Pinda awapa angalizo wabunge

singidadodoma

JF-Expert Member
Nov 11, 2013
4,394
1,531
WAZIRI Mkuu mstaafu, Mizengo Pinda amewataka wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kujenga hoja vizuri katika Bunge linalotarajia kuanza vikao vyake wiki ijayo mjini Dodoma, kwa kuwa wabunge wa vyama vya upinzani wameongezeka bungeni.
Hayo yalisemwa jana Dar es Salaam na Pinda, baada ya kuaga mwili wa aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalumu, Leticia Nyerere, aliyefariki akiwa Maryland nchini Marekani akipatiwa matibabu.
Akizungumzia Bunge la sasa, Pinda aliwashauri wabunge wanaounda Bunge hilo ambao wengi wao ni vijana, kuzingatia maslahi ya taifa na sio itikadi za vyama vyao na kuwasisitiza wabunge wa CCM, kujipanga na kwenda na hoja.
“Kila upande ujiandae kwenye kuwasilisha hoja, kuna ongezeko la wabunge wa upinzani, sasa wabunge wa CCM ni lazima nao wajipange na kujenga hoja vizuri,” alisema Pinda. Alisema kwa mtazamo wake, Bunge ni zuri na sio la mivutano kwa kuwa kila mmoja amejipanga kuwasilisha hoja zitakazomgusa mwananchi kwa lengo la kumsaidia.
Akizungumzia utawala wa Awamu ya Tano wa Rais John Magufuli, Pinda alisema kila zama zina kitabu chake; na kwa utawala wa Rais Magufuli ameanza vizuri na kuomba Watanzania kumuunga mkono ili kufanikisha azma ya maendeleo ya taifa.
Alisema katika uongozi wake, ndio muda wa kuhakikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo inayoisha baada ya miaka 10 ijayo, inapaswa kuwa imetekelezwa, hivyo hatua mbalimbali anazozifanya rais, ikiwa ni pamoja na kubana matumizi, ni mambo muhimu.
“Hatua zinazofanywa na Rais Magufuli ni za msingi katika kuhakikisha dira ya Taifa ya Maendeleo inatekelezwa, ni vyema Watanzania wote tumuunge mkono juhudi zake”, alisema Waziri Mkuu mstaafu Pinda. Katika hatua nyingine, wabunge wa CCM wamepewa semina elekezi za namna ya kutekeleza ilani ya chama hicho.
Katibu wa Uenezi na Itikadi wa CCM, Nape Nnauye alisema hayo jana wakati akizungumzia kikao cha wabunge wa CCM, kilichofanyika kwa muda wa siku mbili. Alisema kikao hicho kilikuwa cha mashauriano juu ya wajibu wa mbunge wa CCM kwa jimbo na chama chake, kwani asilimia 68 ya wabunge ni wapya na wamefunzwa namna wabunge watakavyotekeleza Ilani ya CCM.
Pamoja na hayo, aliwataka waandishi wa habari wasiwe na mijadala yao kwani taarifa nyingi za magazeti wakati wa kikao hicho, zilikuwa za mitaani kwani mengi yaliyoripotiwa hayakujadiliwa kwenye semina elekezi. “Bora mngeniuliza kuliko kutafuta habari za mtaani, mengi ya yaliyoandikwa ni ya kutunga,” alisema Nape.
Wakati huo huo, vikao vya Kamati za Bunge vinaanza leo mjini Dodoma kwa Spika wa Bunge, Job Ndugai kutoa majina ya uteuzi wa wajumbe wa kamati. Atafanya hivyo kwa mujibu wa Kanuni za Bunge.
Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano cha Bunge, Owen Mwandumbya alisema kwa mujibu wa ratiba, leo kutakuwa na uteuzi wa Kamati za Kudumu za Bunge na kufuatiwa na uchaguzi wa Wenyeviti na Makamu wao na wajumbe wa kamati kuelezwa wajibu, kazi na mipaka ya kazi za kamati, kupokea na kujadili mpango kazi wa kamati unaoisha Juni 2016.
Mwandumbya alisema Januari 22 kutakuwa ni mkutano wa wabunge wote na mada zitakuwa ni kanuni za kudumu za Bunge na uendeshaji wa Bunge, nadharia ya mgawanyo wa madaraka katika mhimili wa dola, haki na kinga na madaraka ya bunge, mamlaka ya spika na bunge, kazi, wajibu na masharti ya mbunge.
Pia Januari 23 mkutano wa wabunge wote, utaendelea na mada zitakuwa pamoja na maadili na miiko ya wbaunge, nafasi ya mbunge katika usalama wa taifa na itifaki ya mbunge.
Jumapili kutakuwa na kikao cha Kamati ya Uongozi na Jumatatu Januari 25 ni maelezo ya wabunge wote kuhusu Mpango wa Taifa wa Miaka Mitano, unaokusudiwa kutekelezwa katika Jamhuri ya Muungano.
 
Back
Top Bottom