The Emils
JF-Expert Member
- Apr 16, 2011
- 568
- 124
SITAKI Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, ahubiri siasa za kuomba huruma. Wiki hii bungeni, alilitaka bunge, Watanzania wote na wenye nia nzuri kwa taifa hili, kusimama na serikali kupinga alichoita udhalilishaji wa kampuni ya Uingereza. Kampuni ya Uingereza inaitwa BAE (BAE Systems plc). Inatengeneza vifaa vya elektroniki vya ulinzi kwa majeshi na vyombo vya usafiri ndege na meli. Ni BAE wanaotengeneza rada za kuongozea ndege za kiraia na kijeshi na mitambo mingine kwa shughuli hizo. Ni BAE waliouza rada kwa Tanzania kwa bei ya kuruka zaidi ya sh 40 bilioni. Ni BAE waliogundulika kutoa rushwa kwa baadhi ya watendaji serikalini ili kuwalainisha; ili wakubali kununua rada haraka na kwa bei ya kuruka. Baada ya kashfa hii kufumuka, kuchunguzwa na hatimaye kujua kilichofanyika na waliohusika, BAE wamepewa sharti la kurejesha fedha zinazozidi kwenye bei halisi ya rada hiyo. Fedha hizo, zaidi ya dola milioni 20 za Marekani (dola 1 = sh 1,500), siyo chenji kama wezi wanavyotaka tuamini. Ni fedha zilizoibwa kwa kutumia madalali na mawakala ndani ya nchi; ndani ya serikali. Sasa pamoja na BAE kukiri ilichofanya, inasema haitaki kurejesha fedha hizo moja kwa moja kwa Serikali ya Tanzania. Kampuni hiyo inasema inataka kupeleka fedha hizo kwa shirika au mashirika yasiyokuwa ya kiserikali nchini Uingereza ili kwa kupitia huko, zitumike katika tasnia za kijamii. Membe hataki. Serikali yake haitaki. Wanasema huu ni udhalilishaji wa mamlaka ya nchi na raia wake. Wanatutaka kusimama nao kupinga udhalilishaji huo. Kwa jicho la nyongeza, BAE na serikali, wote ni kashfa tupu. BAE walitaka kuiba; wakaiba lakini sasa wamepatikana. Dunia inataka warudishe chetu. Lakini walioiba walishirikisha watendaji ndani ya serikali ya Tanzania kuwezesha au kulainisha au kurahisisha wizi kwa kutoa ushauri wenye mkengeuko au kunyamazia wizi. Kashfa ni kashfa, lakini kashfa ya serikali inawagusa zaidi na kuwaelemea wananchi. Tangu kufumuka kwa kashfa hii, hakuna lolote la maana ambalo wananchi wameshuhudia serikali yao ikifanya. Baada ya uchunguzi wa jinsi mauzo yalivyofanyika, bei halisi ya rada, waliohusika katika udalali na fedha zilizotolewa, ilitarajiwa serikali ichukue hatua. Bado iko kimya. Shirika la Uingereza la uchunguzi wa makosa makubwa ya jinai (Serious Fraud Office SFO), lilifanya kazi nzuri. Pamoja na kugundua na kuanika wizi wa kampuni ya nchini mwake; ilitaja Watanzania ambao walishiriki katika wizi huu mkubwa. Serikali haijachukua hatua zozote dhidi ya waliohusika. Hata ilipofahamika kuwa BAE wamekiri ufisadi na kwamba watarejesha fedha hizo Tanzania, bado serikali haijawagusa waliotajwa. Hebu liangalie hivi. Aliyehonga hadi kupata bei kubwa kwa rada ya bei ndogo, amekiri na kutaka kurejesha fedha alizokwapua; serikali ambayo watumishi wake ndio walisaidia wizi, bado iko kimya. Aliyeuza kwa bei ya kuruka anamwangalia yule ambaye watu wake walimsaidia kukwapua mabilioni ya shilingi (serikali ya Tanzania) na kuona hachukui hatua. Anajiuliza: Niwape haohao au zipite kwingine ambako matumizi yake yataonekana? Atakuwa na uhakika gani kwamba fedha hizo zitafika zinakopelekwa? Hapa kuna ukweli na unafiki pia. Ukweli ni kwamba kuna shaka juu ya fedha hizo kufikishwa zinakopaswa kupelekwa na kutumika baada ya kuingia mikononi mwa serikali. Kwa mfano, hadi sasa serikali inasema haijui Kampuni ya Kagoda, iliyoiba zaidi ya sh 40 bilioni kutoka Benki Kuu (BoT), iko wapi na ni mali ya nani. Lakini wakati huohuo kuna taarifa kuwa serikali ilipokea mabilioni ya shilingi kutoka Kagoda ili kampuni hiyo isishitakiwe. Serikali ina ndimi mbili. Au, chukua mfano mwingine. Hakuna uwazi wowote kuhusu fedha zilizorejeshwa na makampuni ya kifisadi yaliyoiba kutoka BoT. Maswali ni mengi mno. Nani hao waliorudisha fedha ili wasishitakiwe? Kwani Rais Jakaya Kikwete alisema wakirejesha sehemu ya fedha walizoiba, hawatafikishwa mahakamani. Hapa hoja ni kutofikishwa mahakamani; si kutotajwa hadharani ili watu wajue wezi hao. Hivyo, hatua ya kuweka siri kati ya serikali na wezi, inaiondolea hadhi serikali. Si hivyo tu, hatua hiyo inafanya serikali isigundulike inafanya nini na nani. Inafanyia kazi zake katika giza nene linaloweza kuwa limefunika ufisadi mwingine; labda mkubwa zaidi. Ni mambo haya ambayo yameiweka serikali katika mazingira ya kutiliwa shaka, kutoheshimika na kutoaminiwa. Mlundikano wa kashfa za Meremeta, Deep Green, IPTL, Richmond/Dowans, Kagoda na nyingine nyingi, zinaiacha uchi serikali na kuianika hata kwa wezi wakubwa wanaotumia madalali na wachonga dili ndani ya utumishi wa umma. Ni tabia na mwenendo huu vinavyofanya hata mwizi mwingine apate nafasi na ujasiri wa kudharau na hata kunyanyasa serikali. Hapo ndipo tunakuta unafiki wa mwizi wa Ulaya akituhumu anayelinda wezi bila kuwakamata na kuwashitaki ndani ya nchi, kuwa huenda asifikishe kwa wananchi fedha anazotaka kurudisha. Unafiki ni kwamba lini BAE wamegundua umuhimu wa fedha hizo kwa wananchi? Hivi hawakujua hili wakati wanazikwapua? Huu siyo tu mchezo mbaya; ni mchezo mchafu. Katika mazingira haya, Waziri Membe anawataka wananchi kusimama na serikali kupinga unyanyasaji wa BAE. Tatizo ni kwamba BAE wanafanya kama wanavyoona serikali inafanya katika maeneo tuliyojadili hapo juu. Wanapata ujasiri. Kama serikali haitaji wezi; haiwi wazi juu ya makusanyo ya fedha kutoka kwa wezi; kama inakaa na watuhumiwa wakuu wa wizi na ufisadi na inakataa kuwakamata na kuwashitaki; basi inajinyima fursa ya kupendwa, kuheshimiwa na kuaminiwa. Serikali inajinyima utetezi wa wananchi wake. Membe anaweza kuacha kulia machozi, akalia damu; lakini ukweli unabaki palepale: serikali yake inafanana na anaowatuhumu kutunyanyasa. Uzalendo hauji tu pale tunapokabiliana na watu au makampuni ya nje. Unapaswa kuwapo wakati wote ndani ya taifa letu na katika mipaka ya nchi. Tayari kuna minongono hata ndani ya Bunge kwamba Membe ametoa taarifa yake bungeni kabla ya kushirikisha kamati ya uongozi ya chama chake. Membe anaweza kuwajibu kwa swali: Je, waliokwenda kuiba kwa kuchukua mlungula, waliripoti au kuomba ruhusa kwangu au serikali? Ni ubabe kwa ubabe. Lakini hapo ndipo ulegevu wa serikali ulipofikisha nchi. Hata makampuni ya nje yanakoromea serikali. Hata walioiba wanaweka masharti ya kurejesha fedha. Tumebakiwa na nini? Machozi ya Membe au machozi ya papa? Kwani hata ndani ya Bunge wamo watuhumiwa wa mlungula wa rada. Serikali inawabusu. Inawafuta jasho. Uko wapi uzalendo ambao Membe anataka umsaidie kutunisha kifua kupambana na BAE? Uko wapi?Source: Mtanzania daima