Serikali yanyonga magazeti binafsi

Halisi

JF-Expert Member
Jan 16, 2007
2,802
613
Serikali yanyonga magazeti binafsi

lC.gif
Mwandishi Wetu​
Juni 23, 2010
rC.jpg

SERIKALI imeamua kutoa ruzuku kwa vyombo vyake vya habari kupitia matangazo ya bajeti za wizara mbalimbali ambazo zimekuwa zikisomwa bungeni, imefahamika.
Hadi sasa, kiasi cha wiki mbili baada ya kusomwa kwa Bajeti ya Serikali, hakuna magazeti yenye majina na mtandao mpana wa usambazaji nchini, ukiacha Daily News na Habari Leo, yote ya Serikali, gazeti linalomilikiwa na chama tawala, Uhuru, na mengineyo yanayoendeshwa na maswahiba wa wanasiasa, ambayo yamepewa matangazo hayo ya bajeti.
Utaratibu huu mpya unatii maelekezo ya Ikulu kwa maofisa wa habari wa wizara na idara ambayo watendaji wa magazeti binafsi wanayaona kuwa yenye kulenga kubana uhuru wa vyombo hivyo kimapato na kiutendaji.
Baadhi ya maofisa habari katika wizara na idara za Serikali wameiambia Raia Mwema kwamba utaratibu huu mpya umekuwa ukisukumwa na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais iliyo chini ya Salva Rweyemamu.
Chini ya utaratibu huu, magazeti yote yanayoonekana kuikosoa Serikali mara kwa mara yamelengwa, nayo ni pamoja na Mwananchi, Tanzania Daima, Mwana Halisi, na Raia Mwema, kwa kutaja machache.
Kwa kawaida, na hasa kwa mwaka huu ambao shughuli za Bunge zinagongana mara kwa mara na michuano ya Soka ya Kombe la Dunia, inayoendelea Afrika Kusini, wasomaji wengi wangependa kusoma hotuba za bajeti kupitia magazetini jambo ambalo sasa linashindikana kutokana na kwamba magazeti yanayopendelewa na Serikali hayana mtandao mpana kiasi hicho.
Ni jambo linalofahamika ya kuwa magazeti ya binafsi nchini ndiyo yana usomaji mkubwa na yanasambaza nakala nyingi yakilinganishwa na kundi la magazeti ambayo yanamilikiwa na Serikali na chama tawala pamoja na yale ya maswahiba wa vigogo.
Utaratibu wa kutumia matangazo ya serikali na mashirika yake kama silaha ya kisiasa hutumika mara nyingi katika nchi za Afrika kama njia ya kuviadhibu vyombo vya habari vinavyoikosoa serikali na kuvizawadia vile vinavyonyenyekea mbele ya watawala. Mhariri mmoja mwandamizi alipoulizwa na gazeti hili kuhusu hatua hiyo ya Serikali alisema kwamba hiyo ni dalili ya utashi wa kuyanyonga magazeti yasiyo chini ya CCM na serikali yake.
“Aidha hii ni hatua ya kutoa ruzuku kwa magazeti ya CCM na serikali na kusaidia kuendesha kampeni za chama hicho tawala” aliongeza mhariri huyo ambaye hakutaka jina lake litajwe. “Kutoa matangazo kwa magazeti ya CCM na serikali na kuyabagua magazeti binafsi ni kuyasaidia ya kwanza na kuyauumiza haya ya pili, na pia ni njia moja ya kuvuruga Uchaguzi Mkuu kwa njia ya mlango wa nyuma kwani njia moja ya kutoa msaada kwa chama cha siasa ni kukisaidia kuimarisha vyombo vyake vya propaganda. Sasa hawa mawaziri wanachota fedha serikalini na kuwapa CCM kupitia magazeti yake. Sasa hapo uchaguzi huru na wa haki utatoka wapi? ” aliuliza mhariri huyo.
Salvatory Rweyemamu ambaye anadawa kuwa ndiye aliyetoa maelekezo kwa watumishi husika wa wizara kutokutoa matangazo ya hotuba za bajeti mwenyewe aliwahi kuwa mhanga wa maelekezo kama hayo wakati alipokuwa Mhariri Mtendaji wa magazeti ya Habari Corporation na serikali ya awamu ya tatu, chini ya Benjamin Mkapa ikawa inayatenga magazeti hayo kwa kuyanyima matangazo ambayo yalikuwa yakitolewa kwa magazeti mengine, hata madogo, yakilinganishwa na yale ya Habari.
Kwa kawaida inatakiwa matangazo yatolewe kwa kuangalia wingi wa nakala za magazeti zinazouzwa na ‘ufiko’ (reach) wa gazeti husika. Kwa mujibu wa wafuatiliaji wa masuala haya magazeti ya CCM na serikali yake yanachapa nakala chache yakilinganishwa na magazeti kama Mwananchi, Tanzania, Daima, Nipashe na Raia Mwema.
Magazeti yaliyopata matangazo ya hotuba ya Bajeti ya Serikali iliyosomwa na Waziri wa Fedha, Mustafa Mkulo ni mawili tu, Daily News na Uhuru wakati hotuba ya Waziri wa Nchi, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, Hawa Ghasia ilitolewa na gazeti la Habari Leo.
Aidha, hotuba ya Waziri Mkuu, Mizengo Peter Pinda ilitolewa na Daily News na Uhuru. Uhuru iliongezewa pia hotuba ya maelezo ya kiutendaji ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Celina Kombani.
Rweyemamu alipoulizwa kuhusu kurugenzi yake kuwa kikwazo cha magazeti yasiyokuwa ya chama na Serikali kupata matangazo ya hotuba hizo alikataa katakata.
Alisema kwamba kurugenzi yake haihusiki na maamuzi yoyote yanayofanywa na wizara namna kutangaza hotuba zake za bajeti katika magazeti.
“Mimi ni msemaji wa Ikulu, si wa wizara, sihusiki na maamuzi yanayofanywa na wizara,” alisema.
“Lakini si nyinyi wenyewe mlioripoti ya kuwa wizara zimeamua kupunguza matumizi yake? aliuliza.
“Mimi sielewi bwana, lakini nyinyi (Raia Mwema) si mlipata hotuba ya Wizara ya Kilimo? aliuliza akiwa amesahau kwamba Raia Mwema ilichapisha hotuba hiyo mwaka jana, na si mwaka huu, na pia wakati akizungumza wizara ya Kilimo ilikuwa bado kuwasilisha hotuba yake katika kikao cha Bunge kinachoendelea hivi sasa.
Rweyemamu alisema anashangazwa na uvumi ulioenea kwamba yeye ndiye aliyetoa maelekezo ya magazeti binafsi kunyimwa matangazo ya Serikali.
“Mimi nitoe maelekezo hayo wizarani kama nani na mimi shughuli zangu ni za Ikulu?” alisema. “Hivi mmesahau tulipokuwa Rai (gazeti la Habari Corporation ambako alikuwa mmoja wa wakurugenzi wake) jinsi tulivyokuwa tunakosa matangazo ya Serikali?”
Kuhusu yeye kukutana na maofisa wa habari wa wizara, msemaji huyo wa Ikulu pia alikana kukutana na maofisa hao kupitisha uamuzi wa kuyanyima matangazo magazeti binafsi.
Hata hivyo, alikubali kwamba kurugenzi yake hufanya vikao na maofisa habari wa wizara mara kwa mara.
Alisema ya kuwa vikao hivyo ambavyo hufanyika kila Alhamisi huwa chini ya ofisa wake, na si yeye na kwamba yeye huingia kama msikilizaji.


Serikali yanyonga magazeti binafsi
hs3.gif
 
Maoni yangu ni kwamba naunga mkono uamuzi wa serikali kutumia magazeti yake lakini siungi mkono serikali kutumi amagazeti ya chama (CCM) haya ya Uhuru na Mzalendo. Najua kabisa wanajipa Ruzuku ya uchaguzi jambo ambalo ni uchafu ktk nchi hii tunayoiita ya vyama vingi.

Kama wameamua kutumia magazeti ya chama basi hata mengine kuna haki ya kulalamika, lakini kama wataumia ya serikali tu, hakuna haki ya kulalamika na nimekuwa nikitegemea maamuzi kama hayo hata ktk mambo mengine. Mfano kwa nini afisa mkuu wa serikali asafiri kwenda Mwanza kwa pesa ya serikali akitumia kampuni kama Precission Air ... na kuacha Air Tz ambayo ni National carrier!

Lakini yote haya ni kukosa standards. hatuna vigezo vya uongozi. Si umeona kikwete akichukuwa fomu na mtoto wake akapewa ukuu wa kukusanya sahihi! where on earth except idd Amin-type people.
 
Kwanini magazeti yanategemea biashara kutoka serikalini? si kwamba wanaweza kujikuta wanashiriki katika ufisadi ule ule wanaojaribu kuupinga?
 
Mzee,
Biashara ya maana ya matangazo iko wapi kungine zaidi ya haya serikali yanayokamata kurasa mbilitatu?
 
Kwanini magazeti yanategemea biashara kutoka serikalini? si kwamba wanaweza kujikuta wanashiriki katika ufisadi ule ule wanaojaribu kuupinga?

Hapo umenena Mzee wangu:
Ni lazima magazeti binafsi yanayoendeleza kampeni dhidi ya ufisadi yajitegemee yenyewe, na sana sana yasitegemee hela za matangazo kutoka serikalini. Yakisha anza kufanya hivyo, basi yatashindwa kutimiza wajibu wao na watapoteza readership, kwani wataanza kuogopa kuwaanika viongozi wa serikali waliowapa matangazo.
 
Ni uamuzi mzuri sana, for short run magazeti binafsi yataumia, for long run yataacha unafiki wa kufumbia macho uchafu wa serikali kwa kuogopa kunyimwa matangazo.....nimeshuhudia mara nyingi baadhi ya magazeti kushindwa kuandika ukweli wa habari fulani kwa sababu ya maslahi ya matangazo.
 
Magazeti ya Serikali si yanapata ruzuku kutoka serikalini? (mfano wafanyakazi wake utakuta wanalipwa na serikali), Kwa kuwa magazeti binafsi yanatakiwa yalipe kodi, ambayo ni sehemu ya hiyo ruzuku, hivyo naamini wana haki ya kulalamika ili nao wapate matangazo.

Hii ni sawa na biashara ya kutoa tenda, ukisema tenda zote ziende kwenye kampuni za Serikali itakuwaje?
 
Halisi,

Wakati umewadia kwa taasisi binafsi kuacha kuitegemea Serikali na kuinyenyekea hasa katika kupata mapato. Ndiyo Serikali ni Cash Cow mzuri lakini kwetu Afrika mambo si hivyo.

La muhimu hasa katika sekta ya habari ni kuwa na reform zitakazohakikisha kuwa Magazeti hayavuki ule mstari uliowekwa kama mtego, uwe ni mambo ya maadili, uendeshaji, kulipa kodi au ufuataji wa kanuni za uandishi na sheria ya habari na magazeti.

Vyombo binafsi vya habari visiache kukosoa Serikali kisayansi, vendeleze kuichambua Serikali kwa kutumia takwimu na habari zenye uhakika. Tabia ya kuandika habari zilizokaa ki-udakuudaku iachwe kama vinataka kupewa heshima inayostahili.

Mfano mzuri ni kukosekana kabisa kwa uchambuzi wa kauli aliyotoa Prof. Maghembe kuhusiana na mafanikio ya Shule za kata au kukopa kwa Serikali kutoka Benki binafsi kusaidia bajeti yetu.

Naomba mwende huko mawizarani na wakikataa kuwapa matangazo wakisema wameambiwa na Ikulu au wizara mama, ombeni ushahidi wa maandishi.
 
Leo nimenunua gazeti moja ambalo siku zote huwa ninafurahia kulisoma kutokana na msimamo wake. Lakini cha kushangaza ni kwamba nimekuta limepiga "about turn" moja ya nguvu sana na kuandika mambo yaliyonifanya nipate mshangao mkubwa. Ni dhahiri WAMESHANUNULIWA kukipigia debe CCM ama wanajipendekeza wapate wauziwe matangazo! Aibu tupu.
 
Leo nimenunua gazeti moja ambalo siku zote huwa ninafurahia kulisoma kutokana na msimamo wake. Lakini cha kushangaza ni kwamba nimekuta limepiga "about turn" moja ya nguvu sana na kuandika mambo yaliyonifanya nipate mshangao mkubwa. Ni dhahiri WAMESHANUNULIWA kukipigia debe CCM ama wanajipendekeza wapate wauziwe matangazo! Aibu tupu.

What/which gazeti is that? huna haja ya kusema gazeti fulani! litaje mkuu hapa ni pa ukweli.
 
Leo RaiaMwema wamepata kurasa 18 za hotuba ya bajeti ya Wizara ya Maji. Kelele hizi zinasaidia?
 
Back
Top Bottom