HADITHI: THE ODYSSEY OF GAVIN LUCA (LIONELA)
MWANDISHI: FEBIANI BABUYA
STORYTELLER: BUX THE STORYTELLER
WHATSAPP: 0621567672
EMAIL:
thomasibabuya@gmail.com
AGE: 18+
********************
UKURASA WA ISHIRINI NA TANO
SONGA NAYO................
“Hiyo sio kazi yako kujua na nimekupa nafasi ya kuuliza maswali hivyo sitegemei kuulizwa tena kwa sababu maswali yako yanatosha, ungehitaji hayo yote ulitakiwa kuuliza kwa pamoja. Jibu la swali lako la mwisho ni kwamba tuliamua kutoweka kwa sababu ya kuleta amani kwenye hili taifa. Kama tungeamua kuendelea kuwepo basi lazima kuna watu wangetutafuta na hilo lingezalisha mauaji ya watu wengi jambo ambalo bosi wakati anaaga hakutaka kabisa hilo lifanyike.
Alitamani baada ya pale itawale amani, alitamani kuona tupo sehemu ambayo tungeishi maisha ya kawaida kama watu wengine lakini hilo lisingewezekana tena ndiyo maana tuliamua kuondoka kwenye makazi ya watu na kuja kuishi huku mbali ambako tumekuwa na amani kwa muda mrefu mpaka sasa. Tunaishi kwa amani kwa sababu kuishi na wanadamu ni jambo gumu kupita kiasi, wanadamu ni washenzi, wanadamu unaweza ukaamua kuyaishi maisha yako ya amani lakini wakatafuta sehemu ya kuamua kukuonyesha kwamba wao wanatakiwa kukutawala.
Na tatizo kubwa huwa linaanzia hapo kwa sababu hakuna mtu ambaye yupo tayari kukutana na hali kama hiyo ndiyo maana watu huwa wanakuja kufanya maamuzi yaliyo magumu na vurugu zinaanzia hapo. Maisha ya ukimya wetu hayakuwa ya kijinga kwa sababu tuliwahi kuwa na hisia kwamba kuna siku yale matatizo yangerudi tena ndiyo sababu tuliwatafuta watu ambao tungeweza kuwaamini kwa ajili ya kuwatengeneza wafanye kazi na sisi na miongoni mwa hawa watu miaka ya hivi karibuni ni wewe na ulipata nafasi hiyo kiasi kwamba ukafanikiwa kupewa na mafunzo japo naona bado haujaiva vya kutosha.
Kuna ulinzi mkali ndani ya hili eneo, hakuna mahali unaweza kufanya jambo la kipuuzi uwapo ndani ya hili eneo hivyo hata wewe usije ukathubutu lakini pia yule mtu ambaye amekupa huu mzigo uulete ambaye ndiye alikuwa mwalimu wako ni moja kati ya vijana wangu watiifu na ninawaamini sana ndiyo maana kazi ya kumalizana na wewe niliiweka kwenye mikono yake kwani niliamini ni mikono ambayo ipo salama wakati wote na kanithibitishia hilo.
Niliwahi kuwa na uhakika kwamba kuna siku ungekuja kuwa kijana wangu mhimu ndiyo maana nikataka utengenezwe kwenye misingi yetu kwanza kabla ya kukupa nafasi ya kuweza kukutana na mimi na rasmi leo nakuapisha unakuwa mmoja wetu. Tuna sheria zetu za namna ya kuishi na kuyaendesha maisha lakini kwenye sheria hizo kuna machaguo mawili tu, ufe ukiwa unaipigania nembo yetu ama uishi ukiwa mshindi wa kuilinda nembo yetu. Kwa maana hiyo ni kwamba hauruhusiwi hata siku moja kutoa siri yoyote kuhusu sisi mahali popote na kwa gharama yoyote kwa sababu kufanya hilo ni kwamba lazima utatafutwa ili uuawe. Hakuna kosa ambalo linasameheka ukiwa ndani ya hilo vazi kwa sababu huruma za kusamehe wakosaji zimewahi kutuletea matatizo makubwa sana miaka ya huko nyuma na huenda zisingefanyika basi leo tusingeishia huku na mtu wa kwanza kufanya hilo kosa alikuwa ni bosi mwenyewe Gavin Luca kwa kumpa nafasi ya kuishi kwa mara ya pili mtu ambaye alistahili kufa tena kwa maumivu makali.
Tangu niwe kiongozi wa hawa watu, najua kabisa kila uhai wa mtu unayategemea maamuzi yangu hivyo sijawahi kufanya kosa lolote la kijinga ambalo linaweza kuyabeba maisha ya watu wangu kwa namna yoyote ile. Lile tukio la mauaji ya watu mbele ya mahakama ni ishara mbaya kwamba dunia inatuhitaji kwa mara nyingine, kuna mahali nahisi tulifanya kosa lingine miaka hiyo na kila nikijaribu kuhitaji kufahamu kwamba ni wapi tulikosea, nashindwa kabisa kuelewa.
Nina uhakika lile jambo halijatokea kwa bahati mbaya kwa sababu siku ambayo kitabu kimetangazwa kutoka ndiyo siku ambayo lile tukio limetokea, hiyo ni ishara kwamba kuna mtu anatutafuta, sasa hapo kuna mawili; kwanza huenda kuna mtu alisahaulika ama aliweza kuigiza vyema na kukaa mbali kwa wakati ule ama kuna mtu anauhitaji utajiri ambao upo kwenye mikono yetu ama anataka vyote kwa pamoja.
Mpaka wakati huu bado sijafanikiwa kujua kwamba anaweza kuwa nani ambaye atakuwa anahitaji jambo kama hilo kutoka kwetu. Vijana wanaendelea kufanya huo utafiti kwa makini na kama kuna mahali kutaonekana alama yoyote basi itakuwa mara ya kwanza mimi kurudi tena mtaani kwa ajili ya kazi. Unajua sababu ya wewe kuwepo hapa Jabari?” alipewa maelezo marefu ambayo yalimfanya aisikilize hadithi hiyo kwa umakini mkubwa kwa sababu watu hao walikuwa huko milimani lakini ni wazi walikuwa wanajua kila jambo ambalo lilikuwa linaendelea huko duniani.
“Bado, kiongozi wangu ambaye alinifundisha kwa ile miaka miwili alikuwa akinisisitiza kwamba natakiwa kuwa msaada kwa taifa langu, alidai ananifundisha ili niwe na uwezo wa kujilinda kwa sababu ule msimamo wangu wa kuamua kulipigania taifa langu ndio ambao ulimvutia kunipambania. Alisisitiza kwamba nisipokuwa na uwezo wa kujilinda mwenyewe basi nitakufa nikiwa sijatimiza jambo hata moja la kulisogeza taifa mbele hivyo nikakubali kufanya haya.
Lakini hata yeye alikuwa akinisisitiza kwamba kuna mtu ambaye ndiye alikuwa kiongozi wake, mtu ambaye ndiye alitoa ruhusa ya mimi kuingia kwenye jamii hii ambayo ingenilinda na kunifanya niwe sababu ya maisha mapya, aliniambia kwamba muda ukifika basi nitafanikiwa kuonana naye tena akikutaja kwa jina la Ghost. Alikuwa akinipatia maelekezo ya jambo gani la kulifanya, wapi pa kwenda na nani wa kumfuata kwa muda gani, naweza kusema ramani ya maisha yangu ni yeye alikuwa akiiweka sawa muda wote na ndiye amenifanya mpaka watanzania wakanijua kwa mara nyingine ila zaidi ya hapo hakuna jambo ambalo nalifahamu zaidi”
“Kabla ya kukupatia majukumu yako ambayo yamekufanya uwepo hapa, kuna jambo dogo ambalo nitakupa elimu hapa ili baadae usije ukayarudia makosa ambayo wanadamu wengi wamekuwa wakiyarudia miaka na miaka. Kwenye kurasa za vitabu huwa kuna maelezo mengi ila kuna kurasa kadhaa tu ambazo huwa zinabeba maana nzima ya kitabu kizima. Kurasa hizo huwa zinapuuzwa na wengi kwa sababu huwa hazivutii Jabari, na unajua kwanini hazivutii?
Ni kwa sababu watu wanapenda kusikia kile ambacho wao wanakitaka ama wanakihitaji, sasa kwenye hizo kurasa za kuhesabu mara nyingi huwa kuna taarifa ambazo wengi hawazipendi. Hawazipendi kwa sababu huwa zinaelezea uchungu mkubwa na ukweli wa mambo, wanadamu wengi hawapo tayari kuambiwa ukweli kwani ukweli unauma mno ila ukiwa mtu mwerevu unatakiwa kuupenda ukweli kwa sababu utakupatia somo kubwa juu la jambo gani unatakiwa kulifanya na wapi ulikuwa umekosea kwa mara ya kwanza.
Moja kati ya wapigania haki wakubwa na wasomi kuwahi kutokea duniani Dr Martin Luther King Jr aliwahi kunukuliwa akisema “Haki haiwezi kutolewa na wanyanyasaji kama zawadi bali inatakiwa kupiganiwa na wale ambao wananyanyaswa” Hii kauli ina maana gani? Ni kwamba huwezi ukafanikiwa au kumaliza tatizo lako kwa sababu ya kufarijiwa na uongo bali unaweza kulimaliza tatizo lako kwa kuukubali ukweli na kutafuta njia sahihi za kulitatua wewe mwenyewe.
Rejea kwenye hoja yangu ya kitabu, kwahiyo ile sehemu ambayo inakupa ukweli wewe hautakiwi kuichukia kwa sababu tu vimeandikwa vitu ambavyo huvipendi bali itumie kama somo kwako ili usije kufanya makosa ama kufanya mambo ambayo yanaweza kuyafanya maisha yako kuwa magumu kwa hapo baadae. Kama umezingatia maelezo yangu, sikuwa nayazungumzia maandishi wala kitabu, nilikuwa nawazungumzia watu.
Siku zote kwenye haya maisha watu wengi wanafeli kwa sababu huwa wanatanguliza hisia kutaka kusikia vile ambavyo wao wanavitaka na si kusikia vile ambavyo vinatakiwa kusikika. Kosa la kwanza la wanadamu huwa linaanzia hapo! Nakwambia haya kwa sababu kuingia kwenya maisha ya hii familia ni mazuri kwani utaendelea kuwa na pesa nyingi ambazo mpaka sasa tumekupatia za kutosha kwenye akaunti yako lakini maisha haya pia yanatisha kuliko unavyo fikiria wewe.
Haya maisha hayatakuwa kama yale ambayo wewe unayataka bali yatakuwa yale maisha ambayo yanatakikana wewe kuyaishi haijalishi utayapenda au hautayapenda. Unaenda kuwa muuaji Jabari, yale mauaji ambayo ulikuwa unayaripoti kwenye vyombo vya habari kwa sasa wewe ndiye ambaye unakwenda kuyafanya ili uelewe kwamba huwa inakuaje kuua watu wengi tena kikatili. Wewe kwa sasa unaenda kuwa sehemu ya hatari ya taifa kwa watu ambao wanaongoza, kwa sasa wewe utakuwa miongoni mwa watu ambao watakuwa wanatafutwa sana kwenye taifa hili je upo tayari?
Kabla ya kujibu usijiwazie wewe, iwazie familia yako, kwa sababu ili wawe hai na salama unatakiwa kuwafuta kwenye moyo wako na kukaa nao mbali. Hautakiwi kufanya nao mawasiliano ya namna yoyote hata kama kutakuwa kuna nafasi ya wewe kukutana nao kwa sababu wakati hayo yanafanyika kuna watu watakuwa wanakusubiri wewe ufanye hilo kosa la hisia za mapenzi ya familia ili wakupate wakiwa wana imani kwamba inaweza kuwa sababu ya kujua tulipo sisi ama utakuwa na taarifa zetu.
Ukurasa wa ishirini na tano unafika mwisho.
FEBIANI BABUYA.