Serikali inaumwa, inajimwaga Loliondo

Rutashubanyuma

JF-Expert Member
Sep 24, 2010
219,470
911,174
Serikali inaumwa, inajimwaga Loliondo
ban.isango.jpg


Josephat Isango​

amka2.gif
NIMEZUNGUMZA mara nyingi sana, kuhusu umakini wa serikali yetu na sitakata tamaa kuandika.
Ingekuwa ujinga unatibika katika dawa za Loliondo, basi serikali ilipaswa kuwapanga watendaji wake wote watibiwe akili ili waweze kufikiri sawasawa.
Suala la ujinga ni hali ya kutokujua, na linasababiswa na uzembe wa kufikiri. Viongozi wengi wa serikali, tena viongozi wakubwa nao ni wazembe wa kufikiri. Wanakubali majibu yanayotolewa na msemaji wa kwanza bila kujiuliza kwanini mtu huyu kasema hivi na si vile.
Suala la tiba ya Loliondo limekuwa gumzo sana katika nchi yetu kwa siku za karibuni. Katika makala haya sitajihusisha kusema kuwa tiba hiyo ni halali au si halali, inatibu au haitibu, isipokuwa ninajikita zaidi katika kauli ya serikali iliyotolewa kuwa dawa hiyo haina madhara.
Serikali haikuona aibu, na wataalamu waliotumwa hawakufikirishwa vichwa vyao, wakalipeleka suala hili kisiasa, akili zao zikasitisha mkataba wa kufikiri, wakafikiri kinyume na hawakugundua mpaka sasa kuwa wamewahadaa watanzania. Kweli Tanzania bado tuna safari ndefu sana.
Mchungaji mstaafu wa Kanisa la Kiinjili la Kiluteri Tanzania, KKKT, alisema hadharani wala hakusema kwa siri kuwa dawa yake imepata uponyaji wa kimungu.
Ni neno la Mungu ndilo linatibu. Tena akaeleza kuwa dawa yenyewe ameoteshwa katika ndoto na Mungu, hivyo akakiri kuwa dawa yake ni tofauti na dawa nyingine kwani dawa nyingine mgunduzi ni mwanadamu na zimefanyiwa utafiti.
Lakini hii ya Loliondo ni ya neno la Mungu lililomjia katika ndoto. Serikali yetu isiyofikiri sawa sawa, na watendaji wake wasio makini, wanaopendelea kufanya siasa katika kila kitu, wakakurupuka, wakaunda timu kwa ajili ya kufanya utafiti.
Serikali yetu mara kadhaa imekiri hadharani kuwa yenyewe haina dini, vipi kwa suala la Loliondo ambalo linaonekana kuwa chimbuko lake ni dini wamekuwa tayari kutoa ushirikiano kwa kila hali?
Tunukuu kauli ya serikali na wataalamu wake. Serikali imesema imeridhishwa na dawa inayotolewa na Mchungaji Ambilikile Mwasapile wa Kijiji cha Samunge, Loliondo ikisema haina madhara yoyote kwa matumizi ya binadamu.
Akitoa tamko la timu ya wanasayansi waliofanya uchunguzi wa awali wa tiba hiyo, Kaimu Mkurugenzi wa Mamlaka ya Chakula na Dawa Tanzania (TFDA), Charys Ugullum, alisema timu hiyo ilianza utafiti wake wa awali Machi 7, mwaka huu.
Alisema timu hiyo ilijumuisha wataalamu kutoka Wizara ya Afya, TFDA, Taasisi ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR), Mkemia Mkuu wa Serikali na Taasisi ya Utafiti wa Dawa za Asili ya Chuo Kikuu cha Afya ya Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS).
Serikali yetu imenukuliwa ikisema imeridhishwa na dawa inayotolewa na Mchungaji Mwasapile wa Kijiji cha Samunge, Loliondo tena haina madhara yoyote kwa matumizi ya binadamu.
Katika suala hili kwanza serikali imechelewa kutoa tamko, kama dawa hiyo ingekuwa na madhara kwa wanadamu wangapi wangeathirka, na kwanini serikali ilisubiri muda mrefu wote mpaka karibu viongozi wote wa serikali wamekunywa ndipo inatoa tamko. Ni uzembe au kutokuwa makini?
Tamko la timu ya wanasayansi waliofanya uchunguzi wa awali wa tiba hiyo, lilisemwa na Kaimu Mkurugenzi wa Mamlaka ya Chakula na Dawa Tanzania (TFDA), Charys Ugullum, kuwa ilianza utafiti wake wa awali Machi 7, mwaka huu.
Hivi wasomi hawa wote hawakufikiri hata mara moja kuwa ni ujinga kupima kitu kilichosemwa ni neno la Mungu kwa kutumia vifaa vya maabara?
Tangu lini na wapi ndoto zinapimwa kwa kutumia vifaa vya maabara, Mkemia Mkuu anajua nini kuhusu Elimu ya ndoto?
Dawa inayosemekana inatoka kwa Mungu, inayolingana dozi kwa kila ugonjwa, inayohusisha imani kabisa bila nguvu za kisayansi, kweli serikali ilipaswa kutenga pesa kutafiti kama neno la Mungu linatibu?
Serikali yenyewe ingemwona wapi Mungu na kuuliza nguvu ya uponyaji ya huo mti uliokuwepo katika mazingira hayo kila siku?
Serikali bila aibu inasema, “tena kinachofuata sasa tutachunguza kama kweli dawa hiyo inatibu magonjwa hayo matano aliyoyasema Babu. Hivyo wananchi wawe na subira ili watupe nafasi tufanye utafiti wa kina zaidi.” Je, ikitokea kuwa dawa hiyo haitibu watachukua hatua gani?
Serikali ikaamua kujiingiza kisiasa, tena kichwa kichwa kuzungumzia suala la hatimiliki, Mkurugenzi wa Uendelezaji na Uratibu Utafiti kutoka Tume ya Sayansi na Teknolojia, Dk. Rose Kingamkono akasema wanafuatilia ili waweze kujua kama kuna hatimiliki ya tiba hiyo.
“Wananchi wasitoe mbegu au mti huo ovyoovyo maana wajanja wanaweza wakauchukua kwenda kutengeneza dawa kisha kuja kutuuzia tena kwa gharama kubwa.” Jamani viongozi wa serikali yetu wanafikiri sawa sawa? Mti upo porini, inasemekana umetiwa nguvu ya uponyaji na Mungu kwa kupitia mchungaji Mwasapile, wala si mtu mwingine, ndiyo maana hata wataaalamu hao wa tiba hadi sasa hawajachukua mizizi kupeleka Muhimbili, Bugando au KCMC kutibu wagonjwa, iweje mtu afikirie neno la Mungu kuwekewa hatimiliki, na kuzuia nguvu ya utendaji au uponyaji wa Kimungu usiende kwingine?
Je, mtu mwingine akiota Kenya leo, Uganda kesho na Uturuki wiki ijayo na kupewa uwezo kama wa Mwasapile, serikali yetu itazuia huduma za ndoto za Kimungu katika mataifa mengine kwa kuwa mtanzania ndio alikuwa wa kwanza kuota ndoto na kupewa maelekezo na Mungu?
Msajili wa Baraza la Tiba Asili na Tiba Mbadala, Dk. Paulo Mhame alisema hivi sasa wako katika hatua za mwisho za kumpatia cheti cha usajili Mchungaji Mwasapile. Wanampatia kama mganga wa jadi kwa utaratibu upi?
Dawa ni ya neno la Mungu, mchungaji anakiri kuwa yeye hatibu ila anatibu Mungu kwa kupitia dawa aliyomuotesha mchungaji huyu. Je, cheti hicho na hatimiliki kitaandikwa jina la Mungu au neno gani? Na kama wanampatia leseni, ni kwa sababu Babu wa Loliondo ameomba au serikali inayofanya siasa hata kwa neno la Mungu imeamua kujipendekeza?
Kuna mengi sana tunapaswa kuhoji kwanza kabla ya kuyatolea matamko. Katika suala hili serikali yetu imechemka. Kwanza kuunda timu, pili, kutumia pesa, tatu kutoa tamko, nne kutoa michango, tano kuanza kupima kwa kutumia maabara vitu vya kiimani.
Walipaswa kujiuliza neno la Mungu halifanyiwi kazi na timu, ndiyo maana Mungu hakutoa ndoto hiyo kwa timu ya serikali, walipaswa kutotumia pesa kuanza kufanya utafiti kwa mambo yasiyoonekana, ila ni ya kusadikiwa tu, akili iliyoumbwa inawezaje kufanya utafiti kuelewa kilichowekwa akilini na Muumbaji?
Zaidi ya hayo ni udhaifu sana kupima kinachosadikiwa kuwa ni neno la Mungu kwa kutumia vifaa vya maabara, na ukatoka hadharani ukasema kitu hiki hakina madhara, tukiendelea hivyo basi kila maabara inaweza kupima na kujua dini ya mtu bila kumuuliza.
Serikali yetu imesema uongo, haijafikiri sawa sawa, inakurupuka, haijifikirishi kutoa matamko, inafanya kazi kwa staili ya ujima, na kutoa majibu kana kwamba Watanzania wote tuna sare ya mawazo kama ya wataalamu hao.
Namnkuu paroko mmoja aliyetupa mawazo ya kujifikirisha kidogo kuwa "Sina chuki wala tatizo lolote na tiba ya Loliondo, lakini kama unataka kwenda lazima ujiulize maswali manne yafuatayo:
Kwanza, tiba inayotokana na miujiza ya Mungu lazima iwe endelevu, isiwepo kwa kipindi kifupi tu.
Pili, watu wajiulize kama miujiza kutoka kwa Mungu huwa na masharti?
Tatu, wajiulize kama tiba hiyo inafanya kazi ndani ya Loliondo, kwanini isifanye kazi Dar es Salaam na kwingineko?
Nne, wajiulize kuhusu tiba hiyo ya magonjwa sugu ukiwemo ukimwi, je, Mungu aliwaumba wanadamu na kisha kuamua kuwaangamiza? Au wanadamu wanaangamia kutokana na vitendo vyao vya ujanja ujanja?
0786426414
 
Babu Loliondo atoa wasia kwa wagonjwa Send to a friend Wednesday, 30 March 2011 00:08
babuloooo.jpg
Waandishi Wetu
MCHUNGAJI Ambilikile Masapila anayetoa tiba ya magonjwa sugu katika Kijiji cha Samunge, Loliondo amewataka wagonjwa kuendelea kutumia dawa za hospitali hata baada ya kunywa dawa yake.Akizungumza kijijini hapo jana, Mchungaji Masapila alisema hakuna madhara kwa mgonjwa kuendelea na dawa zake za awali hata baada ya kunywa dawa yake na kwamba si vyema kuacha ghafla kutumia dawa hizo."Hii dawa yangu inatibu, lakini haizuii kunywa nyingine, unaweza kunywa na ukiona umepona kabisa usiendelee kunywa dawa hizo," alisema.

Vurugu zazuka Samunge
Polisi jana walilazimika kutumia nguvu za ziada kuwadhibiti watu waliokuwa wamefunga barabara ya kuelekea katika Kijiji cha Samunge na kusababisha msongamano mkubwa wa magari.Barabara kuu ya kuingia katika kijiji hicho ilikuwa katika msukosuko kiasi cha baadhi ya watu kutishiana kwa silaha.Habari zilizolifikia Mwananchi zilisema, ulitokana na baadhi ya magari kutaka kuingizwa kwenye foleni bila kufuata utaratibu.

"Hapa kuna watu wanajifanya wao ndiyo Serikali au wao ndiyo kila kitu, sote ni wagonjwa na tunataka kwenda kwa Babu kunywa dawa, sasa kama mtu anafikia hatua ya kututishia sisi kwa bastola Serikali iko wapi?" alihoji mmoja wa watu, Heriel Mushi mkazi wa Mwika, mkoani Kilimanjaro.

Kutokana na hali hiyo, Mkuu wa Polisi wa Wilaya ya Ngorogoro (OCD), Listone Mponjoli jana alilazimika kuongoza askari wenzake kuendesha doria katika barabara hiyo ili kudhibiti dalili za uhalifu ambazo zimekuwa zikiripotiwa, pamoja na kuyaelekeza magari kukaa upande mmoja wa barabara ili kuruhusu kutumika kwa upande mwingine.

Katika doria hiyo, OCD Mponjoli alijikuta katika wakati mgumu pale wananchi walipozuia hata gari lake kupenya kuelekea eneo la Kibaoni, wakidai kwamba hawana imani naye kwani polisi wamekuwa wakivusha watu kinyemela na kuwawahisha kunywa dawa.Kulikuwa na vizuizi vya miiba vilivyokuwa vimewekwa kudhibiti upitaji holela wa magari katika eneo lililopo umbali wa kilometa kama tatu kutoka nyumbani kwa Mchungaji Masapila.

Mvutano mkubwa ulizuka katika mpaka wa Vijiji vya Samunge na Yasimbito ambako wasafiri walitumia magari yao kuziba barabara na OCD Mponjoli alipofika katika eneo hilo alizuiwa, hali iliyozusha mabishano makali baina yake na raia.Mkuu huyo wa polisi wa wilaya alisema ukaidi wa watu wanaokwenda kunywa dawa ndiyo chanzo cha vifo vinavyotokea kwani hata gari la kubebea wagonjwa wanaozidiwa linalosimamiwa na Chama cha Msalaba Mwekundu, limekuwa likizuiwa kwa madai kwamba 'linachakachua foleni'.

"Hatuwezi kuacha hali hii iendelee, lazima tuimarishe usimamizi wa usalama wa watu. Tukiachia raia waamue kufanya kila kitu, haki haiwezi kutendeka. Lazima watu waache ubinafsi wajue kwamba polisi tupo kwa ajili ya kutoa msaada kadiri tutakavyoona inafaa," alisema Mponjoli.Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro, Elias Wawa Lali aliliambia Mwananchi kuwa watu wanaokwenda Samunge kunywa dawa, wamekuwa wakali kiasi cha kuzuia utekelezaji wa shughuli nyingine zisizohusiana na utoaji wa tiba ya Mchungaji Masapila.

"Hapa ni wilayani kuna shughuli nyingi, sasa watu wanaokwenda pale Samunge wamefunga ile barabara ya kuingia pale kijijini na tunashindwa kutekeleza majukumu mengine ya kijamii kwa sababu tu ya hii tiba,"alisema Lali na kuongeza:
"Tunawaomba wananchi wanaofika kijijini pale wawe na uelewa kwamba ile barabara ilikuwapo kabla ya kuanza kutolewa kwa tiba ya Baba Mchungaji, hivyo inafaa iendelee kutumika kwa shughuli nyingine hata kama siyo za tiba."

Serikali yamkuna Mchungaji
Mchungaji Masapila ameelezea kufurahishwa kwake na matokeo ya utafiti uliofanywa na Serikali uliothibitisha kwamba dawa anayotoa ambayo inatokana na mti wa mugariga haina madhara.Akizungumza na Mwananchi jana asubuhi alisema hata hivyo, kwamba hakushangazwa na matokeo hayo kwani tayari Mungu alikwishamthibitishia kwamba dawa hiyo haina madhara yoyote kwa binadamu."Naishukuru Serikali maana naona wananiunga mkono, hii ni dawa kutoka kwa Mungu na wala sio mti pekee na nilijua wakipima hawatakuta madhara yoyote kwani Mungu alikwishanieleza kuwa watapima wataalamu wa ndani na nje ya nchi dawa hii na watakuta haina madhara," alisema.

Alisema dawa ambayo anatoa imekuwa na mafanikio makubwa katika afya za watu, kwani wanampa taarifa za kupona magonjwa mbalimbali hata yale ambayo hakutegemea kwamba yataponywa na dawa hiyo."Watu wenye vidonda vya tumbo wanapona, kina mama wanapata mimba, watu wanapona kifafa, pumu, kansa na magonjwa mengine, hivyo hili linathibitisha ubora wa tiba hii," alisema.Mchungaji Masapila pia alisema kazi ambayo amekuwa akifanya kwa saa zaidi za 13 kila siku, haimsumbui akidai kwamba tayari alikwishamuuliza Mungu kwamba atawezaje kutoa tiba kwa watu wengi ilihali ni mzee na akaelezwa kuwa ataongezewa nguvu.

Ushuhuda waliopona
Baadhi ya watu ambao tayari wamepata tiba jana waliendelea kutoa ushuhuda. Mmoja wao ni Hassan Kaniki Mkazi wa Dar es Salaam ambaye alisema tangu amekunywa dawa hiyo Alhamisi iliyopita amepona ugonjwa wa kisukari.Kaniki alisema kwa zaidi ya miaka mitano amekuwa akitumia dawa za kisukari lakini tangu juzi, sukari imeshuka na kufikia 5.5 jambo ambalo halijawahi kutokea.

"Tangu juzi nakunywa soda, nakula wali nakula nyama na situmii dawa. Nimepona kabisa, sijui labda baadaye," alisema Kaniki ambaye bado alikuwa Samunge akisubiri familia yake kupata tiba.

Mkazi mwingine wa Dar es Salaam, Merere Mwambene naye alidai kuwa amepona ugonjwa wa kisukari na kwamba tangu juzi jioni alipokunywa dawa hiyo alikunywa soda na jana asubuhi alikunywa chai yenye sukari bila kuathirika.
"Kabla sijanywa dawa nisingeweza kukaa muda wote huu bila kujidunga dawa na ilikuwa nikipitisha muda tu, macho yalikuwa mazito na kuanza kushindwa kuona kabisa, lakini hali ni tofauti tangu nilipokunywa dawa."
Mgonjwa mwingine ni Jonathan Magesa kutoka Mwanza ambaye amekuwa akisumbuliwa na pumu. Alisema tangu ametumia dawa hiyo anajisikia kupona na hatumii tena dawa.

Pemba walilia
Wakazi wa Pemba, wamemwomba Mchungaji Masapila kuwasogezea huduma ya tiba ya magonjwa sugu ili nao wanufaike nayo.Baadhi ya wakazi hao waliofika kwenye ofisi za gazeti hili zilizopo katika Jengo la Bandari, Tanga walisema wamekuwa wakifuatilia kwa karibu tiba hiyo kupitia vyombo vya habari na kugundua kuwa kimsingi ina ukweli.

Mmoja wa wakazi hao, Shaame Ussi alisema baada ya kusikia kuwa dawa hiyo inaponyesha na kuwaona hata viongozi wa Serikali wanainywa, ni vyema sasa huduma hiyo ikawasogelea watu ili wanufaike nayo.Ussi alisema ingekuwa vyema kama mchungaji huyo angeipeleka huduma hiyo mkoani Tanga ili kuwawezesha wakazi wa Pemba kuipata.

Habari hii imeandikwa na Salim Mohamed, Neville Meena na Mussa Juma, Samunge
 
Agizo la Babu langonga mwamba


*Ni la kuzuia wagonjwa wapya kwenda kwake
*Wabuni njia yao mpya inayokwepa vizuizi


Na Said Njuki, Arusha

WAKATI wananchi wanaokadiriwa kufikia 6,000 wakiwa wamekwama njiani kwenda kwa
Mchungaji Kanisa la Kiinjili la Kilutheri (KKKT), Ambilikile Masapila wa Kijiji cha Samunge, Loliondo wilayani Ngorongoro baadhi watu wamepuuza agizo la serikali na ombi la mchungaji huyo, baada ya kubuni njia ya panya ili kufika kwa mchungaji huyo.

Uchunguzi uliofanywa na Majira na kuthibitishwa na baadhi ya mashuhuda umebaini watu hao wanapita barabara ya Longido, kupitia Ziwa Natron na kuibukia kijijini kwa Babu baada ya kutoa kitu kidogo.

Uchunguzi huo umebaini kuwa pamoja na kuwepo kwa ulinzi katika eneo hilo lakini ni hafifu nyakati za usiku kutokana na baadhi ya magari kupenya kutokana na wamiliki au madereva wa magari hayo kutoa kati ya sh. 20,000 hadi sh. 50,000 ili kufanikisha azma hiyo.

Tayari serikali katika kutekeleza mapendekezo ya Babu imeweka utaratibu wa vituo kwa ajili ya usajili wa wagonjwa wanaokwenda katika kijijini humo.

Vituo hivyo vipo Arusha katika Uwanja wa NMC, Babati mkoani Manyara, Mugumu na Musoma katika Mkoa wa Mara kw wale wanaotoka Kanda ya Ziwa.

"Bado shughuli ya kupenyeza wagonjwa kwenda kwa Babu linaendelea hasa kupitia Longido na Ziwa Natron na njia hiyo inawajumuisha watu wanaotoka wilaya hiyo na nchini Kenya kwa sababu kupitia Mpaka wa Namanga hali hii itachelewesha azma ya mchungaji ya kumaliza wagonjwa waliokuwa wamefika huko kabla ya Aprili Mosi mwaka huu kama alivyopanga," alisema mmoja ya vyanzo vyetu vya habari.

Kutokana na hali hiyo baadhi ya watu waliozungumza na Majira wameiomba serikali kudhibiti njia zote muhimu ili utekelezaji wa mapendekezo ya mchungaji yawe na tija, la sivyo utekelezaji wake utakuwa mgumu hivyo kuwa sawa na kutwanga maji.

"Kumekuwepo na udhaifu wa utekelezaji wa mapendekezo kadha wa kadha kutoka hata kwa viongozi wa juu serikalini hapa nchini vivyo hivyo hata katika hili la mchungaji litakwama iwapo serikali haitakaza
kamba," alisema Bw. John Kiwelu.

Hata hivyo, hali bado inazidi kuwa mbaya kwa wagonjwa walioziuwa huko katika vizuizi vya Mto wa Mbu na Meserani wilayani Monduli kwa kuwa sasa yamefikia magari 500 yenye watu zaidi ya 3,000.

Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro, Bw. Elias Wawa Lali amewatahadharisha wagonjwa wanaojiandaa kwenda kwa Babu na walio katika vizuizi mbalimbali kufuata utaratibu na kanuni zilizowekwa na Babu ili kuleta utekelezaji wenye tija kwa manufaa ya watu wote.
 
Waziri Simba aonja joto ya jiwe kwa Babu


na David Frank, Loliondo


amka2.gif
WAZIRI wa Maendeleo ya Jamii Wanawake na Watoto Sophia Simba, ameonja joto ya jiwe baada ya kuzuiwa na wananchi kumfikia Mchungaji Ambilikile Maisapila, kwa madai kuwa ‘alichakachua' foleni kumfikia.
Waziri Simba alifika katika kijiji cha Samunge majira ya alasiri (Alhamisi iliyopita), akiwa katika msafara wa magari manne na kutaka kwenda moja kwa moja kumwona Babu eneo alilokuwa akitolea tiba hiyo.
Ghafla waziri huyo alivamiwa na kundi la watu wenye hasira ambao wengi wao walikuwa wamekaa kijijini hapo kwa zaidi ya siku saba, wakisota kumwona Babu.
Mashuhuda wa tukio hilo la aina yake, waliliambia Tanzania Daima Jumatano kuwa Waziri Simba alizuiliwa kwani alitaka kumwona Babu muda mfupi tu baada ya kuwasili kijijini hapo bila kufuata foleni.
"Watu hawakujali uwaziri wake, walimzonga na kumhoji imekuwaje amefika na kukimbilia kikombe bila kupanga foleni kama wanavyofanya wao. Uliibuka mzozo mkubwa kati yake na wananchi hao ambao baadhi walikuwa wakisema hovyo kwa hasira," alisema shuhuda wetu.
Wakati tafrani hiyo ikitokea, wasaidizi wa Babu pamoja na baadhi ya viongozi wa serikali ya kijiji cha Samunge, walikimbia kwa hofu ya kupewa maneno makali na wananchi, hali iliyomlazimu Babu kusitisha tiba yake kwa muda kutuliza hali hiyo.
Wakati akituliza hali hiyo, Babu akiwatahadharisha wananchi waliofurika kijijini kwake kwamba wanapaswa kuwaheshimu viongozi wanaofika hapo kwani mbali ya kupata kikombe, pia wanaratibu shughuli zinazohusiana na tiba hiyo ya ajabu.
"Nawaomba muwaheshimu viongozi wanaokuja hapa kwani mbali ya kuja kupata tiba wanafika kuona namna ya kuboresha hali ya mazingira ili tiba hii iweze kuwa endelevu," alikaririwa Babu akisema.
Babu alimwongoza Waziri Simba kwenda kumpa kikombe pamoja na ujumbe wake na baada ya kupata tiba hiyo, waliondoka kurudi Arusha.
Katika hatua nyingine siku chache tu baada ya Babu kusitisha huduma kwa watu na wagonjwa wanaotoka ndani na nje ya nchi, kumeibuka staili mpya ya magari kusafiri na kupeleka watu kwenda kijijiini Samunge kupitia njia za panya.
Uchunguzi uliofanywa umebaini kuwa mbali na barabara zilizowekewa vizuzi, yapo magari yanayotumia barabara ya Longido kupitia Ziwa Natron na kuingia moja kwa moja kijijini Samunge.
"Pamoja na kuwepo vizuizi maalumu kama vile vya Arusha, Mto wa Mbu, Babati mkoani Manyara, Mugumu na Musoma mjini mkoani Mara, bado madereva watukutu wanafanya hila na kusafirisha watu na wagonjwa hao kupitia Longido na kuchepukia Ziwa Natron na kuunganisha moja kwa moja kwa Babu," alisema mmoja wa viongozi wa wilaya ya Ngorongoro.
Wakati hayo yakiendelea, magari zaidi ya 300 yamezuiliwa katika kizuizi cha Mto wa Mbu, huku zaidi ya magari 100 yakiwa yamekwama eneo la Melerani wilayani Monduli, yakiwa njiani kwenda Loliondo.
Kuzuiliwa kwa magari hayo ni sehemu ya utekelezaji wa mapendekezo ya mchungaji huyo ambapo aliomba wagonjwa wapya kusitisha kuingia Loliondo katika kipindi cha wiki moja.
 
Back
Top Bottom