Basi la Scandnavia lateketea kwa moto
• Abiria 21 wanusiraka kifo
na Ghisa Abby, Morogoro
WATU 21 wamenusurika kifo baada ya basi lenye namba za usajili T 641 AGA aina ya scania la Kampuni ya Scandnavia lililokuwa likitokea jijini Dar es Salaam kwenda mkoani Mbeya kuteketea lote kwa moto eneo la Melela Kibaoni.
Akizungumza na waandishi wa habari katika eneo la tukio jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Thobias Andengenye, alisema chanzo cha basi hilo kuungua moto hakijajulikana mpaka sasa.
Kamanda Andengenye alisema tukio hilo lilitokea Machi 8 mwaka huu majira ya saa 4.30 asubuhi katika eneo la Melela, wilaya ya Mvomero.
Alisema basi hilo lilikuwa likiendeshwa na dereva John Steven (45) mkazi wa Yombo Vituka, Dar es Salaam ambapo aliongeza kuwa abiria wote waliokuwemo walinusulika kifo baada ya kutokea madirishani.
Kamanda Andengenye alisema baadhi ya mizigo ya abiria iliteketea kwa moto huku mizigo michache ikiokolewa na wasamalia wema.
Baadhi ya abiria waliozungumza na waandishi wa habari, walisema tangu wakiwa standi ya mabasi Msamvu walianza kusikia harufu ya moshi wa kitu kama kinaungua, lakini waliona ni kawaida tu wakaamua kuendelea na safari.
Walisema walipofika eneo la Melela waliona ghafla moshi ukifuka na baadaye moto ukaanza kuwaka kwa nguvu na ndipo walipoanza kuokoa maisha yao kwa kupita madirishani.
Wakati huo huo, watu watatu wamefariki dunia mkoani hapa, akiwemo kijana aliyetuhumiwa kuiba vyombo vya nyumbani zikiwemo sufuria za wali na maharage kupigwa na wananchi wenye hasira huku mwingine akiangukiwa na jiwe akichota maji mtoni.
Kamanda Andengenye alisema tukio la kwanza lilitokea Machi 5 mwaka huu majira ya saa 11:00 jioni katika milima ya Kiegeya kitongoji cha Kitundu kijiji cha Kiegeya tarafa ya Magole wilayani Kilosa ambapo mwanamke Joyce Mwehanga (37) alifariki dunia baada ya kuporomokewa na mawe wakati akichota maji mtoni huku mvua ikiendelea kunyesha.
Alisema katika tukio jingine, lililotokea Machi 7 huko Misufini kijana mmoja aliyefahamika kwa jina moja la Mazoea anayekadiriwa kuwa na umri wa kati ya miaka 25 na 30 alipigwa na wananchi wenye hasira na kufariki dunia baada ya kutuhumiwa kuiba vyombo mbalimbali vya ndani ikiwemo sufuria la wali na maharage.
Katika tukio jingine lililotokea Machi 7 katika eneo la Kidatu wilayani Kilombero mwanafunzi wa darasa la kwanza, Fred Benfred (11) alifariki dunia baada ya kunaswa na umeme katika dimbwi la maji ambalo lilidondokewa na waya zenye umeme.
Source: Mtanzania daima