Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Njombe kupitia Chama cha Ukombozi wa Umma (CHAUMMA), Sigrada Mligo, ametoa wito kwa taasisi zote za Serikali na umma mkoani Njombe kushirikiana naye ili kuharakisha maendeleo kwa wananchi.
Akizungumza mara baada ya kurejea mkoani humo, Sigrada amewashukuru Wananchi kwa ushirikiano wao na kusisitiza kuwa ataendelea kufikisha Bungeni kero na changamoto ambazo kwa miaka mingi zimechelewesha utekelezaji wa miradi muhimu ya maendeleo.
Amesema kuwa kama Mbunge, lengo lake ni kufanya kazi kwa umoja na wadau wote wa serikali ili kuhakikisha Njombe inasonga mbele. “Nitume salamu kwa taasisi zote za serikali kwamba mimi ni Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, hivyo tushirikiane kuijenga Njombe yetu,” amesema.
Pia ameeleza kuwa katika hotuba yake Bungeni, Rais Samia Suluhu Hassan aliahidi kuendelea kutekeleza miradi inayolalamikiwa na wananchi nchini, ikiwemo ile ya muda mrefu mkoani Njombe.
Ameitaja barabara ya Njombe–Ludewa, ambayo ujenzi wake umekuwa ukisuasua kwa miaka mingi, na kuahidi kuwa ataifuatilia kwa karibu ili kuhakikisha inakamilika na kuwanufaisha wakazi wa Njombe.