RIWAYA: Ripoti kamili

RIWAYA: Ripoti kamili

Kuna wanaume wengi hujitamba kuwa wao wanawajua wanawake nje ndani huenda na wewe ni mmoja kati yao. Kama ni kweli wajiaminisha kuwa unawajua viumbe hawa nje ndani nachukua fursa hii kukupa pole.
Wanawake ni mfano wa kitabu kikubwa kilichosheheni kurasa nyingi zilizonakshiwa kwa maandishi madogomadogo tena yaliyoandikwa kwa lugha ya kigeni usiyoielewa hata chembe.
Jiulize utawasoma vipi na kuwaelewa wanawake???

NA HII NI SEHEMU YA SABA.......

“Tina nimevumilia mengi hadi leo hii ninapozungumza na wewe haya, mengine yanatia hata aibu kuyasimulia. Najisikia aibu sana kwa sababu tu niliujua ukweli huku nikiwa bado nakupenda sana, unaikumbuka safari yangu ya ghafla kwenda Kilimanjaro.... nilikuwa sina jiopya sana lakini nilienda kuupooza moyo wangu katika baridi lile maridhawa kutoka katika kilele cha mlima Kilimanjaro. Niamini mimi kuwa sikuwa na jingine zaidi ya hilo. Kuna mambo mengine unaweza ukamsimulia mtu akakuona wewe mjinga kupindukia, kuna jambo hata mama yako mzazi ukimueleza anaweza kukuona mtoto wake unaelekea kurukwa na akili kwa sababu tu hauchukui maamuzi ambayo angekuwa yeye angeyachukua.
Na nd’o maana sikutaka kwenda kujipooza nyumbani kwa mama yangu, sikutaka kwenda kwa marafiki, sikutaka hata kwenda kwa ndugu na jamaa zangu wa karibu najua kuna siku uchungu ungenizidia na ningesema kila kitu, nikaamua niende Kilimanjaro mkoa ambao hapo kabla sikuwahi kufika, hivyo sikuwa na mtu ninayemtambua kule. Hii ilinipa sababu za kuendelea kuwa mvumilivu.. kila yaliponizidia nilikuwa najifungia chumbani na kulia sana... hiyo nd’o ilikuwa tiba pekee.” Nilisita na kumtazama Tina aliyeonekana kutoelewa sababu hasa ya mimi kusafiri hadi Kilimanjaro.
“Tina unakumbuka nikiwa Kilimanjaro nilikupigia simu na kukueleza kitu gani mke wangu?” nilimuuliza. Akatikisa kichwa kuashiria kukubalia.
“Sawa, nilikueleza kuwa Steven kijana aliyekuwa anatufugia kuku pale nyumbani aondoke ukaniuliza kwanini nimesema hivyo nikakueleza kuwa nilikuwa ndotoni wakati naongea na wewe yakaisha.... si kweli kwamba nilikuwa ndotoni. Nilikuwa na akili zangu timamu sema siku hiyo uchungu ulipitiliza hali yake ya kawaida nilium,izwa na hisia, nikajitazama mimi nilikuwa nina mapungufu gani haswa, kwabnza kufikia wakati ule pesa ya kuhonga msichana yeyote nilikuwa nayo na ulikuwa unajua kabisa maisha yetu yamebadilika nd’o maana hata tukaanza kufuga kuku, tukahamia nyumba kubwa ya kutosha na tukaanza ujenzi wa nyumba yetu. Lakini sikuona haja ya kujaribu ladha ya mwanamke wan je ulikuwa unanitosheleza sana, kilichoniumiza ni hali ya wewe kutoridhika, najua haujui kama niliwahi kuketi na Steven tukazungumza.....” nikasita na kumtazama Tina akinipigia magoti huku akinisihi nisiendelee kumuadhibu kwa maneno yangu makali. Alilia sana macho yakawa mekundu na yakiwa yamevimba sana..... nilijisikia vibaya kumuona vile lakini nilijitahidi huruma isinitawale.
“Keti Tina, bila kuzungumza ninaweza kufa muda wowote. Niache tu nizungumze.....
Nilizungumza na Steven akanieleza kuwa siku moja uliwahi kumkaribisha mwanaume pale nyumbani na sio yule mwanaume wako wa kwanza...... kuna kitu kisichokuwa cha kawaida Steven alikigundua na wewe ukafahamu kuwa amegundua. Ukamsihi asinieleze jambo lolote lile na yeye akakuopa sharti kuwa ili akutunzie siri basi lazima na yeye umpe anachotaka, na hapo akakuomba penzi lako. Tina ukasalimu amri mbele ya kijana yule eti na yeye ukamruhusu... tena wakati huo kaSonia kalikuwa kadogo kweli, hukukaonea aibu Tina?? Ama isiwe aibu, haukukaonea huruma kwa kitendo hicho.... ok nilisema sitaki useme lolote hadi nitakapomaliza naomba basi unieleze huyo mwanaume aliyekuja ukamuingiza chumbani kwangu ni nani??” nilikoea pale na kumtazama usoni.
Huku akiwa anatawaliwa na kilio cha kwikwi Tina alinieleza mkasa wa kwenda kwenye harusi ya rafiki yake, harusi aliyoenda kinyemela pasipo kuniaga.
Akanieleza kuwa akiwa huko harusini wakati wa kutoka akaibiwa pochi yake, na mbaya zaidi hakuwa na mwenyeji zaidi ya shoga yake huyo ambaye alikuwa amelewa vibaya mno akiwa hajielewi kabisa, katika hangaika ya hapa na pale ndipo akakutana na mmoja kati ya washiriki katika harusi hiyo, akamuombea lifti kwa rafiki yake, kweli akapata lifti.... akamueleza huyo bwana sehemu aliyokuwa anaishi jamaaakamueleza hakuna shida ila kuna kifaa fulani lazima akipitie mahali na ndipo atampeleka nyumbani.... mwenye chake muheshimu Tina hakuwa na kipingamizi, wakaenda nyumbani kwa huyo bwana, baada ya kuchukua kifaa na kukifunga garini kama alivyoongopa eti gari likagoma kuwaka, na hapo ilikuwa tayari saa nane usiku.
Nikamkatisha Tina asiendelee kusimulia kisa kile kwa sababu tayari nilikuwa nimeanza kuupata mwanga.
“Oooh! Ni siku hii ambayo ulirejea asubuhi ukaniambia kuna rafiki yako alizidiwa ukampeleka hospitali?” nilimuuliza huku nikilazimisha tabasamu lakini moyoni ikiwa ni hasira inanichemka. Tina akatikisa kichwa kukiri....
Ndugu msikilizaji na msomaji wa ripoti hii, licha ya kuwa mwanamke aliletwa kuipamba dunia na pia kuwa ubavu wetu wanaume. Mwanamke alibarikiwa kitu kingine cha kushangaza, mwanamke akiamua kabisa kukuongopea anakuongopea na unakubaliana naye kabisa, sijui ni ile sauti yao bembelezi waliyobarikiwa nayo, sijui ni yale macho yao ya kurembua waliyotunukiwa?? Lakini hakuna kiumbe mwenye ushawishi wa haraka kama mwanamke!!
Yaani siku ambayo Tina aliniongopea kuwa anatokea kwa rafiki yake, nilimuamini sana na nilimpa pole ya dhati kutoka katika sakafu ya moyo wangu kisha nikamkumbatia kwa nguvu, nakumbuka hata neno nililomueleza siku ile.
Nilimwambia kamwe aischoke katika kutenda mema... akajibu AMINA!!
Kumbe alikuwa amebeba siri nzito sana.....
“Tina usijiulize nimeyatoa wapi mashaka hadi kufikia kuujua mkasa wa Steven kijana wetu wa kufuga kuku. Sikuwahi kukueleza ila ni kwamba siku kadhaa baada ya tukio lile na niliposhiriki na wewe tendo la ndoa, nilianza kupatwa na muwasho jambo ambalo si kawaida kabisa kwangu na si la kawaida kwa sababu nacheza mchezo salama nikiamini na wewe mwenzangu upo hivyo....... sasa Tina mpenzi wangu yaani kweli ikatokea bahati mbaya basi ukafanya zinaa na huyo mwanaume ama na hao wanaume yaani hata kuwakumbusha kutumia kinga mpenzi wangu huwakumbushi. Hivi ungeniambukiza Ukimwi mtoto wa watu mimi leo ungewaelezaje wazazio wangu labda... nambie ungewaelezaje wakuelewe!!!
Nilienda kwa daktari baada ya miwasho ile akanieleza ni dalili ya gonjwa la zinaa, nikamueleza naambukizwaje labda akanieleza gonjwa la zinaa haliambukizwi kwa kugusana migoni, linaambukizwa kwa kuifanya zinaa yenyewe. Akanieleza huku akitabasamu.
“Sasa bwana we naona pete kidoleni si una mke wewe?” nikamjibu ndio.
“Achana na hizi mechi za ugenini mkuu, watakuharibia hawa. Tulia na mama watoto....” alimaliza daktari yule huku akinielekeza chumba cha sindano.
Baada ya huduma ile ndipo akili yangu ilipoanza kuniwasha huku ikitaka majibu ya upesi sana, maana mimi nilikuwa ninao uhakika kuwa sijacheza mechi za ugenini kama alivyosema daktari basi kama sio mimi basi Tina amecheza na mwisho ndo huu kuniambukiza..... nilighadhabika sana Tina na kama unayo kumbukumbu vizuri kuanzia wakati huo nilianza kutumia kinga nikiwa na wewe ukaniuliza sababu nikakuambia sitaki tupate mtoto wa pili wakati Sonia angali mdogo sana.
Wala hilo halikuwa tatizo, tatizo lilikuwa moja tu nilikuwa nahofia unaweza kuniua, kuanzia hapo ndoa yetu tamu ikageuka vita vya kimyakimya......


**Ni Ripoti kamili iliyofanyiwa utafiti wa kina, jiulize nini mwisho wa ripoti hii......... je ungelikuwa wewe ungelifanya nini??

Usikose muendelezo wa mkasa huu wa mapenzi.....
 
Wanawake hulalamika sana karibia katika kila kitu kuwa wanaonewa ama kunyanyaswa. Na wanawake hudai kuwa adui yao wa kwanza kabisa ni mwanaume... lakini hii haipo sawa, adui wa kwanza kabisa anayewanyanyasa wanawake na kuwanyima haki zao ni KUTOJIAMINI.

NA HII NI SEHEMU YA NANE.

“TINA hadi sasa wewe ni mke wangu kabla ripoti hii haijamalizika lakini sijui itakuwaje baada ya ripoti hii lakini nitapenda kama utakuwa balozi muhimu kwa wanawake wenzako, nenda ukawaeleze kuwa nguvu ya uhakika ya mwanamke ni kujiamini na kosa kubwa kabisa wanalofanya wanawake ni kujifanya wanajiamini wakati hawajiamini. Naamini unaelewa maana ya kujiamini na kujifanya wanajiamini.
Na kama haujaelewa nitatumia mfano huu.
Mwanamke akiitwa na mwanaume faragha na hana mahusiano yoyote na mwanaume yule na moyo wake ukajipa tahadhari kuwa huenda wito ule si salama. Mwanamke akasema sihitaji tukutane huko nahitaji tukutane sehemu ya wazi huko ni KUJIAMINI.
Mwanamke huyohuyo akipata wito kama huohuo, na moyo ukapatwa na mashaka, akaamua kuvaa suruali inayobana akiamini kuwa ndiyo kinga thabiti ya kuepuka lolote litakalotokea huko, huyu anajiafanya anajiamini lakini hajiamini. Na wengi kati yenu mnaangukia daraja la pili, kujifanya mnajiamini huku hamjiamini na huyu ndiye adui yenu mkubwa.
Tina nahitaji uwe mtulivu na uamini kuwa haya yametokea kwa sababu maalumu huenda umechaguliwa kuwakomboa wenzako kifikra.
Tabia ya wasichana kujifanya wanajiamini ndo ilikukuta Tina mpenzi wangu, halafu kama ilivyo akili ya wenzako wengi wanajifanya kujiamini. Ukaona suluhisho pekee ni kumvulia mwanaume nguo akufanye anavyotaka, sikia Tina kizazi hiki kinateketea kwa kukosa maarifa, ukimkubalia mwanaume kuwa unamvulia nguo ili akutunzie siri basi umeamua mwenyewe kwa hiari yako mwenyewe kurejea zama za utumwa, leo ataonja na kusema hataonja tena lakini kumbuka ile siri haifutiki katika kichwa chake milele. Siku akijisikia tena anakwambia uende, mazoea yanageuka kuwa tabia.. hutaki anavujisha siri zako.
Kipi bora, kupatwa na ajali moja kisha ukaamua kuzungumza na mumeo huku ukijutia kilichotokea?? Ama kumficha mumeo na kuendelea kuhudumia wanaume watatu kwa wakati mmoja.

Nilikuwa nakuonea huruma sana Tina wangu nilipogundua kuwa sasa unanihudumia mimi, unamuhudumia Steven kijana wetu wa kufuga kuku, pia unamuhudumia yule bwana aliyekupa lifti na kama hiyo haitoshi mume mwenzangu aliyekutoa usichana na yeye alikuwa pale katika foleni akihitaji huduma yako.
Tazama jinsi ulivyokuwa umeubeba mzigo mzito..... faida moja mliyonayo wanawake ni kwamba mnaweza kuhudumia sehemu tofautitofauti na uchungu mkaendelea kuutunza nyie pekee bila hawa wahudumiwa kushtuka kama wapo wengi.
Maana nyie hamuishiwi vijisababu, na sauti zenu za kubembeleza ni kisu chenye makali ya kutisha.

Tina hakuna kiumbe aiyeridhika linapokuja suala la mahusiano kama mwanaume, mwanamke anaweza kuridhika na hata kama hajaridhika kuna ugumu sana wa kutafuta pengine pa kujiridhisha. Tazama mwanaume ni rahisi kupata msichana wa nje kuliko mwanamke kupata bwana mwingine......
Namaanisha kwamba ukimvulia nguo leo kesho atawavua wengine. Ukitoka hapa naomba uyawasilishe haya vyema, waambie wasichana kuwa dawa ya kupendwa sio kujilahisisha!!!
Waambie kuwa wewe Tina ulikuwa mke wa mtu na ukajirahisisha kwa bwana wa zamani na mwisho wa siku umekutana na siku mbaya kama hii ya kusomewa ukweli wa mabaya yako yote kipande kwa kipande!!”
Nilisita nikavuta pumzi na sasa nikarejea tena katika kijitabu changu kile, lakini jicho langu likimshuhudia Tina akiwa anahema juu juu, sasa machozi yalishakauka na sidhani kama yangeweza kutoka tena.
Ndugu msikilizaji usiombe yakakukuta!! Yasikie kwa marafiki ama uyaone katika filamu lakini yasikukute, awali nilisema mke anauma sana, narudia tena na tena mke anauma hasahasa mke wako halali.....

“Tina mpenzi wangu unaponyanyua kinywa chako na kumueleza mtu kuwa unampenda kwa moyo wako wote, ni heri uulize kwanza moyo wako sio tu mdomo unajiropokea kwa sababu mwili umepandwa na hulka. Ninajiuliza mpaka leo hivi ni kweli ulivyosema unanipenda ilikuwa kutoka moyoni mwako?” nilimkazima macho na kumruhusu kunijibu.
“Na..nilimaanisha kutoka moyoni lakini.....”.... sikutaka kumruhusu aendelee kusimulia, nilimziba mdomo wake na kumweleza kuwa jibu lile lilikuwa limenitosha kabisa. Akatii, nikaendelea kuzungumza.
“Asante sana kwa sababu ulinipenda pasipo kulazimishwa na mtu yeyote yule, hili ni jambo la heri sana. Nakumbuka hata siku za awali wakati nazozana nawe kuhusu kunikubalia nilikueleza kuwa sina chochote cha ajabu cha kukufanya wewe uwe nami, nilikuelexza kuwa sina elimu kubwa bali najua kusoma na kuandika, nilikueleza sina mali nyingi lakini kamwe sitaki kubaki katika umasikini kwa sababu nilibarikiwa kuwa na viungo vyote kamilifu, nilikueleza kuwa sishindani na mwanaume yoyote kuhusu kuwa na mvuto bali namshukuru Mungu kwa uumbaji wake aliokusudia kwangu, na mwisho nilikueleza kuwa nina mapenzi yamejaa tele na yapo maalumu kwa ajili yako..... awali ilikuwa ngumu lakini hatimaye ukanikubali huku nikiwa nimekueleza yote kuhusu mimi. Sikuwahi kuongopa kuwa nina milioni kumi benki, sikuwahi hata kukueleza kuwa wazazi wangu ni matajiri niliusema ukweli wote kwa sababu nilihitaji kuishi katika uhalisia mkubwa sana na wewe. Naam! Ukanipokea bila kuwa nimetumia nimetumia uongo wowote. Nikakukabidhi moyo wangu ukanihakikishia kuwa moyo wangu upo sehemu salama kabisa....... lakini Tina. Hii inamaana gani labda, mtu aliyejivua nguo zote mbele zako na kuusma ukweli wote hatimaye unamlipa hivi......tazama sasa hadi leo hii nazungumza nawe ndipo nagundua kuwa mpaka sasa bado unaniongopea.....” nikasita nikafungua pochi yangu na kutoka na karatasi ambayo tangu niitunze katika pochi hiyo sikuwahi kuitoa kamwe hii ilikuwa siku ya kuitoa.
Nikaitoa na kuikunjua kidogo kisha nikamrushia Tina katika mapaja yake.
“Kama kweli ulinipenda na unadai kuwa unanipenda hadi sasa ni nini hicho Tina.....”
Tina aliishika ile karatasi na alipoifungua kidogo tu, akaiachia ghafla kisha akasimama wima na baada ya hapo akajishika eneo lake la moyo na mara akalainika na akawa anaelekea kuanguka chini.
Nikawahi kumdaka tukaanguka naye.... Tina akapoteza fahamu huku akiwa anatokwa jasho jingi mno..
Hapo sasa nikalazimika kuiweka ripoti kamili kushoto na nikatilia maanani usalama wa Tina mke wangu......


*Ripoti inazua balaa, Tina kimemsibu nini tena baada ya kuiona karatasi ile..... ni kipi kimeandikwa humo hadi ameshindwa kuhimili na kupoteza fahamu......
Usikose sehemu inayofuata......
Duniani kuna mambo jama!!!
 
Kweli hii ripoti kamili, unaweza kuomba ardhi ichimbike ukajifiche... lol! Tina umenipa somo kubwa...!
 
Nimejifunza kitu chini ya jua kwamba si kila mvumilivu huishia kula mbivu, wapo waliovumilia sana na bado wakaishia kula maumivu.
Na si kila subira huvuta heri, subira nyingi huishia kuizidisha shari....
Tena kubwa zaidi jingine wale waliosema mwenda pole hajikwai, hii si kwa wote kuna akina mimi tuliojaribu kwenda polepole lakini matokeo yake hatukuishia kujikwaa tu bali kupoteza kucha na vidole vya miguu.
Na hapo nikajifunza kuwa maisha hayana kanuni!!!

NA HII NI SEHEMU YA TISA.

Tina aliishika ile karatasi na alipoifungua kidogo tu, akaiachia ghafla kisha akasimama wima na baada ya hapo akajishika eneo lake la moyo na mara akalainika na akawa anaelekea kuanguka chini.
Nikawahi kumdaka tukaanguka naye.... Tina akapoteza fahamu huku akiwa anatokwa jasho jingi mno..
Hapo sasa nikalazimika kuiweka ripoti kamili kushoto na nikatilia maanani usalama wa Tina mke wangu......
NILIONGEZA mwendokasi wa lile pangaboi na kisha nikamsogeza Tina hadi akawa usawa wa pangaboi lile, nikainamakuhakikisha iwapo kwanmza anapumua vizuri, nilipohakikisha kuiwaanapumua vyema nikaona ni heri kumvutia subira nione nini kitajiri.....
Zilipita kama dakika tano akiwa bado ametlia vilevile.... nikaingia bafuni na kuchota maji kidogo ili nije kumwagia nione kama patakuwa na mabadiliko ama la niombe msaada zaidi kutoka katika hoteli ile.
Niliporejea na maji nilimkuta Tina akiwa ameketi kitako akiwa anashangaa huku akijibinyabinya kichwa chake.
“Nimekuwaje Mjuni?” aliniuliza.
Nikamueleza kuwa alipoteza fahamu, lakini nikamsihi awe mtulivu tu... nikamueleza kuwa mimi ni mume wake halali kabisa na asiwe na papara zozote kama nilivyomsihi kuanzia mwanzo.
“Tafadhali Mjuni nakuomba uichome moto karatasi hii, nipo tayari kusikia maneno yote lakini si maandishi hayo nakuomba sana, mimi ni mkosefu lakini nisaidie katika hili...” alinisihi sana huku akijaribu kujiweka tena katika sehemu aliyokuwa ameketi awali.
Nilimuelewa na kumweleza kuwa sitamsomea maandishi yale na baada ya mazungumzo hayo nitaichoma moto karatasi ile.
Akanishukuru, nikamueleza kuwa muda wa chakula umefika maana oda tuliyoweka ilikuwa tayari na ilikuwa ni sisi tu kupiga simu waweze kutuletea.
Tina alisema ni kweli anayo njaa lakini hajui kile chakula kitaingilia wapi. Nilizidi kumpa ujasiri na kumueleza kuwa ni vyema ajilazimishe kula kuliko kuacha kabisa kula kwa sababu atajizulia mambo mengine yanayoepukika, nikamkumbusha juu ya vidonda vyake vya tumbo.
Akakubaliana na mimi kuwa atajilazimishakula hivyohivyo. Nikanyanyua mkonga wa simu nikabofya kuwaeleza kuwa watuletee chakula.
Ndugu msikilizaji kwa Tina nilikubali kuacha kumsomea ujumbe ule katika maandishi yale kwa sababu mwandishi alikuwa ni yeye na hivyo alijua kila kitu alichokuwa amekiandika katika karatasi zile lakini siwezi kukuacha wewe na maswali, ni maandishi yaliyonipondaponda na kuondoka na uvumilivu wangu wa muda mrefu.
Maandishi yale yaliyoandikwa na mwanamke ninayempenda kabisa yalisomeka hivi..
Wasalaam Eric,
Ni matumaini yangu upo salama kabisa ukiendelea kufurahia maisha na mke wako kipenzi. Mimi pia ni mzima lakini sina furaha Eric wangu.
Kama nilivyokueleza siku ile kuwa natamani mimi ningekuwa mke wako halafu mkeo awe mke wa huyu mume wangu....
Eric sijielewi kabisa juu yako, kuna wakati nakurupuka usiku naanza kuwaza eti muda huo wa usiku umemkumbatia huyo mke wako, najikuta napatwa hasira sana na roho yaniuma waziwazi.
Eric, japokuwa haunipi nafasi kama mimi ninayokupa katika moyo wangu tambua kuwa sijiwezi kabisa bila wewe. Hakuna mwanaume anayeweza kuchukua nafasi yako. Sio kwamba mume wangu hanipendi, ananipenda sana lakini hisia zangu bado ni kwako tu..... ujue nilidhani kuwa nikiolewa nitakusahau, kumbe nd’o nimezidisha tatizo sasa nateseka zaidi. Kuna kama mara mbili hivi nimewahi kuchanganya jina la mume wangu badala ya kumuita Mjuni nikamuita Eric. Sema hakushtukia...
Kiukweli ndani ya hii nyumba nipo kwa sababu natakiwa kuwepo tu.... ule upepowa mahaba unaovuma nikiwa nawe hapa hakuna kabisa na siwezi kujilazimisha..
Huwezi amini Eric, yaani wakati mwingine ili nipate walau hisia za kumkumbatia lazima nifumbe macho nione kama mbele upo wewe hapo ndo Napata unafuu.. halafu hali hii inazidi kuwa mbaya kadri ya siku na siku zinavyozidi kusonga mbele.
Najua utajiuliza sana kwa nini nimeamua kukuandikia barua badala ya kukupigia simu, najua nikipiga simu utasikiliza kwa sikio hili na kisha yatatokea kule, lakini maandishi haya naomba la ukijisikia uyasome na utambue kuwa sina cha kujizuia kwako.
Na kwa maandishi haya nakuapia Eric ili niwe na furaha lazima nikuzalie mtoto. Nikiwa namuona huyo mtoto nione kama nipo na wewe...
Na siku tukikutana nitakueleza kitu kingine kizuri mpenzi wangu ambacho naamini utaniunga mkono tu.
Tafadhali nimeiacha barua hii kwa kijana wako wa dukani na wewe naomba ukishanijibu uiache hapo dukani nitaikuta..
Tafadhali usiache kunijibu mpenzi wangu na mume halali wa Tina.
Nakupenda!!!


Ilimalizika barua hiyo iliyomalizia kuuponda moyo wangu, na tangu siku hiyo nikatambua kuwa ninampenda sana Tina. Kwa sababu badala ya kuwaza nini cha kumfanyia kama adhabu nikawa nawaza ni kitu gani nifanye ili Tina wangu aweze kutulia katika himaya yangu.
Lakini baada ya kuwatembelea washauri kadhaa na kuwashirikisha juu ya hali kama hiyo bila kuwaeleza kama inanihusu mimi moja kwa moja na mke wangu walinipa ushauri ambao ulikuwa kama marudio tu, lakini kuna mmoja aliyetoa ushauri mfupi sana. Aliniambia “Mjuni kijana wangu, milele utabaki kuwea Mjuni na huyo Eric atabaki kuwa Eric hauwezi kuwa Eric kamwe!!”

Ni kweli msikilizaji, Eric alibaki kuwa Eric ambaye ameuteka nyara moyo wa Tina na mimi Mjuni nilibaki kuwa mume jina tu kwa Tina.
Kufikia hapa nikasalimu amri na kuamini kuwa si kila mvumilivu hula mbivu, Mjuni mimi nilikua nimeishia kula maumivu!!

Chakula kililetwa nikala pamoja na Tina ambaye kiuwazi alikuwa anajilazimisha tu kula lakini ilibidi iwe hivyo kuliko kubaki na njaa.
“Mjuni mume wangu naomba unipe nafasi nizungumze najisikia kifua changu kinaweza kupasuka, adhabu hii imenitosha Mjuni niruhusu niseme lolote mume wangu. Najua haupendi kusikia nikikuita mume wangu lakini tafadhali nakuomba....” Tina alinisihi huku akitokwa machozi, tatizo nililokuwanalo na hata wewe linaweza kukukumba ikiwa tu umewahi kupenda kwa dhati.
Chozi la Tina bado lilikuwa linaupondaponda moyo wangu.
Kuna watu wanaweza kunitafsiri kama mwanaume mjinga lakini ni heri nisikuongopee lolote katika ripoti hii, elewa kuwa Tina alikuwa chaguo langu.
“Tina utazungumza sana nikimaliza mimi, na nitakusikiliza sana....” nilimjibu na kumsihi aendelee kula.
“Hapana Mjuni... naomba walau dakika tano tu....” alizidi kunisihi..
“Tina hii ni ripoti kamili naomba uniachie nafasi niikamilishe kwanza zimebaki kurasa chache tu!!” niliusimamia msimamo wangu.......


##Ni ripoti kamili mdau, yenye mambo lukuki ndani yake...... bado muafaka haujapatikana wala ripoti haijamalizika....
Endelea kufuatana nasi!!!
 
KINACHOUMIZA na kutesa linapokuja suala la mahusiano ya kimapenzi basi ni kumbukumbu, ukimwona mtu anakondeana na kukosa raha kisa mapenzi ujue kinachomuumiza sio kuachwa ama kuacha, kinachomtafuna ni kumbukumbu.
Laiti kama pasingekuwa na nafasi katika ubongo ya kuhifadhi kumbukumbu kamwe mapenzi yasingekuwa yanazungumzwa kama yanavyozungumzwa leo hii....

NA HII NI SEHEMU YA KUMI.

Nakumbuka katika kipindi kile Tina yu mjamzito na mama yake mzazi alipatwa na homa za matumbo kiasi cha kuzidiwa na kuhitaji uangalizi wa karibu sana, nikiwa kama mkwe kwa mama yule niliguswa na hali ya yule mama. Hadi ninapoyaandika haya sina maisha ya juu sana lakini pia sipo katika maisha mabaya ya kutisha.
Na hata wakati ule nilikuwa na hali ya kiuchumi ya kawaida, nilifanya maamuzi magumu sana, nikaacha kumlipia mdogo wangu ada, pesa yote nikaamua kuitumia kumuhudumia mama yule alienizalia Tina wangu.

Naikumbuka sikukuu ya wapendanao, Tina aliniletea zawadi na aliponikabidhi zawadi ile alinieleza kuwa kwa yote niliyomtendea mama yake mzazi hadi kurejea katika hali yake ya awali basi hana cha kunilipa zaidi ya upendo wake wa dhati.
“Tina ni upendo gani huo wa dhati uliomaanisha kwani? Kwanini ukaniletea pigo kubwa kama lile... kwanini ukanitundika katika mti wenye miiba na kisha kuniponda na makaa ya moto? Samahani Tina awali niliahidi kusikiliza kila utakalonieleza lakini sasa nakuomba sana unyanyuke ukiwa kimya kabisa... ingia bafuni osha uso wako hasahasa hayo macho yako. Kisha nitambeba mtoto na tutatoka nje kana kwamba hakuna lolote lililotokea kati yetu...... tutaongozana hadi nyumbani kwa amani tele kama tulivyoingia. Kisha utalala ukiwa kimya kabisa, ukitafakari yote niliyozungumza na wewe.. halafu upate na maamuzi thabiti kabisa. Na asubuhi ikifaa utachukua hatua ya maamuzi yako. Lolote utakaloamua as long as halimuathiri mtoto huyu nitalibariki kwa mikono miwili.”
Tina anayetetemeka vibaya sana alifuata niliyomuelekeza na alikuwa ananiogopa sana, hata kupishana na mimi ili aende bafuni alinipishia mbali sana. Nilijaribu kuvaa viatu vyake na kugundua kuwa hata kama ningekuwa mimi ningekuwa katika hali ileile.
Aliingia bafuni akanawa kisha akatoka.........
Alinikuta tayari nikiwa nimembeba mtoto, alipotoka nikamkumbatia na kumkumbusha kuwa bado nampenda!!
Tukatoweka nikaaga mapokezi........

*****
(acha nafasi kidogo)

Kweli tulifika nyumbani kwa kutumia usafiri uleule wa Taksi, tukaingia chumbani Tina akiwa bado anatetemeka mno. Ni kama mtu aliyehisi muda wowote ule naweza kuchukua aidha kisu ama silaha yoyote ile na kisha kumjeruhi vibaya mno.
Kosa ambalo ninakiri nilifanya ni kujilaza nikiamini kuwa maneno yangu ya kumtia moyo Tina basi na yeye atalala na kufanya tafakari kisha ataamka akiwa na maamuzi sahihi kabisa. Na hata kabla ya kulala nilimsihi sana kuwa awe na amani sana tutazungumza asubuhi.
Nikapitiwa na usingizi, na nilipokuja kushtuka asubuhi nilijikuta naingia katika ulimwengu mwingine kabisa.
Sio Tina wala mtoto ambaye alikuwa katika kile chumba, nilipotazama saa ilikuwa ni saa kumi na moja alfajiri. Nilihangahika huku na kule nijue ni kitu gani kimetokea. Nilijaribu kupiga simu ya Tina lakini ilikuwa haipatikani.
Alfajiri ile ningeanzia wapi? Sikuwa na pa kuanzia......
Nilisubiri hadi palipopambazuka nikaanza kuzurura kwa ndugu wa Tina kuwauliza iwapo wamemuona Tina lakini walinieleza kuwa hawajamuona. Nilipiga simu nyumbani kwao na wao hawakuwa na taarifa yoyote.
Hali ilizidi kuwa tete hadi kufikia saa sita mchana bado nilikuwa sijajua Tina alipokuwa, mbaya zaidi alikuwa ameondoka na mtoto. Naapa kwamba laiti kama Tina angekuwa amemuacha mtoto hakika nisingekuwa katika wakati mgumu kiasi kile.... niliwaza sana ndugu msikilizaji, Tina atakuwa ameenda wapi na yule mtoto.....
Wazo la kwanza lililokivamia kichwa changu baada ya kujifikiria kuwa yaliyomtokea Tina yangekuwa yamenitokea mimi... wazo la kwanza ni kujiua, na kama ni kujiua basi hata kile kiumbe asingeweza kukiacha hai na chenyewe lazima angekiua tu.
Hapo sasa damu yangu ilinisisimka mno na mara kwa mara nilijaribu kujiwekea hoja pingamizi kuwa yule sio mtoto wangu, lakini nikalikumbuka lile tabasamu la kile kitoto nikajisikia kama mtu ambaye nilikuwa nimewahi kuonana na malaika aletaye heri. Sasa yule malaika yananijia mawazo kuwa kuna uwezekano akafanyiwa kitu kibaya kabisa.
Nilikimbia hadi mlangoni na kuufungua mlango lakini kiunyonge kabisa nikaufunga mlango ule kwa sababu sikuwa na pa kwenda kwa sababu kama ni kuuliza basi kila sehemu nilikuwa nimeuliza. Nilibaki pale mlangoni huku ikinijia picha kichwani jinsi kitoto kile kitakavyokuwa kinanyongwa na Tina kikijaribu kutupa vikono vyake vidogo katika namna ya kupambana lakini kisifanikiwe hadi pale kitakapokata roho.
Niliuma meno yangu na kisha kukigongagonga kichwa changu kuzilazimisha fikra zile ziende mbali nami......

Wazo la pili baada ya kutulia niliwaza juu ya Tina kuwa ni mwanamke mwenye moyo wa huruma sana, japokuwa alinitenda vile lakini bado alizaliwa akiwa na huruma. Basi kama hatamdhuru huenda atamtelekeza katika sehemu mojawapo kati ya nyumbani kwa yule hawara wake ama nyumbani kwa mama yake.... hawezi kumtelekeza sehemu nyingine tofauti na hapo..
Basi baada ya kuwaza mambo haya nikakusudia kupambana kwa ajili ya yule malaika Sonia.
Nikaamua kuanzia nyumbani kwa yule bwana, litakalotokea huko nitakuwa tayari kulipokea. Ningepata amani ya nafsi iwapo tu ningeelezwa kuwa mtoto Sonia yupo salama.... nafsi yangu ilitawaliwa na hasira sana kujipeleka mikono nyuma kwa mwanaume ambaye alikuwa akimfanya mke wangu vyovyote alivyotaka kumfanya. Lakini ningefanya nini???
Niliingia bafuni nikaoga, nikavaa na kisha nikaifunga nyumba na kuondoka zangu, uziri ni kwamba nyumbani kwa mwanaume yule nilikuwa napatambua vizuri sana..
Nilifiika nikabisha hodi nikakaribishwa na mtoto mdogo aliyekuwa anafanana pua na mtoto Sonia... hali hii iliniumiza sana kwa sababu nilizidi kuamini kwa vitendo kuwa yule bwana kweli alimzalisha mke wangu.
Niliongozwa na yule mtoto hadi sebuleni, huko nikakaribishwa na mwanamke ambaye alikuwa anafanania na kuwa mama kwenye nyumba ile..... nikamsalimia akanijibu kwa furaha huku akitabasamu. Nikamuuliza mume wake kama yupo akaniuliza iwapo nina miadi naye........
Niliposema hapana, akadai kuwa hayupo. Nikafahamu kuwa hilo jibu ni la kupewa.. mume wake amemueleza akija mtu ambaye hawana miadi basi amweleze kuwa hayupo.
Nilishusha pumzi kidogo na kisha nikawa katika mashauri mawili, je nimwage ukweli wote mbele ya yule mwanamke ama niondoke kwa ahadi ya kurejea tena........


**Haya sasa, Mujuni katika harakati nyingine Tina yupo wapi na mtoto je????
 
MUNGU na akutie nguvu ewe uliyempoteza mama yako, ama wewe usiyemjua mama yako kabisa.
Mungu ni kimbilio la yote lakini mama ni kimbilio la mengi sana..... ukipatwa na jambo ambalo unahisi kwa kiasi fulani linaizidi akili yako tafadhali mkimbilie mama mueleze pasi na kumficha chochote!!
Niamini mimi, hautaondoka kama ulivyoenda..... hautakosa chembe za matumaini. Kama ulikuwa umeanguka utasimama tena........

NA HII NI SEHEMU YA KUMI NA MOJA.

BAADA ya kutafakari kwa kina ni ni kitu gani ambacho naweza kufanya kwa wakati ule nikiwa katika nyumba ile nikaona hapo la kufanya ni kuondoka bila kuamua chochote. Nikamuaga yule mama nikamueleza kuwa nitarejea tena, akaniuliza mimi ni naniili mumewe akirejea amueleze nikamueleza kuwa naitwa Steven lakini mumewe hanifahamu kabisa mpaka nijieleze zaidi.
Akaniaga nikaondoka!!!
Nilipofika nje ya uzio ule nikaichukua simu yangu nikatafuta sehemu imetulia nikaingiza namba za mama yangu na kumueleza kuwa iwapo anayo nafasi ninahitaji sana kuzungumza naye. Akaniambia nimpigie bada ya nusu saa, tukaagana hivyo. Nikaondoka hadi nyumbani nikajirusha kiotandani, ile nusu saa ilikuwa imemalizika tayari na sasa ulikuwa wakati wa kumueleza mama kile ambacho kilikuwa kinanisibu kwa wakati hu.
Nilimueleza mama hatua kwa hatua niliyopitia hadi hapo nilipokuwa, nilimwambia kuwa nilitamani sana nizungumze naye ana kwa ana maneno haya lakini wakati unanitupa mkono nahitaji ushauri wake ni kitu gani nifanye ambacho ni sahihi kwa wakati huo. Mama alishusha pumzi zake kwa nguvu sana, kisha akaniita jina langu la utotoni jina la Nshomile.
Nikaitika kwa utulivu akanieleza kuwa na yeye ana mengi ya kuzungumza lakini akasema tumweke kando Tina na sasa tuzungumze kuhusu mtoto.
Akaongezea kuwa yupo tayari kuniunga mkono kwa lolote jema ambalo litanifanya mimi nifurahi, na kwa hili pia akanieleza kuwa ni jema kwa sababu mtoto nimemlea na ninampenda basi huyo ndiyo furaha yangu, isitoshe hata kliniki jina aliloandikwa ni jina langu.... hivyo cheti chake cha kuzaliwa kinamtambulisha kama mtoto wangu.
Mama akanieleza kuwa. Yeyote aingiaye katika vita kwa pupa huishia kuangukia pua lakini yule aingiaye kwa tahadhari kubwa anazo asilimia nyingi sana za ushindi. Akaendelea kunieleza kuwa hii ni vita na sehemu kubwa tayari nilikuwa nimeipigana tena kwa ushindi mnono sana, hivyo kuimaliza si kazi ngumu, mama akanishauri niende kuonana na mgoni wangu, huyo aliyekuwa akimfanya Tina vile alivyokuwa anapenda kumfanya. Akanieleza kuwa nikishakutana naye nisiwe na papara bali mpole na niliyekubali kujishusha kabisa.

Dah! Ushauri wa mama niliuona mzito lakini akanieleza kuwa kama nilijishusha mbele ya Tina huku najua kila alichofanya, nashindwa vipi kumalizia kwa huyo mwanaume ili nijue kipi kinaendelea. Nikamuelewa mama na nikajipanga jioni ya siku hiyo kwenda kuonana na huyo bwana wa kuitwa Eric. Maneno ya mama yalikuwa yamenitia nguvu sana....
Na sikutaka siku hiyo ipite kabla ya kuonana naye, nikahairisha mpango wangu wa kulala na badala yake nikaamua nifunge safari kwenda nyumbani kwake tena lakini safari hii sifiki ndani ila nitajiweka nje na kutazama kila anayeingia na kutoka, akiingia tu na mimi naingia ama akitoka tu na mimi namfuata......
Wazo hili nikaliona ni wazo stahiki, nikavaa viatu vyangu kisha nikaufikia mlango wangu nikaufungua.
Moyo wangu ulipiga kwa nguvu sana yaani ilikuwa kama filamu fulani hivi isiyokuwa na ukweli ndani yake.
Filamu ambayo mwandishi wake ameunda tukio la mimi kufungua mlango na wakati huohuo mtu ambaye naondoka kwa ajili yake akiwa amesimama mlangoni kwangu akijiandaa kubisha hodi.
Alikuwa ni Eric akiwa amesimama huku mikono yake ikiwa inatetemeka, sijui kama na yeye aliuona mshtuko wangu lakini mimi niliuona mshtuko wake vyema kabisa.
“Karibu bwana!” nikamkaribisha.....
“Tafadhali bwana Mjuni nakuomba sana unipe nafasi ya kunisikiliza nakuomba Mjuni!!” alinisihi nikabaki kushangaa... lakini hapohapo hofu ikaanza kuniingia kutokana na wasiwasi wake yule bwana.
Na wasiwasi wa kwanza kabisa ulikuwa ule wa kupokea taarifa za msiba wa Tina na mtoto wake, nilikuwa tayari kupokea taarifa yoyote ile lakini sio taarifa hii. Niliamini kuwa nitakatishwa tamaa mno klulisikia jambo kama hili kwa masikio yangu.
“Karibu ndani bwana Eric... karibu tafadhali...” nilimsihi akaingia ndani nikafunga mlango.
Akaketi katika kochi mojawapo sebuleni na mimi nikaketi mkabala naye, nikawa namtazama kwa nukta jinsia livyokuwa akijiumauma kuzungumza... alikuwa anarudia rudia maneno sabna na hadi dakika tano zinapita nilikuwa sijaelewa lolote alilokuwa akisema zaidi ya kusisitiza kuwa anahitaji sana msamaha wangu.
“Tina yupo wapi?” hatimaye nilimuuliza, na kabla hajanijibu nikaliboresha swali, “Tina na mtoto wapo wapi kwanza kabla ya yote?” nikasita na kumpa nafasi azungumze.
“Kaka, ni mimi niliyetaka kukuuliza hilo swali.... nipo tayari umuite Tina na mtoto niwaombe radhi wote kwa pamoja....”
“Hah! ina maana hujaonana na Tina ama?” nilimuhoji.
“Nina zaidi ya wiki moja sijawahi kuwaona....” alinijibu, sasa alikuwa anatulia kiasi fulani....
“Na ni kipi hasa chanzo cha wewe kuja hapa?” nilimuuliza. Akanieleza kuwa nilipoenda nyumbani kwake alikuwa ndani na aliweza kufuatilia baadhi ya maongezi kati yangu na mkewe na kwa sababu alikuwa ananitambua alijua pia nini dhumuni langu la kwenda kwake.
Akaendelea kunisihi kuwa mkewe ana matatizo ya moyo na laiti kama akigundua jambo hili la mimi kwenda kushtaki kuwa yeye ana mahusiano na mke wangu basi anaweza kufa palepale.
Nilimsikiliza na kuuona udhaifu wa hoja yake ya kujitetea, alinikasirisha sana, yaani alikuwa anamuonea huruma mkewe lakini katu hakuwahi kufikiria ni uchungu kiasi gani ninapitia mimi kwa kutambua kuwa anahusiana na mke wangu tena mara kwa mara wanakutana na kisha kunisema watakavyo. Niliidhibiti hasira yangu lakini ikashindikana.
“Eric unasema kwamba..... yaani unamuonea mkeo huruma lakini mimi haujali uchungu wangu si ndo hivyo....” nikaenda mlangoni na kuufunga mlango vyema na kutoa funguo.
“Sasa Eric nahitaji tufahamiane vizuri kuwa nani ni mwanaume... umenitesa sana mwanaharamu mkubwa wewe....”
Sasa ni hasira ilikuwa inaniongoza, nilimvamia Eric na kumkaba shingo yake, kilichosababisha hasira ipungue makali kidogo nmi kile kitendo chake cha kutopambana na mimi bali kuniacha nifanye nifanyavyo.......
Mwishowe nilimuachia na kuruhusu machozi yanitoke..... na hapo nikaendelea kuzungumza.
“Eric, nimeumia sana... umeniumiza sana... na bado unataka kuendelea kuniumiza. Yuko wapi Tina na mtoto....” nilikuwa nasita kila mara kumalizia mtoto wangu kwa sababu nilitambua kuwa aliyekuwa mbele yangu alikuwa baba halali.
“Mjuni.. nielewe tafadhali... sijui na sina taarifa yoyote juu ya hili....” alizungumza huku akisihi haswa na nikaamini kabisa kuwa alikuwa haongopi.....
“Sasa atakuwa wapi labda, ok! Tuachane na haya ya kale kwanza tuyaweke kiporo... tafadhali sana Eric nadhani waweza kuwa na mawazo walau mawili matatu ni wapi Tina anaweza kuwa.” Nikamueleza Eric huku nikimueleza pia kwa ufupi juu ya kilichotokea kabla Tina hajaondoka.
Akafikiria kwa muda na kisha akanieleza kuwa huenda ameenda kwa shoga yake fulani hivi, akanielekeza mahali anapoishi, tukakubaliana kwenda wote. Tukafanya hivyo.....

ITAENDELEA
 
Back
Top Bottom