri kupokea kiasi cha Sh. 1.6 bilioni kutoka kwa Rugemalira. Hata hivyo, alisema kuwa fedha ambazo alipokea zilikuwa ni mchango wa shule yake ya Barbro Johanssen ya jijini Dar es Salaam na Kajumulo Girls High School iliyoko Bukoba.

Kwa mujibu wa taarifa, Dk. Hoseah alimruhusu Rugemalira kutafuta msaada popote pale, ikiwa ni pamoja na nje ya nchi na kwamba ofisi yake “ingetoa maofisa kumsaidia.”

“Kama una jambo la msingi kufanya nje ya nchi, una baraka zangu zote. Watakapohitajika maofisa wa TAKUKURU kwa ufafanuzi, wako tayari kukusaidia pale uliko,” anaeleza Dk. Hoseah na Rugemalira andishi lake la 16 Novemba 2014.

Dk. Hoseah anamaliza kwa kumueleza Rugemalira, “…nakutakia kila la kheri.”

Rugemalira alikuwa anaomba TAKUKURU kuingilia kati kile kinachoitwa, “mgogoro wa hisa kati ya IPTL na Benki ya Standard Chartered (SCB) ya Uingereza.”

Hata hivyo, Rugemalira anaonywa na Masilingi, ambaye wakati huo alikuwa balozi wa Tanzania nchini Uholanzi, kuwa mwangalifu na mtulivu wakati suala hilo linaendelea.

Alisema, “mimi nikiwa mwanasheria, ninakushauri wewe na kampuni yako kushirikiana kwa ukamilifu na TAKUKURU. Suala la IPTL ni gumu. Limekuwa na mchanganyiko mkubwa. Akili nyingine haziwezi kulielewa.”

Masilingi anasema, “…nimebaini kwamba TAKUKURU ndio wanaolichukulia suala hilo kwa usiri mkubwa katika hatua za uchunguzi na wenyewe wanaweza kukusaidia kupata hukumu iliyo ya haki.”

Benki ya Standard Chartered ilikuwa inadai na mpaka sasa bado inadai kuwa mitambo ya kuzalisha umeme ya IPTL na fedha zilizopo kwenye akaunti ya Escrow, ni mali yake.

Inadai kuwa kampuni ya MECHMAR ya Malasia ilishindwa kurejesha mkopo iliochukua benki na kwamba hilo ni jambo linalosababisha mitambo ya IPTL iliyopo Tegeta Salasala, jijini Dar es Salaam, kuwa mali yake.

Akihutubia taifa kupitia wazee wa mkoa wa Dar es Salaam, wiki tatu baada ya Bunge kuagiza waliohusika katika wizi wa fedha za Escrow wachukuliwe hatua, aliyekuwa Rais wa Jamhuri, Jakaya Mrisho Kikwete alikiri kuwapo udanganyifu katika kufikia utoaji wa fedha hizo.

Alikiri baadhi ya nyaraka kughushiwa. Akakiri kuwa kampuni ya PAP imekwepa kodi ya serikali na kudai kuwa serikali yake bado inaendelea kuitafuta kampuni ya MECHMAR iliyodaiwa kuuza asimia 70 ya hisa zake ndani ya IPTL.

Rais alikiri kuwa aliyepewa fedha na serikali – PAP – hakuwa na sifa; serikali yake haikufanya uchunguzi yakinifu kuhusu historia, uhalali, sifa na uwezo wa kampuni ya PAP katika uwekezaji wa umeme, ununuzi wa mitambo na mtaji.

Naye mwanasheria wa Rugemalira, Camilo Schutte, katika barua aliyomwandikia Rugemalira, anasema “…baada ya kusoma ushauri wa Masilingi juu ya msaada wa TAKUKURU, itakuwa busara kuomba TAKUKURU kusubiri hukumu kati ya Standard Chartered na IPTL.”

Anasema kampuni ya Rugemalira (VIP) “…inapaswa kuomba TAKUKURU kufanya uchunguzi juu ya sera ya benki ya Standard Chartered kuhusu ununuzi wa madeni ambayo mchakato wake unaweza kuwa na rushwa.”

Camilo Schutte anamueleza Rugemalira katika barua yake hiyo na ambayo imenakiriwa kwa majaji, mawaziri, kiongozi wa TAKUKURU, maofisa wa Ikulu na watu wengine kuwa, “…tatizo la benki ya Standard Chartered, kama zilivyo taasisi nyingine, ni kufanya biashara ili kujipatia faida kubwa.”

Akiandika kwa Dk. Gideon Shoo, mwanasheria wa Rugemalira (Camilo Schutte) anaelekeza kufanyika mambo matatu kwa haraka.

Kwanza kutafuta, kwa “gharama yoyote ile,” watu wote wenye ushawishi mkubwa kwenye jamii ambao wanapigia kelele ukwapuaji wa fedha katika akaunti ya Tegeta Escrow.

Miongoni mwa waliotajwa, ni Zitto Kabwe, mbunge wa sasa wa Kigoma Mjini; David Kafulila, ambaye alikuwa mbunge wa Kigoma Kusini; Balozi wa Uingereza nchini, Dianna Melrose; Wilson Masilingi na balozi wa Finland nchini.

Pili, Camilo Schutte anasema, ni sharti mtandao wao ujiridhishe ikiwa watu wanaolizungumzia jambo hilo wanalifahamu kwa undani au wanalijua nusunusu au hawalijui kabisa.

Kwa maoni ya mwanasheria wa Rugemalira, wabunge waliokuwa wameshupalia jambo hilo walikuwa hawana taarifa zozote muhimu kuhusu suala hilo.

Tatu, mwanasheria alimtaka Dk. Shoo kuangalia athari za taarifa zilizosambazwa juu ya ukwapuaji wa fedha hizo, kwa kampuni ya IPTL na Rugemalira binafsi.

“Baada ya kukamilisha haya, naomba unijulishe haraka ili tuweze kupanga mikakati ya kukabiliana na kila tatizo nililolitaja hapo juu,” anaeleza Camilo Schutte.

Kupatikana kwa mawasiliano haya kumekuja mwaka mmoja na nusu baada ya mabilioni ya shilingi kukwapuliwa BoT; na Bunge kuelekeza serikali kufanya uchunguzi.

Aidha, kupatikana kwa taarifa kuwa Rugemalira alikuwa na mawasiliano ya karibu na “kindungu” na mkuu wa TAKUKURU, kumekuja wakati ambapo taasisi hiyo imeshindwa kuanika orodha ya watu walionufaika na mgawo wa fedha hizo kutoka benki ya Stanbic.

Bunge liliagiza serikali kufikisha mahakamani watuhumiwa wote wa Escrow, ikiwa ni pamoja na kufilisi mtambo wa IPTL na kuitangaza benki ya Stanbic kuwa taasisi ya kutakatisha fedha.

Bunge liliagiza pia kuchunguza na kuwajibisha majaji waliotajwa kunufaika na mgawo wa fedha kupitia benki ya Mkombozi na kumfukuza nchini, anayejiita mmiliki wa IPTL, Harbinder Sigh Seth.

Akizungumzia kutajwa kwa Dk. Hoseah na baadhi ya majaji katika mawasiliano na Rugemalira, mbunge wa Singida Mashariki (CHADEMA), Tundu Lissu amesema jambo hilo linaongeza shaka juu ya uadilifu wa viongozi wa CCM na serikali yake.

Ameliambia gazeti hili katika mahojiano kwa njia ya simu, “…hili liserikali lote limeoza. Kuanzia Ikulu, mfumo wa mahakama hadi viongozi wa madhehebu ya kidini; kote kumejaa rushwa.”

Lissua ameongeza, “Tulisema ndani ya Bunge, kwamba majaji wamehongwa na hivyo tukataka wachunguzwe, lakini serikali ya CCM imegoma kwa kuwa walioiba waliwajua na walishirikiana nao.”

Mwanasiasa huyo wa upinzani anasema, “utapeli huu ulifanywa na serikali ya Rais Kikwete, BoT, Benki ya Stanbic na PAP.”

Amesema, “…sasa kama kweli wanataka kusafisha nchi, basi waanzie hapo. Siyo kukimbizana na vidagaa. Waanze na maofisa wao wa Ikulu waliokuwa wameigeuza ofisi ya umma kuwa ofisi binafsi.”


Chanzo: MwanaHalisi
 
Hata wapambe wanaomuimbia mapambio , habari kama hizi hawataki kuzisikia Magufuli anatafuta cheap popularity hawezi na hana ubavu wa kudeal na rushwa kubwa kubwa
Umeusemea moyo wangu mkuu. Nimeshasema repeatedly kuwa JPJM ana sifa za watu waoga na wenye kutafuta kupendwa kwa nguvu kama vile anajaribu kuthibitisha kuwa hata kama hakujiandaa kuwa raisi lakini anaiweza kazi. Matokeo yake lazima aonekane kuwa anaweza na atafanya hivyo kwa kufanya mambo madogo (kukuna vipelee na kutumbua vijipu vidogo vidogo; tena hadharani) ili aonekane kuwa anafikia matarajio ya wengi ambao hawakumpigia kura huku akizuia mijadala bungeni isionekane kwa wananchi.

Mtu mwoga hawezi kuigusa skendo ya escrow na nyingine kama hizo. JPJM hataigusa skendo ya escrow isipokuwa kama atapata presha toka kwa wawakilishi wa wananchi walioko bungeni.

Kumbuka kuwa mara nyingi mtu mwoga ndiye ambaye huwa anakazana kuonekana jasiri.
 
Hii sentensi si kweli:
"madhehebu ya kidini", ukweli ni dhehebu moja tu tena ni la kanisa katoliki ndilo lililotumika.

Kwanini mpotoshe na kusema "madhehebu"?

Cc BAK
336_ruge.JPG
Hujambo Mama I was waiting your comment.
 
Labda iundwe tume ya maridhiano kama iliyoundwa na Mandela baada ya apartheid,vinginevyo kazi ya kutumbua ni ngumu zaidi ya tunavyofikiria,iundwe tume waitwe hao mafisadi,wahojiwe, wanao kiri na kurudisha hazina fedha walizokwapua na kuwa tayari kufilisiwa wasamehewe na wapelekwe chuo cha maadili miezi kadhaa kwa ajili ya rehabilitation, wakionekana wamebadilika basi waendelee na kazi,watakaogoma basi wapelekwe mahakama ya ufisadi,vinginevyo ni overhaul ya system yote kwani karibu vigogo wote wanaguswa.Kama anavyosema Lisu,short of that tutaendelea kutumbua vidagaa tu
 
20 Reactions
Reply
Back
Top Bottom