Simulizi: Ulimwengu Ndotoni Mwangu

Simulizi: Ulimwengu Ndotoni Mwangu

Chilojnr

JF-Expert Member
Joined
Jul 5, 2012
Posts
308
Reaction score
1,354
Sehemu ya 01.

Nataka nicheze mpira, niwe na mafanikio makubwa, kama yule aliyekuwa anachezea Brazil ambaye uliniambia sana kuhusu yeye!” alisikika kijana mmoja akimwambia mwanaume aliyekuwa amekaa pembeni ya redio yake akisikiliza mechi kati ya Simba na Yanga iliyokuwa ikichezwa Uwanja wa Taifa.
“Nani?”
“Yule Mbrazil!”
“Oh! Unamzungumzia Pele?”
“Ndiyo! Nataka nicheze mpira kama yeye!”
“Ni jambo zuri, ila soma kwanza!”
“Kwani yule alisoma?”
“Hakusoma! Ila wewe utatakiwa kusoma sana!”
“Na niliwahi kusikia ulikuwa ukicheza mpira tangu shule, ikawaje ukaacha?”
“Nilivunjika mguu, nikauchukia mpira!”
“Basi mimi nitacheza! Na nitakuwa mchezaji mkubwa sana,” alisema kijana huyo.

Walikuwa watu wawili waliokuwa wakizungumza kama mzazi na mtoto. Kijana wa miaka kumi na tano aliyeitwa kwa jina la Amon, alikaa pembeni ya baba yake aliyeitwa Stefano huku wakisikiliza mechi iliyokuwa ikiendelea Uwanja wa Taifa na kuzungumza mawili matatu.

Amon alikuwa mtoto wa mwisho wa mzee Stefano, kipindi hicho walikuwa wakiishi Manzese Kwa Mfuga Mbwa. Maisha yao yalikuwa ni ya shida, hawakuwa na pesa, katika mtaa huo, wao walikuwa miongoni mwa zile familia zilizokuwa na maisha ya dhiki kipindi hicho.
Hawakuwa wakila milo mitatu kwa siku, walipokuwa wakila asubuhi, kula tena ilikuwa ni usiku. Mzee Stefano alikuwa akifanya kazi za ujenzi ndani na nje ya Jiji la Dar es Salaam. Kila siku asubuhi alikuwa akipitiwa na wenzake na kwenda Mbezi Beach ama Goba kwenye ujenzi kwani kwa kipindi hicho mji ulikuwa unatanuka na kulikuwa na nyumba nyingi zilizokuwa zikijengwa.

Miaka hiyo ya nyuma wakati akiwa kijana mzee Stefano alikuwa na ndoto za kucheza mpira, alihitaji kuyajenga maisha yake katika mchezo huo. Alikuwa mchezaji mzuri, aliyejua kulisakata kabumbu na kumfanya kuwa nyota wa Timu ya Lipuli ya Iringa iliyokuwa ikitamba miaka ya nyuma.

Kupitia mpira, mwaka 1985 akafanikiwa kukutana na msichana mrembo, Zuri Michael Wambuli, msichana aliyekuwa akiishi Kariakoo. Kumsikia mtangazaji akitangaza mechi za Lipuli na kulisikia jina la Stefano kila wakati ikamfanya kutamani kuonana na mwanaume huyo, mbwembwe za mtangazaji huyo zilimfanya kuwa na kiu kubwa moyoni mwake.

Baba yake, mzee Michael Wambuli alikuwa shabiki mkubwa wa timu hiyo, kila alipokuwa akikaa sebuleni na kuzungumzia mpira, alimzungumzia sana Stefano kiasi cha binti yake huyo kutamani kumuona hata mara moja tu.

Moyo wake ukatokea kumpenda, alimpenda mwanaume ambaye hakuwahi kumuona alifananaje, moyo wake ukaanza kuburuzwa na mapenzi, kila alipokuwa akisoma, hakuwa akisoma kwa raha, alitamani sana kumuona mwanaume aliyekuwa akiutesa moyo wake.
Alitamani kumuuliza baba yake zaidi kuhusu huyo Stefano, alifananaje, alikuwaje, ni mzuri ama? Alikuwa na nywele nyingi zilizojulikana kama Afro ama? Alikuwa akivalia mabwanga kama wanaume wengine ama? Yaani kwa kifupi alitamani sana kuona mwanaume huyo alikuwa na muonekano gani.

Siku moja baada ya baba yake kununua gazeti la Mzalendo ndiyo siku aliyoiona picha ya Stefano kwa mara ya kwanza, ilionekana kwa ukubwa nyuma, kama alivyokuwa akitaka ndivyo mwanaume huyo alivyokuwa.

Kichwani alikuwa na nywele nyingi, alipigwa picha akiwa na amekaa kwenye kiti, suruali yake ilikuwa ni bwanga, zile za zamani ambazo kwa chini zilikuwa pana na alivalia shati ya mikono mirefu.

Muonekano ule tu ilitosha kumwambia Zuri kuwa mwanaume huyo alistahili kuwa mpenzi wake, ampende kufa na kuzikana, ampe chochote kile lakini mwisho wa siku waoane na kufunga ndoa.

Siku hiyo alilichukua gazeti hilo, akachana kipande kile kilichokuwa na picha ya Stefano na kuiweka ndani ya daftari lake, kila alipohitaji kumuona mwanaume huyo, alilichukua daftari lile, akaitoa picha ile na kuiangalia.

Mapenzi yakazidi kuchomoza, akashindwa kuvumilia, hakutaka kuona akiumia kila siku na hiyo ndiyo sababu iliyopelekea kumwambia baba yake kuwa alitaka kuangalia mpira, naye aende uwanjani.

Mzee Wambuli aliposikia hivyo alishangaa, hakutegemea kumsikia binti yake akimwambia naye alitaka kwenda uwanjani kutazama mpira, hakutaka kumkatalia, akakubali na hivyo katika mechi iliyofuata ambayo ilikuwa ikichezwa kwenye uwanja wa Taifa (Uhuru) wakaelekea huko.

Macho yake yakatua kwa Stefano, mwanaume huyo alikuwa na mvuto wa aina yake, mashabiki walikuwa wakiliimba jina lake, alikuwa mchezaji tishio ambaye kila mmoja alimuogopa, mwili wake ulijaza na alivalia pensi fupi iliyoyafanya mapaja yake manene kuonekana vilivyo.

Huo ndiyo ukawa muendelezo mwingine wa kumpenda mwanaume huyo, akampenda kupita kawaida na siku moja aliposikia timu ya Lipuli inakwenda kufanya mazoezi katika uwanja wa Shule ya Wasichana ya Jangwani kujiandaa na mechi dhidi ya Simba, akatamani kumuona.

Siku hiyo hakuondoka, alibaki darasani akijifanya kujisomea lakini lengo lake kubwa lilikuwa ni kumuona Stefano kwa mara nyingine tena. Hilo halikuwa tatizo, akafanikiwa kumuona mwanaume huyo, alimwangalia, alikuwa mtu wa mazoezi, alivutia kwa kila aliyekuwa akimwangalia.

Alikaa na kuvumilia, alipowaona wanafunzi wenzake wanasogea kwa karibu uwanjani, naye akajisogeza na kuanza kumwangalia kwa ukaribu zaidi, huyo Stefano alikuwa na mvuto kupita kawaida.

Mazoezi yalipomalizika, wanafunzi wakapata nafasi ya kwenda kuzungumza mawili matatu na wachezaji, haraka sana naye akamfuata na kuanza kuongea naye huku akijisikia aibu mno.

Ilikuwa ni lazima kufanya hivyo, kwa mtu kama Stefano ilikuwa vigumu sana kumuona sehemu na kuzungumza naye, alikuwa mkazi wa huko Iringa, alikwenda Dar es Salaam alipokuwa akicheza mechi tu, hivyo ilikuwa ni lazima afanye juu chini kuhakikisha anazungumza naye.

“Unajua sana kucheza mpira,” alisema Zuri huku macho yake yake yakiwa kwa mwanaume huyo.
“Ahsante sana!”
“Baba yangu anakupenda sana. Natamani hata siku moja uje kumuona!” alimwambia.
“Kweli?”
“Ndiyo! Aliniambia mengi sana kuhusu wewe,” alimwambia.
“Yapi hayo?”
“Kwamba unajua kucheza mpira!”
“Nadhani alikosea!”
“Hapana! Hakukosea! Unajua sana!”
“Ulishawahi kuona nikicheza?”
“Niliwahi kuja uwanjani kukuangalia!”
“Lini?”
“Mwezi uliopita! Unajua sana!” alisema Zuri.

Walibaki wakizungumza kwa dakika kama tano hivi, baada ya hapo Zuri akachukua namba ya posta kwa lengo la kumwandikia barua mwanaume huyo.

Hakutaka waishie hapo, ilikuwa ni lazima waendee kuwasiliana na lilikuwa jambo zuri kama wangefikia hatua ya kuandikiana barua kwani Zuri alitarajia kumaliza kidato cha sita mwezi unaofuatia.

Huo ndiyo ukawa mwanzo wa wawili hao kufahamiana, wakaandikiana barua, Stefano akapata nafasi ya kwenda kumtembelea, akakutana na mzee Wambuli, wakawa marafiki mpaka pale alipotangaza nia ya kumuoa msichana huyo ambaye alianza kufanya kazi katika Shirika la Reli Tanzania (TRL)

Mwezi mmoja baada ya kufunga ndoa ndipo Stefano akavunjika mguu na vipimo vilipofanyika, hakuruhusiwa kurudi uwanjani. Alikuwa na ndoto nyingi za kuendelea kucheza mpira, aende Ulaya, afanikiwe, apate pesa lakini ndoto yote hiyo ikafutika, ikafa moja kwa moja.

Ilikuwa ni huzuni kwake, moyo wake ulimuuma mno, alikuwa mtu mzima lakini hakuacha kulia, alilala kitandani usiku kucha akilia, alitamani kile alichoambiwa kiwe kwenye ndoto na atakapoamka basi aende uwanjani kujiandaa na mazoezi lakini haikuwa hivyo.

Wakahama Iringa na kuhamia jijini Dar es Salaam, alipofika huko, mke wake akamtafutia kazi hapo Shirika la Reli, akafanikiwa, na kwa kupitia jina lake kubwa, akakubaliwa na hatimaye kuanza kazi.

Je, nini kitaendelea?
Screenshot_20211227-184810_Instagram.jpg


Sent from my SM-A107F using JamiiForums mobile app
 
Sehemu ya 02.

Maisha yalikuwa ya kawaida, yaliendelea hivyo, wakafanikiwa kupata watoto watatu, James, Hezron na Amon ambaye ndiye kipindi hiki alikuwa na hamu kubwa ya kutaka kuwa mchezaji mkubwa, arithi mikoba ya baba yake na kuwa na jina, ikiwezekana hata zaidi ya baba yake.

Akiwa na miaka kumi na saba kipindi hicho tayari Amon alionekana kuwa na uwezo mzuri wa kucheza mpira, alionekana kuwa tishio, shuleni kwao alifanikiwa kuwa mfungaji bora katika mashindano mbalimbali.

Baba yake alimpenda lakini siku zote alimwambia jambo moja tu, asome sana kwani maishani mwake hakutakiwa kutegemea mpira tu, aliogopa, alipatwa na hofu kwamba inawezekana kuna siku naye angepata matatizo kama aliyokuwa ameyapata, hivyo alimsistizia kuishika sana elimu.

“Nitasoma, ila nitacheza mpira sana tu!” alisema Amon huku akimwangalia baba yake.

Kati ya watoto wake wote aliamini Amon ndiye ambaye angekuja kurithi kipaji chake kama alivyokuwa kipindi cha nyuma, alijibana sana, akamnunulia viatu, jezi na mpira, akapata muda wa kwenda uwanjani kucheza na wenzake.

Alipofikisha umri wa miaka kumi na saba, akafanikiwa kuitwa katika Kituo cha Mpira cha Golden Park kilichokuwa Posta jijini Dar es Salaam.

Kituo hicho kilikuwa na watoto zaidi ya mia saba ambao walikuwa wakifundishwa mpira. Walikuwa watoto kutoka kwenye maisha mazuri, wazazi wao walikuwa wakilipa zaidi ya dola elfu mbili kwa mwaka, ila kwa mtu kama Amon alichukuliwa baada ya kuonekana kuwa na kipaji cha kulisakata kabumbu mtaani, hivyo hakutakiwa kulipia kitu chochote kile.

Akawa mwanafunzi katika kituo hicho, alicheza kwa bidii sana, alitamani kuwa kama baba yake, kama mzazi wake alishindwa kwenda Ulaya, yeye alitaka kwenda, aiinue familia yake kutoka pale ilipokuwa, awe na pesa nyingi kama walizokuwanazo wachezaji wa Ulaya.
Katika kituo hicho cha mpira ndipo akafanikiwa kuanzisha urafiki na kijana mwingine aliyeitwa kwa jina la Gideon George, kijana mrefu, mweupe aliyetoka kwenye maisha mazuri. Wakawa marafiki, wakapendana, wakawa wanataniana huku Gideon kimwambia ilikuwa ni lazima siku moja Amon amuoe mdogo wake, Angelina.

“Kwanza mzuri?” aliuliza Amon huku akimwangalia rafiki yake huyo.
“Nani? Mdogo wangu? Mzuri kishezi!” alijibu Gideon huku akicheka.
“Kwa nini unataka nimuoe dada yako?”

“Kwa sababu wewe ni rafiki yangu sana, halafu kwa mtu kama wewe ukimuoa dada yangu na ukamuumiza, kukuua ni rahisi sana!” alijibu Gideon na wote kuanza kucheka.

Amon hakumjua Angelina, hakuwahi kumuona, alikuwa akimsikia tu kutoka kwa rafiki yake huyo. Waliendelea kuwa kuwa pamoja na siku ambayo wazazi wa Gideon na mdogo wake walipofika kituoni hapo kwa lengo la kumuona kijana wao ndiyo siku hiyo Amon akapata nafasi ya kumuona Angelina.

Alimshangaa, ni kama alikutana na mtu asiyekuwa wa kawaida hata kidogo, alikuwa msichana mzuri kwa sura, mweupe, mwenye vishimo mashavuni mwake, sura ya upole, mwanya wa mbali, mwili wake ulikaa kisichana na kifua kilisimama vilivyo, udenda ukamtoka Amon.

“Nilikwambiaje!” alisema Gideon.
“Kuhusu nini?”
“Mdogo wangu!”
“Nani? Angelina?”
“Ndiyo! Huyo unayemwangalia kwa tamaa kama fisi ndiye mdogo wangu!” alisema Gideon huku akimwangalia Amon aliyekuwa ameduwaa tu, hakika uzuri wa Angelina ulimchanganya, damu yake ilizunguka kwa kasi katika mishipa yake.

Na moyo ulidunda kwa kasi kama ulitaka kuchomoka.

Kwenye maisha yake aliwahi kukutana na wasichana wengi warembo, waliomtaka kiasi cha kushindwa kuamua ni yupi alitakiwa kuwa naye. Kati ya wote ambao alikutana nao basi kwa kifupi tu huyo Angelina alikuwa balaa.

Alikuwa mzuri, kama ulikuwa unatafuta maana halisi ya neno mzuri, basi ilipatikana kwa huyo Angelina. Alikuwa mrefu kidogo, miguu yake ilikuwa ya kawaida kwa maana ya si minene wala membamba, alikuwa na sura nyembamba ya Kitusi, hipsi zilichomoka kidogo na kichwani alikuwa na nywele za singasinga.

Huyo Angelina hakuisha hamu, alivutia na kupendeza machoni mwa kila mtu aliyewahi kumuona. Muda mwingi waliokuwa wamekaa kwenye viti macho ya Amon yalimwangalia mno msichana huyo kuliko watu wote waliokuwa mahali hapo.

Upendo aliokuwanao moyoni mwake ukawa mkubwa na kujiahidi kwamba piga ua ilikuwa ni lazima siku moja amuoe Angelina, aishi naye na kuzaa naye watoto.

“Ni mzuri sana! Hivi ni ndugu yako baba mmoja ama?” alimuuliza Gideon huku akimwangalia.
“Yeah!”
“Sasa mbona wewe mbaya sura kama nyani?” alimuuliza huku akianza kucheka.
“Hiyo ndiyo maana halisi ya mwanaume, ulitaka niwe mzuri kama wewe nitongozwe na wanaume wenzangu?” alimuuliza Amon, wakaendelea kucheka, kutaniana ilikuwa kawaida yao.

Wakati akiendelea na hayo yote, Amon alikuwa kidato cha tatu, aliambiwa asome na kucheza mpira, hakutaka kusoma lakini alifanya hivyo kwa ajili ya wazazi wake tu.

Maisha yao hayakuwa mzuri sana, baba yake hakuwa akifanya kazi kipindi hicho, aliwahi kuambiwa aliachishwa baada ya kuingia kwenye ulevi, hivyo mtu aliyekuwa akiingiza pesa alikuwa mama yao, yeye ndiye aliyekuwa akiilisha familia.

Ndoto ya Amon ya kuwa mchezaji mpira mkubwa duniani iliendelea kuchipua moyoni mwake, kila siku baba yake alimchukua na kwenda kutazama mpira kwenye vibandaumiza, alimwambia kuna siku angetamani kumuona akicheza, yaani awe anakwenda humo kumwangalia yeye tu.

“Nitaweza baba?” alimuuliza baba yake.

“Utaweza tu! Unajua kucheza mpira, una kipaji kikubwa sana, utaweza tu!” alisema baba yake.
“Kabisa baba?”
“Amon! Nisikilize mwanangu. Kila mtu aliyefanikiwa duniani alikuwa na ndoto zake moyoni, kufeli na kufanikiwa kwa watu kunaanzia mdomoni, unaotamka huwezi, jua kweli hautoweza na utakaposema utaweza, ni lazima utaweza kwa sababu umesema kwa mdomo wako,” alimwambia na kuendelea:

“Ninahitaji ufanikiwe. Kitu cha kwanza amini kwamba unaweza, unapoamini, Mungu anatenda kazi, usipoamini, shetani anaichukua hofu yako, anaigongelea msumali na maisha yako yote hautoweza kufanikiwa kwa kuwa haukuwa ukiamini.

“Ili ufanikiwe kuna mambo mawili, jambo la kwanza unatakiwa kutamka kwa ulimi wako, tena maneno yatoke ndani ya uvungu wa moyo wako,” alimwambia.
“Na la pili?”

“Utatakiwa kuamini kile unachokisema mdomoni mwako!” alimjibu.
“Uliwahi kuamini utakuja kuwa mchezaji mkubwa baadaye?” alimuuliza, swali lake lilikuwa na mtego mkubwa.
“Ndiyo! Niliamini!”
“Kwa nini hujawa?”
“Niliwahi kukwambia ni kwa sababu ya kuvunjika mguu. Baada ya kuona sitoendelea kucheza mpira, nikamwambia Mungu kwamba ninataka mtoto wangu mmoja aupende mpira, acheze na kufanikiwa, awe mchezaji mkubwa badala yangu. Baada ya kusema hivyo, nikaanza kuamini. Mungu akanipa wewe,” alimwambia.
“Aiseee!”

“Amon mwanangu! Unatembea na imani yangu! Unacheza sana mpira kwa sababu nilimuomba Mungu uwe kama hivyo hata kabla hujatoka tumboni mwa mama yako. Mungu wangu ni mwaminifu sana na ninaamini atajibu siku moja. Tutakaa sehemu na kukwambia sasa hivi wewe ni mchezaji bora wa dunia,” alisema mzee Stefano, kwa kumwangalia usoni tu alionekana kuwa siriazi kwa kile alichokuwa akikizungumza.
“Kweli itatokea?”

“Ukiamini itatokea, usipoamini, hutoweza kufika popote pale,” alimjibu.
Maneno ya siku hiyo yalimuingia kichwani Amon, akagundua ili ufanikiwe kwanza ulitakiwa kutamka na baada ya hapo kuamini. Aliona safari ndefu sana mbele yake lakini kwa maneno ya baba yake yakamfanya kuiona safari hiyo kuwa nyepesi kabisa.
Kuanzia siku hiyo akabadilika, kila alipokuwa akitazama mpira na baba yake, alimwambia kuna siku moja atakaa nyumbani na kumwangalia kwenye televisheni.

Mzee Stefano alifurahi sana kusikia hivyo, aliendelea kumwaminisha kila kitu ni rahisi mno, hapakuwa na jambo lolote lililokuwa gumu mbele za Mungu aliye hai.

Tangu alipoonana na Angelina hakuwahi kumuona tena japokuwa uzuri wake uliendelea kuwa kichwani mwake. Ukaribu wake na Gideon ukaongezeka, naye aliendelea kumsifia ndugu yake kwa rafiki huyo kwani aliamini kuna siku moja isiyokuwa na jina Amon asingekuwa hivyo, angekuwa mtu mwingine kabisa.

Alitamani mpaka siku hizo zinafika basi mtu pekee ambaye angekuwa na Amon awe ni ndugu yake na ndiyo maana alihakikisha anamshirikisha mambo mengi kuhusu msichana huyo.

Alisoma huku akiendelea na mazoezi, alifanya hivyo kwa mwaka mmoja, akaingia kidato cha nne. Hapo, baba yake akamsisitiza sana kuhusu elimu, alimwambia asome zaidi kwani kulikuwa na mtihani wa taifa mbeleni.

Kama alivyoambiwa ndivyo ilivyokuwa, alisoma sana, alisoma na kusoma huku ndoto yake ya kuwa mchezaji mpira ikiendelea kuwa kichwani mwake. Hakutaka kuwa dokta, mwanasheria ama mwalimu, kitu pekee alichokuwa akihitaji ni kuwa mchezaji mpira tu.
“Ngoja nimwambie Angelina awe anakufundisha, ana akili sana,” alisema Gideon.

Hiyo ilikuwa nafasi yake nyingine ya kuhakikisha Amon anakuwa na ndugu yake, alimwambia hivyo kwa kuwa alihitaji kuwaona hao wawili wakiwa pamoja.

Hilo likafanikiwa, akazungumza na Angelina ambaye kwake hapakuwa na tatizo lolote lile. Kila alipokuwa akitoka mazoezini, Amon alikwenda mpaka nyumbani kwa akila Gideon na kuanza kusoma, alikuwa akichoka sana lakini kwa kipindi kama hicho ilikuwa ni lazima kufanya hivyo.

Japokuwa Angelina alikazania kumfundisha sana Amon lakini mwenzake mawazo hayakuwa hapo kabisa, kila alipokuwa akimwangalia, alimpenda, uzuri wake haukuwa wa kawaida hata kidogo.
“Hivi unanielewa kweli?” aliuliza Angelina huku akimwangalia Amon.
“Unajua wewe ni mzuri sana,” alimwambia huku akitabasamu.
“Unaanza kuzungumzia uzuri sasa!”

“Kwani nadanganya?”
“Hebu shika kalamu kwanza, nataka tufanye haraka!” alimwambia.
“Naomba nikutoe out!”
“Ya wapi?”
“Tukale chakula popote pale, nitajisikia mwenye bahati sana kwenda pamoja nawe,” alimwambia.
Japokuwa Angelina hakuwa na muda huo lakini aliamua kumkubalia tu. Maneno aliyokuwa akiambiwa kuwa ni mzuri yalianza kuubadilisha moyo wake taratibu, akaanza kuona raha na mwisho kabisa akakubaliana kutoka naye mtoko wa chakula.

Amon hakuwa na kitu mfukoni, Angelina alilielewa hilo, walipotoka, msichana huyo alitumia pesa zake, walikuwa wakizungumza mengi na ndiyo siku hiyo uhusiano wao ukaanza, safari ndefu ya mapenzi ilianzia siku hiyo.
“Unataka kuwa nani hapo baadaye?” aliuliza Amon huku akimwangalia msichana huyo.
“Cardiologist!” alimjibu.
“Ndiyo nini?”
“Daktari wa misuli!”
“Ooh!”

“Na wewe unataka kuwa nani?” alimtupia swali.
“Mchezaji wa mpira maarufu sana, kama Cristiano Ronaldo au Messi!” alimjibu.
“Mchezaji wa mpira?”
“Ndiyo!”
“Wa miguu?”
“Huyohuyo!”
“Mh!”
“Nini sasa?”
“Hamna kitu!”

Je, nini kitaendelea?

Sent from my SM-A107F using JamiiForums mobile app
 
SEHEMU YA 03

Kwa Angelina kilikuwa kama kitu kisichowezekana, ni kweli alisikia Amon alikuwa akicheza mpira na ndugu yake lakini moyo wake haukutaka kuamini kama angeweza kuwa mchezaji mpira maarufu hapo baadaye.

Alikuwa na uwezo wa kumwambia asingeweza lakini hakutaka kufanya hivyo zaidi ya kumtia moyo kuwa angeweza tu ila alitakiwa kupambana sana.

Kulikuwa na watu wengi waliokuwa wakicheza mpira, walitoka kwenye familia za hovyo, waliziinua familia zao, walipata pesa kubwa na kupata kila kitu walichokuwa wakihitaji, kwa Amon, endapo angefanikiwa na kuwa mchezaji mpira mkubwa, Angelina aliamini angefanikiwa mno na kuwa na pesa nyingi, umaarufu na mengine mengi.

“Nitanunua gari la kifahari na kuishi kama tajiri, kila likizo nitakwenda Marekani, natamani sana nifike Los Angeles kwa kuwa kuna maisha mazuri sana, Mungu akifanikisha, nitakuwa na hoteli kule,” alimwambia Angelina.

“Una ndoto kubwa sana Amon.”

“Ni kwa sababu naamini kwenye kipaji changu, ninaamini kuna siku yote yatatokea, na nitakukumbusha hili ninalokwambia leo,” alisema Amon, wakati huo walikuwa wamepanda Bajaj mpaka Kinondoni alipokuwa akiishi msichana huyo, wakaachana na yeye kuelekea nyumbani.

Siku ziliendelea kukatika huku wawili hao wakiendelea kuwa karibu, muda mwingi walikuwa wakionana, walisoma pamoja huku penzi lile walilolianzisha likiendelea kukua kila siku.

Wazazi wao hawakujua kama wawili hao walikuwa wapenzi, ilikuwa siri kubwa, mtu pekee ambaye aliyafahamu hayo yote alikuwa Gideon ambaye aliambiwa kuyafanya kuwa siri kubwa.

Baada ya miezi kadhaa, hatimaye mtihani wa taifa wa kidato cha nne ukawadia na wawili hao kufanya. Kila mmoja alikuwa na matumaini makubwa ya kufanya vizuri kwani walisoma sana na waliamini ndoto zao nyingine zingeweza kutimia endapo tu wangefaulu mtihani huo.

Mtihani ukafanyika na hatimaye wakaanza kusubiri matokeo. Katika kipindi hicho walikuwa karibu zaidi, walikuwa wakikutana na kuzungumza mambo mengi. Amon hakuacha kucheza mpira kwa mafanikio makubwa, alisifiwa kila kona na mara nyingi alikuwa akipelekwa mpirani na mpenzi wake, Angelina.

Aliyaona mafanikio mbele yake, alijua tu kuna siku angefanikiwa na kuwa mchezaji mkubwa tu, hivyo alikuwa akipambana kwa nguvu zote kufikia mafanikio yake hayo.

Baada ya miezi kadhaa, hatimaye matokeo ya kidato cha nne yakatoka, kwa Angelina yalikuwa mazuri sana ila kwa Amon, alifeli vibaya na kupata Division 0.

Moyo wake uliuma mno, hakuamini kama angefeli namna hiyo, ni kweli hakuwa na akili za darasani kwa kiwango kikubwa lakini si kufeli kwa namna hiyo.

Siku nzima ya matokeo akakaa chumbani kwake, alikuwa akilia, aliona aibu na kuuona mwisho wa maisha yake. Aliwakumbuka wanafunzi ambao walikuwa na ndoto za kuwa na nyadhifa kubwa serikalini, kwake, zisingeweza kutokea tena kwa sababu tu alifeli mitihani hiyo.

Hakutaka kuongea na mtu siku hiyo, ilikuwa ni ya huzuni tele, aliiona dunia kama ikimuelemea na wakati alikuwa na uwezo mdogo wa kupambana nayo. Mama yake aligonga mlango mara kadhaa, hakufungua, kaka zake waligonga mlango lakini napo hakufungua.

Angelina alimpigia simu sana lakini hakupokea, hakuwa na cha kumwambia, msichana wa watu alifanya kila kitu kuhakikisha anafaulu lakini hakuna lililowezekana, alifeli vibaya.

Baba yake aliporudi, kitu cha kwanza kuambiwa na mama yake kilichotokea, kuhusu matokeo ya Amon, hivyo mzee Stephano kuelekea mlangoni na kuanza kuugonga mlango.

“Ronaldo! Fungua mlango!” alisema baba yake.

Ni jina hilo ndilo likamfanya Amon kuinuka kutoka kitandani na haraka sana kuelekea mlangoni, akaufungua mlango na baba yake kuingia ndani.

Uso wake ulikuwa kwenye tabasamu pana, Amon alishangaa, alijiuliza kama baba yake aliambiwa kuhusu matokeo yake ama la! Kama aliambiwa, sasa kwa nini alikuwa anatabasamu kana kwamba kulikuwa na jambo zuri mbele yake.

“Hebu nikumbushe kuhusu ndoto yako!” alisema mzee Stephano hata kabla ya salamu.

“Kuwa mwanasoka mkubwa duniani!” Amon alijibu.

“Niambie wachezaji watatu ambao wamesoma sana!” alimwambia.

Amon akabaki kimya.

“Pele hakusoma, Ronaldo hakusoma, Ronaldinho hakusoma, Wayne Rooney hakusoma, ila wote hao wakaja kufanikiwa, wakaanzisha kampuni na kuwaajiri watu ambao wamesoma sana na kuwa na PhD. Kwa nini una huzuni? Au ndoto yako ilikuwa ni kutaka kuwa mwanasheria?” alisema baba yake na kumuuliza.

“Hapana! Ninataka kuwa mwanasoka,” alijibu.

“Basi pambania ndoto yako. Mungu amekuumba kuwa mwanasoka na si daktari wala mwanasheria. Mwanasoka hata akifeli masomo yote, bado anaweza kutimiza ndoto zake. Inuka ukapambanie ndoto yako,” alisema baba yake. Hakutaka kukaa sana, akainuka na kutoka ndani ya chumba kile.

Maneno hayo yalimfanya Amon kubaki kimya na kumwangalia baba yake, alichokisema ni kweli kabisa, kulikuwa na wanasoka wakubwa ambao walifanikiwa bila kusoma. Elimu haikuwa na nafasi kwenye mpira, kilichokuwa kikihitajika ni kipaji tu.

Hapo akagundua kwamba hata kama amefeli vibaya bado alikuwa na nafasi ya kutimiza ndoto zake, alikuwa na uwezo wa kufanya chochote alichokitaka kwenye ndoto yake hiyo.

Akainuka na kusimama, amani ya moyo wake ikaanza kurudi, furaha ambayo ilikimbia, sasa nayo ikaanza kurudi moyoni mwake, maneno ya baba yake yakamtia nguvu na kumwambia alikuwa nani.

Kuanzia siku hiyo akaanza kufanya mazoezi zaidi ya alivyokuwa akifanya kabla, alibakiza ndoto moja tu maishani mwake, endapo hiyo ingekufa, maisha yasingekuwa na thamani yoyote ile kwake.

Alibadilisha mfumo wake wa maisha, hakutakiwa kuishi kama alivyokuwa akiishi kipindi cha nyuma, ilikuwa ni lazima kuanza kuishi upya kabisa, awe na mipango madhubuti ya kufanikisha kile alichokuwanacho.

Angelina alikuwa akimtafuta kwenye simu lakini hakuweza kumpata, Amon aliamua kuacha kutumia simu kwa muda kwa kuwa hiyo ingemfanya kuweka umakini zaidi kwenye mpira.

Alikuwa mchezaji hatari, aliyejua kufunga mabao mengi akiwa uwanjani, jina lake likawa gumzo na kila kona alipokuwa akipita, watu walikuwa wakimzungumzia. Kwa kuwa alikuwa akisoma katika chuo maalumu cha mpira wa miguu, wazazi wake wakashauriwa kumuacha kituoni hapo, maisha yake yawe hapo na kucheza mpira kadiri alivyoweza.

Hilo likawa nafuu kwake, likamtoa kwenye maisha ya nyumbani na mtaani na kuingia kwenye maisha mengine, ya mpira wa miguu na kila kitu alichokuwa akikifanya mahali hapo kilikuwa ni mpira tu.

Urafiki wake na Gideon uliendelea kuwa mkubwa, walikuwa pamoja na walifanya mambo mengi wakiwa pamoja. Kwa Angelina ambaye alimtafuta sana Amon bila mafanikio, akaamua kumshirikisha ndugu yake huyo suala hilo na ndipo akaambiwa Amon aliamua kubaki kituoni, maisha yake yalikuwa hapo na asingeweza kurudi mtaani tena.

Hilo lilimuumiza mno, Amon aliamua kufanya maamuzi bila kumshirikisha, alisikia kitu chenye ncha kali kikiuchoma moyo wake, alijua kabisa kwamba kijana huyo alikuwa mpenzi wake, walishirikiana na mambo mengi, hivyo kuamua kwenda kuishi kituoni kwake haikumfurahisha hata kidogo.

Hakutaka kukubali, ilikuwa ni lazima kwenda kuonana naye, siku ambayo wazazi wake walikwenda kumtembelea Gideon kituoni na kuangalia maendeleo yake, naye akaenda, alimpanga Gideon mapema kabisa endapo angefika hapo basi amuitie Amon, wakae sehemu na kuongea mambo mengine.

Amon alipoambiwa hivyo, akanyong’onyea, hakutaka kuonana na msichana huyo, ni kweli alimpenda lakini matokeo yale yalimfanya kutokuwa na furaha hata kidogo ingawa tayari alianza kusahau.

Alimkatalia Gideon lakini kijana huyo akaanza kumuomba sana kwa kumwambia dada yake hakuwa na furaha hata kidogo, alimfikiria kila wakati, hivyo aliomba sana kwenda kuonana naye na si kumkatalia kama ilivyokuwa.

Kwa kuwa aliombwa sana, hakuwa na jinsi, akakubali na siku ambayo watu hao walifika kituoni hapo, akamchukua Angelina na kwenda pembeni kuzungumza naye.

Japokuwa hakutaka kuonana na msichana huyo lakini baada ya kumtia machoni mwake, moyo wake ukabadilika kabisa, yale mapenzi yaliyokuwa yameanza kujificha yakarudi kwa nguvu kubwa.

Alimwangalia Angelina, alionekana kuwa tofauti, ule uzuri aliokuwanao kipindi cha nyuma ulikuwa tofauti na kipindi hicho, alivutia, alikuwa na uzuri zaidi ya kipindi cha nyuma.

Pale alipokaa alitamani kumsogelea na kumkumbatia, ambusu na kumnong’oneza sikioni mwake ni kwa namna gani alikuwa akimpenda kuliko mwanamke yeyote katika dunia hii.

“Kwa nini umeamua kufanya hivi?” aliuliza Angelina huku akimwangalia Amon usoni.

“Nilichanganyikiwa sana! Naomba unisamehe sana,” alisema Amon.

Hakutaka kueleza maneno mengi, kwenye suala lolote pale unapoonekana kukosea, kitu cha kwanza ni kuomba msamaha tu. Wapo watu wengine waliokuwa wakitafuta sababu za kila aina, pale zitakapoonekana zimeshindwa kumshawishi mtu ndipo waombe msamaha.

Kwa Amon ilikuwa ni tofauti, ilikuwa ni lazima kumuomba msamaha msichana huyo kwa kuwa alijua alimkosea, kuwa na matokeo mabovu haikumaanisha kumuacha na kufanya mambo yake.

“Nimekusamehe mpenzi! Unafikiria nini kuhusu huu uhusiano?” alimuuliza.

“Nije kukuoa na kuishi na wewe, uwe unanitibu kila ninapopata matatizo ya misuli, si unajua mpira unavyokuwa,” alisema Amon huku kwa mbali tabasamu pana likiwa usoni mwake.

Walizungumza mambo mengi, kila mmoja alimwambia mwenzake ni kwa namna gani alikuwa akimpenda. Moyo wa Angelina ukabadilika, ile furaha iliyokuwa imepotea ikaanza kurudi tena moyoni mwake, huyo Amon alikuwa moyo wake, pumzi yake, alimpenda kupita kawaida.

Maisha yao yaliendelea kama kawaida, Angelina akajiunga na Shule ya Wasichana ya Kisutu huku Amon akiendelea na mambo yake ya mipira.

Baba yake hakuacha kumtia moyo, kila siku kwenye maisha yake aliamini kuwa Amon ndiye mtu atakayekuja kuitoa familia katika maisha waliyokuwanayo kipindi hicho. Alikuwa na miaka kumi na tano lakini aliamini mpaka anafikisha miaka thelathini tayari angekuwa ametimiza ndoto zote alizokuwa amejiwekea kwenye maisha yake.

Baada ya siku kadhaa, hatimaye kituo hicho cha mpira kikapokea barua kutoka nchini Ujerumani, timu yao ilialikwa kwenda kushiriki mashindano ya vijana yaliyokuwa yakitarajiwa kufanyika nchini humo.

Kila mmoja alikuwa na furaha tele baada ya kupokea barua kutoka nchini Ujerumani, na kitu kilichofanyika ni kwa wao kuanza kuchagua timu ambayo ingekwenda kukiwakilisha kituo hicho nchini Ujerumani.

Kila mzazi alikuwa na hamu ya kuona mtoto wake akielekea nchini huko, wapo wengine waliotoa pesa ili watoto wao waende lakini pia wapo ambao hawakufanya hivyo kwa kuwa waliamini watoto wao walikuwa na uwezo mkubwa.

Amon alitulia tu, alikuwa na hamu ya kuelekea nchini Ujerumani, kucheza mpira lakini kwa kile kilichokuwa kikiendelea kituoni hapo, kwamba wazazi walitoa pesa kwa ajili ya watoto wao kwenda nchini humo, hakuona dalili za yeye kwenda ingawa alikuwa na uwezo.

Alimwambia baba yake, aliiona hiyo kuwa furasa lakini mazingira ya rushwa yalimfanya kutokuwa na amani hata kidogo, alitamani kuhonga endapo tu angekuwa na pesa ili mtoto wake aende Ujerumani lakini ilishindikana, wakabaki wakimuomba Mungu.

“Ila si una uwezo? Naamini utakwenda tu,” alisema baba yake.

Aliamua kumtia moyo kwa kuwa kila alipomwangalia Amon, alionekana kukata tamaa, hakuona kama kungekuwa na dalili za kuchaguliwa na kwenda nchini humo.

Baada ya siku kadhaa, hatimaye majina yakatangazwa na miongoni ma vijana ishirini na tatu ambao walitakiwa kwenda Ujerumani, jina la Amon na Gideon yalikuwa miongoni mwa watu hao.

Hakuamini masikio yake, akamsogelea Gideon na kumkumbatia. Kwake ilikuwa ni miujiza, hakuwahi kuhisi kama angekwenda Ulaya akiwa na umri mdogo kama aliokuwanao, alijua angeishia kucheza nchini Tanzania lakini mwisho wa siku, akafanikiwa kuchaguliwa na hivyo kutakiwa kwenda huko.

Ilikuwa ni furaha kwao, kwa wazazi wao, wakafanyiwa maandalizi yote na baada ya wiki moja wakawa ndani ya ndege na kuelekea nchini Ujerumani.

Amon alikuwa kimya, hapo imani yake ya kuwa mchezaji mkubwa duniani ikazidi kuongezeka, kila kitu kilichokuwa kikiendelea kwake kilikuwa kama ndoto fulani hivi ambapo baada ya dakika kadhaa angeamka na kujikuta kitandani.

Masikini yeye, leo hii alikuwa akienda Ujerumani, ni kweli ilikuwa ni kwenda kushiriki mashindano na kurudi lakini tayari kwake yalionekana kuwa mafanikio makubwa mno. Ndani ya ndege kwenye viti vya watu wawili alikaa na Gideon, walikuwa wakiongea mambo mengi, kila mmoja uso wake ulikuwa na furaha tele.

“Siamini kama nimepanda ndege,” alisema Amon huku akijaribu kuyaangalia mawingu kupitia kidirisha kidogo.

“Ni ndoto ya kila mmoja. Wazazi wangu wana uwezo ila sikuwahi kupanda ndege aiseee,” alisema Gideon.

“Na Angelina amekwishawahi kupanda ndege?”

“Apandie wapi? Aende wapi sasa? Labda kutoka sebuleni kwenda chumbani!” alisema Gideon huku akicheka.

“Nitampandisha ndege siku moja. Nadhani hii ndiyo nafasi,” alisema Amon huku akionekana kuwa na raha sana.

“Yaani na siku ikitokea umemsaliti mdogo wangu, we fala nitakukamua haja kubwa,” alisema Gideon.

“Na yeye siku akinisaliti?”

“Hahaha! Dada yangu hawezi bwana,” alisema Gideon.

Safari iliendelea, baada ya saa kama ishirini, ndege ikafika nchini Uholanzi ambapo wakabadilisha ndege, wakachukua ndege nyingine na kwenda nchini Ujerumani ambapo hakukuwa mbali na hapo.

Ndege ikaanza kutua kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Berlin. Hali ya hewa nchini Ujerumani ilikuwa ni tofauti na barani Afrika, kulikuwa na baridi kali, hasa kipindi hicho, mwezi wa kwanza ambapo nchini nyingi za Ulaya huwa kwenye baridi kali kali kiasi cha kudondosha theluji ardhini.

Wakaanza kuteremka kutoka ndani ya ndege, kila mmoja alikuwa na koti kubwa. Kukanyaga ardhi ya Ujerumani, kwa Amon ilikuwa ni sawa na kuyaacha matatizo yake yote nchini Tanzania, alijiona kuwa mtu mpya na kila alipokuwa akipiga hatua, alijisemea moyoni kwamba kuna siku dunia ingemjua alikuwa nani, leo hii alikuwa akipita huku watu wakiwa hawana habari naye ila kuna siku kila mtu ambaye angemuona, angetaka kusainiwa kitabu chake.

Baada ya kukamilisha taratibu zote hapo uwanjani, wakatoka, wakapokewa na kituo cha Hohenschonhausen. Wakaingia kwenye basi kubwa na kuondoka mahali hapo.

Macho ya Amon yalikuwa yakiangalia huku na kule, kwa jinsi jini la Berlin lilivyokuwa limepangwa, hakuamini kama alikuwa kwenye dunia ileile iliyokuwa na Jiji la Dar es Salaam.

Aliliangalia jiji hilo, kama vitabu vya dini vilisema Mbinguni palikuwa pazuri kuliko duniani, akaanza kupafikiria huko Mbinguni palikuwaje kwani muonekano wa jiji hilo ulikuwa ni wa kipekee sana.

Hawakuchukua dakika nyingi, wakafika katika makao makuu ya kituo hicho, wakakaribishwa vyumbani, wakajiandaa, wakaenda kula chakula huku wakiwa wameungana na vijana wengine na kufanya timu zote kuwa nane, wangeanza michuano hiyo baada ya siku mbili.

Je, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 04.

“Ila Angelina ni mzuri sana,” alisema kijana mmoja, alikuwa pembeni ya gari lake, kabla ya kuondoka, alikuwa akizungumza na marafiki zake.
Wakati akizungumza hayo macho yake yalikuwa kwa Angelina, alikuwa mmoja wa wanawake wazuri aliowahi kukutana nao maishani mwake. Alibaki akimwangalia kwa dakika kadhaa.
Hakuwahi kumchoka, kila siku alipomwangalia, alihisi mapenzi mazito moyoni mwake na kujisemea ni lazima piga ua siku moja awe mke wake wa ndoa.
Kijana huyo aliitwa Edmund Zilikana. Alijiamini, katika maisha yake hakuwahi kukataliwa na mwanamke yeyote yule kwa sababu kuu mbili, moja; alikuwa mzuri wa sura lakini la pili alitoka kwenye familia iliyokuwa na pesa.
Shuleni hapo yeye peke yake, labda na baadhi ya walimu ndiyo waliokuwa wakienda na magari. Alikuwa na sifa, alitamba na kujiamini kwa kila kitu.
Kulikuwa na wasichana wengi waliokuwa wakitamani sana kuwa naye lakini hakuwahi kukubali hata mara moja, hakuwa na muda nao na mtu pekee aliyekuwa akimtamani sana kutoka moyoni mwake alikuwa huyo Angelina.
Wakati akizungumza hayo alikuwa na wanafunzi wenzake wa kiume, kila mmoja alipomsikia akimsifia Angelina alikubaliana naye na kumwambia alikuwa na uwezo wa kumfuata, kumtongoza na hatimaye kuwa naye.
Kwa kipindi cha miezi mitatu ya kwanza hapo shuleni, Angelina alifuatwa na wavulana mbalimbali, walimtongoza lakini kamwe hakutaka kuwakubali, mawazo yake yalikuwa kwa mtu mmoja, aliyeuteka moyo wake na kuugalagaza vilivyo, mtu huyo alikuwa Amon.
Huyo ndiye aliyekuwa akijivunia naye, haikuwa siri, hakutaka kujifanya kutunza sana siri kwenye uhusiano huo, kila alipokuwa akifuatwa na mwanaume, alimwambia dhahiri alikuwa na mpenzi aliyekuwa akimpenda sana na kamwe asingeweza kumuacha.
Wengi walikasirika na kuumia, wakatamani kumuona mwanaume huyo, alifananaje? Alikuwa na pesa? Umaarufu, kila mtu akataka kumuona tu, waliamini alikuwa mmoja wa wanaume waliokuwa na bahati ya kuwa na wanawake wazuri.
“Nataka nimfuate na kuzungumza naye, ameuteka sana moyo wangu,” alisema Edmund huku akiwaangalia wenzake.
“Atakubali?”
“Kwa nini akatae?”
“Kuna wengi wamemfuata!”
“Halafu?”
“Wamekataliwa!”
“Sababu?”
“Eti ana mtu wake!”
“Mtu gani?”
“Wala hatumjui, nadhani huko kwao,” alijibu jamaa mmoja.
Kwa Edmund hakutaka kukubali, hakuamini kama kulikuwa na mwanamke aliyekuwa na uwezo wa kumkataa, kulikuwa na wanawake wengi waliomfuata, walimtongoza kila leo hivyo aliamini hata huyo Angelina asingeweza kumfanya lolote lile
Hakutaka kumfuata siku hiyo, alitaka kumpa muda kwanza kama wa siku mbili na baada ya hapo ndipo amfuate na kumwambia ukweli wa moyo wake. Alisubiri, akawa mvumilivu na baada ya siku hizo akaamua kumfuata.
Siku hiyo Angelina alikuwa amekaa kwenye kiti chake akisubiri muda wa vipindi vianze, darasani kulikuwa na watu wengi waliokuwa wakifanya mambo yao, Edmund alivyoingia tu, watu wote wakamwangalia, ukimya kidogo ukapita kwa staili ya kusema kuna shetani kapita.
Edmund hakutaka kujali sana, alisimama na kuangalia huku na kule, macho yake yakatua kwa Angelina aliyekuwa bize na kitabu chake cha simulizi cha Damu ya Mwanamwali Kitandani kilichoandikwa na mwandishi, Ally Katalambula.
Haraka sana Edmund akachomoka pale mlangoni na kumfuata msichana huyo huku uso wake ukiwa na tabasamu pana.
Wanafunzi wote walikuwa wakimwangalia, walitaka kuona kile ambacho kingetokea kwani kwa mtu kama Angelina hakuwa rahisi kuzungumza na mwanaume ambaye hakuwa na mazoea naye.
“Angelina!” aliita mara baada ya kumfikia.
Akayainua macho yake na kumwangalia mtu aliyemuita, alikuwa Edmund, alimfahamu mwanaume huyo kwa kusikia sifa zake kemkemu lakini hakutaka kuzifuatilia sana.
“Naruhusiwa kukaa?” aliuliza huku akikivuta kiti cha pembeni.
“Muda wa masomo!”
“Ila sitochukua muda mrefu!”
“Hapana! Unaweza ukaniacha nikaendelea kusoma?” alimuuliza huku akimwangalia.
“Naomba nikuone baadaye!”
“Sina muda. Ninakuwa bize sana, samahani.”
“Angelina! Ninahitaji kuzungumza nawe, dakika tano tu zitatosha,” alimwambia huku akijitahidi kuweka sura iliyokuwa na huruma tele.
Angelina hakutaka kuzungumza kitu chochote kile, alimwangalia na kuendelea kusoma kitabu chake. Wasichana waliokuwa wakiangalia tukio lile roho iliwauma mno, hawakuamini kama Angelina alikuwa akileta dharau kama zile, kwa mtu kama Edmund ambaye alikuwa akitakwa na kila msichana.
Kwake hakujali, mtu aliyekuwa naye alikuwa wa umuhimu kuliko huyo aliyekuwa amemfuata, wengi waliambiwa Angelina alikuwa na mpenzi wake na kama alimletea jeuri Edmund basi waliamini inawezekana msichana huyo alikuwa na mpenzi mwenye uwezo kuliko huyo Edmund.
Edmund akawa mnyonge, akaanza kujisikia aibu pale alipokuwa, akasimama na kuondoka huku akionekana kuwa mpole tofauti na alivyokwenda. Kila mmoja alimuonea huruma na walipomwangalia Angelina, hakuwa na habari yoyote ile, kwake, kile kilichotokea ndicho kilichotakiwa kutokea.
Kwa Edmund huo haukuwa mwisho, aliamini kabisa siku zote mwanzo huwa mgumu sana, alitaka kujipa muda zaidi ya kuzoeana na msichana huyo lakini mwisho wa siku amchukue na kuwa mpenzi wa maisha yake.
Alichokifanya baada ya kuondoka ni kusubiri mpaka muda wa mchana na kuanza kumtafuta tena Angelina. Hakukoma, bado kila alipokuwa akiangalia mbele aliona kabisa alikuwa akienda kuwa mpenzi wa Angelina, na alijiahidi kwamba ni lazima amuoe na kuwa naye maisha yake yote.
Kwenye kumtafuta, hatimaye akamuona na kumfuata kwa lengo la kutaka kuzungumza naye. Angelina alikuwa na marafiki zake, walipomuona Edmund amesimama mbele yao, wote wakaondoka na kumuacha msichana huyo peke yake, wakaanza kuangaliana.
“Umependeza sana,” alisema Edmund huku akimwangalia.
“Kawaida tu!”
“Inawezekana kwako, ila si kwangu. Kila ninapokuangalia, macho yangu yanakuwa na hamu ya kukuangalia zaidi na zaidi,” alisema Edmund.
“Sawa.”
“Naomba unisamehe kama nilikukosea asubuhi. Nilishindwa tu kujizuia,” alimwambia.
“Usijali!”
“Nitahitaji nizungumze nawe mambo mengi tu!”
“Haiwezekani!”
“Kwa sababu gani Angelina? Sitopenda nizungumze nawe mahali hapa, najua unaogopa labda, nataka upate muda wa kuzungumza nawe nje ya hapa. Nakuomba,” alimwambia.
“Haiwezekani!”
“Kwa sababu gani?”
“Sina muda.”
“Angelinaaaa...”
“Nadhani umesikia na kunielewa, ahsante,” alisema msichana huyo, akasimama na kuanza kuondoka zake.
Kwa mara ya pili Edmund aligonga mwamba, hakuamini kama kweli alikataliwa na msichana huyo, hakuzoea maisha hayo, kila alipomfuata mwanamke yeyote yule, wala hakuchukua dakika nyingi tayari walikubaliana na kuwa naye lakini kwa Angelina ilikuwa tofauti kabisa.
Hapo ndipo alipopata jibu kwamba si kila mwanamke alikuwa na tamaa ya kuwa na mwanaume aliyekuwa na kipato kikubwa ama mali, wengine walikuwa wakiangalia malengo yao, hata walipokuwa na watu wasiokuwa na pesa, mioyo yao iliamini kuna siku wangepata pesa na kubadilisha maisha yao kwa ujumla.
Alibaki akiwa amesimama huku akimwangalia msichana huyo aliyekuwa akiondoka zake mahali hapo. Alitamani amuite na kuzungumza naye tena lakini ilishindikana kabisa, alipotea machoni mwake na kutoka nje ya eneo la shule hilo.
“Nitampata tu! Nitamuoa na kuwa naye maisha yangu yote,” alisema Edmund, moyo wake ulikuwa na uhakika kwamba kuna siku isiyokuwa na jina angekuwa na msichana huyo mrembo.

Je, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 05

Kama kulikuwa na matukio ambayo yanaweza kuonekana kama ndoto machoni mwako basi kwa lile la Amon kusafiri na kwenda nchini Ujerumani tayari kwa kushiriki mashindano ya mpira na timu yake ya kituo chao kutoka Tanzania basi ingeweza kuwa ndoto kubwa.
Hakuwa akiamini macho yake, kwa kile kilichokuwa kikiendelea kilionekana kama moja ya ndoto kubwa.
Vyumbani walikuwa wakikaa wawili wawili, alichagua chumba cha kukaa na Gideon, kila mara alikuwa akimwambia ni kwa namna gani alitamani sana kuona akiwa na msichana wake, Angelina.
Huo ndiyo ulikuwa moyo wake, hapakuwa na kitu alichokipenda kama huyo, alimthamini na kumuweka namba moja mbali na wazazi wake na ndugu zake wa kuzaliwa tumbo moja.
Alitamani kuwa na msichana huyo muda wote na hilo hakusita kumwambia Gideon, alitaka kujua ni kwa namna gani alikuwa akimpenda ndugu yake na alikuwa tayari kwa lolote lile.
Usiku mzima siku hiyo walikuwa wakiongea mambo mengi, kila mmoja hakuwa akiamini kama kweli walikuwa nchini Ujerumani, moja ya nchi za Ulaya waliyotamani sana kwenda.
“Nitacheza mpira mpaka nichanganyikiwe,” alisema Amon huku akimwangalia Gideon.
“Tukomae! Hii ndiyo nafasi yetu, bila hivyo tutashindwa kabisa na kwenda kuishi Tanzania,” alisema Gideon huku akimwangalia Amon.
Walipanga kucheza kwa juhudi zote kwa kuwa huo ndiyo ungekuwa mwanzo wa kupata maisha mazuri. Walijua kulikuwa na watu wengi waliotamani sana kuingia nchini humo, kucheza mpira na kufanikiwa, wawe na maisha mazuri kama wachezaji wengine na ndiyo maana walipanga kucheza kwa nguvu zote.
Siku iliyofuata walianza mazoezi kamili kwenye uwanja wa Chuo cha Berlin. Hapo, wanachuo walijazana na kuanza kuwaangalia. Kwa nchi za Ulaya, kulikuwa na idadi kubwa ya watu waliokuwa wakipenda mpira wa miguu, hivyo walivutiwa na kuwaangalia watu hao.
Kwa jinsi walivyokuwa wakicheza, kila mmoja aliona kabisa watu hao walikuwa siriazi na mpira, hawakuwa na utani hata kidogo. Walijua kutuliza mpira, kupiga chenga na hata kufunga.
Amon ndiye alionekana kuwa mtu hatari, alikuwa na kasi kubwa, kwenye mazoezi tu alionekana kuwa tishio kiasi cha watu kugundua huyo ndiye alikuwa roho ya timu hiyo, alipenda kufunga mabao kuliko kitu chochote kile.
Walifanya mazoezi kwa siku kadhaa na hatimaye siku waliyokuwa wakiisubiri kuwadia, kuanza mashindano hayo. Muda mwingi Amon alikuwa akimuomba Mungu, alitamani kucheza mpira kama alivyokuwa akicheza Tanzania, asipate tatizo lolote lile, yaani ule ubora wake wa nchini humo uonekane huko.
Mechi yao ya kwanza kwenye makundi walikuwa wakikutana na timu ya vijana ya Hertha Berlin ya hapohapo Ujerumani. Wakati mpira unaanza tu watu walijua timu hiyo ya nchini Ujerumani ingeweza kushinda kwa mabao mengi lakini kilichotokea, Amon alionekana kuwa mwiba mkali mbele yao.
Alijua kuwanyanyasa mabeki waliokuwa na uchu wa kupana na kupeleka mashambulizi, hakuwa mshambuliaji wa kutulia, alikuwa mtu hatari ambaye aliwasumbua sana.
Uwezo wake wa kufunga mabao ndiyo ulioonekana kwani mpaka mechi inakwenda mapumziko, tayari alifunga mabao mawili na kuwaacha wenyeji wakishangaa tu.
Huyu Amon alikuwa mtu tofauti kabisa, alikuwa mdogo lakini uwezo wake wengi walisema angekuwa mrithi sahihi wa Lionel Messi, alijua kupiga chenga na kufanya vitu vingi ambavyo Messi alikuwa akivifanya, tofauti ni kwamba mchezaji huyo wa FC Barcelona alikuwa na uwezo wa ziada zaidi yake.
Amon akaonekana kuwa kivutio, kila mtu alitaka kumwangalia akicheza kama ilivyokuwa kwa Ronaldinho, kila alipogunda mpira watu walikuwa wakimshangilia, pale alipokuwa akifunga, kelele nyingi zikalipuka.
Hiyo ilikuwa mechi ya kwanza ambayo Amon alionyesha uwezo mkubwa na kuiwezesha timu yake kuibuka na ushindi mnono wa mabao matano huku akiwa amefunga mabao matatu na Gideon kufunga mawili.
Umahiri wake ukawafanya watu kuwaambia wengine kuanza kumfuatilia kijana huyo. Mawakala mbalimbali wa timu za hapo Berlin wakafika na kuanza kumwangalia, walihitaji kuona kile kilichokuwa kikizungumzwa na watu wengi.
Uwezo wake uliwashangaza sana, hakutakiwa kuishi nchini Tanzania, kwa uwezo aliokuwanao alitakiwa kucheza moja ya ligi kubwa barani Ulaya. Mechi zilipokuwa zikiisha, alifuatwa na waandishi wa habari wa kujitegemea wa mitandao ya kijamii na kuanza kumuhoji.
Akaanza kupata umaarufu mdogo mitandaoni hapo Ujerumani, kila mtu aliyemsoma alitamani sana kumuona kwani alipambwa kiasi cha kila mtu ambaye hakuwahi kumuona kujuta, hivyo mechi iliyofuata kujazana uwanjani.
Timu kutoka Tanzania ikawa maarufu, ikapendwa, ikaanza kukusanya watu wengi uwanjani. Kila walipokuwa wakisikia timu hiyo inacheza, watu waliacha mambo yao na kwenda uwanjani, walitaka kumuona huyo Amon tu, alichezaje na kwa jinsi gani alikuwa tishio na kutangazwa sana mitandaoni.
Watu wengi walimpenda na kuubali uwezo wake, miongoni mwa watu hao alikuwa msichana wa miaka ishirini, aitwaye kwa jina la Anita Windhorst.
Huyu alikuwa binti mrembo aliyekuwa akiisimamia klabu ya Hertha Berlin ambayo ilikuwa ikimilikiwa na baba yake, mzee Lars Windhorst. Hakuwa na lengo la kuangalia mashindano hayo, alikuwa bize na masuala ya kazi na masomo ambayo ndiyo alikuwa akimaliza mwaka huo.
Baba yake alikuwa na pesa ndefu, alikuwa akimiliki timu hiyo ambayo kwa kipindi hicho ndiyo ilikuwa imepanda daraja nchini Ujerumani. Siku mbili kabla aliambiwa na rafiki yake kuhusu huyo Amon kwamba alikuwa mmoja wa wachezaji tishio sana ambao kama wangemchukua basi inawezekana timu yao ingekuwa na nguvu fulani.
Kwanza akapuuzia, alipoambiwa alikuwa Mwafrika, hakutaka kuamini kama angejua kucheza mpira kama alivyoambiwa. Kila siku alimwambia rafiki yake huyo kwamba angekwenda kumuona huyo Amon lakini hakuwa akifanya hivyo.
Huku siku zikiwa zimebaki chache ndipo akakutana na jina hilo kwenye mitandao ya kijamii na picha za kijana huyo. Picha hizo ziliendana na video, alizifungua na kuziangalia.
Hakuamini macho yake kama alikuwa akimwangalia kijana kutoka barani Afrika, alikuwa na uwezo mkubwa, aliwanyanyasa Wazungu alivyotaka yeye, uwezo wake ulikuwa mkubwa mno.
Hapo ndipo Anita akaanza kujuta, aliambiwa na rafiki yake kuhusu kijana huyo, alipuuzia lakini mwisho wa siku alikutana na jina hilo mitandaoni na kuona kile alichoambiwa.
Hertha Berlin ilikuwa klabu ya kawaida sana, wachezaji wake hawakuwa na uwezo mkubwa kabisa, walipanda daraja lakini hawakuwa na uhakika wa kubaki ligi kuu kwani walijua wangeshuka, yaani walipanda daraja kwenda kuyafurahia maisha ya huko na msimu ujao washuke tena.
Akaangalia ratiba, wakati huo timu hiyo ya Watanzania iliingia nusu fainali na ilikuwa ikikutana na timu ya vijana ya Leicester kutoka nchini Uingereza. Siku iliyofuata mapema kabisa Anita akafika uwanjani hapo, kama kawaida watu walikuwa wamejazana.
Miongoni mwa timu zilizoonyesha uwezo mkubwa kwenye mashindano hayo ilikuwa hiyo Leceister. Kila mmoja alitabiri wangekuwa mabingwa lakini kila walipomfikiria Amon, waliamini kijana huyo angeweza kubadilisha kila kitu.
Anita alitulia juu kwenye viti vya VIP, akiwa hapo macho yake yakatua kwa maskauti kadhaa waliokuwa wamekwishafika kwa lengo la kuangalia walichokuwa wakikihitaji na kuondoka nacho.
Kwenye mawakala hao walikuwepo wa kutoka kwenye Klabu barani Ulaya kama Bayern Munich, Borussia Dortmund, Genk, Nac Breda na timu nyingine. Wote hao waliokuwa hapo walitaka kumuona Amon ambaye ndiye aliyekuwa akiongoza kwa ufungaji bora kwa kuwa na mabao kumi na moja kwenye mechi nne tu alizocheza, yaani mechi tatu za makundi na moja ya robo fainali.
Moyo wa Anita ulikubaliana na rafiki yake kwamba Amon alikuwa mchezaji hatari sana ambaye alitakiwa kuchukuliwa na kutunzwa kwa ajili ya matumizi ya msimu unaokwenda kuanza lakini kila alipowaangalia maskauti wakubwa kutoka katika klabu kubwa, aliona kabisa angeshindwa kumshawishi kijana huyo.
“Ila mimi ni mwanamke, nadhani natakiwa kuwa mjanja zaidi,” alisema Anita na kuendelea kuangalia mechi hiyo.
Kwa mara ya kwanza aliuona uwezo mkubwa wa Amon, hakuwa kama wachezaji wengine, alikuwa tofauti, kwa jinsi alivyokuwa akipokea mipira, kusambaza na hata kulikaribia lango la adui alionekana kuwa mtu mwingine kabisa, aliyekuwa hatari ambaye hakuwa na masihara hata kidogo.
Alivutiwa na kila kitu kutoka kwa kijana huyo kiasi cha kukubaliana kumchukua na kumpeleka kwenye chuo chao, akae huko hata kwa miezi kadhaa na kisha kuanza kucheza timu ya wakubwa kwa kuwa uwezo wake haukuwa wa kawaida.
Wakati yeye akipanga hilo, nao maskauti wa timu nyingine walikuwa na mipango yao vichwani mwao, walivutiwa na Amon na walijua hapo baadaye angekuwa mchezaji hatari endapo tu angekuwa na uangalizi mzuri, walitaka kuwa naye, wanufaike naye na kumfanya kuwa mchezaji mkubwa.
Kila skauti alikuwa na kitu chake kichwani, walikuwa wakimpigia hesabu ni kwa namna gani wangeweza kumchukua kijana huyo na kumfanya mmoja wa wachezaji katika timu zao.
Kwenye mechi hiyo ya nusu fainali, akina Amon walifanikiwa kushinda kwa mabao manne kwa bila huku kwa kutumia miguu yake akifunga mabao mawili yaliyomfanya kuonekana kuwa na thamani zaidi.
Baada ya mechi, waandishi wa habari wakaanza kuwasogelea na kuwahoji, kwa kuwa Anita alikuwa na mpango wake, akazungumza na mwandishi mmoja, akampa vazi lake, akamlipa euro elfu moja na kumfuata Amon huku akiwa na kamera mkononi mwake.
Kulikuwa na waandishi kama watatu waliokuwa wamemzunguka, kila mmoja alitaka kusikia kutoka kwake. Hakuwa akizungumza Kiingereza kizuri lakini kwa kile kile watu walikuwa wakimuelewa vilivyo.
Walimuhoji na baada ya hapo, Anita akamsogelea na kuanza kuzungumza naye, lengo kubwa likiwa ni kutaka kumchukua na kuwa mmoja wa wachezaji katika timu yake.
“I need an appointment, we have a lot to talk about,” (Ninahitaji miadi na wewe, tuna mengi ya kuzungumza) alimwambia huku akimwangalia.
“What is it about?” (Kuhusu nini?)
“Your future!” (Maisha yako ya mbele)
“How?” (Kivipi?)
“I want to you to be the next Lionel Messi,” (Nataka uwe Lionel Messi ajaye) alimjibu.
“Mh!”
“This is my business card, please don’t let me down,” (Chukua kadi yangu hii, usiniangushe, tafadhali) alimwambia na kumpa kikaratasi hicho.
Amon akakichukua, kwa kipindi hicho maskauti hawakutakiwa kuzungumza na wachezaji mpaka pale mashindano yatakapomalizika na ndiyo maana kwa Anita akajifanya kuwa mwandishi wa habari lakini alikuwa na mambo yake.
Kwa jinsi alivyovaa miwani na kofia, muonekano wake uliwafanya watu wengine kupata ugumu kumgundua msichana huyo mrembo, alifanana na mwandishi wa habari.
Alipomaliza, akaondoka na kurudisha kila kitu kwa mwandishi aliyekuwa amemuazima na kurudi nyumbani kwake. Alipofika huko, kitu cha kwanza kilikuwa ni kumpigia simu baba yake na kumwambia kuhusu Amon, uwezo wake na kila kitu alichokifanya.
Mzee Windhorst akafurahi, akakenua, moyo wake ukawa na furaha, kwa jinsi alivyoambiwa na binti yake kuhusu kijana huyo, akashikwa na hamu ya kutaka kumuona zaidi, akaingia kwenye mitandao ya waandishi na kuanza kumwangalia.

Je, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 06

Kwa miaka mingi watu walisema kusingekuwa na mchezaji ambaye angeibuka, mwenye uwezo kama wa Lionel Messi lakini kwa jinsi Amon alivyokuwa akicheza, alikuwa na uhakika baada ya Messi kustaafu basi mtu aliyekuwa akifuata alikuwa kijana huyo kutoka nchini Tanzania.
Hakuamini kama kweli binti yake alizungumza na kijana huyo, kwa jinsi alivyokuwa, alikuwa pesa, endapo wangempata na kucheza timu yao basi wangechukua kombe, na siku ambayo wangeamua kumuuza, basi wangepata pesa nyingi sana.
“Una uhakika umeongea na huyu kijana ninayemwangalia ama?” aliuliza mzee Windhorst, sasa aliamua kumpigia simu binti yake na kumuuliza.
“Ndiye huyohuyo!”
“Una uhakika?”
“Asilimia mia moja.”
“Basi tumepata bonge moja la mchezaji!”
“Nalijua hilo baba!”
“Ila ulikuwa peke yako hapo ama na maskauti wengine?” aliuliza.
“Walikuwepo na wengine!”
“Sasa tutampata kweli?”
“Inawezekana! Kumbuka mimi ni mwanamke. Nina ushawishi mkubwa sana,” alimwambia.
“Basi haina shida.”
Wakati huo huo Amon alikuwa chumbani kwake na Gideon alimwambia kilichotokea, jinsi alivyokutana na Anita ambaye alijifanya mwandishi wa habari kumbe alikuwa na lake.
Gideon alimsikiliza, akamuonyesha na ile business card ambayo alimpa na kumtaka kuonana naye, kwa Gideon ilikuwa ni furaha tele, kwa jinsi ambavyo Amon alivyokuwa akicheza mpira, alistahili kabisa kufuatwa na vilabu vingine, kucheza huko na si Tanzania, ila kubwa zaidi lilikuwa kwa mdogo wake.
Alitamani sana kuona Amon akimuoa mdogo wake, aliangalia mbali kwa kuona hata mafanikio ya Amon yangekuwa sehemu yake na ndiyo maana alilitamani sana hilo litokee.
“Utatusua sana! Ila na mimi nina langu nataka nikushirikishe,” alisema Gideon.
“Lipi hilo?”
“Nataka ulifanye kuwa siri, asijue mtu yeyote yule,” alimwambia.
“Haina shida. Lipi hilo?”
“Nataka nizamie, nisirudi tena Bongo!” alimwambia.
“Uzamie?”
“Yeah! Sihitaji kurudi Tanzania, nitataka nitoroke, niache kila kitu, nataka nitafute maisha huku, haiwezekani niwe nimefika Ulaya halafu kifala tu nirudi Tanzania, huo upuuzi sifanyi,” alimwambia.
“Gideon! Mbona una hatari sana?”
“Amon, hakuna jinsi! Nazamia, naomba iwe siri yako, nitaandika barua kwa wazazi wangu, utakwenda nayo, utawaambia tu kwamba nitafanikiwa na kurudi Tanzania nikiwa tajiri,” alisema.
“Gideon....”
“Tunza siri!” alisema Gideon.
Amon alibaki kimya, kile alichoambiwa kilimvuruga kabisa, alimwangalia rafiki yake huyo na kila kitu alichokisema kilikuwa akikijirudia kichwani mwake, hakutamani kumuona rafiki yake akizamia Ulaya na badala yake arudi naye nchini Tanzania.
Alimwambia mambo mengi kwamba hakutakiwa kufanya hivyo lakini Gideon hakutaka kuelewa, kurudi nchini Tanzania kilikuwa kitu kisichowezekana hata kidogo.
“Ila hutotakiwa kuondoka mpaka tucheze fainali,” alimwambia.
“Haina shida. Tutacheza fainali, usiku wa siku hiyo naondoka zangu. Nikaanze maisha huko mbele, najua nitapata shida kipindi cha kwanza, ila naamini kuna siku nitafanikiwa na kufikia ndoto zangu,” alisema Gideon, yaani alionekana kukata tamaa na maisha ya nchini Tanzania, hakutaka kurudi kabisa.
***
Edmund alikuwa akipanga mipango yake kabambe kuhakikisha anampata Angelina kama alivyokuwa anataka. Alijua kulikuwa na ugumu mkubwa lakini kwa kuwa aliringia utajiri wa baba yake, uzuri wa sura yake, aliona kabisa angefanikiwa kwa kile alichokuwa akihitaji.
Siku zilikatika, mawazo yake yalikuwa kwa msichana huyo, alitamani kuwasiliana naye lakini hakuwa na namba yake ya simu kitu kilichompa wakati mgumu mno. Ili kulikamilisha hilo ndipo akaamua kuongea na rafiki yake Angelina aliyeitwa Esta kwa lengo la kumuomba namba.
Alimbembeleza Esta lakini msichana huyo alikataa, alijua namna rafiki yake asivyotaka kuona namba yake ikitolewa hovyohovyo kwa watu wengine. Baada ya kuona asingefanikiwa kwenye hilo, Edmund akaamua kutumia pesa sasa.
Akamwambia Esta alikuwa na laki mbili endapo tu angempa namba hiyo ya simu. Kwa mtu kama Esta, mwanafunzi ambaye hakuwa na majukumu ya kununua chakula wala nguo, kwake kiasi hicho cha pesa kilikuwa kikubwa mno.
“Ila usimwambie kama nimekupa mie,” alimwambia.
“Hilo wala usijali, siwezi kuuza ramani ya vita kambini mwa adui,” alimwambia.
Esta akampa namba, kwa Edmund ilionekana kama ushindi mnono kwake. Alijua kuchati na wanawake, alikuwa na maneno matamu mno, kwa kila msichana ambaye alijaribu kuwasiliana naye kwa njia ya simu hakuwa akitoka hata kama alikuwa mgumu kiasi gani.
Usiku wa siku hiyo hakutaka kuchelewa, haraka sana akampigia simu msichana huyo, akaipokea na kuanza kuzungumza naye. Kitu cha kwanza alichouliza Angelina ni nani alikuwa akiongea na namba yake aliipataje.
“Ni stori ndefu sana,” alimwambia.
“Hata kama ni ndefu. Niambie umeipataje?” alimwambia.
“Haina shida. Nitakwambia kila kitu endapo tu utanikubalia kitu kimoja,” alimwambia.
“Kitu gani?”
“Kukwambia hilo ana kwa ana,” alimjibu.
Kidogo ukimya ukatawala kwa sekunde chache kutoka kwa Angelina, akakataa, hakutaka kabisa kuonana na mwanaume huyo mpaka amwambie namba yake aliipata wapi.
“Utashangaa sana nilipoipata, halafu hutoamini!” alimwambia.
“Wapi?”
“Najua utanilaumu sana, ila pamoja na hayo nitahitaji msamaha wako kwenye hili,” alimwambia.
“Hili lipi?”
“La kupata namba yako bila ridhaa yako, niliichukua kibabe sana,” alisema.
“Kutoka kwa nani?”
“Nitakwambia tukionana, ila na wewe unatakiwa kuniahidi kitu kimoja!”
“Kipi?”
“Kwamba hutomwambia mtu huyo, anaweza hata kuniua!”
“Mtu gani?”
“Aliyenipa namba.”
“Kwani nani?”
“Hujaniahidi nilichokwambia. Utaweza kunitunzia siri?” alimwambia.
“Sawa. Ila niambie.”
“Naomba kesho tuonane shule nitakwambia, naomba usinilaumu. Wakati mwingine hata sisi binadamu huwa tunakosea,” alimwambia.
“Sawa.”
Huo ndiyo ulikuwa mtego wa Edmund, ilikuwa ni lazima kumwambia maneno yote lakini afanikiwe kile alichokuwa akikitaka. Alimwambia hivyo kwa kuwa alihitaji kuonewa huruma, aonekane alikuwa na kosa na kumpa hamu Angelina kutaka kufahamu kilichotokea.
Kumwamini na ile huruma iliyokuwa imemuingia ndiyo kilikuwa kama kosa kubwa kwa msichana huyo. Siku iliyofuata wakaonana na kitu alichohitaji ni kuambiwa kilichotokea.
Kwa Edmund hakuwa na jinsi zaidi ya kutengeneza uongo mkubwa kwamba kulikuwa na mvulana aliyekuwa na namba yake, aliiba simu yake na kuichukua namba hiyo, kosa kubwa alilolifanya ni kwamba mpaka muda huo hakuwa ameirudisha hiyo simu.
“Kwa hiyo uliiiba?”
“Ndiyo! Kwa ajili yako! Na ninayo hapa, nashindwa namna ya kuirudisha kwa mwenyewe!”
“Iko wapi?”
“Ndani ya gari?”
“Mwenyewe nani?”
“Anaitwa Godfrey Mbilinyi!”
“Ndiye nani?”
“Huwezi kumjua. Ni kijana wa kidato cha sita.”
“Hata kunionyesha kwa kidole,” alimwambia.
“Usijali! Ngoja tukitoka nitakuonyesha, ila itunze hiyo siri!”
“Nitaitunza endapo utairudisha!”
“Haina shida.”
Huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa kuzungumza na msichana huyo kwa dakika nyingi zaidi, hilo ndilo alilokuwa akilitaka Edmund, alifanikiwa kumteka, wakawa wanaonana mara kwa mara, wanazungumza na kuagana.
Mara ya kwanza Angelina alichukulia kama urafiki wa kawaida tu lakini ghafla akaanza kusikia kitu cha tofauti moyoni mwake, akaanza kuumisi ukaribu wa Edmund, alipokuja kushtuka na kutaka kutoka, tayari alitekwa na kijana huyo.
Ukaribu ukawa ukaribu, wakaanza kutembeleana nyumbani kwa kisingizio cha kuwa wanafunzi pamoja lakini baada ya wiki moja kupita tu, tayari walianza kushikana mikono, kiuno na mwisho wa siku kubusiana.
Mapenzi yalikuwa kama mchezo fulani wa kijinga. Mara nyingi mawasiliano na ukaribu vilikuwa vitu vilivyotengeneza sana ukaribu, kitendo cha Angelina na Amon kukaa kwa kipindi cha wiki mbili huku Edmund akichukua nafasi kubwa kwa msichana huyo, hatimaye akaanza kusahaulika moyoni mwake.
Taratibu akaanza kutoka, zile ahadi alizoambiwa na Amon zikaanza kusahaulika tena wakati mwingine akijiambia inawezekana huko alipo Amon asingeweza kurudi na pia alikuwa na mwanamke mwingine.
“Usiwaamini wanaume!” yalikuwa maneno yaliyosikika kichwani mwake mara kwa mara, hakujua alitakiwa kutokumwamini nani, ni Amon ama Edmund aliyekuwa ameingia kwa kasi moyoni mwake, akabaki njiapanda lakini moyo wake uliamini mwanaume wa mbali hakutakiwa kuaminika hata kidogo.

Je, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 07

Akili ya Gideon ilibadilika kabisa na katika kipindi hicho jambo pekee alilokuwa akilifikiria lilikuwa ni kuzamia hukohuko Ujerumani na sirudi tena nchini Tanzania.
Kulikuwa na watu wengi waliokuwa wakizamia, waliishi kwa shida lakini mwisho wa siku maisha yao yalikwenda vizuri tu, walikuwa na maisha mazuri na kuwahamasisha watu wengine kwamba huko Ulaya maisha yalikuwa bomba sana.
Kichwa chake kilikuwa kikifikiria maisha yake baada ya kuzamia nchini humo, hakuona dalili za kusajiliwa na timu yoyote ile na ndiyo maana aliamua kutaka kuzamia na kuishi huko mpaka kifo chake.
Huku akiwa na mawazo hayo, siku zilikuwa zikienda tu, Amon alitamani kuwasiliana na Anita na kumwambia kuhusu suala lake la kujiunga na timu yao lakini aliona muda bado, alikuwa na nafasi ya kuendelea kuonyesha ubora wake, kuwa bora zaidi ya alivyokuwa kipindi hicho.
Baada ya siku kadhaa fainali ikafika na hatimaye kucheza na timu ya Bayern Munich ya vijana. Siku hiyo watu walijazana mahali hapo, kila mmoja alitaka kuiangalia fainali hiyo kwa sababu zilikutana timu kali mno.
Mbali na fainali hiyo watu walivutiwa zaidi na Amon, walisikia sifa zake mitandaoni, video zake na hivyo walitaka kumuona laivu wauone uwezo wake ambao uliwavutia watu wengi kutazama fainali hiyo.
Muda wote Amon alikuwa akimwangalia rafiki yake, Gideon, alikuwa akicheza namba kumi, karibu na yeye, kitu alichokifikiria ni kuubadilisha uamuzi wa Gideon kupitia mechi hiyo.
Hakutaka kucheza kwa ubora wake, alihitaji Gideon acheze kwa ubora zaidi ili kama kweli watu walitaka kuchukua wachezaji basi wamchukue na yeye. Hilo likafanyika, mechi ilipoanza, alifanya mambo mengi, alimpa Gideon pasi nyingi na kumfanya kufunga mabao mawili.
Watu hawakuridhika, walitaka kuuona ubora wa Amon na alipoona Gideon amefanikiwa kwenye hilo, sasa akaanza kuonyesha ubora wake aliouficha kwa dakika arobaini na tano za kwanza.
Hapo ndipo watu wakamuona Amon akibadilika, alikuwa mtu mwingine kabisa, mwiba mkali, uliochoma na kuwaumiza wapinzani wake. Alicheza kwa uwezo mkubwa na yeye kufunga mabao mawili, jumla walishinda mabao manne na kuchukua kombe hilo.
Anita alikuwa miongoni mwa watu waliokuwa uwanjani hapo wakimwangalia Amon, aliridhika kwa asilimia mia moja na hivyo alitaka kuzungumza naye baadaye hotelini ili kukubaliana.
Haikuwa ikiruhusiwa lakini hakutaka kuona akiwahiwa, usiku walipokuwa hotelini huku Gideon akijiandaa kutoroka, Amon akamfuata na kumwambia asubiri kwanza, hakutakiwa kutoroka.
“Kwa nini?” aliuliza.
“Nakuja! Ukiniona nimerudi, naomba tuongee!”
“Haina shida.”
Amon alimpigia simu Anita na kuonana naye mahali faragha na kuanza kuongea naye, alimwambia lengo la timu yao, walitaka kumsajili, aichezee timu yao kwani alikuwa na uwezo mkubwa mno.
“Nitakubali kwa sharti moja tu,” alisema Amon.
“Lipi?”
“Mumsajili na Gideon pia! Ni rafiki yangi, ana uwezo mkubwa ambao utanifanya ning’are zaidi,” alimwambia.
“Gideon ndiye nani?”
“Yule niliyecheza naye mbele!” alijibu.
“Ila sisi tunakutaka wewe tu!”
“Bila yeye hakuna usajili. Yeyote atakayekubali kutusajili wote wawili, hakika nitakubali kuungana nao,” alimwambia.
Ni kweli alifanya kosa, bahati ilikuwa yake lakini hakutaka kujiangalia yeye, Gideon alikuwa mchezaji mzuri, aliyekuwa shemeji yake ambaye alitamani sana kuzamia huko Ulaya.
Hakutaka kuona hilo likitokea, kulikuwa na watu wengi waliokuwa wakizamia na asilimia kubwa walikuwa wakipotea, hakutaka hilo litokee kwa rafiki yake na ndiyo maana aliamua kumwambia Anita hivyo.
Msichana huyo alibaki kimya kwa sekunde kadhaa, kwa lile sharti alilolisema Amon hakika lilikuwa gumu kwani wao hawakumuhitaji Gideon, waliyekuwa wakimuhitaji alikuwa yeye tu.
Akachukua simu yake na kumpigia baba yake kwa lengo la kumpa taarifa juu ya kile kilichotokea. Baba yake akapokea na kuanza kuzungumza naye, alimwambia kila kitu.
“Kwa hiyo sharti ni hilo tu?” aliuliza.
“Ndiyo!”
“Sasa kuna ugumu gani hapo? Chukua wote wawili, hii biashara hatutakiwi kuiacha,” alisema baba yake na kukata simu.
“Haina shida,” alisema Anita huku akimwangalia Amon.
Ilikuwa ni furaha kwake, hakuamini kama alikubalika kwa kile alichomwambia, kwa kitendo cha rafiki yake kuchaguliwa na kuwa mmoja wa wachezaji wa timu hiyo kilimfurahisha mno.
Hawakutakiwa kusajiliwa kipindi hicho japo aliambiwa kwanza wangesaini mkataba wa awali kabla ya ule ambao walitakiwa kuusajili rasmi chini ya uangalizi kwa kuwa hawakufikisha miaka kumi na nane, baada ya kuzungumza sana, hatimaye akaondoka na kurudi chumbani.
Huko akamkuta Gideon akiwa tayari kwa safari, aliliandaa begi lake na kitu pekee alichokuwa akikisubiri ni Amon kurudi na kumwambia sasa alikuwa tayari kuondoka.
Amon alipoingia, uso wake ulikuwa na tabasamu pana, alimwangalia rafiki yake huyo huku akiwa amekwishaandaa begi tayari kwa safari.
“Kwa hiyo?” aliuliza.
“Tunasajiliwa wote, hakuna kutoroka hapa,” alijibu Amon.
Gideon akashtuka, hakuamini alichokisikia, alimwangalia rafiki yake yule, maneno aliyoyasema yalimshangaza, ilikuwaje amwambie wangesajiliwa wote na wakati aliitwa peke yake?
Amon akaanza kumuhadithia kilichotokea, Gideon hakuamini masikio yake, alimwangalia Amon, alipata marafiki wengi kwenye maisha yake lakini rafiki huyo wa kipindi hicho alikuwa zaidi ya rafiki.
“Umefanya yote kwa ajili yangu?” alimuuliza huku machozi yakimlenga.
“Wewe ni rafiki yangu Gideon, tumeshirikiana mambo mengi mno. Tutacheza wote timu moja,” alisema Amon na kumkumbatia rafiki yake huyo.
Siku hiyo kila mmoja alionekana kuwa na furaha, walikaa nchini Ujerumani kwa siku tatu kwa lengo la kufanya shopping, kwenye pesa za kufanya manunuzi hayo, Anita aliwapa euro elfu kumi kwa siri kama kuwavutia kwake, zaidi ya shilingi milioni ishirini kwa ajili ya kufanya manunuzi tu.
Hawakufanya manunuzi makubwa, walibakiza pesa nyingine na siku iliyofuata ilikuwa ni ya kurudi nchini Tanzania huku msichana huyo akimwambia angemtuma mwakilishi wao kwa lengo la kuzungumza na kituo chao kwa lengo la kuwasajili watu hao wawili waende wakaanze maisha yao nchini Ujerumani.
“Haina shida,” alisema Amon.
Wakiwa ndani ya ndege kila mmoja alikuwa na furaha, hapakuwa na mtu aliyejua kilichotokea, kila kitu walikifanya kuwa siri yao. Humo ndipo Amon akaanza kumkumbuka mpenzi wake, Angelina, alimkumbuka sana, alitamani kwenda na kuonana naye.
Ulipita mwezi mmoja na nusu hawakuwa wamerudi nchini Tanzania. Moyo wake ukamkumbuka, macho yake yakatamani kumuona. Walizungumza mengi kuhusu Angelina na alimwambia sasa angekwenda kumuoa, awe mke wake, aishi naye huko Ujerumani.
Hakujua kama muda huo msichana huyo alikuwa na mwanaume mwingine.

Je, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 08

Angelina aliamua kwa moyo mmoja kuwa na mpenzi wake, Edmund, hakuwa na moyo wa uvumilivu na kwa jinsi alivyokuwa akiishi na Amon, alijua tu kuna siku moja wangeachana na kuendelea na maisha yake.
Hakutaka kumfikiria mwanaume huyo tena, alimuheshimu kwa kuwa tu aliwahi kuwa naye kwenye mahusiano, aliutoa usichana wake lakini hapakuwa na jingine zaidi ya hilo.
Kila siku wao kama wapenzi walikuwa na kazi ya kupeana ahadi kemkemu kuonyesha ni kwa namna gani walikuwa wakipendana kwa mapenzi ya dhati.
Kwa Edmund alikuwa makini sana kwenye penzi na msichana huyo, kipindi cha nyuma alimuona kuwa msichana mrembo mno, uzuri ambao hakuwahi kuuona lakini baada ya kumvua nguo na kuona ni kwa namna gani alivyokuwa, penzi likaanza kutoka moyoni mwake.
Kilichobaki kilikuwa ni huruma tu, alimuonea huruma, angeishi vipi endapo tu angemwambia hataki kuwa naye tena, kila alipofikiria madhara ambayo yangetokea, hakutaka kufanya hilo tena.
Maisha yaliendelea, shule nzima ilijua jinsi wawili hao walivyokuwa wakipendana, hapakuwa na mtu ambaye hakujua kuhusu wawili hao, wengine walimuonea wivu Angelina kwa kuwa alikuwa kwenye mahusiano na mtu aliyetoka kwenye familia ya watu waliokuwa na pesa.
“Ila ana bahati sana yule msichana,” alisema msichana mmoja, alikuwa akiwaambia wenzake.
“Kwa nini?”
“Wewe Edmund unamuonaje? Ana pesa sana, baba yake anafanya kazi TRA,” alijibu msichana huyo, kwa jinsi alivyoongea tu alionekana kuwa na wivu sana.
Baada ya kupita mwezi mmoja huku wakiwa kwenye mahusiano, mara baada ya kurudi nyumbani, macho yake yakatua kwa kaka yake, Gideon aliyekuwa amerudi kutoka nchini Ujerumani.
Kumuona mwanaume huyo akashtuka, kama alikuwa amerudi inamaana hata Amon naye alirudi. Akaanza kujisikia aibu, kwa kile alichokifanya sasa kikaanza kuutafuna moyo wake.
Akamsogelea na kumkumbatia, akamkaribisha na kuanza kuongea mambo mengi kuhusu huko Ujerumani, jinsi ilivyokuwa mpaka kurudi jijini Dar es Salaam.
Wazazi wake na Angelina walikuwa wakimsikiliza tu, kwa jinsi alivyokuwa akiongea alionekana kuwa na furaha. Aliwaambia kuhusu mechi zilivyokuwa, Amon alivyowabeba mpaka kubeba kombe hilo.
“Yule kijana anajua sana mpira,” alisema baba yake huku akikenua.
“Na ananunuliwa na klabu moja ya Ujerumani,” alisema Gideon.
Kauli hiyo ikamshtua Angelina, hakuamini alichokisikia. Huyo Amon alikuwa njiani kununuliwa na klabu moja ya Ujerumani, akataka kusikia zaidi kuhusu jambo hilo, kwa uwezo wa kichwa chake alihisi kama kitu hicho hakiwezi kutokea.
Hatimaye akaanza kuwaambia kila kitu kilivyokuwa, Anita alivyomuita Amon na kuanza kuzungumza naye, mpango wake wa kutaka kuzamia lakini Amon alihakikisha anamsaidia na yeye kusajiliwa kwenye timu hiyo.
“Kwa hiyo na wewe utasajiliwa?” aliuliza baba yake.
“Ndiyo! Amon aliongea na huyo dada, alimwambia hatoweza kusajiliwa kama mimi sitosajiliwa, wamekubaliana kutuchukua wote wawili. Siamini kama Amon angeweza kunifanyia jambo hilo. Yule ni zaidi ya ndugu,” alisema Gideon huku akiwaangalia watu hao.
Maneno hao yalikuwa msumali wa moto moyoni mwa Angelina, hakuamini kama Amon angeweza kufanya jambo kama hilo kwa kaka yake. Alijua dhahiri alifanya hivyo kwa sababu yake tu, kwa kuwa alikuwa akimpenda, akaamua kumsaidia, ishara ya kumuonyesha ni kwa namna gani alikuwa akimpenda.
Mbali na kumfanyia hivyo kaka yake, aliamua kuachana naye na kuchukuliwa na mwanaume mwingine. Kwake, hayo yalikuwa ni maumivu yasiyoelezeka hata kidogo. Alibaki akijuta lakini kwa kipindi hicho hakuwa na cha kufanya.
“Siwezi kudate na wanaume wawili. Ni lazima nimwambie ukweli Amon,” alijisemea.
Akainuka na kuelekea ndani, akaoga, alipomaliza akabadilisha nguo zake. Akasikia anaitwa na kaka yake, akaitikia na kumfuata huko. Alimkuta kwenye meza ya kulia chakula na kumwambia akae na kuzungumza naye.
“Angelina! Umepata mwanaume ndugu yangu. Hii ni nafasi yako ya kipekee. Nilizungumza sana na Amon, kitu alichoniambia ni kwamba atakuwa mwaminifu kwako maisha yake yote, ataishi na wewe, atakupenda zaidi ya mwanamke yeyote mbali na ndugu zake.
“Nimekutetea sana kwamba na wewe utampenda hivyo, hivyo usiniangushe, usituangushe kama familia. Siku utakayosababisha mpaka muachane, hakika utakuwa umeniumiza sana, yaani tutakuwa tumerudishia wema kwa ubaya,” alisema kaka yake huku akimwangalia ndugu yake huyo.
Angelina alikuwa kimya tu.
Moyo wake hao ukagawanyika, upande mmoja ulimwambia amwambie Gideon ukweli lakini upande mwingine ulimuonya kufanya hivyo, kama alitaka kuzungumza ukweli basi mtu pekee aliyetakiwa kumwambia alikuwa Amon tu.
Alimsikiliza Gideon kwa dakika zaidi ya kumi, alipomaliza, akamuaga na kuondoka zake. Safari hiyo ilikuwa ni kwenda nyumbani kwa akina Amon. Alitakiwa kumwambia ukweli kabla ya kitu chochote kile ili kama ana nafasi ya kutafuta mwanamke mwingine, afanye hivyo lakini asahau kuhusu yeye.
Njiani alikuwa na mawazo tele lakini hakuchukua dakika nyingi, akafika na kuingia ndani. Alikaribishwa kwa mbwembwe nyingi, Amon alipomuona, akasimama na kumsogelea, akamkumbatia huku akionekana kuwa na furaha tele.
“Karibu sana mpenzi,” alimwambia kwa sauti ya chini, ya kunong’oneza wakati alipokuwa amemkumbatia.
“Nashukuru sana!”
“Hakika umekuwa msichana mrembo sana. Nilikukumbuka mpenzi wangu!” alimwambia.
“Nilikukumbuka pia,” alisema.
Akakaa na kuanza kuzungumza mengi, hakutaka kumwambia hapo Amon kwani alikuwa na wazazi wake, kuhusu jambo hilo walitakiwa kuzungumza wakiwa wawili tu.
Muda wote Angelina alionekana kuwa na hofu moyoni mwake, alikuwa akijifikiria namna ambavyo angeonekana, yule Amon aliyekuwa akiongea naye hakutakiwa kufanyiwa jambo baya lolote lile.
Alimpenda.
Alimjali.
Alimuheshimu.
Lakini kwa upumbavu wake, akaamua kumsaliti.
“Naomba unisindikize,” alimwambia Amon, tayari ilikuwa ni saa moja jioni.
Wakainuka na kuanza kuondoka mahali hapo. Njiani Amon alionekana kuwa na furaha tela kumuona mpenzi wake lakini kitu kilichomshangaza, msichana huyo hakuwa na furaha kama aliyotakiwa kuwa nayo, hivyo akataka kujua sababu.
“Kuna nini?” aliuliza.
“Nataka kuzungumza nawe!”
“Kuhusu nini?”
“Mahusiano yetu!”
“Yamefanyaje? Mbona unanitisha?”
“We are done! I am sorry!” (Tumemalizana! Nisamehe) alisema huku akimwangalia.
“What?” (Nini?)
“I am sorry Amon.” (Samahani Amon)
“Kwa nini?”
“Naomba uniache Amon! Naomba unisamehe pia. Nimekuwa kwenye wakati mgumu kukwambia hili, ila naomba unisamehe sana sana sana,” alisema msichana huyo huku akimwangalia Amon ambaye alibaki akiwa amesimama huku miguu ikimtetemeka.
“Yaani unamaanisha....”
“Tumeachana. Nichukulie kama rafiki yako tu.”
“Lakini kwa n...”
“Kwa heri Amon. Nisamehe sana,” alisema msichana huyo na kuanza kuondoka.
“Angelina....Angel...Angel....” alijaribu kumuita lakini msichana huyo hakugeuka nyuma, akachukua bodaboda na kuondoka mahali hapo haraka sana huku machozi yakimtoka, kwa kile alichomfanyia Amon, alikiri mwenyewe hakutakiwa kupata msamaha wowote ule kutoka kwa kijana huyo.

Je, nini kitaendelea?
 
Jitaidi bas ata kila siku uwe unapost angalau sehem moja
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom