Simulizi: Tugawane Maumivu

Simulizi: Tugawane Maumivu

Shunie

JF-Expert Member
Joined
Aug 14, 2016
Posts
157,076
Reaction score
463,977
Mtunzi Juma hiza

Sehemu ya 01

Shauku niliyokuwa nayo ni jinsi nitakavyomuona dada na shemeji kwani mara ya mwisho ni siku ya ndoa yao iliyofanyika kwenye ukumbi wa New Msasani Club.

"Wengi wanasemaga mwanamke akishaolewa anapungua mwili, lakini mwanaume anaongezeka. Sijui ndivyo ilivyo kwa hawa shemeji na dada?
Niliwaza, wakati huo basi la Happy Nation nililopanda lilikuwa likisubiri taa ziwake pale Ubungo ili lipite kwenda stendi kuu ya mabasi.

Kila hatua ya basi picha ya dada na shemeji zilinijia kiasi kwamba nilijiuliza ni kwanini? Ni kwanini niliwakumbuka sana kuliko siku zote?

"Au labda kwa sababu nakwenda kukutana nao?" nilijiuliza.
Ndugu mbalimbali walikuwepo kituoni wakitumbulia macho ndani ya basi kutafuta nafasi ya haraka haraka kuwaona wageni wao. Na mimi macho yangu yalikwenda mpaka nje ambako yalikuwa yakitafuta watu walio wawili. Mtu mke na mtu mume. Yaani shemeji na dada.

Kwa haraka macho yalipowaona wanaume watupu sikushughulika nao, au wanawake watupu pia sikushughulika nao.
Niliyarudisha macho ndani kisha nikachukua begi langu na kuteremka nikijua labda shemeji na dada wamechelewa kufika stendi, hivyo nitawasubiri. Niliwaza.

Nje ya basi nilitembea na begi langu kuelekea kwenye kibanda kimoja kinachouzwa kadi za simu kwani wakati huo niko njiani nilichati sana na boyfriend wangu nikamaliza credit kwenye simu.

"Maria. Maria," nilisikia nikiitwa.
Niligeuka haraka huku kichwani nikitafuta sauti hiyo.

"Ha! Dada," alikuwa ni dada yangu Light yupo na mwenzake lakini sikujua kama ni rafiki yake, mfanyakazi mwenzake au mpangaji mwenzake.

Sijawahi kumsalimia dada shikamoo hata siku moja nyuma, sijuinni kwanini. Lakini safari hii tulipokutana baada ya kukumbatiana na mabusu kibao nilimsalimia.

"Shikamoo dada Light," nilimsalimia na mwenzake, naye akaniitikia. Lakini dada Light alionekana kufurahia zaidi shikamoo yangu. Kumbe alikuwa na hamu nayo sana.
Alinisaidia begi kwa kulibeba yeye kisha tukawa tunaelekea sehemu zinapopaki taksi.
"Basi mi mawazo yangu utakuwa umekuja na shemeji," nilimwambia dada Light.
*
*
Itaendelea
20210608_124447.jpg
 
Sehemu ya 02.

"Noo! Alikwenda Kigamboni toka asubuhi. Huyu ni rafiki yangu anaitwa Eliza. Tunakaa naye nyumba moja. Lakini yeye anafanya kazi Bahari Beach," dada Light alinitambulishakwa rafiki yake.

"Okay. Nimefurahi kumfahamu," Eliza akasema naye amefurahi kunifahamu mimi kwani alikuwa ananisikia tu kutoka kwa dada Light.

Njiani wakati tunaelekea nyumbani dada Light alikuwa akinitania kwa kusema kuwa, nimezidi kujazia zaidi, nimenona na kutakata. Mbaya zaidi nimekuwa mdada fulani hivi kuliko nilivyokuwa wakati wa harusi yake.

Akasema vijana wa mtaani watakoma ubishi.
Rafiki yake Eliza naye akaunga mkono kwa kusema kuwa, yaani nimeumbwa vizuri sana. Kwa mwanaume mwenye kujua nini maana ya mwanamke mzuri hawezi kuniacha nipite bila kunipa 'Hi'.

"Jamani mbona kawaida tu," nilimjibu.
Tulifika nyumbani na kuanza kuuona ukarimu wa dada. Kumbe kwa sababu alikuwa anajua mimi nakuja aliniandalia kila aina ya chakula. Aliniandalia pilau kidogo, biriani kwa mbali, chips kwa nyama ya kuku ya kukaanga! Vipande vya nyama choma. Kulikuwa na mapapai, ndizi na maparachichi.

Soda aliona si kitu cha thamani kwangu, yeye alinitengenezea juisi ya apple yenye mchanganyiko na embe.

Eliza naye akaja na mambo yake. Alikuja na ugali na samaki mkubwa wa kukaanga. Vyote vilikuwa ndani ya kontena! Yaani ili mradi ni kula kula tu.

Jioni ya saa kumi na mbili shemeji alitokea. Jamani shemeji alikuwa amenenepa sana. Amenenepa kupita kawaida. Mishavu hiyo, kitumbo kwa mbali kilianza kuchomoza.

Nikakumbuka yale mawazo yangu ndani ya basi, kwani ni kweli dada hakuwa amenenepa wala kukonda. Alikuwa vile vile. Kidogo tu alikuwa ametakataka. Pengine kwa sababu ya mambo ya kujipodoa.

Kiasili mimi ni mtundu sana hata dada analijua hilo. Kwa hiyo salamu yangu kwa shemeji yangu niliipeleka kisasa. Mabusu kibao, kukumbatiana kwa sana tu. Lakini wakati dada alichekelea, rafiki yake Eliza alionekana kutofurahishwa na tabia yangu hiyo niliyoifanya kwa shemeji yangu. Alikunja uso.

"We hujaacha tu utundu wako," shemeji aliniambia huku akicheka, siyo kutabasamu.
*
*
Itaendelea
 
Sehemu ya 03.

"Ataacha huyo, wakati ndiyo mrithi wa mzee Mushi," alisema dada.
Mushi ni baba yetu mzazi ambaye naye kiasili ni mtundu sana, kidogo amepunguza siku hizi baada ya uzee kumjia.
***

Maisha ya dada na rafiki yake Eliza yalikuwa mazuri kwa ujumla, lakini kwa upande wangu niliyaona kama kuna tatizo kidogo.

Tatizo lenyewe ni kwamba, Eliza alizoea kuja sebuleni kwa dada wakati mwingine shemeji akiwa hayupo aliingia hadi chumbani wakati dada hakuwa muingiaji wa sebuleni kwa Eliza wala kuingia chumbani kwake.

Na mbaya zaidi naye alikuwa ana mume anaitwa Martin. Anafanya kazi bandarini.
Nilikuwa nimemaliza chuo Moshi, ndiyo maana nilikuja kwa dada kuangalia ustaarabu mwingine.

Ni mwezi mmoja ulipita toka kufika kwa dada Light, nikagundua jambo fulani.
Rafiki yake Eliza alikuwa hanipendi kabisa mimi, kwani mara kadhaa amekuwa akimwambia dada na mimi nikisikia kwamba, yeye hakubali mdogo wake aje kuishi nyumbani kwake kwani ameshawahi kusikia mara nyingi kuwa, kuna ndoa zimewahi kuvunjwa na wadogo watu.
Nilikuwa nikimshangaa sana kwani kwa jinsi ya ufahamu wangu mdogo sikuona sababu ya yeye kuongea hivyo na mimi nipo. Kwanini asinitete?

Ilifika mahali nikawaza kuwa, huenda anahofia ningemchukulia mume wake. Na mimu moyoni nikaahidi kuwa, lazima nitakuja kumchukulia mume wake siku moja ili kumkomesha hata kama hatajua.
Jumapili moja asubuhi. Niliamka na kuvaa khanga yangu moja ya kukatiza kiunoni. Ndani sikuwa na kitu.

Sikuvaa kufuli wala funguo. Juu nilivaa kiblauzi kifupi tumbo nje.
Nikawa nafagia uwanja. Ilikuwa ni zamu ya dada, sasa kwa sababu mimi nipo na sina cha kufanya sikuona sababu ya kumwachia msichana wa kazi ambaye toka saa kumi na moja alfajiri alikuwa anahangaika na matayarisho.

Nyumba ilikuwa kubwa sana, kiasi kwamba nilianza kufagia saa kumi na mbili na nusu hadi saa moja na nusu.

Wakati huo shemeji na dada walitoka kwenda kazini kwa pamoja.
Dakika kama tano baadaye alitoka Eliza na mumewe.

"Shikamoo dada Eliza," nilimsalimia lakini hakuitika na kujifanya anapekua begi lake kama vile kuna kitu alikuwa amekisahau ndani.
*
*
Itaendelea
 
Sehemu ya 04.

"Shikamoo shemeji," nikamsalimia mumewe ambaye aliitikia kwa amani huku macho yake yakigota gota sehemu mbali mbali za mwili wangu. Yalienga kitovuni nikajua amezuzuka na tumbo nje.

Akalenga miguu nikajua amechizika na miguu yangu isiyokuwa na vitufe kama viroba. Ni softi mtindo mmoja. Halafu akaenda kichwani nikajua amezimia jinsi nilivyoziweka nywele zangu.

Hazikuwa kompliketedi kama nywele za mkewe. Amezisokota kama nini sijui.
Ziliingia huku zikatokea kule, zikakata kona na kurudi huku tena. Matokeo yake akiwa mbali utafikiri amebeba tumbaku.
Mkewe alipoona mumewe ananiangalia sana akamsemesha kiaina. Najua lengo lilikuwa ni kumtoa kwenye kuniangalia mimi. Wivu huo sasa.

Kwa hali ilivyokuwa Eliza alipunguza hata kuja kwa dada kama zamani. Dada aliligundua hilo na akaniambia siku moja.
"Maria unajua Eliza amepunguza sana kuja kwangu siku hizi. Si kama zamani."

"Unadhanu ni kwanini?"
"Mh! Yule bwana hata yale maneno aliyokuwa akisema kwamba yeye hakubali mdogo wake aje kwake kirahisi kwa sababu amesikia wengi wamevunja ndoa za dada zao inawezekana anahofia wewe utamchukulia mumewe," dada Light aliniambia.

"Hata mimi dada Light niliwaza hivyo hivyo aliposema hivyo siku ile," nilimjibu dada Light.

"Lakini si urafiki wenu uko vile vile?" nilimuuliza dada Light.
"Uko vile vile kama unavyoona, uani tuko wote. Nje tuko wote kasoro kuja ndani kwangu tu," dada alinijibu huku akitabasamu.
Chumba cha kulala cha dada Light na chumba cha kulala cha Eliza vilipakana ukuta. Kwa mtu aliyekuwa kwa nyuma angeweza kuwasikia wote wakiongea kwa kupitia madirisha yao ambayo yote yalikuwa upande mmoja.

Siku moja mimi nilikuwa huko nyuma. Dada Light hakuwepo, lakini shemeji alikuwepo chumbani.
Kwa upande wa Eliza, yeye alikuwepo lakini mumewe hakuwepo.

Kitu kimoja kilinishangaza ni kwamba mlio wa meseji wa simu ya Eliza ulipolia, haikupita muda ukasikika na mlio wa meseji wa simu ya shemeji.

Nilifuatilia hilo kwa muda wa dakika kama ishirini na kugundua watu hao wawili walikuwa wakichati.
*
*

Je, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 05.

Hilo lilianza kunisumbua sana kichwani. Nilijiuliza maswali kibao lakini majibu yalikuwa kiduchu.

Wakati naendelea kuwaza, nikamsikia shemeji akiongea kwenye simu...sasa naona aliamua kupiga kabisa.
"Poa tu dear, vipi umelala nini?...Aah nipo nipo....eee haiwezekani si unajua kuna huyu mdogo wake!"

"Tuwe makini d, unajua akijua patachimbika, si unamjua mkeo alivyo mshari."
Mazungumzo ya Eliza yalikuwa yakijibiwa na shemeji ambaye nilikuwa simsikii vizuri anavyoongea kwani nilikuwa jirani na dirisha la chumba cha Eliza.

Niligundua walikuwa wakimsema da' Light. Pia niligundua shemeji na Eliza ambaye ni shoga mkuwa wa da' Light ni wapenzi licha ya kwamba Eliza alikuwa ana mume wake.
Nilitoka na kwenda chumbani ambako nilifika kitandani. Nilikuwa na wakati mgumu sana. Nilijiuliza nimwambie da' Light kuhusu nililoligundua au nimezee?

"Nikimwambia nitakuwa nimetia sumu kwenye macho. Lakini pia nikiacha sidhani kama nitakuwa na amani. Yaani dada yangu wa toka nitoke achukuliwe mume hivi hivi naona halafu nikae kimya?"
Haki ya Mungu vile niliomba ujasiri kutoka kwa Mungu.

Jioni da' Light aliporudi kutoka kibaruani nilikaa naye na kumuuliza mambo fulani fulani ambayo yeye hakujua nilikuwa na maana gani kumuuliza.

"Hivi da' Light huyu rafiki yako Eliza sijui mnaishi naye vipi, mbona simuelewi?"
Da' Light aliachia tabasamu kwanza kisha akasema.

"We acha tu mdogo wangu...ukiwa mvumilivu utaweza kuishi na watu vizuri, hata wewe nataka uwe kama mimi."
Moyoni nilimjibu kuwa, niwe kama wewe kwa kukubali kuchukuliwa mume wangu na shoga yangu au?

Lakini kwa nje nikamjibu.
"Napenda niwe hivyo lakini itategemea da' Light. Halafu mbona anaonekana kama ana mambo ya kuzungukana zungukana?" nilijaribu kumpa tip da' Light lakini wapi, hakunielewa.

"Yaani mdogo wangu huyo ndivyo alivyo. Halafu hajatulia, maana kila siku mumewe wanagombana kuhusu simu. Anamwambia mumewe mtu asishike simu ya mwenzake. Sasa kama uko safi kwanini unahofia simu yako kushikwa na mumeo?"

Mapigo ya moyo yalikuwa yakienda kwa kasi kwani niliamini dada Light alikuwa anajua kila kitu, lakini kumbe bila.
*
*
Itaendelea
 
Sehemu ya 06.

"Mi mwenyewe ni shoga yangu mkubwa lakini simu yake sijawahi kuishika hata siku moja. Hata kama simu yangu haina pesa yake ina pesa kidogo hanipi.

Ni mchoyo sijapata kuona," dada Light aliendelea kunipa habari, lakini mimi nikawa nimeelewa kitu. Eliza alikuwa hataki kumpa simu yake dada Light kwa kuogopa anaweza kukutana na meseji za shemeji.
"Lakini dada Light mi nitamkomesha tu," nilimwambia.

"Utamkomesha kivipi sasa?"
"Najua mimi. Ana mambo fulani hivi sijapenda lakini siwezi kukwambia hadi hapo nitakapofanikiwa kumkomesha," nilimwambia dada Light, akashtuka na kunikodolea macho, lakini nikatoka kwenda sehemu nyingine ili kumaliza ile mada huku moyoni nikiwa na usongo kwa jinsi dada Light alivyokuwa mgumu wa kugundua tabia ya ndani sana ya Eliza wakati iko wazi.

Kesho yake baada ya dada Light kuondoka kwenda kazini, nilimsikia Eliza akisema kuwa, siku hiyo haendi kazini, anajisikia kichwa kumgonga na alikuwa akijiandaa kwenda hospitali.

Shemeji naye alikuwa akisuasua kuondoka. Mara aingie chumba hiki mara chumba kile.
"Shem leo huendi kazini?" nilimuuliza shemeji yangu.

"Aa, bado kidogo shemeji. Lakini nakwenda sasa hivi," shemeji alinijibu huku akionekana kuwa na wasiwasi sana. Nilitamani kumuuliza "au una kideti na mama jirani nini?"

Lakini nikaona nitakuwa nimemboa mapema kwa kuwa kwangu pale kwake.
Kuna wakati niliingia chumbani kwangu nilipotoka sikumuona shemeji. Nikashangaa kama atakuwa ameondoka bila kuniaga. Atakuwa na mambo ya kiswahili sana.

"Shemeji shemeji," niliita lakini sikuitikiwa.
Nilifanya uchunguzi kama Eliza alikuwepo ndani kwake, lakini nikashindwa kugundua.
Mlango wa sebuleni kwake ulikuwa umefungwa kwa funguo. Na ukiingia sebulenu ndipo kuna mlango wa kuingia chumbani kwake.

Nilizunguka tena nyuma ya nyumba ambako kwa kupitia dirishani ningeweza kugundua kama alikuwepo ndani au la.

Nilisikia sauti zikinong'ona. Nikajua shemeji alikuwa chumbani kwa Eliza. Nilijitahidi sana kutaka kujua nini kinaendelea....lakini sikuambulia kitu zaidi ya mihemo ya nguvu sana baadaye ukapita utulivu wa hali ya juu...nilijua walikuwa wanafanya nini.
*
*
Itaendelea...
 
Sehemu ya 07.

Nilitamani sana kumpigia simu dada aje haraka kufumania lakini kwa foleni za Dar nilijua asingewahi.

Niliingia ndani na kukaa kwenye korido ili kuona kama watatoka wao au wengine.
Mara mlango ulifunguliwa, akatoka kwanza Eliza.
"Vipi mdogo wangu, niliamua kulala kidogo kwanza kisha ndo niende hospitali," Eliza aliniambia.

Nilimuitikia sawa, lakini moyoni nikiwa nasikia uchungu kupita kawaida.
"Yaani dada Light anaibiwa kirahisi hivi, tena humu humu ndani....!"

Eliza alikuja kusimama karibu yangu huku akijifanya kujishika kichwa. Macho yalikuwa myekundu kwa kuchokeshwa na shemeji. Kwa mbali alionekana kutokwa na jasho jembamba huku akijinyoosha nyoosha.

"Hebu njoo nikwambie kitu mdogo wangu," Eliza aliniambia huku akiingia ndani kwa dada Light. Nilijua alitaka kufanya ujanja wa kumtoa shemeji, hakuna lingine. Nilisimama na kumfuata kwa nyuma.

Kule ndani Eliza alianza kuniuliza uliza maswali yasiyokuwa na kichwa wala miguu huku akiandika meseji kwenye simu yake. Nilijua alikuwa akiwasiliana na shemeji kwamba atoke sasa, kuko shwari.
Nilisikia mlio wa mlango wa sebuleni kwa Eliza, pale pale nikatoka haraka. Eliza alinirukia kutaka kunishika blauzi, lakini hakufanikiwa.

"Nakuja sasa hivi dada Eliza," nilimwambia nikifungua mlango kutoka. Nilimkuta shemeji akitoka kwa Eliza huku akifunga zipu ya suruali vizuri.
"Haaa! Shemeji," niliita.
*
*

Je, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 08.

Shemeji alishituka sana kama vile ndo alikuwa amekutana na mwenye mali ambaye ni dada Light.

"Aa, vipi shem. Unajua kuna mtu nilikuwa namwanga...eee!Nilikuwa nataka kujua ni saa ngapi nikaona niangalie kwa huku...aa! Nilijisahau badala ya kuingia kwangu nimejikuta naingia huku," shemeji alibwabwaja kwa domo lililojaa uongo.
Mara Eliza naye alitokea. Alipoona nimekutana na shemeji akasema.

"My Godness! Nimekwisha!"
Kumuuliza shemeji nilishindwa kumwambia Eliza kwamba nilifuatilia mwenendo wao toka kumekucha pia nilishindwa. Mimi na shemeji tulibaki tunaangaliana tu! Miguu ilikuwa ikimtetemeka shemeji huku Eliza akiwa amejiziba kinywa kwa kutumia mkono mmoja wa kulia.

Kauli ya Eliza kusema amekwisha ikawa inaniingia akilini taratibu nikiichambua maana yake. Ina maana alikuwa amekiri wazi wazi akijua nini kilitokea. Kama kweli shemeji alikuwa amejichanganya kwa bahati mbaya kuingia kule kwa Eliza, sasa kwanini Eliza alinizuia nilipotaka kutoka nje?
Kwanini alisema amekwisha aliponikuta niko uso kwa uso na shemeji?

"Maria naomba njoo tuongee, please!" Eliza aliniambia akinivutia sebuleni.
Nilipenda kujua alitaka kuniambia nini, nikamfuata kwa nyuma. Shemeji aliendelea na safari. Sasa sijui alitoka nje kabisa au aliingia ndani kwake.

Kuingia tu sebuleni kwa Eliza, cha kwanza nikaokota kitambaa cha mkononi cha shemeji ambacho ni mimi mwenyewe nilikipiga pasi asubuhi.

Nilikikumbuka kwa sababu ni cheupe lakini kina doa jeusi katikati na hilo doa halikutoka wakati wa kufuliwa.

Eliza alipoona nakiokota kile kitambaa alishituka lakini si sana. Najua sababu.
Sababu ni kwamba alitambua mimi nilishajua kila kitu kuhusu uhusiano wake wa kimapenzi na shemeji yangu, mume wa dada yangu ambaye yeye ni rafiki yake kipenzi tena wa pika n'kupakulie.

"Sikiliza Maria mdogo wangu. Najua umegundua kitu. Niko chini ya miguu yako mezea. Please! Nakuomba Maria," alisema Eliza akipiga magoti chini mimi nimekaa kwenye kochi dogo.
"Kwanini utembee na mume wa rafiki yako kipenzi?" nilimkandika swali hilo.
*
*
Itaendelea....
 
Sehemu ya 09.

"Aa, unajua. Shemeji yako aliwahi kuniita baa kwa mara ya kwanza. Akaniambia kuwa, mkewe, yaani dada yako hamtoshelezi kimapenzi wanapokuwa kitandani. Eti hajui kumfanya mwanaume adate, asa ndo akaniomba mimi na yeye tuwe wapenzi lakini kwa siri."

"Yeye alijuaje kama wewe utaweza kumtosheleza kimapenzi?" nilimuuliza Eliza huku nikitamani kucheka kwani kwa umri wake na wangu hakupaswa kunipigia magoti vile.

"Alisema amekuwa akisikia mume wangu anavyogugumia usiku akajua lazima nilikuwa namfanyia mambo makubwa. Halafu akasema anapenda mimi ninavyoliaga."
Nilimwangalia Eliza kwa muda kisha nikataka aniambie ilikuwaje kuwaje hadi shemeji akapata namba zake wakati hataki simu yake iguswe na mtu yeyote yule.
"Ee ni stori ndefu kidogo," Eliza alinijibu kimkato. Alionekana hakuwa tayari kunisimulia hilo.

"Please kama kweli umeomba mambo yasifike kwa dada basi niambie la sivyo nampigia simu sasa hivi," nilimwambia Eliza huku nikishika simu yangu. Akanizuia kwa kunishika mkono.

"Ilikuwa hivi. Siku moja ya jumapili mume wangu akiwa amesafiri, alinipigia simu kwa namba nisiyoijua. Muongeaji alikuwa mwanaume akiwa na sauti nzito, lakini ya kuvutia. Nikamuuliza ni nani na anataka nini?
"Akasema anashida na mimi sana. Na yupo Hiza Hotel akinisubiri. Basi nilijiandaa nikijua nakwenda kukutana na mwanaume mwenye sauti nzuri akiwa na shida na mimi lakini sikujua ni shida gani.

"Kufika, nikamkuta shemeji yako. Lakini akajikausha kama vile nilimkuta kwa bahati mbaya na wala si yeye aliyekuwa na miadi na mimi.

"Kwa kuwa najua ni shemeji yangu nilimfuata na kumsalimia. Wazo kwamba ni yeye ndiye aliyenipigia simu sikuwa nalo kwani sauti yake naijua....!"

Eliza alipofika hapo nikamuuliza swali kabla hajaendelea na maelezo yake.
"Sauti yake unaijua....je, si ya kuvutia kama hiyo ya kwenye simu?"
"Inavutia naye lakini sikumfikiria kama ni yeye."

"Sawa endelea," nilimwambia Eliza.
"Basi, nilipomsalimia nikamwambia kuwa kuna mtu amenipigia simu yuko hapo hotelini, lakini simjui ndo nimefika ili kumuona.

"Akaniambia niwe makini sana kwani kuna watu wa aina hiyo hapa mjini. Anakupigia simu ili akuibie. Niliogopa nikijua kuwa huenda ni kweli.
*
*
Itaendelea.....
 
Sehemu ya 10.

"Nikawa napiga simu ya huyo mtu siipati. Kila nikipiga siipati. Shemeji yako akaniambia pengine alizima simu au iliisha chaji, cha msingi ili kukaa na kusubiria, kama iliisha chaji mwenyewe atapiga.

"Nilivuta kiti kwenye meza aliyokuwepo yeye, nikakaa. Aliniagizia bia na kuanza kunywa. Lakini huku nikiendelea kuipiga ile simu. Wakati mwingine yeye shemeji yako aliniomba namba hiyo na yeye aipige, lakini pia haikupatikana.

"Yeye naye alikuwa anakunywa bia kama mimi. Hivyo kuna wakati tulianza kulewa. Ndipo alipoanza kunitongoza akidai kuwa, amekuwa akijihukumu kila siku kwani ananipenda sana lakini hajapata nafasi ya kuongea na mimi japo kwa dakika mbili tu.
"Akasema amekuwa akiamini kuwa ninayajua mapenzi kuliko dada yako..."
Eliza alipofika hapo moyo wangu ulinipasuka pwaa!

Nikahisi ndo mimi sasa nasikia mpenzi wangu au mume wangu anamwambia mwanamke mwingine tena ninayemfahamu kwamba amemzimia kwa sababu anaonekana anayajua mapenzi kuliko mimi. Kwa vyovyote vile moyo utaniuma kupita kiasi.

"Enhe...." nilimwambia.
"Basi si unajua tena pombe nikakubali na ndipo akanitumbulia jipu kuwa yeye ndiye aliyekuwa amenipigia simu kuniita. Na alitumia namba mpya kwenye simu yake.
"Tulipolewa sana alichukua chumba tukaenda kufanya mambo yetu. Kuanzia hapo ndo tumekuwa wapenzi hadi leo. Please Maria usimwambie Light, najua anaweza hata kufa."

"Aaa, aliniambia kuwa, kuna siku alikuwa akitumia simu ya sista wako akaona jina langu akaisevu kwenye simu yake. Na baada ya kuisevu kuna siku aliniona kwa mbali akai-beep ili kuona kama nitapokea ajue ni mimi kweli au la. Akaona nafungua mkoba kuitoa, alipokata simu nikairudisha mkobani akajua ni mimi mwenyewe mwenye namba ile."

"Sasa tukubaliane kitu kimoja. Na mimi nitahakikisha mumeo anatembea na dada Light japo kwa mara moja tu halafu basi ili kulipa kisasi."

Niliposema hilo Eliza alishituka sana na kusema.
"Noo, haiwezekani my dear," pale pale shemeji naye akaingia.
*
*

Je, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 11.

Alichoamini shemeji ni kwamba dada Light atakaporudi ningemweleza ukweli wote kuhusu uhusiano wake na Eliza, hivyo aliniomba msamaha nisimwambie chochote kile, ninyamaze kwani hakufanya vile kwa kukusudia bali ni ibilisi tu alimpitia.
Baada ya wote wawili kuniomba huku wakikiri makosa yao ilibidi niwaambie sitomweleza dada ukweli.
***
Jioni dada Light alipofika toka kazini na alipopumzika aliniuliza aliko Eliza.
"Nadhani yuko kwake, kwani vipi?" nilimuuliza da' Light.

"Nashangaa hajaja kunisalimia wakati si kawaida yake. Kwa sababu yeye ndiye anayenitangulia kurudi, basi nikija tu hata dakika kumi hazipiti anakuja kunisalimia, leo naona mpaka giza linaingia hajaja," dada Light alisema huku nikimuonea huruma. Hakujua kama Eliza si shoga ake bali ni mke mwenzake.

Mazungumzo ya kumjadili Eliza yaliisha kwa mimi kumjulisha kwamba, siku hiyo hakwenda kazini alisema anaumwa na kichwa.

"Ala! Mbona hajaniambia. Kuna wakati nilimtumia meseji kumuuliza vipi kazi akanijibu inakwenda safi kumbe anaumwa?"
"Anaumwa, kashinda hapa hapa!"
Wakati huo shemeji alikuwa hajarudi, kwani naye baada ya kumhakikishia kwamba sitasema kwa dada aliaga kwenda kazini sasa.

"Hivi da Light hebu niambie, shemeji mlijuana juana vipi?" nilimuuliza da Light kwa sauti yenye utani mwingi.
Da Light ni wangu mimi, nilijua ataniambia tu. Alicheka kidogo kisha akaanza kwa kusema.

"We acha tu mdogo wangu. Mvua hizi...!" Alianza kusema da Light kisha akaendelea.
"Mimi nilikuwa na rafiki yangu anaitwa Jane, huyu shemeji yako ndiye aliyekuwa mchumba ake. Nilizoeana na wote, Jane kama rafiki yangu na huyu mume wangu kama shemeji yangu.

Siku moja nilikuja hapo mbele kwenye hoteli ya Legho, si unajua?"
"Ndiyo najua," nilimwitikia dada. Akaendelea.
"Basi pale palikuwa na kikao cha harusi ya mtoto wa mzee Mtiku, si unamjua?"
"Ee, si yule binti yake Salome?"

"Ee, ilikuwa niende kwenye kikao hicho na rafiki yangu Jane, lakini kwa bahati mbaya sana alisafiri ghafla, nikaenda peke yangu.
"Mpaka giza linaingia nilikuwa bado kikaoni, si unajua tena sikuwa na mtu nyumbani wa kuniuliza kwanini nilichelewa kurudi."
"Wakati huo unakaa Kurasini?" nilimuuliza dada Light.
*
*
Itaendelea....
 
Sehemu ya 12.

"Ndiyo katikati ya kikao mvua kubwa sana ilinyesha. Ilikuwa ni mvua ya kutisha kwa kweli, radi nyingi, upepo kwa wingi mpaka mwenyekiti akakiahirisha kikao mpaka wiki inayofuata.

"Baadhi ya watu walianza kuondoka na mvua huku wakinyeshewa kwani ilionekana haikuwa na dalili ya kukatika.
"Mimi naye nilipoona hivyo, tena nilikuwa nimebaki peke yangu sasa, nikaona sehemu iliyo jirani na pale baa ni hapa kwa mchumba wa rafiki. Nikaja mpaka hapa."

"Lakini mpaka hapo ulikuwa unajua kwamba rafiki yako Jane amesafiri?" nilimuuliza dada Light.

"Nilikuwa najua, lakini kwa hali ya mvua ilivyokuwa sikuwa na jinsi, Legho iko Sinza, mimi nakaa Kurasini, unafikiri ingekuwaje?" dada alinijibu kama vile alihisi maswali yangu yalikuwa yanalenga wapi.

"Enhe endelea....!" nilimwambia da' Light.
"Basi wakati huo shemeji yako alikuwa banda la uani, ana chumba na sebule tu. Kwa hiyo nikajua mimi nitalala sebuleni, yeye atalala chumbani.

"Nilifika nikapiga hodi, lakini ilikuwa kazi sana kunisikia kwani mvua ilikuwa kubwa sana na upepo ule huku ukisindikizwa na radi, nilikuwa nimeloa chapa chapa."
"Masikini pole sana," nilimwambia. Badala ya kushukuru akacheka.

"Enhe?" nilimruhusu aendelee kusema.
"Basi ikanibidi nizunguke kwa nyuma dirishani mpaka akasikia, akaniuliza we nani. Nikamwambia shemeji yako Light.
"Akanifungulia mlango. Nami nikaingia mpaka sebuleni. Niko chapa chapa kwa mvua.

Nilivaa suruali ya jinsi na T-shirt.
"Nilimweleza kisa chote kilichonifanya mimi niende kwake, akanipa pole sana. Nikamwambia nilikuwa tayari kulala hata sebuleni. Alinikubalia, akaingia chumbani kwake na kutoka na khanga mbili na mashuka mawili akaniambia nitandake kwenye kochi nilale.

"Sasa ilipofika asubuhi ndipo makubwa nilipoyaona, kumbe bwana alikuwa na mwanamke ndani na anafanya kazi mjini. Alitakiwa kutoka saa kumi na mbili asubuhi, sasa mimi si nipo na anajua ni kipenzi na mchumba wake Jane, akawa anashindwa kumtoa. Mimi nimelala sebuleni.

Niliwasikia wakishindana kule chumbani, bwana mi natoka hivyo hivyo, shemeji yako anasema piga simu ofisini waambie unaumwa utachelewa kufika.
"Mwishowe akatoka kwa kujikaza huku mimi nikiwa bado nimelala kwenye kochi.
*
*
Itaendelea....
 
Sehemu ya 13.

Baada ya kumsindikiza, akarudi na kuanza kuniomba samahani. Oooh, shemeji unajua tena, rafiki yako kasafiri asa mi nilikuwa na hamu ndo nikamleta huyu mwanamke ndani naomba sana usije ukamwambia Jane akirudi.

"Nikamwambia wala usiwe na wasiwasi shemeji. Mi nilichotaka hapa ni hifadhi ya kulala tu kwa sababu ya mvua, mambo yako sina haja nayo. Akasema mi nitaamini vipi kama hutasema?

"Nikamjibu we unataka uamini vipi?"
"Mi nataka wewe ndiyo unihakikishie shemeji! Nikamuuliza nikuhakikishieje? Ooh, sijui wewe. Sasa ili kumtuliza kwa sababu alikuwa amekaa jirani na mimi kwenye kochi nikamshika na kumbusu, kisha nikamwambia amini.

"Basi naye akanibusu akasema sasa naamini kwani ukinisemelea na mimi nitamwambia ulinibusu. Aliposema hivyo wote tulicheka, kisha yeye akaniinamia na kunibusu. Mchezo ukaanzia hapo. Nami nimambusu tena naye akanibusu.

"Tukajikuta tumekumbatiana na kila mmoja yuko juu. Sijui nini kilitokea mdogo wangu, lakini nilijikuta nimemsaliti rafiki yangu Jane kirahisi sana."

Da Light alipofika hapo alinifanya na mimi nijione mjinga sana, kumbe naye alipindua kama Eliza anavyotaka kumpindua.
"Kumbe dada ana haki ya kusalitiwa?" niliwaza moyoni.

"Enhe sasa Jane aliporudi ikawaje?" nilimuuliza.
"Mh! We acha tu mdogo wangu!"
*
*
Itaendelea.....
 
Sehemu ya 14.

"Ilivyotokea baada ya kumsaliti shoga yangu hapo, hatukuacha. Hata pale Jane aliporudi mimi na shemeji yako tuliendelea kumsaliti kwa siri. Siku nyingine shemeji yako alikuja nyumbani kwangu Kurasini, wakati huo huo mimi nikawa nampigia simu Jane kumwambia sipo nyumbani ili asije akamkuta mchumba wake kwangu.
Tukawa tunaponda maraha na mchumba wa rafiki yangu.

"Nilijua kuwa, siku ya Jane kugundua ataumia sana, lakini sikuwa na jinsi ya kulikwepa penzi la John. Siku moja John alikuja nyumbani Kurasini, nikajisahau kumpigia simu Jane kwamba sipo nyumbani. Naye alipotoka kazini akaja.

Sikuwa na hili wala lile. Mlango wa chumbani ulikuwa wazi, John alikuwa kitandani na bukta tu...si unajua tena!
Mimi niko pembeni yake na kanga moja tu....si unajua tena!"

"Ndo maana yake. Jane hakuamini wala hakuwahi kufikiria kama mimi na jamaa yake tuna mawasiliano ya aina ile. Alipoteza fahamu kwa dakika kadhaa. Lakini alipokuja kupata fahamu, aliondoka na sikuwahi kuonana naye hadi leo.

Mimi nikachukua jahazi mpaka leo na ndoa tukafunga. Lakini kuna wakati nikiikumbuka ile hali ya usaliti najisikia vibaya sana. Kwa maana hiyo na mimi siku nikijagundua shoga yangu anatembea na mume wangu nitahakikisha namtoa utumbo," da Light hilo lilitoka moyoni.

Nilimuogopa sana dada kwa mkasa wake huo. Na huo ukawa mwisho wa maongozi yake. Nikawa nimepata jibu la swali langu la mwanzo kabisa nililomuuliza yeye na shemeji John walikutanaje?
***
Siku hiyo shemeji alirudi mapema sana tofauti na kawaida yake. Alipokutana macho na mimi aliyakaza zaidi. Akaonekana kama amehisi kitu fulani.

Da Light kama alivyokwishasimulia mkasa wake alikosa raha. Kwa hiyo hata mumewe alipokuja alikuwa hajarejea kwenye hali yake ya kawaida. Inaonekana ile hali ya yeye kumsaliti shoga yake akiikumbuka alikuwa anajihisi hukumu iliyokuu.

Baada ya kusalimia shemeji alipitiliza chumbani. Nilihisi kuwa moyoni mwake alikuwa akiamini mimi nilikuwa namsimulia da Light kuhusu yeye kutembea na Eliza.
Dada naye aliamka kitini na kumfuata mume wake chumbani. Haikupita muda da Light alitoka akisema anakwenda kumnunulia shemeji maziwa ya mgando.
*
*
Itaendelea....
 
Sehemu ya 15.

Mara shemeji naye alitoka chumbani wakati dada ameshatoka. Alishika kikaratasi na kunipa kiaina...

"Shemeji Maria naona dada yako kama hayuko sawa, ingawa mwenyewe anadai yuko sawa. Isije kuwa umemwambia, utaua shemeji kama umefanya hivyo."
Huo ndiyo ujumbe alioandika kwenye kikaratasi alichonipa.

Mimi sikuona sababu ya kumjibu kwa kumwandikia meseji, nikamtumia ujumbe mfupi wa maandishi kwenye simu yake.
"Nilishakuahidi shemeji kwamba sitamwambia.

Kwa hiyo ahadi yangu iko pale pale, bado ahadi yako kwangu," nilimjibu.
"Asante kama ni hivyo. Bado ahadi yangu, ipi hiyo?" naye aliniuliza kwa meseji.
"Nataka zawadi."
"Oooh usijali shemeji. Unataka zawadi gani?" aliniuliza.

"Zawadi ni zawadi tu shemeji. Hata ukiniletea Big G! Ni zawadi tu."
"Basi kesho shemeji nitakuletea seti ya chupi za ndani na sidiria zake."

Kabla sijaijibu meseji hiyo, kwa kutanguliza shukrani zangu, Light aliingia. Wakati huo shemeji alikuwa chumbani. Aliponipa kikaratasi mara ya kwanza tu alirudi chumbani.

Light alitangulizana na Eliza ambaye alionekana kukosa raha hata kwa macho ya kawaida tu yasiyohitaji mwanasaikolojia.
Dada alikuwa mchangamfu lakini yeye alipooza.

Nilimkaribisha bila kinyongo japo nilijua ni shetani wa dada. Alikaa jirani na nilipokaa mimi huku akijishaua.

"Vipi mdogo wangu mpenzi?" aliniuliza akijifanya yeye na sisi ni damu damu.
Dada alichukua glasi na kumimina yale maziwa kisha akaenda chumbani. Nilijua alikwenda kumuita shemeji aje kunywa mgando wake alioagiza.

Alitoka dada peke yake. Akakaa kwenye kochi kubwa. Nilimwelewa kwamba, alifanya vile ili shemeji akija wakae wote kwenye kochi hilo.

"Sasa shoga kumbe unaumwa, kwanini hukuniambia unaumwa, kwanini hukuniambia hata kwa meseji?" da Light alimuuliza Eliza.

"Sikuwa siriasi sana, nikaona unaweza kuhofia ukashindwa kufanya kazi," Eliza alijibu macho yakiwa kwangu badala kwa mtu aliyemuuliza.

Shemeji alitoka chumbani akiwa amevaa bukta tu! Tumbo liko wazi. Da Light akaonekana kutofurahishia kile kitendo.
"Mwenzetu si ukavae hata singlendi," alisema da Light.
"Kwani kuna nini?" shemeji alihoji kabla ya kwenda kutekeleza.
*
*
Itaendelea....
 
Sehemu ya 16.

"Kwani mwenyewe huoni. Kuna Eliza hapa, halafu ni sebuleni wanaweza kuja wageni ghafla," alisema dada.

Yaani angejua, afadhali hata angesema kuna shemeji yako Maria hapa, kuliko huyo Eliza aliyemtaja.
Yeye aliamini Eliza si wa kustahili kuona tumbo la mumewe, wakati kumbe mwenzake ameshaona mpaka kiuno.
Wakati shemeji kageuza kurudi chumbani huku nyuma dada Light alikuwa akisema.
"Mi sipendi mtu mwingine kama vile shoga yangu ajue alama za ndani za mume wangu. Yaani ajue kumbe mume wangu tumboni ana alama nyeusi.

Kumbe mbavuni ana kipele, sitaki kabisa. Mimi mimi, shoga angu shoga angu. Ndo maana moyoni nimeweka nadhiri kuwa, siku nikibaini shoga yangu ananizunguka kwa mume wangu," kabla dada hajamaliza kusema mumewe alitokea. Akasita.

Eliza alisinyaa haraka sana kwa kauli ile. Japo hakuimalizwa, lakibu alivyoianza ilionesha mlengo wake ulikuwa wapi.
Kesho yake shemeji na dada walitoka kwa pamoja kwenda kazini. Eliza na mumewe nao waliongozana baadaye.

Nyumbani nilibaki mimi na msichana wa kazi wa dada, msichana wa kazi wa Eliza na mtoto mdogo.

Kuna wakati niko sebuleni nikisoma gazeti, niliwasikia wasichana wa kazi wakiongea nje kwa sauti ya kunong'ona.

"Mi namshangaa sana dada Eliza. Yaani hata huruma hana. Afadhali angefanya hivi kama mwenzake angekuwa anaishi mbali, lakini ndani kwa ndani....!"
Msichana wa kasi wa dada naye akawa na yake.

"Tena siku moja dada alikwenda Morogoro, Eliza akaingia mpaka chumbani kwa dada, akalala na shemeji. Mumewe karudi akawa anamtafuta. Simu kazima mi nikamdanganya kwamba nilimuona akitoka na mfuko!"
Nilisimama na kusogea mlangoni ili kuwasikilizs zaidi.

"Iko siku mi nitamwambia shemeji," alisema msichana wa kazi wa Eliza.
Mara siku yangu ililia kuashiria ujumbe mfupi wa maneno umeingia.

"Njoo hapa New Top Land Hotel, Magomeni," kuangalia namba siifahamu.
Nilimuuliza mtu huyo kwa meseji yeye ni nani na ana shida gani lakini hakujitambulisha.

"We ukija utanikuta na utanitambua tu, njoo sasa hivi," alijibu na yeye.
Akilini nilimwaza shemeji, kwamba huenda ametumia simu ya mtu mwingine kuniita mahali kwa lengo la kutaka kuzungumzia zaidi masuala yake. Nikaamua kum-beep kwanza. Naye akapiga.
*
*
Itaendelea.
 
Sehemu ya 17.

"Vipi shemeji yangu, kuna tatizo lolote?"
"Hapana shemeji, nilikuwa napenda kukusalimia tu. Uko kazini?" nilimuuliza kwa kujigongagonga kwani niligundua hajui lolote kuhusu ile meseji.

"Niko kazini, au ubakumbushia zawadi zako nini?" shemeji alinihoji. Nikazidi kubaini kuwa, si yeye aliyenitumia meseji ile ya kuniita New Top Land Hotel.
"Hapana shemeji, nakusalimia tu," nilimjibu.
Basi, baada ya kumaliza kuongea na shemeji meseji iliingia nyingine.

"Sasa unakuja au?"
Nilimjibu mtu huyo kwamba sina nauli ya kuendea Magomeni. Lakini naye akakomaa, akanitumia meseji akisema nichukue taksi na kufika pale New Top Land kwa sababu ananifahamu atanifuata ili kunilipia.
Mtihani!

Nilijiuliza mara mbilimbili anaweza kuwa nani? Ananifahamu! Je, mimi namfahamu? Nilijiuliza sana.
*
*


Je, nini kitaendelea?
 
Sehemu ya 18.

Sijui ni nini kiliniingia, kwani ghafla sana nikajisikia ushujaa na kuamua kujiandaa ili niende, lakini nilihakikisha nakuwa na pesa ya taksi, si mwa kumtegemea mtu. Je, nisipomkuta?

Niliamua kuvaa ile mivao ambayo kwa msichana kama mimi nikikatiza mtaa, achana na wanaume, wanaume wenyewe wanakata shingo kuniangalia, ingawa najua wengine watasonya!

Nilitembea mwendo mdogo sana hadi kituoni, nikachukua taksi. Nilimuomba dereva anipeleke New Top Land Hotel, Magomeni.

Njiani meseji ziliingia tena mbili. Moja huyo mtu alikuwa akiniuliza nimefika wapi, nyingine akinisisitiza kuchukua taksi.
"Niko njiani kwenye taksi naja," nilimjibu.
Kichwani mawazo kibao yaliniingia, kwamba nimwambie dada Light kuhusu safari yangu ya kwenda kwa mtu nisiyemfahamu au nitajua mbele kwa mbele?

"Aa, nitajua huko huko. Akiniambia niingie chumbani sikubali, kama anataka tukae hotelini tu," niliwaza haraka haraka.
Teksi ilipaki kwa mbele kidogo ya New Top Land Hotel. Hivyo kushuka kwangu hakukushuhudiwa na watu waliokuwa hapo New Top Land Hotel.

"Shilingi ngapi babu?" nilimuuliza taksi dereva ambaye hakuwa na unywele mweusi hata mmoja, si kichwani si kidevuni wala kuzunguka kinywa.

"We mtoto mzuri bwana, nipe yoyote uliyonayo halafu unipe namba ya simu," eti yule taksi dereva na uzee wote ule aliniambia maneno hayo.
"Babu achana na mimi, hujui nina matatizo gani, niambie....!"

"Elfu mbili unusu basi," alisema.
Nilimpatia zikiwa kamili kisha nikashika njia kwenda hapo New Top Land.
Kumbe hoteli iko juu, yaani ilibidi nipande juu ghorofani!

Kufika nilivua miwani na kuanza kuangaza huku na kule kama nitamuona mtu aliyeniita kwa kumfahamu.

Kwa vile wanaume walikuwa wengi hotelini hapo kuliko wanawake, aibu ya kike iliniingia. Nilishindwa kuangaza sana, nikatafuta kiti na kukaa hapo.

"Nikusaidienini anti?" Mhudumu alishafika siku nyingi hata kabla sijakaa vizuri.
"Nitakuita anti, acha nipate japo upepo," nilimjibu huku nikimwangalia kwa kumteremsha na kumpandisha hadi kichwani. Mwenyewe alijua nimemnyali.
Nilichukua simu yangu kuziseti namba za yule mtu kisha nikam-beep...!
*
*
Itaendelea..
 
Sehemu ya 19.

"Namba unayopiga haipatikani kwa sasa, tafadhali jaribu tena baadaye!" Eti ndivyo kompyuta za simu zilivyonijibu.
Nilitamani kuzijibu na mimi kwamba ziache uzushi, lakini nikajiona nitakuwa mjinga mimi.

"Khaa yale yale," nilijisemea moyoni kwani wazo la kuchukua pesa ya taksi lilinijia nikijua binadamu wengine si wakweli.
Nikatuma meseji kwamba nimeshafika nikijua kuwa, kama alizima simy yake kwa muda akiifungua tu meseji inaingia!
Lakini ikawa 'pending' muda mrefu.

Mara yule yule mhudumu alinijia tena, nikataka kumtukana kwani nilishamwambia nitamuita, sasa nini tena!
"Antu unaitwa ukasalimie pale," mhudumu aliniambia.

Nilifuatilia kwa macho kidole chake na kugundua kuwa aliyekuwa akiniita ni mume wa Eliza, shoga yake dada Light.
Moyo ulinilipuka puu!
*
*
Itaendelea...
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom