J.K.T MAFINGA
Saa kumi na mbili na nusu jioni.
Ndani ya moja kati ya ofisi za Jeshi la Kujenga Taifa (JKT),mlango uligongwa gongwa na mtu aliye nje.Sauti nzito ya mtu aliyekuwa ndani ilisikika ikisema "karibu".Mlango ulifunguliwa kisha ajenti Mick-reuben akiwa amevaa suti nyeusi iliyomkaa vyema ikisindikizwa na shati jeupe na tai nyeusi huku sikioni akiwa amevaa kifaa maalum cha mawasiliano kinachoitwa 'Tube Coiled Earpiece'.Kijana huyu alifunga mlango nyuma yake baada ya kuingia kisha akakaa katika kiti kilichokuwa mbele ya meza huku akitazamana na yule aliyekaa nyuma ya meza, mtu mzima mmoja ambaye alionekana kama mwenye umri kati ya miaka 50 hadi 55 hivi.
"Naitwa Mick-reuben kutoka C.T.I, nadhani ulipata ujumbe kuhusu ujio wangu".Aliongea kwa nidhamu kijana huyu huku akiwa katika hali ya utulivu wa hali ya juu.
"Ok, nimepata habari kutoka makao makuu na ndiyo maana niko ofisini hadi sasa.Mimi naitwa Aloyce Mwasambili.Ni mkuu wa kambi hili la Hapa mafinga.Nimepewa maagizo nikupe ushirikiano kwa kila utakachokitaka.Sijui nikusaidie nini kijana wangu."Aliongea kwa nidhamu pia mzee huyu ambaye mabegani alichafuka kwa nyota kadhaa.Alionekana kuwa mtu kwenye cheo cha juu.
"Kubwa hapa ni kuhusu tukio lililotokea na ambalo bado ni la moto kwa taifa letu na mataifa mengine.Tukio la kutoroka kwa gaidi wa kimataifa Omar al-Mahmood. Namna pekee ya kujua aliko kirahisi ni kwa kuwatambua baadhi ya watu wanaotuhumiwa kusaidia kutoroka kwake. Moja ya watu wanaotuhumiwa kuhusiana na tukio hili ni mtu ambaye hapo mwanzo alidhaniwa kuwa ji marehemu tangu mwaka 1998.Lakini katika upelelezi imegundulika kuwa yupo hai na anahusishwa moja kwa koja kwa kuhusika na tukio hili kwa namna moja au nyingine.Tumemtambua mtu huyu,kwa jina anaitwa John Karobota.Kwa kuwa hakufariki, ninaweza kusema kuwa alipotea akiwa na cheo cha luteni katika jeshi la wananchi,yaani JWTZ."Alianza kujieleza Mick kisha akaacha kwa muda kidogo kumuacha mwenyeji wake ayatafakari haya kabla hajaendelea kumueleza kwa kina.
"Sasa picha iliyopatikana inayotushuhudia kuwa mtu huyu yupo hai , imerekodiwa na kamera za kambi hii kwa hiyo tunaamini mtu huyu alikuwapo ndani ya kambi hii aidha kwa muda mrefu au kwa muda mfupi.Picha yenyewe ya mtu huyo ni hii hapa,sijui kama unaweza kuitambua".Alimaliza kueleza Mick huku akitoa 'Tablet' kutoka katika mfuko wa suruali aliyoivaa, kisha akapapasa kioo hapa na pale kisha picha waliyoipata ya John Karobota ikaonekana vizuri kabisa.Ni picha ya muda mrefu,lakini mkuu wa kambi hii bwana Aloyce alionekana kuitambua mara baada ya kuiangalia kwa sekunde chache tu.
"Picha hii siyo ngeni kwangu......Ahaa....Nadhani nimekumbuka kitu.Miezi kama mitatu hivi iliyopita,nilipigiwa simu kutoka makao makuu ofisi ya C.D.F(Mkuu wa Majeshi Tanzania). Simu hii ilipigwa na katibu muhtasi wa C.D.F, ambaye alinipa maagizo kuhusiana na ujio wa mtu huyu, kwamba atakuja katika kambi hii kwa muda mfupi kwa sababu ya kazi maalum anayoifanya katika mipaka ya nchi upande huu wa nyanda za juu kusini,yaani katika mkoa wa Mbeya kisha ataondoka.Kwamba hapa ndiyo itakua kituo chake kikuu wakati wote atakaokuwa akifanya kazi hiyo. "Alijieleza kwa maelezo ya mwanzo mkuu huyu wa kambi kisha akanyamaza kidogo akionekana kufikilia jambo fulani kwa kina kabla hajaendelea.
"Nilitambulishwa jina lake.Anaitwaaaaaaaa (huku akitafuta kitu katika makabrasha mengi yaliyokuwa katika droo za meza yake na kisha kutoa bahasha moja ya ukubwa wa 'A4'.akaifungua haraka na kutoa karatasi mbili zilizounganishwa kisha akaiangalia kwa haraka), yes....Anaitwa Jeremiah Mwakibinga.Cheochake ni Luteni. Lakini hiyo picha uliyonionesha haina utofauti sana na sura yake.Labda tu hiyo picha naweza kusema inamuonesha akiwa kijana zaidi ya alivyokuja hapa, au labda kama ni ndugu yake aliyefanana kwa asilimia mia."
"Na hii ni barua yake aliyokuja nayo na pia nilitumiwa ' email' kwa anwani ya makao makuu ya jeshi( huku akibonyeza hapa na pale katika keyboard ya kompyuta iliyo mezani pake) ambayo ni hii hapa".Alimaliza kuongea mkuu huyu wa kambi huku akimgeuzia Mick kompyuta yake ili aweze kuona barua pepe ile.
"Wewe umewahi kuzungumza na katibu muhtasi wa C.D.F kabla"Alihoji Mick Reuben.
"Ndiyo nimewahi kuzungumza naye zaidi ya mara ya tatu na hii ilikuwa ni ya nne.Tena kwa namba hiihii tangu nilipoteuliwa kuwa mkuu wa kambi hii miaka mitano iliyopita."Alijibu mkuu huyu wa kambi hii ya JKT.
Kisha mara tu alipojibu akaonekana kukumbuka kitu kwa ghafla ambacho ni kama kilimshitua kidogo.
"Lakini, kuna kitu nimekumbuka ambacho sijawahi kukifikiria hapo mwanzo.Nilipoongea naye mara ya mwisho,sauti yake ilikuwa kama inakwaruza hivi, siyo ile niliyowahi kuisikia kabla.Na siku ile alikuwa akiongea kama mtu aliyechangamka sana tena kirafiki kuliko kawaida ya siku zingine ambapo huwa anazungumza akiwa yupo siriasi , tena kwa sauti kama ya ki-amri amri hivi."Alimalizia kuongea mkuu huyu wa kambi,Aloyce Mwasambili.
Kengere ya hatari ikalia katika kichwa cha Mick.Tayari alikwishaunganisha maelezo haya na mambo ambayo yeye alikuwa akiyahisi, na kung'amua jambo katika kichwa chake.
"Ahsante.Ila kwa kukumbushana tu nadhani unafahamubkuwa tuliyoongea hapa ni siri kubwa na hakuna mtu anatakiwa kufahamu.Nikikuhitaji tena nitakutafuta.Naomba niondoke na barua hii kwa upelelezi zaidi pia naomba unitumie barua pepe hiyo uliyotumiwa katika anwani hii( huku akimuandikia anuani ile)." Akamaliza kuongea Mick.
"Haina shida.Nafurahi tu kama maelezo yameweza kukusaidia kwa lolote.Wakati wowote utakaponihitajiunakaribishwa sana".Aliongea mkuu wa kambi kisha wakapeana mikono na Mick.Mick akaondoka huku akionekana kufikiria mambo kadhaa kichwani.
******;********************************************************************************************
"Nimefanyia utafiti ile barua uliyokuja nayo pamoja na barua pepe.Nikianza na barua.Imefanana na barua za makao makuu ya jeshi kwa asilimia kubwa sana.Asilimia chache zilizobaki kufika asilimia mia iko katika muhuri uliopigwa katika barua hii.Kama unavyoona, muhuri wa jeshi uko katika umbo la duara.Lakini nikifananisha na barua nyingine kutoka makao makuu ya jeshi, zinatofautiana kidogo katika kipenyo kwa milimita moja na nusu.Pia umbali kati ya herufi na herufi umetofautiana kwa umbali ambao haiwezekani kutambua kwa macho ya kawaida.Mimi mwenyewe nimeng'amua hayo baada ya kui'scan' katika kompyuta na kutumia programu maalum ya kompyuta inayoweza kupima vitu hivyo."
"Nimeitafiti barua pepe ambayo ilitumwa kwa mkuu wa kambi ya jeshi Mafinga.Nimetafiti pia na namba ya simu ambayo mkuu wa kambi ya JKT Mafinga anadai kuwa ilipigwa kutoka makao makuu ofisi ya C.D.F na katibu wake.Vyote hivyo,yaani barua pepe na simu vilitumika kuwasiliana kutokea eneo la ofisi za mamlaka ya mapato (TRA) Mbeya. Ninadhani mpigaji simu na mtumaji wa barua pepe hiyo alikuwa mtaalamu au aliwezeshwa na mtaalamu wa teknolojia ya habari na mawasiliano na inawezekana alitumia programu maalum kufanya mawasiliano hayo.Programu hiyo inamsaidia mtumiaji kuingilia mawasiliano ya mtu mwingine,na hivyo nadhani mawasiliano ya ofisi ya C.D.F yaliingiliwa. Nathubutu kusema mtaalam wa teknolojia aliyehusika kufanya haya yawezekana ni mtaalamu wa hali ya juu sana kuweza ku-'hack' hata mawasiliano ya taasisi kubwa kama ofisi ya mkuu wa majeshi".
"Kwa sababu hiyo ninaweza kuhitimisha kuwa mawasiliano hayo pamoja na barua ile ni feki na wala hazihusiani na ofisi ya C.D.F."Alimaliza kuongea Clara.Wasikilizaji wake walikuwa ni ajenti Mick,mkurugenzi wa C.T.I, Maajenti wengine watatu wa C.T.I pamoja na mtu mmoja aliyekuja pamoja na mkurugenzi wa C.T.I ambaye wengine walikuwa bado hawajamfahamu.
"Kwanza naomba niwatambulishe mgeni wetu huyu. Kutokana na majukumu kuwa mengi, raisi wa jamhuri ya muungano wa Tanzania mheshimiwa George Katumba amemteua Josephat Moses kutoka idara ya usalama kitengo cha ulinzi wa rais,kuwa makamu mkurugenzi wa idara ya C.T.I. Sahani kwa kuwa mpaka wakati huu amekwisha kuhudhuria kikao chake cha kwanza ndani ya idara bila nyinyi kumgundua.Hii ni kwa sababu rais ameagiza aanze kazi mara moja."Aliongea mkurugenzi wa C.T.I na wanaidara waliokuwemo katika kikao hiki wakapiga makofi kama ishara ya kumkaribisha mgeni huyu.
"Lakini pia ,kutokana na alichokigundua Mick pamoja na maelezo haya ya ajenti Clara, basi ninadhani kuna umuhimu wa ajenti Mick na ajenti Clara kwenda kwenda huko Mbeya ofisi za mamlaka ya mapato TRA mkaanzie hapo.Wengine tutaendelea kutoa usaidizi kutokea hapahapa ofisini. Mtapata usaidizi wote mtakaouhitaji."Alimaliza kuongea mkurugenzi wa C.T.I.
Dakika ishirini baadaye,Ajenti Mick pamoja na Ajenti Clara walikuwa ndani ya helkopta iliyo na chapa ya polisi wakielekea Mbeya .
***************************************