Askofu Zakary Kakobe mpuuze na hoja igeuze. Huna haja wala hoja ya kutubu kwa toba kwakuwa unatoa tiba kwa miiba ya Tanzania. Unatibu bila tabu yaliyokuwa majaribu mujarabu kwa watanzania. Usitubu! "Hakuna asiye Na dhambi maishani ,lakini kuna watu wa aina mbili,wanaojitahidi kutofanya dhambi Na wasiojali kama wanatenda dhambi"
Usijali. Tunakuombea na kukujibia. Tutamjibu kwa mbwembwe kuliko kunyoa kwa wembe hadi Askofu ajione mzembe. Tutampa majibu ya mbali na karibu hadi aulaumu utaratibu uliomsibu. Usitubu!
Jijenge, jitenge na waingize mkenge. Jifagilie, jiandalie na jifurahie. Ni wakati wako chamani na Serikalini. Kataza hata kwa kuliza fujo za hovyo za mikutano na kuhutubia kwa kujielezea. Huna haja ya kutubu!
Kula nanasi kunahitaji nafasi. Unayo nafasi bila kufosi ya kujinafasi bila wasiwasi na kutajwatajwa wewe tu. Hutubia, tumbua, kemea, kamatia, zingatia, puuzia, koromea na kagua. Ni wewe tu, usitubu!
Demokrasia huleta ghasia. Mikutano hubadili mtazamo. Giza husaidia. Giza hulinda na kuunda. Tuache bila mikutano wala mitazamo. Tukusikie na kukufuata wewe tu. Usitubu, usijipe tabu!
Mambo ya expansion joints hayo!
Mzee Tupatupa wa Lumumba (mapumzikoni Nairobi,Kenya)