Riwaya: Mabastania

Maybach 255

Member
Jan 25, 2020
18
31
WAHUSIKA, SEHEMU, MAJINA NA MATUKIO YALIYO KWENYE RIWAYA HII NI KAZI YA SANAA NA SIO HALISI. UFANANI WA AINA YOYOTE NA MAMBO HALISI NI NASIBU.
____________

1

Kwenye Jumamosi tulivu; mawingu meusi ya masika yalitanda, mvua ilitishia kunyesha...na matope kwenye njia nyororo iliyopita kati ya kati shamba kubwa la katani yalikuwa yamekauka. Watoto wawili walipita wakisimama kwa dakika kadhaa, kubishana na kisha kuendelea na safari yao iliyokuwa inaonekana kutishiwa na mvua, ambayo walionekana kuto kujali.

"Mel," Maya, mwenye umri wa miaka mitano hivi alimuita yule mtoto aliyekuwa mbele yake, akitembea kwa kasi kidogo.

"We Mel!" Maya aliita kwa sauti ya juu kuliko ya kwanza. Ila yule mtoto alijifanya kutosikia.

"Kaka Mel wee," Maya alijaribu kwa mara nyingine. Mara hii yule mtoto wa mbele yake alisimama na kumgeukia.

"Nini sasa? " Melvin aliuliza. Kwa hasira. " Unashindwa kuwahi? Yaan nyie wasichana mko waviv..."

"Af Mel! Nitamwambia mama, tukirudi nyumban...ashasema, hiyo mbaya."

"Sa huwezi kuwahi..tu kuniita ita...na kushitaki shitaki"

"Ila Mel," kalisimama ka Maya na kupiga tumakofi twake, kama wamama walioko kwenye mabishano. " Kwani sukari si nimekukuta unailamba? Mama ashasema hamna kulamba sukari...we..."

"Haya! Haya, umeshinda..wahisha tumiguu twako," Alisema Melvin akimtazama mdogo wake kama kituko.

"Afu Mel! Ni miguu sio tumig..."

Melvin na Maya, waliendelea kubishana kwa dakika kadhaa, na Maya alipoelekea kushindwa alilia kumlazimu Melvin anyamaze. Ilikuwa kawaida yao kama ilivyokuwa kwa watoto wengine kwenye kijiji cha Chiro. Vutoto vywa kike vuliwaiga mama zao kimatendo na kitabia...baadhi kama, Maya, vuliwaiga hadi kimatamshi.

Mawingu yalizidi kutanda, nao walikuwa kwenye mzozano mwingine.

"...nilikusema? Eeh Eh, jibu kwanza...we ulipo dokoa nyama, nlikusema?" Aliuliza Melvin kimajigambo.

Melvin alimzidi mdogo wake miaka miwili tu, na walifanana katika namna tofauti, kikubwa ni kuwa walipenda kuingia kwenye mizozano na kuona yupi alishinda. Maya alionesha kushindwa hivyo alibaki kimya na kuanza kuondoa tumagugu kwenye ka gauni kake ka zambarau.

Melvin alijihisi vibaya, alidhan labda amezidi mipaka kwa kumsumbua mdogo wake kiasi kile...hivyo alijaribu kubadili mada;

"Wahi basi, sikusumbui tena...mvua itatukuta njiani, barua ya shangazi iloe...aanze kukasirika," alisema Melvin.

Maya aliacha kuondoa magugu kwenye gauni lake, na kumpa mkono Melvin amshike, walikuwa wamekuwa marafiki tena. Ila kulikuwa na kitu hakiko sawa, kulikuweko wanaume wawili waliofanana waliolekea kwao kwa haraka. Walikuwa mapacha. Waliwatazama kwa hali ya kutisha, na kuendana na walivyokuwa wamevaa na walivyowaangalia, Melvin alijua moja kwa moja kuwa hawakuwa wanakijiji wa Chiro na hawakuwa na nia njema.

"Shkamoo," Maya alisalimia, ila hawakuitikia.

"Unawajua..au tu unasalimia salimia?" Alinon'gona Melvin.

"Ila Mel..." Maya alianza, ila hakumaliza sentensi yake. Japo bado alikuwa mdogo, miaka mitano, alihisi kuna kitu hakikuwa sawa. Wale watu waliangaliana na kutabasamu kisha kuongeza kasi wakielekea Mel na Maya walikokuwa.

"Mel..tukimbie," Maya alinong'ona kwa Melvin na bila mahojiano, walianza kukimbia kuelekea waliko toka. Ila walikuwa watoto, na waliowakimbiza walikuwa watu wazima, hivyo hapo hapo...kabla hata ya kupiga hatua ya maana, walidakwa.

Melvin, akiwa mwepesi, alimuuma pua yule pacha aliyekuwa amemshikiria, na kumponyoka. Alienda akipiga mayoe ya kila aina, kama akili yake ya utotoni ilivyomtuma.

"Mel! Mel! Mel! " alisikika Maya akilia kwa mbali, na baada ya muda sauti iliishiria kabisa. Hawakuwa wakimkimbiza, aligundua; na wao walikuwa wakikimbia na Maya. Hivyo aliongeza juhudi na baada ya muda alikuwa nyumbani.

Mama yake, aliyekuwa akianika nguo, alijua papo hapo kuna kitu hakikuwa sawa, hivyo alimkimbilia.

"Poa, Poa baba 'angu, nambie kulikoni? Maya? Maya yuko wapi?" Alimuuliza Melvin ambaye alikuwa akitafuta pumzi.

"Poa, Poa,"

"Watu...pacha...piga...beba Maya...mi...mi...kaja kuita...mi..ponyoka" alijitetea Melvin.

Hakuhitaji kuambiwa mara mbili,

"Baba Mel, Baba Mel!" Mama Melvin aliita huku machozi yakimtoka.

Siku tatu nzima, Maya alitafutwa nyumba baada ya nyumba, ila hakuweza kupatikana, hai au hata mwili, matangazo yalifanywa kwenye redio, mapolisi na wapelelezi waliitwa, ila hapakuweko namafanikio. Maya, akiwa mdogo, miaka mitano, aliibwa, na hakuweza kupatikana.

Tatizo liliokuwa limeukabiri mkoa wa Arusha, tatizo lililokuwakuwa likisika kwenye redio, lilikuwa limekifikia kijiji cha Chiro, na Maya akiwa muathirika wa kwanza.

ITAENDELEA
 
2
"Maya! Maya!" Melvin alistuka kutoka kwenye ndoto yake mbaya iliyomuandama karibia kila usiku. Alivuta pumzi kwa sekunde kadhaa na kuyaruhusu mapigo yake ya moyo kutuama. Pole pole alijiinua na kutazama ukutani picha ya Maya, na tabasamu lake lililomfanya akumbuke mambo mengi ya utotoni mwake. Alitikisa kichwa na kujikakamua, aliyafuta machozi yaliyokuwa yakimtiririka taratibu na kimya kimya akaanza kuomba sala yake ya asubuhi.

Miaka kumi na tano ilikuwa imepita toka Maya anyakuliwe na mapacha wale wasio na huruma. Melvin ambaye kwa sasa alikuwa na miaka ishirini na miwili, aliikumbuka siku ile kiundani zaidi kwa kuwa ilijirudia kila usiku kwenye ndoto zake.

Ni nyakati kama hizi ambapo alikuwa akijilaumu kutobaki na kumsaidia Maya. 'Ila sikuwa na nguvu' aliwaza. Labda angebaki naye wakampeleka, ila alijua tu alipaswa kujisamehe na kusahau. Maana, tukio lile na msako uliofanywa baada ya hapo ulipelekea kukamatwa kwa watuhumiwa zaidi ya kumi na tano kwenye wilaya ya Engorora ambapo watatu walitoka Kijiji cha Chiro. Toka hapo, hakuna tukio jingine la kukamatwa kwa mtoto lililofuata mkoani Arusha, kiujumla. Kwa miaka yote kumi na tano...watoto walikuwa salama. Watoto peke yao walikuwa salama.

Melvin alipomaliza kuomba sala yake, alitazama saa kwenye simu yake, ilikuwa saa moja kasorobo. Aliwasha radio na kisha kutwaa dawa yake kutoka kwenye kopo malumu la miswaki na kupaka kweye mswaki wake.

"...zinaendelea kutikisa taifa. Pia, Bwana Abbas M. Jembe bado yuko mbinde mbinde katika kampeni za kuwania u meya wa jiji la Arusha huku akishindana na mpinzani wake wa kitambo Kabil Patel. Nani ana dalili za kukubaliwa? Usikose kwenye habari zetu za ndani leo hii saa...."

Melvin, ambae muda wote huu alikuwa amesimama akisikiliza kwa makini, alitikisa kichwa na kuzima redio.

Chumba chake kilikuwa kikubwa, chenye dirisha pana kwenye kuta ya kusini. Picha mbali mbali zilitundikwa kutani, huku Picha ya Maya, ambayo ilikuwa imekuzwa kuliko nyingine zote, ilining'inia peke yake kwenye ukuta wa Mashariki. Magharibi, karibu na ukuta, ndipo kitanda chake, cha sita kwa tano, kilipo kuwa. Kuta, kama lilivyokuwa paa, zilikuwa nyeupe kama seruji.
Kaskazini, pembezoni mwa mlango, kabati jeupe la nguo lilikomba nafasi na kushoto kwake, ndipo kijimeza kidogo alichotumia kuandikia kilipo kuwa, Radio, Vitabu kadhaa, na magazeti vilitandaa kwenye kijimeza hichi. Kilikuwa ni kitu peke kwenye chumba, mbali na kitanda ambacho hakikuwa safi, na katika mpangilio.

Ilimchukua takribani dakika kumi na tano kuoga na kujiweka sawa, aliwabandikia wazazi wake chai na kuwatayarishia sebuleni pamoja na kitafunwa...baada ya hapo akaamua kwenda shamba. Hayo ndio yalikuwa maisha yake, na hakujua yangeendelea hivyo kwa muda gani; kikubwa ni kuwa hakuyachukia.

Toka Maya apotee kwenye mazingira ya kutatanisha, alikuwa akisumbuliwa na ndoto zilizokuwa zikiihusu hiyo Jumamosi. Na ilikuwa ngumu kwake kuendelea na maisha ya kawaida, ila baada ya kupitishwa kwenye vipimo maalumu--therapy, kama vilivyojulikana--aliweza endelea na elimu. Sasa, miaka kumi na tano baadae, alikuwa mhitimu wa chuo kikuu kwenye stashahada ya sanaa maendeleo. Kwa uhaba wa ajira, aliamua kurudi nyumbani na kujiendeleza kwanza kupitia kilimo.

Ilikuwa mwendo wa dakika saba hivi kutoka kwao hadi shamba alilolima lilipokuwa. Na alipofika tu, alianza kulima.

Alilima na kulima.

'Angekuwepo Maya angekuwaje?' Alijiuliza huku akilima. Alitikisa kichwa chake kama vile kwa kufanya hivyo kungeyasukuma mawazo yake mbali.

Kwa mbali kwenye kichochoro kidogo kilicho pita shambani, wasichana kadhaa wa makamo walipita wakiwa na ndoo zao. Wote walikuwa wakitabasamu na kunon'onezana vitu.

"Mtoni, mida hii?" Melvin alianzisha maongezi walipofikia aliko kuwa.

"Enhe..." Alijibu mischana mmoja wa makamo ambae kwa kuulizwa vile alianza kung'ata kucha na kuchora ardhini kwa vidole vyake vya mguu. Wasichana wengine kwa mbali waliangalia kwa umakini wakitabasamu.

" Asee, ila ndo nyakati hizi, mvua zitakuja si muda," Aliongezea Melvin na kuendelea kulima.

"Yaani..." mischana yule aliyekuwa akirembua rembua alijaribu kujibu.
Ukimya ulifuata kwa sekunde kadhaa na upepo ulivuma.

"We Sarah!" Msichana mmoja kwenye lile kundi liliokuwa likitazama aliita.

"Na...naenda ivo, " Sarah ambaye alikuwa ameacha kujing'ata kucha alisema, na kubeba ndoo yake.

"Sawa mama, maji ya kunywa...mkiwa mnatoka et, eh?" Alisema Melvin kimatani. Sarah bila kusubiri aitwe tena na marafiki zake, aliondoka huku akitabasamu.

'Mhh...ni shida,' Melvin aliwaza na kuendelea kulima. Toka atoke chuoni, aliweza kuiona hiyo tabia ya ajabu kwenye baadhi ya wasichana hapo kijijini, na baada ya muda, aliweza kuwasoma mienendo yao.

Wengi walipenda kumsemesha japo walimuogopa hivyo, kila nafasi iliyojitokeza walimuacha yeye aanzishe maongezi. Kilichomtatiza ni alipo gundua kuwa walipanga nani ajibu endapo angewasemesha. Hakuwa elewa. Hawa wasichana huwa hawaeleweki, aliwaza na kuendelea kulima.

Alilima na kulima, na muda ulizidi kuyoyoma. Wasichana walipotoka kuteka maji walimsaidia maji ya kunywa nae hakujuta kukumbushia.

"Saa ngapi?" Msichana mmoja aliuliza.

Mhh, Melvin aliwaza. Huyu alikuwa amepata ujasiri wa kumsemesha.

"Er.." Melvin alipapasa kwenye mfuko wa shati lake na kuchomoa simu yake janja, smatifoni, kama zilivyofahamika. "Saa sita dakika mbili, " alijibu na kurudisha simu yake mfukoni.

"Huh," alisema yule msichana, akitabasamu. Sarah alikuwa kwa nyuma pamoja na wasichana wengine wakitazama. Mmoja alimtazama mwenzake, akitikisa kichwa chake kidogo kama vile alikuwa anamwambia: unaona-nilikuambia-ana-smatifoni na yule mwenzake kama vile alikuwaga akibisha, akajichekea kwa aibu.

"Muda unakimbia kwel...a'fu mnatoka mtoni saa hizi, toka saa moja!" Melvin alisema kwa mshangao.

"Tulifua, tukaoga," alijibu Sarah.

"Oh," Melvin naye alisema, nakuweka jembe chini. "Nami, naishia hapa, kwanza nkaoge...kesho nayo siku."

Baada ya kusema hivyo, alikusanya magugu kadhaa, na kuyatupa kwenye rundo kubwa ambalo alikuwa akikusanya toka aanze kulima. Alijinyoosha mgongo na kuweka jembe lake begani.

Aliongoza njia, na baaada ya mwendo wa dakika mbili hivi waliifikia njia panda ambapo aliagana na wale wasichana. Alitembea kwa dakika nne nyingine akipita kwenye mashamba ya katani na mbuni. Baada ya kuvuka barabara iliyokuwa ikielekea Engorora alianza kupaona kwao.

Kwa mbali aliweza kumuona baba yake na mama yake wakiwa wameketi kwenye gawa la kupumzikia. Kwa mbali, aliweza ona kuwa baba alikuwa akisoma gazeti, na mama yake alikuwa akisuka mkeka.

Nyumba yao ilikuwa pana yenye vyumba kumi na viwili, moja ya nyumba chache za kisasa zilizokiwemo kijijini Chiro. Mzee Christopher, baba yake Melvin, aliweza kujibana na kuhakikisha kuwa aliboresha nyumba yake kisawa sawa. Kwa mbele, madirisha ya vioo, 'tinted' , yaliakisi miale ya jua ambalo lilikuwa limeanza kupata makali. Kama ilivyo kuwa desturi kwa nyumba za kijijin, uwanda wa mbele ulikuwa mrefu na wenye upana sawa na wa nyumba. Maua ya aina mbali mbali yalipandwa pembezoni mwa uwanda huu huku nyasi nzuri, aina ya 'pascarum' zikitanda kote. Mandhari yalikuwa yakivutia. Tambo kumi hivi, kutoka nyumba ilipo, kwa upande wa kushoto, Mzee Christopher aliweza kuweka gawa; sehemu ya kupumzikia na kupunga upepo. Ilikuwa meza ya mbao iliyo sanifiwa vizuri ikizungukwa na viti kadhaa, huku paa la nyasi likitoa kivuli. Hakika palivutia.

"Dume langu!" Alisema Mzee Christopher, akimtazama Melvin ambaye alikuwa kawasili nyumbani.

"Baba, njoo huku kwenye kivuli kwanza," Alisema Aleta, mama yake.

Melvin, bila kupoteza muda, aliweka jembe lake chini na kisha kujumuika nao kwenye mgawa.

"Shkamooni," aliwasalimu na kujilegeza kwenye kiti.

"Marhaba, umepiga jembe mno leo...saa sita na kitu et," alisema Mzee Christopher akiweka gazeti lake chini.

"Sehemu ilikuwa imebaki ndogo kwel, nikasema niimalizie..." Melvin alijibu, na kuzuia mhayo. "...japo sijamaliza."

"Duh, utakuwa umechoka...baba ako nae alikuwaga anapenda kulima, ka wewe," alisema Bi alita.

Mzee Christopher alitabasamu kwa majigambo.

"Kulima ni zoezi tosha, kulima,"

"Eeh..."

"Ni zoezi tosha, a'fu ma, jioni nataka nkaende town, n'nna siku,"

"Kwenda utaenda...sema tulitaka kukwambia kuwa tutaondoka ile jioni....tutarudi kesho kutwa," Bi Alita alijibu.

"Er...Jumapili?" Melvin aliuliza akipokea hizi habari kwa mshangao. Haikuwa kawaida ya wazazi wake kusafiri.

"Ndio," Mzee Christopher alijibu, "Binamu yako anatolewa posa, Shangazi yako katutaka tuwepo,"

"Rose??!"

Zilikuwa habari za kushangaza na kustua kidogo. Rose, alikuwa mtoto wa tatu wa shangazi yake; alikuwa msichana pekee kwenye familia yao. Baada ya kufeli mtihani wa darasa la saba, amekuwa akiketi nyumbani, baada ya kushindwa kujifunza kutumia chereani. Melvin alikumbuka mara ya mwisho amemuona binamu yake, ilikuwa miaka mitatu nyuma wakati akienda chuo, na Rose alikuwa na miaka kumi na sita tu wakati huo. Miaka kumi na tisa! Bado mdogo, aliwaza.

"Asee...nani huyo ana bahati?" Melvin aliuliza, akijaribu kuondoa mawazo yake huko.

"Nasikia ni kijana mmoja anatokea huko mjini, Arusha. Anamiliki duka kubwa kweli la nguo, kule Soweto," alijibu Bi Aleta.

"Eti eeh," Mzee Christopher Alizipokea taarifa hizi mpya.

"Enhe," alijibu Bi Aleta.

Ukimya mdogo ulifuata, na Melvin alikuwa kazama tena kwenye mawazo yake, 'Sasa kaa hao walikutanaje?' Aliwaza. Bi Aleta, alizidi kufuma mkeka kwa ustadi zaidi.


"Kuna mapya?" Melvin alimuuliza baba yake akiashiria gazeti.

"Mambo yale yale," alijibu Mzee Christopher. "Dunia hii inakoelekea hata sijui."

Melvin alinyamaza, kumpa baba yake nafasi ya kuelezea zaidi.

"Wasichana wanazidi kutekwa na hao...wasiojulikana?" Mzee Christopher aliangua kicheko cha huzuni. "Huyu Jembe...Abbas, asinge gombea umeya, ukuu wa mkoa ungemfaa zaidi, labda angetuondolea haya mambo Arusha."

"Asee, na hakuna anejua wanakowapeleka?" Melvin aliuliza.

"Baba 'angu, utajuaje? Nasikia ni kuja kwenye vijiji na magari yao...wanasomba, hao...wanaenda," Bi Alita alijibu. Bi Alita alifuta chozi lilikuwa limemteremka, na kujaribu kutabasamu ila hakufaulu. Yaliendelea kumtoka na kimya kimya, aliamka na kuelekea ndani. Mzee Christopher alibaki akitazama juu.

Kwenye ukimya uliofuata, na kile kilichotokea, Melvin hakuhitaji kuambiwa mara mbilimbili, kile alochoshuhudia. Machozi ya mama yake, ukimya wa baba yake. Hii ilidhihirisha zaidi kuwa matukio ya utekaji, yaliyoshika kasi mkoani Arusha katika kipindi hicho cha uchaguzi, yaliwatatiza kama yalivyo mtatiza, ila alijua zaidi; Yaliwafanya wamkumbuke Maya.

Rose. Aliwaza. Binamu yake angeolewa na mfanyabiashara na mwishowe kwenda kuishi nae jijini, Arusha. Labda hivyo ndivyo ambayo ingekuwa kwa Maya, endapo angekuwepo. Kwa kuiweka hivi, alijua jinsi ilivyouma. Alitamani labda angekuwa na maneno ya kutia moyo kuwaambia wazazi wake, ila hakuwa nayo.

"Yataisha, Mungu si Athumani," Alisema kwa baba yake. Japo alihisi kilikuwa kitu cha kipumbavu kusema, ila hakuwa na maneno mazuri kichwani. Aliangalia saa kwenye simu yake, ilikuwa saa sita na dakika arobaini na mbili. Alianza kuhisi uchovu, joto. Bila kuwa msumbufu, kimya kimya, alitoka pale kwenye mgawa na kuokotoa jembe alilokuwa ameliegesha kwa chini, na kuelekea upande wa pili wa nyumba. Huko kulikuwako na stoo, angeweka jembe na kisha kupumzika. Alifanya hivyo.

ITAENDELEA
 
3
Kilomita 18, kutoka kijiji cha Chiro, Abbas Jembe alikoroma kitandani mwake kwenye jumba lake la kifahari, jijini Arusha.

Chumba kilikuwa kipana mno, vitanda 12 vya sita kwa sita vingeenea endapo vingepangwa sambamba. Kushoto mwa kitanda chake, kulikopaswa kuweko ukuta wa nne, kulikuwepo kioo kikubwa kilichotoka kwenye paa hadi sakafu. Hili ndilo lilipaswa kuwa dirisha. Vitu vingi vya kifahari vilitapakaa kwenye meza pana ya kioo iliyokuwa mkabala na kitanda, karibu na dirisha lile kubwa la kioo. Saa tatu za dhahabu, kompyuta mpakato aina ya Apple Macbook Pro, na simu kadhaa za gharama vilitandazwa bila mpangilio kwenye meza ile. Kwa juu, feni ilizunguka kwa kasi ya wastani.

'NGO NGO NGO' NGO' mtu alibisha hodi. Ila hakujibiwa.

'NGO NGO NGO' NGO' Alirudia tena. Bado kulikuwa kimya.

'NGO NGO NG...'

"Arrgh!" Abbas alizinduka kutoka usingizini. " Nini? Nani? Aki ya nan kama...."

"Ni James, mkuu," mtu yule alijibu kwa upande wa pili.

"Oh," Abbas ambaye bado alikuwa amejikunyata kwenye kitanda alijibu. Aliamka na hapo hapo alitumia mkono wake kuyakinga macho yake kutokana na mwanga wa jua uliokuwa ukipita kwa urahisi na kwa wingi kwenye dirisha lake kubwa. Alijipa muda na kuyafunua macho yake taratibu.

"Ingia," alisema na kunyanyuka kutoka pale kitandani, na kusimama kwenye ukuta ule wa kioo, dirisha. Kwa njee aliweza kuona mandhari ya nyuma ya jengo lake yaliyovutia. Kulikuweko na bustani nzuri ya maua, na bwawa la kisasa la kuogelea. Magali manne ya kifahali yalipaki kushoto kwenye sehemu maalumu iliyokuwa imejengwa kwa ajili ya matumizi hayo. Chumba chake kilikuwa kwenye horofa ya tatu kwenye jengo lake la horofa tano, hivyo yote aliweza kuyaona kutoka juu. Kwa mbali kidogo aliweza kuziona horofa nyingine za jiji la Arusha, na alivutiwa na mandhari nzima.

Mwanaume, mwenye umri wa miaka therathini hivi, akiwa amevaa suti, tai , na viatu vyeusi, shati tu likwa jeupe, aliingia chumbani humo huku akiwa ameshikilia faili jeusi mkononi. Kwa jinsi alivyotembea---wima, huku kichwa chake kikiwa kama cha mwanajeshi kwenye gwaride---mtu angesema alikuwa roboti.

"Saa ngapi sa hivi?" Abbas ambaye bado alikuwa akitazama nje, aliuliza.

"Saba na dakika tano, mkuu, " James alijibu.

"Shit," Abbas alitamka kimya kimya na kumgeukia James, "Kikao...nlikuwa na kikao!"

"Ndio, mkuu."

"Enhe?"

"Ulikiwa na vikao viwili, mkuu. Cha saa mbili na cha saa nne, nlijaribu kukuamsha, hukuamka, mkuu. Gloria amekuwakilisha." James alijibu kwa unyenyekevu.

Abbas alimtazama James kwa muda, na bila kusema neno aliugeukia ukuta ule wa kioo...na kundelea kutazama nje. Ukimya ulipita kwa sekunde kadhaa. Nae aliruhusu, uendeelee kutawala kwa sekunde zilizofuata.

"Kuna kitu?" Mwishowe aliuliza.

"Ndio, waandishi wa habari wamefika sio muda na wamesisitiza kuonana na..."

"Mimi."

"Ndio, mkuu."

'Pumbavu zao,' aliwaza.

"Sawa, kawaambie nafika, ndani ya dakika kumi kama wataweza subiri."

"Ndio, mkuu," James alijibu. Na kuweka faili lile jeusi kwenye ile meza ya kioo."Maafikiano, kwenye vikao vyote viwili, leo."

"Ntapitia baadae," Abbas alisema, na kupiga muayo. "Vipi, mipango iko kama ilivyopangwa?"

"Ndio, mkuu," James alijibu.

"Vizuri, Gloria asifahamu kitu. Hakikisha kila kitu kinaenda sambamba."

"Ndio, mkuu."

"Nakuaminia, " alisema Abbas na kurudi kuketi kwenye kitanda chake kikubwa. Alisema hivyo kila alipo maliza maongezi na mtu wake wa ndani, na hivyo James, kama alivyoingia, alitoka na kufunga mlango.

Abbas, alihema na kupitisha mikono yake kichwani.

'Saa saba!' Aliwaza. Kwenye mambo ambayo hakuwa akiamini ni kuwa angeweza kulala fofo hadi saa saba mchana. Haijakaa sawa hii, alifikiri. Alijinyoosha na kisha kuelekea bafuni.

Abbas, alikuwa wa urefu wa wastani mwenye mwili imara kwa mtu mwenye miaka hamsini na sita. Mikunjo kwenye sura yake ambayo ilianza kuonesha uzee, ilimfanya kila mtu aliyemuona kwa mara ya kwanza kuwaza kama aliwahi kucheka maishani mwake. Na wengi hawakuwahi kufanikiwa kumuona akifanya hivyo.

Siku hii ilikuwa ya muhimu kwake naye alikuwa ameikosa. Baada ya kujiingiza kwenye siasa na kujaribu kugombea u 'meya' wa jiji la Arusha, alianza kuchoka haraka kutokana na kamepeni alizofanya kwenye wilaya na vimiji kadhaa mkoani humo, hali iliyompelekea kulala sana.

Ndani ya dakika chache aliweza kutoka bafuni, na kubofya kijirimoti kilichokuwa pale mezani, ukuta mmoja wapo, taratibu ulifunuka kuonesha chumba cha siri kilichokuwa na makabati makubwa matatu na sehemu ya manukato.

Alifungua kabati la kwanza---lilikouwa na nguo za kila aina---na kutoa suruali gumu, la kahawia, fulana pamoja na shati jeupe la mikono mirefu. Hakutumia muda kuvaa, na baada ya kuhakikisha alipenda muonekano wake, alifungua kabati lile la pili. Hili lilikuwa la viatu. Kulikuwemo kila aina ya viatu, ilimchukua sekunde therathini hivi kuamua angevaa vipi. Baada ya kuwaza kwa makini lichukua raba, nyeupe na kujivalia. Alijipuliza manukato yake pendwa, na kabla hajatoka kwenye chumba kile, alifikiria kidogo na kufungua kabati lile la tatu. Silaha na bunduki za aina mbali mbali zilitandazwa humo kwa umakini. Alichukua 'Glock 20 SD' kutoka sehemu iliyokuwa na aina kumi hivi za bastora na kisha kufunga kabati lile. Kwa umakini aliichomeka kwenye suruali yake kwa nyuma, na kufungua kabati lile na nguo. Alitoa mkoti wa kahawia na kuvalia kwa juu. Hakuwa na uhakika kwanini alichukua bastora ile, ila hakuirudisha. Alitoka kwenye chumba kile, na kubofya namba kadhaa alizojua yeye, nao ukuta ulijifunga. Kama ulivyokuwa awali, mtu asinge dhani kulikuwa na chumba hicho cha siri nyuma ya ukuta huo.

****
Horofa ya kwanza, kwenye jumba hili la kifahari, lilitumika kama sebule. Masofa marefu ya kuvutia yalipangwa kiupekee huku meza kadhaa za kioo zikifidia ile nafasi iliyobaki kati kati. Kwenye kuta moja wapo, Runinga ya inchi sabini na sita ilitundikwa kwa makini huku mfumo wa sauti ukiwa umeundwa kiumakini kumfanya mtazamaji ahisi sauti ilitoka chini ya sofa alilo kalia.

Siku hii, waandishi wa habari kutoka makampuni mbali mbali walikusanyika humu, kila mtu na peni pamoja na karatasi yake, baadhi wakiwa na 'tepu rekoda' tayari kumhoji Abbas, na kupata cha kuandika kwenye mageziti yao.

Dakika therathini na nane zilikuwa zimepita toka mtu aje na kuwaambia kuwa Abbas angefika ndani ya dakika kumi. Waliendelea kungonjea kwa hamu, huku baadhi wakitazama saa zao za mikononi kila baada ya muda fulani.

"Hellow!" Alisema Abbas, aliyetokea kwenye ngazi zilizokuwa zikielekea kwenye horofa ya pili. Hatimaye alikuwa amefika, na kila nyuso ya muandishi wa habari iliwaka, na furaha isiyofichika.

"Mtaniwia radhi, haikuwa kwenye ratiba yangu kuwa mchana wa Ijumaa hii, ningetembelewa na wanamiyeyusho," alisema kwa mitani huku akiketi. Baadhi walitabasamu, baadhi tu.
Wapiga picha walianza kupiga picha.

"Er...niko tayari kuwasikiliza, natumai mtakuwa na maswali," Alisema Abbas huku akijituliza vizuri kwenye sofa,"...ntajaribu kujibu kadri muda utakavyo ruhusu....saa nane na nusu nina 'interview' pale ShaniTV, hivyo....yap, tuanze!"

Kama ilivyokuwa makubaliano, wanahabari walinyoosha mikono yao, na yeye angechagua nani aulize swali.

Baada ya kuwaangaza kwa muda, alimchagua mmama mmoja aliyekuwa akituliza miwani yake usoni.

"Ahsante," yule mama alisimama na kusema. "Watu wa jiji la Arusha, na watanzania kwa ujumla wangetaka kufahamu, billionea kama wewe, kwanini utake kuwa meya, kwanini sasa hivi baada ya miaka yote hii?"

Abbas alikooa kabla ya kuendelea kuzungumza, na kila mtu alikuwa tayari kuandika.

"Kiufupi, kila mtu ana ndoto, nami nilikuwa na ndoto za kuwa mwanasiasa toka udogoni, nimeipata nafasi hii ambapo mkoa wetu unahitaji mabadiliko, kwanini nisijaribu?"

Wanahabari walimalizia kuandika, kila mtu kwa nafasi yake na mikono ilirushwa tena hewani. Abbas alimchagua mkaka mmoja aliyekuwa na kinasa sauti.

"Shukrani, boss wangu," Kijana yule alianza. "Unazumziaje matukio ya kinyama ambayo yamekuwa yakitokea mkoani Arusha kwa miezi sita mfurulizo?"

"Er," Abbas aliwaza kwa makini kabla ya kujibu. "Hizi ni nyakati mbaya, na haya matukio ya utekaji wa ndugu zetu yanaendelea kwa kuwa vyombo husika havifanyi wajibu wake kiustahiki. Kwa kuwa Meya wa Jiji la Arusha amefumbia macho, yeye na viongozi wengine wa jiji hili, hata na viongozi wa mkoa. Na hii ndio sababu moja wapo nimeamua kugombea ili Kuleta ukomo katika swala hili."

Kulikuwepo minon'gono kadhaa, na baada ya muda, mikono ilirushwa tena juu. Kabla hajachagua, James aliingia na kumnong'oneza kitu sikioni na kisha kuondoka.

"Er....rafiki zangu, muda sio rafiki, ntaruhusu swali la mwisho...ummm..." Aliwaza kwa muda akiwatazama. "....Wewe," alimnyooshea kidole mdada mmoja aliyekuwa kanyoa nywele zake na kuziwekea rangi nyeupe, zile zilizobaki.

"Umm, Ahsante. Kwanini kwa miaka yote hii ya umaarufu wako, hukuwahi kuonekana na mke...au kuwa na mahusiano, Bwana Abbas? Huyu Gloria, tetesi zinasema ni binti yako, je ni binti yako wa..."

"Kumzaa, kuokota au kununua?" Abbas alimalizia swali kuwafanya baadhi wacheke. "Nadhani mtu akimtazama Gloria na kunitazama, jibu analo. Samahani, huko sintogusia." Abbas alisema na kisha kuamka pale alipoketi.

"Bwana Abbas! Bwana Abbas!" Wanahabari walianza kuita....wakirusha mikono yao, maswali mawili matatu hayakuwa yamefidia muda wote waliobaki pale wakimsubiri.

Abbas aliruhusu mbaba mmoja wa makamo, kuuliza swali, alipofika kwenye lango la nyuma.

"Er...tunaweza kufahamu mikakati ya kuanza mradi wako wa 'Mabastania' uliko fikia....na...na...kama ugomvi wako na meya Patel unachangia..kwa ucheleweshaji?"

Mabastania, mnafahamu...nliropoka au?, aliwaza kwenye ukimya uliofuata. Hakuwahi kukumbuka kutamka hadharani kuhusu mradi huo.

"Mimi na Meya Patel, hatuna ugomvi. Ni misuguano ya ki..ya kisiasa, na siwezi muhusisha na kuchelewa kwa 'Mabastania'. Nadhani nliwahi kuwaambia(kama niliwahi) kuwa...huu utakuwa mradi mkubwa utakao tatua tatizo la ukosefu wa ajira kwa maelfu nchini. Unahitaji maandalizi marefu, hivyo ningewataka muwe na subira."

Kulikuwa na minong'ono kadhaa na mikono ilirushwa tena hewani. Bwana Abbas alitazama saa yake, ilikuwa saa nane dakika tisa. Muda sio rafiki, hivyo aliwakimbia.

Alipitia mlango wa nyuma, huku akiacha wanahabari wakimuita na kumwambia asubiri. Muda hakuwa nao. Hivyo hakuwasikiliza. Kwa nje, alikuta gari likimsubiri, na kijakazi aliyekuwa kasimama pembeni ya mlango alimfungulia mlango wa siti ya nyuma kwa heshima.

"Habari, Rashid," Abbas alisalimia na kuingia kwenye gari lile la kifahali aina ya Ferrari GT 32X. Rashid, kwa nje alifunga mlando na dereva wake bila kusubiri amri yoyote, aliwasha ingini na hao walipepea kupitia kwenye geti pana lililojifungua lenyewe na baada ya muda, walikuwa kwenye barabara kuu kuelekea jijini.

Kwenye gari, Abbas alivuta tray nyuma ya siti ya dereva, na kijifriji kidogo kilifunguka, humo kulikuwemo na aina mbali mbali za vilevi, na vinywaji baridi. Alichukua chupa ya mvinyo na glass na kujimwagia mpaka glass ilipotishia kujaa. Kwa umakini, alikifunga kiji friji kile, na kupiga pafu refu la mvinyo, na kutabasamu. Alihisi ubongo wake ulianza kuchangamka.

Ilimchukua sekunde kadhaa, na tumbo lake lililalama njaa. Ilikuwa saa nane nae hakuwa ameweka kitu tumboni. Alivuta tena tray kwenye siti ile pembeni na ya dereva na kijokofu kidogo kilitokea. Humo alichukua vipande kadhaa vya pizza, na kuanza kula.

"Ben...nna njaa," Abbas alimwambia dereva wake akiwa akijaribu kutafuta pande kubwa la pizza mdomoni, "Sikupipo asee!" Alisema kwa matani.

Ben, ambaye alikuwa makini kwenye uskani alitabasamu, na hakusema kitu.

"Hawa waandishi, watakuja kuniua bure, kila vijisiku viwili, washakutembela na vimaswali vile vile, tu kuuliza tofauti ya walivyo fanya mwanzo," Abbas alilalama akibugia kipande kingine cha pizza. "Uchumi ama kweli mbaya, mpaka wanasahau hadhi yao kwa taifa."

"Hadhi yao kwa taifa, mkuu?" Ben ambaye alikuwa kimya mda wote aliuliza. Kwenye mambo ambayo hakuwahi kudhani ni kuwa mwandishi wa habari angeonwa mwenye hadhi yoyote na billionea kama Abbas.

"Acha tu," alisema Abbas ambaye alikuwa amefungua jokofu na kutoa pizza nyingine. Ben alijitahidi kutoangua kicheko, "Usicheke Ben...sijala toka asubuhi na ni saa nane....nlikuwa...nlikuwa," aling'ata kipande cha piza na kufikiria.

"Yes...nlikuwa naongelea hawa wana habari. Enzi zetu kipindi ninakuwa, hawakuwa wakisukumwa na hela, bali mapenzi kwa kazi yao. Kupata interview kwenye TV, au gazeti...ilikuwa mziki kweli kweli,"

"Oh," alisema Ben, bila kutoa macho yake kwenye barabara.

"Enhe...nawashangaa hawa, wanakufuata wenyewe, maswali yale yale, nadhan ukiwapa hongo kidogo wanaweza andika uongo wowote kukuhusu!" Alisema Abbas, huku akimalizia glass yake ya pili ya mvinyo.
Alipenda kuongelea mambo kama haya alipokuwa anakula au ameshiba. Ben alilitambua hili, hivyo alibaki kimya.

Kwa mbali kidogo waliweza ona, horofa ndefu za jiji la Arusha, kwa kushoto, horofa ndefu kuliko zote ndiko waliko paswa kuwa. Lilikuwa jengo la Shani Media PLC, na muwasilishaji wa kipindi cha BiasharaLeo aliomba kupata nafasi hii na Abbas.

Ilikuwa Jumatano, na karani wa Abbas alipiga kumuambia kuwa ilikuwepo simu, kutoka ShaniTV kumhusu. Aliipokea nae aliulizwa kama alikuwa na muda kuhudhuria kipindi cha BiasharaLeo kilichoruka kuanzia saa nane na nusu mchana hadi saa kumi na mbili kamili jioni. Abbas hakukataa.

Walifika kwenye sehemu ya kuegeshea magari, nae Ben kwa umakini aliegesha gari, kwenye nafasi iliyokuwa wazi.

"Tumefika, mkuu," Alisema na kuizima injini.

"Vizuri, Ben," alisema Abbas aliyekuwa akinywa kinywaji maalumu kwa ajili ya kuondoa harufu mbaya mdomoni. Alifanya hivyo ili kuondoa harufu ya mvinyo. Wananchi hawakuwa wakijua kuwa alikuwa akitumia vilevi, naye hakutaka wajue. "Waweza kuendelea na shughuli zako, ila saa kumi na moja dakika arobaini uwe hapa...nataka nikawahi nyumbani."

"Ndio, mkuu."

Baada ya kuyasema hayo, Abbas alitoka nje na hapo hapo, alipokewa na mhudumu wa pale ShaniMedia tayari kumpeleka kwenye studio husika.

Kwa nyuma, Ben, ali ungurumisha gari na kutoweka.

ITAENDELEA
 
4
"...amka,"

Mel aliyekuwa kwenye usingizi mnono, alisikia sauti kwa mbali, ikimuita, naye akastuka.

"Mel? Umo?" Bi Aleta aliuliza akiwa amesimama nje ya chumba cha Melvin.

"Nimo, mama," Melvin aliitikia kwa uchovu na kupapasa kwenye kijimeza kilichokuwa pembeni mwa kitanda chake.

"Duh...huko ni kulala ama...unaumwa?"

"Hamna...uchovu tu," Melvin alijibu. Baada ya kupapasa kwa sekunde kadhaa, aliweza nyakua simu yake na kuiwasha. Ilikuwa saa kumi na mbili na dakika ishirini na moja, jioni.

"Sawa...baba, af hata hukula," Bi Alita alisema kwa sauti iliyoonesha alitatizwa kidogo.

"Ma, niko sawa....ntaoga afu, nile,"

"Sawa, sisi ndo tunaenda hivyo,"

"Eh,"

"Enhe...baba ako katangulia mbele,"

"Anha...basi mkienda, Rose mnipee salamu zangu," Melvin alisema na kujinyoosha.

"Sawa, baba...baki salama," alisema Bi Aleta, na kuondoka.

"Sawa..kwa kheri," alisema Melvin.

Kwa muda uliofuata, aliketi kitandani, na kuanza kuwaza. Vimilio kwenye simu vilikuwa vikilia kwa wingi. Hicho ndicho kilicho tokea endapo alizima simu kwa muda mrefu, marafiki zake walimtafuta kama uvumba. Alikumbuka tukio lilokuwa limetokea saa sita ya siku hiyo hiyo kwenye mgawa. Mama yake alikuwa amedondosha machozi na kumuacha na baba yake kimya. Aliyasukuma mawazo pembeni na kuingia bafuni. Baba yake alikuwa amemuwekea bafu la ndani, chumbani mwake.

Dakika na uchafu, toka aingie bafuni, simu yake iliyokuwa mezani ilianza kukoroma huku vijikengele vikilia. Alitoka bafuni nduki akiwa na povu kichwani kisha kupokea.

"Hallo,"

"Chalii, vp? Natuma texti hujibu..."

"Hey..."

"..afu...enhe unasemaje mwa'ngu?"

"Afu nini...ulitaka kusemaje?"

"Unakuja au huji.....akina Amani, Tuma wapo,"

"Sikia Jacky, ndo najiandaa hapa...nlipiga job, hatari leo...nlipotoka tu, nkapiga mbonji, ndo kuamka,"

"Nshasema....niiteni Jackson, mambo ya Jacky yamekaa kike kike,"

"Duh," Melvin alicheka," sawa bwana, Jackson."

"Poa...tunakusubiri." Jackson alisema na kukata simu.

Ilikuwa dakika ishirini na tisa tayari, hivyo, haraka haraka alirudi bafuni na kuendelea kuoga. Haikumchukua muda kujiweka sawa, alivaa tisheti nyeusi yenye maneno 'W E U S I' na dingirizi ya bluu. Kwa chini alivalia, raba nyeusi. Aliweka simu pamoja na wallet yake mfukoni. Alikuwa tayari kuondoka. Alijitazama kwenye kioo, na kutabasamu. Baada ya hapo alizima taa iliyokuwa inawaka wakati wote chumbani mwake na kufunga mlango.

Sebuleni, aliweza nyofoa chapati mbili na glass ya maziwa kutoka kwenye jokufu, akapigia shuta shuta. Alitazama saa kwenye simu yake, ilikuwa saa moja kasorobo. Alizima taa ya sebuleni na kuwasha ile ya nje. Kisha aliufunga mlango, ule wa mbao na wa chuma uliofuata. Alienda kwenye stoo, nyuma ya nyumba na kuchukua kijibaiskeli chake, na kufunga milango yote ya huko nyuma. Alipanda kibaiskeli na kwa udadisi na kasi iliyopendeza, alinyonga baiskeli yake kuelekea Engorora.

*****

Kwenye siti ya nyuma ya gari lake, Abbas alijituliza huku chupa yake ya mvinyo ikiwa mkononi. Wimbo wa taratibu wa kingereza ulisikika kwa sauti ya chini. Kwa mbele, Ben alikuwa makini kwenye usukani kama ilivyokuwa kawaida.

Taa za barabarani, zilimulika ndani ya gari kila baada ya sekunde kadhaa. Msongamano wa magari ulikuwa umepungua kwenye barabara kuu, nao waliweza kupata nafasi ya kutoka na kwa sasa walikuwa wakielekea nyumbani.

Simu yake Abbas, Samsung S10, iliita naye alilitazama jina na kisha kupokea. Alikuwa James.

"Naam," Abbas alisema na kusikiliza kwa makini.

"Bado! Nilikuambia kufikia saa kumi na mbili muwe mmemaliza," Abbas aliifokea simu.

"Nakupa li saa, James," Abbas alisema na kukata simu. "Ahh!" Abbas aliguna kwa hasira. Na kupiga pafu tatu za mvinyo. Aliruhusu kilevi kisisimue mwili wake, na baada ya muda alijituliza kweti siti yake.

Ghafla, kasi ya gari iliongezeka, nalo liliama babarabara kuu.

"Ben?" Abbas aliuliza kwa wasiwasi na butwaa.

Ben hakujibu, aliliongoza gari kupita kwenye njia mkato nyembamba isiyo ya rami.

"Ben! Unafanya nini?" Abbas ambaye alikuwa kamwagikiwa na mvinyo aliuliza tena, hofu yake ikiongezeka.

"Mkuu, ningeomba ufunge mkanda na kutulia, nadhani hayo magari manne yanatufuata." Ben, alisema kwa utulivu, huku kasi ya gari ikizidi kuongezeka.

Abbas, aligeuka na kutazama nyuma, range rover nne nyeusi, ziliwafuata kwa mbali kidogo, kwenye hichi ki njia mkato. "Huh!" Abbas hakuhitaji kuambiwa mara mbili, alikaza mkanda na kutulia. "Nifikishe nyumbani salama, Ben."

"Ndio, mkuu."

*****
Engorora ilikuwa mfano wa vijisenta vilivyokuwa, taratibu vinabadilika kuwa miji. Kwenye giza la saa moja, mji ulikuwa ukimeta meta kutokana na taa, za maduka na vituo vingine vingi vya biashara.

Melvin, alipita kati kati ya mji na kuelekea kushoto mwa hospitali ya wilaya, huko ndiko mtaa wa Mabatini uliko kuwa.

Japo ilikuwa usiku, shughuli mbali mbali ziliendelea kana kwamba ilikuwa mchana. Mama ntilie walikoka majiko yao, wauza mboga mboga, walitandaza bidhaa zao kwenye vijibanda vyao. Wauza chips na chapati nao walikuwa wakijishughulisha. Maduka kadhaa yalikuwa yamefunguliwa, mengi yakiwa madogo, na ya mamachinga, ila yalitimiza lengo...mtu angeweza kunua kitu chochote Mabatini hata kama ilikuwa usiku.

Melvin alipofika, alishuka na kuegesha baiskeli yake, pembezoni mwa ukuta, baiskeli nyingine nyingi zilikuwa hapo. Kwa mbele kidogo, barabara kuu iliyoelekea jijini Arusha, ilitanda....na kushoto kwake, stendi kubwa ya mabasi na magari madogo, ilimeta meta kutokana na wingi wa mabasi yaliyokuwepo.

Kulia, ndiko vibanda vya wauza mboga mboga vilipokuwa....na huko aliweza kuwaona Jackson, Amani na Denisi wakiwasemesha wadada waliokuwa waki tandaza bidhaa zao.

Alifika na kuwapa tano, wote...na kisha kukaa pembeni ya Jackson.

"Chalii, nikadhani huji..." Jackson alisema huku akitabasamu.

"Huyo? Anakosaje kwa mfano?" Amani alisema na wote wakacheka.

"Leteni mapya," Melvin alisema na kuwatazama wale wadada walokuwa wanauza mboga.

"Mapya? Yatoke wa.." alianza Amani.

"Matilda yuko wapi?" Melvin alimuuliza msichana mmoja aliyekuwa akimtazama kwa shauku.

"Kafuata mboga mboga kwa...huyo hapo," alijibu yule msichana, na wote waligeuka nyuma.

Matilda alikuwa msichana, mrefu, mwenye umbo la kuvutia na nywele ndefu. Alivaa gauni jeusi lililomwaga miguuni, na kichwani alikuwa na kikapu cha spinachi.

"Mlikuwa mnanijadili, eeh?" Alisema huku akitabasamu na kutua kikapu chake chini.

"Enhe...mzee mkubwa alikiwa anakuulizia hapa," Tumaini alisema.

"Nani..." Matilda alimtazama Melvin na kutabasamu zaidi, "...Mel? Ndo unamuita mzee mkubwa?"

"Mambo," Melvin aliyekuwa kuwa kimya wakati huo, alisalimu.

"Po-u-wa," Matilda alijibu, akitazama chini.

"Mama hali yake vipi?" Melvin aliuliza.

"Si nzuri, Si mbaya."

"Mhh..."

"Enhe,"

"Chali...sijui kwanza tukakuache kidogo?" Jackson aliingilia maongezi.

"Kwanini?" Melvin aliuliza.

"Uko bizze...afu hatujapata menyu," Jackson alisema.

"Ko mnataka mkapige cha mtume, pe'ke yenu? Acha hizo...tunaenda w..."

PUUH!

Kilisikika kishindo maeneo ya stendi, na kila mtu Mabatini alistuka. Kabla haijajulikana nini kililuwa kimetokea, Land Cruiser na Pick Up kumi na moja, moja baada ya nyingine, kwa kasi ya ajabu ziliingia sokoni mabatini na kupaki moja baada ya nyingine.

Watu waliokuwa wamejivika vinyago usoni huku wakishikilia mitutu, aina ya AK-47, waliteremka kwa kishindo wakipiga risasi kadhaa angani.

Kulikuwa na kelele Mabatini, wale waliojaribu kukimbia walipigwa mateke na ngumi. Wamama wengi na wenye maduka walijilaza chini. Hakuna aliyejua nini kilikuwa kinatokea. Bila kupoteza muda, wale watu walianza kuwanyakuwa wasichana na kuwapeleka kwenye magari yao kwa nguvu na kwa weledi. Matilda anbaye alikuwa kajilaza pembeni ya Melvin, akiwa kapigwa na butwa, naye alinyakuliwa na kuanza kuvutwa kwa nguvu kuelekea magari yalipokuwa.

"Niache, Niache...Wee! Niache!" Alijaribu kupiga kelele huku akijaribu kujiweka huru kutoka kwenye kabali ya mtesi wake.

"Mel! Mel! Mel!" Alianza kuita huku machozi yakimtoka. Wasichana wengine pia waliendelea kuvurutwa kwa nguvu nao walipiga kelele.

'Mel! Mel! Mel!' Maneno yalijirudia kichwani mwa Melvin ambaye wakati wote alikuwa chini kapigwa na butwa. Taratibu akili ilianza kurejea. 'Utekaji, wanatekwa!' Alieweza kutambua na hapo hapo aliinuka.

Toka siku ile alipokimbia na kumuacha mdogo wake, Maya, kupelekwa, aliapa kwa mungu wake kuwa asinge shuhudia mtu yeyote yule akitekwa nae akabaki anaiokoa nafsi yake.

Aliinuka na kuwatikisa marafiki zake....na kisha kuanza kukimbia magari yaliko kuwa. Magari yote yalikuwa yamejaa, na moja baada ya jingine, yalianza kutawanyika. Melvin aliongeza kasi na baada ya muda aligundua kuwa Jackson, Amani, Tumaini na Denisi nao walikuwa wakikimbia kuyaelekea magari yaliko kuwa. Gari la mwisho lilikuwa likiondoka, na wote kwa pamoja walijirusha kujaribu kulidandia. Kwa kukosa kosa, aliweza kudaka chuma kwenye boneti ya nyuma. Yeye, Amani na Jackson waliweza kundandia. Tuamini na Denis, hawakuwekeza nao walianguka kwa kishindo.

Gari liliongeza kasi na kuingia kwenye rami. Kama yale mengine, lilikuwa likielekea jijini Arusha. Kadri kasi ilivyoongezeka, Melvin na wenzake walishikiria kuhakikisha hawakuanguka. Amani alikuwa akilia.

ITAENDELEA
 
5
Kutokana na miaka nane ya kuendesha magari jijini humo, Ben alifahamu karibia kila njia mkato na kichochoro kilichojificha jijini Arusha.

Njia mkato hii, ingemfikisha Simbatini, jumba lake Abbas liliko kuwa. Sababu iliyomfanya ajiengue kutoka barabara kuu, ni kuwa magari yale yangeweza kuwasababishia ajari na kuwaacha aidha wakiwa majeruhi au hata wakiwa maiti. Kama kweli yalikuwa yanawafuata.

Baada ya kuendesha kwa sekunde kadhaa, aliyaona yalivyozidi kulifuatilia gari lao kwa nyuma, japo hakuwa na uhakika, aliihama barabara kuona kama yangewafuata, nayo yalifanya hivyo. Kwa bahati yao, mkato huu ulikuwa na njia panda kibao, naye alihakikisha anayapoteza yale magari.

"Wametuacha?" Abbas aliuliza kwa hofu baada ya muda.

"Nimewapoteza," Ben, alisema kwa majivuno. Kwa umakini aliiendesha gari kupita kwenye mkato wa mwisho, kurudi kwenye barabara iliyoelekea Simbatini. "Hii njia ni ngumu mtu kukufua..." ila hakumaliza.

Kwa dakika kadhaa zilizofuata, kila kitu kilitokea pole pole mno. Range Rover Mbili zilizo tokeza kwa mbele na mbili kwa nyuma, ziliwagonga kwa kishindo kikuu. Ben, ambaye hakuwa amekaza mkanda wake, alirushwa kutoka kwenye siti yake, kupita kwenye kioo na kuangukia kwenye boneti.Magari yale yalirudi nyuma na kurudia kuligonga gari lile kwa nguvu. Mara hii, Ben ambaye alikuwa akilia kwa uchungu kwenye Boneti hakupona.Gari lilimsaga miguu lilipogonga, na lilipokuwa likirudi, liliweza kukikanyaga kichwa. Abbas aliyekuwa kwenye gari..aliyaona yote haya kwa butwa na kila kitu kilienda pole pole mno, kwake ilikuwa kama vile yuko kwenye muvi ya kipigo.

Magari matatu yaliondoka na lile lilobaki, lilizima taa zake. Wanaume wawili waliokuwa wamevaa suti nyeusi, walitoka na kuuvuta mlango wa nyuma uliokuwa umebonyea kutoka kwenye gari la Abbas. Humo, walimyakuwa kwa nguvu na kumtupa kwa mbele ya Bonnet. Pembeni ya minyama nyama ya Ben, ambaye hakuwako tena. Abbas, akipumua kwa nguvu huku akitetemeka, aligeuza kichwa na kuitazama minyama nyama ya dereva wake pendwa. Kushoto gari lake la kifahari, lilibaki kama kinyago. Wale wanaume walisema kitu ila hakusikia....na papo hapo, walianza kumpiga mateke kwa nguvu.

*****

Melvin hakujua alikuwa kashikilia chuma kile kwa muda gani, ila ilikuwa muda mrefu. Kasi ya gari ilikuwa kubwa kana kwamba upepo ulivuma kwenye masikio yake kwa nguvu, hakuweza hata kusikia mlio wa gari.

Ghafla, kasi ilipungua na kabla hajajua kwanini, kona kali lilipigwa, na wote walianguka....walijitahidi kuamka kwa kasi ila ilikuwa ngumu...mabega yao yalikuwa yamechoka na wao walikuwa wameumia vibaya.

Kwa mbali horofa ndefu zilizometa meta kwenye anga la usiku zilionekana, walikuwa kwenye mtaa mdogo mdogo weye maduka yaliyofungwa.

"Tuko....tuko mjini!" Alisema Amani kwa woga.

"Arusha," Jackson alisema.

"Tunapaswa kwenda polisi!" Ndiyo maneno yaliyomponyoka Melvin, aliyekuwa wa mwisho kuamka.

"Polisi?" Jackson aliuliza; Kwa kupinga.

"Kweli," Amani alisema, "Wanapaswa kujua."

"Chalii,Polisi iliko unakufahamu?" Jackson aliuliza.

"Tunaweza tukawa..." alisema Melvin huku akipapasa mifuko ya suruali lake, "Aahh!"

"Nini?" Jackson aliuliza.

"Simu yangu, sijui iliko potelea..."

"Yoo, mwang' mi naanza kuogopa," alisema Amani.

"Tutembeeni, tukifika jijini kabisa...au....au tukikutana na mtu, tuulize kituo kiliko." Alisema Melvin.

Jackson alitaka kusema kitu ila alijizuia na taratibu wote wakaanza kutembea kwenye usiku huo mzito.

Kwa dakika kadhaa walitembea bila kusemezana. Kila mtu alikuwa akiwaza yake. Labda halikuwa wazo zuri kuyandandia yale magari ya majangiri, Amani aliwaza. Jackson bado alikuwa akijihoji sababu iliyomfanya kurukia yale magari....na njaa. Melvin, alijaribu kudadisi wasichana wale walikopelekwa, walikuwa wakifanyiwa au wakifanyishwa nini. Aliwaza kama Maya ali...

"Yoooo! Ahh! Mu..mta..Aii!...Mtalipa..Na.." Ilisikika sauti ya mtu akipiga mayowe kwenye giza. Amani bila kufikiria mara mbili mbili, alikimbilia sauti iliko kuwa.

"Yaani hili...Arrgh!" Alisema Jackson na kumfuata Amani kwa nyuma. Melvin naye alifuata kwa uangalifu.

Amani, miaka kumi na tisa, alikuwa rafiki yake Melvin toka utotoni. Alikuwa mfupi kidogo kuliko Melvin na Jackson, na pia alikuwa akiwazidi unene...yeye alikuwa bonge.

Wakati yuko kidato cha kwanza, aligongwa na piki piki kupelekea kulazwa miezi minne kwenye hospitali ya wilaya, Engorora. Toka atoke kwenye matibabu, wengi walianza kusema kuwa alipatwa matatizo ya akili...na hakuwa sawa kwa asilimia mia. Labda hawakukosea, Amani alifanya maamuzi ya ajabu ajabu mara kwa mara na mara hii alikuwa kafanya mengine, Alikuwa ameelekea kule yowe liliko sikika, bila mkakati.

"....Arrgh! Nani ...Na..Nani ..kawa.."

Anahitaji msaada, Amani aliwaza. Anahitaji Msaada. Alipolisogelea eneo, harufu ya nyama mbichi ilizisanifu pua zake. Amani alisimama kwa muda nakujaribu kuwaza angefanya nini. Wenzake walifika na wote watatu hawakupenda walichokiona mbele yao.

"....Aiii! Ohh..Mmetumwa na Nani...Hu.."

Mwili ulioonekana kusagika kuanzia kiunoni hadi chini---uliokuwa na minyama nyama na ute, sehemu kulikopaswa kuwa na kichwa---ulilala pembezoni mwa gari lililokuwa limefinyangwa kwa ajari. Melvin aliweza kuiona nembo ya Ferrarri kwenye gari lile. Kwa pembeni kidogo, gari jeusi aina ya Land Rover lilipaki..
.na waliweza kuona sehemu mayowe yalikotokea.

"Hiii!....Aarrrh!...."

Pembezoni mwa mwili ule wa mtu, wanaume waliokuwa wamejivika suti nzuri nyeusi walimpiga mateke kwa nguvu mwanaume mmoja aliyekuwa chini akivuja damu kichwani.

"Mwacheni!" Amani alijikuta akitamka. Melvin na Jackson wote walipigwa ganzi. Wale wanaume waliwatazama; sura zao zisizo na huruma zikiwatazama mmoja mmoja.

Kama vile haitoshi, Amani aliokotoa tofali...

"Amani..unafanya ni.."

...na kulirusha kwa nguvu zake zote kwa wale wababa. Lilimtwanga mmoja kisawa sawa kichwani naye alilia kwa maumivu makali.

Amani, ghafla alijihisi jasiri na kwa kasi alikimbia kumpiga ngumi yule mwanaume aliyekuwa kabaki.

"Amani!" Melvin alijaribu kuita ila alikuwa kachelewa.

Amani alivaana kwa sekunde kadhaa na yule mwanaume, na baadae, alianguka chini...alikuwa amedungwa kisu kifuani.

"Ama..."

TWAA!

Mlio wa risasi ulisikika. Yule baba aliyekuwa akipigwa alikuwa amejitahidi na kunyanyuka. Mikono yake ilitetemeka, na bastora iliyokuwa mikononi mwake ilikuwa ikitoa moshi mwembamba, mweusi.

Mwanaume yule aliyemdunga Amani kisu kifuani, alilia kwa uchungu na kuanguka chini.


TWAA! TWAA! TWAA!

Risasi nyingine tatu zilisikika na wanaume wote kwenye suti nyeusi walianguka, wakiwa wamekufa.

Jackson, machozi yakimtoka alikimbia mwili wa Amani uliko kuwa na kujaribu kuutikisa, kweli alikuwa kafariki.

Melvin alipiga magoti na kuanza kulia....hakuwa akiamini siku yake ya kawaida ilikuwa imefikia hapa. Matilda alikuwa ametekwa, alikuwa kilomita kumi na nane kutoka nyumbani na sasa rafiki yake, Amani alikuwa amekufa.

Yule baba, aliweka bastora yake nyuma ya suruali nakupangusa mikono yake iliyokuwa na damu kwenye mkoti wake wa kahawia.

"Vijana," alianza, huku akiinama kuusaka mwili wa mwanaume mmoja wapo. "Huu si wakati wa kuomboleza, kama mnayapenda maisha yenu...hii sii sehemu ya kuwa. Polisi watakuwa hapa sio..."

Alitwaa funguo kutoka kwenye mkoti wa yule bwana pamoja na simu yake.

"...muda. Tunapaswa kuyeyuka." Alimalizia sentensi na kurudi kwenye gari lake, humo alichukua funguo na pakiti ya sigara. Kwa mbele na nyuma, alichomoa namba za gari lile liliokuwa limefinyangwa.

Melvin ambaye alikuwa akiwaza sauti ile aliwahi kuisikia wapi...alistuka kidogo alipogundua.

"Er...bwana Abbas?" Melvin aliuliza bila kuamini macho yake.

"Kuna mengi hamfahamu kijana," Bwana Abbas alisema na kuingia kwenye land rover ile iliyokuwa imebaki.

Alichomeka funguo na kuvuta moto.

"Mnakuja au lah?" Bwana Abbas aliuliza. Melvin alimtazama Jackson na kisha mwili wa Amani kwa mara ya mwisho na kuingia. Jackson naye alifuata. Bwana Abbas aliutazama mwili wa Ben kwa mara ya mwisho naye aliweka gia, na kulirudisha gari kwenye barabara kuu.

"Tunaenda wapi?" Jackson aliuliza. Kimya. Alitaka kuuliza mara ya pili ila akajizuia.

Kwa mwendo wa dakika kumi hivi, walifika Sombantini, na katika jengo la kifahari la bwana Abbas. Kama kawaida, geti lilijifungua naye aliingiza gari lile ndani; Geti likifunga nyuma yake.

ITAENDELEA.
 
Habari mambo naitwa Mr Equator Nimeandika ujumbe huu kuku omba swala moja tu!
Mimi nimetengeza website ya ku share story ambayo ni http://www.equatorstory.com/
Je umekuwa ukipata tabu kupost story zako hapa?
Hili ndo suluhisho lako.
Mimi nataka nkupe nafasi ya kuwa mmoja wapo wa kwanza kutumia hii website
unda account yako na uweze kupost story yako mpya.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom