Nikionacho mgomo wa wanafunzi udsm

Yona F. Maro

R I P
Nov 2, 2006
4,202
218
NIKIONACHO KATIKA MGOMO WA UDSM


Kwanza kabisa nianze kwa kuwapa pole wanafunzi wa UDSM na wale wa vyuo vikuu vingine kote nchini, kutokana na matatizo mbalimbali yanayowakabili, japokuwa makala yangu itagusia UDSM pekee.

Matatizo hayo ni pamoja na ukosefu wa hostel, kuzuiliwa kwa matokeo kwa baadhi ya wanafunzi, kukosa fedha kwa ajili ya chakula na malazi, kuwepo kwa masharti magumu katika ulipaji wa ada na kupanda kwa gharama za maisha.

Wakati matatizo yakiendelea kuwasonga wanafunzi, viongozi wetu hawashtushwi juu ya hali mbaya inayowakabili wasomi hawa, bado wanaweka mguu juu huku wakitafuna fedha za umma kwa kijiko.


Nasikitika kwa hili kwani hadi sasa hajapatikana mtetezi aliye thabiti na mzalendo anayetumia uongozi wake kwa ajili ya kuwasaidia wasomi wetu. Kutokana na wengi wao kulizungumzia tatizo hili kisiasa zaidi kuliko kiuhalisia.

Bado wanafunzi wanaonekana wafujaji wa pesa kwa kupata 5000/= kwa siku na kudai kuwa haitoshi wakati kuna watanzania wanaoishi chini ya dola moja kwa siku.

Kwanza mwenye mawazo haya namuona ni limbukeni asiyejua nyakati na kuzisoma na pia namshauri kurudi darasani na ajifunze falsafa ili aweze kufikiri sahihi.

Pole zangu hazijaishia hapa bado napatwa na uchungu pale ninapoona wasomi wetu wanakosa ajira na hatimaye tunakutana nao wakijiuza na kutumia dawa ya kulevya baada ya kukosa ajira na maisha kuwa magumu.

Wasomi hawa bado wanakabiliwa na mzigo mkubwa katika kutafuta ajira kwani ajira nyingi ni za kujuana na kutumia hongo, na kwakuwa asilimia kubwa ya wasomi wa UDSM wanatoka katika familia masikini masikini tatizo linakuja nani anamjua nani ili amsaidie na inakuwaje kwa mtoto wa mlalahoi.

Nawapa pole juu ya hili kwa mara nyingine tena.


Hata hivyo jamii nayo inaendelea kuwaona wasomi hawa wa UDSM kama wachochezi wa vurugu na wasiopenda maendeleo, kusoma wala kufikiri kutokana na kujihusisha na migomo mara kwa mara chuoni hapo.

Nasena hivi kwa sababu kumekuwepo na tabia ya baadhi ya vyombo vya habari kuipotosha jamii kutokana na kutoa taarifa mbalimbali zisizo na ukweli juu ya migomo mbalimbali inayotokea chuoni hapo.

Lakini penye ukweli sitoacha kusema japo najua kitakuuma kama ni muhusika. Twende mbele na turudi nyuma, harakaharaka tuangalie sababu mbalimbali za migomo katika chuo kikuu cha Dar es salaam (UDSM).

Kwa tathmini na uchunguzi wangu mdogo, nimegundua kuwa mara nyingi wanafunzi hugoma kutokana na suala zima la uendeshwaji wa mkopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu nchini.

Mwaka 2006/2007 wanafunzi waligoma kwa kupinga sera ya serikali ya uchangiaji wa elimu ya juu, iliyomtaka mwanafunzi kuchangia 40% huku serikali ikimtolea 60%. Pia walipinga fedha iliyokuwa ikitolewa kwa ajili ya chakula na malazi Tsh 3500 kwa siku.

Sababu za wanafunzi hawa ni za umakini na zenye ukweli ndani yake kwani uchangiaji huo haukumpa nafasi mtoto wa mkulima kuweza kusoma, na pia fedha ya chakula na malazi haikuwa ikiendana na hali halisi ya maisha.

Sitauzungumzia mgomo wa miezi michache iliyopita kabla ya kuanza rasmi mwaka mpya wa masomo 2008/2009 septemba 27 mwaka huu, kutokana na kuwepo kwa nadharia nyingi juu yachanzo cha mgomo huo, hali ambayo iliwachanganya si wanafunzi tu bali hata jamii na utawala kwa ujumla.

Kila aliyeonekana kuhojiwa na vyombo vya habari , alitoa sababu tofauti zilizokinzana na za mwezake, hata wanafunzi nao waliogoma walitoa sababu tofautitofauti.

Hadi sasa haijawekwa wazi ni sababu gani kuu iliyopelekea wanafunzi kugoma kwani kila mtu bado anatoa sababu yake.

kabla sijaendelea ningependa kuwashauri wanafunzi wenzangu juu ya kufikiri na kuangalia njia sahihi ya kutatua matatizo yao.

Japokuwa mgomo ndio umeonekana kuwa suluhisho pekee lakini lazima wafikiri mara mbili kabla ya kufikia uamuzi wa kugoma.

Si kwamba kwa kusema hivi namaanisha kuwa mgomo unaotarajiwa kufanyika jumatatu ni batili la hasha! Nataka wanafunzi wadadavue kilichomo DARUSO ili wajiepushe na mawazo ya viongozi wenye itikadi za kivyama waliopo DARUSO.

Mgomo huo wenye lengo la kuishinikiza serikali ifute sera ya uchangiaji wa elimu katika elimu ya juu, wanafunzi wanatakiwa wauangalie kwa pande mbili na sio kuitupia lawama serikali kuwa inawakandamiza wanafunzi wakati kuna baadhi ya wenzao wanaikandamiza serikali.

Mfumo wa serikali wa kutoa mkopo kwa viwango tofauti kimsingi ni matokeo ya mgomo wa 2006/2007 na ni mzuri kwani unampa fursa mwanafunzi kupata mkopo kulingana na uwezo wake.

Lakini nao una walakini kwani haujaweka wazi vigezo vinavyotumiwa katika kutambua hali ya kiuchumi ya mwombaji na hivyo kutokuwepo na usawa katika utendaji wake.

Hali hii inawafanya wanafunzi wengi kutoridhika na viwango vya mikopo wanavyopata na kuiona bodi ya mikopo kama kisima cha ufisadi, kwani hudai kuwa baadhi hawastahi kupata mkopo na wanapata na wanaostahili kupata wanakosa.

Cha ajabu nikionacho mimi ni wanafunzi kuigomea serikali kabla ya kuwagomea wanafunzi wenzao ambao hawastahili mikopo na wanapata na tena utawaona mstari wa mbele wakipinga machoni huku moyoni wakishangilia.

Kama wana uzalendo wajitangaze kwa umma kuwa wanastahili kupata mkopo daraja C na sio A. na sio kugoma eti tu kwa kuogopa kutengwa na wenzao na kuonekana mzalendo kumbe si kweli.

Ningependa wanafunzi watambue kuwa tunaishi katika dunia ya utandawizi kama alivyopenda kuuita marehemu Prof Chachage. Pia tunatumia mfumo wa kibepari na sio ujamaa kama ilivyoandikwa kwenye katiba yetu ya jamuhuri ya muungano wa Tanzania.

Na wakumbuke kuwa katika mfumo huu tuliopo sasa haumruhusu masikini kulingana na tajiri na hata hivyo kwakuwa Tanzania iliingia kichwakichwa bila kutathmini athari zake hakuna kitu cha bure hivyo serikali haitaweza kutoa mkopo % kwa wanafunzi wote wa elimu ya juu Tanzania si kwa umasikini wa taifa pekee, bali ni kutokana na mfumo huu wa kibepari.

Sasa turudi kwenye lengo la makala hii, kwanini nasema wanafunzi UDSM watofautishe viongozi wa DARUSO na viongozi wanasiasa-DARUSO.

Kumekuwa na kawaida ya wanafunzi wanaochaguliwa kuwaongoza wenzao, kutumia nafasi zao kwa maslahi binafsi kwa kile kinachoonekana kwa wengi kuwa hutumiwa na wanasiasa.

Siwezi kutoa jibu kamili juu ya hoja hii kutokana na jambo lenyewe kuwa ni la kisiri zaidi, lakini ninachoweza kusema ni jinsi ya kumbaini mwanasiasa-MDARUSO kutokana na utendaji au maneno yake na sifa zake.

Kwanza mara nyingi mtu huyu hupenda kutafuta umaarufu kwa nguvu, hupanda jukwaani na kuongea kwa jazba akiwadanganya wenzake kuwa haogopi kufukuzwa chuo na yuko tayari kufa kwa ajili ya wenzake.

Mtu huyu hupenda madaraka na huyatafuta kwa nguvu na huweza kufanya hila hata kumpindua kiongozi Fulani ili mradi aingie madarakani na huweza kutangaza vita kabla ya kuingia madarakani na huweza kuanzisha kitu na kuwashawishi wenzake wakikubali bila kuwapa muda wa kufikiri juu ya jambo hilo.

Sifa bado zake kwani mtu huyu hafuati maamuzi ya wenanchi na hulazimisha jambo Fulani likamilike na kuonekana jema kwakuwa tu anataka adhma yake itimie.

Na tena hutangaza hadharani kuwa wanaigomea serikali na sio chuo na hivyo chuo hakihusiki.

Inasikitisha kuona wasomi wanamsikiliza kwa makini na kukubaliana naye moja kwa moja bila kutathmini. Iweje chuo kisihusike wakati shughuli zake za kiutendaji zinasimama kutokana na mgomo huo?

Wanashindwa kuelewa utegemezi wa sekta hizi mbili yaani chuo na serikali kwa wakati mmoja kwakuwa kimeitwa chuo cha serikali na kusahau kuwa unapogomea serikali umekigomea chuo.

Ikiwa mgomo huo hauna dhamira ya kukiathiri chuo watumie njia mbadala katika kudai haki yao ili mradi tu mwathirika awe serikali pekee na sio chuo. Naomba wanafunzi wenzangu watathmini upya katika hili.

Bahati mbaya wanafunzi wengi hupenda mtu wa aina hii kwa kuwa huamini yupo kwa ajili ya wananchi na kusahau kama anawakandamiza na kuwapotosha.

Wanafunzi hugeuka vipofu na viziwi kwa kutofikiria pande mbili za sarafu na badala yake huangalia upande mmoja tu na kuiona kama sarafu kamili.

Pindi baadhi ya wanafunzi wanapomtambua mtu huyu na kumfanya adui, huonekana wasaliti mbele ya macho ya wenzao.

Kutokana na uchache wao mawazo yao huonekana batili lakini hukumbukwa baada ya mabo kuharibika.

Sina nia mbaya katika makala yangu hii, lakini ninaumia sana kuona wasomi wakionekan si wasomi kwa kushindwa kufikiri.

Nashiondwa kuelewa na kutathmini hali ya Tanzania baada ya miaka kadhaa ijayo kama viongozi wetu ni miongoni mwa hawa wasomi.

Je mikataba feki na wizi wa EPA utaisha au utakua? Tathmini, jiamini, tumia uhuru wako kuzunguza na usiogope kutengwa na wenzako kwakuwa tu umefikiri sahihi na kuchukua hatua.
 
Shy, unachosema chaweza kuwa kweli 100% lakini ujue kuwa kinachotokea ni kuwaonyeshwa watawala kuwa hawaridhiki na jinsi mambo yanavyoenda katika nchi hii na migomo inatumika tu kama cover. Naamini kabisa kuwa wengi wao hawana sababu za msingi za kugoma.

Wanajua kuwa Nchi hii si masikini kiasi cha wao kushindwa kusomeshwa na kupata mazingira bora ya elimu wakati ambapo watoto wa Watawala wanasomeshwa nje ya nchi. Kwa ufupi ni ujumbe tu kuwa Watanzania wamechoshwa Watawala.
 
Wagome kistaarabu kama wameamua kugoma. Tabia ya kupiga watu kwa chupa au kujeruhi ni kuonesha jinsi wasivyokuwa na hoja
 
Back
Top Bottom