Pinda abaini madudu chuo kikuu Dodoma

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
268
WAZIRI Mkuu, Mizengo Pinda amekiri kuwa Chuo Kikuu cha Dodoma kina matatizo makubwa likiwemo suala la uongozi kwa baadhi ya vitengo.

Kutokana na kubaini hali hiyo, jana, Pinda alimuagiza Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), kufika mara moja chuoni hapo kwa ajili ya kufanya ukaguzi na kueleza kuwa mkaguzi tayari alikuwa njiani na kwamba kazi hiyo itaanza mara moja leo.

Mbali na hilo pia alijitwika mzigo pale alipoomba wahadhiri wa chuo hicho kumbebesha mzigo wa madeni yote, ambayo yalitokana na mapunjo waliyokuwa wakifanyiwa na kuwaahidi kuwa yote yatalipwa mwishoni mwa Februari mwaka huu.

Pinda alisema hayo jana alipokuwa akisikiliza matatizo na kero za wahadhiri wa chuo hicho, ambao waliingia katika mgomo tangu mwanzo mwa wiki iliyopita kutokana na madai mbalimbali yakiwemo fedha za kujikimu pamoja na makato ya mishahara yao yasiyo na maelezo.

Akiwa katika Jengo la Chimwaga, Pinda ambaye alipokewa na nyimbo kutoka kwa wahadhiri hao wakisema ni ‘mtoto wa mkulima’ na kwamba wangetegemea ukombozi kutoka mikononi mwake, hakuficha hisia zake na kusema wazi kuwa Udom ina matatizo makubwa likiwemo suala la uongozi.

Alisema kuwa yapo matatizo ndani ya chuo hicho ambayo hayakupaswa kuwepo hadi jana, lakini kutokana na uongozi uliopo kushindwa kuwashirikisha wanachuo pamoja na wahadhiri wao ndiyo maana yamefikia katika hatua hiyo.

Desemba 20 mwaka jana chuo hicho kiliingia katika mgogoro baada ya wanafunzi wa Kitivo cha Sayansi ya Jamii, kuitisha maandamano makubwa yaliyozimwa kwa mabomu ya polisi jambo lililowalazimu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa pamoja na Waziri wa Mambo ya Ndani, Shamsi Vuai Nahodha kufika chuoni hapo kwa ndege ya kukodi.

Hata hivyo moto wa wanachuo hao uliwashwa tena Jumatatu ya Januari 10 mwaka huu, baada ya wale wa Kitivo cha Elimu kuandamana ambapo katika maandamano hayo polisi walishindwa kuzima maandamano licha ya kupiga mabomu ya machozi, lakini walizidiwa mbinu za wanachuo hadi wakafika katika eneo lililokusudiwa.

Juzi pia wanachuo hao Kitivo cha Elimu walifanya kile kilichoonekana kama ni kiini macho baada ya kuteka gari la Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mjini, John Tupa kwa zaidi ya saa nne wakishinikiza kuonana na Waziri Mkuu bila ya mafanikio.

“Hapa nakiri kuwa kuna matatizo makubwa ikiwemo pamoja na uongozi, kwani sioni kwa nini mnashindwa kufanya mambo kwa kutumia ubunifu na mnaacha yanakuwa makubwa kiasi hiki? Hii inaonyesha kuwa mlishindwa kuwashirikisha kwa kila jambo watu mnaowaongoza na mkawa wasiri mno,” alisema Pinda.

Jana katika mazungumzo yao mbele ya Waziri Mkuu, wahadhiri walisema kuwa wamekuwa wakinyanyaswa kwa kipindi kirefu na Makamu Mkuu wa Chuo katika Idara ya Utawala na Fedha, Profesa Shaaban Mlacha ambaye walimtaka Waziri Mkuu kuondoka naye jana hiyo kwani walisema yeye ndiye chanzo cha kuibiwa fedha zao.

Wahadhiri hao walisema kuwa kumekuwa na wizi mkubwa ambao Udom hawajapata kuuona na umekuwa ni wizi wa hadharani, lakini kila wanapotaka kuhoji wanakutana na majibu ya ukatili kutoka kwa Mlacha.

"Kumekuwa na wizi mkubwa ambao katika maisha yangu sijapata kuuona na ninasema bila woga kuwa huyo Mlacha ndiyo chanzo cha migogoro yote mheshimiwa Waziri Mkuu na pamoja naye, lakini kuna viongozi hapa ambao hawaitakii mema nchi hii pamoja na chuo hiki kwa ujumla kama ni hivyo basi waondoke mara moja ama toa tamko wewe sisi tunalipwa lini,” alisema Mchungaji Dk Diana ambaye ni mmoja wa wahadhiri waliogoma.

Mhadhiri huyo alisema kuwa kila mara wanapofika kwa Mlacha wamekuwa wakikemewa kama mbwa jambo linalowapa woga hata wa kufuatilia madai yao mengine na kuwafanya kukosa ari ya kufanya kazi.

Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa Umoja wa Wahadhri hao (Udomasa), Iddy Mwerangi aliutaka uongozi wa chuo hicho kuwaomba radhi kutokana na taarifa zilizoripotiwa katika vyombo vya habari zikimnukuu Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Idrisa Kikula kwamba madai ya wahadhiri hao hayakuwa ya msingi.

Kutokana na kauli hiyo ilimlazimu Pinda kumsimamisha Profesa Kikula ambaye aliomba radhi mbele ya mkutano wa wahadhiri hao na wakapokea ombi lake kwa kumpigia makofi ishara ya kuwa wamemsamehe, lakini kila lilipotajwa jina la Mlacha walikuwa wakizomea na kumuita kondoo mweusi.

Pinda aliwataka kukubaliana na wazo lake la kumleta CAG kwa kile alichosema kuwa Kamati ya Makatibu aliyoituma chuoni hapo kabla, ilibaini mapungufu makubwa katika eneo la fedha na kwamba mtu pekee atakayeweza kumaliza hayo yote ni Mkaguzi Mkuu.

“Ninyi mnasema ni bora huyu Mlacha akubali kulipa madeni yenu pamoja na kujiuzulu ama niondoke naye, lakini bado inawezekana kuna na wengine la huyu niachieni nalipeleka kunakohusika, lakini lazima kwanza aje akaguliwe kuanzia kesho (leo) ili kujibu yale atakayotakiwa kufanya hivyo naomba mvumilie kwani mambo yameiva sasa,” alisema Pinda.

Alisema kuwa amempa muda wa wiki mbili mkaguzi huyo kuwa ametoa taarifa kwa usahihi ili wanaohusika waweze kuchukuliwa hatua stahiki huku akisisitiza kuwa wale ambao wana madai yao basi waandike kwa majina na kumkabidhi yeye Pinda ili naye ayawasilishwe Hazina.

Kwa upande wa wanachuo alisema kuwa alibaini mambo mengi pia ikiwemo suala la upungufu wa vifaa vya kujifunzia pamoja na chuo kuendesha mafunzo ya nadharia bila vitendo jambo alilosema kuwa ameliundia tume kwa ajili ya kulishughulikia.
 
tunamshukuru kwa hili ila mbona amechelewa sana kwenda kutatua huu mgogoro!!!pia tahadhari na wengine watagoma sasa hivi!!

WAZIRI Mkuu, Mizengo Pinda amesuluhisha mgogoro uliokuwepo baina ya uongozi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM) na wahadhiri wa chuo hicho kuhusu maslahi yao na wamekubali kuingia madarasani kuanzia leo.

Wahadhiri hao wamekubali kusitisha mgomo na kutoa sharti kuwa madai yao yawe yameshughulikiwa hadi ifikapo mwezi Februari mwaka huu.

Waziri Mkuu ataingia matatani iwapo serikali itashindwa kutekeleza ahadi hiyo, kwani wahadhiri hao wamemtahadharisha kuwa iwapo madai hayo hayatafanyiwa kazi katika kipindi hicho, wataitisha mgomo mkubwa ambao utakuwa mkali zaidi.

Vyanzo vya habari vya kuaminika vimeeleza kuwa serikali imekuwa na kawaida ya kuahirisha migomo na kero mbalimbali zinazotokea kwa ahadi ya kushughulikia, lakini utekelezaji wake umekuwa si wa uhakika.

Akizungumza na wanajumuiya ya wanataaluma wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOMASA) jana kwenye ukumbi wa Chimwaga, Pinda alisema matatizo yaliyojitokeza katika chuo hicho ni mlundikano wa mambo ambayo yamekuwepo siku nyingi, lakini mengi ni ya kiutendaji na yanaweza kuisha bila kupoteza muda mwingi.

"Nimeongea na viongozi wa UDOMASA na kuwaahidi kuwa madai yenu ya posho yanaweza kukamilika mwezi Februari, nilitaka yaishe mwezi huu lakini kwa taratibu za HAZINA sasa hivi wameshaanza kushughulikia mishahara ya Januari kwa hiyo marekebisho yenu hayawezi kuwahi…wameniahidi mwezi ujao yatakamilika," alisema huku akishangiliwa.

Alisema amemwagiza Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) aende kukagua taarifa za mahesabu ya chuo hicho ili kubaini tuhuma zilizojitokeza za watu kulipwa hundi mbili za mishahara, walioacha kazi kuendelea kuwemo kwenye malipo ya mishahara na wengine kukosekana kabisa.

"Taarifa nilizonazo ni kwamba CAG atakuwa hapa kesho… mpeni ushirikiano ili aifanye kazi kwa urahisi…, nia yetu ni kuangalia mfumo mzima wa fedha na utawala ukoje ili ikibidi uweze kurekebishwa," alisema.

Mbali na kusuluhisha mgogoro huo, Pinda alieleza kusikitishwa na uozo mkubwa na ufisadi unaofanywa na uongozi wa chuo hicho ambao umesababisha kutokea kwa mvutano mkubwa kati ya uongozi wa chuo na wahadhiri.

Katika mgogoro huo pia imebaini kuwa tatizo kubwa linatokana na uongozi wa chuo kushindwa kusimamia mipango ya malipo ya wahadhiri huku ikibainika kuwa wapo watumishi hewa ambao wamekuwa wakilipwa mishahara mara mbili.

Aidha, alisema kitendo cha watumishi kushindwa kulipwa mishahara mipya kutokana na waraka wa serikali ni ukiukwaji wa taratibu na kanuni za sheria serikalini na kinachotokea ni walimu kuendelea kulipwa mishahara ambayo haiendani na waraka huo.

Alisema kitendo cha kutowalipa watumishi hao mishahara ambayo inaendana na viwango vyao vya kazi ni ufisadi mkubwa ambao unafanyika kwa njia ya uonevu na kusababisha migogoro ambayo inaweza kuleta majanga makubwa katika jamii wanayofanya nayo kazi.

"Nasikitika kuona uongozi wa chuo umekuwa ukikata pesa za watumishi bila maelezo yoyote kwa watumishi hao na kujifanya miungu watu, jamani ninyi viongozi wa chuo kwa nini mnashindwa kufanya kazi na watumishi katika njia ya uwazi?" alihoji Pinda.

Mbali na hilo, Waziri Mkuu alieleza matatizo makubwa yanayotokea chuoni hapo yanasababishwa na uongozi wa chuo kutokuwa na ushirikiano mzuri na watumishi na zaidi umekuwa ukikiuka taratibu za ulipaji mishahara kwa watumishi kwa mujibu wa waraka wa serikali kutoka hazina.

Alisema kitu kingine ambacho kimekuwa sababisho kubwa la chuo kuingia katika migogoro ni kutokana na viongozi wa chuo kujifanya miungu watu kwa kutumia vibaya madaraka yao ikiwa ni pamoja na kushindwa kukaa meza moja na watumishi juu ya malalamiko yao.

Pamoja na juhudi za Pinda kutatua mgogoro huo uongozi wa umoja wa wahadhiri na wataaluma ulimtaka Kaimu Mkuu wa chuo, Profesa Idris Kikula, kuomba radhi kutokana na kutokuwatendea haki ikiwa ni pamoja na kutoa maneno ya kejeli kwa wahadhiri hao.

Akizungumza kwa niaba ya wahadhiri, Mwenyekiti wa UDOMASA, Paul Louisulie, alisema, Profesa Kikula, amekuwa akishindwa kutoa ushirikiano huku wakidai uongozi wa chuo umekuwa ukifanya kazi kwa mabavu.

Aidha, mwenyekiti huyo wa UDOMASA, alitoa tamko la kusitisha mgomo kwa sharti kuwa iwapo madai yao hayatafanyiwa kazi hadi Februari mwishoni wataitisha mgomo mkubwa ambao utakuwa mkali zaidi.

Kuhusu madai ya wanafunzi ya tatizo la maji, Pinda alisema amemwagiza Naibu Katibu Mkuu (Fedha), John Haule, afuatilie uhamisho wa ndani wa fedha (reallocation) katika Wizara ya Maji, ili zipatikane sh bilioni 1.66 zinazohitajiwa na Mamlaka ya Maji Safi na Majitaka Dodoma (DUWASA) kuchimba visima maeneo ya Ng'ong'ona na Ihumwa ikiwa ni pamoja na kutandaza mabomba hadi chuoni.

Alisema katika mipango ya muda mrefu, DUWASA pia wanatarajia kupata dola milioni 26 za Marekani ambazo zitatumika kuchimba visima vingine na kujenga matanki yenye uwezo wa kuhifadhi lita milioni 12 za maji, hivyo kuondoa kabisa tatizo la maji chuoni hapo.

Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa Idris Kikula, alimweleza Waziri Mkuu kwamba mahitaji halisi ya maji chuoni hapo ni lita milioni 3.5 kwa siku ambazo kati ya hizo, lita milioni 1.5 ni kwa matumizi ya wanafunzi peke yao na lita nyingine milioni 2 ni kwa matumizi ya ujenzi wa majengo unaoendelea chuoni hapo.

Akifunga mkutano huo, Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Prof. Idris Kikula, alimwahidi Waziri Mkuu kwamba maagizo yake yatafuatiliwa na kwamba leo menejimenti, idara ya uhasibu na UDOMASA watakutana ili kuunda timu ya pamoja ambayo itakaa na kubainisha stahili za walimu wote ili orodha hiyo iwasilishwe kwa Waziri Mkuu mapema iwezekanavyo kwa ufuatiliaji.

Wakati huohuo, Chama cha Wafanyakazi wa Taasisi ya Elimu ya Juu, Sayansi, Teknolojia, Habari na Utafiti (RAAWU), kimeipa serikali wiki tatu kulipa malimbikizo yote na mishahara mipya ya wafanyakazi wa umma hasa wa Elimu ya Juu, vinginevyo wataiburuza mahakamani.

Fedha zinazodaiwa ni kuanzia Julai hadi Oktoba, ambapo kuchelewa kwake kumesababishwa na serikali pamoja na kutowajibika kwa menejimenti za taasisi.

Onyo hilo limetolewa jana jijini Dar es Salaam na Katibu Mkuu wa Raawu, Adelgunda Mgaya, alipozungumza na waandishi wa habari.

"Kugoma kwa wahadhiri katika vyuo vikuu nchini ikiwemo Dodoma kumesababishwa na jeuri, umangimeza na uzembe katika kushughulikia haki zao kwa haraka na ufanisi unaofanywa na serikali.

"Raawu kwa mara nyingine tena tunaitaka serikali kukamilisha haraka zoezi la ulipaji wa mishahara mipya na malimbikizo yake na kuondoa kasoro zote zilizojitokeza ifikapo mwishoni mwa Januari.

"Pia haitasita kuwachukulia hatua za utetezi wanachama wake kulingana na sheria za kazi endapo malalamiko hayo hayatashughulikiwa na kumalizwa ndani ya kipindi cha kuanzia sasa hadi mwisho mwa Januari," alisema Adelgunda.

Alisema serikali itambue kuwa wafanyakazi wamekuwa wavumilivu kwa muda mrefu ingawaje uvumilivu unaelekea ukingoni.

Alisema Julai mwaka jana, serikali ilipandisha mishahara ya wafanyakazi wake viwango tofauti kulingana na maafikiano katika vikao vya majadiliano ya pamoja baina yake na vyama husika vya wafanyakazi.

Alifafanua kwa kawaida ulipaji huanza mara moja kwa watumishi wa serikali kuu na serikali za mitaa ambapo kwa taasisi za serikali huanza baada ya kipindi cha miezi miwili hadi mitatu kuruhusu kufanyika kwa marekebisho.

Katika maelezo yake alisema wamefuatilia utekelezaji wake wa malipo hayo, ambapo wamegundua baadhi ya taasisi hazijalipwa hadi sasa.

Alisema katika taasisi zilizolipwa kumejitokeza kasoro mbalimbali ikiwa ni pamoja na mapunjo yanayotokana na makosa ya ukokotoaji na kukosewa kwa kumbukumbu za wafanyakazi uliofanywa na menejimenti.
 
Kumbe ile PhD waliyompa mkwere ilikuwa ni kujikomba!
 
yeah ni lazima wamnyenyekee sababu yeye ndiye aliyewaweka madarakani!watu wanazihangaikia PhD kwa miaka 5-6 na maresearch kibao wakati wengine wanazipata kwa mteremko tu!sasa kuna umuhimu gani wa elimu hapo!mbona hatujasikia kina obama wakipewa za mteremko!
 
heko mtt wa mkulima huyu mtu yupo mwazi sana sema kajikuta yupo chini ya uongozi wa mafisadi
 
Pinda naye!
Huyo mtu atachunguzwa akiwa bado yuko ofisini? Wizi ni kosa la jinai.

Kwa mamlaka aliyopewa na serikali na kuaminika kutumwa UDOM alistahili kumusimamisha kazi mara moja ili achunguzwe kwa amani.
 
Pinda nae goi goi tu maswala ya Dowans, Arusha etc yeye bado analala usingizi hivi anafikiria uwaziri mkuu ni jina?
 
Pinda naye!
Huyo mtu atachunguzwa akiwa bado yuko ofisini? Wizi ni kosa la jinai.

Kwa mamlaka aliyopewa na serikali na kuaminika kutumwa UDOM alistahili kumusimamisha kazi mara moja ili achunguzwe kwa amani.

Nakubaliana na wewe kabisa kwamba Prof Mlacha angesimamishwa ili uchunguzi ufanyike.
 
Back
Top Bottom