Ni jinsi gani CPC inaweza kuiongoza nchi ya China yenye idadi kubwa kabisa ya watu na kuiendeleza kuwa ya pili duniani kiuchumi?

ldleo

JF-Expert Member
Jan 9, 2010
1,010
1,034
VCG111336187628.jpg


Wakati Chama cha Kikomunisti cha China CPC kinajiandaa kuadhimisha miaka 100 tangu kuanzishwa kwake 23 Julai 1921, kumekuwa na mambo mengi yanayofuatiliwa. Je ni vipi chama hicho kilichoanzishwa kikiwa na wanachama 50 tu, kimekuwa chama kikubwa cha kisiasa duniani na kufanikiwa kuiongoza nchi yenye idadi kubwa kabisa ya watu kujenga uchumi wenye nguvu na kutokomeza umaskini? Ni vipi kimeweza kuhimili wimbi la mabadiliko ya kisiasa duniani yaliyodhoofisha vyama vingi vya kikomunisti, na ni mambo gani vyama vingine vinaweza kujifunza kutoka kwa chama hicho?

Jambo la kwanza linaloonekana wazi ni kuwa chama hiki kiko makini kwenye kufanya mageuzi ili kiendane na wakati. Ni bora tukiri kuwa kwa sasa katika bara la Afrika hakuna nchi iliyo chini ya utawala wa chama cha kikomunisti, licha ya kuwa bado kuna baadhi ya nchi zina vyama vya kikomunisti. Sababu ni kuwa vyama hivyo vilipoteza mvuto kutokana na kasi ndogo ya kufanya mageuzi ya kimuundo na kisera, vikabaki kung’ang’ania zaidi itikadi za kisiasa kuliko maendeleo ya uchumi, kutoa kipaumbeke katika kuwajenga na kuwatukuza viongozi kuliko kuzingatia maslahi ya umma na taifa.

Chama cha kikomunisti cha China kilitambua hili toka mwanzo kuwa sera zake za uchumi zilikuwa na matatizo, na mwishoni mwa miaka ya 70 kilianza kufanya mageuzi hatua kwa hatua, kikitanguliza maslahi ya wananchi na taifa mbele, na kufanya maendeleo ya uchumi kuwa njia kuu ya kufikia malengo hayo. Hili ni moja ya mambo yanayofanya chama hiki kiendelee kuwa na mvuto kutoka kwa watu na kiendelee kukubalika. Wakati wimbo la mabadiliko linakuja kwenye miaka ya 90, na watu katika nchi mbalimbali za Afrika na Ulaya Mashariki kutoka mabadiliko, chama cha kikomunisti kilikuwa kimeanza kutekeleza mageuzi hayo kwa karibu muongo mmoja.

Jambo la pili, ambalo chama hiki kimeonyesha katika kipindi chote ni kujiamini. Wachina wamejijengea imani kuwa wao ni watu wenye busara na wanaweza kutumia busara zao kutatua matatizo yao. Kila China ilipokumbwa na changamoto, chama cha kikomunisti kilitegemea busara zake na nguvu ya ndani kutatua changamoto hizo. Isieleweke vibaya kuwa wachina hawapokei mawazo ya wengine, kilichopo ni kuwa nguvu ya ndani ndio msingi wa utatuzi wa changamoto yoyote iwe ni ya kiuchumi au kimazingira. Baadhi ya wanasiasa na wachumi wa nchi za Afrika pia wamekuwa na mtazamo kama huu, na wengine hata wamesikika wakisema sera na nadharia zilizotungwa katika nchi za magharibi, haziwezi kutatua matatizo ya nchi za Afrika. Wengine hata wamekuwa na msemo “majawabu ya Afrika, kwa matatizo ya Afrika”. Nchi za magharibi zimekuwa zikiziamishia nchi nyingine duniani kuwa njia zao ndio sahihi, lakini chama cha kikomunisti cha China kimetoa mfano hai kuwa maendeleo yanaweza kupatikana kwa njia yoyote inayoendana na mazingira ya nchi husika.

Jambo la tatu, moja kati ya mambo yanayopewa kipaumbele na chama cha Kikomunisti cha China ni usimamizi wa nidhamu. Kama ilivyo katika jumuiya yoyote duniani vitendo vya kukosa nidhamu kama vile ufisadi, ufujaji wa fedha za umma, uzembe n.k. vilionekana katika chama cha kikomunisti cha China. Ili kupambana na vitendo hivi kamati ya usimamizi na ukaguzi wa nidhamu ya chama iliimarishwa, na kuelezwa wazi kuwa chama kitatawala kwa nidhamu ya hali ya juu. Rais Xi Jinping ameendesha kampeni kubwa ya usimamizi wa nidhamu ndani ya chama, na kuwashughulikia bila upendeleo maofisa wote vigogo na wasio vigogo wanaothubutu kukiuka nidhamu. Kamati hii imekuwa kama fagio ndani ya chama, linalohakikisha kuwa chama kinakuwa safi na kinakuwa na watumishi wanaotekeleza maagizo ya chama na sio kuangalia maslahi tofauti.

Tukichambua kwa undani mambo haya yaliyofanywa na chama cha kikomunisti katika kipindi cha miaka 100, tunaweza kutambua kuwa chama chochote bila kujali itikadi yake kikiwa na mitazamo kama hii, hakuna sababu ya kupoteza mvuto kwa umma. Chama chochote ambacho kitaweka mbele maslahi ya umma na taifa, chama chochote ambacho kitasimamia nidhamu, na chama chochote ambacho kitafanya kazi ya kutatua changamoto za watu bila shaka kitakuwa na uungaji mkoni wa umma.
 
Back
Top Bottom