Ripoti maalum sumu saba aina saba zatesa wananchi

p_prezdaa

JF-Expert Member
Apr 25, 2011
432
60
Ripoti Maalumu Sumu aina saba zatesa wananchi

Sunday, 26 August 2012 09:17


Nyamongo Claud Mshana
RIPOTI ya uchunguzi wa madhara ya sumu kwa wananchi wanaozunguka Mgodi wa North Mara, uliopo Nyamongo wilayani Tarime, imethibitisha kuwa wakazi wa maeneo ya jirani na Mgodi wa North Mara wameathiriwa na aina saba tofauti za kemikali. Uchunguzi wa Mwananchi Jumapili umebaini kuwa utafiti huo wa kisayansi uliofadhiliwa na Taasisi ya Norwegian Church Aid (NCA) umeainisha sumu zilizowaathiri wananchi hao kuwa ni Arsenic (As), Zinc (Zn), Antimony(Sb), Cadmium (Cd), Lead (Pb), Manganese (Mn), na Copper (Cu).
Wanasayansi hao ni kutoka Idara ya Biolojia katika Chuo Kikuu cha Oslo, wanasayansi kutoka Chuo Kikuu cha Sayansi ya Viumbe Hai, Norway na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo yenye kurasa 70 ambayo Mwananchi Jumapili imeiona nakala yake, shughuli za madini katika mgodi wa North Mara zilisababisha madhara kiafya kwa wakazi wa maeneo ya jirani.
Hata hivyo, matokeo utafiti huo yamekuja huku ikidaiwa kuwa wananchi wa Nyamongo wanaendelea kutumia maji yenye sumu kuzunguka mgodi huo, bila Serikali kuchukua hatua stahili kuwanusuru, hivyo kuendelea kuathirika.
Katibu Kiongozi
Hata hivyo Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue alipoulizwa kama Serikali inafahamu matokeo ya ripoti hiyo alisema: “ Wizara ya Nishati na Madini ndiyo yenye majibu.” Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Muhongo alipoulizwa alisema hilo ni suala linalohusu mazingira akitaka watafutwe wanaohusika na mazingira, huku akimtaka mwandishi asishupalie jambo moja miaka yote.
”Jambo hilo linawahusu watu wa mazingira, watafute wao ndiyo watakupa jibu. Lakini pia hatuwezi kuwa tunaongelea jambo moja miaka yote, lazima tuangalie na mambo mengine,” alisema Profesa Muhongo.
Mwananchi Jumapili lilimtafuta Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira), Dk Terezya Huvisa, ambaye alisema kuwa yupo safarini Kilombero na kutaka atafutwe Katibu Mkuu wa wizara hiyo kwa madai ndiye anayejua kuhusu taarifa zote zinazohusiana na wizara.
Ripoti ya Utafiti Utafiti huo ulifanywa kwa lengo la kuchunguza kama watu wanaoishi maeneo ya jirani na Mgodi wa North Mara ulibaini kuwa wananchi walipata madhara katika kiwango kikubwa kilichoweza kugundulika kupitia nywele, kucha na vipimo vya damu. Sampuli za nywele, kucha na damu zilichukuliwa kutoka kwa wanavijiji 63 wa vijiji vya Nyangoto, Kewanja, Matongo, Nyarwana, Nyakunguru, Weigita na Nkerege na matokeo yalikuwa yakilinganishwa na sampuli za baadhi ya watu walio nje ya maeneo hayo (Jiji la Dar es Salaam).
Utafiti huo ulibaini kuwapo kwa kiwango kikubwa cha kemikali za Arsenic, Manganise na Thorium katika sampuli za kucha kutoka kwa wanavijiji wa vijiji vya Tarime. Kwa mujibu wa matokeo ya utafiti huo, kemikali za Arsenic, Zinc, Cadmium, Copper na Thorium ziligundulika kuwapo kwa wingi katika sampuli za nywele, kucha na damu.
Kemikali za Arsenic ziligundulika pia kuwapo kwa wingi katika maji ya Mto Tighithe, kiwango ambacho ni kikubwa kuliko kiwango kilichokubaliwa na Shirika la Afya Duniani(WHO). Kiwango cha Arsenic kinachopaswa kuwapo kwenye maji ni kipimo cha 10 μg/L. Hata hivyo, kiwango kilichothibitika kuwapo kwenye maji hayo ni zaidi ya 50 μg/L (mara tano zaidi ya kiwango cha WHO). Athari za Arsenic Kwa mujibu wa wataalamu, kemikali za Arsenic huathiri mfumo wa vinasaba (DNA).
Athari nyingine ni kuwa na msongo mkubwa wa mawazo na kuharibu mfumo wa baadhi ya tezi na seli mwilini. Wanasayansi hao wanasema kuwa mtu aliyetumia maji au kitu chochote kilichochangamana na kemikali hizo, anakuwa katika hatari ya kupata saratani ya ngozi na kibofu, ambapo asilimia 20 ya watu waliofanyiwa uchunguzi huo, walionekana kuwa na kiwango kikubwa cha Arsenic katika kucha zao.
“Kuzidi kwa kemikali hiyo pia huweza kusababisha vidonda kwenye ngozi, kuzidi au kupungua kwa rangi ya asili ya ngozi, mabaka makubwa kwenye ngozi ya viganja vya mikono na kwenye nyayo za miguu,” inasema sehemu ya taarifa ya utafiti huo. Dalili za madhara ya kemikali hizo huweza kuonekana ndani ya miaka 8 hadi10 ya matumizi ya maji yaliyochanganyika na kemikali hiyo.
Wataalamu waliofanya uchunguzi huo wanabainisha kuwa wananchi katika Wilaya ya Tarime wameathirika kwa kiwango cha juu kabisa kwa kemikali hiyo ya Arsenic. Walibainisha kuwa kati ya watu 63 waliofanyiwa utafiti, 47 walibainika kuwa na vidonda kwenye ngozi, ambavyo wanaamini vimetokana na kemikali hiyo, huku wakitahadharisha kuwapo uwezekano wa madhara zaidi ya kiafya kutokana na kuwapo kwa kemikali hizo kwenye mwili wa binadamu.

Kemikali za sumu Mwezi Mei mwaka 2009 Serikali ilipokea taarifa ya uchafuzi wa Mto Tighite kutokana na kuvuja kwa maji yenye tindikali toka Mgodi wa North Mara. Baada ya Serikali kuthibitisha tukio hilo, hatua kadhaa zilichukuliwa ikiwa ni pamoja na kufanya tathmini ili kubaini athari za kiafya kwa binadamu na mifugo zilizotokana na matumizi ya maji ya Mto Tighite.
Julai 1, 2009, Serikali ilitoa Amri ya Zuio (Protection Order) kwa Menejimenti ya Mgodi iliyotengua kibali cha kumwaga maji yanayotoka mgodini kwenda kwenye Mto Tighite.
Julai 17 mwaka 2011 timu ya viongozi wa dini katika mkutano wao na wakazi wa Nyamongo kwenye ukumbi wa Hoteli ya Comfort, waliwaeleza wananchi hao kuwa ripoti ya uchunguzi wanayo na kwamba walitegemea kuikabidhi kwa Rais Kikwete hivi karibuni.

Akizungumza kwa niaba ya viongozi hao, Mary Mosha kutoka Interfeight iliyofanya kazi na Baraza la Makanisa Tanzania (CCT) alisema kuwa ripoti hiyo imebainisha mambo mengi ikiwa pamoja na madhara ya sumu kwenye nywele, kucha na madhara mengineyo.
 
haya sasa...watu wanaua watu wenzao huku kila kiongozi akikwepa kadri awezavyo!!!! hili ndo linchi letu chini ya kiranja wetu dhayi-fu!!
 
Back
Top Bottom