Nilionja machungu ya kuwa HIV+, unyanyapaa ni unyama

Memtata

JF-Expert Member
Jul 27, 2013
552
1,800
Kisa kilianzia miaka 20 na iliyopita, nilikuwa na mpenzi wangu mmoja (nilikuwa kijana muaminifu sana kwenye mahusiano). Tulikuwa kwenye mahusiano kwa muda lakini tulikuwa hatujaoana, kwao walinijua na kwetu walimjua. Baada ya mahuasiano ya muda mrefu huyu binti aliugua muda mfupi na kufariki.

Mpenzi wangu akazikwa nikaanza maisha ya ufiwa, hali ilikuwa mbaya sana kwangu karibia kila siku nilimuota huyu binti. Niliteseka sana nikakondeana kwa mawazo. Kumbe wakati nateswa na majonzi kuna watu wanalipika la kuniumiza zaidi.

Ilianza kama utani, nilipokuwa nikipita sehemu naona watu kama wananisema niliona ishara za kupointiwa vidole au wakati mwingine walio ndani hutoka nje haraka baada ya kuitwa na kuonyeshwa mimi.

Sikuwa na mawazo hasi kuhusu jambo hili kwamaana kubwa moja. Hapa mtaani nilikuwa maarufu sana kwa upole na hekima na mahusiano yangu na huyu dada yalikuwa ni ya mfano hadi taarifa zilikuwa zinaturudia kwamba wengi wanatamani wangekuwa na mahusiano kama yale.

Kutokana na hili nilijua kabisa wanaonisema hawanisemi kwa ubaya bali wanasikitika kwa kuondokewa na nimpendaye na kila mtu alitamani kunijua mimi ni nani. Kumbe haikuwa hivyo.

Mara ya kwanza naanza kupata matokeo ni kwasababu ya binti mmoja mzuri sana alipotaka kuanzisha mahusiano na mimi.

Huyu binti alikuwa ni jirani yetu na wakati huo alikuwa anamalizia kidato cha nne, sasa siku hiyo ilikuwa ni weekend amekuja kwao kusalimia na kurudi shuleni (alikuwa anasoma boarding hapohapo mjini). Kwa muda niliwaona wanaongea na jamaa yangu mmoja ambaye alikuwa na ki mini supermarket pale mtaani.

Demu aliponiona akashtuka na kuaga haraka haraka na kuondoka, tukapishana njiani akinisalimia kwa uoga uoga huku jamaa yangu akitabasamu na kuniangalia. Nilipofika pale dukani jamaa akaniambia kuwa huyu binti (tumpe jina Spicy) ametoka hapo kwasababu moja tu, kamuomba (jamaa) aniunganishe nae.

Nilichukulia utani lakini jamaa alikomaa kweli Spicy anataka tuonane na mimi nilichukulia utani na kawaida sana kwakuwa sikuwa na tamaa na mahusiano kwa muda huo pili Spicy alikuwa ni binti mzuri sana sikuamini kabisa kama angeanza kutaka mahusiano na mimi.

Mwisho nikakubali jama akanipa maelekezo kwamba Spicy aliacha namba ya simu ya matron nikiwa na shida nimpigie tupange tunakutana vipi. Kiuhalisia mabinti hawa wazuri (baadhi yao) huwa watata sana, fikiria alivyo na maelewano na matron hadi kumruhusu mwanaume apige simu yake kumkutanisha. Basi siku moja nikapiga simu nikajieleza na kuomba kuongea na Spicy, ndani ya muda mchache mtoto akapewa simu tukaanza maongezi. Aliongea machache sana lakini aliniomba Jumamosi inayofata akija kwao tuonane.

Jumamosi ilipofika mida ya jioni Spicy kweli alikuwa kwao na alinitafuta kwa namba nyingine tukawasiliana akaniomba samahani kwamba hakuweza kupata muda siku hiyo na aliniambia akifika shuleni tungechat kupitia simu ya matron.

Siku hiyo kwa mara ya kwanza akanitamkia kuwa ananipenda sana, kwa upende wangu sikuwa na pingamizi kwasababu ukweli huyu binti alikuwa ni mzuri sana machoni mwangu. Tuliongea mengi hadi akaniambia jinsi watu walivyokuwa wanasifia mahusiano yangu na mpenzi wangu aliyefariki. Nilifarijika sana moyo ukaanza kutulia na kuanza kumpenda Spicy japokuwa bado sikutilia sana maanani.

Rafiki yangu akaniuliza matokea nikampa mchongo kamili akafurahi sana na akanishauri nisipoteze muda cha kwanza nile mzigo mengine ndio yafuate, wakati huo mimi niliwaza kabla ya lolote inabidi tupime HIV. Kumbe wakati mimi nawaza hayo na mwenzangu anawaza yake…

Nilianza kumkomalia Spicy tukutane lakini mwenzangu alikuwa ananichenga na nilikuwa napata habari zake kama siku fulani alikuwa kwao lakini hakuweza kunitafuta tuonane. Hata nilipomtafuta matron nae alianza visa, kuna wakati hakupokea simu wala hakujibu meseji na alipopokea simu alisema huyu hayupo jirani nilipomwambia akija anijulishe alisema hana salio la kunijulisha. Basi mwanaume natuma vocha ya buku tano (wakati huo hakuna vocha ya jero wala buku) na bado sikutafutwa.

Basi sikumoja nikaandika meseji ndefu sana kutaka ukweli wa jambo hili nilimuomba awe wazi ili nisimsumbue tena, ujumbe ukamfikia siku hiyo akanipigia na kuniomba msamaha akisema yuko bize na masomo lakini next weekend atajitahidi aje nyumbani tuonane. Nikafurahi sana nikasubiri hiyo siku kwa hamu kubwa sana, moyoni nikiwaza nimle au nisimle? Niliwaza kama ni kumla basi nitafute vipimo vya HIV niwe navyo ghetto. Wakati huo nilikuwa nimepanga nyumba tukishirikiana na rafiki yangu wa uhamiaji.

Katikati kabla ya kufikia siku yenyewe kuna maswali yalianza kunipa wasiwasi, Spicy alikuwa ananipigia au kunitumia sms kuniomba nisije kumfanyia ukatili wowote. Kwamba ameniamini sana kukutana na mimi ananiomba nisinmfanyie chochote bila ridhaa yake.

Nilianza kushtuka… anamaanisha nini huyu?! Kwanini nisimfanyie kitu kibaya?! Anamaana mimi nitambaka au nitamfanyaje? Basi wazo la kukutana nae kwangu nikalifuta na sikutaka tena kununua vipimo na hamu ya kuendelea na mahusiano na huyu binti ikaanza kuyeyuka.

Siku ikafika Spicy akanipigia nikamwambia nilipo tukakutana, alikuwa na wasiwasi sana hadi hamu ya kuwa nae ikakata kabisa. Akaanza kuniuliza nampeleka wapi nikamwambia tunaenda kilimani Hotel. Akazidi kuwa na wasiwasi akaniambia nakuomba nipo chini ya miguu yako usinifanyie chochote kibaya, nikamjibu kwa mkato sitaweza kukufanyila lolote usilolitaka.

Hao tukaenda hadi Kilimani nafikiri alidhani nimechukua chumba, mimi huyo hadi kwenye vibanda vya kupumzikia tukakaribishwa na kuletewa vinywaji. Hotel ilikuwa kimya na tulivu sana, nikamuangalia Spicy alikuwa amelowa makwapani kwa jasho nadhani ilikuwa ni sababu ya hofu.

Baada ya habari mbili tatu nikamwambia Spicy nimefurahi sana kukutana nae maana tangu tukutanishwe na rafiki yangu tulikuwa hatujawahi kukutana uso kwa uso. Nikamueleza jinsi nilivyokuwa na shauku ya kuwa na mahusiano nae kwasababu ya uzuri wake nikamtania kama ni tabia sina shaka na yeye. Akatabasamu akishusha pumzi lakini bado alikuwa ni mwenye wasiwasi.

Baada ya maelezo hayo nikamwambia Spicy ukweli nilipenda sana awe mpenzi wangu tena nilitamani sana lakini kuna vitu vimenipa wasiwasi. Kutokana na hofu hiyo nilimuomba Spicy tusiwe wapenzi bali tubaki kama watu tunaojuana tu au marafiki wa kawaida hii ni kwa manufaa yetu sote.

Chaajabu huyu mwanamke akajifanya kunishangaa kwanini naongea maneno yale, akabadilika na kuwa mwenye huzuni akaniomba nisimfanyie hivyo maana atateseka sana kwasababu alishaniweka moyoni. Nilivyo mjinga nikashuka nikaanza kumbembeleza na kukubali ombi lake na kumuomba anisamehe maana nilifanya hivyo baada ya kumtafsiri tofauti.

Tukaachana na Spicy siku hiyo mapema jioni akirudi kwao, mimi nilifurahi nikaanza kupanga mashambulizi tena ili nimvute home nimpime kisha aliwe. Ningejua mapema hata nisingepoteza muda wangu kilichofuata kiliniumiza zaidi.

Spicy alivyorudi shule alikuwa hanitaki kabisa hakupokea simu wala kujibu sms mbaya zaidi sikumoja nakutana nae maeneo ya yule jama yangu mwenye mini supermarket, nilipomsogelea akaniambia kwamba nisimsogelee kuna noma mama yake yuko hapo jirani. Basi mimi nikajikataa kumkwepa nikakaa pembeni nikaona haraka anaondoka huku akigeuka kuniangalia na kupotea. Hakukuwa na mama yake wala bibi yake.

Siku nyingine nipo mjini natembea namuona yule mbele yangu na rafiki zake aliponiona wakaongea kitu na kuanza kucheka huku wakikimbia kukwepa nilipotokea.

Mchezo ukawa hivi hadi siku moja yule mdogo wangu ninaeishi nae akanifumbua macho. Ni kama alifukua kaburi la mpenzi wangu, niliishi kwa mateso sana baada ya kujua hili. Mdogo wangu aliniambia amesikia watu wanasema mpenzi wangu alikufa kwa UKIMWI na mimi nina virusi ndiomana nimekondeana. Aliongea kwa masikitiko akilaumu maneno hayo na kusema mbona shemeji amekufa kwa tatizo fulani? Hii habari ya UKIMWI imetokea wapi!

Tangu siku hiyo amani ya moyo wangu ikaporomoka nikaanza kuunganisha dot. Kumbe wale waliokuwa wananipoint sio kwamba walisikitishwa na kufiwa bali walionyeshana ili nisiwaambukize! Kumbe Spicy alinikimbia kwa maana hii! Kwanini asingenambia tukapime kama ana wasiwasi na mimi?

Maisha yalikuwa magumu sana, tangu siku hiyo ndio nilijua kwanini watu huanza kujinyanyapaa kabla ya kunyanyapaliwa. Fikiria wakina dada wa mtaani kwangu hawakutaka kabisa mazowea na mimi, ikitokea umekutana nae ukisimama kumsalimia yeye anakujibu huku akitembea tena wengine ni wale waliokuwa shemeji zangu rafiki wa karibu wa marehemu mpenzi wangu.

Niliishi katika maisha haya kwa muda mrefu sana, japokuwa nilikuwa na hamu lakini sikupata mpenzi nani angenikubali. Kutokana na hili nikaanza kuwa mlevi wa kupindukia na kukesha kwenye ma club sikuweza vya kuchinja tena nikahangaika na vya kunyonga.

Nakumbuka siku moja nipo clup na mdogo wangu nikamtuma aniitie dada mmoja hivi, yule dada akaja aliponiona tu akageuka na kumvuta mdogo wangu na kurudi alipotoka. Dogo alivyorudi akaniambia amesema kumbe ni vijana wa Kilimahewa siwezi. Fikiria hadi wa club nao walinigwaya wengi sikuwajua ila walinijua.

Maisha yalienda hivyo kuna wakati nikaanza kuwabahatisha, tabia hii iliwakera sana nyumbani taarifa zilienea kwamba kwangu kila siku nabadilisha wanawake. Wazee wakaniweka kikao wakanishauri nioe ili niishi maisha bora. Marafiki zangu waliamini nilishajikatia tamaa ndomana naambukiza kwa makusudi.

Tatizo utamuoa nani? Siwezi kuoa kabla ya kuanza mahusiano (sio lazima ya kingono). Unapoanzisha mahusiano watu wanaambiana wanakukacha kabla hata ya kusema tupime kujua afya zetu.

Nilinyanyapaliwa maeneo mengi sana hata kwenye kutoa huduma, nilikuwa natabia ya kujitolea damu kila mwaka lakini kuna jamaa zangu walinikejeli na kuniona kama nafanya mambo kujionyesha tu wakati ukweli naujua.

Kuna siku jamaa yangu mmoja aliniambia rafiki yake alifiwa na mke kwa sababu ya kukosa damu, alikuwa anahitaji O Negative, kama ujuavyo damu hii ni adimu sana. Nikamwambia mimi ni group hilo la damu sikujua ningeenda kumtolea, jamaa alicheka kwa kejeli ikaishia hapo hapo. Ilipotokea shida ya watu kujitolea damu mimi sikufatwa kabisa.

Mzimu wa HIV+ umening’ang’ania hadi leo hii nilishahama nyumbani nipo mkoa mwingine nna mke wa watoto watatu, lakini bado kuna maneno nasikia watu huko nyumbani wanasema mke wangu alizaa lakini hakuwa akiwanyonyesha watoto sababu ya UKIMWI.

Niliamua kuyaishi maisha haya sababu kila nilipotumia nguvu kuwaaminisha watu kwamba mimi sina HIV ndivyo walivyozidi kuona ninao ila najikosha. Hata siku nimechumbia huyu mke wangu wa sasa ametoka mbali na nyumbani lakini cha ajabu habari ziliwafikia kwao bahati nzuri tulikuwa tumeshapima mapema.

Inawezekana nimekuchosha kwa maneno mengi lakini utakuwa umejifunza kitu, sio rahisi kujua maumivu ya kunyanyapaliwa kwa maelezo tu ila nikwambie inaumiza sana sana ndugu yangu.. Kuna watu hufa mapema sababu ya kutengwa na jamii, hata mimi ningekuwa bado mazingira yale ya nyumbani inawezekana lolote lingetokea. Elimu zaidi inatakiwa maana hadi sasa haya mambo bado yapo.

Mwisho nikupashe kuhusu Spicy, aliolewa Canada na tunawasiliana aliniambia habari zile aliambiwa na rafiki wa karibu wa marehemu mpenzi wangu ndio maana aliamini na hakutaka tujadili hilo sababu aliamini ni kweli mimi ni HIV+.
 
Doa la ukimwi likishakuangukia uwa HALITAKATI kamwe.

Bro wangu(sina udugu nae). Hadi leo kakubali yaishe na kapata single mama mmoja alieziba maskio na leo wanaishi.

Back then akapata kadada chap akakaslimisha mipango ya mahari ikafanyika chap. Siku 3 nyuma ya kupeleka mahari baba mkwe akamuita akamwambia:, mkwe 1/2/3.

Nasikia unatumia Dozi. jamaa akakanusha,akasema story isiwe ndefu twenden hospital kupima.
Baba bint akakubali, jamaa akarudi nyumbani kesho yake arudi kwa ajili ya vipimo.

Jion yake akapokea ujumbe, baba bint anasema vipimo vifanyikie mbali na mji(wilaya) waliyopo. Madaktar wengi waliopo ndani ya huo mji wanafahamiana na jamaa so uenda wakatoa majibu ya uongo ili kumlinda.

Jamaaa akasema si shida ni jambo dogo tu ilo,twenden wilayani. Asubuhi ilipofika akawapigia simu hawapokei. Makubaliano ilikuwa ni kukutana saa 3 asubuhi kwa ajili ya kwenda hospital lakin sasa simu hawapokei.

Wakati akiwa anatafakari ujumbe ukaingia unasema:, WATU WAMETUAMBIA MTU MWENYE VIRUSI VYA UKIMWI AKINYWA COKE VIRUSI UPOTEA KWA MUDA.

MKWE TUNAOMBA SAMAHANI KWA USUMBUFU ULIOUPATA SISI TUMEGHAILI.
 
Hao wote wanatakiwa waje waishi Mbeya, Iringa, Njombe wakati nipo Dar nilikuwa naona ukimw kitu cha ajabu ila nilipofika Mbeya nilipoenda Chunya, Mbarali (ubaruku, kapunga) aisee ukimw ni kitu cha kawaida sana yaan watu hawana ata hofu nayo wanakwambia kabisa "ngoja nikachukue dawa niende porini nikafuate mzigo".
 
Hao wote wanatakiwa waje waishi mbeya, iringa, njombe wakat nipo dar nilikuwa naona ukimw kitu cha ajabu ila nilipofika mbeya nilipoenda chunya, mbarali (ubaruku, kapunga) aisee ukimw ni kitu cha kawaida sana yaan watu hawana ata hofu nayo wanakwambia kabisa "ngoja nikachukue dawa niende porini nikafuate mzigo".
Njombe kuna mahali nilikuta mpaka majirani wanapitiana kwenda kuchukua ARV. Siku ya kugawa dozi utadhani kuna soko, kumbe ni foleni ya ARV.
 
Ki ukweli waathirika wananyanyapaliwa miaka hiyo kulikua na jirani yetu alikua nao enzi hizo wanaita miwaya ilikua hatari maana hata akifika nyumbani anaishia kukaribishiwa nje na akiondoka povu la sabuni litapigwa eneo lote maana alikua akipenda kutematema mate

Sema naona kwa wakati ule na ujinga ulikua unachangia tofauti na sasa watu wana elimu kiasi
 
Tatizo na wewe ulikua kinyonge sana.

Huo uamuzi wa kulewa na kua shit ulikua wa kinyonge sana.

Kua smart, nenda gym, kula vizuri, vaa vizuri, perfume hadi shumileta roho imuume. Eti wewe ukaanza kulewa na kua malaya
 
Back
Top Bottom