Penzi bila maumivu

Penzi bila maumivu

Shunie

JF-Expert Member
Joined
Aug 14, 2016
Posts
157,054
Reaction score
463,869
SEHEMU YA 01...- NYEMO CHILONGANI
“Sijui atazaliwa mtoto gani.”
“Labda wa kiume.”
“Mmmh! Mimi napenda awe mtoto wa kike ili na sisi tujivunie kwa mara nyingine.”
“Ila yeye mwenyewe si alitaka wa kiume?”
“Nani?”
“Sangiwa!”
“Ndivyo alivyosema?”
“Ndivyo nilivyosikia, eti kwa sababu ana watoto wengi wa kike, hivyo anataka apate na mwingine wa kiume!”

“Mmmh! Nafikiri hizo ni tetesi tu.”
Yalikuwa ni mazungumzo ya wanawake wawili miongoni mwa watu wengi waliokuwa wamekusanyika nje ya nyumba pekee iliyokuwa imeezekwa bati na kujengwa kwa matofali, nyumba ya mzee aliyeaminika kuwa na fedha nyingi katika Kijiji cha Chibe kilichokuwa mkoani Shinyanga.

Kila mtu alitaka kujua ni mtoto gani ambaye angezaliwa na mke wa Sangiwa aliyekuwa na fedha nyingi kijijini hapo. Watu walimpenda Sangiwa kwa kuwa hakuwa mtu wa majivuno, kile alichokuwa nacho, alitamani wengine pia wakipate.
Kipindi cha nyuma alikuwa na maisha magumu, masikini kama watu wengine, alidharaulika sana kijiji hapo, hakuwa na nyumba kwani wazazi wake walipofariki, hata ile nyumba aliyokuwa akiishi, akafukuzwa.

Alipitia maisha magumu, hakuona afadhali ya maisha hata siku moja, kila siku alikuwa mtu wa kuomba misaada tu, wapo waliokuwa wakimsaidia lakini pia kulikuwepo na wale waliokuwa wakimnyima.

Alipoona kijijini Chibe maisha yalikuwa magumu, hapo ndipo alipoamua kuhama na kuhamia kijiji cha jirani cha Beda. Maisha hayakubadilika, bado aliendelea kuishi kwenye maisha ya kimasikini hali iliyomfanya kwenda kuomba kazi kwa mzee Mwiku aliyekuwa kijijini hapo.
Kwa kuwa mzee huyo alikuwa na ng’ombe wengi, akampa Sangiwa kazi ya kuwa mchungaji wa mifugo yake. Hilo halikuwa tatizo kwa Sangiwa, kwa kuwa alikuwa na shida, hakuwa na fedha, akakubaliana naye na hivyo kuanza kazi hiyo.
Ilikuwa kazi ngumu mno, kitendo cha kuchunga zaidi ya ng’ombe elfu kumi huku akiwa na wenzake wawili tu ilikuwa kazi kubwa. Kuna kipindi wanyama hao walikuwa wakiingia katika mashamba ya watu, waliwafukuza na hata wakati mwingine kusemwa sana huku wakipokea vitisho vya kila aina.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 02...
Waliogopa lakini hawakuwa na jinsi, hawakuachana na kazi hiyo, waliendelea kuchunga kila siku. Walipokuwa wakirudi na kufika nyumbani, walitengewa maziwa na ugali na kuanza kunywa.

Hayo ndiyo maisha waliyotokea kuishi, walikubaliana nayo kwa kuwa hawakuwa na lolote la kuweza kufanya. Urafiki wake na wachungaji wenzake, Milenze na Olembetu ukazidi kukua kwa kuwa kila wakati walikuwa pamoja.
“Umemuona Frida?” aliuliza Milenze.
“Frida gani?”
“Mtoto wa bosi.”
“Amefanya nini?”
“Alivyokuwa akikuangalia!”
“Mimi?”
“Ndiyo! Alikuwa akikuangalia sana, mpaka nikashangaa.”
“Haiwezekani, hawezi kuniangalia hivyo, au kama nilikosea kuvaa hii suruali,” alisema Sangiwa.

“Mmmh! Sidhani. Ila nahisi kuna kitu.”
“Kitu gani?”
“Au anakupenda!”
“Anipende mimi masikini?”
“Hata mimi nashangaa!”
Hakukuwa na mtu aliyejiamini, kila mmoja alijiona kuwa masikini hivyo kupenda na msichana aliyetoka katika familia ya mtu mwenye hela lilionekana kuwa tatizo. Siku hiyo, Sangiwa akaamua kufuatilia kujua kama kile alichokuwa akiambiwa kilikuwa kweli au la.
Walipofika nyumbani, wakatengewa chakula na wasichana wa mzee Mwiku akiwemo huyo Frida. Kama alivyokuwa akiambiwa ndicho kilichokuwa kimetokea, muda mwingi Frida alikuwa akimwangalia mpaka kumfanya kijana huyo kuanza kuogopa.

Alikuwa masikini sana, alikuja kijijini hapo akiwa peke yake, hakuwa na kitu chochote kile zaidi ya zile nguo alizokuwa amezivaa. Alikaribishwa kijijini hapo na mwisho wa siku kupewa kazi na mzee huyo.

Hakutaka kuamini kile kilichokuwa kikiendelea, eti msichana ambaye baba yake alikuwa tajiri ampende yeye masikini asiyekuwa na kitu, kwake ulionekana kuwa muujiza mkubwa.
Sangiwa hakutaka kukubaliana na uhalisia uliokuwepo kwamba alipendwa na msichana huyo, alichokifanya ni kuachana naye na kuendelea na maisha yake kama kawaida.

Frida hakupunguza kumwangalia Sangiwa, kila aipokuwa akikaa, macho yake yalikuwa usoni kwa kijana huyo, alitokea kumpenda mno, moyo wake ukatekwa na hakukuwa na njia nyingine ya kufanya zaidi ya kupanga kumwambia ukweli.
“Hivi atanikubalia kweli?’ alijiuliza.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 03...
“Sidhani, lakini mbona kama ananiogopa? Mungu! Naomba anikubalie nitakapomwambia ukweli,” alisema Frida huku mapigo yake ya moyo yakidunda mno.
Hakuwa na jinsi, hakutaka kuendelea kuteseka, alitaka kuhakikisha kwamba mvulana huyo anakuwa wake peke yake. Alitumia muda mwingi sana kujipanga ili pindi atakaporudi basi aweze kumwambia ukweli juu ya kilichokuwa kikiendelea moyoni mwake.

Ilipofika saa 12 jioni, kwa mbali akaona ng’ombe na wanyama wengine wakianza kurudishwa, hakuwa na wasiwasi kwamba hiyo ilikuwa mifugo yao na miongoni mwa wachungaji wale alikuwepo mvulana aliyekuwa akimpenda sana.
Walipofika, Frida akaanza kupitisha macho yake kuwaangalia wachungaji wale, kitu kilichoonekana kumshtua sana, Sangiwa hakuwepo. “Mmmh! Sangiwa yupo wapi?” alijiuliza pasipo kupata jibu lolote lile.

Moyo wake ukajawa na presha kubwa, kitendo cha kutokumuona kijana huyo akirudi na wachungaji wale kilimshtua kwa kuona kwamba inawezekana kulikuwa na tatizo, au alikimbia kwani vijana wengi kwa kipindi hicho walikuwa wakitoroka sana kuelekea mjini kutafuta maisha.
Hakutaka kukubali, hakujisikia amani moyoni mwake, kwani hata alipokuwa akiangalia kwa mbali katika njia ile waliyokuwa wakiitumia wachungaji, hakuweza kumuona Sangiwa.
“Naomba nikuulize kitu Olembetu,” alisema Frida, aliamua kumfuata mmoja wa wachungaji wale.
“Kitu gani?”
“Sangiwa yupo wapi?” aliuliza Frida.
“Kuna tatizo lilitokea.”
“Tatizo gani?”
“Kwanza baba yupo?”
“Ndiyo! Yupo.”
“Ngoja nikamuone,” alisema Olembetu.
“Kwanza niambie nini kimetokea,” alisema Frida huku akimvuta Olembetu.
“Nitakuja kukwambia, subiri kwanza,” alisema Olembetu na kuondoka mahali hapo.

Frida akawa na hofu moyoni mwake, hakujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea mahali hapo, aliambiwa kwamba kulikuwa na tatizo lililokuwa limetokea lakini kila alipotaka kufahamu tatizo hilo lilikuwa lipi, akakosa jibu.
Akabaki akiwa na presha kubwa, akabaki mlangoni huku akionekana kuwa na mawazo. Hakuwa na hamu ya kula, hakuwa na hamu ya kufanya jambo lolote lile, akili yake yote ilikuwa ikimfikiria Sangiwa tu.
 
SEHEMU YA 04
Wala hazikupita dakika nyingi, mlango ukafunguliwa, baba yake, mzee Mwiku akatoka huku akiwa na hasira kubwa, alichokifanya mzee huyo, akachukua viatu vyake vilivyokuwa mlangoni na kuondoka mahali hapo huku akionekana kama mtu aliyechanganyikiwa.
Hali hiyo ikamtia hofu Frida.
***** Wachungaji walikuwa kwenye wakati mgumu, walijitahidi kuwazuia ng’ombe wao kwenda katika mashamba ya watu wengine lakini hali hiyo ilikuwa ngumu kwao. Ng’ombe walikimbilia kwenye mashamba ya watu yaliyokuwa na mavuno mengi na kuanza kula mahindi.
Sangiwa, Olembetu na Milenze

waliendelea kujitahidi kuwazuia ng’ombe wale lakini ilishindikana kabisa.
Waliwafahamu vizuri wakulima, mara kwa mara walikuwa wakipambana nao na hata wakati mwingine kuuana kwa kile kinachosemekana kuwa dharau kutoka kwa wafugaji ambao walionekana kuwaachia ng’ombe wao makusudi na kwenda kuvamia mashamba yao.
Kwa kila ng’ombe aliyekuwa akiingia shambani mwao, walikuwa wakiwakamata, wanawachinja na maisha kuendelea.
Wakati Sangiwa na wenzake

waliposhindwa kuwazuia ng’ombe wale na kuingia mashabmbani, tayari wakajua kwamba ugomvi mkubwa ungetokea kwani mara kwa mara tukio kama hilo linapotokea, wakulima hupandwa na hasira na kuwaua ng’ombe au hata kuwachukua wachungaji wenyewe.
Wote walionekana kuwa na hofu, kitendo cha ng’ombe wale kuingia katika shamba la mzee Matumbo tayari kukaonekana kuwa na ugomvi mzito ambao ungetokea. Vijana wa mzee huyo ambao mara kwa mara walikuwa shambani mule wakilima au hata kuhakikisha mazao yanachungwa, walipowaona ng’ombe wale, wakawakamata.

“Jamani tunaomba mtusamehe,” alisema Sangiwa, alionekana kutia huruma, kosa kubwa la kutokuweza kuwazuia ng’ombe wale kuingia shambani mule, tayari kukaonekana kama kungetokea ugomvi mkubwa.
“Kwa nini mmewaruhusu ng’ombe kuingia shambani kwetu?” aliuliza kijana mmoja, alionekana kuwa na hasira tele.
“Hatukuwaruhusu, tulishindwa kuwazuia,” alijibu Sangiwa huku akionekana kuwa na hofu.
“Tunawaua kama kawaida yetu.”
“Naomba msiwaue, nawaombeni tafadhali,” alisema Olembetu huku akipiga magoti.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 05
Wakati maongezi yakiendelea mahali hapo, ghafla mzee Matumbo akatokea mahali hapo, alipowaona ng’ombe wale shambani kwake, akashikwa na hasira kali mno, akaanza kuwasogelea wachungaji wale huku akionekana kuwa na shari kabisa.
“Kwa nini mmewaruhusu ng’ombe wetu kuingia shambani kwangu?” aliuliza huku akionekana kughadhibika.

“Hatukuwaruhsu mzee, naomba utusamehe, walituzidi nguvu,” alisema Sangiwa.
“Ng’ombe wa nani hawa?”
“Mzee Mwiku.”
“Kamuiteni mwenyewe, la sivyo ng’ombe hawatoki hapa,” alisema mzee yule.
“Mzee, tunakuomba utusamehe.”
“Nimesema kamuiteni, kama hamtaki, mmoja wenu abaki na ng’ombe waende.”
“Hakuna tatizo. Acha nibaki mimi,” alisema Sangiwa maneno yaliyoonekana kuwashangaza wenzake wote.
Hakukuwa na cha kufanya, alitaka mwenyewe kubaki ili mladi wale ng’ombe wachukuliwe na kurudishwa nyumbani. Kwa mzee Matumbo, hakutaka kufanya kitu chochote kibaya, alimheshimu sana mzee Mwiku kwa kuwa walifahamiana sana.

Alikuwa mzee tajiri aliyekuwa na mifugo mingi, alipendwa na watu wengi, si katika kijiji chake bali hata watu wa vijiji vingine walimpenda mzee huyo aliyeonakana kuwa na roho ya huruma na kusaidia watu.
Kutaka kijana mmoja abaki, kwake ilikuwa kama nafasi ya upendeleo, hakutaka kuingia kwenye ugomvi na mzee huyo kwani kama jambo hilo lingetokea, mapigano yake yangekuwa makubwa na kusingeweza kupatikana kwa amani milele.
*
*

Mzee Mwiku alikuwa amechanganyikiwa, alipoambiwa kwamba kijana aliyekuwa akimpenda kuliko wote, Sangiwa alikuwa amezuiwa na mzee Matumbo kulimuumiza na hivyo akaamua kwenda huko yeye mwenyewe.
Mwendo wake ulikuwa ni wa harakaharaka, hakutaka kuangalia nyuma, wakati mwingine alikuwa akikimbia kwa kuona kwamba alikuwa akichelewa.

Binti yake, Frida hakutaka kubaki nyumbani, hakutaka kuona mvulana aliyekuwa akimpenda sana, Sangiwa akamatwe sehemu halafu yeye awe na amani nyumbani, alipomuona baba yake akiondoka, naye akaanza kumfuata kwa nyuma, ila alikuwa mbali.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 06...
Kila alipokuwa akipiga hatua kadhaa, alikuwa akijificha, hakutaka kuonekana kabisa. Safari iliendelea, baada ya mwendo wa dakika arobaini na tano, wakaanza kuingia katika sehemu kubwa iliyoonekana kuwa kama shamba kubwa, huko ndipo mzee Mwiku alipokutana na mzee Matumbo.

“Afadhali umekuja,” alisema mzee Matumbo.
“Kuna tatizo?”
“Ndiyo lipo. Unamfahamu huyu?” aliuliza mzee Matumbo,.
“Ndiyo namfahamu, ni kijana wangu.”
“Sawa. Ng’ombe wako walirudi tena shambani kwangu,” alisema mzee Matumbo, tayari kigiza kikaanza kuingia.
“Naomba umruhusu aondoke, sisi tubaki tukizungumza kama wazee,” alisema mzee Mwiku, hilo halikuwa tatizo, Sangiwa akaruhusiwa kuondoka.

Njiani hakutaka kutembea, mwendo wake ulikuwa ni kukimbia tu, alitaka kuwahi nyumbani kwani giza lile lililokuwa likikaribia kuingia, lilimuogopesha sana. Alikimbia mpaka alipotoka nje ya mashamba yale, hakutaka kuangalia nyuma, macho yake yalikuwa mbele tu.
Moyoni alimshukuru Mungu, hakuamini kile kilichokuwa kimetokea, kitendo cha kuruhiswa kuondoka huku akijua kwamba kulikuwa na ugomvi mkubwa baina ya wakulima na wafugaji, kwake aliona kama muujiza.

“Sangiwaaaa.....” ilisikika sauti nyuma yake.
Kwanza akaogopa, tayari giza lilibakia dakika chache kukamilika, alipoisikia sauti hiyo, akaogopa, alijua kwamba alikuwa porini, sasa ni nani alikuwa akimuita, hofu ya kudhani kwamba sauti hiyo ilikuwa ni ya jini au mchawi ikamuingia, hivyo akaongeza kasi.
“Sangiwa nisubiri....Sangiwa nisubiri...” ilisikika sauti ile.

Masikioni mwake haikuwa ngeni, aliifahamu vilivyo, ilikuwa ni sauti ya msichana Frida, lakini pamoja na hayo, hakutaka kusimama.
Aliendelea kukimbia mpaka alipofika umbali fulani, sauti ile iliendelea kumuita, akaona bora asimame, kama ilikuwa ni ya jini kama alivyofikiria, hakuwa na jinsi, alikuwa tayari kufa.

Akageuka nyuma, kwa mbali akaanza kumuona mtu akija kwa kasi, mwili wake ukazidi kutetemeka, mapigo ya moyo yakaanza kumdunda kwa kasi kwa kuona kwamba kulikuwa na hatari ambayo ilikuwa ikimsogelea mbele yake.

Itaendelea.
 
SEHEMU YA 07...
Akakosa nguvu za kukimbia, kikafika kipindi akajuta kwa nini alisimama kumsubiria mtu huyo aliyekuwa akija kwa kasi, alipokaribia, akamwangalia, alikuwa msichana aliyevalia gauni refu, alipokaribia zaidi, akagundua kwamba alikuwa Frida.
“We Frida, unafanya nini huku porini?” aliuliza Sangiwa huku akionekana kushangaa.

“Nimekufuata wewe.”
“Umenifuata mimi?”
“Ndiyo! Niliambiwa kwamba upo huku. Nini kilitokea?”
“Hapana, hebu twende nyumbani.”
“Subiri kwanza. Niambie,” alisema Frida.
Kadiri walivyokuwa wakiongea na ndivyo msichana huyo alivyozidi kumsogelea Sangiwa mpaka kumfikia karibu kabisa kama watu waliotaka kukumbatiana. Mapigo ya moyo wa Sangiwa yakazidi kudunda, akazidi kuingiwa na hofu, kuwa na binti wa mzee Mwiku porini, tena usiku, kulimtia hofu.
“Frida...” aliita Sangiwa wakati msichana huyo akishika maeneo ya zipu.
“Nakupenda. Naomba unipe.”
“Unasemaje?”

“Naomba unipe,” alisema Frida.
Hata kabla Sangiwa hajasema chochote, ghafla wakaanza kuzisikia sauti za watu wakija kule walipokuwa, zilikuwa kama sauti za watu watatu, walipozisikiliza vizuri, waliigundua sauti ya mtu mmoja, alikuwa mzee Mwiku.
Kila mmoja akaogopa.
“Baba...” alisema Frida huku akionekana kutetemeka.

***** Akili ya Sangiwa ikacheza fasta, aliona kama asingeweza kufanya kitu cha ziada basi wangeweza kuonekana mahali hapo jambo ambalo lingekuwa baya sana kwake, alichokifanya, tena kwa haraka sana ni kumshika mkono Frida na kisha kumpeleka katika kichaka kilichokuwa pembeni.
“Nyamaza, usipige kelele,” alisema Sangiwa kwa sauti ya chini na Frida kutii.
Walikaa pale mpaka walipomuona mzee Mwiku akipita na watu wengine wawili, alikuwa mzee Matumbo na kijana mwingine, walikuwa wakimsindikiza kuelekea Beda.

Waliendelea kubaki kichakani pale mpaka walipopita na ndipo wakatoka na kusimama huku wakiangalia kule wazee wale walipoelekea.
“Si unaona ulitaka kusababisha tukamatwe,” alisema Sangiwa.
“Naomba unisamehe, lakini ninakupenda Sangiwa,” alisema Frida kwa sauti ya chini.

Sangiwa hakutaka kuelewa kitu chochote, alichomwambia ni kwamba walitakiwa kuondoka mahali hapo na kuelekea kijijini tena kwa kupitia njia nyingine tofauti na ile waliyopita wazee wale.
 
SEHEMU YA 08...
Hiyo ndiyo ilikuwa siku ya kwanza kwa Frida kumwambia Sangiwa kwamba alikuwa akimpenda. Kwa kijana huyo, mambo yalionekana kuwa magumu, hakutaka kuwa na msichana huyo kwa kuwa alifahamu kwamba mapenzi hayakuwa na siri, hivyo kuna siku baba yake angegundua hilo.

Kwa Frida, maisha yalikuwa magumu, hakutaka kuelewa chochote kile, kila siku ilikuwa ni lazima kutafuta muda maalumu na kuzungumza na Sangiwa. Alimuonyeshea dalili zote kwamba alikuwa akimpenda, hakuona kama kulikuwa na umuhimu wa kuficha chochote kile.

Siku zikakatika, Frida, ambaye alipewa jina hilo kama mrithi wa Mzungu aliyewahi kuja mahali hapo, akaendelea kukua zaidi, maungo yake yakatanuka na kifua chake kujaa kitu kilichomuweka Sangiwa kwenye wakati mgumu.
“Leo nahitaji,” alisema Frida huku akionekana kumaanisha kile alichokuwa akikisema. Ilikuwa imepita miaka miwili, katika kipindi chote hicho alikuwa akizungushwa tu.

“Haiwezekani.”
“Kwa nini isiwezekane? Mimi si ni mpenzi wako?”
“Ndiyo! Lakini haiwezekani,” alisema Sangiwa huku akionekana kuogopa.
“Hapana, leo utanipa tu, ukikataa namwambia baba ulitaka kunibaka,” alisema Frida.

Maneno hayo aliyokuwa amezungumza yalionekana kuwa mwiboa mkali moyoni mwa Sangiwa, hakuonekana kutania hata kidogo, alimaanisha kile alichokuwa akikizungumza kwamba endapo asingekubali kufanya naye mapenzi basi ilikuwa ni lazima kumwambia baba yake kwamba alitaka kumbaka.
Kwa Sangiwa ukawa mtihani mgumu, hakutaka binti huyo akamwambie baba yake, alichokifanya, tena kishingo upande ni kukubaliana naye tu na mchezo kufanyika.

Huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa kila kitu, wakazidi kupendana kila siku mpaka kikafika kipindi ambacho Sangiwa akaacha mzee Mwiku ajue, na mambo yalipogundulika, Sangiwa akaamua kumuoa msichana huyo na kupewa ng’ombe themanini kama zawadi ya kuanza maisha yake.

Haohao ng’ombe ndiyo waliobadilisha maisha yao, Sangiwa alikuwa na akili ya maisha, kupitia ng’ombe hao, waliongezeka, akaanza kuwakamua maziwa na kisha kwenda kuyauza mjini Shinyanga.
 
SEHEMU YA 09...
Ilikuwa biashara kubwa na yenye wateja wengi ambapo kidogokidogo akaanza kufanikiwa. Maisha yake yakabadilika na mpaka mwaka mmoja ulipopita, mkewe akajifungua mtoto wake wa kwanza wa kiume aliyempa jina la Malima.
Maisha yaliendelea zaidi. Mwaka wa tatu ulipoingia baada ya kuishi maisha ya ndoa na mkewe, wakapata wageni Wazungu kutoka nchini Uingereza ambao walifika hapo kwa ajili ya kueneza elimu ya ufugaji katika vijiji mbalimbali.

Miongoni mwa Wazungu hao wanne waliofika kijijini hapo alikuwepo msichana mrembo aliyeitwa kwa jina la Tatiana.
Wazungu hao walikuwa msaada mkubwa, hawakuwa na maisha ya kifahari kijijini hapo, walisaidiana na wanakijiji wengine kufanya shughuli mbalimbali za maendeleo.
Tatiana ambaye alionekana kuwa mrembo zaidi, kila siku akawa akiamka asubuhi na kuwakusanya watoto wengi na kuanza kucheza nao. Maisha ya kijijini yakawa tofauti, amani ikatawala, watu wengi wakawapenda Wazungu hao walioonekana kuleta mabadiliko makubwa.
“Ni msichana mrembo, anavutia machoni kwa kila mwanaume,” alisema jamaa mmoja, aliyagandisha macho yake usoni mwa Tatiana aliyekuwa akicheza na watoto.

“Kwa mfano ukawa na msichana kama huyu, yaani kwa mfano tu, halafu akakupenda, hivi si itakuwa balaa kijijini!” alisema jamaa mwingine.
“Ndiyo hivyo! Anavutia sana jamani.”
Tatiana akawa stori ya kijijini hapo, watu waliendelea kumpenda sana. Mpaka mwezi wa sita unaingia baada ya kukaa kijijini hapo, Wazungu wale wakaamua kuondoka kurudi nchini Uingereza kitu kilicholeta majonzi makubwa.

Mwaka uliofuata, Mwiku akapata watoto wawili, walikuwa mapacha, aliwapenda mno, aliwajali na mapenzi zaidi yakawa kwa mkewe. Hiyo ndiyo ilikuwa familia yake, alipata watoto watatu kwa mke wake, hakutaka tena kuwa na mtoto mwingine, alimshauri mkewe kukubaliana naye, wote wakakubaliana kwamba hao ndiyo wangekuwa watoto wa mwisho.
Maisha yalibadilika, baada ya mzee Mwiku kufariki, akaamua urithi wake wote auache kwa mtoto wake, Frida ambaye hakuwa mbinafsi, akawagawana na watoto wengine, kila mmoja akaondoka zake, waliotaka kuuza, waliuliza na waliotaka kuziendeleza mali hizo wakiwemo ng’ombe, walifanya hivyo.
 
SEHEMU YA 10...
Baada ya mwaka kupita, Sangiwa akashauri wahame hapo na kuhamia katika Kijiji cha Chibe alipozaliwa, Frida hakuwa na kipingamizi, wakahamia huko.
Kila mtu aliyemuona Sangiwa alishangaa, walimfahamu sana, alikuwa kijana masikini ambaye aliondoka kijijini hapo, sasa ilikuwaje awe na mali nyingi, tajiri kiasi hicho?

Alipoingia hapo Chibe tu, kitu cha kwanza ni kujenga nyumba ya kisasa, iliyojengwa kwa matofali na kuezekwa mabati. Kila mwanakijiji akamuheshimu kijana huyo aliyekuwa masikini wa kutupwa kipindi cha nyuma.
“Mume wangu,” aliita Frida.
“Unasemaje mke wangu?”
“Nahisi nina mimba.”
“Unasemaje?”
“Nahisi nina mimba,” alisema Frida huku akiwa amelishika tumbo lake, Sangiwa akachanganyikiwa kwani hakutegemea kupata mtoto mwingie.
“Hebu nione tumbo.”
Akaligusa tumbo la mke wake, Frida.
“Mmmh!” alijikuta akiguna.
*****

Wote wawili hawakutaka kuwa na mtoto lakini haikuwa na jinsi, tayari Frida alikuwa mjauzito kitu kilichomkasirisha kila mmoja. Hawakuwa na jinsi, kile walichokuwa hawakitaki kilikwishatokea hivyo walitakiwa kukubaliana na ukweli wenyewe.
Sangiwa akamuahidi mke wake kwamba angekuwa naye bega kwa bega kuhakikisha mimba inakuwa salama na mwisho wa siku kujifungua mtoto mzuri aliye na afya bora kama alivyofanya vipindi vyote ambavyo Frida alikuwa mjauzito.

Siku zikaendelea kukatika, miezi ikasonga mbele na hatimaye baada ya miezi tisa kukamilika, watu wakajikusanya nje ya nyumba yake kwa ajili ya kusikia ni mtoto wa jinsia gani ambaye angezaliwa siku hiyo.
Kila mtu aliyekuwa mahali hapo alionekana kuwa na furaha, roho nzuri aliyokuwa nayo Sangiwa iliwafanya watu wengi kumpenda na kumtakia mafanikio katika maisha yake yote.

“Natumaini Mungu atakuwa pamoja na mkeo,” alisema mwanaume mmoja, alikuwa akimwambia Sangiwa.
“Natumaini hilo, nina furaha ya ajabu, hatimaye mtoto wangu wa nne anazaliwa,” alisema Sangiwa huku akichia tabasamu pana.
Dakika ziliendelea kusonga mbele, baada ya dakika hamsini, mwanamke mmoja akatoka ndani ya chumba kile, alionekana kuwa na furaha mno huku akiwa na presha kubwa.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom