Olengurumwa: Sakata la Ngorongoro, Loliondo, madai ya rushwa kutawala ni doa kwa miaka miwili ya Rais Samia, kuna nafasi ya kurekebisha

Nyakijooga

Senior Member
Dec 9, 2018
123
202
Mratibu wa Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC), Wakili Onesmo Olengurumwa amepongeza Rais Samia kuleta mageuzi katika maeneo yanayogusa haki za binadamu lakini amedai kuwa katika kipindi cha miaka miwili ya utawala wake sakata la Ngorongoro na Loliondo pamoja na madai ya uwepo wa rushwa , matumizi mabaya ya fedha yanaweza kuwa ni doa.

"Kuna maeneo ambayo hayakwenda vizuri mfano utaratabu uliotumika kuwaondoa watu wa Ngorongoro na Loliondo kuchukua lile eneo haukufuata utaratabu wa sheria na baadhi ya madoamadoa machache ambayo yamejitokeza"amesema Wakili Onesmo Olengurumwa.

ameongeza kuwa"Tunaona changamoto nyingine ni ya rushwa ikitaka kujitokeza kwa kila mahali, ni jambo ambalo limezungumzwa na viongozi wengine na wananchi, kwahiyo hajitaidi kulifanyia kazi"

Akichambua miaka miwili ya Rais Samia Suluhu Hassan Olengurumwa amesema kuwa Rais Samia amefanya mambo mengi yanayogusa haki za binadamu ambayo yalikuwa changamoto awali, baadhi ya mambo ambayo ameyabainisha ni pamoja na kuwezesha mazingira rafiki kwa Watetezi wa haki za binadamu, Asasi za Kiraia, Vyombo vya habari, Vyama vya siasa, Wafanyabiashara pamoja na kuwezesha uhuru kwenye taasisi mbalimbali zikiwemo taasisi za kidini.

"Kwa miaka miwili ya Rais Samia Suluhu Hassan tumefanya mambo makubwa sana, Taifa limeweza kupata uhuru katika maeneo mengi kutokana na mazingira tuliyokuwa nayo kabla ya miaka miwili, nasema hivyo kwa sababu ukiangalia makundi mengi ya katika jamii yalikuwa katika mtanziko yakuwa katika mazingira ambayo yaliwafanya wasihis kama ni watu huru katika Tiafa lao"

Pia Olengurumwa aliongeza kuwa "Eneo lingine ambalo limepata uhuru katika kipindi cha miaka miwili ya Rais Samia Suluhu Hassan ni la Asasi za Kiraia na Watetezi wa haki za binadamu hapa Tanzania. Ili kundi lilikuwa na hali mbaya lilikuwa likipitia magumu, Asasi za Kiraia zilikuwa zinashindwa kufanya kazi sheria kali kali zilibana zilitungwa zaidi kubana, baadhi ya akaunti mbalimbali za Asasi za Kiraia zilifungwa, ilikuwa kutetea haki nchini ni kama kosa la jinai, Watetezi wa haki binadamu walijikuta katika hali ngumu, lakini tunachokiona kwa sasa uwepo wa Mama amekutana na makundi haya na tunaona mabadiliko"

Aidha Olengurumwa amesema Rais Samia ameonesha hekima na ukomavu wa kisiasa kwa kutamka wazi kuhusu hoja ya Katiba Mpya, mabadiliko sheria mbalimbali na jitihada za kufanya maboresho ya mfumo wa haki Jinai nchini.

Hata hivyo Olengurumwa amesisitiza kuwanbaadhi ya wasaidizi wa Rais Samia Suluhu Hassan wanatakiwa kumulikwa akidai kuwa licha ya dhamira njema ya Rais Samia lakini utekelezaji wa kauli zake hautekelezwi kwa uharaka kama inavyotakiwa.

Sanjali na hayo Olengurumwa amesema Rais Samia amefanikiwa kidiplomasia kwa kubadili taswira iliyokuwepo awali, ametolea mfano matarajio ya Tanzania kuwa mwenyeji kwenye mkutano wa masuala ya chakula, mkutano wa haki za binadamu pamoja na uhusiano mwingine na wadau wa Kimataifa.

Ameshauri kuwa zipo changamoto nyingine mabalimbali ambazo zinatajwa na baadhi ya watu ikiwemo namna Serikali inavyoweza kupunguza matumizi katika masuala ambayo hayana umuhimu sana ili kuwezesha upatikanaji wa huduma mbalimbali kwenye jamii.

Akizungumzia suala hilo amesema utawala uliopita chini ya Rais John Pombe Magufuli ulijitahidi kufanyia kazi eneo hilo, ameshauri utaratabu wa kubana matumizi serikalini ukawe endelevu ili fedha itakayopatikana ikafanye mambo mengine yenye tija kwa umma.

Ikumbukwe Rais Samia Suluhu ametimiza miaka miwili tokea alipoingia madarakani kufuatia kifo cha Rais Dkt. John Pombe Magufuli ambaye alifariki Machi 17, 2021.

Mwaka mmoja baada ya kuingia madarakani alipewa tuzo na THRDC kutambua mchango wake katika suala la utetezi wa haki za binadamu, moja kati ya sababu zilizotajwa ni kuwezesha mazingira rafiki kwa Watetezi wa haki za binadamu kutimiza majukumu yao mfano mazingira rafiki kwa wanahabari na vyombo vya habari, mazingira rafiki kwa baadhi ya taasisi zisizo za Kiserikali, mfano kuwezesha kufunguliwa kwa akaunti za mtandao huo.

Lakini katika suala sakata la Ngorongoro na Loliondo ambalo Olengurumwa amelitaja kuwa ni kati ya changamoto zilizojitokeza kwa miaka miwili ya Rais Samia, ilikuwa ikihusiana na baadhi ya wananchi jamii ya kimasai eneo Ngorongoro kuhamishwa (Serikali ilidai waama kwa hiari) kwenda Msomera ikidaiwa kuwa walikuwa wakiisha maeneo hatarishi na ambayo wanakosa huduma muhimu za kiubinadamu kutokana na mazingira ya Hifadhi ya Ngorongoro. Lakini wadau mbalimbali wakiwemo Watetezi wa haki za binadamu walipinga zoezi hilo kuwa lilikuwa likitekelezwa kwa kukiuka misingi ya haki za binadamu.

Pia Sakata la Loliondo ambalo liliibua mijadala mizito lilihusu zoezi ambalo Serikali ilitangaza kulitekeleza kwa kuweka vizimba kwenye mipaka inayoonesha aridhi ya vijiji na eneo la shughuli za uhifadhi, lakini mjadala uliibuka kutokana madai ya eneo la aridhi ya vijiji kumegwa kwa ajili ya shughuli za uhifadhi, hali hiyo iliibua 'taharuki' na kupelekea baadhi ya Viongozi na wananchi kukamatwa na askari mmoja kufariki akidaiwa kupigwa mshale katika mazingira ya sintofahamu huku baadhi ya wananchi wakikimbia na kuziacha familia zao pamoja na mali zao zikiwemo mifumo.
 
Back
Top Bottom