Riwaya za Kijasusi

Riwaya za Kijasusi

RIWAYA: HUJUMA 06
MTUNZI: richard R. M
WAMBE

SHALABAH alitulia kitini akinywa taratibu kahawa yake. Gari moja nyeusi aina ya Toyota Nadia ilisimama mita chache kutoka pale alipokuwa ameketi. Mwanamke mrefu akateremka, aliyevaa kininja, akavuta hatua ndefundefu mpaka pale alipoketi, akavuta kiti na kukaa.
“Sina maneno mengi, ila unajua kuwa nimekwsihamaliza kazi uliyotaka nifanye, nimefata hundi yangu,” Fasendy akamwambia Shalabah.
“Usijali, niliketi hapa kukusubiri wewe, ili kukukamilishia malipo yako lakini pia kuna kazi nyingine ya kufanya,” Shalaba akamwambia Fasendy huku akimpatia bahasha nyeupe ambayo ndani yake kulikuwa na hundi hiyo. Akaifungua na kutazama akaiona ni sawa, akaifutika ndani ya nguo yake.
“haya, ongea linguine,” Fasendy akamwambia Shalabah.
“Nifuate,” Shalabah akamwambia Fasendy kisha akanyanyuka na kuingia ndani ya jengo hilo lililoonekana kama gofu, lililotelekezwa kwa muda mrefu sana, wakapita koridoni mpaka kwenye moja ya chumba, wakaingia na kukatiza milango kama mitatu hivi, mlango wan ne ulikuwa mlango wa kioo safi uliozungukwa na kamera za cctv ili kulinda usalama wa eneo hilo. Shalabah akabonya kitufe na mara mlango ule ukafunguka, wakaingia ndani.

Kilikuwa ni chumba kidogo lakini chenya kila kitu kinachohitajika katika ofisi yoyote duniani. Shalabah akamkaribisha Fasendy na wote wawili wakaketi katika viti vyenye vono safi. Katika meza iliyokuwa mbele yao kulikaliwa na mtu mmoja mnene mwenye mwili mkubwa aliyejaa katika suti kali nyeusi, kichwa chake kilionekana kuungana na kiwiliwili, hakuonekana shingo yake kama ilikuwepo au ilimezwa na unene huo.
“Karibu sana mwanamke,” akamkaribisha Fasendy, akajikohoza na kuendelea, “ kwanza nikupongeze kwa kazi ngumu nay a hatari uliyoifanya ya kutuletea wale watu wawili wanaojifanya kufuatilia nyayo za samba. Nafikiri malipo yako umeshayapata, lililobaki huku mbeleni tuachie sisi tunajua cha kuwafanya, lakini nina jambo moja, hawa Watanzania wakishaona wenzao hawapatikani kwa mawasiliano kwa vyovyote watatuma mtu mwingine au watu wengine kuja kuwatafuta, sasa nataka nikupe kazi nyingine ya mkataba wa miezi mitatu, ya kuhakikisha kila anayeingia hapa ni kumpoteza moja kwa moja kama tulivyofanya kwa wale Waamerika waliojifanya waandishi wa habari, upo tayari?” yule mtu akauliza.
“Wewe unajuaje kama watatuma watu wengine?” Fasendy akauliza.
“Mimi najua, ninalokwambia ndilo hilo, kumbuka tuna wanajeshi wao ishirini na tano, na hawa wawili, unafikiri watavumilia? Tunataka kuhakikisha biashara yetu inakwenda safi kabisa,” yule Bwana akamaliza.

Fasendy, akatulia kimya akiitafakari uzito wa kazi hiyo.
“Sawa, hamna tabu,” akajibu Fasendy. Yule mtu mnene akasimama na kumpoa mkono Fasendy kisha akamruhusu aende. Shalabah akamsindikiza hadi nje na kuagana naye.
“Sharon,” yule mtu mnene akaita. Sharon akajitokeza kutoka katika mlango Fulani pembenzoni mwa chumba kile, akasimama akisikiliza, “Boss ansema uhakikishe wale mateka wawili wanajutia walichokifanya na upeleke onyo kali kwa waliowatuma, kisha simamia biashara nzima, wateja wetu wamesema watakuja baada ya siku tatu kuangali makombora yaliyobaki, kama kuna shida yoyote wasiliana na Shalabah, yeye ndiye mwenye uwezo wa kuwasiliana na mimi na Mr Lonely kwa utatuzi wa mwisho,” yule Bwana akamaliza na kuagana na watu wake, kisha akabaki yeye na Shalabah tu.

§§§§§
MOQDISHO TEXTILE

Jamil alikuwa amefungwa kamba na kuning’inizwa kichwa chini miguu juu, hakuweza kufanya lolote kwani pembeni yake alikuwa akilindwa na vijana wawili wadogo waliokuwa na silaha za maana zilizodungwa mkanda mrefu wa risasi, hawakuona taabu kummiminia yeyote atakayeleta shida katika himaya hiyo. Walikuwa ni vijana wawili wenye kukadiriwa umri wa miaka kumi na tano na kumi nane. Vinywani mwao waote walikuwa wanakula mirungi. Jamil aliwatazama kwa zamu ili aone kama kuna jinsi ya kujiokoa lakini hali ilikuwa siyo, kwa kuwa mlango wa chumba hicho ulikuwa ni wa chuma madhubuti kabisa. Jamil alitulia palepale huku akiwaza ni wapi Gwamaka atakuwapo kwani alimuacha hotelini.
Mara mlango ukafunguliwa, Sharon akaingia ndani na vijana wengine wawili waliovaa kiraia lakini wakiwa na silaha nzito. Jamil aliona wazi hawa jamaa hawajui matumizi ya silaha kwamba silaha hii nitumia vitani na sio kutembea nayo nah ii nitumie wapi, ilikuwa haishangazi kumkuta mjini au sokoni begani mwake amejitwika RPG huku akitalii akitazama hili na lile.

“Mfungue, umtoe hapa,” Sharon aliamuru, kijana mmoja akaja na kisu na kukata kamba iliyofunga miguu ya Jamila, akaanguka na kutanguliza kichwa, akajipiga kwenye sakafu na kubwagika chini kama mzigo. Jamil akatoa mguno hafifu wa maumivu, kisha akatulia kimya. Wakamfungua kamba za miguu na kumuinua, akasimama wima lakini akiegemea ukuta maana alikuwa akisikia kizunguzungu cha hali ya juu.
Sharon akamsogelea Jamil.
“Komandoo, koamndoo utakuwa wewe? Hiyo serikali yenu bora iombe msaada niwape hawa watoto wawili tu ni sawa na vikosi vyenu kumi vya kijeshi, na sasa utajuta, kukamatwa na sisi, sisi hatuna serikali kwa taarifa yako, na sasa utaenda kushuhudia ndugu yako anavyouawa na hiyo ndiyo salamu kwa serikali yako, mataifa ya magahribi yameshindwa itakuwa ninyi, ninyi ni nani hata mjifanye mna uchungu?” Sharon alimwambia Jamil, alipomaliza tu kusema akageuka na kuwaamuru watu wake kumuongoza Jamil upande wa pili wa jengo. Wakamto ilhali akiwa na kamba mkononi mwake.

Ulikuwa ni ua mkubwa sana wenye malori kadhaa yaliyokuwa yameegeshwa. Watu wenye silaha walikuwa wengi, vijana, watu wazima, walikuwa na silaha nzito nzito.
“Simama hapa” Jamila aliambiwa na wale waliokuwa wakimlinda, akasimama pamoja na watu wengine wawili, wazungu walioonekana kuchoka sana. Mara akachukuliwa mmoja wao na kupelekwa katikati ya ule uwanja, kelele zikaanza kusikika, kelele za mashangilio, huku wakipiga risasi hewani, yule aliyempeleka pale akachomoa jambia na kumkata shingo, akamchinja na kutenganisha kabisa kichwa na kiwiliwili. Kwa kitendo hicho wenzake wakashangilia sana, ilikuwa ni kama tafrija kwao. Jamil alishindwa kutazama kitendo hicho, aliinama na kufumba macho.

“Watu makatili sana hawa, sidhani kama ni binadamu wa kawaida,” Jamil aliongea kwa sauti ya chini. Kisha yule jamaa aliyemchinja yule mtu akaja kwa Jamil na yule mwingine, akasimama mbele yao.
“Burudani yetu ni kuwachinja watu kama ninyi, siku yenu bado,” akamaliza na kuondoka. Jamil na yule mwenzake wakachukuliwa na kufungiwa ndani ya chumba kisicho hata na dirisha isipokuwa tundu dogo kama shimo la panya lililoweza kuingiza hewa kwa tabu na mwanga kidogo sana.
Kufungiwa ndani ya chumba hicho kwa Jamil haikuwa mateso, bali kukaa bila kujua Gwamaka yuko wapi hilo ndilo lilikua teso kubwa kuliko yote, alibaki hivyo akitafakari bila jibu, hakuwa na jinsi ilimpasa kutulia.

3… Dar es salaam – Tanzania… saa 7:05 mchana

JUA kali la saa saba lilikuwa likichoma kwelikweli, mji wa Dar es salaam uligubikwa na joto kali, kila umuonaye kama hana kitambaa mkononi cha kufuta jasho basi alikuwa kifua nusu wazi ilimradi apate kaupepo hako kadogo. Lakini wote waliokuwa wakiteseka na joto hilo ni wale watu wa KCC yaani Kima Cha Chini, lakini kwa mwenye nazo daima jiji la Dar es salaam ni jiji lenye baridi sana kiasi kwamba kila muda anatembea na suti ya vipande vitatu.
Jiji linalosifika kwa uzuri na linalovutia watalii kwa historia yake ya utulivu na amani. Kila kijana wa Tanzania anaamini kuwa katikan jiji hilo ndiko maisha yanakoanzi hivyo huwafanya wengi kukimbilia huko ili kuanza maisha mapya wakiamini watatajirika. Lakini hali huwa tofauti sana wakifika katika jiji hilo, mwisho wake ndio vibaka, wabwia unga, makahaba kuongezeka katikati ya jiji na kwenye viunga vyake. Ijapokuwa kila mara wanasomba na polisi na kuwekwa mahabusu lakini wakitolewa tub ado huendelea na shughuli zao hizo hizo wanaacha kwenda vijijini wakawekeze katika kilimo na ufugaji, lakini siwalaumu wao, ila nailaumu serikali inayoshindwa kuwawekea mafunzo thabiti ya ujasiriamali tangu wakiwa shule ya msingi, hata somo la sayansi kilimo lililokuwapo shuleni siku hizi hata haliko katika mitaala, basi waache vijana wajikimbilie mjini na taifa kuwa taifa la vibaka.

Katika ofisi ya wizara ya ulinzi na jeshi lakujenga taifa, Mwenge, Mlalakuwa hali ya utulivu ilikuwa imetawala, ni bendera tu ya Taifa iliyokuwa ikipepea huku na huko kadiri ya upepo ulivokuwa ukiitaka. Geti lilifunguliwa taratibu na mwanajeshi aliyekuwa lindoni siku hiyo.
“Kuna mzigo wenu hapa,” kijana mmoja aliyekuwa juu ya pikipiki aina ya Yamaha alikuwa akiwaambia walinzi hao.
“Ok, nenda mlango ule pale kuna mwanadada pale mkabidhi,” yule MP akampa maelekezo baada ya kusoma anwani na kukuta imeelekezwa katika ofisi ya waziri mwenyewe.
Katibu muhtasi wa wizara, Miranda, alisaini kitabu cha dispatch cha kijana huyo kamba ameupokea mzigo huo katika hali ya usalama. Kisha wakaagana.

Kilikuwa ni kikasha cha mbao, kilicho tengenezwa vizuri na kupigwa vanish safi, pembeni anwani yake ilikuwa imeandikwa kwa maandishi ya chuma yaliyokuwa yaking’aa sana, na kwa sababu kilikuwa na anwani ya ofisi haikuwa tabu kwa Miranda kukifungua kujua ndani kuna nini kwa kuwa ni mzigo wa kiofisi, akachukua kijinyundo kidogo na kubabazua mfuniko wa kikasha hicho nao ukafunguka, ndani yake akakuta kitu kama box hivi, alipoligusa lilikuwa la baridi kama lina barafu ndani yake, akaondoa gundi iliyofunga box hilo na kulifungua ndani, huko akakuta kasha maalum sililoruhusu barafu kuyeyuka akaondoa mfuniko wake.
“Aaaaaaaaaaaaaaaiiiiiiiiiggghhhhhhhhh!!!!!!!” ilikuwa ni kelele moja kali kutoka kwa Miranda, mara ikakatika ghafla na kishindo cha kikasikika, Miranda akaanguka na kupoteza fahamu.

Mp aliyekuwa getini alisikia kelele ile na ukinya uliofuata akamwachia mwenzake lindo akakimbia kutazama kuna nini, alipoingi alimkuta Miranda chini hana fahamau, akaomba msaada haraka na wengine wakatoka maofisini kuja kumsaidia kwa huduma ya kwanza, hakuna aliyejua ni nini kimeamfanya aanguke. Ni pale mwanajeshi mmoja aliposogelea lile box akabaki kaduwaa, kinywa wazi. Hakutaka kuyaamini macho yake kwa kile yanachokiona. Kichwa cha binadamu, kichwa cha Gwamaka kilikuwa kimetulia ndani ya box lile, hakuongea kitu alitoka nje na kulia sana. Kila aliyeingia ndani ya ofisi hiyo alitoka akilia kwa uchungu…
 
HUJUMA 07
MTUNZI richard R. MWAMBE



Brigedia jenerali Kyambassa alikuwa hatulii ofisini, alitoka kona hii ya ofisi na kwenda ile kule, akishika hiki na kuacha kile, kama umemzoea ungeweza kumjua wazi jinsi alivyoshikwa na hasira kwa ndita zilizojipanga katika paji la uso wake, na kufanya kama matuta ya kuwalazimisha madereva kupunguza mwendo barabarani. Hakuwa na amani mwilini wala moyoni, kijasho kililowesha suti yake ya kijeshi yenye rangi ya kijani kibichi, kama haikutosha hata viatu alivyovaa vilionekana kumbana ghafla, akavilegeza gidamu zake na kuendelea kuizungukan ofisi hiyo bila kuchoka, hakuweza kukaa kwani alihisi kiti ni cha moto.
“Hii ni dharau, dharau iliyopita kipimo,” Kyambassa aliongea kwa ukali kuwaambia watu wachache waliokuwamo katika ofisi hiyo. Kwa ujumla hakuna aliyeongea kila mtu kama si kutiririkwa na machozi basi alibaki katumbua macho akitazama lile kasha la mbao safi lililotumwa kwao likiwa na zawadi ya kichwa.
"Afande, kiukweli ni swala linaloumiza sana, sasa kama huyu wamemfanya hivi ni vipi kuhusu Jamil, komandoo wetu, kwa maana tunajua thamani ya komandoo mmoja, sisemi Marehemu Gwamaka hakuwa na thamani ila yeye tayari tumeshampoteza hatuwe zi kuimjadili, lakini vipi huyu aliyebaki ambaye hatuna mawasiliano naye na wala hatujui yuko wapi, pia na vipi wale wanamaji wetu ishirini pamoja na wale Warussia watano?” aliongea kwa uchungu Kanali Hosea Mlawa. Ukimya ukatawala tena.

“Hapa tutajadili lakinin jibu halitapatikana, mi nafikiri sisi kama wapiganaji ambao usalama wa watoto wetu uko mikononi mwetu tuamue jambo moja, tuiongie kijeshi Somalia, tukawatwange hao wanaojiita maharamia tuwachukue ndugu zetu,” aliongea kwa jazba mwanamama pekee aliyekuwa katika jopo hilo la watu wa juu kabisa wa JW.
Brigedia Jenarali Kyambasa, alionekana kujifuta machozi kila wakati, mara hii alikuwa ameketi katika kiti chake cha kazi ambacho mbele yake kilizungukwa na na viti kadhaa vyote vikiwa vimekaliwa na watu waliofura mpaka mashavu yao yakavimba, hakika kama angetokea Msomali hapo angegombaniwa kama mpira wa kona.
“Ukiona mtu mzima analia waziwazi mbele za watu, ujue kuna jambo, mimi ndugu zangu, nimehuzunishwa sana na kitendo hiki, nimekerekwa tangu ndani, ningekuwa na uwezo ningeshusha kombora moja na kuipoteza hiyo nchi katika uso wa dunia,” Kyambassa alizungumza.
Ukimya bado ulikuwa ukichukua nafasi kila wakati kati ya jopo lile kwa maana simanzi ilitawala kuliko maamuzi.
Mjadala uliochukua takribani masaa mawili haukuzaa matunda, ilibidi uhairishwe kwanza ili kila mjumbe akatafakari kuhusu hilo, lakini kwa wakati huo iliazimiwa kichwa cha Gwamaka kikahifadhiwe katika hospitali ya jeshi ya Lugalo na shughuli za mazishi zisiwepo mpaka ufumbuzi utakapopatikanaili mpiganaji huyo mahiri azikwe kishujaa. Swala lilibaki ni kumuokoa Jamil kama bado yuko hai na wengine ishirini na watano waliokuwa wakisafiri na meli hiyo.
Ilibidi Brigedia Jeneral Kyambassa akaonane na mkuu wa majeshi ili kuona wao wawili tu wafanyeje. Bado hata walipokutana mjadala kati ya wawili hao haukuwa na muafaka na ikaonekana wazi kuwa shauri hilo la kuingia katika nchi nyingine kwa nguvu linaweza kuleta shida katika uhusiano wa kimataifa kwani aliyewatenda hayo ni kikundi tu Fulani na maamuzi ya mwisho kikatiba kutangaza swala hilo au kulisaoni ni Rais tu mwenye mamlaka.

“Hapana Kyambassa, najua nia yako lakini tusifike huko, tunahitaji amani na majirani zetu, ni kweli usemavyo kuwa hatuwezi kufanikisha hili kidiplomasia kwa sababu nchi yenyewe haina serikali, kila mtu anaamua anavyotaka, lakini tutumie mbinu nyingine, mi nadhani peleka makomandoo wengine wawili wakamalize hiyo kazi,” alimaliza kuzungumza Jenerali Mubah aliyekuwa mkuu wa majeshi mwaka huo, yeye hakukubaliana na uamuzi wa kuingia kijeshi ila akatoa mbinu mbadala ya kufanya.
Brigedia Jenerali Kyambassa akakubaliana na mkuu wake wa kazi, akampigia saluti na kuondoka ofisini hapoi kurudi ofisini kwake ili kuongea na wale aliowaacha ambao walikuwa wanasubiri jibu kutoka kwa mkuu.
Jopo lilirudi tena mezani chini ya Kyambassa, wakapewa mrejesho wa kikao chake na mkuu, kila mmoja alionekana wazi kutoridhiswha na uamuzi huo lakini waliombwa subira ichukue nafasi, swali likawa gumu, nani aende akashike kazi hiyo katika nchi ya Somalia. Jopo likamteua Komandoo mchanga kabisa Daudi wa Daudi akisaidiana na mwingine Sebeki.
Daudi alikuwa ndiyo kwanza anamalizia mafunzo yake huko Cuba na Sebeki alikuwa tayari nchini akiendelea na majukumu mengine ya kitaifa.

§§§§§

Daudi alipokea barua kutoka kwa mkuu wake wa kikosi akitakiwa kufika Somalia moja kwa moja ili kuifanya kazi hiyo, barua ilimpa maelekezo ya nini kilichotokea na nini anachotakiwa kufanya. Kwa kuwa tayari alikwishakuwa mwana wa jeshi hakuwa na la kukatata bali jibu kwa mkuu wake wa mafunzo hapo Havanna, Cuba lilikuwa ni “Yes, Sir!” na siku iliyofuata aliagwa rasmi na kuondoka Havanna kuelekea Mogadishu kuokoa jahazi.

§§§§§
BANDARI YA ZAMANI-MOGADISHU

“Mimi watu wabishi nawapenda sana, hivi wao hawakuwahi jiuliza kuwa kwa nini wenzao wenye nguvu huko Maghalibi wametelekeza meli zao?” Sharon alikuwa akizungumza katika kikao kidogo na vijana wake ndani nya kijichumba kimoja katika bandari ya zamani ya Mogadishu huko Somalia. Tayari walikwishajua kuwa kuna makomandoo wawili kutoka Tanzania wameingia nchini mwao kwa minajili ya kuokoa wenzao.
“Hii ni vita Sharon,” Shalabah alimwambia Sharon kutoka pale alipokuwa ameketi.
“Kama ni vita basi tutapigana mpaka mwisho, wanamkanyaga nyoka mkia, wanafikiri walivyompiga Idd kule Uganda mpaka leo wana uwezo ule? Wameumia, hapa ndipo watakapofia na kuzikwa,” Sharon alikuwa akiongea huku akishikashika kisu chake kikali alichokichomoa kutoka alani mwake.
“Kwa hiyo mkuu unatuambiaje?” kijana mmoja mwembamba mrefu kana kwamba anakula saruji alisimama na kumuuliza Sharon, mgongoni mwake alikuwa na bunduki kubwa AK 47 na kujizungushia mkanda mrefu wa risasi.
“Hakuna linguine, haina haja ya kuwaacha hai, muwasake mkiwapata muwaue hapohapo wala msiniletete mimi,” Sharon alimaliza na kuwataka vijana hao kutawanyika.

Fasendy alishusha sigara yake kutoka kinywani mwake ilimokuwako kama dakika mbili mfululizo, aliitazama kama imesiha lakini ilikuwa bado inafaa kuendelea kuvutwa, akapiga pafu moja na kuteremsha mkono, akaweka kishungi hicho ndani ya kibompoli maalum kwa kazi hiyo. Akashusha pumzi ndefu na kisha akajimininia glasi moja kubwa iliyojaa maji. Akaendelea kutega windo lake palepale, maana alijua wazi kuwa windo hilo litapita tu tena muda si mrefu sana. Pembeni akiwa na bunduki kubwa ya masafa marefu maalum kwa kudunguli lenye kuingia risasi moja tu, aliendelea kusubiri akiwa juu kabisa ya jengo la ghorofa lilikuwa likitazamana na hoteli ya Somali Hotel, katikati ya mji wa Mogadishu. Fasendy alikuwa akimfuatilia komandoo Sebeki tangu siku aliyoingia pale uwanja wa ndege bila ya yeye kujua.
Sebeki hakujua kama Daudi kafika na wapi yupo alkadhalika kwa Daudi nako ilikuwa hivyohivyo, Fasendy alijua ujio wa Sebeki lakini hakuujua wa Daudi, hivyo alimweka kwenye uangalizi wake kwanza ili ajue mtu huyo atafikia wapi na uwezo alionao katika shughuli hiyo.
Sebeki ye akiwa hana hili wala lile, aliendesha maisha kama raia wa kawaida, akifuatili chinichini kujua ni wapi yalipo maficho ya maharamia hao ili asababishe vurugu ambayo itawaachia historia. Kwa ujumla aliwapania sana. Hii ilikuwa ni mbinu yake anapotaka kuvamia sehemu, kujichanganya na wakaazi na kufanya kila kitu pamoja nao lakini akiwa na wazo moja tu kichwani mwake, kulipa kisasi kabla hawajamuwahi kwa maana hapo alijua wazi kuwa ni lazima mmoja amuwahi mwenzake ili shughuli inoge.

Wakati maharamia wameamua kuwa wakimuona basi ni kumuua tu nay eye alijiseme atakayejipendekeza nayeye atahakikisha anatenganisha mwili na roho. Alikuwa akitembea taratibu kwenye vijia vya hotel hiyo. Muda wote Sebeki alikuwamo katika pembe za hotel hiyo akipata chakula cha mchana pa si na wazo lolote. Alipokwishamaliza, aliondoka na kuelekea katika chumba chake, wageni walikuwa ni wengi sana katika hotel hiyo hivyo kulikuwa na nyendo nyingi za hapa na pale.
Fasendy katika angalia angali zake alimuona Sebeki, kama alivyoelekezwa akaweka sawa bunduki yake akaitazamisha kule kunako lengo lake na kutumbukisa jicho lake katika kiona mbali kilichofungwa juu kidogo ya bunduki hiyo, akajaribu kutafuta shabaha lakini ilikuwa ngumu kwa Sebeki alikuwa akipishana na watu mbalimbali. Dole la shahada la mkono wa kulia la Fasendy lilikuwa tayari katika kifyatulio, likiminya kidogo na kuachia mara kadhaa.

“Shiit!” aling’aka pale alipomuona Sebeki akiingia kwenye mlango Fulani na kupotelea humo. Akaiachia ile bunduki yake na kutoka pale alipolala, akachukua sigala yake nyingine na kuiwasha kabla ya kuanza kuivuta kwa fujo.
“Idara ya usalama Tanzania imeishiwa, mpaka inawatuma hawa, mi ilitegemea kumuona Kamanda Amata hapa, na angekuja yule nakwambieni kweli Mogadishu pangekuwa padogo kama kidonge cha pirton,” Fasendy akamwambia kijana mwingine aliyekuwa nae hapo.
“Kwa nini unasema hivo?” yule kijana akauliza.
“Eh, we acha tu, yule shetani, ana mbinu za kijasusi ni hatari, na sijui kapatwa na nini mpaka simuoni kwenye mkasa mkubwa kama huu,”

MOSCOW - URUSI

Maofisa wa jeshi walikuwa wamekusanyika katika makaburi, wakiwa kwenye ibada maalumu ya mazishi ya kiongozi wa juu wa jeshi hilo ijapokuwa alikuwa amestahafu lakini bado alikuwa na heshima yake kubwa katika jeshi la nchi ya Urusi.
Akiwa katika kumalizia ibada hiyo, mkuu wa jeshi la Urusi Bwana Vladimir Kalachinikov alipenyezewa kijibahasha mahali alipokaa, alipokichuku na kusoma juu kilikuwa kimeandikwa kwa lugha ya kiingereza, Confidencial….
 
RIWAYA: HUJUMA 08
MTUNZI: richard MWAMBE


Akiwa anvuta hatua fupifupi akitoka katika eneo hilo la makaburi, Vladimir alikuwa akiifungua bahasha ile huku akihakikisha haionekani na mtu mwingine. Akaanza kuisoma taratibu huku akiendelea na mwendo wake, mlinzi wake alikuwa nyuma kidogo. Colonel Vladmir akasimama ghafla, akatzama saa yake, akashusha mkono chini, akatikisa kichwa kama kuna kitu kilikuwa kinamsumbua kwa ghafla, akaiweka ile bahasha katika mfuko wa koti lake.

Baridi ilikuwa kali sana, theruji iliganda kila mahali, miti, maua, magari, nyumba vyote vilikuwa vyrupe vikipendezesha na hali hiyo hadimu kwa nchi zetu zenye uoto wa kisavanna, hiyo yote ilihashiria kuwa Krismasi imekaribia. Akafika mahali akasimama huku amejishika kiuno, palepale alipo gari yake ikasogea na kusimama mbele yake, akaingia pamoja na mlinzi wake na kumwamuru dereva amfikishe kwa waziri wa ulinzi mara moja.
Mazungumzo yake na mkubwa wake wa kazi ambaye ni waziri wa ulinzi wan chi ya Urusi yalikuwa ni yale yale jinsi ya kuwakomboa wanajeshi wao watano waliokuwa pamoja na wengine wa Tanzania.
“Unajua, Colonel Vladimir, wale jamaa sio wa kuwaongia ovyo kama unavyofikiri, ni wanyama wabaya kuliko wanyama wenyewe,” alizungumza waziri wa Ulinzi akimweleza Colonel Vladimir Kalachinikov.
“Sasa tunafanyaje kiongozi, na unajua hali halisi iliyopo kule ni karibu wiki sasa, watu wetu wanateseka,” alilalamika Vladimir.
“Ok, fanya hivi, chagua mtu mahiri anayeweza kuifanya kazi hii kwa umakini, umtume, mwambie afanye kazi hiyo kwa siri maana akijulikana tu, wale jamaa watafanya kweli,” Waziri wa ulinzi akamaliza hapo. Colonel Vladimir Kalachinikov akasalute na kutoka ofisini hapo.

KAMBI YA JESHI YA SARATOV-URUSI

COLONEL Vladimir Kalachinikov, alikuwa ameketi kitini katika ofisi ndogo anayopenda kuitumia mara kwa mara kama anakuwa na mambo magumu ya kuamua juu ya idara hiyo ya ulinzi. Siku alikuja hapa na ujio wake ulikuwa ghafla hata kwa viongozi wa kambi hiyo ya mambo ya anga na milipuko mikubwa ya jeshi la Urusi inayojulikana kama ‘Eagle Air Force Base au Eagles – 2’.
Alikuwa ameketi kimya akiwa hajui la kufanya, alishika hapa na pale lakini yote hayo yalikuwa ni bure. Baada ya dakika kama kumi hivi, mlango ukafunguliwa na wanajeshi wengie sita wenye vyeo vya juu waliwasili ofisini hapo, wakatoa salute zao na kila mmoja kuchukua kiti chake, wote waliweka kofia zao juu ya meza kwa mtindo wa kupendeza.
“Karibuni sana makamanda, najua mtashangaa sana leo nimewaita mje Saratov badala ya Moscow tuliyoizoea, kuna jambo moja la kuamua kwa pamoja, na hili si jipya ni lile ambalo mnalijua, juu ya ile Manowari ya Tanzania iliyotekwa kule Somalia ikiwa na makobora kumi na mbili ambayo yalikuwa yakija hapa bahari ya Caspian kwa majaribio, ukiachana na hilo, tuna wanajeshi watano wako pale wanashikiliwa na hao Maharamia, sasa kwa sauti yetu moja, tunafanyaje kwenda kuwakomboa watu wetu?” colonel Vladimir alimaliza kuzungumza. Wajumbe wakabaki kimya kwa muda, wakitafakari jambo au mambo Fulani.

“Colonel, mi nafikiri hili swala tulishalizungumza, na tukaona kwa kuwa Tanzania imechukua hatua, basin a tuangalie wanafikia wapi vinginevyo kama watahitaji msaada wetu, ila kwa idara ya usalama Tanzania nawaaamini asilimia 95, wanaweza kazi, labda tungepata ripoti kwanza,” akazungumza mkuu wa jeshi kutoka Tupolev.
“Makamanda, kule hali ni tete sana, komandoo mmoja wa Tanzania amechinjwa, na mwingine hajulikani alipo, ijapokuwa wizara ya ulinzi ya Tanzania imeamua kupeleka wengine wawili, lakini kule ni kule tu,” Colonel Vladimir alitoa majibu kwa kifupi. Baada ya mabishano makali, akasimama mkuu wa kikosi cha wanaanga wa Saratov.
“Mimi sioni haja ya kucheka na hawa watu, watatusumbua mpaka lini? Nchi nying za maghalibi meli zao zimetekwa mpaka sasa wamekaa kimya hakuna jitihada wanazofanya, haya bora wao ni meli za mizigo, sasa hii ya sasa ni ya kijeshi, ina uhusiano mkubwa sana na sisi, hatuna haja ya kucheka nao, tufanye uchunguzi, tuone walipo mi ntatuma ‘tai’wawili tu wanatosha kufagia hao mende wote,” kila mtu katika mkutano huo akacheka baada ya kauli hiyo iliyotoka kwa bwana
Makubaliano yakapitishwa, mchunguzi apelekwe akafanye uchunguzi wa eneo zima, wapi hao jamaa wanajificha na wapi wanafanyia shughuli zao, awape maelekezo kwa vipimo vya ardhini, na baadae wakafanye kazi ya kuwakomboa wenzao. Hilo likapita kwa wajumbe wote. Kikao kikavunjwa na colonel Vladimir akapeleka mapendekezo wizara ya ulinzi ili kuanza mara moja, ijapokuwa hakuwa na uhakika kama litakubaliwa kwani kutuma ndege vita kwenye nchi ya mwenzako kwa sheria za kimataifa ni uvamizi.

MOGADISHU

SEBEKI alikuwa akitoka kuoga, mara tu alipofika katika chumba chake cha kulala akasikia hodi, mlango ukigongwa mara kwa mara, akajiweka tayari, akachukua bastola yake na kuikamata sawia, akauendea mlango na kuufungua, kabla hajamkaribisha aliyegonga akaingia ndani.
“Vipi, mbona unavamia vyumba vya watu?” Sebeki akauliza huku bastola lake likiwa limemtazama mwanadada huyu.
“Usiniue, nina kitu cha kukwambia,” akasema yule msichana.
“Sema haraka, kabla sijabadili mawazo,” Sebeki akamwambia yule dada.
“Ndugu yako, ndugu yako amekamatwa na maharamia, nenda kamsaidie watamuua vibaya,” yule msichana aliongea huku akikatakata maneno.

“Wewe, kama ni maigizo sisi Watanzania ndio tuna chuo cha sanaa hiyo, mi kwetu sina ndugu, na nani aliyekutuma?” Sebeki akamuuliza, akamkamata kwa kono lake moja la kushoto na kumsokomeza bastola mdomoni, “Nafumua ubongo wako, sijaja kucheza huku!” akamalizi kusema na kuitoa ile bastola kinywani mwa yule msichana, akamwacha akitetemeka pale chini. Sebeki aligeuka na kuliendea kabati, yule msichana alitumia nafasi hiyo, alichomoa bastola yake iliyopachikwa juu kabisa mapajani kwa ndani ya nguo, kwa haraka alimlinga Sebeki. Sebeki aliposikia mliowa kiondoa usalama akajua tayari, kumbe alifanya hivyo kwa makusudi mazima, alijirusha upande wa pili wa kitand na ile risasi ikamkosa. Akanyanyuka kama umeme akatuliza guu lake kichwani mwa yule msichana na kumbamizia ukutani, akamnyanyua mzima mzima kwa mikono yake miwili, kifua chake kilichokuwa wazi kilituna na misuri ilidinda kwenye mikono yake, akamrusha yule msichana katika dirisha la kioo na kudondokea nje.
Kelele za alam za magari zilisikika baada ya ule msichana yule kudondoka juu ya gari zilizokuwa maegeshoni. Sebeki akakung’uta mikono yake, na kufungua kabati, akavaa nguo zake haraka haraka na kuchuku bastola zake mbili, akajiandaa kuteremka chini ili aone nini kinaendelea.

Akashuka chini na kuzunguka upande wa pili wa ile hotel, akatazama watu waliokuwa pale wakimsaidia yule msichana aliyedondoka kutoka ghorofa ya tatu, akachukuliwa na kupakiwa kwenye gari moja iliyochoka sana, na wale waliompakia walionekana wazi si wema sana. Sebeki akili ikamcheza, ‘lazima niwafuatilie’ akajisemea, akachomoka pale alipo na kuikimbilia gari yake.
“Nooooooooooo!!!!!!!!!!!!” sauti kali ya mtu ilisikika nyumaya Sebeki umbali kama wa mita mia moja, Sebeki hakuifuatilia kwani hapo palikuwa na mkanganyiko wa watu. Akaingia na kujifungia mlango, mara akasikia kioo cha gari yake kikipigwa kwa ngumi, hakumjua mtu huyo. Sebeki akawasha gari, lo, kumbe maharamia wale walikuwa wametega bomu kwenye injini ya gari ile, na vitendo vyote hivyo Daud aliviona kwani aliwafuatilia toka mbali.

Mlipuko mkubwa ukatokea, anga yote ikawa nyekundu na moshi mzito, ile gari ilinyanyuliwa juu na kugeuzwageuzwa kama kiberiti, ikaanguka na kutua juu ya gari nyingine nazo zikadaka moto, kizaazaa. Kwa kishindo kile, Daudi aliwahi kulala chini, lakini msukumo wa mlipuko ule ukamsukuma na kumbamiza kwenye gari ya jirani, Daud, akajiviringa na kutumbukia kwenye mtaro wa maua na kushuhudia ule moto ukiwaka hewani.
“Kazi imekwisha! Nimeshaingiza pesa,” Fasendy alizungumza na kugeuka akiuacha mlipuko ule ukiendela nyuma yake, akatembea taratibu kuelekea gari iliyoandaliwa kumchukua, akiwa anavuka barabara ndipo akamuona Daud akiwa hajiwezi, anahangaika ndani ya ule mtaro.
“Usipofanya jitihada za kuondoka ndani ya masaa manne nakuua,” Fasendy akamwambia Daud kisha akaingia kwenye gari na kuondoka zake.

§§§§§

DAR ES SALAAM

Tarumbeta maalum ya maazishi ilimaliza kupulizwa, amri ya kijeshi ikatolewan risasi kadhaa zikapigwa hewani huku wanajeshi wengine wakiwa wamepiga salute kama heshima yao ya mwisho kwa wapiganaji hao Sebeki na Gwamaka ambao walikuwa wakizikwa rasmi katika makaburi ya Kinondoni.
Ilikuwa siku ya huzuni sana kwa familia zao, na wapiganaji wote kwa ujumla, hasira na uchungu zilitawala miongoni mwa wale wenye dhamana. Manyunyu ya mvua yalinyurunyuta na kufanya hali ya hewa ya jiji la Dar es salaam kuwa tulivu kama wakazi wenyewe ambao walikuwa wakifiuatilia habari hiyo ama kwenye Tv au redioni, kila mtu alishikwa na hasira.
Siku hiyo gumzo kwenye vyombo vya habari lilikuwa hilo, wahariri wakaandika kwenye tahariri zao,vipiondi vya kuruhusu watu wapige simu navyo vikawa ni shida, kila aliyepiga alilaumu, na alipendekeza hata kama jeshi basi lipelekwe likafanye kazi hiyo kwa mapana yake.

§§§§§

Brigedia Jenerali Kyambassa alifuta machozi, na kuiangalia jopo lake lote, hakuna aliyekuwa na furaha.
“Tumepoteza askari 1600 na 1600 wengine hatujui walipo, nafikiri mmenielewa kwa lugha hiyo, kwa maana komandoo wetu mmoja ni sawa na battalion moja, yaani askari 800, hawa jamaa yumkini kama si mashetani basi wana mbinu za ajabu sana kwenye mashambulizi yao,” Kyambassa aliongea kwa ukali.
Akiwa katika kikao hicho, mara katibu wake akaingia na moja kwa moja akamwendea, akamnpng’oneza kitu.
“Naombeni mnisamehe kidogo makamanda,” Kyambassa akatoka na yule katibu wake wakaingia ofisi ya pili. Kyambassa akakutana na Miranda, katibu muhtasi wa wizara ya ulinzi.
“Karibu Miranda,” akamkaribisha. Miranda akatoa bahasha moja ya serikali na kumkabidhi. Kyambassa alitetemeka akajua hapo tayari hana kazi na hakuna kitu kingine, akaipokea na kuanza kuifungua taratibu huku mikono yake ikitetemeka…
 
RIWAYA: HUJUMA 09
MTUNZI: richard R. MWAMBE


Kyambassa akashusha pumzi ndefu, akamtazama Miranda usoni, Miranda nae alikuwa kakaza macho kwa mzee huyo aliyechafuka kwa vyeo vya kijeshi.
“Ok, Nimeelewa,” akamwambia Miranda kisha akainuka na kurudi kikaoni. Akawakuta wajumbe wakiwa wanabadilishana mawazo, alipoingia wote wakarejesha ukimya. Kyambassa akaenda palepale alipokuwa kwanza, akajiweka sawa na kuwatazama wajumbe wa kikao.
“Ndugu wajumbe, nimepata taarifa sasa hivi ya kiofisi, kusitisha mara moja operesheni yoyote inayohusiana na utagutwaji au uokozi wa watu wetu huko Somalia, hivyo sina budi kusema kikao hiki hakina haja kuwepo mpaka tutakapopata taarifa nyingine, mission aborted,” Brigedia Jenerali Kyambassa akawaambia wajumbe wake. Kikao kikavunjika na kila mtu akarudi kuendelea na majukumu yake ya kulijenga taifa.

§§§§

GINA binti Komba Zinga Zinga alikuwa ametulia tuli katika ofisi ya AGI investment, ndani ya jengo la JM Mall, ghorofa ya tano. Akiwa anaangalia televisheni, ni kipindi kirefu sana alikuwa ndani ya ofisi hiyo bila boss wake kamanda Amata ambaye mara tu alipoachishwa kazi miezi sita iliyopita alijikita kwenye kilimo huko kwao Lindi. Ni mara chache sana alikuwa akija kutembelea ofisi hiyo, hata yeye Gina alikuwa akija mara chache sana, mara nyingi alikuwa akifanya kazi zake za kiofisi katika kituo cha polisi cha kati kwa kuwa yeye alikuwa ni muajiriwa wa jeshi la polisi.

Simu ya ofisini hapo iliunguruma kwa fujo, Gina akaitazama simu hiyo ambayo ni siku nyingi hakuwahi kuitumia, aliitazama na kuinyakuwa pa si kuotea ni wapi intoka, kaiweka sikioni na kusikiliza.
“Hello, Gina!” iliita sauti ya upande wa pili mara tu Gina alipoiweka simu ile sikioni. Ilikuwa ni sauti ngeni hakuwahi kuisikia kabla.
“Ndio mimi, unasemaje?” Gina akajibu.
“Unaongea na idara ya usalama wa taifa kitengo maalumu kisicho na mipaka, TSA,” ile sauti ilimwambia.
“Nakusikiliza,” Gina akajibu.
“Unatakiwa kufika katika ofisi hii kesho saa mbili asubuhi, asante sana,” ile sauti ikatoa agizo na kukata simu bila kusubiri jib u la ndio au hapana. Gina akatahayari kwani alijiuliza ni vipi watu hao wamejua kuwa yuko ofisini hapo mpaka watumie simu ya ofisi kuweza kumpata. Akaitua simu na kuiweka kwenye kikalio chake kisha akaketi kitini, akaitazama ofisi hiyo ambayo ilikuwa bado haijapata mtu wa kukaa kama boss baada ya Amata kutoka. Ilikuwa ni ofisi maalumu ya kitengo cha usalama lakini ikionesha kuwa inafanya kazi za kijamii kumbe ndani yake kuna kikubwa kinachoendelea.

Ni Kamanda Amata aliyempendekeza Gina kuwa kama katibui muhtasi ndani ya ofisi hiyo miaka kadhaa nyuma pindi tu kilipoanzishwa kitengo hicho. Gina alikuwa ni polisi (WP), ambaye kwa kipindi cha miaka mitatu alikuwa akisomea sheria katika chuo kikuu cha Dar es salaam.
Gina alishtushwa na wito huo, ‘Kwa nini asipige Madam S au mtu mwingine ninayemfahamu?’akajiuliza. Kichwani mwake alihisi kuchanganyikiwa, hakujua kama ni wito wa kweli au ni mtego kwake, maana ni siku nyingia hakuingia kwenye kashkash za namna hiyo. Akachukua simu yake ya mkononi na kuimpigia Madam S.
“Yes madam, shikamoo!” alimsabahi.
“Marhaba Gina, mbona kimya sana mwanangu, upo?” madam aliuliza katika simu.
“Nipo mama niende wapi?” Gina alisema, akatulia kidogo na kupisha mazungumzo ya hapa na pale na Madam S huku moyoni akiwa na shaka kumuuliza juu ya ile simu lakini mwishowe akaamua kuuliza.
“Aaaa Gina, we fanya kama simu hiyo ilivyokuelekeza, usiwe na wasiwasi,” Madam alimtoa hofu binti huyo na simu ikakatika. Gina akpigwa na butwaa, ‘kuna nini?’ alijiuliza.

SIKU ILIYOFUATA saa 2 asubuhi
OFISI YA T.S.A

MADAM S alikuwa na shughuli maalumu siku hiyo katika ofisi ya TSA, akiwa nadhifu katika suti yake ya rangi ya udongo, nywele alizotengeneza katika saluni kubwa ya kisasa, alikuwa amesimama mbela ya meza yake kubwa kabisa ya ofisi, mezani hapo kukiwa na kikasha kimoja cheusi kimetulia. Pembeni ya Madam S kulikuwako Chiba, Dr Jasmine, Scoba na Gina. Dr Jasmin alikuwa amesimama akitazamana na Madam S. ukimya ulitawala kati ya wote.
“Dr Jasmine, baada ya kufanya kazi kwa kipindi kirefu na ofisi ya TSA, leo hii ofisi hii, kwa mamlaka iliyopewa na ofisi ya Rais, inakuteua kuwa mmoja wa wanaunda idara hii nyeti, ukiwa kama daktari bila kupoteza taaluma yako, sasa utatambulika kwa utambulisho maalum, TSA 3, utasaidia ofisi hii kwa kila jambo linalohusisha utabibu,” Madam S aliongea maneno hayo huku akimtazama Dr Jasmine aliyekuwa kasimama mbele yake kiukakamavu. Madam S Litoa baeji maalum ya rangi ya dhahabu, yenye nembo ya serikali na chini yake ikipambwa kwa maandishi yenye nakshi ya kuvutia, Tanzania Secrety Agency 04. Madam S hakuishia hapo, alikinyanyua kile kikasha cheusi pale juu ya meza na kukifungua.

“Na hizi ndio zana zako za kazi tangu leo, hutakiwi kuiacha nyuma, unatakiwa uibebe kila uendapo, kwa utii na uangalifu ili itumike pale tu inapobidi,” madam S akamkabidhi kile kikasha, ndani yake kulikuwa na bastola moja ya kisasa na risasi nane, pembeni yake kulikuwa na kiwambo cha sauti kwa ajili ya bastola hiyo. Dr Jasmin akakipokea kikasha hicho na kurudi alipokuwa mwanzo. Dr Jasmine kabla ya kuwa daktari alikuwa ni muajiriwa kati jeshi la kujenga taifa, baada ya kuacha kazi hiyo akajikita katika udaktari zaidi chini ya wizara ya afya akiwa ni muajiriwa, Kamanda Amata alipenda sana kumtumia daktari huyu katika mambo yake hasa yakihitaji taaluma ya kiganga, alimuamini kwa kuwa alikuwa msiri, jasiri na asiye na woga, Madam S alipopewa pendekezo la kumtumia mwanadada huyo hakuwa na kipingamizi na Kamanda, alimruhusu aendelee kumtumia.

“Gina binti Komba Zinga Zinga, baada ya kufanya kazi kwa kipindi kirefu na ofisi ya TSA, leo hii ofisi hii, kwa mamlaka iliyopewa na ofisi ya Rais, inakuteua kuwa mmoja wa wanaounda idara hii nyeti, ukiwa ni muajiriwa wa jeshi la polisi na ofisi hii inalitambua na kuliheshimu hilo, sasa utatambulika kwa utambulisho maalum, TSA 5, utasaidia ofisi hii kwa kila jambo utakalotakiwa kufanya, kuanzia sasa nafasi yako katika jeshi la polisi haitakuwepo tena kwa mujibu wa sheria iliyowekwa juu ya kuunda na kuteua wadau wa ofisi hii,” Madam S vilevile, kama alivyofanya kwa Jasmine alimkabidhi beji maalum Gina iliyoandikwa Tanzania Secrety Agency 05. Kisha akamkabidhi vifaa vile vile kama alivyofanya kwa Dr Jasmine.

Baada ya shughuli hiyo walipiga picha ya pamoja, Madam S, Chiba TSA 02 idara ya teknohama, Scoba TSA 03 idara ya usafirishaji na uokoaji, Dr Jasmin TSA 04 idara ya afya, Gina TSA 05 asiye na idara maalum. Timu ilikuwa imekamilika, lakini bado ofisi hiyo ilikuwa haijapata mtu wa kushika beji ya TSA 01 ambayo mwanzoni ilikuwa na Kamanda Amata.
Tafrija fupi ndani ya idara hiyo nyeti ilikuwa ikiendelea, mara mlio wa chombo cha mawasiliano ukasikika, Madam S akabofya kitufe Fulani na screen maalum iliyo katika ukuta wa ofisi hiyo ikapata uhai, picha iliyoonekana hapo haikuwa nyingine ni ya waziri wa ulinzi.
“Ndiyo mheshimiwa,” Madam S aliitika.
“Nakuhitaji ofisini kwangu mara moja, bila kuchekewa,” Waziri wa ulinzi alimwambia Madam S kupitia chombo kile.
 
RIWAYA: HUJUMA 10
MTUNZI: richard R. MWAMBE

§§§§

“Madam S, nimekuita mara moja kuna dharula ambayo tunahitaji ofisi yako iweze kutusaidia,” Waziri wa ulinzi alikuwa akimwambia maneno hayo Madam S aliyekuwa ameketi kitini, akisikiliza neno moja baada ya jingine. Mheshimiwa waziri akaendelea, “Manowari yetu kubwa Kirov Class, imetekwa Somalia na maharamia, leo ni wiki ya tatu, tumepelea makomandoo lakini wawili wameuawa kikatili na wawili hatujui walipoa, ndani ya manowari hiyo kulikuwa na wanajeshi 25 Watanzania isihirini na Warusi watano pamoja na makombora makubwa kumi na mawili, tunahitaji ufumbuzi wa jambo hili, haraka iwezekanavyo”.
Madam S aliendelea kumtazama waziri wa Ulinzi hata baada ya kumaliza kuongea, alitamani kumuuliza jambo lakini aliamua kuacha.
“Sawa nimekusikia, lakini unajua wazi kuwa ofisi yangu imepungukiwa tena imepungukiwa nguvu kubwa sana, unafikiri nitawezaje kulifanya hili kwa sasa? Kama mmetuma makomandoo na wawili wameuawa, we unaionaje hiyo kazi?” madam S akauliza.

“Ni kazi ngumu inayohitaji umakini sana,” akajibu waziri.
“Na unafikiri mtu makini ni nani wa kuweza kuikamilisha kazi hiyo?” Madam akauliza. Waziri wa ulinzi akamkazia macho Madam, akamtazama kwa hasira, maana alielewa kile anachokizungumza, kabla hajaongea kitu Madam S alikuwa amekwishanyanyuka na kutoka kwenye ofisi ile. Kichwa kilizunguka, hakujua nini cha kufanya, ugumu wa kazi aliyopewa na serikali aliuona ukimwelemea waziwazi, akitazama kwenye jopo lake hakuna amtu wa makabiliano ya ana kwa ana na mwenye wepesi na akili za haraka kama Kamanda Amata ambaye sasa hayupo kazini.
Alirudi ofisini akawakuta vijana wake bado wanagalipo wakiendelea na viburudisho vilivyo hapo. Akawaita wote mbele ya meza yake na kuwaketisha.
Kabla hajaongea kitu alijiinamia kwanza kwa dakika kadhaa akifikiria jambo.
“Tuna kazi ya kufanya Somalia, kuirudisha manowari iliyotekwa na wanajeshi waliopotea,” madam aliwaambia, wote wakatazamana, na minong’ono ya hapa na pale ikatawala.

“Samahani Madam, hapa katika hili tusifanye masihara hata kidogo, hii kazi ni ngumu sana na kiukweli bila Kamanda Amata tumefeli,” Gina alieleza na kuungwa mkono na wote waliopo katika kikao hicho.
“Kumbukeni Kamanda hayupo kazini, hivyo tunapoteza muda sana kumzungumzia kuliko kujipanga,” Madam S aliwaeleza na kuwaacha hapo yeye akatoka nje ya ofisi.
“….Siwezi kufanya kazi bila Kamanda Amata, we mwenyewe unajua uzito wa kazi,” ilikuwa sauti ya Madam S alipokuwa akiongea kwa simu, hakuna aliyejua ni nani anayebishana nae humo simuni.
Baada ya kama dakika kumi na tano hivi, Madam S alirudi ofisini akiwa katika hali tofauti na mwanzo, akaketi kitini. Akavuta simu yake na kuipiga namba Fulani kisha, akatulia kusikiliza.
“Scoba, chukua helkopta, sasa hivi kamlete Kamanda Amata, Gina atakuongoza anajua ni wapi alipo, nawasubiri hapa,” Madam alimaliza. Scoba na Gina wakachomoka, na kuingia garini, safari ilikuwa ni katika kituo cha polisi Oyserbay ambapo helkopta yao ya ofisi ilikuwa anaegeshwa hapo, baada ya kusainiana na ofisa anayehusika, Scoba na Gina walioondoka.

4… nangumbu – Lindi Vijijini

WATOTO wa shule ya msingi walisikika wakipiga kelele za woga, wakikimbilia madarasani na wengine porini. Waalimu wao walitoka nje kuangalia watoto hao wanakimbilia nini. Helkopta kubwa lilikuwa likitua katika uwanja wa shule hiyo.
Nyumba kubwa iliyozungukwa na maua mengi ya kupendeza, ilikuwa mbele yao, gina aliielekea mpaka mlngoni na kugonga kengele. Kamanda Amata akaibuka mlangoni na kuwatazama wawili hao.
“Karibuni sana,” akawakaribisha.
“Kamanda sisi sio wa kukaa,” Scoba akamwambia.
“Hata kama sio wa kukaa, lakini Gina hapa ni nyumbani kwake hawezi kuingia na kutoka,” Kamanda akawaambia huku akitoa miwani yake usoni, shati lake lilionesha wazi kuwa alikua ni mtu katoka shambani muda si mrefu.
“Kamanda Amata, hali ya mama yako ni mbaya sana, unatakiwa kuja nyumbani kumsaidia,” Gina alimwambia Kamanda kama alivyoagizwa na Madam S.
“Najua, na nanjua kuwa hali yake mbaya lakini kwa sasa mwacheni afe, sina msaada,” Kamanda Amata alijibu huku akiipachika tena miwani yake usoni.

“Kamanda, hebu fikiri mara mbili juu ya hili, mpaka kukufuata na usafiri maana yake ni kuwa tuondoke sasa hivi,” Scoba alikazia.
“Haitatokea, nimebanwa sana na shughuli za kilimo, mahindi yangu yananihitaji, mikorosho nayo ndiyo hiyo hapo, vyote hivyo vinanisubiri, mifugo yangu hata sina mtu wa kuniangalizia nikitoka,” Kamanda akawaambia. Mazungumzo yalikuwa magumu sana kati yao na Kamanda Amata, haikuwa rahisi kwa Kamanda kukubali wito huo.
“Ninyi nani aliyewatuma, mpaka mnapoteza mafuta ya hilo chopa, kulileta huku porini kwetu?” Amata akauliza.
“Tumetumwa na ofisi, bibi kachanganyikiwaanakuhitaji nyumbani,” Scoba akasisitiza. Gina wakati huo alikuwa ameingia ndani na kuwaacha wawili hao wakiwa bado na mvutano.
“Sikiliza Scoba, nenda kamwambie Bibi, siwezi kuja hata kwa mkinivuta kwa bulldoza,” kamanda Amata akamaliza mazungumzo yake akanyanyuka na kuondoka zake. Akamtazama Scoba palepale alipomuacha yeye akapanda pawatila yake na kuingia kazini.

§§§§

Madam S, aliinama mezani, alionekana wazi kuchanganyikiwa kwa jibu alilolipata kutoka kwa Gina na Scoba.
“Amekataa kabisa amesema hawezi kuja kwa lolote,” Gina akamaliza.
“Hata wewe Gina umeshindwa kumbembeleza Kamanda aje, unaniangusha Gina, umeingia kitengo cha ujasusi lazima ujue sometime kutumia body language,” Madam S alimwambia Gina. Ukimya ukatawala kati yao, Madam S hakuwa na la kusema, akanyanyuka na kutoka nje ya ofisi, akachukua gari yake na kuondoka.
Breki yake ya kwanza ilikuwa mbele ya ofisi ya wizara ya ulinzi, moja kwa moja akaingia katikia ofisi yam zee huyo anyependa kuitwa mheshimiwa pa si kuwajibika sawasawa kwa Watanzania.
“Ndiyo Madam, najua umerudi na jibu zuri kinywani mwako,” mheshimiwa waziri akasema.

“Hapana, hapa nimekuja kukwambia kuwa ofisi yangu haiwezi kiufanya kazi uliyonipa kwani uwezo tulionao ni mdogo sana kiutendaji mpaka tujipange nah ii itachukua miaka mingine sita,” Madam S akamwambia waziri wa ulinzi. Alipomtazama usoni waziri huyo alionekana kuvimba sura kwa hasira.
“Madam S, wizara ikishakupa kazi imekupa, utajipanga vipi utajua wewe, sasa habari za kunambia kuwa hauko tayari mimi sizielewi, unajua kabisa kuwa hili tayari limeshaiweka ofisi yangu katika hali ya sintofahamu, Mheshimiwa Rais atanielewaje wakati nimemhakikishia kuwa kila kitu kitakuwa sawa?” Waziri wa ulinzi akaongea kwa ukali, huku akiwa amesimama, kauma meno yake na kupigapiga ngumi mezani kwake.

Madam S naye alipoona hayo akawa amesimama akimtazama baba huyo aliyekuwa akipiga kelele bila mpangilio.
“Sikia, mheshimiwa, ulimpomfukuza kazi Kamanda Amata ulitegemea nini?” Madam S akamwuliza waziri. Kimya kifupi kikatawala kati yao.
“Kwa hiyo unasemaje?” waziri akamwuliza Madam S.
“Nasema kazi haiwezekani, nenda kamwambie na mheshimiwa Rais hivyohivyo kuwa TSA haiwezo kufanya kazi hii mpaka miaka sita ijayo, watakapomtengeneza TSA 1 mwingine,” Madam S akamaliza na kugeuka kuondoka zake.
“Madam,” waziri akaita, Madam S akasimama akageuka kumtazama, “Kibarua chako kipo mashakani,” akamwambia, huku akiwa ameuma meno kwa hasira. Madam S akatoka na kubamiza mlango nyumba yake.
Hali ilikuwa tete kwa waziri wa ulinzi, aligundua kosa kubwa sana alilofanya miezi sita nyuma katika mkasa ambao uliandikwa kama riwaya na kupewa jina la Julai 7. Aliwaza na kuwazua hakuna jibu alilolipata juu ya hilo, alihisi uzee ukimjia kwa kasi, hasira zilimtawala, akatoka ofisini kwake mara moja na kuondoka zake.

§§§§

Kikao cha baraza la usalama la taifa kiliitishwa kwa dharula katika ofisi maalumu ndani ya Ikulu ya Dar es salaam, kikihudhuriwa na wadau wa juu kabisa wa usalama. Katika ofisi hiyo ndogo inyojulikana kama Mraba wa Kilimanjaro, hoja ilikuwa nzito juu ya hatima ya wapiganaji wa Tanzania waliokuwa huko Somalia, hakukuwa na habari kabisa juu ya wapi walipohifadhiwa, au kufichwa, wazima au wameuawa, hali ilikuwa tete katika ya wadau hao wa juu kabisa wa usalama ambao hatima ya usalama wa Watanzania ipo juu yao. Mwanamke pekee katika jopo hilo Madam S alikuwa akiwasikiliza kwa makini na akipinga kabisa swala la idara yake kuingizwa katika sakata hilo hali hana nguvu ya kutosha, mwanamke alitunisha misuli ndani ya ofisi hiyo mpaka kila mmoja akabaki kimya. Baada ya mazungumzo hayo lawama zote zikarudi kwa Waziri wa ulinzi kwa kuwa yeye ndiye aliyeng’ang’ania Kamanda Amata aachishwe kazi kwa kile kilichodaiwa utovu wa nidhamu.
“Hatuwezi kufanya kazi hii bila ya Kamanda Amata,” akasema makamu wa Rais aliyekuwa akiongoza jopo hilo.

“Hapo mheshimiwa nakuunga mkono, hatukufanya jambo la busara kabisa kumtoa kazini Kamanda Amata, na kwa sababu hiyo ndiyo maana hata sasa tunakutana hapa ambapo si kawaida yetu, kwa nini Kamanda Amata asirudishwe kazini?” Mkuu wa majeshi aliliambia jopo na kuungwa mkono na jopo zima. Waziri wa ulinzi alikuwa kimya, hakuongea kabisa alikuwa akiwasikiliza wajumbe hao.
“Mimi nahitaji Kamanda arudi kazini, hapo ndiyo nitaifanya kazi hii kwa ufanisi wa hali ya juu,” Madam S akalieleza jopo. Uamuzi ukapitishwa wa kamanda Amata kurudishwa kazini, ikaandikwa barua na kusainiwa na jopo zima kama ilivyokuwa mwanzo, akakabidhiwa waziri wa ulinzi ahakikishe Kamanda Amata anarudi kazini.
“Mheshimiwa waziri wa ulinzi, lazima tu ukubali kuwa umekata tawi ulilokalia,” Madam S alitamka maneno hayo na kumuudhi sana waziri wa ulinzi.
 
Asante sana don. Usionje kimya wengine humu wanasoma kimya kimya. Watu wakinogewa wata comment tu. Hadithi humu kwa sasa zipo nyingi
 
RIWAYA: HUJUMA 11
MTUNZI: richard MWAMBE


§§§§

Ugeni mpya ulifika nyumbani kwa Kamanda Amata siku ya pili baada ya Gina na Scoba, waziri wa ulinzi akifuatana na ujumbe wa watu watatu. Kamanda Amata alikuwa akiendelea na shughuli zake za shamba.
“Salama Kamanda?” sauti hiyo ikamshtua Amata kutoka katika kazi iliyoiteka akili yake, akaacha na kugeuka nyuma, akakutana uso kwa uso na waziri wa ulinzi aliyekuwa na bahasha mkononi mwake. Mheshimiwa waziri akavuta hatua mpaka aliposimama Kamanda Amata.
“Samahani sana Kamanda kwa yaliyotokea, yaliyopita si ndwele tugange yajayo,” waziri wa ulinzi akamwambia Amata huku akiwa amekwishamfikiapale alipo, akamkabidhi ile bahasha. Kamanda akaipokea na kuifungua bila kusema chochote, akaisoma, barua ya kumtaka kurudi kazini. Alipokwishakumaliza kusoma, akainuan uso wake na kumtazama mzee huyo.
“Asante, nitawajibu kwa maandishi,” kamanda akajibu na kuitia mfukoni ile karatasi kisha akapanda pawatila na kupotelea shambani. Waziri wa ulinzi na wapambe wake wakabaki wakitazamana, hakuna jipya, waliamua kuondoaka zao.

“Taifa linautambua sana mchango wako katika mambo mbalimbali, umepigania haki, uliyaweka hatarini maisha yako kwa ajili ya Watanzania. Kumbuka ubinaadamu upo, hivyo serikali inakuomba kurudi kazini na kusaidia tena taifa lako ulipendalo, Watanzania wanahitaji akili, nguvu, umakini na utayari wako…”
Ilikuwa sehemu ya barua aliyoandikiwa kutoka baraza la usalama la taifa, akaikunja tena ile karatasi na kuirudisha mfukoni. Akajaribu kufikiria mateso ya wapiganaji wa Tanzania ambao wapo huko Somalia kama wanayapata yatakuwa makali kiasi gani, moyo wake ukamuuma sana, akamfikiria madam S jinsi atakavyokuwa anahangaika katika hilo, Kamanda akaangusha chozi, akakata kauli na kurudi nyumbani kwake.
“Nasafiri mara moja, naomba muangalie shamba na mambo mengine, nitarudi labda baada ya wiki moja au mbili,” Kamanda akawaambia watu anaoishi nao wakiwemo wafanyakazi wake wa mazingira, akamshika mkono binti yake Jenny.
“Jenny, nitakuona nikirudi, sawa mrembo wangu?” Kamanda akaagana na binti yake. Jenny akaitikia kwa kutikisa kichwa.
Baada ya kuweka sawa zana zake chache muhimu katika begi lake, Kamanda Amata akaingia ndani ya Land Rover Defender, gari ya kazi na kuelekea mjini.

§§§§

Ilikuwa ni siku nzito sana, Madam S alikuwa na uchovu wa ajabu, aliegesha gari yake katika maegesho ya nyumba yake huko Masaki na kuingia ndani kupumzika, kabla hajawasha taa akiwa anaelekeza mkono wake katika switch, taa ya sebuleni ikawaka yenyewe, akashtuka na kutazama huku na huko kwa hadhari kubwa.
“We unafanya nini hapa?” akatamka baada ya kumuona Kamanda Amata akiwa ameketi kochini na mbele yake kwenye kijimeza kulikuwa na pombe kali aliyokuwa akiigida kwa madaha.
“Nimekuja kwa mama yangu,” Kamanda akamjibu Madam S. madam S akamtazama kijana huyu, kisha akavuta hatua chache na kujitupa kwenye kiti. Hakushangaa kwa kamanda Amata kuwa ndani ya nyum,ba hiyo kwani anamju wazi utundu wake wa kucheza na vitasa vya kila aina na kuingia bila uharibifu.
“Karibu konyagi,” Kamanda akamkaribisha Madam S, akamsogezea glass iliyojaa nusu.

“Asante Kamanda,” Madam alijibu huku akiinyanyua glass na kupiga funda moja la nguvu.
“Kamanda, hali ni tete hapa, mi nafurahi umekuja, na nilijua utakuja, ila umenyanyasa sana yule mzee. Kwa ujumla tumeshapoteza makomandoo wawili na wawili haijulikani walipo, ukiachana na wanajeshi wa maji ishirini wa Tanzania na watano wa Urusi pamoja na meli yetu kubwa ya kivita ililiyokuwa na makombora ya masafa marefu na uzito wa hali ya juu kumi na mbili, Mama amechanganyikiwa kupoteza mali zote hizo,” Madam S alimweleza Kamanda Amata.
“Hujuma?” Kamanda akatupa swali.
“Sijajua,” Madam S akajibu.
“Hujuma, hiyo ni hujuma, ina maana hao maharamia na washirika wao wanajuaje serikali inapotaka kutuma watu kwenda kule? Mpaka wawaue kirahisi namna hiyo? Hujuma, Madam kubali kataa hiyo ni hujuma,” Kamanda alisisitiza juu ya hilo.
“Kamanda, sikuwahi kufikiria hilo, sasa unaanza kunipa mwanga, ila mheshimiwa umemnyanyasa sana, au ni yeye?” Madam aliuliza.
“Sijui labda ni wewe Madam, maana ukiwapa siri wale wanakupa pesa ya maana sana kuliko unavyofikiria,” Kamanda akajibu, akainua glass yake na kupiga funda moja.

“Mi nimekuja kwa heshima yako, na kwa familia za wale wa liotekwa, lakini sio kwa sababu ya waziri wa ulinzi wala nani ni hayo mawili tu,” Kamanda akajibu, na kunyanyuka, “Mi naondoka tutaonana kesho,” akasema huku akivuta hatua kuuendea mlango.
“Kamanda subiri TSA 5 atakuja kukuchukua, huwezi kwenda peke yak oleo,” Madam S akamwambia. Kamanda akageuka na kurudi kama hatua mbili akajishika kiuno na kumtazama Madam.
“TSA 5?!” akauliza kwa mshangao.
“Ndiyo, TSA 5, tuko namba tano sasa ila moja bado ilibaki wazi mpaka sasa, imeniwia ngumu sana kuteua namba hizo ukizingatia nilikuwa na Chiba tu,” Madam akamwambia.
“Ok, 3 ni nani? 4 ni nani na 5 ni nani?” kauliza Amata.
“Scoba TSA 03 idara ya usafirishaji na uokoaji, Dr Jasmin TSA 04 idara ya afya, Gina TSA 05 asiye na idara maalum,” akajibu Madam S, “nimewatawadha leo kwa mujibu wa sheria iliyowekwa ya kuunda na kuteua juu ya idara hii ya ujasusi,” akaongeza.
Kamanda Amata akampongeza Madam kwa kumpa mkono, “Hata kama ungenishirikisha hao ndio ningekupendekezea kwa sasa, timu imetimia,” Akasema Kamanda.

§§§§§

Shalabah, alikuwa ametulia tuli juu ya kiti na kutazama kwa makini skrini iliyojitokeza mbele yake, Mr Lonely alikuwa akiongea na kijana huyo wa juu kabisa katika timu yake, akimpa hili na lile. Mr Lonely, alikuwa ni mtu asiyebishiwa, ila unaruhusuwa kumwuliza, na kauliu yake ni ya mwisho, akisema Fulani auawe basi auawe hakuna linguine. Yeye alikuwa akiishi ndani ya jumba lake la fahari sana lililojengwa baharini, chini, sio kila mtu alikuwa anaweza kuongea na huyo bwana, na hakun a aliyejua kama bwana huyo ana mke na watoto au hana kwani utaambia amesafiri lakini hukuwahi kumuona akitooka na gari ndani ya jumba hilo lakini amesafiri, kwa hiyo hakuna aliyeamini kama bwana huyo ni mtu wa kweli au wa kufikirika, lakini sauti yake ilisikika na picha yake ilionekana uingiapo sebuleni hapo kuzuingumza naye.
“Hakikisha, yeyote anayekuja kufuatilia habari hii anauawa mara moja, mmefanya vizuri kuwauwa wale wawili, na hao wengine hakikisheni wanapata mateso mpaka wanakufa, pia watupatie na siri nyingine, kwani biashara ya safari hii ina tija sana na najua hawatakubali kuacha hivi hivi lakini we endelea kupanga vijana kwani mauzo ya bidhaa hii ni siku kumi zijazo na hao watu wao tutawazika wazimawazima,” maneno mazito ya Mr Lonely yalipenya katika ngoma za masikio ya Shalabah.
“Sawa, Lonely,” akajibu Shalabah.

“Hakikisha macho yote kuanzia uwanja wa ndege mpaka mahotelini yanafanya kazi sawasawa, jicho letu lililoko Tanzania linafanya vizuri, lazima tuitazame dunia kama tunavytokitazama kiganja cha mkono, kwa heri,” Lonely alamaliza kuongea, kabla Shalabah hajajibu chochote, ile skrini pale ukutani ikarudi taratibu chini mahali inapojihifadhi na kopo lenye maua ya kunukia likachukua nafasi yake.
Shalabah alipoliacha jumba hilo, moja kwa moja alifika katika ofisi yao nyingine, ofisi ya siri ambapo alimkuta Sharoni na vijana wengine, akawapa maagizo yote yaliyotolewa na Mr Lonely na kumpa kazi Sharon ya kuimarisha ulinzi mpaka biashara ile itakapofanyika.
“Kwani we una wasiwasi kuwa watatuma tena mtu? Hiyo sahau, tumeshaua wawili na tunao mkononi ishirini na saba, haji mtu hapa, serekali isiyo na akili itafanya hilo,” Sharon akamwambia Shalabah, wote wakacheka na kisha wakatoka eneo hilo kuelekea bandari ya zamani ambako kwa ujumla mambo yote yalikuwa hapo.

5..Dar es salaam

“Hebu nambieni kwanza juu ya hali ya usalama wa vijana wetu huko Somalia,” Mkuu wan chi ambaye dhamana ya taifa lote na watu wake lipo mkononi mwake alimuuliza waziri wa ulinzi aliyekuwa mbele yake, ukimya ukachukua nafasi, waziri hakujibu lolote, “Unajua kupoteza makomandoo wawili ni hasara sana kwa jeshi letu, wakati mnajua kuwa wapo na zipo idara nyeti za kuifanya kazi hiyo na siyo wanajeshi kwa kuwa wao wako kwa ajili ya kazi kubwa zaidi,” akaongeza. Waziri wa ulinzi alikuwa akiona muda hauendi kabisa kwa maswali aliyokuwa akibanwa na mkuu huyo.
“Ah… eh…. Mh…. Unajua mheshimiwa, tulighafirika kidogo na kuwapeleka wale watu tukijua kuwa wataifanya kazi hiyo vizuri kutokana nja kwamba adui tuliyekuwa tukimkabili alikuwa kivita zaidi,” akajibu waziri.
“Ni uzembe, lazima ukubali ni uzembe na hao mlioshirikiana juu ya hilo wote ni wazembe na mtawajibika kwa hili, naomba uende, sasa nitaamua mimi la kufanya juu ya hilo inaonekana wewe umeshindwa kama waziri,” akamaliza kuongea Mkuu wa nchi, amiri jeshi mkuu.

§§§§

“Kwa nini mpaka sasa, wapiganaji wetu wanapoteza maisha na we upo hapa unatazama?” swali kutoka kwa mkuu wan chi lilitua katika ngoma ya sikio ya Madam S.
“Sikuwa na nguvu ya kutosha kukabiliana na swala hilo mkuu,” Madam S alijibu.
“Sijakuelewa, hukuwa na nguvu kivipi na wakati mwingine ulikuwa na nguvu kivipi?” akaulizwa tena.
“Mheshimiwa, wewe unajua kitengo chetu ndio kimeanza miaka mitano hii na mpaka sasa nilikuwa na watu wawili tu yaani TSA 1 na 2, kutokana na sakata la Julai 7 la kupambana na magaidi lilipokamilika TSA 1 aliachishwa kazi kwa ajili ya utovu wa nidhamu, nikabaki na TSA 2, ndio nikakuandikia barua ya kuomba kuongeza nguvu kikosini kwangu, ukanikubalia, nimeongeza juzi watu wa watatu, lakini bado sina TSA 1, nitafanyeje?” Madam S akajibu kinagaubaga na kumuona wazi mkuu wa nchui akikodoa macho kumshangaa.

“Nani anayeweza kumuondoa kazini mtu wa kitengo cha ujasusi? Kile kitengo kiko chini yaofisi yangu ni mimi tu ninayeweza kumuondoa mtu au kumuingiza mtu na si mtu awaye yote, sasa popote alipo TSA 1 arudi kazini kwa amri yangu, na mara moja akabidhiwe hiyo kazi aende akaokoe jahazi,” Mkuu wan chi aliongea kwa hasira.
“Sawa mkuu, TSA 1 amekwisharejea kazini,” Madam S akajibu.
“Sawa, umefanya vyema, na nitafurahi zaidi ukinambia kuwa usiku wa leo atakuwa tayari ameondoka, kama hakuna ndege basi ya serikali itampeleka, asante, nasubiri jibu lako,” Mkuu wan chi akamaliza kuongea na kuagana na Madam S.
Madam S akaiacha ofisi hiyo na kupita kwenye korido ndefu iliyomtolea kwenye sebule ya kupumzikia wageni, akapita mlango mkubwa na kuziteremka ngazi harakaharaka, akaingia kwenye gari yake na kuondoka katika viwanja vya Ikulu.

§§§§§

Gina alikuwa ameketi ndani ya ofisi aliyoizoea, macho yote yakiwa kwenye luninga akitazama habari za kimataifa kupitia channel ya Al-Jazeera. Akiwa hana hili wala lile, mlango wa ofisi ukafunguliwa bila hodi, mtu asiyemtegemea akaingia ndani.
“Kamanda!” akajikuta akitamka.
“Ndiyo mimi hakuna mwingine,” Kamanda Amata akajibu na kuvuta kiti chake, akaketi. Gina
 
RIWAYA: HUJUMA 12
MTUNZI: richard MWAMBE


JNIA – saa 2:00 usiku

MADAM S alimpa mkono Kamanda Amata alipokuwa uwanja wa ndege wa kimataifa Dar es salaam tayari kwa safari.
“Kila la kheri Kamanda, nakuaminia sana,” Madam alimwambia. Kamanda Amata akasaluti kisha akamuendea Gina na kumbusu.
“Nahitaji urudi Kamanda, urudi na pua yako,” Gina alimwambia Kamanda.
“Usijali, nitarudi na kila kitu changu,” Kamanda akaagana na wote pale uwanja wa ndege kisha akaingia katika chumba cha wasafiri tayari kwa safari.
“Habari ya jioni,” mtu mmoja alimsalimu Kamanda Amata walipokuwa ndani ya chumba cha wasafiri.
“Salama kabisa,” Kamanda akajibu na kuendelea kusoma gazeti lililo mkononi mwake.

“Unaelekea wapi?” yule mtu akamwuliza Kamanda Amata. Kamanda Amata akamtazama kuanzi kiatu alichovaa mpaka nywele, ndipo alipomgundua mtu huyo kwa mbali ana asili ya watu kama Wamburu.
“Naenda Arusha, wewe je?” Kamanda akamwuliza.
“Naenda Moqdishu,” yule mtu akajibu, akajikohoza na kuendelea, “Sasa unaenda Arusha kwa Ethiopia Airline!” akaongeza.
“Hilo halikuhusu, nina uwezo wa kwenda Morogoro kwa British Airways,” kamanda alipomaliza kuongea hayo, tayari mlango ulikuwa wazi na abiria wakaanza kuingia ndegeni.

§§§§§

Yule mtu aliyekuwa akiongea na Amata pale uwanja wa ndege alikuwa mara kwa mara akienda maliwato ndani ya ndege hiyo. Kamanda Amata alikuwa ameketi siti za mbele ilihali yule bwana alikuwa siti za nyuma, kamanda Amata aliweza kumuona vizuri kwa kupitia miwani yake ambayo iliweza kumuonesha vinavyotokea nyuma yake.
Baada ya kumtazama kama mara nne akienda maliwato, mara hii Kamanda Amata akainuka kutoka katika kiti chake na kuelekea upande wa nyuma wa ndege hiyo. Moja kwa moja akaenda mpaka katika mlango wa maliwato, akasimama kusikiliza kama mtu huyo anaongea chochote, akasikia lakini kwa sauti ya chini sana kutokana na mlango huo jinsi ulivyotengenezwa, kamanda Amata akachomoa kifaa kidogo chenye mfano wa koni akakiegesha hapo mlango na kusikiliza kila kinachoongelewa, alipoona kuwa mtu huyo anakaribia kumaliza mazungumzo Amata akashika kitasa cha mlango huo na kukifungua kwa nguvu kwa kukivunja, akausukuma mlango ndani na kuingia kisha akaufunga nyuma yake.

Ndani ya choo hicho akakutana na yule bwana, Kamanda Amata akamtazama kwa jicho baya.
“Nani ulikuwa unampa habari zangu?” akamwuliza.
“Hapana, mimi nilikuwa naongea na ndugu zangu,” akajibu huku akitetemeka.
“Ndugu zako ndio unawatajia jina langu?” Kamanda Amata akauliza, kisha akatazama kifaa alichokuwa anatumia kuwasiliana na jamaa hao, kilikuwa ni kifaa cha ajabu sana kidogo kwa mfano wa kiberiti, alikiunganisha kwa ufundi sana kupitia nyaya ndogo zinazosafirisha mawasiliano ndani ya ndege hiyo. Kamanda Amata akakitazama na kuzing’oa zile nyaya zake pale alipoziunganisha na zile zilizo kwenye mfumo wa ndege hiyo.
Alipohakikisha anacho kile kidubwasha mkononi mwake, akamwamuru yule jamaa kutoka ndani ya choo kile.

“Sasa utakwenda kukaa pale nilipokaa mimi na mimi nitakaa hapa ulipokaa wewe,” Kamanda alimwambia yule jamaa.
“Ah, siwezi kukaa kule kwani mi sti yangu ni hii hii,” yule bwana alilalama. Kamanda Amata hakujibu, alimtandika kofi moja kali sana, mpaka yule bwana akakaa chini. Wahudumu wa ndege wakamfuata Kamanda kumwambia kuwa analolifanya haliruhusiwi ndani ya usafiri huo, wakamwomba akae kwenye siti yake. Kamanda Amata akawaonesha kitambulisho chake halisi. Hapo wakamwacha afanye atakalo, kwa kuwa huyo ni mtu wa kuaminika. Yule mtu akaketi kwenye siti ya Amata na Amata akakaa kwenye siti yake, sasa alikuwa akimwangalia kwa mbele.
Baada ya kutua Nairobi, yule bwana aligeuka nyuma kwa woga kumtazama Amata, hakumwona.
Kamanda Amata alishuka katika uwanja wa ndege wa Jommo Kenyatta bila yule bwana kujua. Baada ya kufanyiwa itifaki za kiusalama, hakuchukua muda mrefu alikwea ndege shirika la Dubai Airline na kuelekea Mogadishu, tayari kabisa kuanza kibarua alichotumwa.

MOGADISHU – SOMALIA
Uwanja wa ndege wa ADEN ADDE

SHALABAH alikunja sura baada ya kupata taarifa kuwa Kamanda Amata hayupo katika ndege waliyoitarajia. Alionekana wazi kupumua kwa nguvu, akiwaza jambo.
“Shalabah, vipi?” Sharon akamuuliza.
“Huyo wanaemwita Kamanda Amata hayupo katika ndege tangu watoke Nairobi,” Shalabah akamwambia Sharon. Sharona naye akaonekana wazi kupigwa butwaa.
“Atakuwa kaamua kukatisha safari?” Sharon akauliza.
“Hapana, huyu anataka kutuchezea mchezo, nina uhakika yuko humohumo, kajificha sehemu, hebu ongea na watu wetu upande wa cargo kuwa wanaangalia vizuri, bado saa moja ndege itatua,” Shalabah akatoa maelekezo na Sharon akawapanga upya watu wake.

“Vipi?” Fasendy akamwuliza Sharon, pindi alipotoka pembeni kuvuta sigara.
Fasendy alikodiwa katika mpango huo ili kummaliza Kamnda Amata palepale uwanja wa ndege kwa kumdungua, alikuwa tayari kajipanga kwa hilo, alichoambiwa yeye ni kuwa atapewa maelekezo tu ya jinsi mtu huyo alivyo.

§§§§

NDEGE ya Dubai Airline ilikanyaga ardhi ya Mogadishu ikiitangulia ile ya Ethiopia ambayo maharamia hao walikuwa wakiisubiri kwani walishaambiwa kuwa Kamnda yuko humo, na walitahadharishwa kuhakikisha haingii mjini kwani ni mtu hatari sana. Mpaka dakika hiyo walikwishakubaliana na hilo kuwa mara hii wanapambana na mtu makini mwenye akili za ziada kwa mchezo tu aliowachezea kwenye ndege hiyo.
Kamanda Amata alikiacha kiti chake, akaweka kijibegi chake mgongoni na taratibu kuziteremka ngazi za ndege hiyo na kwa mara ya kwanza aliweka unyanyo wake katika ardhi ya Mogadishu, uwanja wa ndege wa Aden Adde. Akiwa na miwani yake usoni aliweza kuona vyema kabisa katika mianga ya taa kali za umeme iliyokuwa ikimulika eneo hilo, akavuta hatua ndefundefu na kuelekea katika eneo la kukagulia mizigo. Kamanda Amata aliinyakua mizigo yake na kuibwaga mezani kwa mwanadada mrembo wa Kisomali, mwanadada yule alikagua vizuri kabisa mizigo ya kamanda lakini hakuona hata kitu kimoja cha hatari wakati ndani yake kulikuwa na silaha nyingi za kijasusi.

Alipomaliza akatoka katika mlango mkubwa, huku akisindikizwa na kijana mmoja aliyekuwa akisukuma kile kitorori cha mizigo. Macho ya Kamanda Amata yalikuwa yakicheza huku na kule kuwaangalia wote waliopo katika uwanja huo ili aone kama adui yoyote. Kutokana na kazi zake za kijasusi aliweza kuitambua ni ya mtu kwa kumwangalia tu usoni mara moja. Akingiza mkono mfukoni na kutoa kidubwasa kidogo ukubwa wa kidole gumba akaminya sehemu ya katikati ambayo ilikuwa na kitufe chekundu. Gari moja iliyokuwa katikati ya nyingine ikawasha taa zake na kujiwasha injini, ikabaki inaunguruma.
“Asante sana kijana nimekwishampata mwenyeji wangu,” alimshukuru yule kijana na kumpa dola za kimarekani hamsini. Yule kijana hakuamini, aliigeuza huku na huku ile noti hakuamini, akabaki kukenua huku akimwangalia kamanda Amata.
“Unaitwa nani?” kamanda akamwuliza.
“Naitwa Ahab,” yule kijana akajibu.
“Una simu?” Kamanda akamwuliza.
“Ndiyo, ndiyo ninayo,” akajibu na kuitoa simu ya kizamani kidogo iliyokuwa imeshikizwa kwa mipira.

Akamnda Amata akatikisa kichwa na kumtazama kijana huyo aliyeonekana mjanja machoni na matendo yake pia. Kamanda Akachukua namba ya kijana huyo akamwahidi kumtafuta usiku wa siku inayofuata. Yule kijana akafurahi sana na kuondoka eneo hilo. Kamanda Amata akaisogelea ile gari ambayo hata hakujua ni nani aliyeiweka mahala hapo. Akafungua mlango na kuketi baada ya mizigo yake kuitupia kwenye buti ya gari hiyo. Akaketi kwenye kiti cha dereva na kujiweka sawa, ile gari ikamkumbusha kufunga mkanda.
‘Tanzania tumeendelea sana kiteknolojia,’ akajiwazia wakati gari hiyo ikimpa maelekezo mafupi juu ya matumizi, aliporidhika akaitoa mahali pale taratibu na kuiingiza katika barabara kubwa ya kutokea nje ya uwanja huo.

JAZEERA PALACE HOTEL

KAMANDA Amata aliegesha gari katika maegesho ya hotel hiyo, akashuka na kutoa mizigo tayari kuelekea ndani.
“Karibu sana Jazeera palace Hotel,” sauti tamu ya kike ikamkaribisha Kamanda alipokuwa pale mbele ya kaunta.
“Asante sana, nimekaribia, natumaini kupata huduma safi na bora kuliko mahala popote nilipowahi kwenda,” kamanda akajibu karibisho hilo.
“Usijali, kila huduma inapatikana,” yule msichana akamwambia.
Baada ya kuandikisha na kumaliza kila kilichohitajiwa pale kaunta, Kamanda Amata akaingia kwenye lifti na kupanda ghorofa ya tatu.

305, ilikuwa namba ya chumba iliyomtazama mbele yake, akaingia ndani na kuufunga mlango nyuma yake, kabla ya lolote, akachukua kifaa chake maalumu kwa kazi ya ukaguzi kama kuna kitu chochote cha hatari, alipohakikisha usalama upo aliweka vizuri mambo yake, akatazama simu yake ilikuwa saa saba za usiku, akajua bado dakika kumi na tano tu ile ndege ya Ethiopia itakuwa hapo Mogadishu, Kamanda Amata alitaka kuwa pale ili aone kinachoendelea; hasa kumuona yule mtu aliyemgundua akitoa maelezo fulani kwa ndugu zake, akabadili nguo na kuvaa mavazi ya kazi: suruari nyeusi, koti la suti jeusi lililotanguliwa na kabashingo nyeusi, shingoni akaninginiza mkufu mzito wa dhahabu, akaichukua bastola yake mpya kabisa aliyokabidhiwa na Chiba, akaiweka tayari na kuificha ndani ya koti hilo, akakusanya silaha zake za siri na kuzipachika katika sehemu mbalimbali za suruali yake, akajitazama kwenye kioo, akajiona kamili. Akaufunga mlango na kuteremka kwa ngazi mpaka chini, akatoka nje na kuingia kwenye gari yake aina ya Kilimanjaro, akaondoka kuelekea uwanja wa ndege. ‘Hakuna kulala…’
 
RIWAYA: HUJUMA 13
MTUNZI: richard MWAMBE


JNIA – saa 2:00 usiku

MADAM S alimpa mkono Kamanda Amata alipokuwa uwanja wa ndege wa kimataifa Dar es salaam tayari kwa safari.
“Kila la kheri Kamanda, nakuaminia sana,” Madam alimwambia. Kamanda Amata akasaluti kisha akamuendea Gina na kumbusu.
“Nahitaji urudi Kamanda, urudi na pua yako,” Gina alimwambia Kamanda.
“Usijali, nitarudi na kila kitu changu,” Kamanda akaagana na wote pale uwanja wa ndege kisha akaingia katika chumba cha wasafiri tayari kwa safari.
“Habari ya jioni,” mtu mmoja alimsalimu Kamanda Amata walipokuwa ndani ya chumba cha wasafiri.
“Salama kabisa,” Kamanda akajibu na kuendelea kusoma gazeti lililo mkononi mwake.

“Unaelekea wapi?” yule mtu akamwuliza Kamanda Amata. Kamanda Amata akamtazama kuanzi kiatu alichovaa mpaka nywele, ndipo alipomgundua mtu huyo kwa mbali ana asili ya watu kama Wamburu.
“Naenda Arusha, wewe je?” Kamanda akamwuliza.
“Naenda Moqdishu,” yule mtu akajibu, akajikohoza na kuendelea, “Sasa unaenda Arusha kwa Ethiopia Airline!” akaongeza.
“Hilo halikuhusu, nina uwezo wa kwenda Morogoro kwa British Airways,” kamanda alipomaliza kuongea hayo, tayari mlango ulikuwa wazi na abiria wakaanza kuingia ndegeni.

§§§§§

Yule mtu aliyekuwa akiongea na Amata pale uwanja wa ndege alikuwa mara kwa mara akienda maliwato ndani ya ndege hiyo. Kamanda Amata alikuwa ameketi siti za mbele ilihali yule bwana alikuwa siti za nyuma, kamanda Amata aliweza kumuona vizuri kwa kupitia miwani yake ambayo iliweza kumuonesha vinavyotokea nyuma yake.
Baada ya kumtazama kama mara nne akienda maliwato, mara hii Kamanda Amata akainuka kutoka katika kiti chake na kuelekea upande wa nyuma wa ndege hiyo. Moja kwa moja akaenda mpaka katika mlango wa maliwato, akasimama kusikiliza kama mtu huyo anaongea chochote, akasikia lakini kwa sauti ya chini sana kutokana na mlango huo jinsi ulivyotengenezwa, kamanda Amata akachomoa kifaa kidogo chenye mfano wa koni akakiegesha hapo mlango na kusikiliza kila kinachoongelewa, alipoona kuwa mtu huyo anakaribia kumaliza mazungumzo Amata akashika kitasa cha mlango huo na kukifungua kwa nguvu kwa kukivunja, akausukuma mlango ndani na kuingia kisha akaufunga nyuma yake.

Ndani ya choo hicho akakutana na yule bwana, Kamanda Amata akamtazama kwa jicho baya.
“Nani ulikuwa unampa habari zangu?” akamwuliza.
“Hapana, mimi nilikuwa naongea na ndugu zangu,” akajibu huku akitetemeka.
“Ndugu zako ndio unawatajia jina langu?” Kamanda Amata akauliza, kisha akatazama kifaa alichokuwa anatumia kuwasiliana na jamaa hao, kilikuwa ni kifaa cha ajabu sana kidogo kwa mfano wa kiberiti, alikiunganisha kwa ufundi sana kupitia nyaya ndogo zinazosafirisha mawasiliano ndani ya ndege hiyo. Kamanda Amata akakitazama na kuzing’oa zile nyaya zake pale alipoziunganisha na zile zilizo kwenye mfumo wa ndege hiyo.
Alipohakikisha anacho kile kidubwasha mkononi mwake, akamwamuru yule jamaa kutoka ndani ya choo kile.

“Sasa utakwenda kukaa pale nilipokaa mimi na mimi nitakaa hapa ulipokaa wewe,” Kamanda alimwambia yule jamaa.
“Ah, siwezi kukaa kule kwani mi sti yangu ni hii hii,” yule bwana alilalama. Kamanda Amata hakujibu, alimtandika kofi moja kali sana, mpaka yule bwana akakaa chini. Wahudumu wa ndege wakamfuata Kamanda kumwambia kuwa analolifanya haliruhusiwi ndani ya usafiri huo, wakamwomba akae kwenye siti yake. Kamanda Amata akawaonesha kitambulisho chake halisi. Hapo wakamwacha afanye atakalo, kwa kuwa huyo ni mtu wa kuaminika. Yule mtu akaketi kwenye siti ya Amata na Amata akakaa kwenye siti yake, sasa alikuwa akimwangalia kwa mbele.
Baada ya kutua Nairobi, yule bwana aligeuka nyuma kwa woga kumtazama Amata, hakumwona.
Kamanda Amata alishuka katika uwanja wa ndege wa Jommo Kenyatta bila yule bwana kujua. Baada ya kufanyiwa itifaki za kiusalama, hakuchukua muda mrefu alikwea ndege shirika la Dubai Airline na kuelekea Mogadishu, tayari kabisa kuanza kibarua alichotumwa.

MOGADISHU – SOMALIA
Uwanja wa ndege wa ADEN ADDE

SHALABAH alikunja sura baada ya kupata taarifa kuwa Kamanda Amata hayupo katika ndege waliyoitarajia. Alionekana wazi kupumua kwa nguvu, akiwaza jambo.
“Shalabah, vipi?” Sharon akamuuliza.
“Huyo wanaemwita Kamanda Amata hayupo katika ndege tangu watoke Nairobi,” Shalabah akamwambia Sharon. Sharona naye akaonekana wazi kupigwa butwaa.
“Atakuwa kaamua kukatisha safari?” Sharon akauliza.
“Hapana, huyu anataka kutuchezea mchezo, nina uhakika yuko humohumo, kajificha sehemu, hebu ongea na watu wetu upande wa cargo kuwa wanaangalia vizuri, bado saa moja ndege itatua,” Shalabah akatoa maelekezo na Sharon akawapanga upya watu wake.

“Vipi?” Fasendy akamwuliza Sharon, pindi alipotoka pembeni kuvuta sigara.
Fasendy alikodiwa katika mpango huo ili kummaliza Kamnda Amata palepale uwanja wa ndege kwa kumdungua, alikuwa tayari kajipanga kwa hilo, alichoambiwa yeye ni kuwa atapewa maelekezo tu ya jinsi mtu huyo alivyo.

§§§§

NDEGE ya Dubai Airline ilikanyaga ardhi ya Mogadishu ikiitangulia ile ya Ethiopia ambayo maharamia hao walikuwa wakiisubiri kwani walishaambiwa kuwa Kamnda yuko humo, na walitahadharishwa kuhakikisha haingii mjini kwani ni mtu hatari sana. Mpaka dakika hiyo walikwishakubaliana na hilo kuwa mara hii wanapambana na mtu makini mwenye akili za ziada kwa mchezo tu aliowachezea kwenye ndege hiyo.
Kamanda Amata alikiacha kiti chake, akaweka kijibegi chake mgongoni na taratibu kuziteremka ngazi za ndege hiyo na kwa mara ya kwanza aliweka unyanyo wake katika ardhi ya Mogadishu, uwanja wa ndege wa Aden Adde. Akiwa na miwani yake usoni aliweza kuona vyema kabisa katika mianga ya taa kali za umeme iliyokuwa ikimulika eneo hilo, akavuta hatua ndefundefu na kuelekea katika eneo la kukagulia mizigo. Kamanda Amata aliinyakua mizigo yake na kuibwaga mezani kwa mwanadada mrembo wa Kisomali, mwanadada yule alikagua vizuri kabisa mizigo ya kamanda lakini hakuona hata kitu kimoja cha hatari wakati ndani yake kulikuwa na silaha nyingi za kijasusi.

Alipomaliza akatoka katika mlango mkubwa, huku akisindikizwa na kijana mmoja aliyekuwa akisukuma kile kitorori cha mizigo. Macho ya Kamanda Amata yalikuwa yakicheza huku na kule kuwaangalia wote waliopo katika uwanja huo ili aone kama adui yoyote. Kutokana na kazi zake za kijasusi aliweza kuitambua ni ya mtu kwa kumwangalia tu usoni mara moja. Akingiza mkono mfukoni na kutoa kidubwasa kidogo ukubwa wa kidole gumba akaminya sehemu ya katikati ambayo ilikuwa na kitufe chekundu. Gari moja iliyokuwa katikati ya nyingine ikawasha taa zake na kujiwasha injini, ikabaki inaunguruma.
“Asante sana kijana nimekwishampata mwenyeji wangu,” alimshukuru yule kijana na kumpa dola za kimarekani hamsini. Yule kijana hakuamini, aliigeuza huku na huku ile noti hakuamini, akabaki kukenua huku akimwangalia kamanda Amata.
“Unaitwa nani?” kamanda akamwuliza.
“Naitwa Ahab,” yule kijana akajibu.
“Una simu?” Kamanda akamwuliza.
“Ndiyo, ndiyo ninayo,” akajibu na kuitoa simu ya kizamani kidogo iliyokuwa imeshikizwa kwa mipira.

Akamnda Amata akatikisa kichwa na kumtazama kijana huyo aliyeonekana mjanja machoni na matendo yake pia. Kamanda Akachukua namba ya kijana huyo akamwahidi kumtafuta usiku wa siku inayofuata. Yule kijana akafurahi sana na kuondoka eneo hilo. Kamanda Amata akaisogelea ile gari ambayo hata hakujua ni nani aliyeiweka mahala hapo. Akafungua mlango na kuketi baada ya mizigo yake kuitupia kwenye buti ya gari hiyo. Akaketi kwenye kiti cha dereva na kujiweka sawa, ile gari ikamkumbusha kufunga mkanda.
‘Tanzania tumeendelea sana kiteknolojia,’ akajiwazia wakati gari hiyo ikimpa maelekezo mafupi juu ya matumizi, aliporidhika akaitoa mahali pale taratibu na kuiingiza katika barabara kubwa ya kutokea nje ya uwanja huo.

JAZEERA PALACE HOTEL

KAMANDA Amata aliegesha gari katika maegesho ya hotel hiyo, akashuka na kutoa mizigo tayari kuelekea ndani.
“Karibu sana Jazeera palace Hotel,” sauti tamu ya kike ikamkaribisha Kamanda alipokuwa pale mbele ya kaunta.
“Asante sana, nimekaribia, natumaini kupata huduma safi na bora kuliko mahala popote nilipowahi kwenda,” kamanda akajibu karibisho hilo.
“Usijali, kila huduma inapatikana,” yule msichana akamwambia.
Baada ya kuandikisha na kumaliza kila kilichohitajiwa pale kaunta, Kamanda Amata akaingia kwenye lifti na kupanda ghorofa ya tatu.

305, ilikuwa namba ya chumba iliyomtazama mbele yake, akaingia ndani na kuufunga mlango nyuma yake, kabla ya lolote, akachukua kifaa chake maalumu kwa kazi ya ukaguzi kama kuna kitu chochote cha hatari, alipohakikisha usalama upo aliweka vizuri mambo yake, akatazama simu yake ilikuwa saa saba za usiku, akajua bado dakika kumi na tano tu ile ndege ya Ethiopia itakuwa hapo Mogadishu, Kamanda Amata alitaka kuwa pale ili aone kinachoendelea; hasa kumuona yule mtu aliyemgundua akitoa maelezo fulani kwa ndugu zake, akabadili nguo na kuvaa mavazi ya kazi: suruari nyeusi, koti la suti jeusi lililotanguliwa na kabashingo nyeusi, shingoni akaninginiza mkufu mzito wa dhahabu, akaichukua bastola yake mpya kabisa aliyokabidhiwa na Chiba, akaiweka tayari na kuificha ndani ya koti hilo, akakusanya silaha zake za siri na kuzipachika katika sehemu mbalimbali za suruali yake, akajitazama kwenye kioo, akajiona kamili. Akaufunga mlango na kuteremka kwa ngazi mpaka chini, akatoka nje na kuingia kwenye gari yake aina ya Kilimanjaro, akaondoka kuelekea uwanja wa ndege. ‘Hakuna kulala…’
 
RIWAYA: HUJUMA 14
MTUNZI: richard MWAMBE

Uwanja wa ndege wa ADEN ADDE saa 7.15 usiku.

Kamanda Amata aliegesha gari yake na kuteremka kuelekea eneo ambalo wageni hufikia kusubiri mizigo yao. Usoni akiwa amevalia miwani yake yenye uwezo wa kupiga picha na kuona upande wa nyuma. Akavuta hatua chache na kusimama karibu na mti wa mtende ulio pembezoni tu mwa barabara inayotenganisha upande wa maegesho na upande wa jengo kuu la uwanja huo. Akijifanya kuwa hajui lolote au hana la maana mahala hapo, Kamanda Amata alitulia kwa kujiegemeza katika mti huo, akitazama wanaoingi na kutoka. Ilikuwa ni muda huohuo ndege ya Ethiopia ilitua katika uwanja huo.
Punde si punde, lile alilolitarajia lilitukia; kutoka katika mlango mkubwa wa jengo lile alimuona yule bwana akitoka huku akisukuma kitoroli cha mizigo, mara kidogo akalakiwa na watu watatu, wanaume, akajaribu kuzinasa picha zao kwa kutumia miwani yake, akabahatika japo kwa shida kidogo. Baada ya tukio hilo aliwafuatilia kwa macho akitazama walikokuwa wakielekea, kutoka mbali aliwaona kana kwamba walikuwa wakilaumu jambo kutoka kwa huyo mwenzao waliyekuja kumpokea. Kamanda Amata kwa haraka kidogo akarudi katika gari yake na kuketi kitini, nyuma ya usukani, akiendelea kuwatazama huku miwani yake ikimuonesha kwa uzuri zaidi. Baada ya kusimama kidogo mahala fulani, ikaonekana wamekubaliana jambo, wakaingia garini wote wanne. Kamanda Amata akaitazama ile gari ilipokuwa ikitoka kwenye maegesho hayo na kuingia barabara kubwa, akaitazama namba zake za usajili na kuzikariri akilini mwake, kisha akaiacha kidogo itoke, na ye taratibu akawa anatoka kuelekea barabara kubwa, lakini kabla hajaingia barabarani gari nygine pick up, ilimpita mbele yake kwa kasi nay eye ikabidi asimame ghafla, baada ya hapo akaendelea kuifuata kwa mbali.

§§§§§

“Yaani wewe imekuwaje ukampoiteza yule wakati wote mpo ndege moja?” akauliza Sharon akiwa kageuza nusu ya mwili wake nyuma kwa yule mgeni.
“Yaani Sharon, mi hata sielewi yule Bwana kanipotea vipi,” akajibu yule mgeni huku akibabaika. Kisha ukimya ukatawala kati yao.
“Sasa mmeangalia vizuri kwenye mizigo?” Shalabah nae akauliza.
“Ndiyo mkuu, tumetazama na hayupo, sasa sijui itakuwaje.”
Baada ya mazungumzo marefu kati yao, ile gari iliegeshwa kwenye moja ya hoteli kubwa pale mjini, Jabir Hotel. Kamanda akamshuhudia yule bwana akishuka na kuwaacha wenyeji wake wakiendelea na safari nay eye akachukua uelekeo wa mlango mkubwa wa hotel hiyo huku akisaidiwa mizigo yake na mhudumu wa hapo, ile gari iliyomleta ikaondoka zake. Kamanda Amata akasukuti kwa nukta kadhaa, akaona kuwa hiyo ni nafasi pekee ya kuanzia kazi yake. Akaondoa gari yake na kuiacha ile hotel kuwaelekea wale jamaa wengine. Lakini haikuwa nia yake, alipofika mbele kidogo eneo lililokuwa na maghorofa mengi aliegesha gari yake katika supamaketi moja kisha yeye akashuka na kuingia ndani yake akiwa kama mteja, lakini lengo kubwa ilikuwa ni kuangalia kama kuna anayemfuata nyuma yake. Alipohakikisha kuwa hakuna, alitokea upande wa pili na kuchukua taxi.
“Jabir Hotel tafadhali,” alimwambia dereva huku akiketi sawia katika kiti cha nyuma. Dakika kumi na tano hivi alikuwa tayari amekwishafika alipopakusudia, akamlipa dereva taxi na yeye kuuendea mlango wa hoteli hiyo. Jambo la kwanza alilofanya ni kuona kama anaweza kumpata yule kijana aliyemsaidi mizigo yule mgeni. Haikuwa tabu kumpata, alimwendea na kumwita kama mtu mwingine yeyote mwenye shida.

“Samahani, kuna mgeni tumemleta hapa kama dakika thelethini zilizopita,” alijaribu kiumwuliza yule mhudumu naye kwa kuwa anapokea wageni wengi haikuwa rahisi kujua ni yupi, lakini baada ya kumuelekeza vizuri alimkumbuka japo hakuwa na uhakika.
“Kama ni huyo yupo chumba namba 243,” akajibu yule mhudumu.
Kamanda Amata akashukuru na kushika njia, akapanda ghorofa ya pili kwa kutumia ngazi na isha kutokea kwenye korido ndefu ambayo ilikuwa imetanganisha vyumba vingi upandee mmoja na mwingine. Akatazama milangoni huku na huku na kujikuta mbele ya chumba hicho, namba 243 ilisomeka mlangoni bila kificho, akatulia kusikiliza kama kuna lolote ndani humo. Ukimya ulikuwa sehemu kubwa ya chumba hicho, Kamanda Amata hakuwa na uhakika kama ni sahihi mtu huyo yuko humo ndani, alipotaka kukata tama alisikia kwa mbali maji yakimwagika, hapo akawa na uhakika kuwa mlengwa wake yupo. Akachukua funguo yake na kuitumbukiza tunduni, lakini akajikuta anakabiliwa na upinzani kwani ndani ya mlango huo kulikuiwa na funguo ambayo iliikwamisha ile yak wake kufanikisha zoezi hilo. Akaitazama ilivyokaa akaiona kuwa imekaa sawia, akaisukuma ikaangukia ndani kisha akaipachika ya kwake.
Kitendo cha ile funguo kuanguka kilimshtua mtu wa ndani, Kamanda Amata alisikia nyayo za mtu aliyekuwa akitembea kuelekea mlangoni huku akipiga mruzi, akakinyonga kitasa wakati funguo yake tayari ilikwisharudi mfukoni, yule bwana alipokuwa akiipachika ile funguo kwa upande wa ndani, Kamanda Amata akaufungua mlango kwa ghafla na kumpiga usoni yule mtu.
Sekunde tano tu, Kamanda Amata alikuwa kajaa ndani kuufunga mlango nyuma yake, huku bastola uyake ikiwa mkononi. Yule bwana alikuwa chini kwa kusukumwa na ule mlango.
“We n… na….. nani? Aliuliza kwa kukatisha maneno.
“Hunijui”?
Yule bwana alionekana kuchanganyikiwa na kile kitendo, akawa anasota kwa makalio kurudi nyuma, akagota ukutani, hakuna njia.
“Niambie ulikuwa unatoka Tanzania kwa nani?” Kamanda akamuuliza.
“We mambo yangu unayatakia nini?” yule bwana akajibu kijeuri.
“Sikiliza wewe bwege, sijaja kupoteza muda na mtu, nitakuuwa sasa hivi,” Kamanda alimtahadharisha yule bwana aliyeonekana kutokuogopa chochote. Akiwa katulia kamtumbulia macho Amata, kwa mara ya kwanza, Kamanda Amata aliiamuru bastola ile ndogo ifanye kazi yake, risasi moja ikavunja mguu wa yule bwana, akalia kwa uchungu, kisha Kamanda Amata akamwendea pale na kumkanyaga kwenye jeraha lake.
“Aaaaaiiigggghhhh, unaniumiza!” alipiga yowe, akiongea kwa lugha ya Kiswahili, “Nitakwambia kaka, nitakwambia.”
“Sema.”

Kamanda Amata akalegeza mguu wake kutoka pale kwenye jeraha, akamtazama yule bwana pale chini, damu zikitiririka mguuni mwake. Mara ghafla yule bwana aliufyatua mkono wake uliokuwa na kisu mkononi kuulenga mguu wa Amata. Kamanda Amata aliuona mchezo huo kwa kuchelewa, akaruka nyuma lakini kile kisu kilipita kwenye suruali yake na kuchana kipande karibu na ugoko ila hakikufika kwenye ngozi. Kitendo kile kiliiamsha akili ya Kamanda Amata, kabla yul;e bwana hajafanya jambo linguine, teke kali lilitua mkononi mwake na kukiondoa kile kisu, teke la upande mwingine lilitua shavuni na kumrudisha chini. Yule bwana ijapokuwa alikuwa na jeraha mguuni mwake hakujali, alichomoa bastola kutoka kwenye kiuno chake lakini kabla hajafyatua tayari risasi ya Amata iliyotoka kimyakimya ilipenya kwenye paji la uso wake na kumlaza palepale chini; chali.
Kamanda Amata akasonya kwa kukosa maelezo yoyote toka kwa huyo mtu. Akamwendea na kumpekua mifukoni, hakuwa na kitu chochote zaidi ya kiburungutu cha pesa za kisomali. Alipotazama kitandani aliona baadhi ya vikolokolo, akaviendea, na kuichukua hati ya kusafiria ya mtu huyo, baadhi ya kadi za kibiashara na kijitabu kidogo, akakiacha chumba hicho na kuondoka zake.
Akiwa ndani ya gari yake, aliiangalia ile hati ya kusafiria na kuisoma hapa na pale, akamtambua kijana huyo kwa jina lake la Shaib, mwenye umri wa miaka thelathini na sita. Akaitupa pembeni na kupekuwa vitu vingine.

…Dar es salaam Club, saa 6.30 mchana…

Ilikuwa ni moja ya miadi aliyokuwa akitakiwa kufanya na mtu fulani hapo katika hiyo club. Kamanda Amata akawasha gari yake kuondoka kutoka katika eneo hilo, moja kwa moja akarudi hotelini kwake.

SIKU ILIYOFUATA saa 2.00 asubuhi

Kamanda Amata alikuwa akifuatilia habari katika televisheni ndogo iliyowekwa ndani ya chumba chake, kati ya habari zilizokuwa zikirushwa asubuhi hiyo ni pamoja na ile ya kukutwa marehemu ndani Jabir Hotel. Aliisikiliza kwa tabu kidogo kutokana na kuwa alikuwa haelewi lugha iliyokuwa ikitumika, alijaribu kuangali nyuso za watu waliokuwa eneo lile lakini hakuna aliyemhisi kwa lolote.
Asubuhi hiyo aliiacha hoteli aliyofikia na kufunga safari kuelekea Ramada Plaza Hoteli, iliyopo pembezoni kabisa mwa bahari ya Hindi karibu na bandari ya Mogadishu, kwa maelezo aliyokuwa ameyasoma katika taarifa aliyopewa kuwa katika hoteli hiyo ndipo Gwamaka na Jamil walikuwa wamepanga. Kamanda Amata alikuwa na miadi feki aina mbili, mmoja katika hoteli hiyo na mwingine ni Dar es salaam Club.
Kamanda Amata aliegesha gari yake mbele ya hoteli hiyo kubwa, akashuka na kuufunga mlango wa gari hiyo ya kisasa, akasimama na kuangalia kwa makini lango kuu la hoteli hiyo, akavuta hatua mbili tatu mbele, akasimama na kuangalia vizuri, akajifanya anafunga kamba za viatu kisha akaendelea na safari yake mpaka mapokezi. Akakutana na mhudumu wa ofisi hiyo, msichana mrembo, mweupe wa haja, Kamanda Amata akamtazama kwa jicho la husuda.

“Habari mrembo,” alimsalimu.
“Nzuri, sijui nikusaidie nini?” yule mhudumu akajibu na kuuliza.
“Ok, naitwa Jaffar kutoka Tanzania, nimekuja hapa nina shida kidogo, siku za nyuma kuna kaka zangu walikuja kikazi wakafikia hapa lakini mpaka sasa hatujapata habari za wapi, nimekuja kufuatilia habari zao,” kamanda alimueleza yule mhudumu.
“Ok, naomba uingie ofisi namba tano kuna mtu atakuhudumia,” akajibiwa. Kamanda Amata bila hofu akaenda na kuingia katika ofisi hiyo, pale akamkuta bwana mmoja aliyevali nadhifu kabisa. akamsabahi na kumueleza shida yake.
Yule bwana akamkazia macho Kamanda Amata.
“Unasema unaitwa Jaffar?” akauliza.
“Ndiyo,” akajibu Kamanda.
Yule mtu akainua simu yake na kupiga namba Fulani, mara kijana mmoja akaingia na mabegi manne makubwa.
“Hizi ni mali za kaka zako, ila taarifa nyingine ya kujua wapi walipo ndugu zako kiukweli hatujui, na hatuna msaada mwingine zaidi ya huu tuliokupa sasa,” yule bwana akajibu. Kamanda Amata akayatazama yale masanduku na kuwaamuru wale wahudumu wayafungue nao wakafanya hivyo; Kamanda Amata akatazama vitu vilivyomo katika masanduku hayo kwa harakaharaka aliporidhika akamshukuru yule bwana. Kwa kusaidiwa na wale wahudumu akatoka nay ale masanduku lakini muda huo tayari alikuwa amekwishayasoma mazingira ya hoteli hiyo.

Saa 6.00 Mchana- Dar es salaam Club

Akiwa ameketi kwenye moja ya viti vilivyojaa katika ukumbi wa club hiyo, Kamanda Amata alikuwa aking’aza macho huku na kule kumwangalia mgeni asiyemjua. Moyo wake ulijaa hasira sana na watu hao wanaojiita maharamia. Aliendelea kutulia pale huku akitazama wanaoingia na wanaotoka.
Akiwa katika hali hiyo, mara waliingia watu watatu, wanaume walioongozwa na kijana mmoja aliyeonekana machachari. Walipita kona mbili tatu na kuelekea upande wa nyuma ambao ulikuwa na vyumba vya V.I.P, vyumba vilivyotumika kwa kazi au mazungumzo maalum. Akiwa katika kushangaa watu hao mara alihisi kitu kama bilauri ikitua juu ya meza yake, akageuka na kukutana macho na msichana aliyekuwa ameketi mbele yake bila kukaribishwa.

“Usishtuke kaka Jaffar,” yule mwanadada akamwambia. Kamanda Amata akashtuka kusikia jina lake likitamkwa sawia na binti huyo. “Naitwa Farheen, nafanya kazi hoteli ya Ramada Plaza,” akajieleza. Kamanda akamtazama bila kummaliza.
“Nikusaidie nini?” akamuuliza.
“Sikia Jaffar, najua huko hapa kwa minajiri gani, lakini ninachokwambia usifanye hicho unachotaka kufanya, utajiweka hatarini, tukiachana hapa, hakikisha unauacha salama mji wa Mogadishu, tayari wanajua lile ulilolifanya leo pale Jabir Hotel, sina zaidi,” yule mwanadada akamaliza na kunywa kinywaji chake kisha akaondoka kutoka pale mezani na kuingia upande ule wenye vyumba vya V.I.P.
Kamanda Amata alimtazama yule mwanamke na kisha akamfuata alikokwenda, alipouaona mlango alioingia naye akaelekea huko, hakuogopa, aliingia moja kwa moja ndani ya chumba hicho na akajikuta yeye na mwanadada yule tu wakitazamana…
 
RIWAYA: HUJUMA 15
MTUNZI: richard MWAMBE


“Unanifuata?” akauliza, “Watakuua,” akaongeza huku akionesha ishara ya kukata shingo kwa mkono wake.
“Bila shaka unajua mengi sana juu ya kaka zangu, nataka unieleze, nani aliyewaua?” kamanda akauliza.
Yule mwanadada akatoa cheko la dharau, na alipotulia akamtazama kamanda huku akiweka vizuri gauni lake refu lililomfunika mpaka miguuni, “Wauaji, wamewaua kaka zako,” akatoa jibu tata. Kamanda Amata akageuka na kutoka ndani ya chumba kile akimuacaha yule mwanamke peke yake, kabla hajavuta hatua nne au tano akakutana na watu wengine wawili wakamzuia. Kamanda akasimama katikati ya watu hao na yule mwanamke, lakini yule mwanamke akatoa ishara ya kuwa wamuache aondoke, akaondoka zake.

§§§§§§

“Inaonekana sasa Tanzania wamemleta mtu makini, maana hata kuzifuata nyayo zake lazima hujipange, ama atakupotea au atakupoteza,” aliongea mmoja wa watu wale walioingia katika chumba cha V.I.P pale Dar es salaam Club.
“Ndiyo, maana jinsi alivyoingia tu hapa Mogadishu imetosha kutuonesha kuwa ni mtu hatari, inabidi juu chini ashughulikiwe mara moja,” mwingine akadakia.
“Aaaaa sio kazi kubwa kumtia mkononi yule mende, ni kumuotea tu chumbani kwake basi,” mtu wa tatu aliongeza.
“Tutamuoteaje?” yule mjumbe wa kwanza akauliza kwa shauku huku akijivuta kwa mbele kusikiliza hoja hiyo.
“Tunamtegea mtu chumbani kwake amsubiri, akiingia tu asimpe nafasi, ammalize,” wazo likatolewa, wote wakalipitisha. Baada ya hapo wakazungumza machache kati yao na kuagana wakiwa na mikakati kabambe ya kumnasa kamanda Amata.

§§§§§§

Kamanda Amata kwa hatua za taratibu alijivuta na kuingia ndani ya gari yake, akaketi kimya akitazama nyendo za hapa na pale, dakika arobaini na tano baadae aliwaona wale watu wakitoka ndani ya club ile na kuziendea gari zilizokuwa hapo, kila mmoja akaingia katika gari yake na kuondoka. Kamanda Amata akaichagua moja kati ya gari hizo tatu na kuifuatailia mpaka inapoishia.
Kwa mwendo wa wastani alikuwa nyuma ya gari kama tatu hivi huku ile anayoifuata ikiwa mbele sana lakini alihakikisha kuwa haimpotei katika macho yake. Baada ya mwendo kama wa dakika ishirini na sita hivi, ile gari ikaingia katika jumba Fulani la kifahari ambalo lilizungukwa na ukuta mkubwa sana ulioziba eneo kubwa na kufanya jumba hilo lionekane kwa tabu. Kamanda akapita na kutupia jicho jumba hilo, mbele kidogo akaegesha gari yake na kutulia akisubiri ni wakati gani yule bwana atatoka. Akiwa ametulia ndani ya gari yake alijikuta akipitiwa na usingizi mtamu wenye ndoto mbalimbali, haloi hiyo ilikuwa ikimsumbua sana, wakati akigombana na hali hiyo aliiona ile gari ikitoka langoni na kurudi kwa barabara ileile iliyojia.

Amata naye akaigeuza gari yake na kuifuata kwa mwendo wa wastani akihakikisha kuwa yule mtu asijue kabisa kama anafuatwa. Baada ya kupita mitaa kadhaa ile gari ilitokea upande wa baharini na kufuata barabara kandokando yake. Akiendelea kupishana na magari kadhaa makubwa kwa madogo, Kamanda Amata aliendelea kuifuata ile gari, sasa aliiona ikiongeza kasi kuliko mwanzo, akilini mwake akajua kwa vyovyote mtu huyo amejua kama anafuatiliwa. Amata naye akabadilisha gia na gari yake aina ya Kilimanjaro ikaanza kuinyanyasa barabara kwa mwendo kasi, akiwa katika kasi hiyo akiifukluza ile gari nyingine, alisikia sauti ya honi ya garimoshi, alipotazama vizuri kulikuwa na reli inakatisha eneo lile. Kizuizi cha barabar kilikuwa kikiteremka taratibu kuzuia magari yasivuke katika reli hiyo, lakini aliishuhudia ile gari anayoifuata ikivuka kwa kasi na kuvunja kile kizuizi ambacho tayari kilikuwa kimefika chini

Kamanda Amata alisonya kwa hasira kwani alielewa jambo alilofanya mtu yule, hakuwa na jinsi ilibisi kusubiri mpaka ile treni ilipomalizika, hakuweza tena kuiona ile gari, naye kwa kuonesha kuwa ni mwelevu akageuza gari na kurudi alikotoka hakuifuata ile njia.
Breki ya kwanza ilikuwa ni katika hoteli ya Ramada Plazza, akaegesha gari yake na kuingia tena ndani ya hoteli hiyo. Mara hii alipita mapokezi na kuzunguka upande wa maofisi, akasimama katika mlango ulioandikwa ‘Security Room,’ akagonga, mlango ukafunguliwa, akaingia ndani na kukuta watu wawili.
“Samahani hairuhusiwi mtu kuingia humu ndani,” mmoja wao akamwambia Kamanda Amata lakini kabla hajajibiwa alikuta akipewa kipigo cha dharula na kupoteza fahamu, vivyo hivyo kwa yule mwingine. Kamanda Amata akavuta droo na kupekua pekua huku akisoma tarehe za disc hizo ndogo zilizohifadhi kumbukumbu za matukio ya kila siku. Alipoona katika saraka hiyo hakuna anachokitaka akapekuwa saraka nyingine na kuiona ile aliyoihitaji, alipojiridhisha kuwa ndiyo hiyo akaipachika katika chombo maalum kwa kazi hiyo na kuanza kurudisha nyuma kuangali matukio ua siku hiyo.

Aliirudisha nrudisha nyuma picha hiyo ya video iliyopigwa kwa kamera za usalama, ikionesha Jamil alivyokamatwa, akiamriwa kuweka mikono kichwani. Kamanda Amata alitazama kwa makini sana, akajaribu kuangalia sura za watu wale waliokuwa na silaha nzito za kivita, alitazama jinsi walivyompakia Jamil kwenye jeep na kuondoka nae. Kamanda Amata akaichukua disc hiyo na kuitia mfukoni kisha akatoka nje ya ofisi hiyo na kuondoka zake.
Moja kwa moja akaenda kufuata taarifa za Sebeki baada ya kujua kuwa naye alikufa kwa mlipuko wa bomu mbele tu ya hoteli aliyofikia, nako alipata disc kama ile iliyohifadhi picha za video zikionesha mlipuko ule, Kamanda Amata alitazama kwa makini sana, mara hii aliona taswira ya mwanamke, alijaribu kurudisharudisha mara kwa mara kumwangalia mwanamke huyo lakini hakuweza kumtambua, aliichukua disc hiyo na kupotea zake.
Dakika kumi na tano baadae alifika kwenye hoteli aliyofikia, hoteli ya Jazeera Palace, kabla hajashuka garini, alifungua kompyuta ndogo ndani ya gari yake, akapachika zile disc moja baada ya nyingine na kuzituma picha hizo katika idara ya usalama Tanzania ili zifanyiwe kazi. Alipohakikisha kazi imekamilika akateremka na kuvuta hatua kuingia ndani ya hoteli hiyo.

“Ujumbe wowote!” akamwambia mhudumu wa mapokezi, yule mhuidumu akainama na kutoa bahasha moja ya kaki akampatia. Amata akainyakua na kuondoka zake kuelekea ghorofa ya juu. Alifika mlangoni mwa chumba chake, kabla hajashika kitasa alisimama kwa sekunde kadhaa, akagundua kuwa ndani ya chumba chake kuna mgeni, alitazama alama ndogo aliyoiacha kwenye kitaza cha mlango ambayo haikuwepo tena. Akachomoa bastola yake na kuiweka sawa, kisha akafungua mlango na kuuacha wazi bila yeye kuingia, ukimya ukatawala. Amata hakuingia ndani na wala aliyekuwa ndani hakutoka nje, waliwindana. kamanda Amata akaamua kuingia kwa kasi huku akijirusha kwa ustadi wa hali ya juu sana na kutua upande wa pili wa chumba, kwa haraka alimuona mtu aliyemtarajia nyuma ya mlango, yule jamaa alifyatua risasi iliyomkosa padogo Kamanda na kuchimba ukuta, Kamanda Amata akavingirika na kupita chini ya kitanda, risasi ya pili nayo ikamkosa padogo vilevile, wakati huo Kamnda Amata akawa tayari ametokea upande wa pili, kwa kasi ya ajabu alifyatua risasi iliyopiga sawia bega la mtu huyo.

“Aaaaaaaaiiiihhhhgggghhhh!!!!” yowe la maumivu likamtoka yule mtu huku akiidondosha bastola yak echini. Ksbls hsjsfiks chini sakafuni risasi ya pili ilifumua kifua cha mtu huyo na kumbwaga chini. Kamanda Amata akawahi pale alipoanguka kabla hajakata roho.
“Nani kakutuma?” akamwuliza, lakini yule mtu alikuwa akipumua na kuangusha mabonge ya damu kutoka kinywani mwake. Akamtazama Amata, lakini hakujua ajibu nini, “Wapi mmemweka Jamil?” akauliza tena.
“Gha…la….ni…” akajibu kwa tabu.
“Ghalani wapi?” Kamanda akauliza tena.
“Ki…wa…nda… cha ngu…. Nguuuoo” baada ya kujibu hilo yule mtu akanyamaza kimya, roho ikauacha mwili.
Amata akairudisha bastola yake katika mahali husika, akaugeuza mwili wa yule mtu na kupekuwa mifukoni, akatoa simu moja, zaidi ya hapo hakukuwa na kitu chochote kingine. Kamanda Amata aliitazama ile simu kwa makini sana, ilikuwa ni simu ya kisasa sana iliyofungwa mtambo wa GPS ambao unaweza kukuonesha mahali ulipo au mahali unapaotaka kwenda. Kamanda Amata akachana bahasha aliyopewa na ndani yake kukadondoka kijikadi kigumu kimoja, akakiokota na kukisoma.

‘Mujabba Club 2030’

Akairudisha ndani ya bahasha ile na kuitia katika begi. Kisha akainua mkono wa simu na kubofya namba za chumba cha usalama cha hoteli hiyo.
“Haraka sana mfike chumba namba 305 kuna shida,” akakata simu baada ya kutoa taarifa hiyo. Nukta chache tu mlango wa chumba chake ukagongwa, akawaruhusu kufungua. Vijana wawili waliokuwa na askari mmoja mwenye silaha waliingia na kulakiwa na dimbwi la damu, wakapigwa na butwaa.
“Huyu ni nani na ameingiaje chumbani mwangu?” Kamanda akawauliza.
“Hata sisi mzee hatujui, na ndo maana tunashangaa,” akajibu mmoja wa vijana wale.
“Haya ondoeni mzoga wenu,” Kamanda akawaamuru, nao mara moja wakapiga simu na gari ya wagonjwa ikafika pamoja na polisi kadhaa. Kamanda Amata akatoa maelezo kwa maandishi, misatari miwili tu ilitosha na kuwarudisia faili lao. Yule askari aliposoma akamtazama kamanda usoni.
“Ni hivi tu?” akauliza.
“Ndiyo ni hivyohivyo tu,” akajibu Kamanda.

§§§§§§

Shalabah alionekana kuchanganyikiwa, alikuwa akizunguka huku na kule akiwa kama mtu aliyesahau kitu, viajana wake walikuwa wameketi kwa utulivu kabisa.
“Sharon,” akaita, na Sharoni akainua uso kumtazama, “Tuna kazi kubwa.”
“Huyu ni chui sijui au tumwiteje, maana hatabiriki,” Sharon alijibu.
“Mpaka sasa amekwishatuondolea watu takriban watatu, tunamfanyeje mtu huyu?” Shalabah akauliza.
“Leo ni kumfanyia uvamizi wa maana na kummaliza,” Sharon, ambaye ndiye kiongozi wa kikosi hicho hatari alitoa uamuzi.
“Yule ni zaidi ya jeshi kaka, tutumie mbinu nyingine tu, lakini swala la kumvamia tusithubutu kulifanya,” Shalabah alitoa rai. Mara mlango wa chumba hicho ukafunguliwa, Fasendy akaingia kati ya wanaume hao.
“Nimekuja,” Fasendy akasema.
“Karibu sana, bila kuchelewa nataka uongoze kikosi hiki ukisaidiana na Sharon kumkabili mtu huyu, muilete roho ama ndani ya mfuko au mikononi mwenu, malipo makubwa umeahidiwa kutoka kwa Mr. Lonely,” Shalabah alimwambia Fasendy na kuitupa picha ndogo mezani, fasendy akaiokota na kuitazama.

“Mbona umeshtuka?” Shalabah akauliza.
Fasendy akatikisa kichwa juu chini, “Sasa Mogadishu imekuwa ndogo.”
“Kwa nini unasema hivyo?” Sharon akauliza.
“Huyu jamaa ni hatari sana, usije kujidanganya kumkabili ana kwa ana, huu ni ama mzimu au roboti ana akili ya ajabu ana mbinu za utatanishi,” Fasendy alieleza.
Shalabah na Sharon wakatazamana, kisha wakarudisha macho yao kwa Fasendy.
“Kwa hiyo unasemaje?” Shalabah akauliza.
“Kufa atakufa tu lakini si kwa ngumi wala teke, huyu labda tumwekee sumu,” Fasendy akajibu.
“Fasendy, mbona sikuelewi?” Sharon akauliza.
“Utanielewa tu Sharon siku ukikutana naye, ninamaanisha huyu jamaa tujipange upya ili kumkabili,” Fasendy akaeleza.
“Yuko Jazeera Palace chumba namba 305, fanya unaloweza, niletee majibu ya kuridhisha,” Shalabah alimpa maagizo Fasendy kisha yeye kuwaacha hapo na kuingia mlango mwingine.

CLUB MUJABBA saa 2.30 usiku

KATIKA kona moja ya ukumbi mdogo wa club hiyo, Kamanda Amata alitulia kimya akiwa na juisi baridi huku akisubiri huyo aliyemuachia ujumbe kule hotelini. Hakuwa na hofu kwa kuwa alikwishzoea kukutana na watu asiyowajua.
Haikumchukua muda mrefu, mbele yake alimuona mzee wa makamo aliyeonekana kuishiwa nguvu tayari akiwa anatembea kwa msaada wa mkongojo, alitembea kwa taabu mpaka pale kwenye meza ya Kamanda Amata, akavuta kiti na kuketi kwa mtindo wa kutazamana.

Kamanda Amata alimtazama shaibu huyo mwenye nywele nyeupe zilizojaa mvi, miwani ya macho, suti iliyomkaa vizuri na mkononi mwake alikuwa na saa kubwa ya gharama sana ikitanguliwa na pete ya dhahabu.
“Kamanda Amata,” akaita kwa tabu huku akisindikiza maneno yake na kikohozi kikavu.
“Yeah ndo mimi, wewe, wewe ni nani?” kamanda akauliza kwa uoga kidogo.
“Haunijui, lakini utanijua mimi ni nani,” akasema yule mzee na kuanza kukohoa, akakohoa sana mpaka Kamanda akamwonea huruma.
“Babu, nikupeleke hospitali,” kamanda akamwambia.
Yule babu akamwangalia Kamanda usoni, “Ngoja kidogo,” akamwambia.
Akakohoa tena mara mbili kwa nguvu, mkononi mwake kikadondoka kitu cheusi, akakipekuwa kwenye kohozi la njano, Kamanda Amata, alishikwa na kichefuchefu lakini alivumilia.

“Kamanda Amata, kazi hii uliyopewa ni wewe tu unayeweza kuifanya kwa kuwa nakufahamu tangu ujana wako, nakufahamu tangu ukiwa C.C.P kabla hujatolewa kuja idara ya usalama,” yule mzsee akamwambia, akakohoa lakini sasa kikohozi kilikuwa cha kawaida, akaendelea, “Umeiona hiyo chip? (Kamanda akatikisa kichwa huku akiifuta kwa kitambaa) ndani yake kuna kila kitu juu ya sakata hili, Kamanda hii ni hujuma kubwa sana, mimi mwenyewe nimeijua wakati niko pale Msanga Mkuu, Mtwara, najua, najua sana,” akajishika mikono yake usoni na kuvua sura la bandia alilokuwa amelivaa usoni mwake, lililotoka na nywele zile nyeupe, akabaki na sura yake halisi.
Mshtuko mkubwa ukampata Kamanda Amata, akabaki mdomo wazi, hakuamini anachokiona mbele yake, mzimu.
 
RIWAYA: HUJUMA 16
MTUNZI: richard MWAMBE

“Usiogope, sio mzimu ni mimi,” Yule mzee akaongea kwa upole.
“Mwalimu?” Kamanda akauliza.
“Ndiyo ni mimi, sikufa kama unavyojua au niseme mnavyojua, ile ilikuwa ni mbinu yangu ya kutoroka na kwenda katika upeo wa macho na akili zenu, niko hai,” yule mzee alijieleza.
“Ni ngumu kuamini, ni ngumu sana kuamini,” kamanda alisema huku akiwa kajishika kichwa chake.
“Kamanda Amata, ninakuamini sana ndiyo maana nimejidhihirisha kwako, na ninajua kuwa hautamwambia mtu yeyote kuwa umekutana na mimi, lazima uchanganyikiwe, lazima Kamanda na ninajua kwa nini, lakini mimi kufa mbele ya macho yenu ilikuwa ni kuondoka kwa sababu nilishaijua hujuma inayokuja na ambayo ningehusishwa kwa namna moja au nyingine, sikuwa tayari kwa hilo, nikajiondoa kwa njia ile, sasa habari iko hivi,”

Miaka kumi na nne iliyopita
Wizara ya nishati na madini

ILIKUWA ni ajenda ndefu iliyojadiliwa kwa siku kadhaa ndani ya ofisi hiyo nyeti katika serikali ya Tanzania. Yote hiyo ilitokana na ugunduzi uliofanywa na wanasayansi wa Tanzania wakisaidiwa na wale wa Urusi waliokaa katika pwani na bahari ya Hindi huko Mtwara. Madini ya Urani na mengineyo hatari kabisa kwa maisha ya binadamu na viumbe vingine yaligunduliwa kutoka katika kina kirefu cha bahari eneo la Msanaga Mkuu. Baada ya kugundulika na kuwa na uhakika kuwa ndiyo yenyewe serikali ya Urusi ilitaka kuingia mkaba na serikali ya Tanzania ili kuchimba na kurutubisha madini hayo hapahapa nchini. Baada ya kusainiwa kwa mikataba pale wizara ya madini; serikali hizo mbili zilikubaliana kugawana kwa asilimia, ile ya Tanzania 60% na ile ya Urusi 40%. Kwa mkataba huu ilikuwa Tanzania ifaidike sana. Kubaliano linguine lilikuwa ni lile la kuunganisha nguvu za kijeshi kwani nchi hizo mbili zilitaka kurutubisha madini hayo na kutengeneza silaha kali za na nzito za kivita.
Katia ya watu waliokuwa wakifuatilia kila hatua ya mkataba na makubaliano hayo tangu kuanza kwa uchunguzi huo alikuwa ni mwanausalama mashuhuri sana katika idara ya usalama Tanzania ambaye mara kadhaa aliwahi kufanya kazi na mashirika makubwa kama NSA, CIA, MOSSAD na mengine mengi kwa kutoa ushauri au mafunzo fulani ya mbinu za kijasusi; hata alipostahafu bado serikali ya Tanzania ilimchukua kwa kazi maalum ikiwa ni pamoja na kuanzisha idara ya kijasusi, idara nyeti ya kushughulikia matatizo ya kimataifa katika Nyanja ya kiusalama. Mzee huyo waliyempa jina la ‘The Chamelleon’ lakini kwa jina lake halisi ni Mzee Mwambe, kachero aloyewahi kuwekwa kwenye jeneza mara kadhaa ikidhaniwa amekufa lakini alikuwa akifanya danganya toto. Mzee Mwambe alijichanganya katika kundi la watafiti wa Tanzania na kuangalia kila kinachofanyika, kwa kuwa serikali ilimuweka kwa malengo maalum alikuwa akipewa nafasi za juu makusudi ili akutane na watu mbalimbali na ajue nini kinazungumziwa katika mradi huo.

Mzee Mwambe ‘The Chamelleon’, aliushtukia mchezo mchafu unaotaka kufanywa na baadhi ya watu katika mradi huo. Tajiri mmoja mkubwa kutoka nchi za Magharibi, tajiri asiyeonekana kwa macho ya binadamu alikuwa akiyataka madini hayo ama yawe yamerutubishwa au yawe ghafi. Alitoa pesa nyingi sana kuhonga huku na kule na wale wenye uchu wakazipokea pesa hizo na kuzifanyia watakayo. Mmoja wa wanasayansi wakubwa wa Urusi alijiingiza kwenye sakata hilo na kuwa akitoa siri kwa tajiri huyo ya kuwa nini kinaendelea katika mradi huo. The Chamelleon aliyekuwa akiujua mchezo mzima huo, alikuwa akitoa taarifa zake katika idara ya usalama ya serikali ya Tanzania kuwa wakae macho na hujuma hiyo inayotaka kufanywa na baadhi ya wenye uchu wa pesa chafu. Kila aliyekuwa akihusika kwa namna moja au nyingine, serikali ya Tanzania ilikuwa makini kuwawajibisha na kuwatimua kazi wote wanaohusika, hakukuwa na mchezo hata kidogo.
Baada ya miaka kadhaa ikajulikana kuwa ni nani anayetoa taarifa hizo serikalini, walijaribu kila mbinu ya kumshawishi The Chamelleon, kwa rushwa za aina mbalimbali lakini aliwakatalia katakata.
Mkutano wake wa mwisho kabla ya kufa kwake aliufanya na Rais wa nchi pale katika Ikulu ndogo ya Chamwino, Dodoma, kilikuwa kikao cha siri sana.

§§§§§§§
CHAMWINO – DODOMA

ULIKUWA ni mkutano wa siri lakini uliochukua muda mrefu wa kutosha ndani ya Ikulu hiyo ndogo pale Chamwino. Mzee Mwambe, kachero aliyekuwa kazini kwa shughuli maalum alikuwa akikutana na Rais, mkuu wan chi kujadiliana mambo kadhaa. Tayari aliiona hatari kubwa mbele yake, mpango kabambe wa kumuondoa duniani ili wapenda pesa wafanye kile watakacho.
Alipogundua hilo alifanya haraka kumshawishi Rais kuanzisha kitengo hicho cha kijasusi katika Tanzania, TSA, wazo ambalo halikupingwa na mpango ulianza mara moja.
“Sasa unajua kama ulivyosema kuwa ni muhimu kuwa na kitengo hicho, sawa, lakini unafikiri ni nani anaweza kukiongoza, muaminifu?” Mheshimiwa Rais alihoji.
Mzee Mwambe alitoa maelekezo yote mpaka jinsi ya kukiweka kitengo hicho. Baada ya mazungumzo hayo ndipo alipompa taarifa mpya juu ya maendeleo ya kazi za ujenzi wa kituo cha kurutubisha Urani huko Mtwara, lakini alionesha wazi hofu yake ya kupangiwa njama ya kuuawa na wabaya wake ambao walikuwa wakifanya juu chini kuhujumu mkakati huo.
“Nilifikiri kukukabidhi wewe kitengo hiki,” Mheshimiwa alimwambia Mzee huyo.

“Hapana, mpe Madam S, yeye ni mtu wangu wa karibu na ni jasiri sana, msiri aliyebobea kwenye kazi hizi,” Mzee Mwambe akajibu kwa kutoa maelekezo.
“Na upande wa vijana je?”
“Nimemwandaa vyema Amata Ric, yeye atakuwa Kamanda wa kikosi, baadaye tutaona jinsi ya kuwapata vijana wengine wenye hari na uzalendo wa taifa lao, kama unavyojua nimempa kazi nyingi ngumu za kimataifa, amezifanya kwa ustadi wa hali ya juu sana, yeye amefuzu katika kila Nyanja ya mapambano, sasa yuko huko Sierra Leone, kuna kazi nyingine nimempa,” Mzee yule alieleza.
Mheshimiwa Rais aliinamisha kichwa mezani, kisha akainua uso wake na kumtazama Mzee huyo.
“Ok, mi nafikiri kazi uliyoifanya mpaka hapa imetosha, nikuondoa kwenye nafasi yako nisije kukupoteza kama walivyopanga wabaya hao,” Mheshimiwa Rais alionesha wasiwasi wake wa wazi wa kumpoteza Kachero wake wa juu kabisa ingawazje alikuwa amestahafu. Mzee Mwambe alikuwa kimya akimsikiliza, akakohoa kidogo na kusema, “Sawa, ni wazo zuri lakini huna budi kumchagua mtu makini kukaa pale”.
Ilichukua masaa takribani matano kuhitimisha kikao hicho ambacho kilimuacha Rais na maswali mkubwa, shaka nzito na hofu ya kutosha, ‘wananisaliti?’ alijiuliza.

§§§§§

Ilikuwa ni baada ya kuagana na Rais pale Chamwino, Mzee Mwambe alikuwa akitoka na gari yake akiiacha barabara ya kuingilia Chamwino, sasa alikuwa alkiingia barabara kubwa ya Dodoma-Morogoroalipokutana na lori kubwa la mizigo lililoigonga gari yake kwa kishindo, ngao kubwa la chuma la lori lile liliifinya vibaya gari ya Mzee Mwambe na matairi makubwa kuibonda, kisha ile lori haikusimama, iliendelea na safari kama kilomita tano na dereva akaitelekeza na kuondoka.
Hali ilikuwa tete, Mzee Mwambe alitolewa kwenye gari ile kwa shida na kukimbizwa hospitali ya Dodoma kwa matibabu, lakini wakiwa pale Dodoma ilionekana wazi kuwa hawezi kupata matibabu stahiki kwa jinsi alivyokuwa ameumia hasa kwa ndani, hivyo alipewa rufaa na usiku huohuo aliondoshwa na ndege ya serikali mpaka hospitali ya Taifa ya Muhimbili. Pale napo hali ilikuwa hivyohivyo, Mzee Mwambe aliondoshwa na kupelekwa nje ya nchi kwa matibabu, alikuwa huko kwa siku kadhaa ndipo taarifa mbaya ilipokuja Tanzania kuwa Mzee huyo, Kachero wa siku nyingi, The Chamelleon, amefariki dunia katika hospitali kubwa ya Appolo.
Ilikuwa ni taarifa iliyotikisa idara nzima ya usalama katika serikalai ya Tanzania, wakati upande huu unasikitika basi upande mwingine ulikuwa unafurahia, tafrija kubwa iliangushwa katika hoteli ya Embassy pale Dar es salaam, tafrija ya kushangilia ushindi, ‘Tumekata mzizi wa fitna.’ilikuwa kama kauli mbiu.

6…rejea, MOGADISHU
CLUB ya MUJABBA

“Kamanda Amata, mimi sikufa, ile ilikuwa ni mbinu niliyoipanga nikiwa hospitali mara tu baada ya kuipata nafuu na kuhakikishiwa uzima,” Mzee Mwambe alimwambia Kamanda Amata. Mshangao wa wazi ulionekana usoni mwa Kamanda Amata.
“Usishangae Kamanda, inapobidi unafanya hivyo ili kujiondoa machoni mwa watu, na wapo wengi waliofanya hivyo hasa majasusi wan je kwa nini isiwe mimi.
“Sasa unaishi wapi Mzee?” kamanda akauliza.
“Naishi Tanzania, Lindi kwetu, mi nilirudi Tanzania mwaka mmoja baadae, na moja kwa moja nikaenda kuishi kwetu Lindi, lakini harakati zangu hazikukomea hapo, Kamanda, ukiwa mzalendo ni mzalendo tu na ukiwa fisadi ni fisadi mpaka vizazi vyako.

Nilirudi na kuishi maisha duni sana hiyo ilikuwa ni mbinu yangu, nikapata kazi ya ulinzi palepale Msanga Mkuu kwenye duka moja kubwa la Prakesh, ambalo kutoka lilipo, kufika kwenye kile kinu hapakuwa mbali, hivyo niliendelea kufuatilia nyendo zote za ule mchezo bila wao kujua, nilikuwa nina uwezo wa kuingia mle ndani ya jengo lao kwa njia zangu mpaka nilipojua kilichopo, nilipotega vifaa vyangu vya kunasa sauti ndani ya ofisi ya mkurugenzi ambaye alikuwa na asili ya Uarabu ndipo nilipopata siri hii (akamwonesha ile memory card), nikajua kuwa ile meli lazima itekwe pale Somalia kwani huyu mkurugenzi alikuwa na mawasiliano na Maharamia, na ni mchezo uliochezwa, watu wanajua. Siku manowari ile ilipopakia yale makombora kwa ajili ya majaribio, nilikuwa naona kila kitu, kabla haijaondoka mimi niliondoka na kuja Somalia,” Mzee Mwambe akakohoa kidogo kisha akaendelea na simulizi yake ambayo ilimuwacha Amata katika hali ya bumbuwazi, “Unasikia, Kamanda Amata, hawa jamaa wamejipanga, sasa kila unaporudi hotelini kwako hakikisha unapita kaunta utakuta ujumbe wako, ukiona siku hakuna ujumbe wowote ujue nimepatwa na hatari kubwa, naomba tuagane,” Mzee Mwambe akamaliza na kuiweka vizuri sura yake, kisha akainuka na kutoka ndani ya club ile. Kamanda Amata alikuwa akimwangalia mzee huyo mpaka alipopotea, moyoni mwake hakuwa anaamini wala hakuwa haamini, alifikicha macho mara kadhaa kuona kama yuko usingizini lakini sivyo.
 
RIWAYA: HUJUMA
MTUNZI: richard MWAMBE
“Nakubaliana na hilo, lakini huku ni mbali sana, na mi nataka nikamilishe kazi hii mapema iwezekanavyo,” Kamanda akajibu.
“Usijali, kwanza kabla ya kuendelea kufanya kazi hii unatakiwa ufanye kazi moj ya ziada, umpate Jamir, kutoka kwake utapata jinsi ya kuimaliza hii kazi ndani ya dakika chache,” Chamelleon akamwambia Amata.
“Jamir! Bado yupo hai?” Kamanda akauliza.

“Jamir yupo hai, nitakuelekeza alipofichwa, ukiweza ukamtoe ili pamoja au vyovyote vile umalize sakata hili, nitafurahi sana kama utaimaliza hujuma hii na wahujumu wajulikane,” Chamelleone akamweleza Amata.
Kabla ya kuanza mazungumzo yale na Amata kwanza akawataka wale watu wake kutoka mle ndani ili abaki yeye na kijana wake tu. Hali ilipotulia alimtazama Kamanda usoni kisha akashusha uso wake mahala pake.
“Unahitaji kupumzika, macho yako yanaonesha wazi umechoka na una usingizi,” The Chamelleone akamwambia Amata, “…Utakapoamka ndipo utaianza kazi hii kwa umakini zaidi kwa sasa kutokana na uchovu wako hutokuwa makini, watakukamata,” almalizia.
Kamanda Amata akaitikia kwa kichwa na kutulia kochini, “Umepata mzigo?” akamwuliza.
“Ndiyo, nimeupata na baadaye nitauchunguza kuona kama ni sahihi au kuna mchezo mwingine uliochezwa katika hili, nakusubiri uamke ili tuone pamoja, (akamtazama Kamanda kwa makini) naona bado una maswali uliza tu,” Chamlleone alimwambia.
“Hapana sina swali, nahitaji kupumzika,”
“Ok, Kamanda.”

Yule mzee mtu mzima akanyanyuka kitini na kuiendea simu iliyopachikwa ukutani, akaipachua na kuminya tarakimu Fulani kisha akaiweka sikioni; akaongea maneno machache kwa lugha ya kiarabu na kisha kurejea kitini. Haikupita sekunde kumi mwanadada mrembo alitokea katika mlango mmoja kati ya mingi ya jumba lile, akiwa amevalia siketi ndefu iliyonyima nafasi japo vidole vya mguu kuonekana, kuyoka kiunoni kwenda juu alivalia sidiri inayowakawaka kwa vingaro vyake vya kupendeza huku akiwa na kiblauzi cha mtindo huohuo kisicho na vifungo mbele na nikifupi kiasi kwamba hakijafika kiunoni, kwa jinsi hiyo tumbo lake mwororo lilikuwa wazi na kuruhusu kitovu mbonyeo kuonekana wazi.
Moja kwa moja alikuja kwa Kamanda Amata na kumsalimu kwa adabu.
“Mfuate,” ilikuwa sauti nzito ya Chamelleone ikimwambia Kamanda, naye akanyanyuka na kumfuata yule mrembo aliyekuwa akitembea mwendo wa ki-paka ulioyafanya makalio yake madogo kuyumba huku na kule, bila shaka alikuwa miss, Kamanda alijiwazia kichwani mwake huku macho yake yakiburudika kwalo.

§§§§§§

Chumba kikubwa kilimlaki Kamanda Amata, kitanda kikubwa chenye miguu mirefu, kitanda cha kisultani, aliendelea kuwaza.
“Utapumzika hapa na kwa shida yoyote utapiga simu, namba zote zipo hapo, asante,” yule mrembo alimwambia Kamanda Amata.
“We unaenda wapi, mi nilijua unabaki na mimi,” Kamanda akaanza uchokozi. Yule mwanadada akacheka na kutoka nje, lakini kabla hajaufunga mlango alimtazama Amata, “Namba za simu hizo hapo…” akamwambia kisha akaufunga mlango nyuma yake. Kamanda Amata akakitazama kile chumba kwa haraka haraka, akabonyeza itufe Fulani kwenye saa yake na kuigeuzia huku na kule aone kama kuna chochote kilichotegeshwa ndani humo hasa vinaa sauti na vitu vyenye madini ya milipuko. Usalama ulikuwa kwa 100%, akaufunga mlango na ufunguo kisha akajiandaa kujiswafi kabla ya mapumziko.

§§§§

“Fasendy, umefanya nini? Tangu nimeanza kukupa kazi leo umenivuruga akili yangu,” aliongea kwa wahka bwana Shabalah, huku akimtazama mwanamke huyo aliyesimama kando kidogo ya mlango wa kijiofisi hicho ambacho daima hupenda kukutania kwa mipango yao.
“Shalabah, sikufanya makusudi, wakati mimi nimemuweka kwenye shabaha mtu wangu, huyu Jeslaim akanigonga begani kuniambi kitu hivyo bunduki ikacheza nyuzi chache sana lakini kutokana na umbali wa mlengwa tayari ilikuwa ni Off-Target,” akajitetea. Jeslaim aliyekuwa pembeni kidogo akisikiliza juu ya matokeo ya umbea aliouleta, sasa alipambana na jicho kali la Shalabah, macho yakamtoka pima kwa woga, akajua wazi kuwa amekwishaingia matatizoni kwa swala ambalo si la kweli.

“Msilete mchezo katika hi…” kabla hajamaliza kutoa onyo lake simu yake ya kiganjani ikaita kwa fujo, akainyakua na kuweka sikioni.
“Hello…” akaita na kuisubiri sauti ua uapnde wa pili kujibu.
“…aonekani pande zote za jiji? (…) ok, sasa hakikisheni mpo karibu na hiyo gari kwa maana lazima atarudi tu hata kama ni wiki ijayo.”
Shalabah akakata simu na kuipachika kwenye kibweta chake. Akawatazama wale watu wawili, mmoja baada ya mwingine. Kisha hakuwa na la kusema aliwataka kuondoka mara moja.
Na dakika ileile Sharon aliingia mle ndani na kulete habari nyingine kwa Shalabah.
“Sikia, weka watu wawili chumbani mwake, kule kwenye gari weka kama wane hivi kisha wengine wawe tayari-tayari kwa amri yoyote ile, mkiona tu jicho lake mulitungue, Fasendy atasubiri tayari kwa amri utakayompa, mi naandaa kikao cha biashara kesho, jamaa wanakuja kununua yale makombora kesho na wataingia na meli yao hapa usiku wa manane wa kesho hiyohiyo, hakikisha pia ulinzi unaimarishwa baharini, weka doria kali yule majinuni asituharibie,” Shalabah akamaliza na kuketi kitini huku akifungua kile kitambaa cha kichwani na kukiweka juu ya meza, akashusha pumzi ndefu na kubaki akitazama ukuta usiyo na picha wala pambo lolote kama zezeta.

Dar es salaam

Gina binti Komba Zingazinga aliishusha miwani yake myeusi, bado alikuwa ameegemea gari yake upande wa mbele wa boneti, akihakikisha hampotezi mtu huyo ambaye ni windo analolifuatilia siku ya pili sasa. Alimtazama akiwa ametoka katika hoteli ya Kilimanjaro na kuingia kwenye gari maalumu la kupelekea wageni uwanja wa ndege. Naye bila ajizi akajitoma ndani ya gari yake na kuiwasha kisha akaitoa kuifuata ile gari ya hoteli iliyombeba yule bwana.
Kama kawaida ya jiji la Dar es salaam, jumapili hiyo barabara zilikuwa nyeupe kabisa, gari zilikuwa ni chache sana, hivyo haikuwapa taabu kuufikia uwanja wa ndege wa Julius Kambarage Nyerere kule pande za Ukonga. Kati ya gari yake na ile ya hoteli kulikuwa na kama gari nne katikati lakini walipofika pale kwenye kona ya kuingia uwanjani ni yeye alikuwa wa kwanza kuitoa kushoto kidogo gari yake na kuwasha indiketa, hivyo hivyo sekunde chache baadaye na ile gari ya hoteli ikafanya hivyo na kuanza kukunja kona kuingia uwanja wa ndege.

Alishuka na kuufunga mlango wa gari yake, akaipachika tena ile miwani usoni pake na kuvuata hatua za madaha, hatua za mwanamke mrembo kuelekea katika jengo kubwa la uwanja ule, hakuonesha dalili za kumfuatilia mtu wala lolote lile, alionekana kuwa kivyake, moja kwa moja akaufuata mlango wa kuingilia abiria, mlango ambao yule bwana alipita pale muda si mrefu, Gina akasimama mbele ya mwanadada mmoja mrembo aliyejipaka rangi yam domo kama kachinja njiwa kwa meno. Akamsalimi na kumtupia swal, “Umemuona yule bwana mwenye suti ya kijivu?” akamwuliza yule mhudumu. Yule mhudumu akajibu kwa kutikisa kichwa, “Niambie anakwenda wapi sasa hivi?”
“Kwa nini unauliza, mi sio kazi yangu kutoa habari za wasafiri nenda paleeeee ofisi ya Maelezo,” yule mhudumu alijibu huku akimuonesha kwa kidole ofisi ndogo ilioandikwa kwa Kimombo na Kiswahili, Information/Maelezo.

“Sikiliza mrembo,” Gina alianza lugha ya ulaghai, “Nisaidie mwanamke mwenzio, yule mzee ni m’me wangu, kaniaga anaenda Nairobi kikazi sasa mi nataka nijue maana kila wakati ananidanganya”. Gina alisema hayo huku mezani kwa mhudumu huyo kukiwa na noti ya shilingi elfu kumi, yule mhudumu alimtazama na kucheka, ndoa zina mambo, ndo maana sitaki kuolewa, yule mhudumu alijisemea kwa sauti ya kujisikia mwenyewe.
“Anakwenda Mtwara na ndege ya saa 4.30 asubuhi hii,” akajibiwa. Gina akatikisa kichwa juu-chini kuashiri kaelewa.
“Na kurudi lini?” akaongeza swali.
“Leo hii hii jioni, ndege ya saa 12.00,” akajibiwa Gina akafurah9i moyoni, akaaga na kutoka nje, moja kwa moja akaenda na kusimama mbele ya luninga kubwa iliyokuwa ikionesha ratiba ya ndege zinazoondoka. Air Tanzania - TC 206 saa 4.30 as- Dar – Mtr, aliisoma ile ratiba na kuitazama saa yake ilikuwa imebaki dakika sabini na tano hivi ile ndege iondoke, akasogea mahali ambapo hakuna watu akaiinua saa yake ya mkononi na kubofya kitufe fulani, “Mission Mtwara,” akatamka maneno hayo huku akitazama ile saa.

Sekunde chache baadaye saa yake ikamfinya kwa upande wa chini, akaitazama ilikuwa ikiwaka-waka kijimwanga cha kijani, aliitazama na kubofya mahala fulani, ile saa ikatoa kijimkanda chenye maandishi katika moja upande wake, Gina akakavuta na kukasoma. Bon Voyage aliyasoma maneno hayo ya Kifaransa yaliyomtakia safari njema, tayari alielewa kuwa anatakiwa aende Mtwara muda huo bila kuchelewa.
Kwa hatua za haraka, alikimbilia kwenye ofisi moja ya Air Tanzania na kuingia ndani.
“Samahani dada, ninahitaji tiketi ya sasa hivi nakwenda Mtwara,” Gina alieleza.
“Ndege imejaa,” akajibiwa.
“Hata kama, ni bora abaki rubani mimi niondoke,” Giana akasisitiza. Yule mwanadada aliyevalia nguo nadhifu, sketi nyeusi na blauzi ya rangi ya machungwa ilipachikwa na kitambaa shingoni mwake kikining’inia kwa nyuma, aliinua uso wake wa duara na kumtazama Gina, Mtazame vile, ka’ katumwa, alijiwazia na kisha akasimama mbele ya Gina kati yao wakitengwa na meza kubwa yenye fomeka safi juu yake, akamsogezea sura yake Gina kama anamshushua kitu, “Ndege imejaa mdada, umeelewa?”

“Hata kama imejaa, lazima niende, uwe na lugha ya kistaarabu kwa wateja,” Gina alaing’aka na kufungua pochi yake, akatoa kikadi maalum na kumpa, yule mwanadada alikipokea na kukigeuza-geuza, hakuamini. Ilikuwa kadi maalumu inayomtaka ampa usafiri wakati wowote bila gaharama ya yoyote bila swali lolote, usafiri wa kwenda popote ndani ya ardhi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Yule dada akagwaya, akajirudisha kitini kama aliyesukumwa na mtu, akabonya kompyuta yake na kuingiza tarakimu Fulani ndani yake, kisha akampa ile kadi Gina.
“Na ya kurudi mrembo, ndege ya saa kumi na mbili jioni,” Gina akaongezea kumwambia kwa nyodo ilhali akijua wazi kuwa anamkera mwanadada huyo. Dakika mbili alikuwa na tiketi mkononi, akaondoka zake.

UWANJA WA NDEGE – MTWARA

SAA 5.15 asubuhi walishuka katika uwanja wa ndege wa Mwara, jua lilikuwa likiwaka kwelikweli, joto la mvuke wa bahari lilikuwa likihisika bila kificho. gina alimtazama yule bwana ambaye alitoka na mkoba wake na kuiendea meza ya ukaguzi na wakati huohuo Gina aliifikia meza hiyo. Kabla hajauliza chochote alijifanya kuinama kuweka vizuri kiatu chake na wakati huohuo akabandika kidubwasha kidogo kwenye mkoba wa bwana huyo ambao ulikuwa chini sakafuni.
“Samahani dada, naweza pata tax hapo nje?” Gina aliuliza na kupewa jibu. Akatoka nje na kutazama, kweli, tax kadhaa zilikuwa eneo lile, akaichagua moja na kuingia kiti cha nyuma.
“Wapi uelekeo dada?” akauliza dereva tax kwa lafudhi ya Kimakonde ambayo haikujificha kabisa ukijumlisha na chale alizokuwa nazo usoni mwake, hivi hawa watu bado wapo! Alishangaa peke yake, “Tulia nitakwambia,” akamjibu.

Dakika kama tano baadae yule bwana alitoka na kuingia kwenye Range Rover moja iliyokuwa ikimsubiri. Muda huohuo Gina akachomoa kidubwasha kidogo cha kupachika sikioni chenye mfano wa kile kifaa atumiacho Kiziwi katika kunasa mawimbi ya sauti (shine sikio au audiometer) na kukipachika sikioni mwake. Kila mtu aliyemuona alijua binti huyo mrembo ni kiziwi kumbe la, kutoka katika kile kifaa aliweza kusikia mazungumzo yote ya ndani ya gari alilopanda yule bwana.
“Ok, twende, nipeleke Makonde Hotel,” Gina alimwambia yule dereva na kisha wakaondoka eneo lile, “Usikimbie sana kuna ndugu zangu kwenye gari ile sasa usikae mbali nao,” alimwambia yule dereva na safari ikaendelea….
 
RIWAYA: HUJUMA 19
MTUNZI: richard MWAMBE


HOTELI Makonde, ni hoteli safi nay a kisasa iliyojengwa pembezoni kabisa mwa fukwe ya Shangani. Watu wengi walipenda kwenda kupumzika katika hoteli hiyo iliyokuwa ikisifiwa kwa utulivu, huduma na usafi wa hali ya juu. Hoteli hiyo iliyokuiwa ikimilikiwa na kijana wa Kimakonde kutoka Mtwara ilikuwa ni hoteli inayovuma sana katika ukanda wa pwani ya Afika Mashariki. Vigogo na matajiri mbalimbali hupenda kwenda kupumzika katika hoteli hiyo kila mwisho wa juma.
Bw. Goloko Mikidadi, mtu wa makamo aliyewahi kuwa kigogo wa serikali ya awamu ya kwanza alikuwa ameketi katika moja ya viti vya kiutamaduni vilivyokuwapo katika ukumbi mkubwa wa hoteli hiyo. Meza iliyotakiwa kuwa mbele yake ambayo kwa sasa ilikuwa kushoto kwake ilibeba chupa kubwa la John Walker na kibweta kilichojaa vibonge vya barafu. Bilauri yenye kiuno ilitulia na kinywaji hicho ndani yake kikisubiriwa kumiminiwa katika tumbo la binadamu huyo. Ni siku nyingi sana alikuwa hajafika katika mkoa ule wa Mtwara, mkoa ulio katika miisho ya nchi, upande wa Mashariki ya Kusini. Alikuwa akiingalia saa yake iliyokuwa ikimuonesha kuwa ni saa tano ikikimbilia kuwa na dakika kumi na tano hivi. Gari iliyokuwa imemleta pale ilikwishaondokakitambo kuendelea na shughuli nyingine. Aliinua ile bilauri na kuipachika kati ya midomo yake na kuibinua kwa mkono wake wa kuume kwa madaa mazito, maisha si ndiyo haya, alijiwazia pindi akiiteremsha mezani ikiwa tupu.

Kutoka mbali, aliiona boti iliyokuwa ikija kasi sana, kwa kuwa yeye alikuwa amegeukia upande wa bahari; aliweza kuiona bila tabu boti ile iliyokuwa ikija kwenye fukwe ya Shangani. Yule bwana alikenua kidogo kisha akafunga kinywa chake, kama ungekuwa jirani naye basi ungejua kuwa ana tatizo la kiakili, lakini haikuwa hivyo bali alikuwa akimfurahia mtu aliyetakiwa kukutana naye siku hiyo.
Ile boti ilifika mpaka katika gati ndogo pale Shangani ambayo hutumika na watu wa michezo ya yacht, nahodha wake akaifunga kamba na kupeana mikono ya asante na yule bwana aliyemteremsha katika boti ile. Alikuwa mnene kiasi, mwenye ngozi ya kizungu iliyopigwa jua la kutosha lililoifanya sasa ionekane kama Mhindi mwekundu, alivaa jeans aina ya Lee na raba matata sana huku kichwani akijifunika kwa pama kubwa lililopambwa na picha ya wanyama wakubwa watano wanaopatikana Tanzania. Alivuta hatua na kuvuka kwa hadhari sana ile barabara iliyokuwa ikikatisha mbele yake. Akazikwea ngazi na kufika ghorofa ya kwanza, ghorofa iliyotengenezwakwa miti na mbao ngumu.
“Karibu Komredi, nimekuwa nikikusubiri kwa hamu sana,” Bwana Goloko Mikidadi alisimama na kumpa mkono wa karibu yule mwenyeji wake.

“Naitwa Mr. Reubellen Vinchinsk,” akajitambulisha.
“Naitwa Bwana Goloko Mikidadi,” naye akajitambulisha.
Kisha wawili hao wakaketi chini kwa mtindo wa kutazamana. Bwana Goloko akavuta mkoba wake na kuufungua kisha akatoa, akatoa kabrasha moja jembamba na kuliweka mezani. Reubellen Vinchinsk akavuta lile kabrasha na kupitisha macho kisha akaingiza mkono katika mfuko wake wa shati na kuchukua peni, akaweka saini mahala Fulani kisha akamrudishia yule bwana naye akaweka saini mahala pengine, wakagawana kila mmoja nakala yake, kisha wakapeana mikono.
Nukta hiyohiyo mhudumu alifika na kuleta vibonge vya barafu vingine pamoja na bilauri ya pili kisha akammininia kinywaji na kuondoka. Wale mabwana wawili waliinua bilauri zao na kugonga cheers, kisha wote wakajimiminia vinywaji hivyo matumboni mwao mpaka vikaisha ndipo wakashusha chini zile bilauri.
“Bwana Goloko, siamini kabisa kama huu mpango umekuwa sawa, kwa jinsi nilivyokuwa napewa taarifa za mambo mengi yaliyotukia huko nyuma juu ya hili, lakini sasa ndiyo naamini kwamba limewezekana,” Reubellen Vinchinsk alimwambia Bw. Goloko.

“Ni kweli, ni mambo mengi sana yametukia, watu wamepoteza maisha katika mkataba ishu hii, watu wameuana hapa kaka, fikiria mkakati ulianza tangu mwaka 1975, ukaleta tabu na katikati ukasimamishwa kwanza, Mwalimu Nyerere alikuwa mkali sana, kila aliyejaribu kufanya blaa blaa ama alitimuliwa kazi, alifungwa maisha na wapo walionyongwa. Kipindi kile mimi nilikuwa katibu wa wizara nyeti ya Maji Nishati na Madini, nilitimuliwa ofisini kama mbwa, ikabidi tukae chini na wadau kuona mbaya wetu ni nani, tulipomgundua, tukamfutilia mbali,” Bwana Goloko akamwambia yule Mzungu koko.
“Aisee, (akamwinamia) mlimuua?” akauliza yule mzungu
“Sasa tufanye nini komredi? Tulimuua ni muda mrefu sasa hata tumemsahau.”
“Alikuwa kitengo gani hapa au serikalini?”
“Yule bwana alikuwa idara ya uchunguzi, lakini kumbe tuligundua kuwa ni afisa wa ngazi ya juu wa usalama wa Taifa hapa Tanzania, na ndiye alikuwa akitoa taarifa Ikulu moja kwa moja, hatukuona haja ya kumuacha, tulimuua dakika chache akitoka kwenye mkutano wake na Mwalimu Nyerere pale Chamwino njia panda,” Goloko alibwabwaja.

“Mlifanya la maana sana komredi, watu kama hao ni kuwafanyia hivyohivyo tu,” yule mzungu akamwambia kisha wakaendelea kunywa.
“Ok, tuyaache hayo, sasa mkakati wa leo unakuwaje?” yule mzungu aliuliza.
“Usiku wa leo naondoka, naelekea Mogadishu, pale tutakuwa na kikao cha mauziano ya ule mzigo kisha kamisheni za kila mmoja zitafanyika baada ya kikao hicho,” Goloko alisema.
“Nategemea akaunti zitacheka soon.”
“Masaa ishirini na nne tu komredi utatajirika kwa kazi uliyoifanya…” kabla hajamaliza kusema wote wakaangua kucheka.
Bw. Goloko Mikidadi akaitazama saa yake tayari ilikuwa imetimu saa nane za mchana, akaagana na mwenyeji wake kisha kila mtu akachukua hamsini zake.

§§§§§

Wakati wawili hao wakiongelea juu ya ule mkakati mzito na ulipofikia, Gina alikuwa ndani ya chumba kidogo alichopanga katika lodge moja iliyokuwa mkabala na hoteli hiyo, aliweza kusikiliza mazungumzo yote huku akirekodi katika kimashine chake kidogo. Alipojiridhisha na alichokipata, alifunga vifaa vyake na kutia mkobani, hakuona haja ya kupoteza pale, alichokitaka sasa ni kumfuatilia yule mzungu ili amjue ni nani na anatoka wapi, alifunga mlango nyuma yake na kuteremka ngazi kumuwahi yule mtu. Alipofika chini alipita kwenye ujuia mdogo na kutokea nyuma ya lodge ile, eneo ambalo lilionekana kuwa ni sehemu ya kufulia nguo, aliruka ukuta mfupi na kutua kwa nje ambako moja kwa moja unaelekea baharini, akavuta hatua ndogondogo na kutokea upande wa kushoto wa lodge hiyo; akachukua ujia na kuufuata taratibu kisha akateremka na barabar ya vumbi iliyokuwa ikielekea baharini. Alipofika jirani kabisa na ile yacht club, akatulia na kumtazama yule bwana mzungu akiwa analipia ile boti yake kisha akaingia na wale viajana wake wakaliwasha na kuliingiza majini, Gina aliinua camera yake ndogo lakini yenya nguvu sana na kupiga picha boti ile. Hakuona haja ya kumfuatilia kwani alichokitaka alikwishakipata.

§§§

MADAM S alimtazama Gina pale alipoketi usiku wa siku ile, “Una uhakika?” akamwuliza.
Asilimia 100, mimi ndiye nilikwenda Mtwara, yule ni Bw. Goloko mwenyewe na mazungumzo yao ninayo kwenye mashine.
“Unasema?” Madama aliuliza kama mtu aliyeshtuliwa.
“Mazungumzo yao ninayo katika masine yangu,” Gina akajibu tena. Kisha akaufungua mkoba wake na kutoa ile mashine akampa Madam S. Madam S akasikiliza mazungumzo yote ya wawili wale, akitazama sss yake ilikuwa tayari ni saa tatu usiku.
“Kama vipi mi’ naona tu n’naona tungemkamata usiku huu,” Gina alishauri.
“Hapana, muache aende ili tumkamate na kidhibiti,” Madam S alijibu, “Asante Gina, naona sasa umeanza kukomaa taratibu, kaa tayari ukihitajika msaada huko Somalia ujue hiyo ni nafasi yako na hakuna mwingine.”
Gina aliitikia kwa kichwa alipokuwa akiinuka tayari kwa kuaga na kuondoka, kabla hajaufikia mlango alisikia Madam akiita, “Gina!” akageuka na kuitika “Yes Madam,”… “uwe muangalifu sasa.”

§§§§§

Kamanda Amata alifumbua macho na kurudiwa na fahamu zake, aliliendea dirisha na kuvuta pazia kando, kigiza kilikuwa tayari kimelivamia anga na kuruhusu nyota nzuri kulipamba anga lile, akameza funda la mate na kuliachia lile pazia kurudi mahala pake. Kwa hatua fupi fupi akakifikia kitanda na kujitupa juu yake, mawazo yalifudikiza fikra zake, aliwaza na kuwazua akapanga na kupangua. Akajaribu kutathmini mpaka hapo alipofikia amefikia wapi, akajisifu kwa ushujaa wake mwenyewe lakini bado aliumiza kichwa jinsi ya bkumaliza na kupata kile alichotumwa na serikali yake, akajiinua tena na kulivamia bafu, akaoga kwa muda mrefu huku akifikiri la kufanya.
Alipohakikisha kuwa yupo tayari kwa kazi usiku ule ambao kichwa chake kiliupa jina usiku wa kazi aliinua simu na kupiga namba Fulani na haikuchukua muda mlango ule ukafunguliwa na binti yuleyule akaingian na kuufunga nyuma yake. Alimkuta Kamanda Amata amekwishajiweka tayari ndani ya kadeti nyeusi, viatu vyeusi vyenye soli ya mpira isiyofanya kelele, fulana nyeusi iliyomshika mpaka kwenye koo, kaba shingo yenye mikono mirefu. Tayari alikuwa amekwishapanga kila kinachohitajikamwilini mwake kama silaha na bastola yake aliyopewa na Chiba ilikuwa tayari upande wake wa kuume wa kiuno.

“Waaaaooohhh!” yule binti alihamaki huku akimsogelea Kamanda Amata pale aliposimama, kwa kutumia vidole vyake laini alitomasatomasakifua cha Amata kilichoonekana kujaa vizuri kimazoezi, Amata akaushika mkono wake na kuushusha chini.
“Nipeleke sebuleni,” alimwamuru yule mrembo naye akatii, akaongoza na kumtoa Amata mpaka sebuleni ambako alimkuta Chamelleone akiwa ameketi akitazama luninga kubwa iliyo mbele yake.
“Naona Kamanda wangu uko tayari,” Chamelleone alimwambia Kamanda Amata huku akijiweka vizuri kitini, “Pata kinywaji kidogo kikuchangamshe mwili, najua mpiganaji hatakiwi kulakula ovyo,” wote wakacheka. Kamanda Amata akainua glass na kugonga cheers, na mzee yule kisha akabugia pombe yote kwa funda moja tu.
“Asante sana mzee, mimi naona niingie town nina mambo ya kukamilisha na kisha nitakujuza kinachoendelea, kuhusu hilo linguine tufanye wakati mwingine,” kamanda alitoa shukrani nna wakati huo alikuwa akiuendea mlango wa mbele wa nyumba hiyo. Gari ile ile iliyomleta ilikuwa ikimsubiri nje, akaingia na kurudi mjini.

§§§§§

Vijana watatu waliokuwa jirani kabisa na gari ya Amata pale katika kituo cha mabasi cha W Sheikh Abaadir walikuwa wameanza kukata tama ya kumnasa mmiliki wa gari hilo. Walikuwa wakibadilisha aina za mikao au misimamo wakingoja na kungoja tangu mchana wa siku hiyo.

Kule hotelini nako vijana waliowekwa kuizingira hoteli ile, walingoja bila mafanikio, kila walipojaribu kufanya mawasiliano huku na kule mtu nhuyo hakuonekana kabisa katika viunga vya jiji la Mogadishu, iliwasumbua akili, walihaha.
“Sasa atakuwa kajificha wapi hayawani huyu?” Sharon alijiuliza kwa sauti ya chini huku akiyupa nje ya gari kichungi cha sigara iliyokwisha, akasonya kwa hasira. Fasendy mwanamke pekee aliyekuwa juu ya landcruiser hiyo yenye mtutu mkubwa wenye nguvu alitulia palepale akicheza gemu katika simu yake. Mpaka giza lilipokuwa likiingia hawakumuona Kamanda Amata wanayemsubiri wala kivuli chake, kila mmoja akakata tamaa. Mara redio iliyokuwa mkononi mwa Sharon ikakoroma kuashiria kuna taarifa mpya inayotaka kuingia muda huo…
 
Back
Top Bottom