Ghazwat
JF-Expert Member
- Oct 4, 2015
- 23,718
- 66,262
Kulingana na mashahidi, mshukiwa alifanya mauaji hayo saa chache baada ya kutibiwa katika zahanati moja kijijini hapo.
Kiongozi wa Kanisa la Trinity United Methodist, Alex Karuri aliiambia Taifa Leo kuwa alikuwa miongoni mwa waliompeleka mshukiwa hospitalini mapema asubuhi kabla ya mauaji hayo.
Alisema baada ya kutoka hospitali, walimpeleka mshukiwa hadi nyumbani kwa wazazi wake ambapo alilala fofofo.
"Alipoamka usingizini saa chache baadaye mchana, alianza kuzua vurugu hivyo mama yake akalazimika kuniita niende kumsaidia kumtuliza", alisema Pasta Karuri.
Baadaye mwanamume huyo alisisitiza kuwa alitaka kwenda kumtembelea rafiki yake anayeishi karibu na barabara ya Naivasha-Nairobi.
Aliruhusiwa kwenda kumtembelea rafiki yake, lakini mchungaji na mama yake walimfuata nyuma ili kuona alipokuwa akienda.
Ghafla
"Alishindwa kumpata rafiki yake na kuanza kutimua mbio kurudi nyumbani. Mimi na mama yake ambaye ana umri mkubwa tulijaribu kumkimbiza lakini akatuzidi kwa kasi", alisema Bw. Karuri
Baadaye majirani walisikia kelele na walipokimbilia katika eneo la tukio walikuta mke wa mshukiwa akiwa amelala chini huku damu zikimvuja. Mshukiwa alikuwa ameshikilia kisu chenye damu mkononi karibu na mwathiriwa.
"Alitishia kuwashambulia vijana waliojaribu kumpokonya kisu hicho. Lakini baadaye alizidiwa na akanyang'anywa kisu hicho", alisema mchungaji huyo.
Mkuu wa Polisi wa Gilgil, Sarah Koki alithibitisha kisa hicho huku akisema kuwa maafisa wa usalama walifahamishwa kuhusu mauaji hayo jioni.
Alisema polisi wameanza uchunguzi kuhusiana na kisa hicho. Na mshukiwa alikamatwa na anazuiliwa katika kituo cha polisi huku maiti ya mkewe ikiwa imehifadhiwa katika hospitali ya wilaya ya Gilgil.
Chanzo: TaifaLeo