Joram hakumjibu, aliondoka zake
polepole lakini kwa hadhari zaidi.
Dakika kadhaa baadaye, hakuwa Joram Kiango yuleyule tena. Alikuwa
mtu mwingine aliyebadilika kimavazi kiasi cha kuweza kumchanganya
mtu yeyote. Sasa alivaa suti yake nyeusi, tai nyeusi, shati jeusi na
kofia nyeusi. Kitu pekee cheupe mwilini mwake kilikuwa ni kitambaa
cheupe alichofunga shingoni.
Kitambaa ambacho kukiondoa hapo kungemfanya aonekane kivuli au
sehemu ya kiza ambacho kilitanda kwa silaha zake ambazo ni pamoja
na bastola, visu, nyembe, tochi yenye ukubwa wa kalamu na dawa
ambazo humsaidia katika shughuli zake.
Akiwa karidhika na hali yake, aliyaacha makazi yake, sehemu za Ilala
na kukiendea kituo cha basi ambapo alijiunga na watu waliokuwa
wakisubiri usafiri wa kwenda mjini kufunga siku kwa starehe za dansi,
sinema na vinywaji.
Hayo yalikuwa yakitokea dakika arobaini na tano tu baada ya Joram
kumwacha mahututi yule jambazi aliyekuwa akimnyemelea katika
vichochoro vya Mtaa wa Jamhuri. Alikuwa amesafiri harakaharaka,
akisaidiwa na usiku ambao ulianza kutawala na kumficha asionwe na
gaidi mwingine na kuweza kusumbuliwa pindi akienda kwake.
Alipofika nyumbani alipiga simu ya haraka kwa katibu wake
kumjulisha hali ilivyo, kisha hima akaanza kubadili mavazi na baadaye
kujitokeza mitaani akiwa kama alivyo. Sura ikionyesha utulivu, mavazi
yakitangaza starehe hali rohoni kabeba furushi la mashaka na taharuki
kwa kufikiria jukumu lililokuwa mbele yake.
Hofu yake haikuwa juu ya maisha yake, ingawa kwa mujibu wa taarifa
ya yule jambazi aliyepambana naye dakika chache zilizopita,
alifahamu kuwa anaelekea eneo la hatari sana. Hasa, hofu yake
ilikuwa juu ya maisha au usalama wa mtu aliyekuwa akimfuata;
Dismas Komba. Aliamini kwamba yupo mashakani. Moyo
ulimshawishi kufanya haraka sana ili kujaribu kumtoa katika hatari
hiyo.
Lilitokea basi lielekealo Posta, Joram alikuwa mtu wa kwanza
kulidandia. Na lilipowasili aliwatangulia wote kuteremka. Akafanya
haraka kuchukua teksi ambayo ilimfikisha Ferry ambako alijiunga na
wavuvi pamoja na watu wengine waliokuwa wakinunua samaki. Alijitia
mteja wa kawaida lakini macho yake yalikuwa kazini yakisoma sura za
watu kuangalia kama alikuwepo yeyote kati ya maadui ambao
walipewa jukumu la kutokumruhusu kufika Kigamboni. Aliporidhika na
nyuso hizo alimshawishi mvuvi mmoja, kijana ambaye alikubali
kumvusha hadi upande wa pili kwa shilingi hamsini akitumia ngalawa
yake.
Joram alimsaidia kijana huyo kwa kupiga kasia kwa namna ambayo
ilimchekesha sana kijana huyo kwa jinsi asivyofahamu kazi hiyo.
Acha tu mzee, alisema kijana huyo. Kisha alibadili sauti katika
kicheko chake na kukifanya kiwe cha kitu kama dharau ama
mshangao. Kicheko hicho kilifuatwa na swali lililodai, Yaonyesha u
tajiri sana mzee?
Kwa nini? Alihoji Joram.
Watu wenye fedha ndogo kama mimi si rahisi kukodi mtumbwi.
Pantoni iko pale na inachukua watu bure kwa haraka na usalama
zaidi.
Ikawa zamu ya Joram kucheka. Kijana huyu hakujua kuwa alikuwa
ameepuka pantoni hiyo kwa hadhari akijua kuwa kama kuna ulinzi
wowote dhidi yake, haikuwepo sehemu nzuri zaidi ya hapo kivukoni.
Hivyo, alikuwa akiepuka kuonekana na jicho ambalo halikustahili
kumwona hasa kwa wakati huo. Lakini alimjibu kijana huyo kwa
kumlaghai, Siku nyingi mno sijasafiri katika chombo kidogo kama
hiki. Hizo shilingi hamsini nilizokupa ni kati ya mia nilizozipata katika
bahati nasibu. Hazikuwa katika bajeti.
Kwa nini basi usingekuja mchana? Saa mbili u nusu za usiku! Utafaidi
nini?
Safari ya usiku naipenda zaidi.
Walipowasili upande wa pili nje kabisa na kituo cha kawaida, Joram
alimshukuru kijana huyu na kisha kuanza safari ya kuingia Kigamboni.
Akiyafuata maelekezo ya yule mtumishi wa Kamata alifikia nyumba
ambayo alidhani ingekuwa ya Komba. Lakini mara baada ya kuuliza
kwa mtoto aliyeketi nje ya nyumba hiyo aligundua kwamba aliikosea.
Ni ile pale. Si yule Komba wa Kamata?
Ndiye.
Ile pale.
Joram alipoanza kuondoka ili aiendee, mtoto huyo alimzuia kwa
kusema, Unakwenda pale mzee? Hapafikiki siku hizi. Hasa usiku kama
huu!
Kwa nini?
Pana miujiza sana. Mambo ya ajabu yanatokea katika nyumba ile.
Nadhani kuna jinsi au majini.
Kwani vipi bwana mdogo?
Mengi yanatukia pale. Wapangaji wote wamehama. Amebaki Dismas
peke yake. Inasemekana kwamba anajifungi achumbani usiku na
mchana. Bila shaka kati ya kesho na keshokutwa atakuwa chizi.
Joram akajikuta akizidiwa na hamu ya kuyaelewa maongezi hayo.
Kijana, nieleze vizuri nikuelewe. Unataka kusema kwamba kuna
mambo ya ajabu ajabu yanatokea katika nyumba ile? Kama yapi?
Nieleze hatua kwa hatua.
Ni habari ngumu kueleweka. Watu wanadai kuwa kabeba jini kutoka
Unguja alikokwenda hivi karibuni. Tangu alipotoka huko mambo yake
hayaeleweki. Siku ya kwanza aliporudi, alikuwa katika hali ya kawaida.
Usiku huo alisikika akilia na kunyamaza ghafla. Jirani aliyeamka na
kumwendea alirudi mbio akilia ati kapigwa kama jiwe tumboni na mtu
asiyeonekana. Asubuhi waliomwona Dismas walidai kuwa alikuwa
kachubuka usoni na damu ikiwa imekaukia puani. Yasemekana alitoka
ili aende mjini, akaingia katika pantoni na kuvuka ngambo, lakini
aliporudi alirudi nalo huku akitetemeka.
Ni hapo alipoanza tabia ya kujifungia ndani. Yasemekana pia kuwa
wapangaji hao waliohama walikuwa wamelala ndani lakini
walipoamka alfajiri walijikuta wamelala nje, uchi wa mnyama, hali vitu
vyao humo ndani vikiwa vimetapanywa ovyo ovyo. Hata sisi watoto
ambao tumekuwa tukicheza mbele ya nyumba hiyo tumeacha baada
ya mwenzetu mmoja usiku wa juzi kutoweka ghafla na kuokotwa
baada ya muda mrefu kalala ufukoni. Alipoulizwa kilichomfanya alale
huko na vipi alienda huko hakuwa na jibu zaidi ya kushangaa tu.
Ni hadithi nzuri, Joram alimjibu akitabasamu.
Siyo hadithi. Yametokea na yanaendelea kutokea
Joram hakuwa na nafasi ya kumsikiliza zaidi. Mawazo yake tayari
yalikuwa kazini yakiifikiria taarifa hiyo. Macho yake pia yalikuwa
yakipambana na kiza kujaribu kutazama eneo la nyumba hiyo ambayo
kiasi ilijitenga na nyumba nyingine kutokana na utaratibu usioridhisha
wa mjenzi au mpimaji. Nyumba hiyo ilizungukwa na kichaka kikubwa
cha miti au maua yasiyo katika utaratibu mzuri.
Kwa mtu kama Joram ilikuwa ni rahisi kuhisi kichaka hicho kingeweza
kuwa hifadhi nzuri ya mtu au watu waliodhamiria kumtendea Dismas
Komba jambo fulani, si kama walivyodhani watu wengine kuwa ni
majini yaliyofanya yote hayo. Joram alimshuku pia kuwa kile kitendo
cha watoto na majirani kilidhamiriwa kuwaweka watu wote mbali ya
eneo hilo ili wapate nafasi nzuri ya kuendelea na harakati zao.
Harakati ambazo zilikusudiwa kupoteza maisha ya Komba. Kwa nini?
Hakuwa na nafasi ya kujijibu maswali hayo. Damu ilikuwa ikimchemka
na moyo kumwenda mbio huku nafsi ikimshawishi kufanya haraka
kabla halijatukia lolote baya zaidi kwa Komba.
Hata hivyo, baada ya kumshukuru mtoto huyo kwa sauti ambayo
haikuonyesha kuwa kaamini lolote kati ya hayo, aliondoka zake
polepole akielekea upande mwingine. Mikono yake ilikuwa shingoni
kuondoa kile kitambaa cheupe. Mara akawa kama kivuli. Ili kupima
kama alikuwa katika hali ya kuridhisha alipiga hatua mbili nje ya
barabara na kusimama.
Watu wengi walipita bila ya kumwona. Mara alitokea mzee, kafutana
na binti mwenye umri wa mjukuu wake. Walikuwa wakizungumza
mambo ambayo yalimshangaza Joram kupita kiasi. Walipomkaribia
zaidi walisimama na kuendelea na maongezi yao.
Nusura atokwe na kicheko kwa kusikiliza utongozaji huo wa kizamani
mno. Lakini alijikuta akishindwa kustahimili kuondoka pindi maongezi
hayo yalipopamba moto na kubadilika kuwa mahaba kwa mtindo
ambao Joram hakutarajia kuwa binti mdogo kama huyo angediriki
kumtendea babu wa kiasi hicho.
Aliondoka kwa kunyata akiifuata nyumba ya Dismas Komba.
Alipoikaribia alitafuta nafasi nzuri katika kichaka cha maua na kuketi
chini akisubiri.
Alisubiri sana. Kusubiri ikiwa miongoni mwa shughuli zake hakukinai
kuketi hapo, akivumilia mirija ya mbu huku macho yake ambayo
yalikwishazoea giza yakiwa wazi kutazama lolote. Nia yake ilikuwa
ifike saa saba au nane ya usiku ndipo aendelee na safari yake hadi
katika nyumba ambamo alikusudia kuonana na Komba. Kwenda
papara baada ya kusikia hadithi ya yule kijana juu ya nyumba hiyo
isingetofautiana na nondo aendavyo katika moto kwa tamaa ya
mwanga.
Joram alipoitazama tena saa yake na kuona ikikaribia saa sita za
usiku, alianza kujiandaa kuisogelea nyumba hiyo. Nia yake ikiwa
ashughulikie dirisha moja au mlango na kuingia ndani ambako
angehitaji kupata hakika kama sehemu ya kiza ikichezacheza hatua
kadhaa mbele yake. Baada ya kutazama kwa makini aliona dalili za
kiumbe hai, kikitembea polepole kuiendea nyumba hiyohiyo. Alikuwa
mtu! Kavaa mavazi mieusi kama yake. Macho ya Joram yaliongeza
juhudi kutazama kama mtu huyo alikuwa peke yake. Hakuona dalili ya
mtu mwingine. Ndipo Joram alipouinua mguu mmoja baada ya
mwingine kwa hadhari na utulivu kama kivuli akimfuata.
Mtu huyo alipoufikia mlango hakuchelewa sana kuushughulikia,
ukafunguka polepole naye akaingia huku akiufunga. Joram alimpa
dakika mbili, tatu kisha akausogelea mlango na kuujaribu. Haukuwa
umefungwa. Akaufungua na kunyata ndani huku masikio yake yakiwa
wazi, mkono wake ukiipapasa bastola yake.
Humo ndani kulikuwa na kiza ambacho kilitisha mno. Nuru hafifu sana
ilionekana kwa shida kutoka chumba kimoja. Joram alikifuata chumba
hicho na kutega sikio lake katika tundu la ufunguo akisikiliza.
Haikuwepo haja ya kusikiliza kwa makini kiasi hicho.
Sauti ya mtu au watu wanaogombana kidhaifu ilimfikia kwa urahisi.
Mmoja alikuwa akisema, Wapi? Usiposema nitakuua
Mwingine
alilalamika tu.
Nitakuua kweli, ilidai tena sauti hiyo nzito zaidi. Ikafuatwa na
malalamiko ya maumivu makali.
Joram hakustahimili zaidi. Akaufungua mlango kimyakimya kwa
haraka zaidi na kujitoma ndani. Aliingia wakati mzuri sana wa kuwa
shahidi aliyeshuhudia jisu kali na refu likiingia katika kifua cha mtu
aliyelala juu ya sakafu.
Pigo la pili Joram alilizuia kwa kumpiga muuaji huyo judo ya shingo.