NILIME MIMI SHAMBANI

NILIME MIMI SHAMBANI

tamu 3

Member
Joined
Dec 11, 2024
Posts
88
Reaction score
216
NILIME MIMI SHAMBANI

1.............
Nilime mimi shambani, jua kali linawaka,
Majasho yanitokeni, mwili wote umechoka,
Kutwa ninalinda nyani, wanasumbua hakika,
Nilime mimi shambani, bei wanapanga wao.

2............
Ng'ombe wa bwana Shabani, wala mazao shambani,
Yanipasa kulindeni, mawio na machweoni,
Wadudu nao jamani, wanasumbua shambani,
Nilime mimi shambani, bei wanapanga wao.

3..........
Pembejeo madukani, beiye haishikiki,
Ila mazao sokoni, bei haitamaniki,
Uwapi wewe diwani, mbona kimya hutamuki,
Nilime mimi shambani, bei wanapanga wao.

4..........
Mkulima Afrika, yu duni ni masikini,
Yu peke ahangaika, maisha yake ya chini,
Watu wenye mamlaka, katu hawamthamini,
Nilime mimi shambani, bei wanapanga wao.

5.......
Ushuru barabarani, mwingi kuliko magari,
Mageti barabarani, wa mazao ya shambani,
Nilime mimi shambani, bei wanapanga wao.

6.........
Bado jembe la mkono, mkulima atumia,
Ni vipi mengi mavuno, shambani atachukua,
Kila siku mgongano, hakuna mbele hatua,
Nilime mimi shambani, bei wanapanga wao.

7..........
Kumbuka tena kumbuka, nchi pasi mkulima,
Sawa sasa na kichaka, pasi ndege na wanyama,
Na serikali geuka, kumlindamkulima,
Nilime mimi shambani, bei wanapanga wao.

8.........
Lini huyu mkulima, atakuja kukomboka,
Lini huyu mkulima, tapewa yake fanaka,
Lini huyu mkulima, atakuja pumzika,
Nilime mimi shambani, bei wanapanga wao.


9...........
Barabara mbovu sana, kijijini kutokea,
Wa gari mtasongana, nauli ajisemea,
Wakupakia vijana, hela wanakuchukua,
Nilime mimi shambani, bei wanapanga wao.

10.........
Kusafirisha mazao, gharama kwenda sokoni,
Ila kule ni kilio, mazao ukiuzeni,
Wenye pesa na tuvyeo, bei watulalieni,
Nilime mimi shambani, bei wanapanga wao.

11........
Ndiyo kisa mkulima, kila siku analia,
Hapewi yake heshima, japo chakula atoa,
Ukisema mkulima, watu wakuhurumia,
Nilime mimi shambani, bei wanapanga wao.

12..........
Wizara hiyo kilimo, mkulima ithamini,
Imutoe kwenye shimo, aondoke utumwani,
Kwenye katiba awemo, asiwe mtu wa chini,
Nilime mimi shambani, bei wanapanga wao.

Denny Jeremias kitumbika
Mtunzi wa mashairi na ngano za Kiafrika
Mufindi Tanzania 4.4.2025
 

Attachments

  • Screenshot_20250404-124948.jpg
    Screenshot_20250404-124948.jpg
    442 KB · Views: 25
Mshahiri batili, umeivamia asili!
kiswahili cha mshahiri, hakijakidhi adili.

umelivuruga shahiri, kwa kichwa habari!
ujilime shambani, kiswahili gani hiki jamani..?

rudi kitabuni, ukajisuke upya
usitutie taabuni, hadhira kunung'unika
ushairi wako taabani, mshahiri umetuzunguka!.
 
Mshahiri batili, umeivamia asili!
kiswahili cha mshahiri, hakijakidhi adili.

umelivuruga shahiri, kwa kichwa habari!
ujilime shambani, kiswahili gani hiki jamani..?

rudi kitabuni, ukajisuke upya
usitutie taabuni, hadhira kunung'unika
ushairi wako taabani, mshahiri umetuzunguka!.
Mshahiri ndio nini?
 
Na tena mvua na jua humwangukia mwilini,
Mkulima huungua kwa kazi kuithamini,
Mimea kupalilia kukwepa umasikini,
Sio leo toka zamani,
Mkulima mtu duni,
 
Back
Top Bottom