sehemu ya 44
“Halo!” niliita, yaani kwa jinsi nilivyochanganyikiwa, nilipokea simu pasipo kujua mpigaji alikuwa nani, yaani nililiona jina lakini ubongo wangu ulishindwa kung’amua ni mtu gani alikuwa amenipigia simu muda huo.
“Halo!” niliita, sauti ilikuwa ya mwanamke.
“Hujambo mkwe!” nilisikia sauti hiyo, hapo ndipo nilipogundua alikuwa mama yake Scaila.
“Oh! Mama! Shikamoo!” nilimsalimia.
“Marahaba mwanangu!” aliitikia.
Nilizungumza naye, muda huo ulikuwa ni saa tatu kasoro, alichoniambia ni kwamba hakuwa akijisikia vizuri hivyo aliniomba sana nimruhusu Scaila aende kulala naye kwani mfanyakazi peke yake asingeweza kama tu ingetokea amezidiwa usiku.
“Pole sana mama!” nilisema kwa huruma.
“Haina shida. Haya magonjwa ya kizee yanatusumbua sana,” alisema mwanamke huyo.
“Kwa hiyo aje sasa hivi?” “Nimekuja kwa mjomba wake, nikirudi mida ya saa tatu, anaweza kuja,” aliniambia mama kwa sauti ya upole mno.
Kwa jinsi alivyokuwa akisikika, nilimuonea huruma mno, kwangu, mwanamke huyo nilimthamini kwa sababu sikuwa na wazazi, kitendo cha kuwa na Scaila, nilimchukulia kama mama yangu.
Nikakubaliana naye! Hapohapo nikatoka sebuleni na kumwambia Scaila kilichokuwa kimetokea, kwamba mama yake alinipigia simu na kuniomba aende nyumbani.
“Mbona hakuniambia?” aliniuliza.
“Labda alihitaji ruhusa kutoka kwangu! Amefanya jambo la maana sana,” nilimwambia Scaila.
Kwanza nikashukuru Mungu mno. Huyu Scaila alipanga kwenda klabu kukutana na mabwana zake, kitendo cha mama yake kuumwa na kumuhitaji kwenda nyumbani kingemfanya kuwa huko muda wote na hata ile nafasi ya kwenda klabu asingeipata kabisa japokuwa aliwaahidi wazazi wake kwamba ni lazima aende huko.
Nilikaa naye na kupiga naye stori sana, aliniambia maneno mengi kuhusu mapenzi yake kwangu, wakati mwingine nilimwamini lakini wakati mwingine moyo wangu uliniambia aliyekuwa akiongea hayo alikuwa Scaila, yuleyule msichana aliyekuwa na matukio mengi nje ya uwanja.
Maneno yake yakaniteka sana, ilipofika majira ya saa nne usiku, akajiandaa na kisha kumsindikiza. Kumbuka gari langu taili lilipata pancha hivyo nisingeweza kumpeleka, ila nilichomfanyia ni kumkodishia bodaboda aende huko.