Aliyekuwa Mkuu wa Wilaya ya Hai Mkoani Kilimanjaro, Lengai Ole Sabaya, amewataka viongozi wa makanisa na waumini kutoingilia au kubishana na mamlaka za serikali, akisisitiza kwamba mamlaka za utawala zinatokana na Mungu, akisisitiza kuwa wanapaswa kudumisha amani na kujitokeza kupiga kura Oktoba 29, 2025.
Sabaya alitoa wito huo alipokuwa kwenye ibada ya kumsimika Mchungaji na Kiongozi wa West Meru iliyofanyika chini ya uongozi wa Askofu Mkuu wa FPCT Jimbo la Arusha. Katika hotuba yake, Sabaya alirejea mifano ya Biblia kuonesha kwamba mamlaka ya kisiasa ni sehemu ya mpangilio wa Mungu.
“Ipo saa Mungu hata kama wewe ni muovu hata kama ni mharibifu, saa yake ya kusema endelea kukaa kwenye hicho kiti mradi ipo, wewe mwache aendelee kukaa maana ni wa Bwana, hivyohivyo inatumika kwa Serikali, Kanisa la kweli la Mungu mtakatifu haijalishi sauli yupoje, haumpendi, unamuona Mama Samia anafaa hafai! Kanisa la kweli la Mungu halibishani na Serikali”, alieleza.
Alisema pia kuwa hata mtu mwenye makosa kwa mujibu wa wakati wake, Mungu ndiye mwenye mamlaka ya kumchagua ni lini ataondolewa au kubadilishwa, hivyo wachungaji na waumini wasiwe chanzo cha vurugu au kuvuruga utulivu.
Sabaya aliwataka waumini wasiwe mashirika ya siasa na badala yake waende kupiga kura, wakizingatia amani na utulivu kama wajibu wa kiraia na wa kidini.