sehemu ya 48
Hilo halikuwa tatizo, kwa mtu mwenye pesa kama mimi, fundi hakuona ugumu kuja kwani alijua ningemlipa malipo mazuri kabisa, tena kwa sababu ilikuwa ni asubuhi, ingeonekana kuwa bahati sana kwake.
Wakati nikiwa njiani kuelekea kwa mafundi wa gereji ambayo haikuwa mbali na mahali nilipokuwa naishi, nikasikia nikiitwa kwa nyuma, sauti ilikuwa ni ya mwanaume, nikageuka na macho yangu kutua usoni mwa jamaa mmoja.
“Aisee bro mambo vipi!” alinisalimia, lafudhi yake ilikuwa ni ya mtu kutoka Kaskazini.
“Poa tu niaje mwamba!” niliitikia na kumsalimia.
“Ni poa chalii wangu! Ebwana unanikumbuka?” aliniuliza. Akanifanya nimwangalie vizuri.
“Hapana! Nikumbushe!”
“Mimi ndiye chalii wa jana niliyemchukua shemeji kumpeleka kwao,” aliniambia.
Hapo nikamkumbuka, alikuwa yule bodaboda ambaye nilimchukulia usafiri Scaila jana yake kwa lengo la kumpeleka nyumbani kwao Tabata.
“Oh! Nimekukumbuka! Niambie! Shemeji yako alifika salama?” nilimuuliza.
“Daah! Bro kwani pale unataka kuoa?” aliniuliza swali lililonifanya nihisi kitu.
“Ndiyo! Kwani nini?” nilimuuliza, nikawa na hamu ya kutaka kusikia.
“Aisee bro yule demu siyo! Jana uliniambia nimpeleke kwao Tabata lakini aisee njiani si ndiyo akanibadilishia ramani!” aliniambia bodaboda huku akiniangalia kwa macho yaliyojaa huruma nyingi.
“Kivipi tena?” niliuliza.
“Aliniambia nimpeleke Maisha Club! Aisee nilipofika kulikuwa na lijamaa lilikuwa likiwasiliana naye, lilipomuona tu, akateremka na kumfuata. Lile lijamaa lilikuwa na matattoo, likamkumbatia na kuanza kubadilishana mate,” alisema bodaboda yule.
Ni kweli nilikuwa nikijua mambo mengi kuhusu Scaila ila hayo ambayo niliambiwa, yalionekana kama mapya kwani yaliniumiza.
Bodaboda aliendelea kuniambia mengi kuhusu Scaila, alivyopokelewa kwa shangwe na lijamaa hilo lililojichora matattoo na kumlipa kisha kuingia ndani.
Moyo wangu ni kama ulipigwa ganzi, nilihisi akili yangu ikienda sehemu ya mawazo na mawazo yakienda sehemu ya akili. Japokuwa nilijisikia hivyo lakini sikutakiwa kumuonyesha bodaboda maumivu yangu.
“Aisee! Ahsante sana kaka! Ndiyo maana tunaambiwa hawa mademu siyo kabisa,” nilimwambia jamaa yule, nikampa shilingi elfu kumi na kuondoka zangu.