Mheshimiwa Raisi,
Niungane na barua ya Mwanakijiji na nyingine nyingi utazozipata mbelini kwenye swala hili la mgomo wa madaktari.
Mgomo huu ulipoanza nilidhani kabisa vyombo husika vitasimamia swala hili – labda kwa kuwa bado na imani na mfumo wa Serikali za Kiraia kutoa dira ya haki za msingi kwa wananchi wake. Na ni kweli, tumeona juhudi za Serikali kupitia Waziri Mkuu na Waziri wa afya lakini zilizoshidwa kumaliza mgomo badala yake kutumia nguvu za dola na mabavu. Nguvu ambazo hazikuwa za lazima. Viongozi wako wangekuwa wasikivu na wafuatiliaji wa madai ya madaktari - madai haya si mageni zaidi wataalamu wanasema mfumo wa afya katika sekta ya umma ni mbovu, vitendea kazi ni hafifu na maslahi duni - vyote vikiadhiri huduma inayotolewa. Sasa kuna ubaya gani mfanyakazi wako kukwambia ukweli?
Mheshimiwa Raisi,
Kiburi cha madaraka ni kibaya sana, hasa kwa viongozi wasiojua ama kwa makusudi kudharau nguvu ya Serikali inayojengwa na watu – na sio mitutu na bunduki - tulipiga kura za hiari. Serikali yako imeziba masikio juu ya madai ya madaktari, kazi yake imekuwa ni kutoa amri na vitisho. Eti warejee kazini ama ajira hamna. Haikuishia hapo tu mara mbwembwe ya madaktari wa jeshi ikaja! Ni mtu tu asiye na utambuzi kamili atayedhani hali tuliyonayo ni ya hatari na kujaribu kutumia nguvu ya dola na wataalamu wa jeshi kwa mgomo ambao ungeweza kuongeleka. Hii, ni dhahiri tunashidwa kutambua tofauti ya serikali ya kidemokrasia na jeshi.
Mheshimiwa Raisi,
Hii nchi haiongozwi na jeshi wala polisi. Tanzania inaongozwa na Raisi tuliyempigia kura, ingawa mimi sikukupa yangu, ila nakuheshimu kwani wewe ndio Raisi wa Tanzania. Hii ni nchi ya kidemokrasia, tena huru ambapo watu wanahaki ya kueleza kyero zao bila woga. Serikali ilipaswa kusikiliza na kuongea na madaktari. Sio kutuletea suluhu za mabavu zisizo za lazima. Ni ufinyu wa mawazo kudhani tuko vitani kutumia hazina ya madaktari wetu wa jeshi kuwa suluhu ya mgomo – tena kutumia kiongozi mkuu kama Waziri Mkuu na Waziri wa afya – kutishia watu kuachishwa kazi na kuleta madaktari wa jeshi. Chakushangaza zaidi, ni viongozi wetu kushidwa kutambua hata hao madaktari wa jeshi ni wachache kulinganisha mahitaji ya wagonjwa. Ni juha tu, anayeweza kucheza mchezo huu wa kuigiza.
Mheshimiwa Raisi,
Hii ni nchi ya utawala wa demokrasia na unajukumu la kuongoza nchi hii. Mimi labda nipishane na wenzangu, sitoi wito wa kusema ujiuzulu ama uachie madaraka, kwani hicho ni kiini macho na ni jambo ambalo huwezi kufanya, wewe kama mtu binafsi na hulka za viongozi wengi ambao wameshakuwa madarakani. Kuacha kuwa Raisi sio rahisi – na sina ndoto kwamba utafanya hivyo. Kwahiyo rai yangu mimi ni kukutaka ubebe majukumu yako ya kutuongoza kwani ni wajibu wako kutuongoza hasa pale ambapo hali ya wananchi inapokuwa tete. Nadhani tunapaswa kuweka kipengele katika utendaji kazi pale ambapo Raisi na serikali yake inaposhidwa kutimiza wajibu wake ndani ya muda stahili ifanywe nini. Maana inaanza kuwa mazoea sasa kwa serikali kukosea wananchi wake na wafanyakazi wake bila kuli uvunjaji wa haki za wananchi wala amani yao. Kama ni haki kumshtumu mwanachi kuvunja amani, na hivyo tutaifanya kosa la jinai kwa Serikali kuvunja imani. Tunaanza kufikiria hilo.
Mheshimiwa Raisi,
Nimesikia uko safari, lakini hali yetu ilipofia unapaswa kurudi nyumbani. Usianze kufanya mazoe kwamba watananzania watapiga kelele halafu watanyamaza. Yawezekana ilikuwa hivyo jana, ya leo hayatabiriki hasa kufuatia maamuzi yako juu ya kuboresha maslahi ya wabunge huku waatalamu wengine wakiendelea kukandamizwa. Kwa hadithi za redioni ama tunapoangalia kwenye luninga, haiwezekani kabisa kuelewa kwanini posho za wabunge zinaongezwa kwenye kipindi kama hiki – ambacho kinachochea vurugu kwa wananchi. Nashidwa kujilazimishwa kuamini kwamba alama hizi za fukuto huzioni – ama unaziona lakini umedharau. Hapa utakuwa umekosea sana tu.
Mheshimiwa Raisi,
Mimi kama mwananchi ambaye familia yangu imebahatika kutibiwa na hospital za umma. Hasa, siku za hivi karibuni, ninakila sababu ya kusema Serikali hawezi kuepuka kutatua mgogoro huu na madaktari. Ni dhahiri, tuna hospital binanfsi, lakini lazima tujiulize ni kwanini hospital za umma ndizo zinazofurika wagonjwa – wakiwemo wale wanaotoka wilayani na hata wale wa kutoka hospital binafsi. Hospital kuu za serikali sio tu kimbilio la watu waliochini lakini ndio sehemu yenye wataalamu waliobobea.
Mheshimiwa Raisi,
Unawajibu wa kujibu hoja za madaktari, kutuhakikishia huduma za afya sisi wananchi, na kuwajibisha watendaji wako. Lakini, la muhimu zaidi unawajibu wakutuhakikishia sisi wananchi unatuongoza katika vipindi vyenye mwamko wa kitaifa kama huu. Hayo sio maombi ni wajibu wako. Unaweza kuamua kujibu kisiasa ama kuangalia uhalisia na kutatua tatizo la sekta ya afya. Hapa tunaongelea mfumo wa sekta ya afya, ambao unawekeza zaidi katika hospital kuu, huku zahanati na wilaya zikiwa hali duni, na kufanya hospitali kuu kulemewa.
Mheshimiwa Raisi,
Ongeza taifa letu.