Simulizi: Namchukia Mama Yangu

Simulizi: Namchukia Mama Yangu

Shunie

JF-Expert Member
Joined
Aug 14, 2016
Posts
157,076
Reaction score
463,977
Sehemu ya 01

Mtunzi Ally Katalambula

Waswahili wanasema uchungu wa mwana aujuaye mzazi lakini kwa mama yetu ilikuwa kinyume. Sikuamini mama yetu mzazi kuwa chanzo cha matatizo ya familia yetu, pengine hata mimi kushindwa kufikia ndoto zangu za kusoma hadi chuo kikuu na kuishia kidato cha nne huku nikifeli vibaya.

Mwanzo sikuelewa lolote kwa vile nilikuwa na akili za kitoto na kuona kila kitu kipo sawa. Lakini nilikuja kuufahamu ubaya wa mama baada ya kuingia kwenye ndoa ambayo iligubikwa na utata mkubwa na hapo ndipo nilipoyaona makucha ya mama.

Ni mama yangu lakini kama asingekuwa mzazi wangu sijui tungefikishana wapi.
Mambo aliyonitendea mama yangu, kama mzazi aliyenizaa kwa uchungu, hakutakiwa kunifanyia kamwe . Lakini kama sitatanguliza shukrani nitakuwa mwizi wa fadhila. Waswahili wanasema mnyonge mnyongeni haki yake mpeni.

Kwanza kabisa lazima nitangulize shukrani zangu za dhati kwa mama yangu mzazi, kwa kunizaa na kunilea, pia kunipa elimu aliyonikadiria mwenyewe. Hiyo ni hatua kubwa sana katika maisha ya mwanadamu anayopitia akiwa mikononi mwa wazazi wake.

Kabla sijafunguka akili nilimuomba Mungu katika maisha yangu awezeshe uwezo wa kulipa hata robo ya yote aliyonifanyia mama yangu, japo nilijua ni kazi kubwa. Toka nikiwa binti mdogo nilijua mama yangu ndiyo kila kitu kwa vile alijitoa kwa ajili yetu.

Maisha yote tuliishi na mama yetu, sikubahatika kumuona baba, nilielezwa alifariki mama yangu akiwa na ujauzito wangu wa miezi sita, kwa hiyo sura ya baba yangu niliiona kwenye picha tu. Siku nilipojua siri ya kifo cha baba nilikuwa hoi. Nimeamini nyuma ya mioyo ya watu kuna siri kubwa, ndiyo maana huwezi kujua dhamira ya mtu. Namuomba Mungu asinipe moyo wa mama.

Najua unataka kujua kwa nini mama yetu alituzaa ili ageuke adui yetu namba moja, kwa vile tuko pamoja naomba twende nami ili siku moja ukubaliane na kauli yangu ili akina mama mwenye roho kama ya mama yangu wabadilike.

Naitwa Mwaija, mtoto wa mwisho katika familia ya marehemu mzee Salmini. Japokuwa sikubahatika kumuona baba yangu naambiwa nilifanana naye sana. Katika familia ya watoto watano, wa kike wanne na wa kiume mmoja. Baada ya kuhitimu kidato cha nne nilipata mchumba wa kunioa.

Ukweli mchumba wangu hakuwa mgeni kwangu, ni mwanaume wangu niliyeanza naye urafiki toka nipo kidato cha pili. Mwanzo tulifanya mapenzi ya siri japokuwa katika dada zangu, mmoja alimfahamu baada ya siku moja kuniona naye kwa mbali. Aliponiuliza nilijaribu kumficha lakini aliponibana nilimweleza ukweli. Basi ikawa kila siku nikikutana na mpenzi wangu lazima nimpelekee dada zawadi.

Ahadi yetu ilikuwa nikimaliza kidato cha nne tuoane, japokuwa mwanzo nilikuwa na ndoto za kufika chuo kikuu, lakini mazingira ya nyumbani yalinifanya nipoteze mwelekeo wa masomo na kuyabadili mawazo yangu yote kuhamishia kwa mpenzi wangu ambaye muda mwingi baada ya masomo nilikwenda kwake.

Hata matokeo ya kidato cha nne yalipotoka na kuonesha nimefeli vibaya sikushtuka kama wengine waliofikia hatua ya kutaka kujiua. Kwangu ilikuwa sawa kwa vile niliamini kabisa muda ule ulikuwa muafaka kwa mimi kuolewa na Beka.

Baada ya matokeo nilimfuata mwenzangu na kumweleza ule ndiyo ulikuwa muda muafaka wa yeye kuja kujitambulisha rasmi nyumbani.

Siku nilipomtambulisha hakuwa mgeni kwa dada, baada ya kuondoka mpenzi wangu, familia yangu ilitaka kujua anafanya kazi gani. Niliwaeleza ni dereva wa teksi.
“Teksi yake au ameajiriwa?” mama aliniuliza.

“Ameajiriwa.”
“Sasa akifukuzwa kazi mtakula nini?”
“Mama mbona umekimbilia kufukuzwa kazi kuliko yeye kununua yake?’
“Atawahi! Mwanangu hawa dada zako wamekosa nini hapa nyumbani?”
“Mama wao hawakupenda kukaa nyumbani bali mapenzi ya Mungu.”

“Hata kama kazi ya Mungu, lakini toka warudi nyumbani wana tatizo gani?”
“Hawana matatizo, lakini wao ndiyo hawataki kuolewa tena.”
“Hawataki kuolewa kwa sababu wanaume wasio na uwezo ni mzigo kwa familia tu, kesho akifukuzwa kazi nikulishe mimi?”
“Mama ni kuniombea kwa Mungu nifanikiwe.”

“Kwa kazi kama hiyo nakuomba uachane na wazo hilo,” mama alinikata maini.
“Mama siwezi kuachana na wazo hilo kwa vile nitakayeolewa ni mimi.”
“Kama una uamuzi wako, sawa olewa kwa amri yako.”

“Mama nipo tayari kuishi maisha yoyote ndani ya ndoa, tutaishi hivi mpaka lini tunajazana nyumbani hata heshima hatuna?”
“Kwa hiyo umefanya vibaya kwenye mtihani ili uolewe?”
“Mama uliniambiaje?”
“Nilikuambia nini?”

“Mama si uliniambia huna hela za kunisomesha tena?”
“Ndiyo umefeli kiasi hicho?”
“Lakini matokeo yalipotoka mama si ulisema afadhali, leo hii umenigeuka?”
“Kote huko tunazunguka, kifupi huwezi kuolewa na kabwela.”
“Lazima nitaolewa,” nilimpinga mama.
“Mimi na wewe nani kamzaa mwenzie? Kama wewe umenizaa utaolewa.”

Kwa kweli kauli ya mama ilikuwa mkuki moyoni mwangu, nilitegemea mimi kupata mume angefurahi kuliko kuendelea kujazana nyumbani. Lakini ilikuwa tofauti kubwa na mawazo yangu, alipenda tujazane huku nyumba yetu ikiwa na sifa mbaya ya kuitwa danguro kutokana na dada zangu kubadili wanaume kila kukicha, kila mwenye fedha ndiye aliyependwa.

Baada ya mama kunikatalia niliwafuata dada zangu kuwaeleza maneno ya mama, nao nilishangaa kugundua wapo upande wake kwa kumuunga mkono, wakanieleza:
“Mwaija umekosa nini mpaka ukimbilie kuolewa na dereva teksi?”

“Dada, ndiye chaguo langu.”
“Muda wa kujichagulia haujafika, unatakiwa kuchaguliwa mwanaume.”
“Dada hata siku moja siwezi kuchaguliwa, mkinilazimisha nitatoroka.”
“We toroka, yakikufika usirudi.”
“Sawa.”
Siku ile nililia usiku kucha na kutishia kujiua kama watanikataza kuolewa na Beka, vitisho vyangu viliwafanya walegeze masharti kidogo.

Mama alikubali niolewe kwa shingo upande. Kwangu sikujali kwa vile niliamini maisha yangu yalinitegemea mimi mwenyewe, baada ya kutimiza miaka kumi na nane nilitakiwa kuwa na uamuzi wangu mwenyewe bila kuingiliwa na mtu.

Ilikuwa tofauti na nilivyodhania kwamba harusi yangu ingedoda kutokana na kuwa na vipingamizi. Maandalizi yangu ya harusi yalikuwa makubwa sana. Mama na dada zangu walishirikiana kwa hali na mali, katika kicheni pati nilipata vitu vya zaidi ya shilingi milioni nne.

Siku nne kabla ya harusi, nyumbani kwetu ilikesha rusha roho mfululizo. Harusi yangu ilitikisa mtaa na ilikuwa tofauti na wenzangu. Baada ya ndoa nilihamia kwa mume wangu Beka aliyekuwa akikaa Tandika Maguruwe.

Sikuamini ushirikiano nilioupata kwa mama na dada zangu muda wote nikiwa mgeni wa ndoa. Nilijikuta nikiyasahau yote yaliyopita ya kukatazwa kuolewa na mwanaume kabwela. Kwa vile nyumbani hakukuwa mbali toka Temeke Mikoroshoni mpaka Maguruwe, ilikuwa haipiti siku mbili au tatu lazima mama afike kunijulia hali.

Miezi sita baada ya ndoa yangu nilipata ujauzito, kwa furaha ya kupata ujauzito nilikwenda kumwambia mama.

INAENDELEA...
 
Sehemu ya 02

Miezi sita baada ya ndoa yangu nilipata ujauzito, kwa furaha ya kupata ujauzito nilikwenda kumwambia mama.
“Mama sipo vizuri.”

“Kivipi?”
“Nina wasiwasi nina ujauzito.”
“Ujauzito?” mama alishtuka.
“Ndiyo.”
“Umejuaje?”
“Baada ya kupima leo asubuhi na kujiona kweli nina mimba.”

“Mmh! Sawa.”
“Mbona kama hukufurahi?”
“Mwanangu unabeba ujauzito wakati maisha ya mumeo unayajua?”
“Mama maisha ya mume wangu na ujauzito wangu vinaingiliana vipi?”
“Mwanangu mtoto anatakiwa malezi.”
“Mama mume wangu mbona ana maisha mazuri tu, hatujawahi kulala na njaa hata siku moja.”

“Mwanangu maisha nayajua mimi mama yako, mwanzo utayaona mazuri baadaye mtafikia hata kipande cha muhogo unakitafuta. Ulitakiwa upitishe hata mwaka ndipo ubebe ujauzito, wewe miezi sita tu, unakimbilia nini unafikiri kuzaa raha?”

“Mama mbona wasichana wa umri wangu wengi wamezaa.”
“Usiishi kwa kuangalia jirani bali maisha yako mwenyewe.”
“Lakini mama kwani tatizo lipo wapi?”
“Ulitakiwa uniulize kuliko kukimbilia kubeba ujauzito.”

“Sasa haya makubwa, suala ya kubeba ujauzito nije kutaka ushauri kwako?”
“Basi tuachane na hayo, vipi mumeo?”
“Namshukuru Mungu, sasa hivi kidogo mambo yanamwendea vizuri amenunua kiwanja.”

“He! Kanunua kiwanja?”
“Ndiyo, mbona umeshtuka?”
“Hapana, kanunua wapi?”
“Charambe.”
“Mmh! Mbona nje ya mji?”
“Mama siku hizi hakuna nje ya mji maadam magari yanafika.”

“Ameshaanza kujenga?”
“Bado.”
Kwa vile muda ulikuwa umekwenda nilirudi nyumbani kuwahi kuandaa chakula cha mchana. Nikiwa nyumbani nilijawa na mawazo mengi kutokana na kauli ya mama kuhusiana na ujauzito wangu.

Niliamua kuipuuzia na kuendelea na mambo yangu huku nikipanga baadhi ya mambo yangu nisimshirikishe mtu yeyote katika familia yangu.
Niliendelea kumshukuru Mungu kwani maisha yaliendelea vizuri tofauti na wasiwasi wangu kutokana na maneno ya mama.

Siku moja nikiwa nimekaa na mume wangu aliniambia kitu ambacho kilikuwa faraja kwangu.
“Mke wangu, Mungu kanijalia kumpata mke mwenye mapenzi yake kweli mwenye nyota ya bahati.”

“Kwa nini mume wangu?”
“Huwezi kuamini kila ninachokifanya sasa hivi kinafanikiwa tofauti na zamani. Wiki ijayo tunaanza ujenzi wa nyumba yetu.”
“Usiniambie!” nilifurahi sana.

“Nilikuwa na wazo la kununua gari, lakini nimeshauriwa kwa vile gari nimeachiwa kama langu, basi nianze kwanza nyumba kisha gari.”

“Tutajenga nyumba kubwa au?”
“Tutasimamisha kwanza vyumba viwili mambo mengine yatafuata.”

Maneno ya mume wangu yalikuwa faraja sana kwangu baada ya kujiona kumbe nami ni mmoja wa viumbe wenye bahati. Niliendelea kumuomba Mungu maisha yasibadilike tuendelee kufanikiwa. Lakini alinionya kitu kimoja kuwa suala letu la kujenga nisimwambie mtu.

“Hata mama?” nilishtuka kusikia vile.
“Mtu yeyote, hata wazazi wangu sijawaambia, watajua siku tukitaka kuhamia kwetu, wanadamu hawaaminiki.”

“Mmh! Sawa.”
“Narudia siri hii ni yangu mimi na wewe tu.”
“Nimekuelewa mpenzi wangu.”
“Si kujenga tu, chochote cha kwetu iwe siri yetu sawa mpenzi?”

“Sawa mpenzi wangu.”
Baada ya kuachana na mume wangu nilijikuta njia panda kutokana na kauli yake ya kufanya mambo yetu kwa siri. Nilijiuliza itakuwaje ikiwa nilikuwa tayari nimeishamwambia mama kila kitu pia nilimuahidi kumpeleka tunapojenga. Nilipanga kufanya siri huku nikumuomba mama naye asimwambie mtu hata dada zangu ili ibakie siri sirini.

Wiki iliyofuata tulianza kuchimba msingi wa nyumba, mwisho wa wiki hiyohiyo ndiyo niliyompeleka mama kwenye kiwanja chetu. Kabla ya kumpeleka nilimweleza kuhusiana na kauli ya mume wangu kuwa hakupenda mambo yetu kila mtu ayajue.

Nilimuomba mama siri ya kwenda kule ibakie moyoni mwake ili mume wangu asinione msaliti.

Tuliongozana hadi kwenye saiti yetu, tulipofika alishtuka sana hatua tuliyofika. Nyumba ilikuwa imeanza kunyanyuka ilikuwa tayari ipo katika kozi tatu. Mume wangu alipanga baada miezi mitatu tuwe ndani mwetu.
“Mmh! Hongera,” aliguna kabla ya kutoa pongezi.
“Mama mbona umeguna kwanza?”

“Walaa, umenisikia vibaya.”
Baada ya mama kupaona tunapojenga tulirudi nyumbani, tukiwa njiani mama alinipa moyo huku akiniombea kwa Mungu tumalize nyumba yetu haraka ili nasi tukae kwetu. Nilimshukuru mama yangu kwa dua lake.

Niliagana na mama na kurudi nyumbani na siri yangu moyoni, nilimuomba Mungu mama naye awe msiri ili kuongeza uaminifu katika ndoa yangu.

Siku zilikatika huku mama akizidi kuja kunitembelea na kunipa maadili ya ndoa. Kwa kweli nilijivunia kuwa na mama mwenye mapenzi ya kweli na familia yake.

Siku moja nilikuwa nikitoka ndani, niliponyanyua mguu kuvuka mlango nilihisi kizunguzungu kikali. Nilijitahidi nisianguke, japo mbele nilikuwa sioni nilishika ukuta na kukaa chini.

Kilichoendelea sikujua mpaka niliposhtuka na kujikuta nipo Hospitali ya Temeke nikiwa nimelazwa tena naongezwa damu.

Nilishtuka kuwa katika hali ile, nikiwa bado nipo kwenye maswali magumu yasiyo na majibu, aliingia muuguzi na kusogea kitandani kwangu na kunisemesha.

“Vipi dada?”
“Poa,” nilijibu kwa sauti ya kutaka kujua nimefikaje pale.
“Pole.”
“Asante,” nilijibu huku macho yangu yakiwaona mama na dada zangu aliyekuwa akisogea kwenye kitanda.
“Mwaija,” mama aliniita.

“Abee mama.”
“Pole mama.”
“Asante.”
“Pole Mwai,” dada zangu nao walinipa pole.

“Asante.”
“Vipi unaendeleaje?”
“Hata najua! Sielewi nimefikaje hapa na pia naumwa nini!” kwa kweli nilikuwa sijui lolote zaidi ya kushikwa na kizunguzungu na kujitahidi nisianguke na kukaa chini, zaidi ya hapo sikujua kitu.
“Pole sana,” mama alinipa pole baada ya kusikia maelezo yangu.

“Asante.”
Baada ya muda alikuja mume wangu na ndugu zake, wote walinipa pole. Jioni ya siku ile nilimaliza kuongezwa damu na kuweza kuzungumza na waliokuja kuniona. Jirani yangu mama Saidi ndiye aliyeniokota na kunieleza kilichotokea siku ile.

“Basi shoga nilipotoka ndani nilikukuta umelala pembeni ya mlango wako ukiwa umepoteza fahamu na chini ulikuwa umetoka damu nyingi kama kachinjwa mbuzi.”

“Mungu wangu!”
“Basi ikabidi niwaite dada zako, pia nilimpigia simu mumeo, bahati nzuri walifika wote kwa pamoja na kukuleta huku.”
“Mmh! Nashukuru dada yangu sijui bila wewe ingekuwaje?”
“Tumshukuru kwa kila jambo.”

“Mmh! Una maana nimetoka damu nyingi?”
“Ndiyo, ulifanya nini?”
“Nifanye nini zaidi ya kukaa chini, jamani mimba haijatoka?” nilishtuka baada ya kujua ujauzito wangu unaweza kuwa umetoka.

“Kwa kweli sijui, kwani daktari anasemaje?” jirani yangu aliniuliza.
“Sijazungumza naye chochote wala sijamuona mtu wa kwanza muuguzi.”

Baada ya majirani zangu kuondoka alikuja mama na kukaa pembeni yangu na kunishika mkono kama ananikanda kuonesha kuna kitu anataka kuniambia. Sikuwa na haraka nilitulia kumsikiliza mama alitaka kusema nini.

“Mwaija,” mama aliniita kwa sauti ya chini.
“Abee mama.”
“Unajisikiaje?”
“Kwa kweli kama nilivyokujibu mwanzo sijui lolote, sijui nimekujaje na sasa nipo kwenye hali gani.”

“Kwani daktari amesemaje?”
“Bado sijazungumza naye na wala sijamuona.”
Mara aliingia daktari na kusogea kwenye kitanda akiwa na muuguzi.

“Samahani, naomba kumhudumia mgonjwa.”
Mama na ndugu zangu walitoka nje ya wodi na kuniacha peke yangu. Baada ya kutulia daktari alianza kunipima mapigo ya moyo na kuandika kwenye kadi yangu, kisha alimuomba muuguzi aondoe chupa ya damu iliyokuwa imekwisha.

Baada ya kuondoa sindano mkono, aliniuliza:
“Unajisikiaje kwa sasa?”
“Kwa kweli sijui chochote.”
“Lazima ujue, ilikuwaje ukaletwa hospitali na hali uliyokuja nayo ukiwa hujitambui na sasa hivi.”

“Nina imani sasa sijambo kwa jinsi nilivyoelezwa.”
“Kichwa vipi?”
“Kimetulia.”
“Kizunguzungu?”
“Sina.”
“Hebu kaa,” nilifanya nilivyoelekezwa na mganga.

“Unajisikiaje?”
“Uchovu tu na njaa.”
“Nina imani unaendelea vizuri.”
“Eti dokta nasikia nimetoka damu nyingi sehemu za siri, mimba yangu haijatoka?”
“Kwani ilikuwaje mpaka ukatokwa na damu nyingi kiasi kile?”

Nilimueleza ilivyokuwa mpaka kuwepo pale hospitali.
“Si kweli inawezekana ulipigwa na kitu tumboni na kusababisha kuharibu ujauzito wako.”

“Mungu wangu mimba yangu imetoka,” nilianza kuangua kilio kama mtu niliyefiwa. Ilibidi daktari na muuguzi waanze kazi ya kuninyamazisha. Ilikuwa kazi ngumu kuninyamazisha, mpaka mama alipofuatwa na kuja kunikemea kwa maneno makali ambayo yalinifanya ninyamaze, lakini moyoni niliumia kupoteza mtoto wangu niliyepanga kumlea kama mboni ya jicho langu.
 
Sehemu ya 03

Ilikuwa kazi ngumu kuninyamazisha, mpaka mama alipofuatwa na kuja kunikemea kwa maneno makali ambayo yalinifanya ninyamaze, lakini moyoni niliumia kupoteza mtoto wangu niliyepanga kumlea kama mboni ya jicho langu.

Baada ya kupata matibabu niliruhusiwa kutoka hospitali na kurudi nyumbani. Mama alitumia muda mwingi kuniasa kuacha kuendelea kulia baada ya ujauzito wangu kutoka.

“Mwaija, kuendelea kulia ni uchuro unaweza ukafunga kizazi usizae tena.”
Mmh! Kauli ya mama ilinitisha sana na kumhakikishia mama sitalia tena japo niliamini ingechukua muda kusahau.
Siku nazo zilisonga, maisha yaliendelea huku nikiendelea kufurahia maisha ya ndoa yangu japokuwa ujauzito ambao ungeongeza ukoo ulitoka.

Nayo mapenzi ya mama yangu yalikuwa makubwa sana, ilikuwa haipiti siku mbili au tatu bila kuja kunijulia hali, japokuwa nami nilikuwa nikienda mara mojamoja tofauti na yeye ambaye kila mara alikuja kwangu.

Ajabu siku zote alizokuja hakutaka kuonana na mume wangu, niliendelea kumshukuru Mungu kutuongozea maisha yetu. Mwaka ulikatika huku suala la ujenzi likiwa limekwama, huwezi amini nyumba ilikomea kozi ya tano.

Maisha nayo yalianza kuwa magumu, biashara nazo ziligoma kiasi cha siku nyingine kulalia chai na kipande cha mkate. Kwa kweli nilianza kuona aibu ya mama kuja kushinda nyumbani kwani sikuwa na kitu. Ili kuficha aibu ile niliingia madeni kwa ajili ya kumpikia chakula nikiamini hali ile ni ya mpito tu.

Lakini kila kukicha ilikuwa afadhali ya jana, kuna kipindi mume wangu alirudi bila hata senti tano. Kuomba msaada nyumbani niliona aibu kwa vile yangetimia waliyoyasema. Lakini siku zote penye moto huwezi kuzuia kufuka moshi.

Pamoja na kufanya siri lakini hali yangu ilionekana, kwani nilianza kupungua mwili kutokana na kukosa kula.

Siku moja mama alipokuja kwa kweli sikuwa na ujanja, sikuweza kwenda kukopa kama kawaida yangu, madeni ya awali nilikuwa sijalipa pia ilikuwa siri yangu na sikutaka mume wangu ajue.

Ajabu siku ile mama hakukaa sana, alipotaka kuondoka alinipa elfu hamsini, kitu kilichonishtua na kunifanya nihoji:
“Za nini mama?”

“Mwaija unauliza za nini, maisha yako sasa yapo sawa?”
Kwa kweli nilishindwa kujibu kitu, moyo wangu uliingiwa aibu na kujua nimeumbuka mtoto wa kike na kumpa nafasi mama yangu kusema.

Nilibakia nimeinama chini kama mwari kwa vile maneno yalikauka mdomoni.
“Mwaija,” mama aliniita huku akinishika kichwani.

“A..a..bee mama.”
“Usijali ni sehemu ya maisha, najua sasa hivi mpo katika hali ngumu, lakini Mungu ataleta heri zake kila kitu kitakwenda vizuri.”

“Na...nashukuru sana mama.”
“Usihofu mwanangu ukizidiwa usione aibu kuja kuomba msaada.”
“Nashukuru mama yangu.”
“Na nyumba yenu imefikia wapi?”
“Mmh! Mama wee acha tu, mbona mwaka huu wetu.”

“Kwa nini?”
“Yaani ulipoona tumeongeza kozi mbili tu, yaani malengo ya mume wangu yameyeyuka kama donge la barafu. Mpaka muda huu alipanga tungekuwa nyumbani kwetu.”

“Mipango ya Mungu yote ya mpito, endeleeni kumuomba atakusikilizeni.”
Kwa kweli nilizidi kumshangaa mama, nilitegemea angeniporomoshea maneno, lakini siku ile alikuwa mpole. Baada ya kunikabidhi fedha ile aliondoka na kuniacha nikiwa na maumivu makali moyoni mwangu, huku nikijiuliza hali ile itaendelea mpaka lini.

Fedha niliyopewa na mama nililipa sehemu ya madeni na kununua mchele na sukari ambavyo niliamini vingetusaidia hata kama hatuna kitu tunaweza kuchemsha na chumvi na chai ili kudanganya tumbo.

Hali ilikuwa ileile, mume wangu kila aliporudi alitia huruma kwani biashara ilikuwa ngumu kila kukicha, kilichokuwa kikimshangaza kila alipofikisha hesabu ya bosi wake biashara ilikata.

Siku nyingine hata hesabu ya bosi ilikuwa haitimii. Wakati siku za nyuma baada ya ndoa yangu alikuwa akiingiza zaidi ya mara tano ya hesabu ya bosi wake, kitu kilichofanya maisha yetu yabadilike ghafla.

Siku moja baada ya chakula cha usiku tukiwa tumekaa sebuleni, mume wangu aliniita.

“Mwaija.”
“Abee mume wangu.”
“Nilikuambia nini?”
“Kuhusu nini?” nilishtuka kidogo.
“Nilikwambia nini kuhusu siri yetu ya ndani?”

“Nisimwambie mtu.”
“Kwa nini umekwenda kinyume?”
“Nimefanyaje mume wangu?”
“Kwa nini umemwambia mama yako?”
“Mimi?” nilijifanya kushtuka huku nikisonta kidole kifuani kwangu.

“Sasa nazungumza na nani?”
“Na mimi.”
“Sasa unaniuliza nini?”
“Mi sijamwambia mtu yeyote.”
“Kweli usemacho?” aliniuliza huku amenikazia macho.
“Kweli kabisa mume wangu,” nilizidi kukataa.

Nilikataa japokuwa mimi ndiye niliyemwambia mama hakuna mwingine. Lakini sikujua kwa nini aniulize swali kama lile, pia nilijiuliza nani kampa siri ile iliyokuwa ya watu wawili.
Wasiwasi wangu labda mama alitoa siri ile kwa mtu mwingine, nilipanga kwenda kumuuliza.

“Kama si wewe basi.”
“Kwani kuna nini mume wangu?”
“Hapana nilitaka kujua tu.”
“Hapana mume wangu, inawezekana kuna kitu umesikia tu?”
“Kama hujasema achana nalo.”
Kwa kweli sikutaka kumuuliza zaidi kwani moyo wangu ulinisuta. Baada ya mazungumzo mume wangu alielekea chumbani.

Kabla nami sijaingia nilimalizia kazi ndogondogo. Kisha niliingia chumbani na kumkuta mume wangu ameshalala.
Nilijilaza pembeni ya mume wangu, macho niliangalia juu nikiwa na mawazo mengi yaliyofanya nichelewe kupata usingizi. Nilikuwa na maswali mengi juu ya kusikia mume wangu kasikia wapi kuwa siri yetu imemfikia mama.

Lakini kwa upande mwingine, sikuona ubaya mama yangu kujua maendeleo yangu kwani bado nilihitaji msaada wake. Siku ya pili alipoamka aliondoka bila kukumbushia tuliyozungumza jana yake. Alipoondoka sikufanya chochote, mimi kiguu na njia hadi nyumbani na kumkuta mama ndiyo kaamka muda si mrefu, alishtuka kuniona asubuhi ile.

“Vipi mama karibu.”
“Asante, shikamoo mama.”
“Marahaba, leo umetukumbuka asubuhi?”
“Ndiyo mama.”
“Karibu.”

“ Asante.”
Baada ya kusalimiana na dada zangu, nilimuomba mama nizungumze naye chumbani kwake. Baada ya kuingia chumbani kwa mama alinisikiliza kilichonipeleka pale muda ule.
“Niambie mwanangu naona ujio huu una kitu.”

“Ni kweli mama.”
“Ehe! Una nini?”
“Eti mama ulimwambia nani kuhusu mume wangu kuwa na kiwanja na anataka kujenga?”
“Sijamwambia mtu,” mama alikataa.
“Maama!”
“Kwani kuna nini?”
“Mama umemwambia mtu wakati nilikwambia ile ni siri!”

“Sijamwambia mtu.”
“Kama hujamwambia mtu sasa yeye amejuaje kuwa wewe unajua siri ile.”
“Labda umemwambia mwenyewe.”
“Sijamwambia kitu, jana karudi swali la kwanza ananiuliza kwa nini nimekueleza kuwa tuna kiwanja na tunataka kujenga nyumba.”

“Kakuuliza hivyo?” mama alishtuka.
“Ndiyo mama.”
“Nani kamwambia?”
“Sasa mi nitajuaje wakati siri ile nilikuambia wewe peke yako.”
“Nakuapia mwanangu siri ile sijamwambia mtu hata ndugu zako hawajui kitu.”
“Mmh! Sasa taarifa za wewe kujua kazitoa wapi?”

“Hapo ndipo hata mimi pananichanganya.”
“Mama hujamwambia mtu?”
“Nakuapia kwa jina la Mungu sijamwambia mtu.”
“Mmh! Sawa, sasa kajua wapi?”
“Kwani alipokuuliza ulimjibu nini?”
“Nilimkatalia kuwa sijui lolote kuhusiana na habari zile.”

“Inawezekana labda ana wasiwasi na kuamini mtu wako wa karibu ni mimi. Kwa nini asimuulizie mtu mwingine mpaka aseme mimi, huoni amebahatisha ili kukuona kama umetunza siri.”
“Mmh! Inawezekana,” nilijikuta nikikubaliana na maneno ya mama.
“We mkatalie tu.”

“Sawa mama nitafanya hivyo.”
Baada ya mama kunihakikishia hajamwambia mtu siri ile, nilirudi nyumbani nikiwa na mawazo mengi juu ya kauli ya mume wangu. Lakini jioni aliporudi hakuulizia tena mpaka tunalala.
 
alafu kuna story huwa naitafutaga ya bibi ambaye alikuwa ametengeneza jeshi lake la wanyama ktk msitu wa naomba, naiomba maana mm huwa napenda sana story na ni mdau wako mkbwa

Sent using Jamii Forums mobile app
 
Sehemu ya 04

Baada ya mama kunihakikishia hajamwambia mtu siri ile, nilirudi nyumbani nikiwa na mawazo mengi juu ya kauli ya mume wangu. Lakini jioni aliporudi hakuulizia tena mpaka tunalala.
***

Siku ya pili aliondoka kama kawaida na kwenda kwenye mihangaiko, majira ya saa nne asubuhi mama alikuja kutaka kujua nini kilijiri baada ya mume wangu kutoka katika mihangaiko yake.
“Vipi aliuliza chochote jana?”
“Walaa hakuniuliza.”
“Unaona! Alikuwa na mashaka tu.”
“Lakini mama jambo lina mwaka iweje aulize jana?”

“Jiulize hata wewe.”
“Mmh! Ngoja tuone.”
“Wala usilifikirie tena hawezi kukuuliza ungebabaika mwanzo angepata pa kusemea.”

Baada ya mama kupata ukweli hakukaa, aliniachia fedha ya kula kama elfu kumi na kurudi kwake na kuniacha na mawazo yangu yaliyokosa jibu na kushangaa siri iliyotoka mwaka mzima siku ile ndiyo aiulizie. Niliamua kuachana naye na kuendelea na mambo mengine.

Jioni ya siku ile mume wangu aliwahi kurudi na alipofika aliingia chumbani kulala. Haikuwa kawaida yake kurudi mapema kiasi kile kitu kilichonishtua sana.

Kwa vile nilikuwa na kazi nilisubiri nimalize ili niende nikamuulize.
Baada ya kumalizia kuosha vyombo nilimfuata ndani mume wangu, nilimkuta amejilaza kitandani mikono kichwani, nilipomsogelea niligundua anatokwa machozi baada ya kuiona michirizi ya machozi pembeni ya macho.

Kitu kile kilinishtua sana, ilionesha mume wangu alikuwa mbali kimawazo, hata nilipoingia na kumwita hakushtuka. Nilimsogelea na kukaa pembeni yake na kumtikisa.

“Mume wangu...mume wangu,” nilirudia zaidi ya mara moja.
“Ee...ee...” alishtuka kuonesha alikuwa mbali kimawazo.
“Vipi?”
“Mke wangu nakupenda,” alisema huku anikumbatia na machozi yake yakigusa mashavuni kwangu.

“Hata mimi mume wangu mbona hivi leo jamani?”
“Sina kazi.”
“Huna kazi! Kivipi?” nilishindwa kumuelewa.

“Nimenyang’anywa gari.”
“Mungu wangu! Kwa tatizo gani?”
“Gari limekuwa halifikishi hesabu, siku nyingine haki ya Mungu mpaka narudi nyumbani sijapata abiria hata mmoja. Unafikiri mwenyewe atakuvumilia mpaka lini. Gari linataka matengenezo, linataka mafuta mi mwenyewe nataka kula.”
“Kwa hiyo?”

“Yaani kama nina gundu, toka ninyang’anywe gari sasa ni wiki.”
“Wiki! Siku zote ulikuwa ukienda wapi?” nilishtuka kusikia vile, baada ya kujua siku zote alizokuwa akiondoka asubuhi alikuwa na gari kumbe alikuwa na wiki nzima hana gari anafanya deiwaka.
“Kijiweni, na huko kila nikipewa deiwaka gari halipati abiria.”

“Mmh!” niliguna.
“Basi nimeona bora nirudi nyumbani nipumzike naweza kugongwa na gari kwa mawazo.”
“Pole mpenzi wangu.”
“Mmh! Hali ni mbaya unafikiri tutakula nini?”

“Tumuombe Mungu kila kitu kina mwanzo na mwisho wake.”
“Tumuombe Mungu vipi ikiwa kodi imekwisha na inatakiwa toka mwezi jana.”

“Mmh! Sasa tutafanyaje?”
“Sina jinsi, japo nakupenda nilikuwa na wazo moja wewe urudi kwenu na mimi nitajua nitaishi vipi kwa vile nyumbani siwezi kurudi.”
“Mume wangu kwa nini tufikie huko, kwa nini nisiende nyumbani kuomba msaada?”

“Tutaomba mpaka lini?”
“Kwani hali hii itakuwa ya kila siku?”
“Mi’ nafikiri we ungerudi kwenu, na mimi nihangaike nijuavyo. Nikirudi katika hali yangu ya kawaida tutaendelea na maisha yetu.”

“Hapana naomba jukumu hili niachie kwanza mimi, nikishindwa nitakwambia.”
Nilimbembeleza mume wangu, akanielewa. Sikutaka kupoteza muda, nilijifunga kitenge na kwenda nyumbani kumweleza mama na kumsikiliza atanisaidiaje. Njia nzima nilikuwa nikijiuliza, mama kweli atakubali kutulipia chumba kwa miezi sita zaidi ya laki tatu?

Wazo la kuambiwa nirudi nyumbani nililiogopa kwani hata kama tungelipiwa chumba bado tusingekuwa na fedha za kula. Nilijikuta nikichanganyikiwa kiasi cha kupitiliza nyumbani mpaka niliposhtuliwa na dada zangu waliojua nina safari zangu nyingine kumbe nilikuwa naenda palepale.

“Wee Mwai vipi, safari ya wapi? Maana unapita kama hutujui,” dada alinishtua katika lindi la mawazo nikiwaza hali yetu ya maisha ilivyobadilika ghafla na kutufanya tupoteze mwelekeo.
“Mungu wangu!” nilishtuka na kuufunika uso kwa mikono.

“Unashtuka nini nawe hukutaka kuja nyumbani?”
“Dada yangu wee acha tu, mbona mwaka huu nitakuwa kichaa.’’
”Kwa sababu gani?”
“Tutazungumza baadaye, mama yupo?”
“Yupo sebuleni anakula raha zake, si unajua mama yako anapenda raha kama paka wa Kiarabu,” dada alitania.

“Anakunywa?” niliuliza kutaka kujua kama mama anakunywa bia.
“Aache! Jioni hii wakwe zake wameshamletea yupo sebuleni kajaa tele kama pishi la mchele.”
Kabla sijaondoka dada alinishangaa kwani miguu ilikuwa imejaa vumbi, nywele zilikuwa timtimu.

Wakati mume wangu alipokuwa anarudi nilikuwa naosha vyombo kisha ndiyo niingie bafuni kuoga. Lakini aliyonieleza yalinichanganya, nilikumbuka kujifunga kitenge chini, juu nilikuwa na gauni la kulalia ambalo tangu niamke nilikuwa sijalivua.
“Wee Mwai!” dada aliniita kama kuna kitu kimemshtua.

“Vipi dada?”
“Mbona sikuelewi?”
“Kivipi dada?”
“Unajiona upo sawa?” nilijua ni kutokana na nilivyokuwa siku ile.
Nilijikuta nikishtuka na kujikagua, hali niliyokuwa nayo ilinishangaza. Lakini sikutaka kuonesha kushangaa kulingana na uzito wa tatizo lililokuwa kichwani mwangu.

“Aah! Dada wee acha tu,” nilimjibu huku nikielekea ndani kwani sikutaka maswali zaidi ya kuzungumza na mama ili nijue atanisaidia vipi.
“Ubishi wako! Ona unavyozeeka, unatufanya dada zako tuonekane kama wadogo zako.”

Sikutaka kumjibu, niliachana na dada ambaye alionekana alikuwa katika mkao wa mtoko. Kwa kweli maisha ya dada zangu sikuyafurahia hata kidogo. Baada ya dada zangu wawili kufiwa na waume zao pia mmoja kuachika katika mazingira ya utata, hakuna aliyekubali kuolewa tena, wote waliishi maisha ya kutumia miili yao kama vitega uchumi.

Katika vitu Mungu alivyotujalia watoto wote wa kike tulifuata umbile la mama. Mama yetu alikuwa na umbile la Kitutsi. Mweusi asilia pia ana shepu ya mvuto. Hilo ndilo lililowafanya wanaume wenye fedha zao kumiminika nyumbani kama kwenye kituo cha akina dada poa.

Japokuwa hali ile ilifanya maisha yetu yawe mazuri kidogo lakini ilishusha hadhi ya nyumba yetu kwa kutufanya wote tuonekane machangudoa. Aibu niliiona mimi peke yangu lakini mama na dada zangu waliiona ile hali ni ya kawaida.

Nilipoingia ndani nilimkuta mama amenyoosha miguu kwenye meza na pembeni yake kulikuwa na bia iliyokuwa imebakia robo kwenye chupa, kwenye glasi kulikuwa na bia nusu. Aliponiona naingia aliyaondoa macho kwenye runinga alipokuwa akiangalia taarab.

“Karibu mwanangu.”
“Ahsante mama yangu.”
“Upo sawa?” mama alinishtukia.
“Mmh! Ha..ha..pana.”
“Tatizo nini kiziwanda changu?”
“Mama mbona mikosi imezidi kuniandama.”

“Tatizo nini?” mama alisema huku akiteremsha miguu kwenye meza na kukaa vizuri kunisikiliza.
Kabla ya kuzungumza lolote, nilimuona akinishangaa kwa kuanza kuniangalia kwa kunipandisha na kunishusha.

Alituliza macho kwa muda usoni kwangu kisha alitikisa kichwa na kuchukua chupa ya bia iliyokuwa imebakia robo na kuijaza kwenye glasi kisha aliinywa yote na kuniangalia tena kama vile bia aliyokunywa ilimfanya anione vizuri.
“Mwaija mama,” mama aliniita akiwa kama ananishangaa.

“Abee mama,”
“Una tatizo gani mwanangu, maana kila kukicha la leo linazidi la jana.”
“Mama wee acha tu mwanao nakuwa chizi sasa hivi.”

“Tatizo nini?”
“Mama kama ulivyosema kila kukicha ya jana yanakuwa na afadhali kuliko ya leo, mume wangu hana kazi.”

“Etii!” mama alishtuka.
“Amenyang’anywa gari.”
“Tokea lini?”
“Wiki ya pili sasa.”
“Tatizo nini?”
“Siku hizi bundi ametua kwenye nyumba yetu, kazi imekuwa ngumu, hesabu ya tajiri imekuwa haifiki mwenyewe kaamua kuchukua gari lake.”

“Mlipokuwa na gari nanga ilipaa, sasa hivi hana gari itakuwaje?”
“Mama yote tisa kumi kodi ya nyumba huu mwezi wa pili sasa.”

“Kodi ya nyumba imefanya nini?”
“Tokea mwezi jana tulitakiwa kulipa lakini mpaka leo hii hatujalipa na hatujui tutalipa lini.”
“Kwani mumeo hana akiba hata kidogo?”
“Hata senti tano nyekundu hana.”

“Kwani ana mawazo gani?”
“Mama hana yoyote zaidi ya kutaka nirudi nyumbani.”
“Ili?”
“Ili ajipange kimaisha.”
“Kwa hiyo ukirudi nyumbani, anakuwa amekuacha au?”

“Hapana siyo kuniacha bali kuja kupumzika ili ajipange upya.”
“ Kwa hiyo kula yako ihamie kwangu?”
“Sasa mama kwa hiyo unataka nitafute pa kwenda?” kauli ya mama ilinichefua sana.
“Siyo pa kwenda, ila uamini mimi mama yako naona mbali, haya niliyaona mapema lakini ukanibishia.”

“Mama huu si wakati wa kubisha, nimefuata msaada.”
“Rudi nyumbani, hapa kwenu huwezi kufukuzwa.”
“Mama shida yangu si kurudi nyumbani.”
“Eeh! Shida gani?”

“Nilikuwa naomba utukopeshe fedha tulipe kodi, mume wangu akipata kazi atarudisha.”
“Hiyo kazi atapata lini?”
“Mungu atasaidia kwani naye anahangaika.”

“Mwanangu kwa ushauri wa mumeo ungekubaliana naye.”
“Mama, kwa nini tuendelee kujazana nyumbani?”

“Hivi katika ndugu zako ambao hawana wanaume nani mwenye shida?”
“Mama siyo shida, bali heshima.”

“Kifupi sina uwezo wa kifedha zaidi ya kuiunga mkono kauli ya mumeo kuwa urudi nyumbani ili ajipange. Kumbuka kuendelea kuwa karibu naye atazidi kuchanganyikiwa mtoto wa watu na kumfanya azidi kuongeza matundu ya mkanda wa suruali.”

“Kwa hiyo mama?”
“Rudi nyumbani.”
“Mamaaa,” sikukubaliana na mama.
“Unatakaje?”
“Kwa nini usitukopeshe tukalipe kodi tutakulipa mume wangu akipata kazi.”
“Hivi wewe na mumeo nani mwenye kauli ya mwisho?”

“Mume wangu.”
“Kama yeye amesema wewe urudi kwenu ameona mbali, hivyo basi rudi nyumbani kwenu ili kumpa nafasi mumeo kutafuta kwa utulivu. Kama utalazimisha utasababisha kijana wa watu aibe ili mpate chakula, mwisho wake atauawa au kufungwa.”

Nilijikuta nikiangua kilio ambacho niliamini lazima kitamshawishi mama kubadili uamuzi wake. Lakini mama aling’ang’ania msimamo wake wa mimi kurudi nyumbani. Kwa upande wa pili nilikubaliana na mama kwani hata kama tungelipa kodi bado chakula kingekuwa shida, hivyo ningezidi kumchanganya akili mume wangu.

Japokuwa sikupenda kurudi nyumbani, ilibidi nikubaliane na mama kwa shingo upande kwa kuamini aliyonieleza.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom