M.M. Mwanakijiji
KAMA kuna wakati nimetamani kunyofoa nywele zangu kwa hasira na kushangazwa ni wakati kama huu. Hakuna watu ambao wamenishangaza juu ya misimamo yao kuhusu maslahi ya taifa kama hawa ndugu zetu masheikh na maaskofu.
Kuna kitu hakiko sawa katika kundi hili na kuna wakati mtu ajitokeze na kuwaambia ukweli. Nadhani wanatumia majoho na kanzu zao za ibada kuanza kulichanganya taifa na kutugawanya wananchi kwa misingi ya kidini huku wao wenyewe wakijiaminisha kuwa wanafanya mapenzi ya Mungu. Nisikizeni enzi maaskofu na masheikh!
Sasa hivi kuna mgongano wa wazi kati ya viongozi hawa wa dini huku kundi moja likionekana kuwa kali dhidi ya serikali na kundi jingine likionekana kutafuta udhuru na kuitetea serikali.
Yote mawili yanajaribu kuaminisha watu kuwa yanafanya hivyo kwa masilahi ya taifa au masilahi ya watu wa kundi lao. Lakini kinachonishangaza zaidi ni kuwa mgongano huu wa viongozi wa dini haumsaidii Mtanzania wa kawaida bali unawaimarisha watawala madarakani; kwani wanajua kuwa nguvu ya kuwakemea haiko katika umoja.
Niliandika makala mwaka 2009 mwezi Oktoba nikielezea kile nilichokiita kuwa ni uenzetu huu yaani kama nilivyofafanua kuwa ni hisia ya kuona mtu mnayefanana kwa namna fulani anaonewa, kunyanyaswa au kulengwa na wengine kwa sababu ya vitu mnavyofanana na si sababu halisi. Nilielezea kwa kirefu katika makala ile kuwa mojawapo ya mambo ya hatari yanayotokea katika Tanzania ni kuwa tunauangalia ufisadi, uongozi na vitendo vya kukiuka maadili ya uongozi kwa rangi ya uenzetu.
Nakumbuka nilihoji (kama masheikh walivyohoji hivi majuzi) kuwa kuna mambo ambayo ni ya kifisadi yalifanyika chini ya utawala wa Rais Mkapa (Mkatoliki) ambayo yamelisababishia taifa hasara kubwa na aibu ya kutosha tu.
Nikauliza kuwa: Hakuna kiongozi yeyote wa Kikatoliki aliyekuwa na ujasiri wa kupiga kelele na kutaka Mkapa arudishe mali hizo za Watanzania alizojipatia kinyemela kinyume na Sheria ya Maadili ya Viongozi ya mwaka 1998 (ambayo yeye mwenyewe aliisaini).
Na hata leo hii ambapo serikali imekiri kuwa Mkapa alijipatia vitu hivyo kinyemela na kuamua kuvirudisha serikalini na kuwabambikizia Watanzania gharama ya kulipa madeni ya Kiwira hakuna kiongozi yeyote wa Kanisa aliyemtaka Mkapa kuwaomba radhi Watanzania na kutengeneza alichoharibu (reparation)?
Nisikilizeni enyi masheikh na maaskofu!
Na nikasema kuwa: Lakini leo hii (maaskofu) wamepata ujasiri mkubwa wa kusema ukweli mbele ya wenye madaraka (speaking truth to power) hasa pale wanayemsemea ni Mwislamu! Hapa, mtu mwingine anaona kuwa kama wangekuwa na ujasiri huo wa kukemea uovu mbele ya Mkapa labda mengine yasingefika huku. Kauli yangu hiyo imerudiwa hivi juzi na uongozi wa Kiislamu kwenye tamko lao la Karimjee. Ukweli ni kuwa uongozi wa Uislamu una hoja katika hilo.
Ni kweli wanahoja kwa sababu wakati leo hii kina Kardinali Pengo wanashangazwa na wananchi kuuawa mikononi mwa vyombo vya dola wengine tunauliza mbona walikufa watu Mwembechai na Pemba mikononi mwa polisi na hakuna maaskofu waliokuja juu?
Je, yawezekana ni kweli kuwa hawakuweza kufanya hivyo kwa sababu serikali ilikuwa inaongozwa na Rais Mkristu mwenzao? Hii hoja inaweza kuwa na nguvu zaidi kwa sababu miaka zaidi ya mitano tangu Mkapa atoke madarakani uongozi wa Wakristu nchini bado hawajathubutu kunyoshea mkono utawala wake kuwa ulichochea ufisadi huku sote tunajua kuwa wizi wa EPA, Meremeta na uvurugaji wa Katiba ulifanyika chini ya utawala wa Mkapa?
Sasa leo maaskofu wanaposimama na kuinyoshea vidole serikali ya Kikwete (Mwislamu) kwanini baadhi ya Waislamu wasione kuwa linatokea kwa sababu za tofauti ya kidini? Nisikizeni enyi maaskofu!
Ili maaskofu wapate mahali pa kusimamia wanapoikosoa serikali ya Kikwete ni lazima kwanza waombe msamaha kwa ukimya wao wakati Watanzania wameuawa Pemba na Mwembechai; si kwa sababu Waislamu waliuawa bali kwa sababu wananchi wameuawa.
Msimamo huo ungetakiwa uwe hivyo hata kama waliouawa wangekuwa ni Wapagani! Kwa kadiri maaskofu hawatoi tamko la kuchukua msimamo wa ufisadi na kutaja kwa majina utawala wa Mkapa, hawana ujasiri wa kumkemea Kikwete; si kwamba hawana hoja au hawana sababu lakini bila ya kusahihisha kosa lao la awali, Waislamu ni lazima na wana haki ya kushuku sababu ya maaskofu kufanya hivyo.
Lakini katika makala ile ile niliandika kitu kingine ambacho nacho kinatokea tena sasa hivi. Nisikilizeni enyi masheikh!
Niliandika hivi: Upande wa pili tunauona leo hii mahusiano kati ya baadhi ya makundi ya Waislamu na utawala wa Rais Kikwete ambaye naye ni Mwislamu. Licha ya madudu ambayo yanafanywa mbele yetu na mengine yenye kuwaathiri Waislamu bado hakujatokea kiongozi au uongozi wa Waislamu ambao wamethubutu kumuambia Kikwete na serikali yake maneno yenye ukweli.
Jambo hili nililiandika 2009 na sasa mwaka 2011 bado linasimama kama ushahidi wa usahihi wake. Hakuna kiongozi wa Kiislamu au chombo cha Waislamu ambao wamethubutu kunyoshea kidole serikali ya Kikwete kwenye masuala ya kitaifa.
Nilifafanua hili kwa sababu naam, wamekuwepo viongozi wa Kiislamu ambao wameilalamikia serikali kwenye masuala yenye kuwahusu Waislamu na tumeliona hili tena siku ya Jumamosi ambapo hoja zao za utetezi zinahusu kile wanachokiita kuwa ni masilahi ya Waislamu. Kama mtu amefuatilia mjadala wao na tamko walilolitoa ni wazi kuwa wamekerwa zaidi na maaskofu waliozungumzia suala la mauaji ya wananchi Arusha si kwa sababu maaskofu wamesema kitu kibaya bali zaidi kwa sababu maaskofu hawakuonyesha kujali hivyo wakati Waislamu walivyouawa huko nyuma. Kwao suala hili ni suala la kidini zaidi.
Niliandika hivi kwa kuhoji katika makala ile kama unabii wa kule tulikokuwa tunaelekea na hatimaye sasa tumefika: Hapa sizungumzii katika masuala yenye kuwagusa Waislamu tu (kama Kadhi, OIC, Hija n.k) bali nazungumzia yale ambayo yanawagusa wao pia kama Watanzania na wananchi. Masuala ya nishati, madini, nafasi za ajira n.k
Leo tunashuhudia mabilioni ya fedha zetu yanatumika kama hayana mwenyewe wakati watoto wetu bado wanahangaika na majengo mabovu ya shule, huduma na miundombinu mibovu katika maeneo mbalimbali licha ya mafanikio ya hapa na pale.
Masuala ya Richmond, Dowans, Loliondo n.k ambayo yanawahusisha baadhi ya watu wenye kufungamana na nchi za Kiislamu hakujavutia hasira ya Waislamu wa Tanzania. Kwanini? Kwa sababu ni wenzao? Kwamba kwa vile watu hawa wanajulikana kuwa ni Waislamu au wanatoka nchi za Kiislamu basi wasipingwe sana kwani wote hawa ni sehemu ya umma wa Waislamu?
Matokeo yake ni kuwa uongozi wa Waislamu Jumamosi hawajatoa tamko lolote kuhusu malipo ya Dowans kwa sabababu wanazozijua wao. Shura ya Maimamu hawajasimama kuhoji uhalali wa wananchi kuuawa huko Mbarali na Arusha kwa sababu mbona huko nyuma wananchi wengine walikufa mikononi mwa serikali?
Marafiki zangu kama kina Prof. Njozi (aliyeandika kitabu cha Mwembechai) mbona hajatoa tamko lolote la kuonyesha kukerwa na mauaji haya? Yawezekana uongozi wa Waislamu hawataki kuonekana na wenyewe wamesimama dhidi ya Rais Mwislamu mwenzao?
Nisikizeni enyi maaskofu na masheikh!
Tanzania ni Tanzania na ni kubwa kuliko makundi yenu ya kidini. Watanzania ni Watanzania zaidi ya Wachagga, Wandengereko, Wamatumbi na Wanyiha! Utanzania wetu uko juu zaidi kuliko dini zetu.
Wale ambao wanataka kutugawa kwa sababu ya dini zetu wanafanya makosa ambayo gharama yake ni kuua Utanzania wetu.
Tunataka viongozi wa kidini ambao wanaposimama kutetea haki basi watetee haki bila kujali anayedhulumiwa ni nani! Hatutaki viongozi wa kidini ambao wanauliza kwanza ni dini gani badala ya kusimama na kupinga dhulma.
Jumatatu hii iliyopita huko Marekani wameadhimisha siku ya mwanaharakati za haki za kiraia na za kibinadamu Mchng. Martin Luther King Jr. Mchg. MLKJr. alitambua kuwa kutetea haki za watu weusi nchini mle haikuwa kwa sababu ya Ukristo wake kwani wengi walikuwa si Wakristu.
Hata Malcom X baadaye alikuja kuelewa kuwa ni haki za watu weusi wote zilizokuwa zinadhulumiwa. Uovu hauna dini na unatakiwa kupingwa na wenye dini na wasio na dini.
Nisikilizeni enyi masheikh na maaskofu; pataneni dhidi ya uovu ili muweze kuukabili. Msipopatana tutawaacha kwenye mataa na kama nilivyowahi kusema huko nyuma mtakuwa hamna mpango (you will become irrelevant)! Kwani wananchi watawashtukia kuwa na nyie mnaongozwa na majoho na kanzu zenu na hivyo Watanzania wasiwategemee kuwa ni watetezi wao.
Kwani hata hao maaskofu ambao leo hii wanaonyesha kuwa wanakerwa mbona hakuna hata aliyesimama kuandamana kupinga vitendo hivi vya kifisadi na dhuluma? Ni lini tutawaona walioshtushwa kina Pengo na Laizer wakisimama na kuongoza maandamano ya kuipinga serikali au uongozi wa dhulma? Je, Masheikh hawataweza kusimama dhidi ya ufisadi hata kama aneyehusishwa ni mtu wa msikiti wao? Au yanakuwa ni maslahi hadi pale yanpogusa maslahi ya Waislamu tu?
Ndugu zangu, kila zama zina mashujaa wake na kila shujaa ana ujumbe wake. Hizi ni zama zetu na ni katika zama hizi tutangeneza mashujaa wetu sisi wenyewe au historia itawanyanyua kati yetu. Haijalishi kama mashujaa hao watakuwa ni Wakristu, Waislamu, wasioamini, wenye kuamini kijadi au vinginevyo.
Hawa maaskofu na masheikh ambao wanafikiri wanaukiritimba wa mbinguni nina ujumbe mmoja kwao; sikilizeni enyi maaskofu na masheikh kwani nanyi zama zenu zinapita na Watanzania watasimama hata kama ni peke yao; kama watawala wetu walioshindwa nanyi msipoangalia mtaingia katika shimo la kusahauliwa kwa kushindwa kuukemea uovu na kumaanisha hivyo.
Ujumbe wangu uko wazi. Pataneni dhidi ya dhuluma na uovu kwani ni katika hilo tu mtahukumiwa. Kwani kama alivyosema Luther dhuluma mahali popote, ni dhuluma mahali pote.
Nisikilizeni enyi masheikh na maaskofu!
Source: Tanzania Daima
Tar. 19 January 2011,
By M.M. Mwanakijiji