Simulizi: Namtaka mpenzi wangu arudi

Simulizi: Namtaka mpenzi wangu arudi

Shunie

JF-Expert Member
Joined
Aug 14, 2016
Posts
157,081
Reaction score
464,063
SEHEMU YA 01-Nyemo Chilongani

“Unahitaji kuwa nani baadaye?” lilikuwa swali la kwanza mzee Jackson Gwamaka alimuuliza binti yake aliyeitwa Nandy aliyekuwa akisoma darasa la sita katika Shule ya Msingi Kurasini, jijini Dar es Salaam.

“Nitataka kuwa muimbaji wa nyimbo za Injili, nitataka nimuimbie Mungu mpaka viwete watembee, vipofu waone na wenye matatizo mbalimbali waponywe,” alijibu binti huyo mrembo huku akimwangalia baba yake kwa sura iliyojaa tabasamu pana.

“Unahisi utaweza kumuimbia Mungu maisha yako yote?”
“Ndiyo! Nitamuimbia mpaka naingia kaburini. Nitataka nimtumikie yeye tu katika maisha yangu,” alijibu msichana huyo.

Mzee Gwamaka akamwangalia binti yake kwa mara nyingine, tabasamu pana likatawala usoni mwake. Alimpenda Nandy, alikuwa mtoto wake pekee katika maisha yake.
Moyo wake ulikuwa na faraja kubwa, alipenda kumuona Nandy akizungumzia kuhusu ukuu wa Mungu. Kila siku alimlea binti yake katika mazingira ya kidini huku akimwambia kuhusu ubaya wa wanaume.

Hakutaka kumuona binti yake akipotea, katika maisha yake alitamani kumuona akiendelea kumsifu Mungu mpaka pale atakapoingia kaburini. Mke wake, alifariki dunia siku alipokwenda kujifungua hospitalini. Moyo wake ulimuuma, alilia sana na ndiyo maana kwa Nandy alikuwa roho yake, faraja yake na hakutaka kumuona binti yake huyo akipotea.

Kila siku alimfundisha Nandy Neno la Mungu, alimwambia mambo mengi makuu ambayo Mungu alikuwa akiyatenda tangu kipindi cha Isaka,Yakobo na vizazi vingine vilivyofuata vikiwemo vya Mfalme Daudi na Suleimani.

Mbali na kutamani kumtumikia kumtumikia Mungu, Nandy alikuwa miongoni mwa mabinti waliokuwa na sura nzuri kupita kawaida japokuwa alikuwa akiishi kwenye umasikini mkubwa.
Mtaani hapo Kurasini alipokuwa akikaa, gumzo lilikuwa yeye tu. Alikuwa na umri mdogo lakini kila mtu aliyekuwa akimwangalia aliamini kwamba msichana huyo angekuja kutingisha sana siku za usoni.

Barabarani, wanaume walimtolea macho, kila aliyemwangalia hakuacha kumwangalia mara moja, alimwangalia mara mbili-mbili huku wengine wakidiriki kusimama na kumwangalia mpaka alipopotea katika macho yao.
 
SEHEMU YA 02

Shuleni hakuwa msichana muongeaji, alikuwa mkimya huku muda mwingi akipenda kujisomea Kitabu Kitakatifu cha Biblia ambacho alikuwa akienda nacho mpaka shuleni.

Watu walimzoea kwa kumuita Sista kwani alionekana kupenda sana dini kuliko hata kusoma masomo ya darasani. Pamoja na sura yake nzuri, mvuto wake, Mungu alimbariki Nandy sauti.

Alijua kuimba, kila alipokuwa akisimama kanisani na kuongoza pambio watu walichanganyikiwa, sauti yake ilikuwa kali, iliyochujwa kiasi kwamba kila mmoja akamtabiria kuwa muimbaji mashuhuru nchini Tanzania miaka ya baadaye.

Siku zilikatika mpaka pale alipoingia darasa la saba na kumaliza. Uzuri wake uliongezeka, nyonga zikatanuka na kifua kuanza kuchuja. Urembo wake ukaongezeka na wanaume wakazidi kumpenda na hata wengine kuanza kumfuatilia kwa kuwa waliamini kwamba alikua hivyo alistahili kulala naye.

Wanaume wakaanza kumchombeza kwa maneno mbalimbali, wale wasiokuwa na aibu ya kutembea na watoto wadogo hawakumuacha, kwao, kitendo cha kifua kuonekana kimejaa tayari alionekana kuwa mkubwa.

Nandy aliogopa, hakukuwa na mwanaume aliyediriki kusimama naye, kila alipokuwa akiitwa, alikimbia, kwake, kwa malezi aliyokuwa amepewa na baba yake yalimfanya kuwaogopa wanaume kupita kawaida.

Wanaume hawakutaka kukata tamaa, kwao, hizo zilionekana kama changamoto na hivyo kuendelea kumfuatilia. Idadi ya wanaume waliokuwa wakimtaka ikaongezeka, kila mtu akatamani kulala na Nandy na kuwa mwanaume wa kwanza kufanya naye mapenzi katika maisha yake.

Nandy alijichunga, hata alipoingia kidato cha kwanza katika Shule ya Wasichana ya Jangwani bado msimamo wake ulikuwa uleule kwamba hakutaka kulala na mwanaume yeyote yule.

Kila walipokuwa wakitoka shuleni, wanafunzi wa Shule ya Wavulana ya Azania walikuwa wakisubiri nje, kila mmoja alitamani kumuona kwani alionekana kuwa msichana wa tofauti sana huku wengine wakihisi kwamba Mungu aliamua kumuumba msichana huyo wikiendi, kipindi ambacho alipumzika na kumuumba kwa udongo wa tofauti na wengine.

“Nandy!” alijikuta mwanafunzi mmoja akilitaja tu jina hilo.
“Amefanyaje tena?”
 
SEHEMU YA 03

“We acha! Yule demu mkali bwana! Demu ni nuksi sana,” alisema mwanafunzi huyo huku akimwangalia rafiki yake na kuanza kucheka.
“Sasa wewe umegundua hilo leo?”
“Hapana! Nimegundua tangu siku ya kwanza nilipomuona. Ninasema hivyo kwa sababu amenichanganya sana. Nandy mzuri mno, demu bomba sana,” alisema mwanafunzi huyo.

Ni stori za uzuri wa Nandy ndizo zilizokuwa zimetawala midomoni mwa wavulana wengi. Walimpenda kwa kuwa alikuwa na sura nzuri, ngozi laini ambayo wanaume wengi iliwafanya kumfuatilia pasipo kumpata.

Nyumbani, mzee Gwamaka aliendelea kukandamiza misumali, kila siku ilikuwa ni kuongea na binti yake na kumwambia mambo mengi kuhusu wanaume, hakutaka kabisa kumuona binti yake akiingia kwenye mahusiano ya kimapenzi kwa sababu tu hakutaka kuona akiumizwa.

Aliwaponda wanaume, akaufanya moyo wa Nandy kuwaona wanaume wana roho ya kinyama, aliwachukia na kila alipokuwa akiitwa, aliogopa na kukimbia.
Aliendelea na maisha hayo ya kuogopa wanaume mpaka alipofika kidato cha nne. Japokuwa alionekana kuwa mkubwa lakini bado aliendelea kuwaogopa wanaume kila siku, hakuacha kuwakimbia kila alipokuwa akiitwa na wanaume.

“Nandy! Tatizo nini kwani?” aliuliza mwanafunzi mmoja huku akiwa amemshika Nandy mkono, hakutaka kumuachia kwani aliwahi kumuita mara nyingi sana lakini msichana huyo alikuwa akimkimbia.

“Niachieee...”
“Nikuachie! Umenikimbia sana, leo niambie ukweli!”
“Ukweli wa nini Mike. Niachieeeee.”
“Nataka uniambie! Unanipenda au hunipendi?”

“Nimesema niachieeeee...”
“Nijibu kwanza.”
“Sikupendi! Sikutakiiiii...” alisema Nandy na kwa kutumia nguvu zake, akajitoa mkononi mwa Mike na kukimbia.
Hilo likaonekana kuwa tatizo, Nandy hakutaka kukubali, alipofika nyumbani tu, kitu cha kwanza kilikuwa ni kumwambia baba yake kilichokuwa kimetokea.

Mzee Gwamaka alivimba kwa hasira, hakuamini kama kungetokea mvulana ambaye angemfanyia hivyo binti yake. Siku iliyofuata, ili kuonyesha kwamba binti yake hakutakiwa kuguswa akaelekea shuleni huko na kuwaambia walimu ambapo baada ya Nandy kuulizwa akamtaja kijana huyo.
 
SEHEU YA 04

Adhabu iliyotolewa siku hiyo, hakukuwa na mwanafunzi aliyediriki kumsogelea Nandy na kumwambia kitu chochote kuhusu mapenzi, wote walimuogopa kwani kila walipokumbuka mzee Gwamaka jinsi alivyokwenda shuleni hapo akiwa amevimba kwa hasira, hakukuwa na mtu aliyediriki kumsogelea.

Mpaka Nandy anamaliza kidato cha nne shuleni hapo bado hakuwa amemjua mwanaume yeyote yule. Aliendelea kujitunza kujitunza huku akimwambia baba yake kwamba malengo yake katika maisha yake yalikuwa ni kumtumikia Mungu mpaka anaingia ndani ya kaburi.

Baada ya kukaa nbaada ya kumaliza kidato cha nne ndipo walipotangaziwa kanisani kwao kwamba kungekuwa na mkutano mkubwa wa injili ambao ulitarajiwa kufanyika katika Viwanja vya Jangwani huku mhubiri mkubwa wa Kimataifa, Benn Hinn akitarajiwa kuhubiri katika viwanja hivyo.

Hiyo ilikuwa ni taarifa njema, kwa kuwa alikuwa na sauti nzuri huku akipewa uongozi katika kuimba pambio, Nandy akaambiwa ajiandae kwani alitakiwa kuongoza pambio katika kipindi chote cha mkutano huo.

Kwake, nafasi hiyo ilikuwa kubwa mno. Alimfahamu muhubiri huyo wa kimataifa aliyekuwa akizunguka dunia nzima huku akilihubiri Neno la Mungu, kitendo cha kuteuliwa kuongoza kikundi cha pambi katika mkutano huo ilionekana kama ndoto yake kuwa kweli.

Matangazo bado yalikuwa yakiendelea kufanyika, makanisani watu walitangaziwa kuhusu mkutano huo mkubwa wa injili. Kila mtu alichanganyikiwa, Wakristo wengi wakatamani kuhudhuria mkutano wa mhubiri huyo aliyekuwa akivuma duniani.

Viwanja vya Jangwani vikaonekana kuwa vidogo kwani Wakristo wengi jijini Dar es Salaam walipanga kwenda huku hata wale waliokuwa mikoani nao wakisafiri kuelekea jijini humo kwa lengo la kusikiliza mahubiri kutoka kwa mhubiri huyo.

Baada ya siku kukatika, hatimaye mkutano mkubwa wa Injili ukaanza katika viwanja hivyo. Siku ya kwanza, alihakikisha anamuimbia Mungu kwa uwezo mkubwa ambao hakuwahi kuimba maishani mwake mwote.
 
SEHEMU YA 05

Sauti yake ilipoanza kusikika, watu walichanganyikiwa, kila mtu akaangalia vizuri jukwaani, alitaka kumuona msichana aliyeimba kwa sauti nzuri na kali kiasi kile. Macho yao yalitua kwa msichana Nandy ambaye alinyanyua mkono mmoja juu huku mwingine akiwa ameshikilia kinasa sauti.

Aliimba kwa nguvu, jasho lilimtoka, hakujali, katika kumuimbia Mungu hakujali kitu chochote kile. Mawazo yake na akili yake ilikuwa kwa Mungu wake, alicheza na kurukaruka kiasi kwamba wakati mwingine alionekana kama kuchanganyikiwa.

Mkutano ulipomalizika, kila mtu alimfuata na kumsifia kwani siku hiyo ya kwanza alionekana kuwa moto wa kuotea mbali kwa jinsi alivyomsifu Mungu. Kila alipopongezwa, hakuchukua utukufu, aliwaambia watu kwamba utukufu ulikuwa kwa Mungu aliyekuwa juu.
“Ila umeimba bwana!”

“Nashukuru mama! Utukufu kwa Mungu,” alisema kila alipofuatwa na kusifiwa.
Akaanza kujiandaa, baba yake, mzee Gwamaka alikuwa akimsubiri kwa kuongea na watu mbalimbali.

Hakutakiwa kuondoka mapema kwa kuwa kanisa lao ndilo lililoandaa mkutano, alitakiwa kuhakikisha kila kitu kinakaa sawa kabla ya kesho kuja na kuendelea na mkutano.

Wakati akiendelea na marafiki zake kuweka vitu vizuri akasikia akiitwa kwa nyuma, alipogeuka, macho yake yakatua kwa kijana mmoja ambaye alipiga hatua kumsogelea pale alipokuwa.
 
SEHEMU YA 06

Kwa kumwangalia kijana huyo, isingekupa kazi kugundua kwamba alitoka katika familia ya maisha mazuri. Alivalia shati jeupe, tai nyeusi na suruali nyeusi huku akiwa na miwani ya macho.

“Bwana Yesu asifiwe Nandy,” alisalimia kijana huyo kwa sauti ya upole kabisa.
“Amen kaka!” alijibu na kuendelea na kazi yake.

“Mungu amekubariki sana, amekupa kitu adimu mno. Umeimba kupita kawaida, hiyo sauti yako, hakika mshukuru sana Mungu!” alisema kijana huyo huku akiachia tabasamu, japokuwa palikuwa na kigiza fulani lakini Nandy aliliona vizuri tabasamu lile.

“Nashukuru! Utukufu kwa Mungu!”
“Naitwa Dickson Kambili!” alijitambulisha kijana huyo na kumpa mkono lakini Nandy hakunyoosha mkono wake kumsalimia.
“Nashukuru kukufahamu!”

“Basi sawa. Ulinzi wa Mungu uwe nawe. Usiku mwema, Mungu akutangulie kama alivyomtangulia baba yetu, Ibrahim,” alisema Dickson maneno mengi ili naye aonekane aliijua sana Biblia.

“Amen!” aliitikia Nandy huku akiendelea kupanga vitu. Dickson hakutaka kujali, huyo akaondoka zake huku akionekana kuwa na furaha kuzungumza na msichana huyo kwa siku ya kwanza.

Je, nini kiliendelea?
 
SEHEMU YA 07

Dickson alikuwa akisubiria kujiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa lengo la kwenda kusomea utabibu chuoni hapo. Moyo wake ulikuwa na furaha tele, hakuamini kwamba mara baada ya kupambana kwa kipindi kirefu hatimaye alikuwa akitimiza ndoto yake ya kuwa daktari katika maisha yake.

Tangu alipokuwa kidato cha kwanza, alikuwa akimwambia baba yake mara kwa mara kwamba alitamani sana kuwa daktari, alipokuwa akienda hospitalini, aliumia kila alipokuwa akiwaona wagonjwa wakiugua vibaya na wengine kushindwa kabisa kusimama kama zamani.

Moyo wake uliuma na kujiona kuwa na uhitaji mkubwa wa kuwasaidia wagonjwa hao na hivyo kupanga kusomea utabibu kitu ambacho alikuwa njiani kwenda kukamilisha ndoto yake. Matokeo yake ya kidato cha sita yalikuwa vizuri na alipata alama za juu na hivyo kutakiwa kujiunga katika chuo hicho.

Alikuwa akisubiri siku ya kwanza kwenda kujiunga chuoni huko. Kwa kuwa baba yake alikuwa na pesa nyingi, alichokifanya ili kumfanya mwanaye kuwa na furaha, aone kile alichokuwa amekifanya kilikuwa na thamani sana, akamchukua na kwenda naye nchini Ufaransa.

Hiyo haikuwa mara ya kwanza, tangu alipokuwa kidato cha kwanza, alipokuwa akifanya vizuri alichukuliwa na kupelekwa nchi mbalimbali kutembea. Alikuwa na maisha mazuri, alipata alichokitaka na kila siku aliishi maisha matamu kana kwamba alikuwa peponi.

Wakati akiwa nchini Ufaransa, akapewa taarifa kwamba mhubiri wa kimataifa, Benny Hinn angekuwa nchini Tanzania katika mkutano mkubwa wa siku saba.
Hakutaka kubaki nchini Ufaransa, kwa kipindi kirefu alikuwa akisikiliza mahubiri kutoka kwa mchungaji huyo, aliyapenda, alipenda namna alivyokuwa akihubiri na hata kuwaombea watu hivyo kumwambia baba yake kwamba ni lazima wakatishe ziara yao ya kutembelea sehemu mbalimbali jijini Paris na hivyo kurudi Tanzania.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom