Ni uozo kwa kwenda mbele.......inasikitisha sana

Nyumbu-

JF-Expert Member
May 26, 2009
987
349
Kama waswahili wasemavyo, kama baba, kama mwana.....
Askari wa wanyama pori wameendeleza yale ya IGP Mwema, kuua raia wasio hatia , tena ukiwa umewafunga pingu!
Ni ukatili wa hali ya juu
Raisi anasema " mtatoka manundu, ngeu nk
IGP anatoa taarifa za kiintelijensia, na kusababisha mauaji ya kukusudia kabisa...
Sasa mgambo nanai awakemee?

Somahapa chini.....
Askari Selous wadaiwa kuua raia kwa risasi Send to a friend Sunday, 13 February 2011 20:57 0diggsdigg

Joseph Zablon
ASKARI wa Idara ya Wanyamapori katika Msitu wa Hifadhi wa Selous, wanadaiwa kuwaua kwa kuwapiga risasi, wakazi wawili wa Kijiji cha Kwala, wilayani Kisarawe, na kumjeruhi mmoja.

Tukio hilo la kutisha lilitokea Februari 5 mwaka huu, katika eneo la Machibwa, lililoko ndani ya Hifadhi ya Selous, ambako watu hao wanadaiwa kuwa walikuwa wanapita wakiwa safarini kuelekea katika Mto Kitogo, kuvua samaki, kwa ajili ya kitoweo.

Mmoja wa watu walionusurika katika tukio hilo, Mfanyeje Kigwiso, ambaye hata hivyo amejeruhiwa kwa kupigwa risasi mbili mgongoni na kwenye bega la kushoto, alisema yaliyomkuta Februari 5 mwaka huu, hatayasahau.

Kigwiso alitoa kauli hiyo huku akizungumza kwa shida, wakati akiwa katika mlango wa kuingilia katika chumba cha upasuaji, katika Hospitali ya Wilaya ya Kisarawe.

Alisema siku ya tukio wakiwa njiani kuelekea Mto Kitogo, walijikuta wamepotea njia katika eneo la Kidunda, jambo lililowalazimisha kutumia muda mrefu wakizunguka kutafuta mahali pa kutokea.

Alisema hata hivyo baadaye walisikia mngurumo wa gari na kupata matumaini ya msaada.

Kigwiso alisema kwa matumaini hayo waliamua kuelekea mahali ambako umlio ulikuwa unatokea na kwamba baadaye walikutana na gari aina ya Toyota Land Cruiser lililowabeba askari watatu wa Idara ya Wanyamapori.

Kwa mujibu wa majeruhi huyo, askari hao walikuwa na bunduki na waliwaamuru kupanda kwenye gari na kuingia nao msituni.

Kigwiso alisema baada ya mwendo wa dakika kadhaa, gari lilisimama na wao, kuamriwa kushuka, hatua iliyofuatiwa na kufungwa mikono kwa nyuma kwa kutumia kamba.

Alisema baadaye sehemu ya kamba hiyo ilifungwa kwenye gari ambalo dereva wake aliamriwa kuendesha na hivyo kuwaburuza huku wakilazimisha kuomba msamaha kwa kosa ambalo hawalijui.


Kigwiso alisema baada ya mwendo wa meta kadhaa, gari lilisimamishwa na kufunguliwa kamba, lakini waliachwa na mipira waliyokuwa wamefungwa mikononi.

Alisema askari hao waliwaamuru kusimama.

"Tulikuwa tunasikia maumivu makali ya kifua kutokana na michubuko ya kuburuzwa na gari, lakini hata hivyo walitutaka tusimame na walimtaka mwenzetu Hamisi Feruzi au Boy,’ atembee kama hatua nne mbele kisha wakamtaka asali sala zake za mwisho,"alisema Kigwiso.

Alisema askari hao bila huruma, walimfyatulia risasi mbili na kuanguka huku wakishuhudia kisha wakamtaka Ramadhani Suta naye kutembea hatua nne kisha na kuamriwa kusimama.

"Zilitoka risasi kama sita mfululizo ambazo zilimwagusha chini," alisema Kigwiso.

Alisema alipoona hali hiyo, aliomba msamaha wa askari hao ambao hata hivyo, hawakumsikiliza na badalayake, walimtaka afanye kama walivyofanya wenzake.

Alisema kwa kuwa alijua kilichotaka kutokea, alijilaza kifudi fudi na kuomba sala zake za mwisho na kwamba yaliyofuatia, hakuyajua hadi aliposhtuka wakati giza la jioni lilipoingia.


Kigwiso ambaye alisema alikaa na risasi kwa kipindi cha siku tano hadi alipofikishwa hospitalini kwa msaada wa Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe, Khanifa Karamagi, alisema alipojaribu kunyanyuka, alijisikia maumivu makali nyuma ya bega la kushoto na katika mkono wa kulia.

Alisema apochunguza vizuri, pembeni aliona miili ya wenzake na fisi ambao waliishawazunguka.

Alisema baada ya kuona hali hiyo, alijitahidi kunyayuka na kutembea kutoka katika eneo hilo, ili kunusuru uhai wake huku akiacha wenzake wakigombaniwa na wanyama fisi.


Kigwiso alisema kwa bahati nzuri alifanikiwa kuondoka katika eneo hilo lakini bila kujua alikuwa anaelekea wapi na kwamba safari yake, ilimchukua muda wa siku tatu.

Kwa mujibu wa maelezo yake, akiwa njiani, alipoteza fahamu kwa mara mbili hadi alipofika katika eneo la jirani na barabara inayoelekea katika kijiji chake cha Kwala, kilichoko jirani na Hifadhi ya Selous.

"Niliiona njia ya kuelekea kijijini na wakati natoka na kuanza safari, nikaanguka tena na kupoteza fahamu. Niliposhtuka nilijikuta nikiwa nimezungukwa na wanakijiji wenzangu ambao walikuwa wakijaribu kuninywesha uji,"alisema.

Kaka wa majeruhi huyo, Shaabani Mohamed, alisema waliwasubiri ndugu zao kwa siku tatu bila kuwaona bila taarifa zao.

Alisema kitendo hicho kiliwalazimisha kuwafuatilia kwa kutumia njia inayoelekea mtoni na baada ya kutembea kwa umbali mrefu, waliona mwili wa mtu ukiwa njiani.


"Tulijiuliza yule ni mlevi au kitu gani na tulipomsogelea, ndiyo tukamtambua ndugu yetu akiwa taabani huku damu zikiwa zimeganda mwili na kutoa harufu mbaya," alisema Mohamed.

Alisema hali hiyo iliwafanya wajiridhishe kuwa wenza wa ndugu wao, lazima walikuwa wameshapoteza maisha na kwamba hiyo inatokana na uzoefu wao wa matukio ya hifadhi hiyo.

Alisema baadaye, waliwapigia simu wenzao na kuwataka waende na pikipiki ili kumchukua majeruhi huyo na kumpeleka kijijini ambako walimpatia huduma ya kumwezesha kurudisha fahamu.


Kwa mujibu wa Mohamed, baada ya kuzinguka, Kigwiso aliwaeleza kuwa wenzake wameuawa na kwamba miili yao ameicha ikiliwa na fisi.

"Tuliwaeleza wenzetu kuwa mmoja tumemuona lakini mikono yote ikiwa haifanyikazi na hao wengine hatujui kama watakuwa wapo hai," alinena.

Alisema baadaye, Diwani wa Kata ya Samvulachole, Juma Dihoma, aliwasiliana na Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe, ambaye alituma gari lililomkimbiza majeruhi hospitalini.

Kutokana na taarifa aliyoitoa kwa wanakijiji wenzake na pia kwa baadhi ya waandishi wa habari na jeshi la polisi, safari ya kuelekea ilipotelekezwa miili ya wenzake hao, ilianza na baada ya mwendo wa saa tatu na dakika kadhaa kutoka kijijini cha Vikumburu, jirani na msitu hatimaye msafara ulifika eneo la tukio.


Katika eneo hilo lilikutwa fuvu la binadamu likiwa bado bichi na hata inzi walikuwa bado wanalizunguka.

Hali kadhalika kulikuwa na baadhi ya mifupa inayoaminika kuwa ni ya binadamu, kipande cha shati kilichokuwa juu ya mti na mabaki ya fuvu lililochomwa moto.

Pia kulikuwa na mabaki ya suruali iliyotambuliwa kuwa ni ya mmoja wa ndugu wa marehemu.

"Kipande hicho cha shati inawezekana kilikuwa kipande cha mwili wa marehemu ambacho kilitwaliwa na chui na kupanda nacho katika mti na kutafuna na baadaye kukibakiza," alisema Feruzi Abdallah mdogo wa marehemu Hamisi Feruzi.

Diwani Dihoma alithibitisha kupata taarifa za tukio hilo na baadaye kuomba msaada wa mkuu wa wilaya.

"Nilipata taarifa ya tukio, nikawasiliana na mkuu wa wilaya na hili ni tukio la tatu katika kipindi cha mwaka jana na mwaka huu. Watu ama wanapotea bila kurudi au wanauawa wakiwa katika msitu wa hifadhi," alisema.
 
Duuu, kweli hiyo ndio tz... kila mtu anajichukulia sheria mikononi mwake :twitch:
 
Inasikitisha sana. Ila kama sehemu ni hifadhi ya serikali na imekatazwa ku tresspass tujitahdi kufuata sheria hizo. Majangili huwa wanatumia mbinu kama kuokota kuni na kukata nyasi ili kuuwa wanyama kwenye hifadhi na hata kuwadhuru askari wanyamapoli. Poleni sana.
 
Hawa dawa yao ni kuwafanyia bonge la revenge, unaua askari wote kwenye huo m'mbuga halafu tuone.... Aaaaaaaaaaargh, inakera sana.
 
inasikitisha sana na ni unyama.kama askari walipaswa kuwakagua kama wana silaha manake jangili anakuwa na silaha,sasa mtu ana vinyavu au ndoano atakuwaje jangili? hii ni kesi ya mauaji nadhani huo majeruhi atawatambua kwenye graride la utambuzi wote waliohusika,awe makini wasije wakammalizia hospitali aliko.Tena hao askari wanatkiwa kuuawa mbele ya halaiki,hakuna cha kusema haki za binadamu wasiuwawe manake nao wameuwa kikatili. Majaji mpoooo???
 
Back
Top Bottom