mtume wawatu
JF-Expert Member
- Oct 30, 2016
- 1,210
- 1,353
Nzuri sana hii
Asante Sana Kaka. Nitashiriki na kuzingatia ushauri wako mkuuHakika riwaya hii inapita riwaya zako zote ulizo Wahi kuandika kwa ubora,elimu,burudani. Umefanya utafititi wa kina imezungumzia migogoro mipya inayo tupata kwa sasa. Sikupaki Mafuta kwa mgongo wa chupa. Mwaka Kesho Naomba ushiriki tuzo za MABAT. lakini yapo machache ya kurekebisha ili watu wa MABAT wakupitishe.Utamuona Enock Maregesi atakusaidia. 2022 TUZO YA MABAT upande wa riwaya ni yako. Sitashiriki kwa Maana umenishinda hata kabla sijaweka riwaya yangu MABAT
Shusha vituKAZI YA MZUNGU 31
MTUNZI: DAVID NGOCHO SAMSON
0629077792
Dr Wu aliingia kwenye geti la wizara ya tafiti, Sayansi na teknolojia kwa mwendo wa fujo. Mwendo alioingia nao eneo hilo ulikuwa hatari. Hata hivyo, alihisi umuhimu wa kufika wizarani hapo ulihitaji mwendo zaidi ya huo aliotumia kufika hapo. Alishuka garini na kutembea mwendo wa nusu kimbia nusu tembea. Hakupoteza muda, aliingia kwenye lifti iliyompandisha juu ili kuingia kwenye afisi ya katibu mtendaji wa wizara hiyo muhimu kwa serikali ya China. Kwa muda sasa simu yake ilikuwa inaita lakini hakuipokea kutokana na ukweli kwamba alikuwa amezingatia zaidi kuendesha gari. Akiwa kwenye lift, akaisikia tena simu yake ikiita kwa bidii. Bila shaka mpigaji alikuwa na jambo muhimu. Dr Wu aliichomoa simu hiyo kutoka mfukoni na kuitazama. Jina kwenye skirini ya simu hiyo lilimtambulisha vema mpigaji. Alikuwa mkurugenzi wake wa CRC, Dr Futodo. Hakupokea. Tayari alikuwa keshafikia mlangoni mwa ofisi ile aliyokusudia kwenda. Kwa haraka aliyokuwa nayo, Dr Wu alizama ofisini kwa katibu mkuu bila kubisha hodi. Kitu cha kwanza kukiona ilikuwa ugeni uliokuwa umetamalaki ofisini humo. Akajipata anapatwa na mshituko mkubwa uliosimamisha mapigo yake ya moyo kwa sekunde kadhaa. Majamaa wawili kati ya wale waliokuwa kwenye kikao hapo awali kwenye ofisi ya mkurugenzi wa taasisi yake, Dr Futodo, wazungu wa Earth Vision 2050, walikuwa wamemakinika sana wakizungumza kwa ushawishi na katibu mkuu wa wizara hii ya tafiti, Sayansi na teknolojia. Sio ajabu kwamba hawakujua uwepo wake hapo mlangoni. Kuwaona watu hao mahali hapa, kuligonga kengele ya tahadhari kichwani mwa Dr Wu. Akili hiyo iliyogonga kichwani haikumpa muda Dr Wu kufikiria mara ya pili, la hasha! Dr Wu alichofanya ni kugeuka haraka sana na kutoka mle ndani bila kushitukiwa na watu wale.
Dr Wu sasa aliweza kubaini ni kwa kiwango gani wazungu wale walivyokuwa wamejipanga vya kutosha. Hawakuwa na mchezo dhidi ya kufikia lengo lao la kuitia ACVV mikononi mwao. Bila shaka ilikuwa wazi kwamba walikusudia kwa njia yoyote ile waitie formula mkononi mwao. Dr Wu alishuka tena kwa kutumia lift, akatafuta jina kwenye orodha ya majina kwenye simu yake, akampigia simu afisa mmoja waliyefahamiana vema. Afisa kutoka idara ya usalama wa taifa ya uchina, Ministry of State Security (MSS). Li Wenqing. Li na Dr Wu walioa sehemu moja, ikiwa ni Li aliyeoa dada wa mkewe Dr Wu. Wakati huo tayari alikuwa keshalifikia gari lake aina ya Harrier nyeusi na kulitekenya kwa funguo kisha kuliondosha hapo kwa mwendo ule ule aliokuja nao hapo awali.
Ajent Li alipopokea simu tu, Dr Wu alianza kutiririka maneno yake yaliyojaa hofu yake dhidi ya adui zake. Akiwa mbio, Dr Wu alishuhudia magari kadhaa nyuma yake yakija waruwaru ungedhani wapo kwenye mashindano ya magari. Dr Wu aliwatambua watu hao kuwa ni wale wazungu wa Earth Vision 2050. Hali hiyo ikamtia wasiwasi.
'Li, nina nyaraka muhimu sana ambazo hivi napoongea kuna wamarekani wanazifuatilia, hapa nilipo nawakimbia lakini naona wananifukuzia. Kama wakizitia nyaraka hizi mikononi mwao, usalama wa taifa letu utakuwa mashakani. Kama likitokea lolote kwangu, ongea na mkeo, mtaa wa Zanzibar kuna mapinduzi baada ya milipuko ya bomu, mkeo atakupa funguo,.' Dr Wu aliongea akiwa anahemea juu juu. Sentensi zake, hazingeeleweka kwa mtu mwingine, lakini Li Wenqing alijua Dr Wu anaongea kwa lugha ya kificho, kwa lengo la kuwapoteza maboya wale ambao huenda wangekuwa wanayanasa mazungumzo hayo.
'Uko wapi sasa?' Li Wenqing aliuliza huku akiliwasha moto gari na kuliingiza barabarani.
'Nakaribia Tiananmen square, kama upo ofisini utaona napita hapo nikifukiziwa na gari jeusi nyuma yangu.' Eneo la Tiananmen na makao makuu ya ministry of state security ni mwendo wa dakika chache tu. Hazikupita dakika mbili, ajenti Li akiwa anachekecha usukani wa gari lake aingie barabarani akashuhudia gari la Dr Wu na nyuma yake kweli gari mbili nyeusi aina ya Forrester yakimfukuzia. Ajenti Li hakutaka tena kupoteza muda, akaingia kwenye mtanange huo wa kushindana mbio. Sasa magari yale ya jamaa wa Earth Vision 2050 yalikuwa kati ya Dr Wu na agent Li.
Waliendelea kufukuzana katika barabara hiyo kuu inayoanzia Fuxing, ambako majengo ya wizara ya tafiti, sayansi na teknolojia yapo. Sasa walikuwa wanaenda nayo kwa mwendo mkali sana na hatarishi kwa watumiaji wengine wa barabara. Mara ajent Li akawashuhudia jamaa wa Earth Vision 2050, wakianza kuligonga gari la Dr Wu kiupande upande. Dr Wu akajitahidi kulimudu gari lake na kulirejesha katikati ya barabara mara kadhaa baada ya kusogezwa pembezoni mwa barabara. Hata hivyo, haikuchukua muda mrefu kabla hajakumbana na kishindo kingine nyuma yake.
'Usisahau maelekezo yangu tafadhali' Dr Wu akaongea kwenye simu halafu akaongezea;
'Wameshikilia familia yangu na….' hakufanikiwa kumaliza kauli, gari lake likagongwa tena, mara hii, halikusalia barabarani. Likaviringika mara kadhaa na kutoka nje kabisa ya barabara kisha likaanza kuwaka moto. Majamaa wa Earth Vision 2050 hawakusimama. Wakaendelea kama vile hapakutokea kitu.
Wakati agent Li alishangaa kuona jamaa yake amefanyiwa ile hujuma, akiwa amepaki gari pembeni, gari moja sawa na lile lililosababisha ajali lilishika break mbele yake, wakaruka majamaa wawili na kulifuata gari la Dr Wu. Wakati ajent anasogea ili kusaidiana na wale jamaa kufanya uokoaji, akawashuhudia jamaa wakirejea kwenye gari lao wakiwa na brief case ya Dr Wu. Katika kuonesha kuwa walijua yeye ni nani, au kwa ajili ya tahadhari, wale jamaa walilishambulia gari lake kwa risasi na kuondoa upepo kwenye matairi. Ajenti Li akawashuhudia jamaa wakitoweka mahali hapo kwa mwendo wa hatari. Agent Li hakuwa na ujanja. Hata hivyo, Sasa alianza kuona hatari aliyokuwemo Dr Wu.
Baada ya wazungu wale kuondoka, ajenti Li alilisogelea gari la Dr Wu, akafanikiwa kumvuta na kumtoa kwenye hatari zaidi ya kuungua na Moto ule. Hata hivyo, ile amemchomoa tu, wakasukumiwa mbali na mlipuko mkubwa wa gari hilo. Mlipuko huo, haukuwa wa kawaida. Zaidi ya mlipuko wenyewe wa gari, ni kama kulikuwa na mlipuko wa ziada wa bomu. Bila shaka jamaa walikusudia kumteketeza kabisa Dr Wu.
Agent Li alipopata fahamu baada ya kupumbazwa kwa muda na mlipuko ule, aliubeba uliowahi kuwa mwili wa Dr Wu na kuelekea eneo lenye usalama. Wasamaria wema walikuwa wanasogea kujaribu kutoa usaidizi. Mmoja wa raia wale ambao walikuwa kwenye mgahawa wa jirani na ilikotokea ajali, akajitolea gari lake kuwawahisha jamaa hospitalini. Wakampeleka kwenye hospital ya wajapani, Ito Yokado. Mtaa jirani wa Qianmen E.
Walipofika hospitalini hapo, madaktari hawakuwa na kazi. Dr Wu Han, alikuwa ng'ambo ya pili kutokea duniani. Baada ya uchunguzi wa maiti yake, kulionekana tobo la risasi. Washenzi wale waliipenyeza risasi kwenye moyo wa Dr Wu bila huruma. Kwao haikutosha kumnyang'anya ile formula. Walikusudia kumpoteza akiwa shahidi pekee ambaye angeeleza nani walikusudia kumnyang'anya ile formula. Earth Vision 2050, hawakuwa na mashaka tena na mpango wao. Wanasayansi wenzie Dr Wu, tayari walikuwa wamesaini mkataba na kupokea marupurupu manono. Sasa, huko ng'ambo ya pili, kumfikia ilikuwa muhali, ajent Li hakuwa na kitu Cha ziada Cha kuwafahamu wale wazungu Ni nani. Dr Wu alikufa akimwachia kitendawili kigumu Cha kutegua. Alibaki akitafakari kauli ya Dr Wu kuwa "Zanzibar Kuna mapinduzi baada ya milipuko ya bomu". Ulikuwa mtihani mgumu kweli kweli. Hata hivyo Agent Li, alibaki kuwa na wajibu wa kutekeleza, kushughulikia maandalizi ya msiba na pia akalazimika kutoa taarifa kwa familia ya Dr Wu.
***
Habari kwamba Dr Wu alikufa akijaribu kutetea taifa lake, tena habari kwamba familia yake ilikuwa mateka, ziliamsha amsha-amsha hatari jijini Beijing. Wananchi na wanaharakati Jijini humo waliitaka serikali kuhakikisha familia ya Dr Wu inarejeshwa. Maandamano makubwa yakashuhudiwa, ya kuishinikiza serikali kuu kuhusiana na familia ya Dr Wu na kutaka majibu ya nani waliomuua Dr Wu, mtu ambaye siku za karibuni alikuwa amebainisha ugunduzi wake wa chanjo dhidi ya gonjwa la Corona. Wachina walikuwa bado hawajasahau virus hao hatari walivyopata kuteketeza maisha ya ndugu zao katika Jimbo la Guangdong mnamo mwaka 2002. Kirusi wa wakati huo alipewa jina SARS COVID 1. Wengi Sasa walihesabu kuwa mwarobaini wa virus hao umepatikana. Kwa vyovyote vile, kulikuwa na hujuma inaendelea.
Hamasa hiyo ya wananchi, ikizingatiwa pia kwamba Earth Vision 2050, walikuwa wameitia briefcase ya Dr Wu mkononi mwao, hawakuona haja ya kuendelea kuishikilia familia ya Dr Wu. Kesho baada ya siku hiyo ya maandamano, familia ya Dr Wu ikaachiwa huru na kutelekezwa kwenye eneo maarufu wanakoonekana watu wa mataifa mbalimbali, mtaa wa San Li Tun. Hata hivyo, walikutwa hapo wakiwa wamefungwa kwa kudu pamoja. Waliporudishwa nyumbani, familia ya Dr Wu hawakujua kuwa baba wa familia yao alikuwa tayari keshaenda zake ng'ambo ya pili. Hivyo, kufika Kwao nyumbani na kukuta msiba wa baba wa familia kukaibua vilio na maombolezo makubwa. Familia hiyo, ikakumbwa na kilio, baba wa familia hangeonekana Tena akiwa hai. Mtafiti na mgunduzi wa tiba kubwa na muhimu nchini China alikuwa kahujumiwa uhai wake na watu wa Earth Vision 2050.
Mkewe Dr Wu, alionekana kuwa na wasiwasi sana. Hawa waliomuua mume wake walikusudia nini? Akakumbuka mume wake alimdokezea juu ya chanjo aliyokuwa amevumbua na jinsi ambavyo ilitokea kuvutia makampuni mbalimbali ya utafiti. Kuanzia kampuni maarufu la mmarekani Steve Curl, Scientific Reality Inc, na Sasa kampuni lingine la kimarekani la Earth Vision 2050. Kampuni hili la pili Dr Wu alimweleza kuwa alikuwa na mashaka nalo, kwa sababu, alihisi kuwa kampuni hili lilikuwa na nia ovu dhidi ya chanjo hiyo. Alipomuuliza kwa nini, Dr Wu alikuwa kamwambia;
'Ni kama wamekusudia kuitia mikononi mwao kwa udi na uvumba. Wanatangaza dau ambalo, linatia tamaa, ili mtu asifikirie mara mbili kutafakari ofa yao', hivyo ndivyo alivyopata kumjibu. Halafu akakumbuka Tena usiku wa siku hiyo, wakiwa wamelala usiku wa manane, na labda yeye ndio alilala, maana Dr Wu hakuonekana kabisa kama alipata usingizi, Dr akamwamsha. Alipoamka, Dr Wu alimweleza maneno haya;
'Mke wangu, nataka ujue kuwa nawapenda sana. Nakupenda sana mpenzi na sipati picha ikiwa nitapata shida halafu niwe mbali na nyinyi…' Dr alikuwa anaongea kama anayewaza. Aliyatamka maneno hayo huku akili yake ikiwa mbali sana hakuwa hapo kimwili, hivyo ndivyo ungetafakari ongea yake usiku ule. Sheng, aliliona hilo lakini akadhania zitakuwa ni stress za kazini zinamsumbua mumewe.. Hapo ndipo Sheng, mkewe Dr Wu akamkatisha kauli na kumwambia.
'Mume wangu mpenzi, unawaza sana baba watoto. Hebu acha akili yako ipumzike mpenzi. Umechoka na bado unalazimisha kufikiria vitu. Ona sasa, unaanza kuwaza mambo ambayo huhitaji kuifikirisha sana akili yako juu yake. Mimi na wanao, tunakupenda sana mpenzi. Lisikufikirishe sana hilo. Lala mpenzi, njoo tulale.'
'Asante mke wangu, kulala tunalala. Kuna kitu nataka nikushirikishe maana asubuhi nitawahi sana kutoka. Pale sebuleni, ile kalenda yetu, kuna tarehe nimezizungushia kwa kalamu, hizo namba ni muhimu sana. Ikitokea nimepata shida kabla chanjo kuzalishwa, hizo tarehe zitakuwa ni funguo ya kuokoa watu. Nahisi wale watu wa Earth Vision 2050 wanakusudia kuangamiza watu wetu kwa aina mpya ya virus ambavyo chanjo yake nimetengeneza. Na ikitokea limenipata baya, Ukipata nafasi, kuna hiyo simu yangu, kuna wimbo nimerekodi, nimeupa jina 'mpenzi dunia' usikilize. Utakupa tafakuri ya liwazo.' Sheng sasa aliona Dr Wu anabwabwaja mno. Unafahamu mazoea ni mabaya sana. Wanawake kwa wanaume hutengeneza mazoea fulani ambayo, hupelekea upuuzaji wa masuala ya msingi kwa kule kuzoeana na wenzi wao. Hivyo ndivyo ilivyoonekana kwa Sheng, hakuyazingatia sana maneno ya mumewe wakati alipokuwa anayaongea. Sasa wakati huu msiba ulipomfika, ndio akakumbuka haya masimulizi ya mumewe usiku ule kabla ya ajali na kuuawa.
Kumbukumbu hiyo, ikamkurupua Sheng mkewe Dr Wu. Akanyanyuka haraka na kuingia ndani chumbani. Juu ya meza jirani na kitanda, akaiona ile simu ya Dr Wu. Kawaida, Dr Wu alikuwa na simu ya mkononi kwa masuala ya kazini na halafu kuna simu hii ambayo mara nyingi alikuwa anarekodi mambo ya kifamilia, haikuwa na laini, bali ilikuwa na memory card yenye ujazo mkubwa, na ndanimwe alijaza video za watoto, mke na yeye mwenyewe. Humo pia alirekodi nyimbo walizoimba wanawe, mkewe au yeye mwenyewe. Simu hii, kwake ilikuwa kama kirekoda cha matukio ya familia, kumbukumbu ya hatua za ukuaji wa wanawe kwa nyakati za furaha na huzuni za familia yake.
Sheng alipoichukua simu hiyo, alifungua bila shida, maana haikuhitaji nywila, ilikuwa huru kutumiwa na mwanafamilia yeyote yule. Akili yake ilitaka tu kupata hicho ambacho mume wake alikuwa amesema kingempa liwazo wakati huu wa majonzi. Ilikuwa kama Dr Wu alitabiri kifo chake. Aliperuzi kwenye audio clips, zilikuwepo nyingi mno, hakuwa na muda wa kuzisikiliza zote. Akaingia kwenye mraba wa kutafutia mafaili, hapo akaandika 'mpenzi dunia'. Ikajitokeza hiyo clip. Sheng akapachika earphones masikioni na kuicheza hiyo audio clip.
'Mambo mpenzi? Kama umekuja hapa kwenye hii clip, basi nitakuwa nimepatwa na jambo, navyokujua wewe, usingekuja hapa kama si kumbukumbu ya kile nilichokuambia. Nakujua sana mpenzi. Basi nikupe pole kwa wakati mgumu unaopitia sasa. Pole mpenzi. Wanangu pia wape pole kwa niaba yangu. Nimekuita hapa kwa sababu hata kama sipo hapo, bado tunaweza kufanya jambo kubwa na la msingi. Tunaweza hatimaye kuokoa kizazi chetu kisiangamizwe na maharamia kutoka nje ya taifa letu. Kunazo njama nimebaini. Taasisi yangu CRC imeingiliwa na mamluki. Wapo tayari kuuza nchi kwa faida zao binafsi. Na mimi sitaishi kuona hilo likitokea. Na nikifa, basi nitakuwa nimekufa mimi, na labda watu wengine pia wakafa endapo utachelewa sana kuupata huu ujumbe. Lakini kama utaupata, hakikisha unamwambia mume wa dada yako, agent Li. Zile namba za kalenda, ni funguo dhidi ya virus vinavyokusudiwa kuachiliwa ili viangamize robo tatu ya wakaazi wa dunia. Namba hizo, zinafungua briefcase ambayo ndani yake kuna formula ya uzalishaji chanjo dhidi ya virus hivyo. Mpenzi, kama nikifa, nakuomba uwe huru. Wewe ni mwanamke mrembo ambaye hastahili kuishi kama mjane. Usiniomboleze mno, maana kufa kwangu ni kupona wengi. Kusudi langu litakuwa limekamilishwa. Nakupenda mpenzi, nakupenda dunia, mpenzi dunia.' Sauti ya marehemu Dr Wu ikahitimisha ujumbe. Sauti ya mumewe hakika ilimtia simanzi, vipi angenyamaza? Sheng alikuwa analia mlango wa chumbani kwake ulipogongwa. Ilikuwa sauti ya dada yake, mke wa agent Li Wenqing. Ujio wa dadake ukamuongezea kilio maradufu.
***
Baada ya kuhakikisha kuwa briefcase yenye formula ipo mikononi mwao, na kwamba Dr Wu sasa hangekuwa kikwazo, watu wa Earth Vision 2050, walielekea kwenye ofisi zao za muda zilizokuwa eneo jirani kabisa na makao makuu ya MSS. Walilichagua eneo hilo, kwa sababu pamoja na mengine, walikuwa katika ujasusi dhidi ya idara hiyo muhimu kwa China, wakiwa wameweza kupenyeza mtu wao ndani ya idara hiyo. Ni kusema kwamba watu Hawa wa Earth Vision 2050 walikuwa wanaweza kupata taarifa muhimu kutoka ndani idara hiyo nyeti.
Kuipata briefcase, ilikuwa hatua muhimu katika harakati zao. Walikuwa na hakika kuwa sasa watafanikisha misheni yao.
Earth Vision 2050 kama lilivyo jina lao, lilikuwa kampuni miongoni mwa makampuni washirika na lile kampuni lingine la ENTRY. Hawa walikuwa na agenda ya Siri. Kampuni hili likiwa na agenda moja kubwa, kufikia 2050, duniani kuwe na idadi ya watu wasiozidi billion 1.5. Sawa na Entry, Earth Vision walikuwa na lengo moja tu. Kuiokoa dunia dhidi ya kile walichodai kuangamia na kupoteza kabisa jamii ya binadamu. Kwa kile walichosema, ni ongezeko kubwa kabisa la binadamu ambalo lingeifanya dunia isiwe salama tena kwa viumbe kuishi kwa utengamano. Walikadiria kuwa Kama ongezeko la watu lingeendelea kuachiliwa kuongezeka kihobela hobela, Basi Kama vile mijusi mikubwa ya zamani (Dinosaurs) ilivyotoweka, ndivyo ingetokea kwa binadamu, matokeo ambayo waliona yanatokea muda si mrefu. Mambo kadhaa yalikuwa Kwao Ni ishara iliyowataka wachukue tahadhari kuzuia kutoweka kwa kizazi Cha binadamu na viumbe wengine. Mioto iliyokuwa inajitokeza kwenye misitu mikubwa ya Amazon huko America, mingine huko Australia na kwingineko duniani, mioto iliyodumu na kushindwa kudhibitiwa na binadamu, kwao ilikuwa ni ishara. Ishara kwamba dunia inaelekea kubaya. Matokeo yake waliyahusianisha na wingi wa binadamu. Suluhu waliyoona, ni kupunguza idadi ya wanadamu duniani.
Katika hatua za awali, walihamasisha na kuanzisha program za uzazi wa mpango. Lakini walibaini kuwa program hizo hazikufua dafu hasa kwa mataifa yanayoendelea huko Africa, Asia na America ya kusini. Ni kweli kwamba kwa kutumia chanjo mbalimbali za magonjwa mbalimbali, walimudu kupunguza kasi ya uzaanaji wa binadamu. Lakini hata hivyo, idadi ya binadamu ilizidi kuongezeka kwa spidi kubwa. Earth Vision 2050 walikadiria kuwa dunia ingefikisha idadi ya watu takribani billion tisa hadi kumi kufikia mwaka 2050. Kwa idadi hiyo ya watu, Earth Vision 2050 waliona dunia ikiangamia. Uchafuzi wa hewa, maji na mazingira ungeichakaza dunia. Magonjwa ya milipuko yasingepata wa kuyasimamisha. Mvua za tindikali, magonjwa ya mfumo wa hewa, mioto kwenye misitu mikubwa inayotegemewa kuzalisha vyanzo vya maji laini, ukame, njaa, n.k. Hivyo ni vitu vilivyotarajiwa kujitokeza mapema hata kabla ya 2050. Earth Vision 2050, waliona wana sababu ya kufanya jambo. Waliona dunia inastahili kuwepo na wanadamu pia wanastahili kuwepo. Hata hivyo, ilihitaji kufanya jambo ambalo si kila mtu angeliafiki. Kuuawa watu ili kuponya watu. Wasingeeleweka, hivyo, wao na washirika wenzao, waliamua kuyafanya haya kimya kimya. Jamii yao ikawa ni jamii ya siri, ikiratibu mambo yao kwa siri.
China pekee ilikuwa na idadi kubwa kuliko idadi yote ambayo kwa makadirio yao, ilistahiki kuwa idadi ya wanadamu wote duniani. China ilikuwa na idadi isiyopungua watu billion moja na nusu, ikifuatiwa na India. Baada ya uzazi wa mpango kushindwa kudhibiti ongezeko la watu duniani, Earth Vision 2050 na washirika wao, wakaamua kutengeneza magonjwa kadha wa kadha lakini usambaaji wake na uangamizaji wake haukuwa kwa ufanisi waliotaka. Sasa walitengeneza kirusi ambacho uambukizaji wake ulikuwa rahisi zaidi. Kwa Vitone vya kohoo, mate, chafya na kamasi, kirusi hicho kingeenea haraka sana. Na kwa uhakika zaidi, kifo kutokana na kirusi hicho, hakisubiri muda mrefu sana hasa kilipompata mtu mwenye kinga hafifu ya mwili. Hatua ambayo walikwishairahisisha hapo awali. Chanjo za awali, zilizokwisha kutolewa zikilenga kukinga magonjwa kadha wa kadha, waliziwekea pia udhaifu. Kusambaratisha uimara wa kinga ya mwili, na kuna baadhi ya visa viliripotiwa vya baadhi ya chanjo kusababisha badiliko la kijenetiki na DNA kwa wahanga.
Kinga dhidi ya virus vipya walivyokuwa wameunda, sasa ilikuwa mkononi mwao. Earth Vision 2050 wakajua mpango wao mapema ungeingia kwenye hatua muhimu. Lakini Earth Vision 2050 wakiwa bado hawajafanya kitu, jimboni Wuhan, jimbo ambalo lipo katikati ya nchi ya China, ulitokea mlipuko wa gonjwa la Corona, safari hii virus hao wakapewa jina SARS Covid 2. Gonjwa ambalo Dr Wu na jopo lake walikuwa wamefanikisha kutengeneza chanjo dhidi yake. Chanjo ambayo, wanasayansi hao walianza kuitafuta kufuatia mlipuko wa awali wa Kirusi aina hiyo kilichopewa jina, SARS covid 1, kikiripotiwa kuibukia huko Guangdong mapema mwaka 2002. Chanzo chake kilisemekana kuwa ni nyoka au popo. Chanjo ya Dr Wu, ilisemekana kuwa ni chanjo ambayo pia ingetumika kama tiba. Chanjo hiyo sasa ikiwa mkononi mwao, Earth Vision 2050 walipata kiburi cha kuachia virus vya SARS covid 2. Lakini kabla ya kuviachia virus hao, mwishoni mwa mwaka 2019, Virus hao wakaenea haraka sana kutokea jimboni Wuhan. Earth Vision 2050, wakashangaa sana maana hawakuwa wahusika. Haikujulikana nani kakiachia kirus hicho kabla ya wao. Hatari yake ikawa bayana kwani wao pia hawakujiandaa kwa mlipuko wa gonjwa hilo. Hata hivyo, hawakuwa na hofu sana. Waliamini kuwa na formula ya ACVV ilikuwa kinga yao madhubuti.
Itaendelea ......
View attachment 1701741
Asante Sana Sana sanaaaaCheki mwendelezo, nshaweka.