Riwaya - Balaa

SIMULIZI.. BALAA
MWANDISHI.. HALFANI SUDY
Simu ...0757 633010

SEHEMU YA NANE

Bibi harusi, Nasra, alirushwa kwa kasi kule nyuma alikokuwa amekaa, na kupenya pale panapokaa kioo cha mbele ambapo sasa kulikuwa na uwazi tu, kioo kilikuwa kimeshavunjika na vioo vyote viliishia usoni kwa dereva na kwa Mzee Mpaukha. Kule nje alikotokea Nasra kichwa chake kilikutana na jiwe kubwa sana. Jiwe lile lilikipasua vibaya sana kichwa kile na kuweka ufa mkubwa. Damu zilikuwa zinatiririka! Nasra alikuwa anatoa muungurumo wa ajabu sana huku akitapika madonge makubwa ya damu mdomoni.

Mpambe wa bibi harusi, Hasina, kona kali iliyokata ile gari ilikata na yeye. Alijigonga vibaya sana pale dirishani, kiasi cha kukibobaza kioo kile kigumu cha gari. Pigo la nguvu katika kioo kile kiliondoka na fahamu zake. kiwiliwili chake kisicho na fahamu kilirushwa mbele na kujipigiza vibaya sana katika boneti ya gari ile na kudondoka chini kikiwa nyang'anyang'a.

Mama Mpaukha ambaye nae alikuwa amekaa siti za nyuma za gari lile. Yeye hakupata athari yoyote ya mwili. Mkanda aliokuwa ameufunga ulimsaidia vizuri wa gari ulimsaidia. Yeye hakurushwa kama wenzake, alibaki palepale katika kiti lakini akiwa hana uhai, bila shaka presha ilimpeleka kuzimu.

Ilikuwa ajari kubwa sana. Iliyoacha majeruhi wanne na kuondoka na roho ya mtu mmoja, mama Mpaukha.
Ajari ilitokea usiku wa manane, na kusababisha msaada uchelewe sana kufika eneo lile. Eneo lote la ajari lilikuwa linanuka damu !

Mwanasheria, ni jina la utani la mlevi maarufu sana katika wilaya ya Kilwa. Hakuna mtu aliyekuwa analijua jina lake halisi. Watu wote walimtambua kwa jina la mwanasheria.
Walimwita mwanasheria kutokana na uongeaji wake uliopita kiasi anapokuwa amekunywa pombe. Akishalewa hujifanya anajua kila kitu, anaelewa kila kitu, yeye ndiye huwa muongeaji mkuu baada ya kunywa pombe chafu.
Ni kiongozi gani ndani ya Kilwa asiyemjua mwanasheria? Alikuwa na namba za viongozi wote kuthibitisha uanasheria wake.

Tarehe ile ya sherehe ya harusi ya Dokta Yusha, mwanasheria alikuwa kilabuni akipata ulabu. Saa tisa ya usiku alihisi pombe zilimtosha. Alirudi nyumbani kwake kwa mwendo wa kupepesuka, huku akiimba nyimbo zisizoeleweka kwa sauti kubwa, na kutupia tusi moja moja hapa na pale, kama ilivyo kawaida ya walevi.
Mwanasheria alifika pale konani, kona iliyomshinda dereva Musa muda mfupi uliopita. Alijitahidi kujikaza ili atembee bila kupepesuka, alishindwa. Kona ilimshinda kama ilivyomshinda dereva Musa, mlevi mwenzie.
Naye alipepesukia kwa nguvu na kuangukia kulekule kwenye mtaro, lilikoingia gari la Mzee Mpaukha muda mfupi uliopita..

ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA
 
SIMULIZI.... BALAA
MWANDISHI...HALFANI SUDY

SEHEMU YA TISA.

Lile anguko la Mwanasheria lilimpeleka moja kwa moja kule kwenye kibonde kidogo lilipoingia gari la Mzee Mpaukha, na kujikuta ameulalia mwili wa mpambe wa Bi harusi,
Hasina Omary.
"Mamaaaaaa"
Mwanasheria alipiga kelele kali sana. Akiwa amemlalia Hasina, macho yake mbele yake alikutana na picha mbaya sana. Picha ya kutisha.

"Ni nini hii, inamaana tumekufa wote" Mwanasheria alijiuliza mwenyewe. Pombe haziongopi kabisa, Mwanasheria alijiona kama na yeye alikuwemo katika ile gari iliyopata ajari, na sasa watu wote wamekufa, akiwemo na yeye. Yalikuwa mambo ya ajabu sana.
Alijiinua taratibu toka katika mwili uliojeruhiwa vibaya sana, mwili wa Hasina, akasimama wima, huku akiwa anayumbayumba, Mwanasheria aliangalia vizuri eneo lote lile la ajari. Japo kwa shida kutokana na giza na kwa macho ya ulevi, lakini alitambua vizuri madhara makubwa yaliyotokea mahali pale.

"Ni nini hii?" Alijiuliza mwenyewe Mwanasheria. Mara akili zake za kilevi zilimtuma kufanya kitu. Alitoa simu yake mkononi na kupiga simu, alipiga simu kwa Robert, alikuwa ni rafiki yake kipenz.

"Hallo Robert" Aliongea kwa sauti ya kilevi.
"Nambie Mwanasheria, mbona usiku sana" Robert aliongea kwa sauti iliyoonesha alikuwa anatoka usingizini.
"Tumepata ajari rafiki yangu"
"Ajari ?"
"Ndio wenzangu wote wamekufa nimebaki mimi peke yangu"
"Ulikuwa na kina nani"
"Siwajui"
Pombe zilimfanya Mwanasheria ajione kama naye alikuwemo katika ile ajari.
"Sehemu gani imetokea hiyo ajari?"
"Mtaroni"
"Come on Mwanasheria be serious"
"Kweli my friend"
"Ulikuwa unatoka wapi mwanasheria?"
"Kilabuni"

Robert alitoa msonyo mrefu na kukata simu. Akihisi Mwanasheria alikuwa katika maruweruwe yake baada ya kunywa pombe za kutosha.

Upande wa Mwanasheria, ulibaki na mshangao, kwanini rafiki yake kipenz Robert kamkatia simu wakati yeye anamueleza jambo muhimu na zito sana.
Mwanasheria alianza kupiga kelele, na maneno ajari na balaa yakisikika mara kwa mara katika kelele zake.
Majirani na lile eneo walisikia walisikia vizuri sana kilio kile cha Mwanasheria, lakini nani katika mji ule alikuwa hamjui Mwanasheria, nani angekithamini kilio cha mlevi yule, kila mtu alipuuzia kilio cha mlevi, Mwanasheria. Lakini Mwanasheria hakupuuza, alizidi kupiga kelele...

Kule hospitali Kivinje hali ya mviziano iliendelea. Baada ya Dokta Yusha kukaa pale kwa muda mrefu, bila simu yake kupigwa, bila kumuona aliyempigia simu, aliamua kuondoka. Huku kichwani alikuwa anawaza, atamwambia nini Nasra na kumuelewa, atawaambia nini wazazi wake. Alitoka nje na kumkuta dereva wa ile pikipiki amesinzia, alimuasha na kupanda.
Wakaondoka.
Wakati wanaondoka walipishana na gari moja lililoingia kwa kasi sana mle hospitali, almanusra liwagonge.
Walipofika Singino, simu ya Dokta Yusha iliita, kuangalia namba ni ya ile sauti ya kizee iliyompigia mwanzo...

ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA.
Maoni/ushauri 0757 633010
 
SIMULIZI... BALAA
MWANDISHI.. HALFANI SUDY

SEHEMU YA KUMI

Sasa, akawa anajishauri, apokee ama asipokee ile simu.
"Hebu simamisha pikipiki kidogo" Dokta Yusha alimwambia dereva wa pikipiki ile kwa sauti kubwa. Pikipiki ikasimamishwa.
Dr Yusha aliipokea simu ile na kuisikia sauti ileile ikimsisitiza aende Kivinje kumsaidia mgonjwa wake.
"Mbona nimetoka hapo hospitali muda huu?" Dokta Yusha aliuliza kwa sauti yenye kukereka.
"Tupo huku nyuma, karibu na jengo la kuhifadhia maiti"
"Sasa mbona nilipofika niliipiga hii simu ilikuwa haipatikani"
"Simu iliisha chaji, yaani hapa nimeilazimisha tu kuiwash..."
Simu ikakatika.
Dokta Yusha aliamini kweli, simu ya yule jamaa haikuwa na chaji, maana ndomana hata sasa ilizimika kutokana na tatizo hilo.
"Turudi hospitali" Alimuamuru yule dereva pikipiki. Yule kijana aligeuza pikipiki haraka, yeye alikuwa kazini, na aliamini ujira wake unaongezeka kila inavyoongezeka safari.

Kule Kivinje, Tano alikuwa hajafanikiwa Mpango wake, hadi Dokta Yusha anapanda pikipiki na kuondoka, hakuiona nafasi sahihi ya kumuua daktari yule kijana. Wakati Dokta Yusha anaondoka Tano alijishauri, amfate Dokta Yusha na kumuua njiani ama afanyaje. Mwishowe aliamua kumrudisha tena Dokta Yusha kwa kutumia ile simu. Na alifanikiwa, Dokta Yusha alikuwa njiani anarudi.
Tano alijificha nyuma ya jengo la kuhifadhia maiti la Hospitali ile, na kisu chake mkononi. Akisubiri kwa hamu ujio wa Dokta Yusha. Daktari wakiyeamini angekuwa kikwazo katika Mpango wao walioupanga usiku wa siku ile.

Muda mfupi baadae, Pikipiki aliyopanda Dokta Yusha iliwasiri pale Hospitali. Dokta Yusha alishuka kwenye ile pikipiki. Siyo kwa haraka sana kama mwanzo. Akawa anaelekea upande wa kushoto kilipo chumba cha kuhifadhia maiti cha Hospitali ile...

ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA
 
SIMULIZI... BALAA
MWANDISHI.. HALFANI SUDY

SEHEMU YA KUMI NA MOJA

Dokta Yusha alikaribia kabisa kile chumba cha kuhifadhia maiti.
Ghafla, alisikia kelele kali sana zikitoka kule mapokezi.
"Uwiiiiiiii, jamani tusaidieni, tumeamua vibaya saaaaana, tusaidieni, madaktariiiiii, tunakufaaaa...." Zilikuwa kelele kali sana. Kelele ambazo zilisababisha Dokta Yusha abadiri uelekeo. Toka kwenye kifo kurudi katika uhai. Dokta Yusha alitimka mbio kurudi kule mapokezi, alikosikia makelele ya mtu akiomba msaada. Alipofika pale alimtambua vizuri sana mpiga kelele, alikuwa Mwanasheria, mlevi maarufu sana Kilwa Masoko. Taratibu alianza kupunguza mwendo akijua Mwanasheria yupo katika makelele yake ya kawaida ya pombe. Lakini kadri ya alivyokuwa anamsogelea Mwanasheria, umakini wake uliongezeka.
Mwanasheria alitapakaa damu mwili mzima, huku kundi dogo la watu likiwa limemzunguka. Dokta Yusha alijitahidi kupenya kundi la watu wale na kumfikia mlevi yule.

"Vipi Mwanasheria?" Baada ya kumkaribia Dokta Yusha lilimtoka swali.
Mwanasheria alimwangalia Dokta Yusha na kumtambua.
"Tumepata ajari Dokta, sote tumekufa" Mwanasheria alitoa kauli iliyomchekesha kila mtu.
"Come down Mwanasheria, wewe hujafa"
"Nimekufa Dokta, nimekufaaaaaa" Alisema kwa sauti kubwa sana.
Dokta Yusha aliona pale hawawezi kuelewana.
"Hao wenzako wako wapi?"
"Wapo humo Dokta" Mwanasheria alisema huku akionesha kwa kidole chumba kulichokuwa karibu na pale walipokaa.
Kwa mwendo wa taratibu Dokta Yusha alielekea kule chumbani. Alikutaba na balaa.
Mwili wa kwanza kuuona ni wa rafiki yake kipenzi, mke wake kipenzi, Nasra. Alienda mbele ya mwili ule uliolazwa vibaya sakafuni na kuuinamia. Dokta Yusha aliona ufa mkubwa sana katika kichwa cha mpenzi wake , pale alipojigonga na jiwe baada ya ile ajari ya kizembe kutokea. Aligusa upande wa kushoto wa kifua cha Nasra, mapigo ya moyo yalikuwa yanapiga kwa mbali sana. Akajua kosa lolote litasababisha ampoteze mke wake.
Alinyanyuka taratibu, huku chozi likimdondoka na kuufata mwili wa pili, alikuwa ni mkwewe, mama Mpaukha. Hakuhitaji kumgusa sehemu yeyote kutambua kama mkwewe kipenz alikuwa amefariki. Aliusogelea mwili wa tatu, mwili wa Alex. Dereva wa Mzee Mpaukha. Alimuona na damu nyingi sana, huku mabaki ya vioo yakiwa yamebaki katika mwili ule. Ilikuwa ni picha mbaya sana kuiangalia. Akausogelea mwili wa nne, wa Hasina, mpambe wa bibi harusi. Aliona mbonyeo mkubwa katika upande wa kulia wa kichwa kile. Pale alipojigonga na kioo Wakati Musa alipojaribu kukata kona ile kali. Mwisho aliusogelea mwili wa Mzee Mpaukha, mwili ambao haukuwa na tofauti sana na mwili wa dereva Musa. Nao mahali ya vioo yalikuwepo katika mwili ule.
"Balaa" Dokta Yusha alijisemea mwenyewe.

ITAENDELEA MUNGU AKIPENDA
Maoni 0757 633010
 
SIMULIZI.... BALAA
MWANDISHI.. HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA KUMI NA MBILI

"Jamani tunakufaaa" sasa ndio alizisikia kelele za Mwanasheria kule mapokezi.
Dokta Yusha alitoka nje kumwangalia Mwanasheria alikuwa ameumia sehemu gani. Alimfikia Mwanasheria na kumkagua mwili mzima. Mwanasheria hakuwa na jeraha lolote zaidi ya zile damu zilizompakaa. Dokta Yusha akawaza labda Mwanasheria kaumia ndani kwa ndani. Wakati akimwangalia Mwanasheria ndipo alipomuona Fred kwa mbali, rafiki yake wa siku nyingi. Na ndiye alikuwa mpambe wake wa harusi siku ile.

"Vipi Fred"
"Ebana wameumia vibaya sana, afadhali nimekuona, nimewafata madaktari mpaka nyumbani kwao, hawapo, sijui wameenda wapi?"
"Kwani kilitokea nini Fred?" Dokta Yusha aliuliza kwa sauti yake yenye kwikwi.
"Mimi kanipigia simu huyo jamaa anayelia, muda mfupi tu nilipofika nyumbani kutoka kwenye sherehe, sijui hata namba yangu aliitoa wapi, yeye alikuwa analia tu, huku akisema wote wamekufa. Alinielekeza mahali ilipotokea ajari. Nilienda haraka kwa gari, na kukuta familia ya Nasra wamepata ajari mbaya sana ya gari aisee, majeruhi wako ndani huko" Fred alisema bila kujua kama Dokta Yusha kashaingia mle ndani na kujionea mwenyewe athari za ajari ile.

Kule nyuma ya chumba cha kuhifadhia maiti, Tano alikuwa anasubiri ujio wa Dokta Yusha. Alikuwa amejiandaa vema kumuua Dokta Yusha pindi atakapotokea tu. Alijibanza konani na kisu chake mkononi. Hakujua kabisa kuwa kwa wakati ule Dokta Yusha alikuwa amesahau kabisa habari ya simu ya mtu yule.
Tano alisubiri na kusubiri.

Alfajiri, mji wa Kilwa Masoko, waliamka na habari kuu mbili.
Habari ya kwanza ilikuwa ni kutokea kwa ajari katika kona inayoelekea mtaa wa Lumumba. Vijiwe vyote vinavyojadiri habari ngumu waliijadiri sana habari hiyo. Habari iliyohusisha ajari mbaya waliyoipata familia ya Mzee Mpaukha.

Habari ya pili ni kukimbia kwa bwana harusi katikati ya sherehe. Habari iliyopambwa na kusimuliwa vizuri sana na mafundi wa kusimulia. Tena wengine hawakuwepo hata katika ile sherehe yenyewe lakini ndio walikuwa wasimuliaji wakubwa. Vijiwe vyote vya waambea waliipa sana 'airtime ' habari hii ya bwana harusi kukimbia katikati ya sherehe kuliko habari ile ya ajari.. .

ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA
 
SIMULIZI... BALAA
MTUNZI ....HALFANI SUDY

SEHEMU YA KUMI NA TATU

Kule Kilwa Kivinje majeruhi wote sasa walikuwa wodini. Dokta Yusha alifanya kazi kubwa sana usiku ule. Yeye mwenyewe alifanya kila kitu kuhakikisha majeruhi wote wanapata huduma. Na ile maiti ya mama Nasra ilipelekwa katika chumba cha kuhifadhia maiti na kusubiri taratibu zingine za mazishi ziendelee.

Hadi Asubuhi, Dokta Mkuu wa hospitali ya Kinyonga, Zaidi Kilumba, Dokta Mkuu wa upasuaji Sharifa Juma, na Dokta anayesimamia chumba cha kuhifadhia maiti, Dokta tamaa Karimu walikuwa hawajawasiri kazini, na wala simu zao zilikuwa hazipatikani.
Hospitalini walikuwa wanafanya kazi manesi, wakishirikiana kwa ukaribu mkubwa na Dokta Yusha.

Hadi saa sita mchana, majeruhi wale wanne walikuwa hawajapata fahamu. Hali ilikuwa tete. Dokta Yusha alifanya kazi kama punda, huku akimshukuru Mungu kwa kuwa alikuwa na likizo kwa ajili ya mapumziko ya ndoa yake.
Madaktari wengine katika hospitali ile, hawakuwa na ari kabisa ya kufanya kazi.

Saa kumi na mbili jioni, kazi ya Dokta Yusha ilianza kuleta mafanikio. Mzee Mpaukha alirudiwa na fahamu. Alifumbua macho taratibu akiwa mbele ya nesi aliyekuwa karibu na kitanda chake.

"Niko wapi hapa?"
"Tulia baba, uko sehemu salama"

Nesi alimjibu huku akiweka vizuri dripu ya maji ilikuwa inaingia mwilini kwa Mzee Mpaukha.
Mzee Mpaukha, alifumba macho na kutafakari. Matukio yote yaliyotokea usiku uliopita yalijirudia mithili ya sinema. Tangu wakiwa ukumbini hadi gari lao lilivyoacha njia.

"Tunakufaaaaaaa!"

Mzee Mpaukha alitoa ukelele mkubwa akiwa pale kitandani. Ukelele huo uliokuwa na faida ndani yake. Ukelele ule alifika moja kwa moja katika masikio ya Musa, na kumuamsha Musa, dereva wake, toka katika usingizi mzito aliolala kuja duniani. Musa naye aliunga kumsaidia Mzee Mpaukha

".....kufaaaaaaa"
Nesi sasa akakimbia kwa kasi kwenda katika kitanda cha Musa. Huku akimshukuru Mungu kwa kuweza kuwaamsha wagonjwa wawili kwa mpigo, tena katika njia ya ajabu.

Nusu saa baadae, Dokta Yusha aliwasiri, alipatwa na furaha isiyo na kifani kukuta wagonjwa wake wawili wamerejewa na fahamu. Ilikuwa faraja kubwa sana kwake. Asilimia hamsini ya kazi alikuwa amefanikiwa. Walipoteza fahamu wagonjwa wanne, wawili walikuwa wamerejewa na fahamu zao na kubaki wawili...

ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA.
 
SIMULIZI...BALAA
MWANDISHI.. HALFANI SUDY
SIMU.... 0757 633010

SEHEMU YA KUMI NA NNE

TANO, baada ya kushindwa mpango wake wa kumuua Dokta Yusha usiku ule. Alirudi mafichoni kwa wenzake kujipanga upya. Usiku wa siku uliofuata kundi lile hatari la SIX KILLERS walikuwa na kazi kuu mbili.

Kwanza Kuhakikisha utoaji wa mioyo kwa maiti zilizokuwepo katika chumba cha kuhifadhia maiti unafanyika bila wasiwasi wowote.

Pia kuhakisha Dokta kijana anayejifanya ana morali ya kazi, Dokta Yusha anauwawa.
Kwa kushirikiana na wale madokta wasiokuwa na maadili ya kazi waliamini watafanikiwa katika malengo yao hayo mawili.

Jioni ya siku ile familia ya Dokta Yusha, ilikwenda hospitali kuwaangaalia wenzao. Yalikuwa majonzi makubwa sana baada ya kusikia mama Mpaukha alikuwa amefariki. Na ndugu wengine wa Mzee Mpaukha nao waliwasiri, na waliamua kuuchukua mwili wa mpendwa wao usiku wa siku ile ili kwenda kufanya maandalizi ya mazishi.

Hadi muda huo, madaktari wakuu katika hospitali hiyo walikuwa hawajulikani walipo. Nia yao ilikuwa ni kukaa mafichoni muda mrefu ili idadi ya watu watakaofariki waongezeke, ili mradi wao wa kupata mioyo kumi na tano kila siku ukamilike. Walijua wasipokuwa kazini wao, wagonjwa wengi watakufa.

Saa nne kamili usiku, mganga Mkuu wa hospitali ya wilaya ya Kilwa, ndugu Zaidi Kilumba, Daktari Mkuu wa upasuaji Dokta Sharifa Juma, Mkuu wa chumba cha upasuaji, Dokta Tamaa Karimu, wale manesi watano, na kundi zima la SIX KILLER waliwasiri katika eneo la hospitali ile, kwa magari aina mbili tofauti. Madokta na manesi walipanda gari yao na lile kundi hatari walipanda gari yao. Walitofautiana kufika eneo la hospitali kwa dakika kumi tu, wakitangulia wale madaktari. Walikuwa wamekuja kufanya kazi ya kutoa mioyo ya maiti, wakifuatiwa na gari la kundi la hatari la Six Killers waliokuja kulinda hali ya usalama pale hospitali, na kumuua daktari aliyeonekana kizuizi kwa kazi yao, Dokta Yusha....

ITAENDELEA MUNGU AKIPENDA
 
SIMULIZI....... BALAA
MWANDISHI..HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA KUMI NA TANO

Wale madaktari waliposhuka tu pale hospitali, walilakiwa kwa furaha na bashasha kubwa sana toka kwa Dokta Yusha. Lakini wao hawakuonesha kabisa sura za furaha, haikuwa kama ilivyo kawaida yao kila walipokuwa wanakutana hapo kabla. Madaktari wale walionesha sura zilizoonesha dharau na kiburi.
Madaktari wote watatu walikataa kushikana mkono na Dokta Yusha wakati wa kusalimiana ! Waliuacha mkono wa Dokta Yusha ukielea hewani.

"Hivi wewe hiki ni kituo chako cha kazi, au unataka kutuaminisha kwamba wanaopanga vituo hawana akili?" Dokta Sharifa alimuuliza swali kwa dharau Dokta Yusha.
Dokta Yusha hakujibu swali lile, alitumbua macho kuonesha mshangao wake. Aliwaangalia kwa zamu madaktari wale. Wote walionesha kutojari kabisa mshangao wake.
"Au unahamu.....?" Dokta Kilumba nae aliuliza swali lililoelea hewani, bila kutanabaisha Dokta Yusha alikuwa na hamu ya nini.
"Mbona siwaelewi ndugu zangu" Dokta Yusha aliongea kwa sauti ndogo iliyokuwa ikiashiria kutoelewa kinachoendelea.
"Naitwa Tamaa Karimu, unaitwa Yusuph Shaweji, sina undugu na wewe na wala sijawahi kuwa na undugu Na wewe, labda hawa wenzangu ndio ndugu zako"
"Nani, mimi nitakuwa na ndugu kama huyo?" Dokta Sharifa alirukia kwa mtindo wa swali.
"Lazima niwe makini, kuna kitu kinaendelea" Dokta Yusha alijionya mwenyewe kimoyomoyo.

Wakati wanaongea na Dokta Yusha, lile kundi la wauaji walikuwa wamejipanga vizuri kule katika chumba cha kuhifadhia maiti. Tayari kwa kulinda usalama ili wale madaktari waje kufanya mchezo wao hatari. Mchezo wa kutoa mioyo ya maiti ! Pale walikuwa wanamchanganya tu Dokta Yusha ili kupoteza umakini wake, na kuwapa nafasi kundi la Six killers wajipange vizuri kule katika chumba cha kuhifadhia maiti.
Na walifanikiwa !

ITAENDELEA MUNGU AKIPENDA.
 
SIMULIZI...BALAA
MWANDISHI.. HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA KUMI NA SITA

Usiku uleule wa saa nne, familia ya Mzee Mpaukha walijipanga kwenda kuchukua mwili wa mpendwa wao kule chumba cha kuhifadhia maiti. Walikuwa wanamsubiri Dokta Yusha tu ili waende kuchukua mwili wa marehemu. Walikuwa wameshaongea na Mkuu msaidizi wa mhifadhi wa chumba cha maiti. Bila kujua Mpango hasi uliokuwemo katika chumba kile.....Balaa !

Alivyotoka kuongea na madaktari wale waliombadirikia, Dokta Yusha moja kwa moja alienda wodini. Hali aliyoiacha wodini ndiyo aliyoikuta. Hadi muda ule. Ni Mussa na Mzee Mpaukha tu ndio waliorejewa na fahamu. Dokta Yusha alisogea hadi kitanda alicholazwa mke wake kipenz, Nasra, alikaa pembeni ya kitanda kile. Huku akimwangalia mkewe aliyekuwa amefumba macho. Akiwa amehama kabisa katika Dunia hii. Mwanamke aliyekuwa nusu mfu kwa sasa. Aliangalia jinsi dripu ikivyotiririka taratibu katika mishipa laini ya Nasra.

Wakati Dokta Yusha akiwa pale na mkewe, Dokta Kilumba aliingia mle wodini. Alisogea taratibu hadi pale kitandani alipokuwa amekaa Dokta Yusha. Taratibu Dokta Yusha aliacha kuiangalia ile dripu na kumwangalia Dokta Kilumba. Dokta waliyetoka kugombana naye punde tu kule nje.
Dokta Kilumba alipofika pale naye hakuongea. Alikaa pale kitandani, karibu kabisa na Dokta Yusha, kiasi kwamba magoti yao yaligusana. Hali ya ukimya iliendelea kama dakika tatu, ndipo Dokta Yusha alikiharibu kimya hiko.

"Vipi Dokta, mbona umekuja kimya kimya halafu hauongei ?"
"Tusamehe Dokta, haikuwa dhamira yetu hali ile itokee"
"Msijari mambo ya kawaida tu kupishana kauli"

Baadae walielewana. Na kuanza kuongea mambo mbalimbali.
Dokta Kilumba alikuja kuongea na Dokta Yusha kwa dhamira maalum. Dhamira mbaya kabisa. Ni kuchelewasha muda kwa Dokta Yusha kwenda kule chumba cha kuhifadhia maiti kuchukua maiti ya mama Mpaukha. Kwa kuwa na maiti ya mama Mpaukha ilikuwa katika orodha ya maiti zilozotakiwa kutolewa moyo siku ile !

ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA.
Maoni/ ushauri 0757 633010
Samahani jana nilikuwa mbali na mtandao ndio maana nimeeka 4 kabisa
 
SIMULIZI; BALAA
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU.. 0757 633010

SEHEMU YA KUMI NA SABA

Kule nje familia ya Mzee Mpaukha walikuwa wanamsubiri Dr Yusha atoke wodini kuangalia hali za wagonjwa, ili waende naye kwenda kuchukua maiti yao kule katika chumba cha kuhifadhia maiti.

Bila kujua lengo la Dokta Kilumba, Dokta Yusha aliendelea kuongea nae. Alifurahi sana kuelewana na daktari yule Mkuu, alijua itakuwa rahisi sana kuwasimamia wagonjwa wake kwa kuelewana na Dokta yule.

Kule katika chumba cha maiti hali ilikuwa ya kutisha. Ilihitaji mtu jasiri kuangalia kilichokuwa kinaendelea. Mioyo kumi na nne toka katika maiti kumi na nne ilikuwa imeshapatikana tayari, na kuhifadhiwa katika deli moja kubwa jekundu!
Sasa ilikuwa zamu ya kutolewa moyo wa kumi na tano, ili kukamilisha idadi yao ya siku ile. Kisha baada ya hapo wakachungulie katika akaunti zao kitaongezeka nini. Waliikumbuka sana ahadi ya Don Genge.

Hali ndani ya chumba cha kuhifadhia maiti ilikuwa ya utulivu sana. Kila mtu akifanya kazi yake kwa umakini mkubwa. Utafikiri walikuwa katika operesheni moja muhimu sana ya kuokoa maisha ya mtu. Kumbe walikuwa wanafanya vitendo vya kinyama sana!

Dokta Sharifa alikuwa ameshika kisu maalum kwa ajili ya upasuaji, mbele yake kulikuwa na kitanda kidogo kikichotumika kulaza zile maiti wakizozitoa mioyo!

Dokta Sharifa alikuwa anapasua maiti na kutoa moyo kisha kuishona tena miili ya marehemu. Wale manesi walikuwa wanafanya kazi ya kubeba maiti na kuzileta pale kitandani, kisha kuzirejesha katika sehemu zao baada ya kufanyiwa upasuaji na kushonwa na Dokta Sharifa. Dokta wa kike katili !

Dokta Tamaa yeye alikuwa anasimamia kazi kama inaenda vizuri, ndiye alikuwa Mkuu kwa muda ule, wakati Dokta Kilumba hakuwepo.

Nje kulikuwa na ulinzi imara. Walinzi wote sita wakiwa na bunduki, walikuwa wamekizunguka chumba cha kuhifadhia maiti , tayari kwa kupiga mtu au kitu chochote kitakachosogelea chumba kile. Walikuwa makini, Kuhakikisha hawafanyi kosa lolote la kiufundi.

Manesi wawili walienda kufungua kabati moja la kuhifadhia maiti. Walivuta droo taratibu. Sura ya maiti yule ilikuwa inaonekana vizuri. Sura tulivu kabisa, sura ya kipole, sura isiyokuwa na hatia yoyote, sura ya mama Mpaukha. Wale manesi wawili waliitoa maiti ile na kuilaza vizuri kwenye machela. Waliisukuma machela ile kuelekea pale alipokuwa Dokta Sharifa, ili Dokta afanye kazi ile ya kikatili !
Kazi ya kuutoa moyo mwili ule, mwili wa mkwe wa Dokta Yusha..

Je watafanikiwa?

ITAENDELEA MUNGU AKIPENDA.
 
SIMULIZI; BALAA
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA KUMI NA NANE

Mwili wa mama Mpaukha ukawekwa katika kile kitanda maalum kwa kazi hii ya kikatili!
Dokta Sharifa alinyanyua mkono wake wa kulia ulioshika kisu juu, akakielekeza kile kisu katika upande wa kushoto katika kifua laini cha marehemu mama Mpaukha, akichana taratibu.

Kilikuwa ni kitendo cha kikatili sana, lakini daktari yule wa kike alikuwa anakifanya bila wasiwasi wowote. Alikizungusha kile kile kisu kwa mtindo wa duara, kisu maalum kilichokuwa kimezama vizuri katika nyama za kifua cha mama yule. Alipoona imetosha aliingiza mkono wake wa kulia, aliokuwa amevaa gloves, alichezesha mkono wake kama dakika moja katika shimo baya alilolijenga pale kifuani, na kutoka na moyo uliozungukwa na damu!
Aliuweka pembeni kwenye sahani ya chuma moyo ule, na kuanza kuushona mwili ule, mwili usiokuwa na moyo kwa sasa.

Kule wodini 'story' zilinoga kati ya Dokta Yusha na Dokta Kilumba. Walikuwa wanasimuliana mambo mbalimbali kuhusu fani yao ya utabibu. Bila kujua mambo ya siri yaliyokuwa wanaendelea katika chumba cha kuhifadhia maiti.

Mara, mjomba wake Nasra aliingia wodini.
"Samahani Dokta, inabidi tukautoe mwili wa marehemu ili tukaufanyie maandalizi"
"Sawa, ngoja tumpigie mtu wa chumba cha kuhifadhia maiti" Dokta Kilumba alidakia ilihal hakuambiwa yeye.
Alimpigia Dokta Tamaa, na Dokta Tamaa alimjibu kwamba mambo yako vizuri wakauchukue tu mwili mpendwa wao.

Dokta Yusha akiongozana na ndugu mwengine walienda kuuchukua mwili ule usiokuwa na moyo kwa sasa na kwenda nao Kilwa Masoko kwa ajili ya maandilizi ili wauzike.

Siku ile ya kwanza kundi la Don Genge kwa kishirikiana na madaktari wale wenye roho mbaya kabisa walifanikisha Mpango wao ule wa kinyama!

Siku ya pili Asubuhi, ndio ilikuwa siku ya kuuosha mwili ule tayari kwa kwenda kuuzika. Mshono waliukuta katika kifua cha mama Mpaukha ulimshangaza kila mtu aliyekuwa mle chumbani wakati wanauosha mwili ule....

ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA.
 
SIMULIZI; BALAA
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA KUMI NA TISA

Wakati mwili unaoshwa, kizaaza kikaibuka!
Mwili wa mama Mpaukha ulikuwa na mshono mkubwa sana ambao ulikuwa haujapona bado.
Mshono uliowaacha midomo wazi waoshaji. Pamoja na mshangao wao lakini waoshaji wale walihisi labda jeraha lile ni mojawapo ya madhara aliyoyapata mama yule katika ajari ile mbaya!
Wakina mama wale Waliamua kukaa kimya na kuendelea na kazi yao ya uoshaji kama kawaida.
Mwili wa mama Mpaukha ulioshwa na kwenda kuzikwa katika makaburi ya Sanga bila uwepo wa mwanae mpendwa, Nasra, bila uwepo wa mumewe kipenzi, Mzee Mpaukha .

Mama Kindumba, alikuwa mlevi maarufu wa kike katika mji wa Kilwa Masoko. Kutokana na kupenda sana kunywa pombe za kienyeji alikuwa na marafiki wengi sana walevi, miongoni mwa marafiki ni Mwanasheria.

Mama kindumba alikuwa anakaa jirani sana na familia ya Mzee Mpaukha. Ujirani huo ndio uliosababisha na yeye apate fursa ya kwenda kuuosha mwili wa mama Mpaukha. Na Mama kindumba ni miongoni mwa watu waliostushwa sana na ule mshono wa mama Mpaukha ulikuwepo pale kifuani.

Baada ya kumzika mama Mpaukha, jioni ya siku ile mama kindumba ilimkuta kilabuni akipata pombe za kienyeji kama kawaida yake. Kikao kilikuwa kimependeza ingawa mwenyekiti wa kikao hiko alikuwa hajawasiri bado.
Baada ya muda mfupi Mwenyekiti aliwasiri huku akiimba wimbo wa bendi ya msondo ngoma. Alikuwa Mwanasheria.

"Eeeeeeh nilikuwa nakusubiri kwa hamu Mwana" mama kindumba aliongea kwa nguvu baada ya kumuona Mwanasheria.
"Kuna nini tena mama kindumba maana nawe huishiwi michapo"
"Ni kuhusu ile ajari yenu" mama kindumba alisema huku anacheka.
"Umeanza kuharibu sasa" sauti ya Mwanasheria ilipoa kidogo.
"Kumbe yule maza alipata bonge la jeraha kifuani. Alichomwa na chuma nini pale"
"Mama gani tena?" Mwanasheria alihoji.
"Si jirani yangu tuliomzika leo kule Sanga"
"Acha zako mama, ushalewa nini, yule mama hakuumia sehemu yoyote. Alikufa bila jeraha"
"We si ulilewa Mwanasheria utakuwa na kumbukumbu kweli, maza alikuwa na jeraha kubwa sana kifuani"
"Hamna kitu kama hicho mama"

Ulizuka mbishano mkubwa sana kati ya mama Kindumba na Mwanasheria. Walevi wengine walibaki kuwa wasikilizaji tu.

"Tusiandikie mate, ngoja nimpigie Dokta Yusha tumuulize, halafu naweka sauti ya nje kabisa" Baada ya mzozo mkubwa Mwanasheria alishauri.

"Simu inapigwa, itakayozua kizaazaa kipya" tusubiri hiyo kesho tuone!"

ITAENDELEA MUNGU AKIPENDA.
 
SIMULIZI; BALAA
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA ISHIRINI

Mwanasheria akatoa simu yake. Akabofyabofya muda mfupi kuitafuta namba ya Dokta Yusha, aliiona na kuipiga.

Wakati simu ile inapigwa, Dokta Yusha alikuwa wodini. Akiwahudumia wagonjwa mbalimbali, wakiwemo mkewe Nasra na na rafiki wa Nasra, Hasina. Mzee Mpaukha na Musa hali zao sasa zilikuwa vizuri sana.

Akiwa amekaa pembeni ya kitanda cha mkewe simu yake iliita. Kuangalia kioo cha simu yake kilisomeka Mwanasheria, alitabasamu. Alitoka nje na tabasamu lake, alikumbuka vizuri sana vituko vya Mwanasheria. Alitoka nje ya geti ili akaongee na Mwanasheria.

"Hallo"
"Dokta tuna ubishi hapa" Mwanasheria alianza kuongea bila hata salamu.
"Ubishi gani tena?"
"Eti katika ile ajari marehemu alikuwa na jeraha lolote?"
"Hapana, alifariki kwa mstuko tu"
"Aliumia kifuani doktaaaa" sauti ya mama kindumba ilisikika katika ile simu kwa sauti kubwa.
"Hapana, hakuumia!"
"Tafuta mtu yeyote aliyekuwepo wakati wa kuosha maiti atakwambia" Mama kindumba alisema.
Na simu ili katika. Bila shaka kwa kuisha salio ama chaji.
Dokta Yusha alichanganyikiwa sana.

Ingawa taarifa ile ilitoka kwa walevi lakini Dokta Yusha aliipa uzito unaostahili. Alipanga kuufatilia ukweli wa taarifa ile na kuujua ukweli wa taarifa hiyo ya kushangaza.

Tano wa kundi la Six killers bado alikuwa anafatilia nyendo za Dokta Yusha. Na nia yao ya kutaka kumuuwa Dokta Yusha bado ilikuwa palepale. Tano alikuwa anapata ugumu sana kwa kuwa Dokta Yusha alikuwa anakaa wodini muda wote. Wodi yenye wagonjwa muda wote, na kufanya kazi ya kumuua iwe ngumu sana.

Wakati Dokta Yusha akiongea na simu ile, Tano alikuwa hatua chache nyuma yake. Alisikia kila kitu alichoongea Dokta Yusha na Mwanasheria....alilishika kichwani jina la Mwanasheria.

"Mwanasheria anahitaji kuuwawa!" Alilipitisha katika kichwa chake.

ITAENDELEA MUNGU AKIPENDA.
 
SIMULIZI; BALAA
MWANDISHI; HALFANI SUDY
SIMU; 0757 633010

SEHEMU YA ISHIRINI NA MOJA

Kule kilabuni ubishi bado uliendelea. Huku Mwanasheria akiwa amepata nguvu na kuelekea kushinda. Ubishi sasa ulipata washiriki zaidi, walevi walianza kuchangia mada, huku walevi wengi wakimuunga mkono Mwanasheria.

Tano aliona mambo yao sasa yameanza kuingiwa na vijidudu vibaya. Na jukumu lake lilikuwa ni kuviondosha vijidudu vyote. Sasa naye Mwanasheria akaingia katika orodha ya kifo!

Baada ya kuongea na simu ile toka kwa Mwanasheria, Dokta Yusha alikuwa na mawazo mengi sana. Kwa uyakinifu mkubwa aliipima ile taarifa ya Mwanasheria. Akajua kuna kitu. Alikaa pale kitandani huku akiingalia bandeji kubwa aliyefungwa mkewe kichwani. Kichwa cha Nasra kiliathirika sana. Huku kukiwa na wasiwasi kama Nasra akiamka atarejewa na kumbukumbu zake.

Dokta Yusha alichukua simu yake na kuitafuta namba ya Shangazi yake Nasra. Alijua kwa vyovyote lazima alikuwepo wakati maiti ya mama Mpaukha inaoshwa. Aliiona namba na kuipiga huku akiwa anatoka nje ya wodi.

"Hallo Shangazi"
"Habari Dokta?"
"Safi kwema Shangazi"
"Tupo tu hivyohivyo"
"Kuna kitu nataka nikuulize Dokta"
"Kitu gani hiko Dokta"
"Ulikuwepo kati ya watu waliomuosha marehemu leo?"
"Ndio nilikuwepo"
"Eti marehemu alikuwa na jeraha lolote?"
"Tena kubwa sana kifuani, aisee bila shaka ndio litakuwa limesababisha kifo chake lile"
"Sehemu gani lilikuwepo"
"Juu ya kifua, sehemu unapokaa moyo!"

Mwili wa Dokta Yusha ulipigwa ganzi. Ni yeye ndiye aliyepima mapigo ya moyo ya mama Mpaukha, mara tu walipoingia katika chumba cha matibabu kabla ya mwili ule kupelekwa katika chumba cha kuhifadhia maiti.
Alikumbuka aliweka kifaa cha kupima mapigo ya moyo sehemu ileile unapokaa moyo. Hapakuwa hata na mchubuko. Iweje leo aambiwe kuna jeraha kubwa sana?

"Halo Dokta....Halloo...unanisikia?"
Shangazi wa Nasra alikuwa anaongea peke yake simuni. Ingawa Dokta Yusha aliweka simu sikioni lakini alikuwa mbali sana kimawazo, alikuwa hasikii chochote....

ITAENDELEA KESHO MUNGU AKIPENDA.
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…