Rais Magufuli usitamani kuwa IGP tafadhali

dosari

Member
Oct 7, 2016
81
84
Rais wangu mpendwa, Dk John Magufuli, nilisikia kauli yako kuwa unatamani kuwa Inspekta Jenerali wa Jeshi la Polisi (IGP) Tanzania. Kiukweli Rais wangu sikufurahishwa na kauli yako.

Unajua Taifa la Tanzania limekuamini kuwa wewe ni Mkuu wa Nchi, Raia Namba Moja, Amiri Jeshi Mkuu, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa nafasi uliyopewa, hakuna kama wewe hapa nchini.

Rais wangu, kwa hii Katiba yetu iliyopo, inakufanya wewe kuwa sehemu ya Bunge, wewe ndiye unaliitisha na kulivunja. Tukienda kwenye Mahakama, Jaji Mkuu na wasaidizi wake wote unawateua wewe. Kimsingi wewe ndiye ‘baabkubwa’ wa mihimili yote.

Kama Amiri Jeshi Mkuu, maana yake vikosi vyote vya majeshi ya ulinzi na usalama vipo chini yako. Unaweza kuviamrisha vifanye kazi unayoona vinatakiwa vifanye kwa namna utakavyo.

Mpaka hapo itoshe kukuonesha kuwa nafasi ambayo umepewa na Watanzania wenzako, inakutambulisha kuwa mtu mwenye hadhi kubwa kwa nchi yako. Hakuna kazi yenye imani kubwa kwa nchi ambayo wananchi wanaweza kumwamini mwenzao kuliko hiyo ambayo sisi Watanzania wenzako tumekupa.

Sasa inakuwaje tena Rais wetu unatamani kuwa IGP? Ili ufanye nini? IGP ni msaidizi wako, jukumu lake ni kuwa kiongozi mkuu wa Jeshi la Polisi Tanzania. Rais wangu, wewe ndiye mwenye polisi kwa sasa, IGP yupo kukusaidia.

Kabla yako, juu ya IGP kuna Waziri wa Mambo ya Ndani, Waziri Mkuu, Makamu wa Rais kisha wewe hapo. Uache kuutamani u-Makamu wa Rais, u-Waziri Mkuu, u-Waziri wa Mambo ya Ndani mpaka u-IGP?

Hapa lazima tuseme ukweli Rais wangu, katika eneo hili hujatutendea haki. Sisi hatujakosea kukufanya wewe kuwa Rais wetu. Tumekuona unatosha kuongoza nchi. Na mchakato uliofanikisha kukuweka madarakani una hadhi ya iliyotukuka.

Kwa mfano, uliposema: “Natamani kuwa IGP!”

Halafu, IGP wetu, Ernest Mangu, angekujibu: “Tubadilishane!”

Sisi Watanzania tungekuwa wakali, maana kukupata wewe Rais wetu tulitumia gharama kubwa. Tulikuchagua kisha ukaapishwa na kukabidhiwa nchi. Narudia, wewe ulikabidhiwa nchi. IGP wetu alikabidhiwa Jeshi la Polisi Tanzania.

Tafsiri ya kukabidhiwa nchi maana yake umepewa jukumu la kuisimamia nchi na vilivyomo kwa kipindi husika. Hata IGP wewe ndiye unamsimamia.

Rais wangu, kwa nafasi yako, wewe unamteua IGP kushika madaraka yake. Unamteua Mkuu wa Jeshi la Wananchi (JWTZ) na wakuu majeshi wote. Hauishii hapo, unateua mpaka wasaidizi wao. Tukupe nini zaidi ya hayo kiongozi wetu mpendwa?

Kwamba IGP hana mamlaka hata ya kumteua Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DCI). Mkuu wa JWTZ (CDF), hana mamlaka hata ya kumteua Mnadhimu Mkuu wa JWTZ. Wewe ndiye unawateulia.

Rais wangu ninayekupenda, wewe hapo unateua Waziri Mkuu, yaani mtendaji mkuu wa shughuli za kila siku za Serikali kisha anapitishwa na Bunge. Na wakati wowote ukijiskia unaweza kumuweka pembeni.

Unateua mawazi na manaibu wao, makatibu wakuu wa wizara, Mwanasheria Mkuu (AG) wa Serikali, wakurugenzi wa mamlaka zote za Serikali, wakuu wa mikoa, makatibu tawala wa mikoa, wakuu wa wilaya, makatibu tawala wa wilaya na kadhalika.

Sasa Rais wangu, unatamani u-IGP wa nini? Mimi nikuombe tu, endelea kuongoza nchi. Wewe unaongoza taifa zima, IGP ni wa polisi tu. Angalia watu ambao wewe unawateua, halafu mtazame IGP, yeye huteua tu makamanda wa polisi wa mikoa na vyeo vingine wa kipolisi.

Hivyo, nakuomba baba tuendeshee nchi yetu. Dhamana hii tumekupa kwa imani kubwa. Yakubali mamlaka yako na uyaishi kwa unyenyekevu kisha Mungu atakubariki na kukusimamia kila siku. IGP wetu Mangu, mwache aongoze polisi.

MAJESHI YOTE YAFANANE

Rais wangu mpenzi Magufuli, siku hiyohiyo uliposema unatamani kuwa IGP, ulionesha kukasirishwa na watu waliojitokeza Kituo Kikuu cha Polisi (Central), Dar es Salaam, kuwasindikiza ndugu zao.

Tafsiri; ulikasirishwa na waumini wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, waliomiminika kituoni kumfuata Askofu wao, Josephat Gwajima kisha kuimba mapambio eno la polisi. Hukufurahishwa na waliojitokeza kwa ajili Mwenyekiti wa Klabu ya Yanga, Yusuf Manji, kisha wakafuta vumbi gari lake kituoni.

Manji na Gwajima, walifika polisi kutii wito wa Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, aliyewaita pamoja na watu wengine 63, kwa ajili ya kuhojiwa kuhusika kwao na biashara ya dawa za kulevya nchini.

Rais wangu Magufuli, ulimwambia Kamishna wa Polisi, Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Simon Siro kuwa siku nyingine watu hao wanapojitokeza polisi na wenyewe wawekwe ndani.

Ulimuuliza Mkuu wa JWTZ (CDF), Jenereli Venance Mabeyo kama angekuwa yeye, angekubali waumini wa Gwajima waende Kambi ya Jeshi, Lugalo kuimba? Jenerali Mabeyo alipojibu “Hapana”, ukasema: “Nataka hiyo hapana ya CDF iwe kwenye majeshi yote.”

Hiyo kauli kuwa majeshi yote yafanane ndiyo yenye tatizo Rais wangu. Haya majeshi yameundwa na sheria zake kila moja lina utaratibu wake wa kazi. Jicho la Polisi kwa raia haliwezi kufanana na JWTZ.

Hata kimafunzo, polisi wamefundishwa kuratibu ulinzi wa raia na mali zao, kulinda amani na kudhibiti uhalifu. Polisi ni rafiki wa raia wema. Rais mwema hatakiwi kuogopa kufika kituo cha polisi kwa sababu yoyote ile.

Tanzania siyo nchi ya amri za kipolisi (Police State) kama ilivyokuwa Dola ya Kisovieti kabla haijavunjika, jinsi Jeshi la KGB lilivyokuwa linawaweka roho juu wananchi, au Chile ya Karne ya 20 ya Augusto Pinochet. Tanzania imesikimikwa misingi ya uhuru na demokrasia.

Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 13, ibara ndogo ya 6 (b), inaeleza kuwa ni marufuku kwa mtu aliyeshitakiwa kwa kosa la jinai kutendewa kama mtu mwenye kosa hilo mpaka itakapothibitika kuwa anayo hatia ya kutenda kosa hilo.

Mtanzania uhuru wake umewekwa na unalindwa. Tanzania siyo Police State kama ilivyokuwa Afrika Kusini ya enzi za Makaburu ndiyo maana Katiba, Ibara ya 9 (h), imekataza vitisho. Kwamba Mtanzania hatakiwi kutishwa, anapaswa kuuhisi uhuru wake na ajivunie kuwa mtu huru ndani ya nchi yake.

Polisi wanafanya kazi ndani ya maisha ya raia. Na kwa masharti yaliyowekwa na Katiba yetu, mtu hawezi kujisikia woga wala aibu kumsindikiza ndugu yake mtuhumiwa wa kesi yoyote ya jinai polisi.

Kama ndugu huyo atatakiwa kushikiliwa basi anaweza kumwekea dhamana kama kosa na mazingira vinaruhusu. Mtanzania hatakiwi kuogopa kwenda polisi kama yeye ni raia mwema.

Mtanzania akiwaona polisi mtaani kwake hatakiwi kujificha, badala yake awafuate awaulize na awape ushirikiano. Polisi wanafanya kazi bora ya kulinda usalama wa raia. Walinzi wako wanakuja mtaani kwako unakimbia kwa sababu gani? Vinginevyo wewe siyo mtu mwema.

Polisi wanapokuja nyumbani kwako kukukamata, wakishakuonesha vitambulisho na kujiridhisha unaweza kuwakaribisha sebuleni kwa mazungumzo. Polisi na raia hawatakiwi kuchukuana kibabe, kupigana, kudhalilishana na kuumizana.

Nguvu za polisi zimefichwa. Wanazo na wamepewa mafunzo kwa ajili ya kupambana na wahalifu hatari. Polisi wanaruhusiwa kubeba silala. Hata hivyo, matumizi ya silaha hizo yamedhibitiwa.

Sheria ya Jeshi la Polisi na Huduma Saidizi (Sheria Kuu ya Polisi), kifungu cha 29 (1) katika vifungu vyake vidogo (a na b), inaeleza ni wakati gani polisi anatakiwa kutumia nguvu na silaha. Polisi atatumia silaha dhidi ya wahalifu wenye kutaka kutoroka, wanaojaribu kutorosha wenzao, wanaozuia wahalifu wasikamatwe.

Hata hivyo, kifungu cha 29 (2), sheria inatamka kuwa mamlaka hayo ya kutumia silaha kwa polisi ni ya nyongeza. Kwamba anapokuwa hana namna nyingine ya kufanya atalazimika kutumia silaha.

Ikitokea polisi wamemdhuru au kumuua raia kwa kipigo cha nguvu au silaha, sheria inataka uchunguzi ufanywe kuthibitisha uhalali wa matumizi ya nguvu uliofanyika. Inapobainika hakukuwa na ulazima wa kutumia nguvu, polisi hupaswa kuchukuliwa hatua za kisheria.

JWTZ DHIDI YA POLISI

Rais wangu Magufuli, JWTZ na Polisi hawatakiwi kufanana. Hiyo hapana ya CDF iendelee kama ilivyo lakini isiwepo kwa IGP.

JWTZ hawakamati raia kwa makosa mbalimbali ya kiraia, sasa hao waimba kwaya wa Kanisa la Ufufuo na Uzima wataenda vipi Lugalo? Ingekuwa JWTZ wanakamata raia, ndugu zao wangekuwa wanakwenda Lugalo, Kizuiani, au hata Ngome kuwaulizia.

JWTZ limeundwa likiwa na mamlaka kamili ya kutumia nguvu yenye kudhuru (deadly force), wakati Polisi mamlaka yake ya kutumia deadly force ni ya nyongeza na yamedhibitiwa. Rejea Sheria Kuu ya Polisi, kifungu cha 29 na vifungu vyake vidogo.

JWTZ wanailinda nchi dhidi ya hatari za kigeni. Polisi wanailida nchi dhidi uhalifu wa ndani. JWTZ wanapokuwa kazini kuilinda nchi hawahitaji ujamaa na mtu wa upande wa pili kuilinda nchi, Polisi wanapokuwa kazini wanahitaji ushirikiano wa raia ili kupambana na uhalifu.

JWTZ wakipita mitaani hapo wanapita tu, maana siyo ofisni kwao. Na ukiwakuta kwenye kambi zao inabidi kufuata amri zao. Ukiwakuta JWTZ mahali wameweka alama zao, inakubidi upokee maagizo yao. Zingatia; wamepewa mamlaka kamili ya kutumia deadly force.

JWTZ ili litumike ndani kwa ajili ya kudhibiti uhalifu fulani ni lazima kweli ionekane hakuna nguvu nyingine inayouweza uhalifu huo zaidi zaidi ya nguvu ya kijeshi. Na Rais lazima alitangazie taifa kisha kuliagiza jeshi kuingia kazini.

Mwaka 2014, katika sakata la Tokomeza Ujangili, tulishuhudia jeshi lilivyotumika kimakosa na madhara makubwa yalionekana kwa Watanzania. JWTZ siyo jeshi la kubembelezana na watu, siyo jeshi la kupambana na uhalifu, ni jeshi la kivita.

Polisi hupaswa kushughulika na raia kwa upole mpaka pale atakapolazimishwa kutumia nguvu. Polisi anapotafuta ushahidi, anaweza kumjua mhalifu lakini akawa anamzunguka ili kumtafutia ushahidi wa kumfikisha mahakamani.

Mzunguko huo ukiwepo Polisi, JWTZ hawazunguki, wanaponusa harufu ya adui hutakiwa kutumia deadly force bila kuchelewa. Wanamuwahi adui kabla hajasababisha madhara.

Polisi ofisi zao ni kwenye vituo vyao na mitaani raia wanapoishi. Polisi atakwenda mitaani na kuzungumza na watu anapokuwa anafuatilia taarifa za uhalifu, raia pia atakwenda kituoni kutoa taarifa za kuisaidia polisi.

Hivyo basi, huwezi kuwatenganisha polisi na watu. Na ili uhalifu udhibitiwe vizuri, milango ya Polisi inapaswa kuwa wazi kwa ajili ya raia wema kwenda kutoa ushirikiano.

Inapotokea mikusanyiko ya watu ambayo siyo halali, Polisi hutakiwa kwanza kutoa taarifa za kuwaambia watu hao watawanyike. Wakikaidi ndiyo nguvu ya kuwatawanya hutakiwa kutumika. Sheria inasema hivyo.

Haiwezekani umekuta mkusanyiko wa watu, hujazungumza nao chochote, unaanza kuwakamata na kuwaweka ndani. Kufanya hivyo ni kuvunja sheria.

Hivyo basi, waumini wa Gwajima na mashabiki wa Yanga waliomsindikiza mwenyekiti wao (Manji), kwa namna yoyote ile, kama uwepo wao Central ulikuwa unasababisha shughuli za kipolisi zisifanyike vizuri, walitakiwa kuambiwa watawanyike.

Polisi kwa misingi yake, imejengwa kuwa rafiki mzuri wa mwananchi ambaye havunji sheria. Ndiyo maana kikosi cha kutuliza ghasia (FFU), hakiingizwi kazini mpaka kuwe na sababu hasa ya kufanya hivyo.

Na kazi ya kwanza ya FFU ni kutawanya, ndiyo maana wanaweza kutumia mabomu ya machozi, maji ya kuwasha na nyenzo nyingine ambazo hazisababishi majeraha au kuua. Polisi yeyote anapompiga raia asiye na silaha ni kosa kisheria. Mtanzania haruhusiwi kupigwa hovyo wala kuteswa. Haki zake zimehifadhiwa.

Hivyo, Polisi ni mlinzi wa raia na mafanikio ya ulinzi huo yamo ndani ya maisha ya kila siku ya raia. JWTZ ni mlinzi wa raia ili asiingiliwe na adui kutoka nje na mafanikio ya ulinzi huo hayaingiliani na maisha ya kila siku ya raia.

Kwa mantiki hiyo, hapana ya CDF, Jenerali Mabeyo iendelee kubaki JWTZ kwenye kambi zao na mipakani. Hiyo hapana ya CDF hapaswi kuwa nayo IGP. Hayo ni majeshi mawili tofauti.

Ni kama Jeshi la Magereza, nalo lina kanuni zake za kulinda wafungwa na mahabusu wasitoroke. Huwezi kusema hapana ya Mkuu wa Jeshi la Magereza ifanane na ya IGP.

NAKUOMBEA RAIS WANGU

Baada ya hayo, binafsi nakuombea kwa Mungu Rais wangu ili uitende kazi ya nchi si kwa bidii na maono yako peke yake, bali kwa muongozo na baraka zake yeye aliye juu. Ni yeye aliyeiumba Tanzania miaka dahari iliyopita kisha akatufanya mimi na wewe tuiishi nchi hii adhimu.

Tunafahamu kuwa kazi ambayo tumekupa ni ngumu sana, maana kama taifa tunakuangalia kwa nafasi ya kwanza. Hata hivyo, usichoke, itende kazi na Mungu atakubariki.

Wewe ndiye mkuu katika nchi hii, kwa hiyo achana na vitu vidogo. Mambo kama ya waumini kuimba mapambio au mashabiki wa Yanga kufuta gari la Manji polisi yaache yashughulikiwe na wasaidizi wa IGP. Wewe ni mkubwa sana Rais wangu Magufuli.

Rais wangu usifanye majeshi yote yafanane na JWTZ, utawafanya Polisi wakose ufanisi kwenye kazi zao. Maana polisi wanawahitaji wananchi kwa ukaribu zaidi ili wafanikiwe kikazi.

Mwisho kabisa Rais wangu Nagufuli, wasaidizi wako wanatoa sana vitisho kwa raia, kazi kidogo vitisho vingi. Hili jambo limekatazwa na Katiba yetu. Wewe ndiye msimamizi mkuu wa nchi na mlinzi mkuu wa Katiba yetu, usikubali mwananchi wako ajione hayupo huru au akose amani.

Mungu akubariki sana Rais wangu, Dk John Magufuli.

Mungu Ibariki Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Ndimi Luqman MALOTO

Chanzo: luqmanmaloto
 
Dah ngoja nijitutumue tu kusema kwa kingereza .." You said it all "

Tatizo mbuzi kumpigia gitaa achezi labda tujaribu marimba anaweza akatingisha mzuzu
 
Kwenye Biblia hakuna kiongozi ambaye hakuwa ni mwanajeshi pia!

Uongozi umejaa ........

But hivi tunahitaji demokrasia kweli?

Real Democracy?

Tunatania!
 
Alisema kwa nia njema
Watu walikuwa wameanza kulidharau jeshi la polisi.
Mie niliipenda kauli ile
 
Back
Top Bottom